JOTO LA MOTO
JF-Expert Member
- Apr 11, 2018
- 766
- 562
SCRIPT ZA IMA.
SEHEMU YA KWANZA.
TITLE:FIMBO YA MBALI.
MTUNZI: IMA WA JONI A.K.A MSANII JOTO LA MOTO.
TEL.0788 135 198.
OFISINI KWA RAY-JIONI.
Ray na Hemedi, vijana watanashati, Ray, 32, na Hemedi, 29, wapo ofisini, Ray akiwa kwenye kiti kikubwa akitumia computer ya mezani na Hemedi akiwa kwenye moja ya viti vilivyopo mbele ya meza akisoma kadi,Ray anashusha pumzi, "hawa jamaa nao si wamechomoa" anasema Ray, "nilishakwambia bila baraka ya dingi zitaendelea kudunda" anasema Hemedi, "hamna kitu" anasema Ray, "nakwambia ukweli" anasema Hemedi, "hiyo ni proposal ya tano unadunda Ray" anasema Hemedi,"hujui unachoongea Medi" anasema Ray, wanabaki kimya kwa muda Ray akiendelea kutumia computer na Hemedi anasoma ile kadi, “sasa hii pati utaendaje na imeandikwa bibi na bwana?” anauliza Hemedi, “sio lazima kwenda bibi na bwana” anasema Ray, “lakini kila mualikwa atakuwa na mwenzake Ray” anasema Hemedi, “itabidi nikutafutie patna wa kwenda nae?” anasema Hemedi,“hebu naomba tuachane na huo mjadala Medi…maana najua unapoelekea” anasema Ray,”mimi nilichokuitia ni hiki” anasema Ray huku akiinua lap top iliyopo pembeni pale mezani na kumpatia Hemedi, “badilisha hiyo program” anasema Ray, “kama nitaipata kesho itapendeza zaidi" anasema Ray, “nitaileta asubuhi..kabla ya saa nne” anasema Hemedi, “kesho sitokuwepo ofisini..nitaenda Moshi kumuona mzee” anasema Ray, “nitaipitia kwako nikirudi” anaongeza Ray, “poa” anajibu Hemedi, “fundi wa TV ulimpata?” anauliza Ray huku anainuka, anachukua koti lake la suti nyuma ya kiti na kulivaa,“yupo kwako..ukifika utamkuta” anasema Hemedi huku anaibofya ile lap top, “sipitii home..naunganisha kwenye hiyo pati” anasema Ray huku anaweka tai yake sawa shingoni, anachukua funguo za gari kwenye droo na kuelekea mlangoni, Hemedi nae anainuka akiwa amebeba lap top na wanatoka
OFISINI KWA RAY-JIONI-NJE
Ray anaingia kwenye gari yake na kuondoka, Hemedi naye anafika kwenye gari yake, anaingia huku akiwa anabofya simu mkononi kwake, anaiweka sikioni.
NYUMBANI KWA RAY-SEBULENI SAA MOJA JIONI.
Mobeto, binti mrembo, 25, akiwa amevalia maridadi, sketi fupi laini iliyobana na kuchora vilivyo mwili wake ulioumbika vema, akiwa amejiachia kochini na glasi yenye juisi mkononi akiimalizia kwa funda moja na kuiweka glasi mezani, simu inaita, anaichukua na kuiweka sikioni, “sema Medi” anasema Mobeto, “huyu jamaa haji huko sasa hivi.. anaenda mount Meru kwenye pati” inasikika sauti ya Hemedi kwenye simu, “kwa hiyo” anauliza Mobeto, “hebu njoo home tuyapange upya” inasema sauti ya Hemedi kwenye simu, “poa” anasema Mobeto na kuitoa simu sikioni, “We mtoto” anaita Mobeto huku anainuka, baada ya sekunde mbili hivi anakuja Dulivan, kijana, 17, “bosi wako akija mwambie nitakuja kumalizia kazi kesho” anasema Mobeto, “hata kugusa hujaigusa hiyo TV” anasema Dulivan, “wewe inakuhusu nini?” anasema Mobeto, kwa ukali, “fuata maisha yako achana na yasiyokuhusu” anaongeza Mobeto huku akimnyooshea Dulivan kidole,“na ole wako umwambie Ray sijafanya kitu” anaendelea Mobeto huku akimkazia Dulivan macho, kisha anaelekea mlangoni,Dulivan anamsindikiza kwa macho huku akimng’ong’a, Mobeto anafungua mlango na kutoka, Dulivan anachukua glasi iliyoisha juisi pale mezani na kuondoka.
BARABARA YA MOSHI ARUSHA-MCHANA.
Toyota Harrier nyeupe ikiwa mwendo wa kasi inaenda na kufika getini nje ya nyumba moja nzuri, inapigwa honi geti linafunguka na gari inaingia, anateremka Ray na kuelekea mlangoni.
NYUMBANI KWA MZEE CHIRO, SEBULENI-MCHANA
Sebuleni yupo Blue, kijana, 28 Linah, dada 22, Monalisa, dada, 30 na Natasha,Mama, 60, wameketi kwenye makochi wakizungumza, mezani kuna jagi na glasi zenye juisi ya machungwa.
Ray anafika, “wasalam” Ray anasalimu, “salama bro” anajibu Blue na Mona, “vipi shem?” Linah anasalimia, “nipo poa shem” anajibu Ray huku anaketi kochini, “bro uko fasta” anasema Blue huku akiangalia saa yake “nusu saa kutoka Arusha?” anaongeza Blue kwa mshangao, “leo hakukuwa na tochi” anajibu Ray na wote wanaangua kicheko, “za Arusha?” anauliza Natasha, “nzuri tu mama..ila sio joto kama huku Moshi” anaongeza Ray, “Mzee yuko wapi?” anauliza Ray, “yupo ndani” anajibu Natasha, unasikika mlango unafunguka, “tena huyoo” anasema Natasha, sekunde chache baadae anafika Mzee Chiro, 70, akiwa amevaa fulana nyeupe na msuli na bakora mkononi akichechemea “shikamoo baba” wote wanasalimia, Mzee Chiro anabaki kimya anawaangalia, zinapita sekunde kadhaa bila kusema chochote kisha anageuza na kurudi alipotoka, Ray, Blue, Linah, Mona na Natasha wananaangaliana, Natasha anainuka na kumfuata Mzee Chiro.
NYUMBANI KWA MZEE CHIRO,CHUMBANI-MCHANA.
Natasha anaingia, Mzee Chiro ameketi juu ya kitanda “mbona umerudi tena ghafla Baba Ray na Watoto wamekuja kukuona?” Natasha anauliza,”unajua vizuri kwa nini nimerudi ndani mama Mona” anasema Mzee Chiro, Natasha anashusha pumzi, “ila sio vizuri ulivyofanya Baba Ray..Watoto wamesikia unaumwa wamekuja kukuona” anaongeza Natasha, Mzee Chiro anabaki kimya kwa muda, anashusha pumzi, “haya nakuja huko” anasema Mzee Chiro, “njoo bana..hayo mambo yenu mengine mtamalizana kwa muda wenu” anasema Natasha huku anainuka na kutoka.
Natasha anarudi sebuleni na kuketi, “Mzee anasemaje?” anauliza Ray, “anakuja..kuna kitu alisahau ndani” anamaliza kusema Natasha kisha inasikika sauti ya mlango ukifunguka, baada ya sekunde chache Mzee Chiro anafika pale sebuleni na kuketi,”Shikamoo baba” wote wanasalimia, Mzee Chiro bila kuitikia anabaki akiangalia chini, anainua kichwa, “hivi wewe Ray” Mzee Chiro anasema huku akimkazia macho Ray, “Mungu wangu” anasema Natasha kwa sauti ya chini huku akishusha pumzi “tatizo lako nini haswa?” anauliza Mzee Chiro, “jamani Baba Mona mbona hivyo tena?” anasema Natasha, “ona mdogo wako hapo” anaendelea Mzee Chiro huku akielekeza mkono kwa Blue na Linah, “amekuja na mkewe..na wana Watoto wao” anasema Mzee Chiro, muda huu wote Natasha amaejiinamia, “dada yako hapo Mona ana mume wake na Watoto” anaongeza Mzee Chiro, “kama mwenzetu upo upande wa pili si useme” anaendelea Mzee Chiro, Ray anashusha pumzi, anainuka na kuondoka, wote wanabaki wakimsindikiza Ray kwa macho anavyotoka “Ray” anaita Natasha, “muache aende” anasema Mzee Chiro, Natasha anainuka na kumfuata Ray.
NYUMBANI KWA MZEE CHIRO,NJE-MCHANA
Ray anatoka huku akitembea kwa haraka na kuingia kwenye gari na kuwasha, Natasha anatoka kwa haraka akikimbilia lilipo gari, “Ray” anaita Natasha, Ray anashusha kioo, “naomba tu umsamehe Baba yako Ray..nadhani hali yake unaiona” anasema Natasha,Ray anashusha pumzi, “Mama..nadhani nilishajieleza kila kitu vizuri kwa Mzee” anasema Ray, “wewe msamehe tu mwanangu” anasema Natasha, Ray anabaki sekunde mbili kimya, “hamna shida mama..uzuri mzee nimeshamzoea” anajibu Ray huku akiweka gia na kuondoa gari na kumuacha Natasha amesimama pale akisindikiza gari kwa macho, anatoka Mona akiwa na glasi ya juisi mkononi, anakuja hadi aliposimama Natasha, “sasa anavimba nini na amepewa ukweli” anasema Mona, Natasha anageuka na kumuangalia Mona kwa ukali, “sasa unamwambia nani?..mfuate umwambie” Natasha anasema huku anaondoka na kurudi ndani akimuacha Mona amesimama pale, Mona anapiga funda moja ya juisi kisha nae anarudi ndani.
BARABARANI YA MOSHI ARUSHA-MCHANA.
Gari ya Ray inaambaa ambaa barabarani na kuvuka kibao kinachosomeka KARIBU ARUSHA, Ray yupo garini akionekana yupo kwenye msongo wa mawazo, anaangalia saa yake kisha anachukua simu juu ya siti, anaibofya na kuiweka sikioni, “Hemedi..upo home niijie lap top?” Ray anauliza, “umeshatoka Moshi mara hii braza?” sauti ya Hemedi inasikika kwenye simu,”hivi ndio naingia Arusha” anasema Ray, “njoo tu mimi nipo kaka” sauti ya Hemedi inajibu, “poa” anasema Ray na kuitoa simu sikioni na kuirudisha pale pembeni kwenye siti ya abiria huku akiendelea kukanyaga mafuta.
NYUMBANI KWA HEMEDI-MCHANA.
Gari ya Ray inafika na kusimama, anateremka, anaenda mlangoni na kugonga, mlango unafunguliwa, anatokea Lulu, binti mrembo, 23, akiwa amejifunga kanga moja kifuani, Ray anashtuka na kubadilika usoni akionekana kushangazwa na hali anayoiona, “Hemedi yupo?” Ray anamuuliza Lulu, “yupo..karibu ndani” Lulu anajibu huku akiondoka pale mlangoni na kurudi ndani, Ray anabaki amesimama kwa muda kisha anaingia, anafika sebuleni na kuketi kwenye kochi, anabaki ametulia akiangalia muziki unaochezwa kwenye TV kubwa iliyopo mbele yake, Lulu anatokea akiwa na glasi mbili na chupa ya mvinyo, “karibu” lulu anasema huku anaweka zile glasi mezani, “Hemedi yuko wapi?” anauliza Ray, “yupo around anakuja sasa hivi?” anajibu Lulu, Ray anabaki anamshangaa Lulu kwa anavyokazana kuandaa vinywaji, “yupo huku ndani au yupo nje?” anauliza Ray, “ametoka kidogo lakini yupo njiani anarudi” Ray anashusha pumzi huku Lulu anamalizia kumimina mvinyo kwenye zile glasi, Ray anatoa simu na kuibofya, inasikika sauti ya kuashiria simu haipatikani,“ameacha mzigo wangu?” anauliza Ray, “hapana” anajibu Lulu, Ray anashusha pumzi na kuinuka, “vipi tena?” Lulu anauliza, “nitakuja wakati mwingine leo nina wageni nyumbani” anajibu Ray huku anaelekea mlangoni, “nina maongezi na wewe Ray” anasema Lulu kwa sauti iliyolegezwa ya ushawishi, “sio leo” anajibu Ray huku anafika mlangoni, anafungua mlango na kutoka, Lulu anabaki amesimama,anashusha pumzi kichovu na kujitupa kochini.
TULIZO BAR-MCHANA.
Gari ya Ray inafika na kufunga breki kali kisha anateremka kwa haraka na kuingia Bar, anasimama mlangoni kwa muda akiangalia huku na kule, anamuona Hemedi akiwa anacheza pool na wenzake, Ray anamfuata Hemedi na kumgusa begani, Hemedi anashtuka na kugeuka kumuona Ray, “naomba tuongee kidogo” anasema Ray, Hemedi anashusha pumzi, anaachia fimbo ya pool pale mezani na wanasogea mita chache kutoka pale, “unafanya michezo gani Medi?”Ray anauliza, “kivipi Ray..sikuelewi”? Hemedi anauliza huku anatoa pakiti ya sigara, anatoa sigara na kuiweka mdomoni, anatoa kiberiti cha gesi na kuiwasha, “kwa nini uliniambia upo nyumbani na hukuwepo?” anasema Ray, Hemedi anapiga pafu moja ya sigara kisha anashusha pumzi huku akiachia moshi mdomoni, “unajua tatizo lako nini Ray?” Hemedi anamwambia Ray, “huwa unapaniki hovyo” anaongeza Hemedi, “kwanza umemkuta Lulu geto?” Hemedi anauliza, “siwezi kuingia kwenye mitego yako ya kijinga Medi” anasema Ray, “Ray kama unamtosa hata demu kama Lulu basi lazima una tatizo” anasema Hemedi,”una maana gani?” anauliza Ray, “unahitaji msaada mkubwa Ray” anasema Hemedi, “isitoshe Lulu ndio kaniomba nimkutanishe na wewe Ray” anaongeza Hemedi, “sijali mtasema nini Medi..haya ni maisha yangu na nitaishi ninavyotaka” anasema Ray,”sio wewe..sio yeyote..hata baba yangu hawezi kunipangia cha kufanya” anaongeza Ray “mimi nina misimamo yangu Medi” Ray anaongeza, “misimamo gani Ray?” anasema Hemedi, “huyo Kidoti unayemtajataja yupo maili milioni moja huko” anasema Hemedi, “na sidhani hata kama kweli Kidoti ni demu wako Ray” anaongeza Hemedi, “hata kama angekuwa yupo kwenye sayari ya Mars..yule ndio chaguo langu full stop” anasema Ray, “msimamo” Hemedi anasema huku akisindikiza kwa kicheko cha kebehi, anapiga pafu moja la sigara, “naomba hiyo lap top” anasema Ray, “kazi yako tayari ila ipo home..nitaileta kwako jioni” anajibu Hemedi, Ray anaondoka, Hemedi anapiga pafu moja kisha anatoa simu anaibofya na kuiweka sikioni, “aise Mona mpango umefeli tena” anasema Hemedi, “imekuwaje?” inasikika sauti ya Mona kwenye simu, “sijui..namsubiri Lulu anipe stori” anasema Hemedi, “na tangu nimejuana na Ray sijawahi kumuona amevimba kiasi hiki..nusura tushikane mashati” anaongeza Hemedi, “pole” anasikika Mona kwenye simu,”ok narudi Arusha leo jioni nitakucheki..tutamnasa tu” anaongeza Mona kwenye simu, “poa” anasema Hemedi na kuitoa simu sikioni, kisha anaendelea kupiga pafu sigara yake.
NYUMBANI KWA RAY-USIKU.
Ray yupo sebuleni amechuchumaa ilipo TV akiibofya hapa na pale huku TV screen ikionyesha tu maandishi,”Duli” Ray anaita huku anainuka, anakuja Dulivan,”fundi amesema TV ina tatizo gani?” anauliza Ray, “alisema anataka mpaka wewe uwepo ndio atengeneze” Ray anashtuka, “ndivyo alivyosema mpaka mimi niwepo?” anauliza Ray, “hata mimi sikumuelewa yule dada bro” anasema Dulivan, “alikuwa ni mdada?” anauliza Ray kwa mshangao,”ndio bro” anajibu Dulivan, Ray anashusha pumzi na kujishika kiuno, “na leo ndio fainali ya Arsenal na barca” anasema Ray huku akielekea kochini na kuketi kwa muda kisha anachukua simu na kuibofya.
SK HOTEL CHUMBANI-USIKU.
Hemedi na Kajala, dada mrembo,25, wameketi juu ya kitanda wakiangalia video kwenye I pad, simu inaita, Hemedi anaichukua anaibofya na kuiweka sikioni, “sema Ray” Hemedi anatamka kwa bashasha, “hivi fundi wa TV uliyemtuma ni wa kike?” anauliza Ray, “kwani haiwezekani mwanamke kuwa fundi Ray?” anauliza Hemedi, “ok..sasa huyo fundi wako hakufanya chochote kwa hiyo inabidi nije kwako kucheki hii mechi” sauti ya Ray inasikika kwenye simu,“sipo home..nipo mahali kwenye kikao na client muhimu sana” anasema Hemedi, “we nenda tu funguo utazikuta pale kwenye..” anasema Hemedi kabla ya kukatishwa na sauti ya Ray, “hapana kama haupo home basi” anasema Ray, “au si uende pale City Bar wana bonge la screen” anasema Hemedi, “hapana siwezi kwenda kwenye lile danguro mimi” inasema sauti ya Ray, “ngoja tu nitafute namna nyingine“ inaongeza sauti ya Ray kwenye simu, “Ok poa kaka” anasema Hemedi na kuitoa simu sikioni, “ni Ray?” anauliza Kajala, “jamaa anaipenda Arsenal kuliko chakula” anasema Hemedi, “hivi ni kweli jamaa jongoo hapandi mtungi?” anauliza Kajala, “ndio mimi na Mona tupo kwenye utafiti" anasema Hemedi, huku akijiweka vizuri kuendelea kuangalia video inayocheza kwenye I pad aliyoishika Kajala.
NYUMBANI KWA RAY-USIKU.
Ray amejilaza kochini akiangalia mpira kwenye simu yake, “goli..dah” anapayuka Ray huku anainuka pale kochini, “Duli” Ray anaita huku anasimama na kuvaa jaketi lililokuwa pembeni, Dulivan anakuja, “fungua geti itabidi niende tu City bar kuangalia hii mechi” Ray anasema huku kwa haraka akielekea mlangoni na kutoka Dulivan akimfuata.