Shairi: Chako ni chako

Love Doctor

JF-Expert Member
Jun 28, 2016
726
786
Kilicho Chako ni Chako

1
Nasema yalo nisibu, ukweli nawaeleza.
Sitaki niwe ja bubu, na nyie mkateleza.
Mkapata masahibu, leo hii nawajuza.
Kilicho chako ni chako, vya watu vina maneno

2
Nilipopewa cha mtu, tukiwa furaha tele
Mwenyewe hakuwa mtu, akawa mwingi wa kele.
Nikazamia msitu, kuwa wake msukule.
Kilicho chako ni chako, vya watu vina maneno

3
Adai kila mahala, bila yeye mi siishi.
Akanipa nyingi hila, ni mtu alo bilashi.
Ni maisha ya kisela, kuyabeba mafurushi.
Kilicho chako ni chako, vya watu vina maneno

4
Nilifurahi mwanzoni, kumbe mwishowe huzuni.
Sikujua ya mbeleni, ntaingia kifungoni.
Nimeishi utumwani, masiku mia tisini.
Kilicho chako ni chako, vya watu vina maneno

5
Kilicho chako ni chako, ukitunze ndugu yangu.
Cha mtu ni chokochoko, kibaya ila ni changu.
Haya ni maisha yako, mja ana lake fungu.
Kilicho chako ni chako, vya watu vina maneno

Abuuabdillah
Omari Juma Kimweri
Jumaomari5@gmail.com
Jumaomari@ymail.com
0744883353
0718569091
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom