Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) inawashikilia na kuwahoji watu saba wakiwemo wafanyabiashara maarufu wawili wa madini ya Tanzanite kwa tuhuma za utoroshaji wa vito vyenye thamani bilioni 7.2.
Akizungumza na vyombo vya habari leo, Septemba 25, 2020, jijini Arusha, Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo, Brigedia Jenerali JohnMbungo amesema wafanyabiashara hao wanahojiwa na upelelezi utakapokamilika watafikishwa mahakamani kwa makosa ya ukwepaji kodi huku wakikiuka sheria, kanuni, taratibu pamoja na miongozo inayohusiana na biashara hiyo.
Mkurugenzi huyo amewataja wafanyabiashara wanaohusishwa na tuhuma hizo ni Joel Saitoti Mollel ambaye ni meneja mkuu wa migodi na mwanahisa wa kampuni ya Gem and Rock Ventures ya Jijini Arusha pamoja na mkewe, Caren Saitoti Mollel.Wengine ni Daudi Lairumbe ambaye ni Wakili wa kampuni ya Gem and Rock Ventures Ltd, Rakesh Kumar Gokhroo (Colour Clarity), George Kivuyo mchimbaji na mfanyabiashara wa madini na mshirika wa kibiashara wa Joel Saitoti, Naiman Mollel mchimbaji wa Tanzanite katika mgodi uliopo Mirerani unaomilikiwa na kampuni ya Gems & Rock Ventures pamoja na Ezekiel Laizzer mchimbaji na mshirika wa kibiashara wa Saitoti
.Brigedia Mbungo alisema uchunguzi wa awali umebaini kuwa mfanyabiashara huyo Joel Saitoti na Rakesh kwa kushirikiana na watuhumiwa hao wanadaiwa kufanya uchimbaji, ununuzi. usafirishaji wa madini bila kufuata sheria Ambapo watuhumiwa wote wamekuwa wakitumia rushwa kushawishi baadhi ya watendaji wa serikali ili kufanikisha azma yao ikiwemo kupunguza thamani ya Madini, ikiwemo kupewa thamani ndogo kwenye soko la madini ambapo watuhumiwa hao kwa pamoja wamepata mali kwa njia zisizo halali zinazofikia Sh bilioni 7.2.
Chanzo: habari Leo