Mkutano wa Kimataifa wa Wanawake umefanyika wiki hii mjini Beijing kufuatia wito wa rais Xi Jinping wa China, na kuweka hatua mpya muhimu katika historia ya maendeleo ya wanawake.
Miaka 30 iliyopita, Mkutano wa Nne wa Dunia wa Wanawake wa Umoja wa Mataifa pia ulifanyika Beijing, ambapo Azimio la Beijing na Mwongozo wa Utekelezaji vilipitishwa, vikiweka kihistoria “usawa wa kijinsia” katika ajenda ya zama. Wakati ule, wanawake wa Afrika bado walikabiliwa na changamoto katika haki za kupata elimu na kutoa sauti zao. Mkutano huo wa Beijing uliwezesha sauti za wanawake kutoka nchi zinazoendelea kusikika na kuthaminiwa kwa mara ya kwanza kwenye jukwaa la kimataifa. Katibu Mkuu wa mkutano huo wa nne, Gertrude Mongella alirudi Tanzania na nyaraka hizo, akiziona kama nuru ya matumaini ya kubadilisha hatima ya wanawake wa Afrika.
Katika kipindi cha miaka hii 30, China imejumuisha "usawa wa kijinsia" katika mkakati wake mkuu wa maendeleo ya kitaifa. Wanawake milioni 690 wameishi katika jamii bora kwa wakati mmoja kama wanaume, idadi ya wanafunzi wa kike waliopata elimu ya juu imezidi nusu ya idadi ya jumla, na wanawake wanaofanya kazi za kisayansi wamefikia asilimia 45.8.
China haitekelezi tu usawa wa kijinsia yenyewe, bali pia imetoa "mpango wa China" kwa maendeleo ya wanawake wa Afrika. Kwa mfano, Reli ya Mombasa-Nairobi, iliyojengwa kwa ushirikiano kati ya China na Kenya, imefundisha takriban wataalamu 2800 wa ndani wa kiufundi na usimamizi, akiwemo mwanamke wa kwanza msimamizi wa treni, Damaris Mutinda. Takwimu zimeonyesha kuwa Shirikisho la Wanawake la China limeanzisha uhusiano na zaidi ya mashirika na taasisi 100 za wanawake kutoka nchi 53 za Afrika zenye uhusiano wa kidiplomasia na China, na limeandaa warsha za mafunzo kwa ajili ya kukuza vipaji vya wanawake wa Afrika.
Kama alivyosema Mongella, ushirikiano kati ya wanawake wa China na wanawake wa Afrika ni kubadilishana maarifa na ujasiri. Miaka 30 iliyopita, Mkutano wa Beijing uliwezesha mbegu za "usawa wa kijinsia" kuota, na Mkutano wa Kimataifa wa Wanawake wa miaka 30 baadaye utafanya matawi ya "maendeleo ya pamoja" kustawi zaidi. Katika siku zijazo, China itashirikiana na pande zote duniani kuhakikisha kwamba "Roho ya Beijing" inaangaza zaidi katika sekta ya maendeleo ya wanawake.