RIWAYA: TAHARUKI
Imeandikwa na HALFANI SUDY
SIMU 0652 212391
Hii ni Sehemu ya Kumi na Tano
“Sawa Daniel, hakikisha unampigia simu mwenzio kuhakikisha kwamba yupo salama” Chifu alisema kwa kifupi na kukata simu.
Alipomaliza kuongea kwa simu na Chifu, Daniel aliitafuta namba ya Martin katika simu yake na kuipiga, ilikuwa kama alivyosema Chifu, Martin alikuwa hapatikani hewani. Akaitafuta namba ya Hannan na kuipiga.
“Habari za asubuhi Daniel” Hannan alisalimia baada ya kupokea simu ya Daniel.
“Nzuri Hannan, najua ushasikia mambo yaliyotokea asubuhi ya leo hapa mjini......”
“Nimesikia Daniel, si kuhusu kutekwa kwa gari la wanafunzi wa shule ya msingi Vanilla?” Hannan aliuliza kabla Daniel hajamwambia ni kitu gani alichokuwa anamaanisha.
“Upo sahihi, ni kuhusu kutekwa kwa wanafunzi wa shule ya msingi Vanilla. Sasa Hannan tumepewa sisi kazi ya kuhakikisha watoto wote wanarudi salama majumbani mwao hiyo, tena wakiwa salama” Daniel alisema.
“Sawa Daniel, hata mimi nilikuwa natamani kazi hii ipewe idara yetu. Nillipata hisia mbaya sana pindi tu nilisikia tukio hili katika vyombo vya habari. Kwa kupewa idara yetu ninaamini tutaifanya kazi hii kwa ufanisi mkubwa sana na tutaikamilisha kwa wakati” Hannan alisema bila ya wasiwasi wowote.
“Halafu kitu kingine Hannan, simu ya Martin haipatikani hewani tangu jana usiku. Nitakutumia namba yake uichunguze ili tujue mara ya mwisho ilikuwa hewani akiwa wapi? Chifu ana wasiwasi sana juu ya usalama wa Martin” Daniel alisema.
“Sawa Daniel, nitumie namba ya Martin. Nitajaribu kuangalia alikuwa wapi mara ya mwisho. Bila shaka hapo ndipo patakuwa sehemu pa kuanzia kuchunguza ni kitu kimemtokea Martin”
“Sawa, ninakutumia sasahivi. Ukimaliza kazi hiyo ninaomba tukutane katika mgahawa wa Cream saa tatu asubuhi, tuone tunaanzia wapi kuwarudisha wanafunzi wa shule ya msingi ya Vanilla” Daniel alimwambia Hannan.
“Sawa Daniel, nitakuwa katika mgahawa wa Cream muda huo” Hannan alikubali.
“Sawa” Daniel alisema na kukata simu.
Daniel alijifuta maji ingawa yalikuwa yameshaanza kukaukia mwilini. Akalisogelea kabati la nguo na kulifungua. Akachagua suruali ya dengrizi ya rangi ya samawati na fulana nyeusi iliyokuwa na mchoro wa nyota nyeupe kwa mbele. Chini alivaa raba nyeusi ambazo nazo zilikuwa na nembo ya nyota tano kwa pembeni, kichwani alivaa kofia aina ya kapelo ya rangi nyeusi pia, mbele ikiwa na mchoro wa mbwa mdogo. Alilifunga kabati na kwenda katika droo ndogo iliyoungana na kitanda, akaifungua na kutoa bastola mbili, akazipachika katika pande mbili za kiuno chake. Akauokota funguo wa gari ulikuwa umelala juu ya kiti cha mbao na kutoka nje. Nje ya nyumba akaingia katika gari aina ya Alterza ya rangi nyeusi na kutoka nayo nje ya nyumba yake.
Saa tatu kamili ilimkuta katika mgahawa wa Cream uliopo katikati ya jiji la Dar es salaam. Alimkuta Hannan akiwa amechagua meza moja iliyokuwa pembezoni kabisa mwa mgahawa wa Cream. Hapo ndipo mahali hukutana mara zote Daniel anapomwambia wakutane katika mgahawa huo.
Juu ya meza, iliyotengenezwa kwa ustadi mkubwa kwa kutumia mti wa mpingo, kulikuwa na bilauri iliyokuwa na sharubati ya chungwa ndani yake. Hannan alikuwa anauvuta mrija ulioingizwa ndani ya sharubati hiyo kwa madaha.
Hannan alikuwa amevaa suruali ya dengrizi ya rangi ya nyeusi. Juu, alivaa fulana ya rangi ya pinki yenye vimdoli viwili vya rangi nyeupe. Chini, alikuwa amevaa raba nyepesi za rangi nyeupe. Alikuwa ana mwili wa kike mdogomdogo ambao ungekufanya umhusudu sana kwa jinsi alivyoweza kuutunza vyema.
Alivuta tena funda la sharubati ya chungwa, akauangalia mkono wake wa kushoto uliokuwa umevaa saa kutoka kampuni ya Casio. Ilikuwa ni saa tatu na dakika mbili, dakika mbili zaidi ya muda waliokubaliana na Daniel. Aliangaza macho yake katika mlango wa kuingilia, ndipo alipomuona Daniel akiingia ndani ya mgahawa wa Cream bila ya wasiwasi wowote. Hannan alitabasamu huku akimwangalia Daniel akielekea katika aliyokaa.
“Karibu sana Daniel, kwa mara ya kwanza leo nimekuwahi” Hannan alisema huku akisimama na kumkumbatia Daniel.
“Ahsante sana Hannan, na hongera kwa mara ya kwanza kunitangulia katika miadi” Daniel alisema huku akicheka.
“Umependeza sana leo..” Hannan alisema wakati wakiwa wameachiana na Daniel.
“Nawe umependeza pia...” Daniel alisema huku akikaa kwenye kiti.
“Ahsante Daniel. Tuache hayo tuelekee moja kwa moja katika kazi iliyopo mbele yetu. Nilifanikiwa kupekua na kufanikiwa kujua mahali pa mwisho ilipokuwa hewani simu ya Martin...” Hannan alisema.
“ilikuwa sehemu gani?” Daniel aliuliza kwa pupa.
“Kusema kweli yametokea majibu ya kushangaza sana, kwa mara ya mwisho simu ya Martin ilikuwa hewani saa mbili zilizopita katika jiji la Paris huko nchini Ufaransa”
“Unasemaje?” Daniel aliuliza kwa nguvu.
“Ndio majibu yaliyokuja, nilijaribu kumpigia simu rafiki yangu anayefanya kazi katika mtandao wa simu wa Teltel ili naye ajaribu kuitafuta namba hiyo. Naye alikuja na majibu hayohayo” Hannan alisema.
“Imewezekana vipi hiyo Hannan?” Daniel aliuliza.
“Kinachonijia katika akili yangu sio kitu kizuri kwa Martin, ninaomba unisamehe kwa kusema hivi, ila ninahisi Martin hayupo sehemu salam” Hannan alisema huku sauti yake ikiwa imeambatana na hofu.
Daniel alibaki akimwangalia tu Hannan, alikubaliana kwa asilimia zote na maneno ya Hannan lakini hakuwa tayari yawe ndio ukweli. Kwasasa alikuwa anamhitaji Martin kuliko wakati wowote ule. Alikuwa anamuhitaji katika kazi kubwa iliyopo mbele yake ya kuhakikisha wanawaokoa watoto waliotekwa wa shule ya msingi Vanilla. Alikuwa anamhitaji kwaajili ya kumalizia walichokianza kuhusu mzigo usioeleweka wa Bilionea Zawiya na wizi mkubwa wa madini ya Tanzanite, hivyo hakutaka kabisa kukubaliana na ukweli wa taarifa kuwa Martin hayupo sehemu salama kwa sasa.
“Unawaza nini Daniel?” Hannan alimuuliza Daniel alipomuona akiwa amezama katika dimbwi la fikra.
“Kauli yako kuwa Martin hayupo sehemu salama imeniogopesha sana Hannan. Katika vitu ambavyo nitajilaumu siku zote za maisha yangu ni kuona Martin anaingia katika hatari bila ya kufanya juhudi yoyote ile ya kumuokoa”
“Ninaelewa unavyojisikia Daniel, ninaelewa hata unachotaka kufanya kwaajili ya Martin. Lakini hauwezi kufanya unachowaza kufanya kwa wakati huu. Mbele yetu tuna kazi ngumu na kubwa sana za kufanya” Hannan alisema huku akimwangalia Daniel.
“Umejua kuwa ninafikiria kwenda nchini Kenya kumuokoa Martin?” Daniel aliuliza kwa mshangao.
“Ndio, nimejua ulikuwa unafikiria hivyo, lakini itakuwa ni ngumu kwa wewe kwenda nchini Kenya huku ukiacha jukumu ulilopewa na Chifu la kuwatafuta watoto waliotekwa na watu wasiojulikana. Ninakushauri tulimalize hili kwanza. Lakini hata hivyo haya ni mawazo yetu tu kuwa Martin yupo katika matatizo, pengine yupo sehemu fulani akiwa salama salmin” Hannan alisema.
“Nimekuelewa Hannan. Sasa yatupasa kutafuta pa kuanzia katika safari ya kuwaokoa watoto wetu waliotekwa. Nilipoongea na Chifu aliniambia kuwa idara yetu imepewa dhamana ya kushughulikia jambo hili lakini kwa kushirikiana na jeshi la Polisi, pia amenambia kuwa miongoni mwa watoto waliotekwa ni mtoto wa Joash Mkubwa”
“Mtoto wa Joash Mkubwa naye ametekwa?” Hannan aliuliza huku sura yake ikiwa katika mshtuko mkubwa.
“Ndio Hannan, na kutekwa kwa mtoto wa Joash Mkubwa kumeongeza hofu sana kwa maana hatujui yule jamaa ataibuka kwa mtindo gani. Lakini tujue tu kwamba kwa mtindo wowote ule atakaoibuka nao utakuwa sio salama kwa serikali ya rais Mark. Yatupasa kuhakikisha jambo hili linamalizika wakati huuhuu ambao Joash Mkubwa akitafuta mtindo wa kuja nao” Daniel alielezea kwa kirefu.
“Nimekuelewa Daniel, sasa mimi nilipiga hatua kidogo baada ya kusikia kuwa watoto wa shule ya msingi Vanilla wametekwa. Nilichugundua katika uchunguzi wangu mdogo ni kuwa, ndani ya gari lililotekwa kulikuwa na watu ishirini na saba ingawa lilitakiwa liwe na watu ishirini na nane; watoto wadogo ishirini na tano, dereva, utingo na msaidizi wa watoto. Ila tukio lilivyotokea dereva aliachwa wakati alipotoka garini kwenda kuziangalia gari mbili zilizokuwa zimeharibika barabarani na kuziba njia. Hivyo mpaka sasa jumla ya watu ishirini na saba walitekwa na hawajulikani walipo. Tuna sehemu mbili ambazo tunaweza kuzitumia kwa kuanzia uchunguzi wetu, kwanza kwa kwenda kumhoji dereva wa gari ya watoto ambaye inasemakana yupo katika kituo kikuu cha Polisi, kwa ajili ya mahojiano na jeshi la Polisi. Sehemu ya pili katika uchunguzi huu ni kuzichunguza hizo gari mbili zilizoziba njia, bila shaka zinahusika moja kwa moja katika tukio la utekaji” Hannan alitoa maoni yake.
“Umewaza vizuri sana Hannan. Hayo maeneo mawili uliyoyasema ni ya kuyazingatia sana, kwa huyo dereva na hizo gari mbili zilizoziba njia. Sasa ninaomba tugawane majukumu, wewe ufuatilie taarifa zote kuhusu huyo dereva, kabla hujaenda kufanya naye mahojiano huko Polisi. Mimi nitaenda eneo lilipotokea tukio kujua zaidi kuhusu hizo gari mbili. Ninaomba tufanye kazi hii kwa uharaka mkubwa lakini bila ya kupoteza umakini. Tukutane nyumbani kwangu baada ya saa mbili kupeana taarifa juu ya tuliyoyapata. Endapo mmoja wetu akichelewa kufika sehemu ya kukutania baada ya muda tuliokubaliana basi tujue kuna tatizo limetokea kwake, na lazima tutafute namna ya kumsaidia”
“Nimekuelewa Daniel, nitafanya kila kitu kama ulivyoagiza, nina imani tunaenda kufanikisha hili na watoto wetu tutawaokoa wakiwa salama” Hannan alisema.
Baada ya maongezi yaliyodumu kwa takriban dakika kumi na tano, waliagana kwenda kufanya kazi waliyopangiana. Hiyo ilikuwa saa tatu na nusu.
Hali ilikuwa ya majonzi makubwa sana katika nyumba moja huko Mbagala Kilungule. Familia ya mzee Mboto ilikuwa katika majonzi makubwa sana baada ya mtoto wao mkubwa wa kiume kuingia matatani na vyombo vya dola.
Saa nne na dakika kumi asubuhi, gari ndogo aina ya Toyota Mark X iliegeshwa mbele ya nyumba hiyo. Watu wachache waliokuwa wamekaa katika kibaraza cha nyumba ya mzee Mboto, macho yao yalielekezwa barabarani ili kumuona mtu atakayeshuka katika gari hiyo. Ingawa kwa siku hiyo, kuwasili kwa magari ya aina mbalimbali katika nyumba hiyo halikuwa jambo la kushangaza, na hii ilitokana na mtoto mkubwa wa nyumba hii kukamatwa baada ya gari alilokuwa anaendeshwa kutekwa na watu wasiojulikana. Hivyo mara kwa mara yalikuwa yanakuja magari mbalimbali kwaajili ya kumpa pole dereva mwenzao.
Raba nyeusi iligusa ardhi ya Kilungule, kabla ya mwili wa dereva wa gari hilo dogo kutoka garini. Dereva wa gari alikuwa mwanamke mrembo, kwa kumkadiria alikuwa hazidi hata miaka ishirini na tano. Kadirio la umri wake lilithibitishwa na umbo lake dogo. Mwanamke alifunga mlango wa gari yake na moja kwa moja alielekea katika nyumba ya mzee Mboto.
“Habari zenu wakubwa, shikamoni” Mwanamke alisalimia watu wote kwa ujumla.
Wengine waliitikia salamu ya yule mwanamke, huku wengine wakibaki wakimtolea macho mwanamke yule mrembo.
“Samahanini kwa kuwavamia bila ya taarifa” Mwanamke alianza kwa kuomba radhi, ”Ninaitwa Hannan nilikuwa nina shida na mwenyeji wa nyumba hii”
“Karibu sana, mimi ndio mwenyeji wa nyumba hii” Mzee mmoja wa makamo alisema kwa sauti ya huzuni huku akimwangalia Hannan.
“Nafurahi kukufahamu mzee, samahani ninaomba tuongee pembeni kama inawezekana” Hannan alisema kwa kujiamini.
Mzee Mboto alitoka katikati ya kundi la watu na kuelekea nyuma ya nyumba, Hannan naye alimfuata kwa nyuma. Watu wengine wote macho yao yalielekea kule walipoelekea mzee Mboto na Hannan.
“Samahani mzee kwa kukutoa mahali pale, kama nilivyojitambulisha awali, mimi ninaitwa Hannan, ni afisa wa jeshi la Polisi kutoka idara maalum. Nimekuja hapa kwa ajili ya kukuhoji machache kuhusu dereva wa gari la shule ya msingi Vanilla ambaye nimeambiwa anaishi hapa” Hannan alisema huku akinyoosha kitambulisho chake alichokuwa amekishika mkononi.
Mzee Mboto alimwangalia Hannan kwa macho ya uwoga kisha akasema, “Karibu sana binti yangu, nadhani hapa sio sehemu sahihi sana ya kunihoji, tungeenda sebuleni nadhani ingefaa zaidi” Mzee Mboto alisema bila ya kufanya jitihada zozote za kukiangalia kile kitambulisho alichokishika mkononi Hannan.
“Usiwe na wasiwasi, hata hapa patafaa, nina maswali machache tu ambayo ninaweza kukuuliza nawe ukanijibu hapahapa” Hannan alisema huku akimwamgalia machoni mzee Mboto.
“Sawa, karibu binti yangu”
Hannan aliingiza mkono wake katika mfuko wake wa suruali na kuwasha kifaa cha kurekodia sauti, aliporidhika kuwa kimeanza kurekodi aliuliza swali, “ Ninaomba unitajie majina yako matatu, kabila na uhusiano wako na dereva wa gari ya shule ya msingi Vanilla lililotekwa leo”
“Kwa majina ninaitwa John Joseph Mboto, kabila langu ni mmatumbi kutoka huko Kilwa Kipatimu, katika mkoa wa Lindi uliopo kusini mwa nchi hii. Erick ni mtoto wangu pekee wa kiume” Mzee Mboto alijibu.
“Una watoto wengine zaidi ya Erick?” Hannan aliuliza.
“Ndio, nina watoto wa kike sita, na mtoto wa kiume mmoja, ambaye ndiye Erick”
“Erick anaishi hapa?”
“Hapa ndio nyumbani kwa Erick, mimi ninaishi nyumba ile pale” Mzee Mboto alisema huku akiionesha kwa kidole cha shahada nyumba iliyokuwa mbele ya nyumba ya Erick.
“Samahani mzee kwa kuuchukua muda wako, najua upo katika kipindi cha majonzi baada ya mwanao kuingia katika matatizo, nikwambie tu haya yatapita endapo ukweli utajulikana, Ninaomba unipe nafasi ya kunijibu maswali yangu kadhaa ambayo bila shaka yatakuwa ni mwanga kuwajua wahalifu waliowateka wanafunzi na mwanao Erick kuwa huru”
“Ahsante sana binti yangu, mimi nipo tayari kutoa ushirikiano wowote ule ilimradi tu Erick wangu awe huru” Mzee Mboto alisema kwa sauti ya majonzi.
“Kwanza ninataka kujua kuhusu Erick, umri wake, familia yake na mambo mengine yanayofanana na hayo”
“Erick ana umri wa miaka thelathini na tano., ameoa na ana watoto wawili. Yeye na familia yake wanakaa katika ile nyumba uliyotukuta, amejenga mwenyewe ile nyumba kwa mshahara anaolipwa huko kazini kwake. Erick ni kijana mkimya sana, ninaweza sema tabia ya ukimya alizaliwa nayo kwa maana yupo hivyo tangu akiwa mtoto. Ukimya wake umemfanya awe na marafiki wachache sana, lakini rafiki yake mkubwa ni John Dukuu. Erick na John ni marafiki walioshibana haswa kiasi kwamba Erick alivyopata hii kazi iliyomletea matatizo alimfanyia mpango John, na kwa bahati nzuri naye aliajiriwa kama utingo katika gari analoendesha Erick. Erick anaipenda sana familia yake pengine kuliko kitu chochote kile. Hayo ni machache ambayo ninaweza kuelezea kuhusu mwanangu” Mzee Mboto alisema.
“Je Erick alishawahi kufanya kosa lolote lile ambalo likampeleka katika vyombo vya dola?” Hannan aliuliza.
“Kwakweli sikumbuki. Sikumbuki kabisa kama Erick alishawahi kupelekwa kituoni kwa kufanya kosa lolote lile. Hajawahi kufanya kosa lolote, na leo ndio kwa mara ya kwanza anapelekwa kituoni” Mzee Mboto alijibu.
“Sawa mzee Mboto, nashukuru sana kwa ushirikiano wako, ninaomba twende ndani, nina maswali kidogo ya kumuuliza mke wa Erick” Hannan alisema.
“Sawa binti yangu, ila ninaomba sana ujitahidi ili kumsaidia Erick, anateseka Polisi bila ya hatia” Mzee Mboto aliomboleza kwa sauti yake ya kizee.
“Usiwe na wasiwasi baba yangu. Endapo mtanipa nafasi ya kuweza kupata fununu juu ya waliowateka wanafunzi wa shule ya msingi Vanilla, basi ninakuahidi Erick atakuwa huru na kuendelea na majukumu yake”
Walitoka kule pembezoni mwa nyumba na kuelekea ndani, sebuleni, waliwakuta wakina mama wanne.
“Mama Adrian, kuna mgeni wako hapa” Mzee Mboto alisema huku akimwangalia mwanamke mmoja aliyekuwa amejifunga kanga huku akiwa amembeba mtoto mdogo mgongoni.
“Sawa baba, karibu sana mgeni” Mama Adrian alisema huku akifanya jitihada za kunyanyuka katika kochi la mbao.
Mama Adrian alifuata korido ndefu huku Hannan akifuata kwa nyuma. Huku akiwa anatembea macho ya Hannan yalifanya kazi ya kuzunguka huku na kule kutafuta chochote kile kitakachomsaidia katika uchunguzi wake. Hadi mama Adrian anasimama, Hannan hakuwa ameona chochote kile.
“Karibu sana mgeni” Mama Adrian alisema huku akimgeukia Hannan, alikuwa amesimama mwisho kabisa wa ile nyumba yenye korido ndefu.
“Samahani dada, mimi ninaitwa Hannan, ni askari wa jeshi la Polisi kutoka idara maalum. Nipo hapa kukuhoji mambo machache ambayo yatatusaidia katika kesi inayomkabili mumeo” Hannan alisema huku akimuonesha kitambulisho chake cha kazi alichokuwa amekishika kwa mkono wake wa kulia.
“Karibu sana” Mama Adrian alisema huku macho yake mekundu yakikiangalia kile kitambulisho alichokishika Hannan.
“Bila shaka Erick ni mumeo?”
“Ndio”
“Mna watoto wawili?”
“Ndio”
“Adrian na nani?”
“Adrian na Adriana”
“Mlioana mwaka gani?”
“Miaka mitano sasa imepita?”
“Unamjua rafiki mkubwa wa mumeo?”
“Ndio”
“Anaitwa nani?”
“John”
“Erick ana rafiki mwingine mkubwa zaidi ya John?”
“Hapana”
“Kwa siku za hivi karibuni Erick hajaanzisha urafiki na mtu mwengine yeyote?”
Mama Adrian alisita baada ya kusikia swali hilo, alimwangalia Hannan kwa macho ya mshangao kisha akajibu,”Alianzisha, lakini sidhani kama atakuwa anahusika na ...........”
“Anaitwa nani?” Hannan alimkatisha mama Adrian.
“Mume wangu alinitambulisha jina lake lakini nimelisahau”
“Alikuwa yupoje?” Hannan aliuliza huku akitoa karatasi na kalamu mfukoni kwake. Alikandamizia ukutani na kuanza kuchora kufuatana na maelezo ya mama Adrian.
“Alikuwa mrefu wastani, ana rangi ya maji ya kunde, sura yake ya duara yenye macho makubwa. Alikuwa na ndevu nyingi alizozichonga kwa mtindo wa O. Pamoja kwamba hakuwa mrefu sana lakini alikuwa na umbo lililojazia kama wabeba vyuma. Ninachokumbuka kingiiine hakuwa na nywele hata moja kichwani” Mama Adrian alielezea mwonekano wa rafiki mpya wa Erick.
“Anafanana na huyu?” Hannan alisema huku akimuonesha mama Adrian picha aliyokuwa ameichora baada ya maelezo ya mama Adrian.
“Ndiye mwenyewe!” Mama Adrian aling’aka kwa sauti kubwa huku macho yake yakionesha uwoga mkubwa. Hannan alimchora vilevile rafiki mpya wa Erick kutokana na maelezo ya mama Adrian.
“Huyu rafiki mpya akija walikuwa wanaongea nini na mumeo?”
“Kusema ukweli mimi hawakunihusisha katika mazungumzo yao, na ilionekana kuwa walikuwa hawataki hata kidogo nisikie walichokuwa wanakizungumza, maana mara kadhaa walikuwa wananyamaza kimya nikikaribia walipo”
“Hakuna neno lolote lile ulilowahi kulisikia wakilitaja katika mazungumzo yao?”
“Kwakweli hakuna” Mama Adrian alisema baada ya kuwaza kidogo.
“Vipi tabia ya Erick ilibaki ileile hata baada ya kukutana na huyo mgeni wake mpya?”
Mama Adrian alionesha mshangao mkubwa kuliko wa awali, alimwangalia Hannan huku akimshangaa, kisha alijibu kwa sauti ya kuchoka,
“Tabia ya Erick ilibadilika....”
“Ilikuwaje?”
“Kiasili mume wangu ni mkimya sana. Tabia ambayo kila mmoja anaijua kwamba anayo, lakini baaada ya kuanza kuja yule mgeni tabia ya ukimya ya Erick iliongezeka maradufu. Mara kadhaa nilimuuliza kama ana matatizo kutokana na mabadiliko hayo ya tabia lakini alisema kuwa hakuwa na tatizo”
“Amekuja hapa nyumbani kama mara ngapi huyo mgeni?”
“Mmmh amekuja kama mara tano au sita”
“Unakumbuka lini ilikuwa mara ya mwisho kuja hapa?”
“Jana usiku” Mama Adrian alijibu bila ya kufikiria.
“Amekuja tena baada ya haya matatizo yaliyompata mumeo?”
“Hajaja, pengine hajapata taarifa kama Erick yupo katika matatizo”
“Sawa, ninashukuru sana kwa ushirikiano wako. Ninaomba namba yako ya simu ili niweze kukupigia endapo kutakuwa na chochote cha ziada nitakachokitaka kutoka kwako” Hannan alisema huku akimpa simu yake mama Adrian.
Mama Adrian alichukua simu ya Hannan na kuandika namba yake ya simu, kisha alimrejeshea simu yake.
“Kwa usalama wa mumeo usimwambie mtu mwingine yeyote kuhusu huyo rafiki mpya wa mumeo” Hannan alisema wakati akiichukua simu yake.
Walirejea tena sebuleni, Hannan aliwaaga wale kina mama waliokuwa pale sebuleni ambao kwa sasa walikuwa wameongezeka, akaenda barazani na kumuaga mzee Mboto, kisha alienda kwenye gari yake, akawasha na kuondoka.
Kutoka Mbagala Kilungule alienda kusimamisha gari yake katikati ya uwanja wa Mbagala Zakheim. Aliitoa ile karatasi yenye picha ya rafiki mpya wa Erick, akatoa simu yake mfukoni na kwenda upande wa kamera, akaipiga picha ile picha. Kisha akaiingiza katika mfumo maalum wa utambuzi ili kumtambua mtu aliyopo katika ile picha. Mfumo ulianza kuzunguka.
‘Ginger Bites’ Ndio jina lililotokea chini ya picha ile, huku picha zingine mbili za huyo Ginger Bites zikionekana kwa chini.
“Ginger Bites!” Hannan alisema kwa sauti kubwa. “Ulikuwa unafuata nini nyumbani kwa Erick?” Hannan alijiuliza huku akiliingiza jina la Ginger Bites katika mfumo maalum wa kuchunguza kazi za watu.
“Hisia zangu zinaniambia kuwa haukuwa wa bure urafiki wa ghafla wa Ginger Bites na Erick” Hannan aliwaza wakati mfumo ukitafuta taarifa zaidi kuhusu Ginger Bites
Hisia za Hannan zimemuhisi vibaya mtu anayeitwa Ginger Bites, je hisia za kwako zimemuhisi vipi Ginger Bites? Tuwe wote katika mwendelezo wa TAHARUKI kutoka kwa mwandishi HALFANI SUDY.
Sent from my Infinix X655C using
JamiiForums mobile app