Riwaya: T A N Z I A

Riwaya: T A N Z I A

Willy Gamba 1

JF-Expert Member
Joined
Jan 5, 2015
Posts
352
Reaction score
377
RIWAYA: TANZIA
MTUNZI: MAUNDU MWINGIZI

SEHEMU YA KWANZA


Ilikuwa ghafla tu, Pepo kali zilipovuma karibu kila
kona ya wilaya ya Kibondo, mkoani kigoma.
Taratibu mawingu mazito yakalifunika anga kiasi
cha kuifanya saa tisa ile ya alasiri ifanane na usiku
wa manane, usiku wa kiza, usiku wa hofu.
Ingawaje ilikuwa ni msimu wa kiangazi na kwamba
ni aghalabu mvua kunyesha, lakini hakuna
aliyeipuuza dalili ya mvua ile ambayo ni mawingu.
Kilichowafanya wakaazi waogope zaidi ni jinsi giza
lilivyozidi kuumeza mwanga, maana hata kama
nd’o dalili yenyewe ya mvua, hii sasa ilizidi!
Baadhi ya wafanyabiashara wakaanza kufunga
maduka yao, wanafunzi wakikimbilia makwao, na
hata mifugo nayo ikaanza kurejea mabandani ikijua
kuwa usiku umewadia. Wale wenzangu na mimi
wenye nyumba za udongo zilizosheheni ‘mawakili’
karibu katika kila ukuta walianza ‘kudhikiri’
vyumbani mwao wakimuomba mola awasitiri…
maana bila hata ya mvua tu, kila siku ukuta
unakuuliza ‘Nikuuwe?’ sasa je ikishuka si kuta
zitageuka biskuti?
Upepo mkali uliendelea kuvuma mithili ya
kimbingunga huku baridi kali ikiwa imeshtadi
kwelikweli, cha jabu hapakuwa na mingurumo, radi,
wala manyunyu…ni upepo, Baridi na giza tu.

***
Wakati hali hiyo ya hewa ikizidi kuchafuka, katika
wilaya hiyohiyo ya Kibondo nyumba ya Bi
Masonganya binti Kalukalange ilifurika umati
mkubwa wa wana-ukoo kutoka sehemu mbalimbali. Watoto, wajukuu, vitukuu na vilembwe
wakiwa wamekusanyika kwa kukizunguka kitanda
cha chuma alipolala Bi Masonganya.
Ni wana-ukoo hao pekee ndiyo waliokuwa wakijua
siri ya hali ya hewa kubadilika ghafla katika eneo
lote la kibondo. Ni kwamba bibi na mama yao
kipenzi, Bi Masonganya alikuwa akikaribia kukata
roho baada ya kuishi kwa takribani miaka miamoja
na sitini! Kwa kawaida kifo huja ghafla tu na hakuna anayeweza kupata taarifa kabla…ila kwa
wana-ukoo hawa walikitumainia kifo cha mama na bibi yao yule.
“Yreeeeeeeew! Watemi woseeee! mizimu yoose!
Makulwa na madoto, na makashindyeee!
Mumsaidie mtu wenu.” Maneno hayo yalitamkwa
kwa sauti kali na babu mmoja aliyekuwa
amesimama pamoja na wana-ukoo wale kisha
akatoa chafya kwa nguvu na sauti kali sana!
Nje ya chumba hicho, usawa wa dirisha alikuwa
amesimama binti wa mwisho wa Bi Masonganya,
akiwa ameshika mwichi mkononi akisubiri ishara
aliyoelekezwa ili atekeleze zoezi muhimu…na ishara
hiyo ilikuwa ni ile chafya aliyoisikia ikitokea ndani.
Kitendo bila kuchelewa akauinua juu ule mwichi
aliokuwa ameushikilia, kisha akaukita kwa nguvu
chini ya ukuta ambao kwa ndani amelala mama
yake akiwa amezungukwa na wana-ukoo.
Baada tu ya kuukita mchi ule chini ya ukuta, kule
chumbani wana ukoo wakashuhudia mama yao
akihangaika kitandani kwa sekunde kadhaa huku
akikakamaa kama askari wa kikoloni akijiandaa
kupiga saluti kwa bwana wake, haikuchukua hata
dakika mbili, Bi Masonganya akanena kwa sauti
kavu ya kukoroma.
“…Akkh…wana-ngu…mme-niwe-zaa mme-ni-u-
waaa!” Hapohapo Bi Masonganya akakata roho.
Sauti za vigeregere, nderemo na vifijo kutoka kwa
wana-ukoo vilizizima chumbani humo, japo
havikuwa vigeregere vya furaha bali viashiria vya
kukamilika kwa kifo kile kilichowabidi
kukilazimisha. Laiti wangejua kilichokua
kikiwanyemelea, wala wasingenyanyua vinywa
vyao kupiga vigeregere. Lakini nd’o hivyo tena
hakuna aijuaye kesho hata mtunzi wa kalenda.
Baada tu ya Bi Masonganya kukata roho, muda
huohuo hali ya hewa ikabidilika tena, mwanga
ukarejea na upepo ukatulia kiasi cha
kuwastaajabisha wakazi wa Kibondo.

***
Sifa kubwa ya Bi Masonganya ilikuwa ni uchawi.
Uchawi uliokubuhu, aliorithishwa na marehemu bibi
yake mzaa mama ambaye kwa asili ni mtu kutoka
Kongo. Uchawi huo ulimfanya Bi Masonganya
aheshimike na kuogopwa karibu na kila mtu. Wapo
aliowaangamiza kutokana na uchawi wake, na
wapo aliowasaidia, lakini mchawi ni mchawi tu
hana muamana asilani.
Ilikuwa Bi Masonganya akaikwambia kuwa
hautoliona jua la jioni basi kimbia haraka
ukamtake radhi, vinginevyo utakufa kweli. Na hata
uwe na kesi ya namna gani endapo utamfuata
kumtaka msaada na akaamua kuivalia njuga basi
piga geuza utashinda tu. Mpaka viongozi wakubwa
serikalini wanaouhusudu ushirikina huwasili kwa Bi
Masonganya kufanyiwa ndumba.
Kuna madhila yaliwahi kumpata Jaji aliyekuwa
akisikiliza kesi ya ubakaji iliyokuwa ikimkabili
mjukuu wa Bi Masonganya aitwaye Ndoza, hiyo
nayo ikawa ni historia ya kushangaza na
kusikitisha! Ni kweli Ndoza alibaka haswa tena saa
saba mchana watu wakishuhudia dhahiri
akimng’ang’ania binti wa watu aliyekuwa akipita
na safari zake, akamvutia kwenye pagara lilikouwa
jirani na kumfanyia ushenzi. Sasa kesi ilipoonesha
dalili zote za kumuelemea Ndoza, ndipo Bi
Masonganya akaibuka na kuikingia kifua.
Akamfuata jaji, akamkanya kwa maneno makali ya
vitisho kuwa endapo ataendelea na mpango wake
wa kutaka kumfunga jela mjukuu wake basi
atakiona kilichomfanya kuku aanze kuota manyoa
mkiani…Jaji akapuuza, pengine kwakuwa naye
alikuwa amejiganga.
Siku ya hukumu sasa Jaji akiwa anaingia
mahakamani baada ya umati kufurika ndipo ghafla
walipoibuka nyuki hata wasijulikane walipotokea,
ikawa ni patashika ya nguo kuchanika kila mmoja
akitafuta njia yake. Kama Nyuki nao huwa na
kichaa, basi hawa nao walihitaji chanjo. Walikua
wanauma ovyoovyo, na wakikuuma, hayo maumivu
yake ni kama umegongwa na koboko.
Matokeo ya hila za nyuki wale ni pamoja na
mafaili yote yaliyobeba kesi ya Ndoza kupotea japo
hilo halikuwa kubwa sana. Lililoshitua zaidi ni
kitendo cha wale nyuki kumfakamia Jaji licha ya
kelele za kutaka msaada alizokuwa akipiga bila
mafanikio mpaka walipomtoa roho.
Kifo cha Jaji kwa kuumwa na nyuki mahakamani
kikazagaa kama moto wa pumba, huku kila mmoja
akijifanya ni fanani wa mkasa ule.
Kesi ya ndoza ikatulia kama maji ya mtungi.

ITAENDELEA......
 
SEHEMU YA PILI
Kifo cha Jaji kwa kuumwa na nyuki mahakamani
kikazagaa kama moto wa pumba, huku kila mmoja
akijifanya ni fanani wa mkasa ule.
Kesi ya ndoza ikatulia kama maji ya mtungi.
Kama ilivyo kawaida ya mawingu, huwa hayatandi
milele…kuna siku husambazwa na kutawanywa
kwa upepo! Na hivyo ndivyo habari ile ya kifo cha
Jaji ilivyosahaulika na kisha baadaye ikapangwa
tena upya tarehe ya kuendelea kwa kesi ya ubakaji
inayomkabili Ndoza na kukabidhiwa kwa Jaji
mwingine.
Huyu sasa naona alikuwa mwepesi kama tishu
maana kazi ya Bi Masonganya ilikuwa ni kama
kupuliza kibatali tu na kukizima kabisa. Ilitokea
kama maskhara tu, siku ya hukumu Jaji akiwa
anatoka nyumbani kwake, kwa bahati mbaya
akajikwaa na kuanguka mpaka chini, hakuinuka
akiwa hai bali alinyanyuliwa na kubebwa akiwa
maiti!
Wakati huohuo Jaji anaanguka, binti aliyebakwa na
Ndoza naye alijikwaa kama ilivyokuwa kwa Jaji!
Na wakati maiti ya Jaji inanyanyulia, na ya binti
yule naye ilinyanyuliwa tokea pale alipoangukia.
Vifo viwili, vilivyofanana japo vimetokea sehemu
tofauti kwa watu wanaohusika na kesi moja vilizua
gumzo mjini Kibondo…kesi hata ilkopotelea!
Unadhani Jaji gani asiyependa kuishi?
Yapo mengi ya kumhusu Bi Masonganya, hata
humohumo kwenye ukoo wake mbali ya
kuwasaidia pindi wapatwapo na matatizo, pia
ameshawamaliza sana watoto na wajukuu kwa
kuwachukua kichawi.
Mbali ya vimbwanga hivyo vya uchawi, pia
inasemekana Bi Masonganya alipata kumeza
‘mpigi’. Mpigi ni dawa ya mtishamba ambayo
ukiimeza basi haufi kirahisi mpaka utapishwe
kwanza dawa hiyo, vinginevyo utazeeka mpaka
ubakie kama mzoga huku ukiwa hai.
Sasa tayari Bi Masonganya alikuwa
amekwishazeeka kiasi hata cha kushindwa hata
kutembea mwenyewe, na kuwafanya wajukuu zake
kuwa wanamtoa nje kumuanika mara mojamoja…
na siku akitolewa kuanikwa, utafikiri alikuwa akitoa
sumu angani maana kama kuna wagonjwa au
watoto wadogo maeneo ya jirani, basi siku hiyo
watashinda ovyoovyo tu wakiwa ta’abani mpaka Bi
Masonganya atakaporejeshwa ndani.
Hata yeye mwenyewe Bi Masonganya alitamani
sana tu kufa sasa ili akapumzike kama kweli
atapata nafasi hiyo, lakini inasemekana kabla
hajaitapika ile ‘mpigi’ pia kuna fununu kwa
nduguze kuwa alitaka kwanza aache amemrithisha
mtu mmoja uchawi wake wote kabla hajafa…hilo
nd’o lililowagutua wana-ukoo na kuamua
kumsaidia kufa mapema kabla hajarithishwa mtu
mwingine huo mzigo wa ulozi. Ndipo akaitwa
mtaalamu ambaye aliusuka mpango mzima wa
kumuondoa duniani bi mkubwa yule. Hivyo ule
mwichi uliokitwa chini ya ukuta baada ya maneno
yale ya kimila yaliyofuatiwa na chafya ya bila
kunusa ugoro ulikuwa nd’o pigo la mwisho la
kummaliza, na kweli wakammaliza…sasa kwanini
wasipige vigeregere?
Ambacho hawakukikumbuka ni kimoja tu, kwamba
Bi Masonganya amekufa na ‘mpigi’ yake kifuani…
hawakuijua hekaheka yake.
***
Baaada ya taarifa kusambaa kila kona kuwa Bi
Masonganya amefariki, kila mmoja alifurahi. Ndugu
kutoka sehemu mbalimbali wakajumuika kwa ajili
ya maziko. Ulikuwa ni msiba wa kimila zaidi,
wafiwa wote walipakwa pemba usoni na ilikuwa ni
marufuku kwa mfiwa yeyote kulia. Na katika
kipindi chote maiti ikiwa ndani, palikuwa na ngoma
maalum ikipigwa taratibu bila kuzimwa, endapo
mpigaji wa ngoma akichoka basi anampasia aliye
jirani yake naye anaendelea kuipiga mpaka
atakapochoka na kumpa mwingine aendeleze.
Siku ya maziko ilipowadia ndipo kikaibuka
kizaazaa kipya, ndugu walipoingia chumbani ili
kuubeba mwili wa marehemu, wakaikuta maiti
ikiwa imefumbua macho!
TOBAA!
Ilikuwa ni mpishempishe kila mmoja akigombea
mlango wa kutokea…ilikuwa ni hali ya ajabu na
kuogofya japo kwa wajuvi wa mambo waliitegemea
hali ile.
“Hebu kaeni chini tusikilizane…” aliongea mzee
mmoja aliyetapakaa mvi karibu robo tatu ya
kichwa chake. Mzee huyo ni kaka wa Bi
Masonganya aitwaye mzee Mtandi bin
Kalukalange. Umati ukamsogelea na kumsikiliza,
kisha akaendelea “…Iko hivi, haya ni mambo
makubwa lakini ni ya kawaida hasa anapokufa
kiongozi mkubwa wa kimila kama Bi Masonganya…
hivyo kuna mambo yanarekebishwa na wakubwa
kisha kila kitu kitatengemaa na sote tutakwenda
malaloni kumsitiri bi mkubwa, cha msingi ni utulivu
wenu tu.” Akamaliza kuzungumza babu yule.
“Ni mambo gani hayo yanayorekebishwa na
wakubwa huko ndani?” Aliuliza mmoja wa majirani
waliojumuika msibani pale “…Na ni wakubwa gani
hao?” akaongezea huku akimtazama jirani
mwenziye.
“Mtoto yasiyokuhusu waachie baba na…”
“Na mama..” Wakaachia kicheko cha kimbea
kilichokatizwa na majibu ya swali lao kutoka kwa
Bi mkubwa mmoja aliyebarizi pembezoni mwa
mpera.
“Kuna kitu alimeza kitambo kirefu sana, hivyo bila
ya kutapishwa itakuwa kama mchezo…atafumbua
macho kila atakapokaribia kupelekwa kuzikwa, na
hao wakubwa waliotajwa ni wachawi magwiji nd’o
wanasubiriwa kama wataweza kumtapisha!”
“Heh…makubwa!”
“…madogo yana nafuu.”
“Hivi kuna gwiji wa uchawi kuliko Bi
Masonganya?”
“Avumaye baharini ni Papa, na wengine pia wamo…
magwiji wapo japo hawajavuma kama yeye!”
“Sasa je kama watamzika hivyohivyo akiwa macho
itakuwaje?” mpambe mwingine alisaili.
“unataka wapitiane ukoo mzima kama kuku wenye
mdondo? Chezea wachawi wewe!”
“Na ikitokezea hao magwiji wakashindwa
kumtapisha, itakuwaje jamani?”
“Hapo nd’o watakapocheza naye makida.”
Saa moja baadaye, aliwasili Bi Kibena akitokea
maeneo ya Kakonko. Huyu alitumainiwa kuwa
angeweza kumtapisha Bi Masonganya ile ‘mpigi’
aliyomeza ili akazikwe maana Bi Kibena naye ni
kiboko kwa uchawi. Baada ya kusalimiana na
wafiwa aliingia mpaka chumbani ilipolala maiti na
kuwaamuru watu wote watoke nje, walipotoka tu
akaanza vimbwanga vyake!

***Mnh! Haya Bi. Kibena...una vimbaga gani zaidi?
ITAENDELEA....
 

Attachments

  • 1422634384344.jpg
    1422634384344.jpg
    39 KB · Views: 334
SEHEMU YA TATU

Saa moja baadaye, aliwasili Bi Kibena akitokea
maeneo ya Kakonko. Huyu alitumainiwa kuwa
angeweza kumtapisha Bi Masonganya ile ‘mpigi’
aliyomeza ili akazikwe maana Bi Kibena naye ni
kiboko kwa uchawi. Baada ya kusalimiana na
wafiwa aliingia mpaka chumbani ilipolala maiti na
kuwaamuru watu wote watoke nje, walipotoka tu
akaanza vimbwanga vyake!
Laahaullah!
Kilichomkuta Bi Kibena alikijua yeye na Mungu
wake, watu walisikia kukurukakara ya haja
ikiendelea mle chumbani mpaka ikabidi wafungue
haraka mlango. Ndipo wakamkuta bi kibena akiwa
kama mchawi aliyeenda kucheza mahepe kwenye
nyumba iliyozindikwa na hatimaye akaya-bhula…
haja kubwa na ndogo vilihitimisha kifo cha bi
Kibena alipofikishwa nyumbani kwake!
“Jamani ndugu wafiwa na majirani, maziko
yameakhirishwa mpaka hapo mtakapotangaziwa
vinginevyo.” Sauti ya Mzee Mtandi ambaye ndiye
msimamizi wa msiba ilihitimisha na watu wote
kusambaa.
Kifo cha Bi Masonganya kilijizolea umaarufu
kutoka kila pembe ya mkoa wa Kigoma huku kila
mmoja akiwana mshawasha wa kutaka kujua nini
hatma yake…ikawa kama mchezo sasa, haipiti japo
saa moja bila ya Bi Masonganya kufumbua macho
japo vipimo vyote vya waganga na hata madaktari
wa kawaida walioshirikishwa vilionesha kuwa
amekwishafariki.
Zikapita takribani siku tatu bila ya mwili wa Bi
Masonganya kuzikwa, huku ndugu wakiswampa
kila uchao kutafuta waganga wa kulitatua tatizo
lililoikumba familia yao, kila mganga aliyefuatwa
alipokaribia tu na nyumba ilimo maiti aliishia nje
na kuingia mitini! Haikuwa kazi rahisi.
Siku ya tano, mwili wa marehemu ukiwa
umekwishaanza kutahayari ndipo wana-ukoo
walipofanikiwa kumpata mganga maeneo ya vijiji
vya mbali kidogo tokea Kibondo mjini.
Ilichukuwa karibu saa saba kutokea huko vijini kwa
mwendo wa gari mpaka kufika hapo Kibondo mjini.
Wakiwa bado hawajafika nyumbani ulipo msiba
ghafla mkwara wa Babu-mganga ukaanza,
akapandisha mashetani yake kichwani na kuanza
kufanya vurugu kubwa ndani ya gari. Alipotulia
akamuamuru dereva asimamishe gari kisha yeye
akashuka na kikapu chake kichafu na kilichochakaa
kama nguo zake alizozivaa…wafiwa waliomuendea
nao wakashuka.
“Vipi babu?”
“Mizimu imenikatalia kwenda kwa gari huko
nyumbani kwenu…yaonekana huyo aliyekufa
hakuwa mtu wa kawaida asilani.” Wafiwa
wakaangaliana, kisha mmoja akamsaili tena.
“Kwahiyo tunafanyaje?”
“Hakuna cha tunafanyaje hapa…twendeni kwa
miguu tu!”
Haikuwa mbali sana na nyumba, hivyo walitembea
kwa karibu nusu saa wakawasili na kupokelewa na
ndugu na majirani walioanza kufurika.
“Jamani mi’ si mkaaji hapa…” alianza kuongea
mganga. “…nataka kufanya kazi yangu haraka
iwezekanavyo ili niondoke zangu.”
“Sawa babu karibu ndani,” Alijibu mtoto wa kiume
wa marehemu huku akifungua mlango mkubwa wa
mbele na kumpisha Babu-mganga aingie ndani.
“Hapana mi’ sipitii mlangoni, naomba mniruhusu
nipande juu ya bati la nyumba yenu kisha nipitie
huko kwa juu.”
Heh!
“Sasa utapitiaje kwa juu babu?”
“N’tafumua bati pamoja na singibodi kama iko
kisha n’taibukia chumbani kwa mtuhumiwa
wenu.”Ilikuwa ni mzaha mwingine msibani hapo,
ila kwakuwa walikuwa wanashida wakamkubalia,
Babu akapanda juu ya nyumba huku watu
wakimshangaa na baadhi ya wafiwa wakitangulia
chumba chenye maiti.
Watu walimshuhudia babu akipanda mpaka juu na
kufumua bati kisha akidumbukia kwa ndani kiasi
cha kuachia kishindo kizito…nyumba nzima
ikatulia, walio nje wakisubiri taarifa ya kitakachojiri
huko chumbani.
Zilipita dakika takribani thelathini nyumba ikiwa
kimya kila mmoja akijiandaa kutimua mbio endapo
maiti itazua songombingo. Haikuwa hivyo,badala
yake zilisikika sauti za vigeregere na shangwe
kutokea chumbani, ikiwa ni ishara ya kazi
kukamilika. Bi Masonganya alitapishwa mpigi yake.
Haikuchukuwa muda mrefu Babu akatoka akiwa na
kikapu chake mkononi akifuatiwa na wafiwa.
Akaaga na kuondoka zake.
Bi Masonganya akaandaliwa na kwenda kuzikwa
kimila, akiwa ameviringishwa ndani ya ngozi ya
Ng’ombe mweusi.
Msiba ukaisha.
Majirani wakasambaa, na wafiwa wakarejea kwao
kumalizia siku tatu zamsiba kabla na wao
hawajasambaana!
***
“Mamaa…mamaa.” Kaguba alikuwa akimgasi kwa
kumuita mama yake wakati kikao cha kumalizia
msiba wa Bi Masonganya kikiendelea. Kaguba ni
mjukuu wa marehemu Bi Masonganya, mtoto wa
kike wa mwanaye wa pili kutoka mwisho.
“Mamaaa…mama.” Kaguba aliendelea kumgasi
mama yake aliyekuwa amempakata miguuni.
Mama Kaguba alimpuuza mwanaye akiamini hana
jipya pengine na umri wake kuwa mdogo. Kaguba
alikuwa ni mtoto wa miaka takribani minne tu.
“Mama ujue mi’ n’namuonea huruma sana
ma’mdogo Nyanzala,” alisema Kaguba na kufanya
kikao kipige kimya kidogo huku watu wote
wakimuangalia kama kituko vile kwa ile kauli yake
aliyoitoa baada ya kuona mama yake hamjibu
chochote akiendelea kufuatilia kikao. Wakajikuta
wote wamecheka!
“Unamuonea huruma ya nini mama?” Mama
Kaguba alimuuliza kimzaha Kaguba wake huku
wengine wakimsikiliza.
“Hivi kwanini sasa ma’mdogo Nyanzala alikubali
kupiga mwichi chini ya ukuta ili amuue bibi?”
alisaili mtoto Kaguba na kuwaacha midomo wazi
wote mle ndani.
Haikuwa jambo la kawaida kwa mtoto mdogo wa
umri wa Kaguba kutambua jambo lile lililofanyika
kisiri. Na hata wakati yote hayo yalipokuwa
yakitendeka yeye(Kaguba) alikuwa uani huko
akicheza na wenziye, sasa ameyajuaje haya.
“Shauri yenu, mjue wamekasirika sana huko.”
Kaguba aliropoka tena.
Ama!
“We’ Kaguba, akina nani hao wamekasirika?
amekwambia maneno hayo?” Mzee Mtandi ambaye
ni kaka wa marehemu alimsaili mjukuu wake kwa
kihoro kikubwa.
“Eeenh…nyie ngojeni tu! Kesho mtaona tu
ma’mdogo Nyanzala naye anakufa!”
SEHEMU YA PILI
Ukumbi mzima ulizizima kwa hofu na mashaka.
Hali ile haikuwa ya kawaida hata kidogo.
Walipojaribu kumdodosa Kaguba wao tena
hakuendelea kusema chochote cha maana zaidi ya
kubwabwaja maneno yasiyo na maana yoyote,
maneno ya kitoto tu!
Raha ikawaisha, kikao kikafa kimyakimya!
Nyanzala alichanganyikiwa maradufu, hofu kuu
ilimvaa, mishipa ya shingo ikawa inampwita kama
moyo wa chura. Kila mara alikuwa akilia tu
akihofia kifo alichobashiriwa na mtoto wa dada
yake. Ndugu walijaribu kumfariji na kumsihi kuwa
yale yalikuwa ni maneno ya mtoto tu ambaye
pengine ilitokezea akawasikia wakiongelea juu ya
mpango wao huo. Haikumuingia akilini kamwe!
Siku hiyo walishinda ovyoovyo tu, chakula
hakikulika. Hatimaye usiku ukaingia na kuzidisha
simanzi kwa wanafamilia. Nyanzala akiogopa kufa,
mama Kaguba naye akiogopa hata kulala na
mwanaye, huku ndugu wengine wakihofia balaa
inayotaka kuukumba ukoo wao. Usingizi ukaota
mbawa. Lakini hali hiyo ya mang’amng’am iliduma
kwa muda tu. Baadaye usingizi ukawapitia.
Siku hiyo usingizi ulikuwa mzito kwa karibu kila
mmoja wa wanafamilia wale, kama ungebahatika
kukatiza nje ya nyumba yao kwa usiku ule,
ungedhani kuna helkopta zinajiandaa kuruka kwa
jinsi walivyokua wakikoroma. Walilala fofofo!
Kilichowashitua asubuhi na mapema ni TANZIA
(Tangazo la kifo) iliyokuwa ikinadiwa kutoka katika
spika kubwa za msikitini. Haikuwa jambo la ajabu
sana kusikia Tanzia kutoka katika spika za
msikitini maana huo ni utaratibu wa kawaida kwa
waumini wa dini zote kubwa kupashania habari
kupitia spika hizo bila kujali tofauti ya dini zao, ila
hii ilikuwa ni taarifa ya kushitua kwao.
“…ifuatayo ni Tanzia, familia ya hayati Bi
Masonganya wa kilogho, Kibondo inasikitika
kutangaza kifo cha mtoto wao, Bi Nyazala.
Kilichotokea usiku wa kuamkia leo…maziko
yatafanyika leo saa kumi Alasiri.” Sehemu ya
Tanzia hiyo ilisikika ikinadi.
Heeh!
Nyanzala amekufa?
Familia nzima ilikumbwa na mshituko na woga
kutokana na tangazo hilo. ukizingatia kuna hadhari
ambayo ilikuwa ni kama Tanzia kabla ya tukio
waliyopewa na mtoto Kaguba na sasa kimeibuka
kioja kipya kwamba tangazo limenadiwa kuhusu
kifo cha Nyanzala bila ya hata wao kama ndugu na
wahusikawa karibu kujua lolote!
“Mama Kaguba…” Aliita Mzee Mtandi kwa sauti ya
mashaka na wahka. “…Mama Kagubaaa..” aliita
tena Mzee yule kutokea chumbani kwake.
“Abee Mjomba,” Alijibu Mama Kaguba.
“Umesikia hilo Tangazo la kifo?”
“Kumbe nawe’ umelisikia?” Jibu hilo la mama
Kaguba liliwafanya familia nzima ishituke, kumbe
kila mmoja kutokea chumbani kwake alilisikia
vyema Tangazo lile. Wote wakatoka wakiwa bado
na mang’amng’am ya usingizi mpaka sebuleni,
wakautwaa mlango wa chumba cha Nyanzala na
kuugonga zaidi ya mara tatu bila kujibiwa.
Hofu ikiwazidia!
Hapakuwa na la ziada, wakauvunja mlango kisha
wote wakakivamia kitanda cha Nyanzala na
kumkuta akiwa amejilaza kiubavu huku roho
ikionesha dalili kuwa iliuacha mwili ule karibu hata
saa tano mbele. Alitulia tuli akiwa amepoa kabisa!
Vilio vikalipuka. Ndugu walilia kwa maombolezo na
vihoro vya hali ya juu, hakika msiba ule wa
maajabu uliwaumiza sana.
Haya sasa Nyanzala ni kweli amekwishaaga dunia
lakini sasa kwanini kifo chake kilibashiriwa na
mtoto mdogo Kaguba? Na kwanini Tangazo la kifo
(Tanzia) linadiwe huko kwenye vipaza sauti ilhali
wao kama wanafamilia waliolala naye nyumba
moja wakiwa hawajapata taarifa ya kifo hicho?
Maana kwa kawaida wao kama ndugu ndiyo
walipaswa kupeleka taarifa za msiba wao msikitini
ili watangaziwe watu…hapakuwa na majibu ya
kutosha zaidi vilio vikali vilivyogubikwa na hofu na
mashaka.
Majirani kama ilivyo kawaida yao wakajaa tele
kama pishi la mchele wakishirikiana bega kwa
bega mpaka walipohitimisha safari ya mwisho ya
Nyanzala. Familia ilijitahidi kuficha ukweli
uliokigubika kifo kile kuwa ulibashiriwa na Kaguba,
ila hawakuwa wapuuzi wa kulipuuzia jambo lile
zito. Wakaendelea kumuandama kwa maswali
Kaguba huku wakimtishia kumchapa viboko lakini
walaa hakusema lolote la maana, ni kama hakuwa
yeye aliyeropoka maneno mazito juzi yake tu. Na
hata walipowakabili viongozi wa msikitini kuhusu ni
nani aliyepeleka tangazo lile bila ya wao kuhusika?
Majibu yalizidi kutatanisha, hata wao hawakumjua
aliyetangaza maana japo walikuwa wameufunga
msikiti lakini waliweza kusikia tangazo hilo
likitokea katika spika hizo…na kweli sauti ya
aliyetangaza haikuwa ile ya siku zote.
Utata!
Hatimaye katika hali hiyohiyo ya sintofaamu,
Nyanzala akazikwa…na shughuli za msiba
zikaendelea kama ilivyo ada.
“Ebyomunyumba tebi totolwa!” Mzee Mtandi
aliwasihi wanawe kwa lugha ya Kinyankole. Wote
walimuelewa kwakuwa alipendelea sana kulitumia
neno hilo kwenye muktadha wa namna ile. Msemo
huo ulimaanisha kwamba ‘Ya vyumbani,
hayajadiliwi hadharani.’ Hivyo siri zilizogubika kifo
hicho wasiweke hadharani.
***
Siku moja ndugu kadhaa wa familia ya Bi
Masonganya wakiwa wameketi nje ya nyumba yao
kwa upande wa barabarani huku wengine wakiwa
wameketi juu ya viti na wengine juu ya daraja
kubwa la maji linalotenganisha nyumba na
barabara kubwa, ikiwa ni siku kadhaa tangu
wamalize msiba wa ndugu yao kipenzi, ndipo
wakasikia sauti iliyowashitua sana…sauti ya
mwanamke anayeonekana kuchoka sana.
“Uuuh…uuh ja-maaa-ni ni-sa-me-he-ni, msi-ni-pi-
ge…nipelekeni taratibu.” Ilikuwa ni sauti
waliyoifahamu fika, sauti ya ndugu yao kipenzi
hayati Nyanzala. Sauti hiyo ya kulalamika kutoka
kwa Nyanzala ilitokea usawa wa chini ya lile
daraja kubwa walilokuwa wameketi juu yake huku
wamening’iniza miguu yao kwa starehe. Wakiwa
wameduwaa ndipo tena ikafuatia sauti nyingine
wasiyoifahamu ikimkemea Nyanzala kwa
ghadhabu.
“Tulia mbwa we’.. tembea haraka…” Sauti hiyo
ilifuatiwa na milio ya mijeredi ya nguvu kama kuna
ng’ombe au punda anayeadhibiwa.
“Uwiiii…naku-faa.. jamani mtaniua, nioneeni
huruma jamani.” Baada ya hapo familia nzima
ilipitiana mieleka, wa huku, kule! Na wakule huko!
Wote wakigombea mlango ili waingie ndani. Hakika
hofu iliwavaa.
Yaani wamemsikia hivihivi ndugu yao
waliokwishamzika, akilia kwa uchungu huku
akiteswa sana, hakika siku iliwaharibikia. Kilio
kikaanza upya, hata wanaume walishindwa kujizuia
nao wakawa wanalia. Inaonekana hao
wanaomtesa Nyanzala waliamua kwa makusudi
kabisa kuja kumtesa mbele yao wakiwaoneshea
umwamba wao. Hawakua na la kufanya,
wakanyamazishana na kwenda kulala! Vitanda
vilikuwa vichungu.

***
“Heeh! NYA-NZALA?” Mama Kaguba aliyekuwa
akipika uani alihamaki baada ya kumuona Nyazala
akiingia mle uani akiwa mchovu, mchafu, hoi bin
ta’aaban.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA NNE

Yaani wamemsikia hivihivi ndugu yao
waliokwishamzika, akilia kwa uchungu huku
akiteswa sana, hakika siku iliwaharibikia. Kilio
kikaanza upya, hata wanaume walishindwa kujizuia
nao wakawa wanalia. Inaonekana hao
wanaomtesa Nyanzala waliamua kwa makusudi
kabisa kuja kumtesa mbele yao wakiwaoneshea
umwamba wao. Hawakua na la kufanya,
wakanyamazishana na kwenda kulala! Vitanda
vilikuwa vichungu.

***
“Heeh! NYA-NZALA?” Mama Kaguba aliyekuwa
akipika uani alihamaki baada ya kumuona Nyazala
akiingia mle uani akiwa mchovu, mchafu, hoi bin
ta’aaban.
“Abee dada.”
“Ni wewe kweli?”
“Ni mimi dada yangu, nimepigwa sana, hapa sina
hali.”
“Enhee Ulikuwa wapi kwanza? Na ninani huyo
aliykupiga hivi? Mbona umeumia hivi jamani
mdogo wangu?” Maswali mfululizo yalimtoka
mama Kaguba.
“Nilichukuliwa kwa Binti Sambayu nd’o nimewekwa
huko, napigwa sana na kupewa kila aina ya
mateso!”
“Heeh! Binti Sambayu?” Mama Kaguba alishangaa
kusikia kumbe siku zote zile Nyanzala alikuwa kwa
Binti Sambayu japo hakuelewa kuwa kwanini Bi
mkubwa yule amchukue ndugu yao na kumtesa
vile. Binti Sambayu ni mdogo’ake na hayati Bi
Kibena, yule mchawi aliyeshindwa kumtapisha
mpigi hayati Bi Masonganya mpaka naye kifo cha
kidhalili kikamkumba.
“Sasa kwanini anakutesa kiasi hiki?”
“Anasema kuwa mi’ nisingeshiriki kumuua Bi
Masonganya nisingesababisha ndugu yake akafa
kifo cha fadhaa namna ile hivyo anamalizia hasira
zake kwangu…sasa leo kuna kazi alinipa ya
kufyeka ile michongoma inayozunguka nyumba
yake, nilipofika karibu na kule chooni kwake
nikaangusha upanga niliokuwa nikiutumia kufyekea
majani, nilipouangalia chini sikuuona kabisa ndipo
akaja yeye mwenyewe na kuanza kunipiga sana na
kunichoma na vijinga vya moto…akaniambia
niondoke haraka nije kuwaambieni kuwa anataka
upanga wake hivyo ninyi mumlipe Laa sivyo
atanitesa sana na hata ikibidi kumuua mtu
mwingine humu ndani.” Nyanzala alikuwa akiongea
huku akilia kiasi cha kumfanya mama Kaguba naye
alie sana kwa uchungu wa mdogo’ake.
“Sasa mbona umevaa ndala mguu mmoja?” Mama
Kaguba alimsaili mdogo wake baada ya kumtupia
jicho mguuni.
“Wakati nakimbia kipigo cha Binti Sambayu nd’o
nikaangusha ndala moja kulekule nyumbani kwake,
nyuma ya choo nilipokuwa nikifyeka michongoma
yake…Dada acha mimi niondoke nisije kufuatwa
tena huku ikawa balaa jingine.”
“HA-PA-NA Nyanzala, usiondoke tafadhali,watak
uua huko mdogo’angu..” Kabla mama Kaguba
hajamilizia sentensi yake, tayari Nyanzala
alikwishatoweka mbele ya upeo wa macho yake.
“NOOO, NYANZALAAAAAA, USIENDE HUKOOOO.”
Sauti kali aliyoitoa mama Kaguma nd’o ikamtoa
usingizini, na kujikuta akiwa kitanda amelala.
Kumbe ilikuwa ni ndoto tu.
Sauti yake hiyo iliwafanya karibu nyumba nzima
washituke, wote wakihamaki kumsikia ndugu yao
akiweweseka kwa kumtaja marehemu.
Wakamkimbilia chumbani mwake ambapo
walimkuta ameketi juu ya kitanda, akihema kwa
kasi sana kama aliyekimbizwa.
“Nini tena mama Kaguba?” alisaili dada yake na
mama Kaguba.
“Nimeota Ndoto…mbaya sana!”
“Ndoto gani hiyo?” Kabla mama Kaguba hajaanza
kusimulia ndoto yenyewe. Ndipo Kaguba aliyekuwa
ameshaamka akaingilia kati kama kawaida yake.
“Halafu huyu ma’mdogo Nyanzala tatizo lake ni
kiburi sana, shauri yake watamuua bure…ye’
ameambiwa awaambie tu mumlipie upanga wa
watu alioupoteza halafu ye’ anakuja kusema
mpaka hayo mambo mengine ya kuteswa na Bi
Kibena. Wakimsikia shauri yake tuu.”
Laah!
Damu zikawasisimka wote mle chumbani, hakuna
aliyeamini kusikia tena maneno ya mtoto Kaguba.
Ikabidi wamgeukie mama Kaguba aliyepigwa na
Butwaa kuona mwanaye anasimulia kitu ambacho
amekiota yeye. Hapo ndipo akajua kuwa ile
haikuwa ndoto ya kawaida na pia sasa ikazidi
kuwadhihirikia kuwa Kaguba si mtu kawaida. Kwa
hofu na kihoro cha hali ya juuakaanza kuwasimulia
ndoto aliyoota, kila moja alihisi mwili ukimfa ganzi
kwa woga.
Hapakulalika tena mapa kulipopambazuka.
Walijaribu kumbana sana Kaguba bila mafanikio.
Walipoona jitihada zao zimeshindikana ndipo
wakakubaliana watafute mganga awasaidie.
“Jamani pamoja na kuwa mmependekeza kuwa
twende kwa waganga ila mi’nina rai moja…”
alinena Mzee Mtandi. “…Tusilikalie kimya jambo
hili la kuteswakwa ndugu yenu…”
“Mjomba, si nd’o tunataka kumleta mganga
kwakuwa hatujakubali kulikalia kimya hili!” alijibu
kwa haraka bwana Kungurume, mtoto wa kiume
wa hayati Bi Masonganya.
“Sina maana hiyo…” wote wakamgeukia mjomba
wao ili wajue ni nini azma yake hasa. “…nashauri
asubuhi hii tukanunue upanga mpya kisha
tumfuate bila uoga huyo binti Sambayu
tukamkabidhi ili aache kumtesa mtoto wetu.”
“Aah mjomba hiyo haiwezakani kabisa, hivi hata
huyo bibi si atatushangaa kuyabeba mambo ya
kwenye ndoto halafu tukampelekee yeye!” Alipinga
Kungurume.
“Na tutanzia wapi sasa kufanya hivyo jamani?
Tutaonekana vituko..” Aliongezea Kabinga, mjukuu
wa hayati Masonganya.
“Mnaona haiwezekani eeh? Lakini nachowaambieni
mimi ni kwamba hii siyo ndoto ya kawaida bali ni
ujumbe maalumu tuliotumiwa na kama mko radhi
kuona ndugu yenu anaadhirika kila siku haya
shauri yenu…mi’ mwenzenu nimekuwa zamani
nimeona mambo mengi sana. Waswahili wanasema
Awashwaye, ndiye ajikunaye…ni lazima tujikune
wenyewe!” Rai hiyo ilikuwa ngumu sana ila baada
ya majadiliano ya kina, na kutokana na heshma na
imani waliyonayo wanafamilia kwa mjomba na
babu yao mzee Mtandi, waliafikiana.

***
Nje ya nyumba ya Binti Sambayu walisimama watu
watatu; Mama Kaguba, Mzee Saadallah, na
Kungurume wakiwa na upanga wao mkononi. Ila
kabla hawajaingia wakawa wanastaajabu kuona ni
kweli michongoma ilikuwa inaonekana kufyekwa
siku si nyingi,bila shaka nd’o kazi aliyokuwa
akiifanya Nyanzala.
Roho ziliwachinyota sanakwa uchungu.
Wakapatwa na wazo jipya, kabla ya kuingia ndani
wakazunguka nyuma ya choo walipotajiwa na
Nyanza kupitia ndoto ya mama Kaguba.
Hamaad!
Wakaikuta ile ndala moja ya mguu wa kushoto
ambayo ya kulia yake ilikuwa imevaliwa na
Nyanzala kule ndotoni. Kufikia hapo sasa
hawakuwa na pingamizi kuwa Nyanzala hakufa
kamwe, na kwamba anateswa na Bi mkubwa yule.
Wakabisha hodibaada ya kuutwaa mlangowa
kuingilia ndani kwa Binti Sambayu, wakakaribishwa
na kuingia ndani. Wakamkuta Bi mkubwa yule
mweusi kama pampu mpya akiwa ametuna juu ya
kiti cha uvivu akiwa ameliatamia jiko lake la mkaa
akiota moto licha ya joto kali lililotamalaki karibu
Kibodo nzima.Kwa jinsi alivyousokota uso wake
kwa ghadhabu na ule mdomo alivyouvuta kama
Ndomolomo hakika kama ungepata nafasi ya
kumtupia jicho mara moja, usingekuwa na hamu
ya kumtazama kwa mara ya pili.
Wakamsalimu na kuketi.
“Mama siye tumekuja tunaomba utupokee, na
tunaomba utuwie radhi kwa hili kama tutakosea.
Tumepoea salamu zako kutoka kwa Nyanzala
kuwa kuna upanga wako aliupoteza hivyo
unamuadhibu sana…tumeleta upanga mpya,
tunaomba sana mama yetu uupokee na umpe
ahueni binti huyo ili apumzike japo kidogo.” Mzee
Mtandi aliongea kwa niaba ya wenziye.
Kikapita kimya cha kama dakika moja hivi! Mzee
Mtandi akainuka na kumkabidhi Binti Sambayu
upanga ule mpya.
Bila aibu wa soni, Binti Sambayu akaupokea
upanga ule kisha akainuka na kuelekea naousawa
wa chumba chake ambacho kimefunikwa gunia
zito kama nd’o pazia. Akapotelea humo.
“NIMEWAELEWA, MNAWEZA KWENDA.” Sauti kali
ya binti Sambayu ikitokea kule chumbani iliwaijia
mpaka pale sebuleni walipoketi. Wakatazamana
kisha Mzee Mtandi akajibu kwa nidhamu.
“Ahsante bi mkubwa, tunakwenda.” Hawakujibiwa.
Wakasimama na kuondoka kimyakimya mpaka
nyumbani kwao ambako walizua kilio kipya,hakika
ilikuwa ni simanzi kubwa kwao.

SEHEMU YA TATU

Baada ya siku kadhaa kupita bila mauzauza yoyote
kuwakuta ndipo wakaketi kikao tena ambapoKwa
kauli moja wakaafikiana kuwa wamuendee Babu
Gao, yule mganga bingwa aliyemtapisha ‘mpigi’
hayati Bi Masonganya. Wakajiteua baadhi na
kumfuata Babu Gao ambaye aliwakubalia ombi lao
la kwenda huko kwao. akawaahidi kuwa
angekwenda kesho yake hivyo wao warejee tu
Kibondo mjini.
Ndugu waliokuwa wakiishi mbali na Kibondo
walishindwa hata kuondoka tena kutokana na si tu
vimbwanga vya mtoto wao, Kaguba bali msiba
mpya wa ndugu yao Bi Nyanzala. Japo watoto wa
mzee Mtandi waishio Kigoma, wao iliwabidi
kuondoka kutokana na majukumu ya ajira zao.
Wafiwa waliobaki wkiwa hapo nyumbani ndipo
bingwa akawasili, Babu Gao akiwa na kilekile
kikapu chake japo safari hii aliingilia mlangoni
tofauti na awali.
“Karibu sana bwana mkubwa!” Mzee Mtandi kama
kiongozi wa familia alimkaribisha Babu Gao, wakati
huo wanafamilia wote wakiwa wamejumuika
pamoja hapo sebuleni.
“Karibu…ahsante, karibu…ahsante,” alijibu Babu
Gao kwa mkwara na mbwebwe za kiganga huku
akitoa dawa zake na kuanza kumwaga huku na
kule ikiwa kama ni kinga yake na familia yote
katika muda atakaokuwa hapo.
Baada ya utulivu, mzee Mtandi alitaka kutoa
muhtasari wa kilichojiri hapo nyumbani lakini Babu
Gao akamzuia na kuanza kuongea.
“Kwanza poleni sana kwa msiba mpya na kila
lililotokea…jana usiku sikulala kabisa ilinibidi
kwanza niyaangalie haya mambo yenu kwa jicho la
mwewe ili kabla ya kuja huku niwe ninajua cha
kuwaelezeni…” alianza kutiririka Babu Gao. “…najua
nyote mlifurahia kuwa Bi Masonganya amekufa
akiwa hajamrithisha yeyote uchawi wake, hapo
ndipo mlipokosea…alikwishamrithisha mtu siku
nyingi, na mtu mwenyewe mwenyewe mnaye
humuhumu ndani...” Wakatazamana wanafamilia
kwa macho ya mashaka huku kila mmojaakimhisi
mwenziye. Babu Gao akaendelea tena kufunguka.
“Aliyerithishwa uchawi ni huyo mtoto wenu
Kaguba!”
Loohsalalee!
“KA-GU-BA?...haiwezekani! amewezaje kumrithisha
mtoto mdogo kama huyu?” alijibu kwa wahka na
kihoro mama Kaguba.
Ukumbi mzima ukatulia na kumtupia macho Babu
Gao ili kumsikia akijibu swali pingamizi kutoka kwa
mama Kaguba.
“Hilo ni jambo la kawaida sana kwa wachawi
wengi tu duniani kuwarithisha vitunga vyao watoto
wadogo kutokana na ukubwa wa uchawi
wenyewe…kama uchawi ni mzito sana hulazimika
kumkabidhi mtoto mdogo kwakuwa hatoukataa,
tofauti na mtu mzima ambaye anaweza kuogopa
masharti yaliyomo ndani ya vitunga hivyo vizito
vya uchawi…” Aliongea kwa utulivu mkubwa Babu
Gao kisha akatulia ili maneno yake yakite katika
vichwa ya wateja wake, halafu akaendelea tena “…
Iko hivi kama kuna mchawi mkubwa katika ukoo
na anataka kuurithisha kwa mtoto mdogo basi
hufanya hivi…kila anapozaliwa mtoto ndani ya
ukoo yeye hufika mapema akiwa na dawa fulani ya
uchawi aliyoifunga kwenye pindo la kanga yake,
kisha anapopata nafasi ya kukibeba kichanga hicho
kuna jambo hufanyika hapo kisirisiri ila ya
kuonekana na mtu…si mnajua mtoto akiwa
mchanga, muda wote hukunja viganja vyake vya
mikono kama aliyekunja ngumi eenh?” alisaili Babu
Gao na kuitikiwa kwa vichwa tu wanafamilia
waliokuwa wameingiwa na hofu, kisha
akaendelea.“…Vizuri, sasa huyo mchawi humkunjua
vidole mtoto huyo na kumwekea dawa hiyo na
hapo ndipo miujiza hutokea…mtoto huyo yeye
mwenyewe huukubali uchawi huo ama kuukataa!”
“Kivipi mtoto mchanga asiyejua lolote akubali ama
kukataa huo uchawi ambao kwanza hata haujui?”
aliuliza Mzee Mtandi.
“Swali zuri, sasa iko hivi endapo mtoto huyo
ataukataa uchawi huo basi hutokea tu hatokifunga
kiganja chake cha mkono baada ya kuwekea dawa
na huyo mchawi…na hapo utamuona huyo mchawi
akiwa amekasirika kabisa na huenda hata
akaondoka na kumwacha mtoto akiumwa ovyo tu.
Na endapo mtoto huyo ataukubali uchawi huo,
basi atakapoachiwa tu mkono wake baada ya
kukunjuliwa kiganja chake na kuwekewa ile dawa
ya kichawi, hapohapo huukunja mkono wake na
kuifumbata vizuri dawa ile ambayo hupotelea
katikati ya kiganja chake…hivyo ndivyo ilivyokuwa
kwa Kaguba alipozaliwa, baada ya kuupokea
uchawi ule akawa ni miongoni mwao hivyo
haikuwa taabu kwake kujifunza vitu vya jamii yake
hiyo ya kichawi maana wahenga walinena;Kifara
nga hakifunzwi kuchakura,” Alinena kwa utuo Babu
Gao.

ITAENDELEAAA....
 
SEHEMU YA TANO
“Swali zuri, sasa iko hivi endapo mtoto huyo
ataukataa uchawi huo basi hutokea tu hatokifunga
kiganja chake cha mkono baada ya kuwekea dawa
na huyo mchawi…na hapo utamuona huyo mchawi
akiwa amekasirika kabisa na huenda hata
akaondoka na kumwacha mtoto akiumwa ovyo tu.
Na endapo mtoto huyo ataukubali uchawi huo,
basi atakapoachiwa tu mkono wake baada ya
kukunjuliwa kiganja chake na kuwekewa ile dawa
ya kichawi, hapohapo huukunja mkono wake na
kuifumbata vizuri dawa ile ambayo hupotelea
katikati ya kiganja chake…hivyo ndivyo ilivyokuwa
kwa Kaguba alipozaliwa, baada ya kuupokea
uchawi ule akawa ni miongoni mwao hivyo
haikuwa taabu kwake kujifunza vitu vya jamii yake
hiyo ya kichawi maana wahenga walinena;Kifara
nga hakifunzwi kuchakura,” Alinena kwa utuo Babu
Gao.
Wanafamilia wakaanagaliana, hakuna aliyekuwa na
cha kubisha maana ni kweli marehemu Bi
Masonganya alikuwa akipenda sana kumtembelea
mtoto wake yeyote punde tu mara baada ya
kujifungua, na hata yeye mama Kaguba aishiye
wilayani Kasulu alipojifungua huyo Kaguba wake, Bi
Masonganya aliwasili huko na haraka aliwahi
kumbeba mtoto yule kama ilivyo ada, hakuna
aliyemzuia wala kumshitukia. Bila shaka hapo
ndipo alipopata fursa ya kutenda huo ufedhuli
wake!
“Uchawi aliokabidhiwa huyu mtoto wenu ni
mkubwa sana, hivi sasa yeye ndiye kiongozi mkuu
wa wachawi wote wa ukanda huu wa magharibi
licha ya umri wake huo mdogo…na ameshauwa
watu wengi sana ambao hata mkitajiwa
hamtoamini,na hata huyu aliyefariki juzi naye
amemalizwa na mtoto wenu huyo kwa maelekezo
au tuseme maombi aliypewa na mmoja kati ya
watendaji wake wakubwa wa kichawi. Ila angalizo
tu kwenu ni kwamba mtoto huyo bado ni mdogo
sana asiyetambua lolote na anayeongozwa na kiini
tu cha uchawi kilichomo ndani yake sasa
mkimwendea vibaya kwanza hatowajibu lolote
kwani kuna muda anakuwa na akili za kitoto kama
walivyo watoto wengine na pia zitakapomjia akili
zake za kichawi anaweza hata kuwateketeza
nyumba nzima…” Babu Gao akiwa anaendelea
kuongea, uzalendo ukamshinda mama Kaguba na
kuanza kulia kwa uchungu na fadhaa! Ikaanzaa
sasa kazi mpya ya kumbembeleza.
“Hebu mleteni hapa huyo mtoto,” aliagiza Babu
Gao, na hapohapo akatoka mtu mmoja mpaka uani
walipokuwa wakicheza watoto wengi. Akamchukua
Kaguba na kurejea ndani.
Cha ajabu, Kaguba aliingia huku akirukaruka ki-
mchezo kama wafanyavyo watoto, ila alipoingia tu
mle sebuleni na kutupa macho yake kwa mganga,
hapohapo akaanza kulia kwa hofu huku
akitetemeka kwa woga.
“Unalia nini sasa wewe?” Mzee Mtandi alimhoji
Kaguba wakati alipofikishwa pale sebuleni.
“Namuogopa huyo…naomba mnisamehe
msinipige.” Kila mtu alielewa kuwa mtoto Kaguba
ni mchawi na nd’o maana ameweza hata
kumtambua mganga. Babu Gao hakuongea lolote,
akaingiza mkono kwenye kile kikapu chake akatoa
kitu kama kibuyu hivi akiwa amekizungushia
shanga za rangi za njano, nyekundu na nyeusi…
“Nami’ ninacho sasa ukileta mchezo nitakuua sasa
hivi hapa, haya tueleze ukweli kwanini umemuua
ma’mdogo Nyanzala?” Babu Gao alimfokea na
kumtisha Kaguba.
“Nisameheni Babu, mi’ nililazimishwa tu kumuua
kwakuwa yeye ndiye aliyemuua Bibi!” Kaguba
alijibu huku akilia kwa sauti yenye kitetemeshi cha
uoga.
“Ni kina nani hao walokulazimisha?”
“Wale wachawi ninao waongozaga usiku nd’o
waliniambia ni lazima tulipize kisasi!”
“Umeshawaua watu wangapi?”
“awwwh..niii.. ni wengi tu!”
“Wataje haraka.”
“Dada Shumbana, mjomba Makanya, kaka Ndugai,
mjomba Zumbe, ma’mdogo Nyanzala na majirani”
Balaa!
Nyanzala, Makanya na Zumbe wote ni watoto wa
marehemu Bi Masonganya, na Shumbana pamoja
na Ndugai ni wajukuu waliofariki kwa awamu
tofautitofauti katika mazingira ya kutatanisha!
“Kwanini sasa huwa mnauwaua wenzenu hivi?”
“Siye usiku huwa tunakula nyama za watu,
kwahiyo ikifika zamu yetu ya kutoa chakula nd’o
mimi na bibi tulikuwa tunamuua mtu mmoja kwa
ajili ya kumla usiku, na wengine huwa hatuwaui ila
tu tunawachukua kwa ajili ya kutufanyia kazi
ngumu za usiku,” Alijibu Kaguba.
“Tutawapataje hao watu uliowaua?”
“Mnh…haiwezekani kuwatoa huko labda ma’mdogo
Nyanzala tu nd’o bado hajakatwa ulimi, ila naye
akikatwa hawezi tena kurudi huku.”
Kimya kikapita.
“Haya nenda ukacheze.” Babu Gao alimruhusu
Kaguba atoke nje, na alipotoka tu Babu Gao
akawageukia wanafamilia na kuwatupia swali.
“Mmeamini jamani? Mmemsikia mwanenu
wenyewe?”
“Ndiyo Babu.”
“Basi hiyo nd’o hali halisi…mtoto huyu ni hatari,
kila siku usiku kabla hajatoka hutumia muda
mwingi yeye na wenziye kuwachezeeni, hakika
huwasumbueni sana…” hakuna aliyebishana na
Babu maana ni kweli mara nyingi huamka wakiwa
hoi kama waliotoka shamba kulima.
“…Nimemaliza kazi yangu, naomba niondoke!”
“Tunashukuru sana kwa msaada wako mkubwa
uliotupa…” alianza kuongea Mzee Saadallah “…
lakini tunakuomba sana utusaidie ili tulimalize
tatizo hili kivyovyote maana sasa mbali ya
kumpoteza huyu mtoto pia tunaweza hata
kuangamizwa na hao wachawi ukoo mzima.”
“Wanyankole wana msemo wao usemao ‘Omusote
oguli muntamu’ yaani ‘Nyoka ndani ya mtungi wa
Udongo’wakiwa na maana kwamba kumuua
unataka lakini hautaki kuharibu mtungi wako wa
udongo…mnataka kuutoa uchawi ndani ya nafsi ya
Kaguba, lakini hamtaki kumdhuru. Jamani hili
jambo siyo dogo kama mnavyodhani, wanaweza
kufa wengi hapa kama umakini na hatua za
makusudi zisipochukuliwa. Na hata kama
tutafanikiwa kuutoa uchawi huo ndani yake bila
kumdhuru ila mkumbue wahenga walinena
‘Chombo kilichopikiwa samaki, hakiachi kunuka
uvumba’…” Alisema Babu Gao akiwa na maana
kwamba hata kama watafanikiwa kuutoa uchawi
ule ndani ya Kaguba,yawezekana akabakia
nashombo ya uchawi huo. na kumalizia. “…Mimi
kwa sasa sina msaada wowote kwenu ila inabidi
niende kwanza kwangu nikaongee na mizimu
yangu, sasa endapo kama itanipa mbinu ya
kupambana na suala hili basi tutawasiliana…kwa
leo nitawaachia dawa tu ambazo mtaziweka
mlangoni, juu ya bati, na kwenye pembe za
nyumba hii ili kumzuia mtoto huyu asitoke usiku
kwenda kwa hao wafuasi wake ili asije akawaeleza
mipango yetu, sawa?”
“Sawa babu, tunakusikiliza wewe tu!”
Babu Gao akafungua tena kikapu chake na kutoa
kibuyu kingine na vipande vya magazeti ambavyo
alivitumia kufungia dawa fulani nyeusi aliyoitoa
ndani ya vibuyu vyake, akawafungia na
kuwakabidhi kisha baada ya kuwapa maelekezo
akaondoka zake!
Wakazindika kila kona kama walivyoelekezwa na
mganga kisha wakaendelea na mambo mengine
kama kawaida.

***
Siku iliyofuata, tofauti na siku zingine
wanafamiliawaliamka wakiwa na nguvu na siha
njema.bila shaka dawa za Babu Gao zilisaidia na
kuwafanya wasichezewe kichawi. Shughuli za kila
siku zikaendelea kama kawaida japo kwa simanzi,
hofu namashaka.
Sasa wakati mama Kaguba akifagiafagia huku
wenziye wakiendea la mapishi huko jikoni, ndipo
kikazuka kioja kingine cha mwaka.

SEHEMU YA NNE

“Mama…angalia hapo unapofagia,” Kaguba
aliongea kwa kumtahadharisha mama yake.
Kutokana na vimbwanga vya mtoto yule, sasa
alikuwa si wa kupuuzwa kwa kila anachotaka
kukisema.
“Kuna nini?” Alisaili mama Kaguba huku akitupia
macho yake eneo hilo alilokuwa akiliswafi.
“Hapo si nd’o mmechimbia ile dawa mliyopewa na
yule Babu ili mnizuie nisitoke usiku! Sasa ukifagia
vibaya utaifukua buree mwishowe usiku nitatoka
tena.”
Heeh!
Yaani kumbe Kaguba alikwishajua kuhusu dawa
zilizochimbiwa mahala pale kwa siri kubwa? Tena
wakati babu Gao anatoa maelekezo ya dawa ile
yeye alikuwa nje huko akicheza…hii kali kuliko.
“We’ mtoto wewe! Nani amekwambia kuwa kuna
dawa hapa?” Mama Kaguba alimhoji mwanaye
huyo mtata, wakati huo na ndugu kadhaa nao
wakisogea kusikiliza habari hiyo mpya ya
kuchachafya ubongo.
“…halafu mama leo nasikia kichwa kinaniuma
sana…jana wachawi wote walikuja kunipitia lakini
wakashindwa kuingia ndani, na mimi nikashindwa
kutoka kutokana na hiyo dawa mliyoweka, sasa
wakawa wananiita kwa makelele sana mpaka
nikashindwa kulala!” kabla hajajibiwa akaendelea
mwenyewe “…unajua mi’ nd’o mkubwa wao tangu
mlipomuua bibi maana alishaganikabidhi vitunga
vyake vote vya uchawi. Mama mi’ mwenziyo ni
bosi we’ nidharau tuu.”
Majanga!
Mama Kaguba na nduguze wakaangaliana kwa
kihoro. Kama ilivyo kwa mtoto mwingine yeyote,
Kaguba alisimama na kutoka zake nje kwenda
kucheza na wenzake bila ya kujali athari ya
maneno yake aliyoacha ameyabwata mbele ya
wazazi wake.
Hakuna kilichofanywa zaidi ya kuendelea kuishi
kwa mashaka huku wakisubiri kama Babu Gao
angerejea na mpya gani. Siku kadhaa zikakatika
bila ya Babu Gao kurejea, japo bilaya kupatwa na
mauzauza mengine yoyote kutoka kwa Kaguba
wala kwa hayati Nyanzala.

***
“…mkuu tunaomba japo idhini yako tu ili tumkate
kabisa ulimi Nyanzala maana tunaona wazazi
wako wanaanza harakati za kwenda kwa waganga,
sasa tusije tukamkosa,” Binti Sambayu aliongea
kwa kumbembeleza Kaguba, akiwa nje ya nyumba
baada ya kushindwa kuingia wala kumtoa Kaguba
ndani kutoka na zindiko kali la Babu Gao.
“Hapana, msimkate kabisa ulimi ma’mdogo wangu
mpaka n’takapokuja mwenyewe,” Alijibu Kaguba
kwa kutokea ndani. Ilikuwa ni usiku wa manane,
Kaguba akiwa dirishani kwa ndani ya chumba huku
Binti Sambayu akiwa kwa nje wakijibizanana.
“Pia tulimfuata usiku wa jana huyo Babu Gao ili
tumpe hongo yoyote atupe dawa ya kuziua nguvu
zile ndumba alizozindika lakini amekataa
katakata.”
“Achaneni naye…”
“Sasa hali hii itakuwa mpaka lini mkuu?”
“Muda si mrefu nitawatoka tu hawa na huyo Babu
Gao nitamuua kwa mkono wangu…kuna kibuyu
chenye uchawi na dawa zote kali, bibi alikichimbia
chini ya kitanda chake, sasa nashindwa kukifukua
kwakuwa kuna watu bado wanalala humo
chumbani mwake walipopafanya kama ufuo. ila
nikikipata tu hakuna atakayethubutu kunisogelea…”
Alisema Kaguba.
“Sasa mkuu, kama hao nduguzo watakigundua
hicho kibuyu itakuaje?”
“Itakuwa hatari sana maana hicho ndicho chenye
nguvu zote za uchawi wa bibi…kama watakipata
na kukichoma moto au kukidumbukiza chooni basi
tutateketea wachawi wote wa kambi yetu ya
Kibondo. Ila ondoa shaka hakuna atakayeweza
kukisogelea maana mtu wa kawaida akikigusa kwa
mkono wake bila ya kukishika kwa majani ya
Vibumbasi, atapigwa na kitu mithili ya radi kali na
kufa hapohapo.”
“Sawa mkuu.”
“Watangazie wachawi wote kuwa jumatano
nitatoka na nitakuja kusikiliza shida za kila mtu,
nadhani msiba utamilizika siku ya jumanne hivyo
mpaka kufikia jumatano nitakuwa nimepata nafasi
ya kukichimbua hicho Kibuyu…ila kwa sasa
msiruke umbali mrefu, muishie mikoa ya jirani tu…
nawatakia uwangaji mwema.” Pamoja na Kaguba
kumuaga binti Sambayu ila maswali kadhaa
yaliwafanya waendelee na mjadala wao.
Waliendelea na majibizano kwa umakini wa hali ya
juu kwa kuhofia kusikika na mtu wa kawaida
maana kama angetokea mtu akiwa macho
angeweza kuwasikia kwa kuwa kwa muda ule
iliwabidi wawasiliane kama watu wa kawaida tu
kwakuwa haikuwa rahisi kwao kuwasiliana kwa
mtindo wao wa kichawi kwani nyumba ile ilikuwa
imezindikwa.
Walipomaliza mazungumzo wakaagana.
Mtoto Kaguba na Binti Sambayu wakaagana na
kuachana wakiwa na matumaini ya kukamilisha
mpango wao. Siku hiyo ilikuwa ni Alkhamisi hivyo
ingewagharimu siku kama sita ili kukipata kibuyu
chao.

***ITAENDELEA***
 
SEHEMU YA SITA

“Watangazie wachawi wote kuwa jumatano
nitatoka na nitakuja kusikiliza shida za kila mtu,
nadhani msiba utamilizika siku ya jumanne hivyo
mpaka kufikia jumatano nitakuwa nimepata nafasi
ya kukichimbua hicho Kibuyu…ila kwa sasa
msiruke umbali mrefu, muishie mikoa ya jirani tu…
nawatakia uwangaji mwema.” Pamoja na Kaguba
kumuaga binti Sambayu ila maswali kadhaa
yaliwafanya waendelee na mjadala wao.
Waliendelea na majibizano kwa umakini wa hali ya
juu kwa kuhofia kusikika na mtu wa kawaida
maana kama angetokea mtu akiwa macho
angeweza kuwasikia kwa kuwa kwa muda ule
iliwabidi wawasiliane kama watu wa kawaida tu
kwakuwa haikuwa rahisi kwao kuwasiliana kwa
mtindo wao wa kichawi kwani nyumba ile ilikuwa
imezindikwa.
Walipomaliza mazungumzo wakaagana.
Mtoto Kaguba na Binti Sambayu wakaagana na
kuachana wakiwa na matumaini ya kukamilisha
mpango wao. Siku hiyo ilikuwa ni Alkhamisi hivyo
ingewagharimu siku kama sita ili kukipata kibuyu
chao.
***
Kulipopambazuka kila mmoja aliamka na kuanza
kutekeleza majukumu ya kila siku, wapo
waliokwenda kuchota maji, wapo waliokuwa
wakipika huku wengine wakisafisha nyumba na
wengine wakiwa wameketi tu sebuleni. Watoto nao,
pamoja na Kaguba waliendelea na majukumu yao
ya kucheza!
Mzee Mtandi alikuwa chumbani kwake akiwa
amemakinika na kijitabu chake kidogo ambacho
hupendelea sana kuandikia kumbukumbu zake za
kila siku. Alikuwa akisoma hikina kuandika kile,
alimuradi alijishughulisha na alichokijua
mwenyewe. Alipoona amemaliza, akakirejesha
kitabu chake kwenye mfuko wa begi lake la nguo
na kutoka mle chumbani mpaka uani.
“Jamani mi’ n’natoka kidogo kuna pahala
ninakwenda mara moja, nitarejea baadaye!” Mzee
Mtandi aliwaaga wapwa zake.
“Mjomba si’ ungesubiri stiftahi kwanza?” alijibu
kwa kusaili Kungurume.
“Hapana, mtaniachia tu nikirudi nitakula ninashida
na bwana mmoja hivi maeneo ya stendi huko.”
Baada ya mazungumzo ya hapa na pale Mzee
Mtandi akadandia baiskeli yake mkangafu na
kuondoka. Hakwenda stendi kama alivyodai, ila
kuna sehemu alikuwa ana shida kubwa sana, shida
ambayo usiku kucha aliumaliza akiifikiria.
Alipotimiza shida yake akapitia kwenye mihangaiko
ya hapa na pale kisha akarejea nyumbani ambapo
kabla ya kuingiza chochote kinywani akaitisha
kikao cha familia nzima nzima.
Wote wakajumuika sebuleni.
“Nimekuiteni hapa wanangu, kuna mambo mazito
kidogo nataka kukuelezeni…naomba muwe na
staha na na utulivu wa hali ya juu…” Alianza
kuongea Mzee Mtandi baada ya kufungua na
kutuliza baraza. “…Kuna jambo zito nimelivumbua,
jambo ambalo kama tutachelewa kufanya ma’arifa
basi matokeo ya uvumbuzi wangu wa hatari ni vifo
vyetu wenyewe, tutapitiana hapa na kufa kama
wagonjwa wa kipindupindu.”
Kimya kilitanda huku kila mmoja akisikiliza kwa
makini, Mzee Mtandi akaendelea.“…Siku zote hizi
ninyi mkiwa mmelala, mi’ huwa naamka usiku na
kujaribu kuchunguza mwenendo wa mjukuu wangu
Kagubamaana kwa sasa hakuna asiyejua u-hatari
wake. Yapo mengi huwa nayang’amua ila hili
nililoling’amua usiku wa kuamkia leo ni kubwa na
la hatari zaidi…ni kweli kama alivyosema
mwenyewe kuwa dawa za Babu Gao zinamzuia
kukutana na wachawi wenziye, hilo nimeligundua
baada ya kumshuhudia kwa jicho langu akiongea
na Binti Sambayu kupitia dirishani, na nimegundua
hila nzito walizozipanga ili kutuangamiza sisi sote,
na hakika tusipokuwa makini tutakufa sote hapa
na kwenda kutumikishwa huko kwenye ulimwengu
usioonekana kama misukule.” Vinyweleo
viliwatutumka kwa hofu wanafamilia wale
waliokuwa kama kondoo anayesubiri kuvamiwa na
chui akiwa hana msaada.
Wakati wanaongea walihakikisha hakuna mtu
mwingine yeyote tofauti na wao tu kama
walengwa wakuu, hata watoto wao wadogo wa
rika la Kaguba hawakuruhusiwa kuingia ndani.
Kama palikuwa na kiumbe chochote
kinachoonekana basi labda ni yule paka wao
wanayemfuga aliyekuwa amejilalia zake juu ya
kochi. Na hata alipoona maongezi yale yakiendelea,
Paka alijitokea zake nje.
“…Bahati nzuri ni kwamba mbali ya mipango yao
ya kutudhuru, pia nimepata mbinu kali ya
kuwaangamiza wote wanaojihusisha na uchawi
kutoka katikamazungumzo yao wenyewe…”
Aliendelea kuogea Mzee Mtandi kiasi cha kuzidi
kuwamakinisha wanafamilia wote. “…
Nilipowaambia nakwenda mara moja stendi,
haikuwa hivyo. Nilikwenda kwa Bi mkubwa mmoja
hivi kumuulizia juu ya wapi nitapa majani
yanayoitwa vibumbasi maana hiyo ni moja ya
kinga tutakayoitumia wakati wa kuishika silaha kuu
ya maangamizi na kuumaliza huu udhia
unaotutesa.”
Ni kweli mzee Mtandi aliushuhudia mchezo mzima
kati ya Kaguba na binti Sambayu. Sasa wakati
anaanza kuwapa habari ilivyokuwa wakati
wakiwasiliana ndipo kikaibuka kitimtim kipya.
Walishangaa tu kuona ghafla mzee Mtandi
akinyamaza kimya kama aliyezimwa kwa rimoti.
Na hapohapo akaonekana kuishiwa nguvu, mara
akaanguka chini ‘PAAA’ macho yakamtoka, povu
likimfumka mdomoni. Taharuki ikawavaa
wanafamilia, ikawa ni mshikemshike mpya.
Hakuna mtoto mdogo pale mpaka asielewe
kilichotokea kuwa ni tukio la kivamizi la kishirikina
lililoazimia kumzuia Mzee Mtandi asitoe siri
aliyokuwa nayo, na hata ikibidi afe nayo kifuani.
Watoto hawakukubali kumpoteza mjomba wao
pamoja na siri yake kubwa yenye lengo la kuwafaa
wote. Haraka teksi ikaendewa na baada ya
makubaliano safari ya kuelekea kwa Babu Gao
ikaanza. Pamoja na Mzee Mtandi mwenyewe,
ndani ya teksi ukitoa dereva aliingia pia Mama
Kaguba na Kungurume.
Wakati wanaondoka, yule paka wao wa kufugwa
aliyetoka wakati walipokuwa wakiendelea na mazungumzo yao alirejea na kuketi palepale kwenye kochi.

***
Safari ilikuwa mbaya na ya matumaini tu maana
kila baada ya hatua kadhaa gari iliwaharibikia, kila
dereva alipojaribu kutengeneza na kuendelea na
safari walitembea umbali mfupi tu kabla ya
kuharibikiwa tena. Wakati huo hali ya Mzee Mtandi
ikizidi kuwa mbaya, hakuwa na fahamu kabisa
hivyo alikuwa amebebwa tu kama mzigo.
Safari iliendelea hivyohivyo kimungumungu tu
mpaka walipofika katika moja ya mapori kadhaa
ambapo ilikuwa wakilimaliza pori lile tu
wangewasili nyumbani kwa Babu Gao, ndipo
kilipoibuka Kimbunga kikali kilichoishambulia ile
teksi mpaka ikazima.
Baada ya kimbunga kumalizika na upepo kutulia
ndipo dereva akateremka ili kutengeneza gari
yake,hilo likawa kosa kubwa!

SEHEMU YA TANO

Ilikuwa kama maigizo tu, mbele ya macho ya
Kungurume na mama Kaguba pale waliposhuhudia
dereva wao akiyeyuka na kupotea punde tu mara
baada ya kuteremka garini. Wakahaha na kuanza
kupiga makelele ya kutaka msaada lakini hakuna
aliyewasikia. Ukimya uliendelea kutuama eneo lile
laporini. Walipiga kelele mpaka wenyewe wakatulia,
hakuna aliyetokea kuwahami. Labda simu zao
zingewasaidia ili wawasiliane na ndugu huko mjini
kama kungekuwa na mtandao katika pori lile,
haikuwa hivyo!
Walikaa pale wakiwa ndani ya teksi mbovu huku
dereva akiwa ametoweka kimiujiza huku hali ya
mjomba wao ikizidi kudorora. Ndipo baada ya
muda fulani ikatokea gari aina ya Landrover.
Haraka Kungurume akajivisha ujasiri maana yeye
nd’o mwanaume aliyebaki, akateremka ndani ya
gari na kulipiga mkono gari lile lililokuwa likipita
akidhamiria kuomba msaada. Cha ajabu gari ile
iliwapita kama nyumba inayoungua moto. Hakujua
ni nini hasa kilichopelekea hali ile ya kutelekezwa
na gari ile.
Labda hawakumuona! Labda walimuogopa
wakidhani ni mtego wa majambazi, au nd’o hila za
akina Kaguba na Binti Sambayu. Hakuna jibu
sahihi!Kungurume akabaki amejishika kiunoni kwa
mikono yake iliyojazia huku macho yake yakitalii
mazingira ya kijani kibichi yaliyotawala pori lile.
Akarudi ndani ya gari huku akitweta, akiwa
amepoteza kabisa matumaini.
“Mwenzangu, hali ngumu,” Alisema Kungurume
akimwambiadada yake.
“Kivipi?”
“Kuna mawili tu yanayoonekana hapa…tutampotez
a mjomba hapahapa mikononi mwetu au
tutaangamia pamoja naye…”
“Mbona unanitisha kaka?” Kabla Kungurume
hajajibu, ndipo ikaibuka tena gari nyingine aina ya
Landcruiser. Haraka Kungurume akateremka ili
kujaribu tena bahati. Akapunga mkono wake ikiwa
ni ishara ya kuomba msaada. Bahati ikawa yake,
gari ile ikasimama.
“Habari zenu wakuu?” Alisalimu Kungurume.
“Nzuri, vipi kuna shida gani?” Dereva wa gari ile
alijibu akiwa ndani ya gari yake bila hata ya
kuteremka.
“Jamani tumepata matatizo, tuna mgonjwa ndani
ya teksi yetu na tumeharibikiwa hapa…hali ya
mgonjwa inazidi kuwa mbaya tu tunaomba
msaada wenu tafadhali.
“Gari imeharibika kitu gani?”
“Kwakweli hata sijui kilichoharibika.” Jibu hili
likamfanya dereva wa ile Landcruiser aangaliane na
mtu aliyembeba.
“Dereva wa teksi hiyo yuko wapi?” Swali hili sasa
kutoka kwa mtu aliyebebwa kwenye ile Landcruiser
lilimfanya Kungurume ajigonge asijue cha kujibu,
maana kama ataeleza ukweli kuwa ametoweka
katika mazingira ya kutatanisha, hakika asingepata
msaada kwani asingeaminika kabisa na hata kama
angeaminika basi angekuwa amekwishawatisha
sana watu hao. Baada ya fikra fupi alijibu.
“Dereva baada ya kujitahidi kutengeneza gari bila
mafanikio ndipo akapata lifti ya kwenda mjini
kuendea sijui kifaa gani huko…sasa sisi tuna
mgonjwa hatuwezi kuendelea kukaa hapa wakati
hali ya mgonjwa ni mbaya na amepoteza fahamu.”
Alidanganya Kungurume akichelea kupoteza
msaada.
“Sasa huku mnampeleka wapi mgonjwa wenu?
Kuna hospitali kweli huku?” alisaili dereva.
“Huku tunampeleka kwa mganga wa kienyeji.” Jibu
hilo pia likawafanya mtu na dereva wake
waangaliane na kutikisa vichwa.
“Yaani kaka mbona unaoekana kama ni msomi hivi
halafu unadriki kuamini mambo haya ya
kishirikina?” Alihoji dereva.
“Kaka, Kitanda usichokilalia huwajui Kunguni
wake…Laiti mngejua masaibu tunayopitia mpaka
tumesalimu amri na kuja huku bila shaka
mngetuonea huruma…imebidi tufanye hivi tu.”
“Okay iko hivi kaka sisi hatuwezi kuwapeleka huko
kwa mganga kwakuwa tuna mambo ya muhimu
tunawahi mjini…sasa msaada pekee tunaoweza
kukupeni ni kuwapakia kwenye gari yetu na kurejea
nanyi mjini na tutukwenda kuwaacha hospitalikama
hamtojali…Upo hapo?”
Duuh!
Haikuwa lengo kabisa, Kungurume akashusha
pumzi nzito ya kushindwa kabisa. Akawaomba
mabwana wale wamsubiri asogee upande wapili
ilipo teksi akaongee nadada yake amweleze kuhusu
msada huo wa kurejea mjini. Wakamkubalia.
Baada ya Kungurume kuifikia teksi yao na kuongea
na dada yake, wakashuka ndani ya teksi na
kuisogelea ile Landcruiser. Baada ya mama Kaguba
kusalimiana na watu wale, alijaribu kuwasihi na
kuwabembeleza ili tu wawapeleke huko kwa Babu
ambapo hapakuwa mbali kutokeahapo walipo…na
ikibidi hata kwa kuwalipa. Mjadala ukaanza upya
huku jamaa wakiwa na msimamo wao uleule lakini
kama ilivyo falsafa ya hayati Albert Mangwea
kwamba ‘Mwanaume kwa mwanamke, ni sawa na
mfupa kwa fisi’ Dereva na patna wake wakasalimu
amri, wakageuza gari na kuisogeza usawa wa
teksi. Wakateremka na kusaidiana kumbeba Mzee
Mtandi na kumpakia ndani ya gari yao.
Wakaingia wote ndani ya gari baada ya
kuhakikisha ile teksi wameifunga vizuri. Dereva
akalitia moto gari, likawaka. Lakini kila alipoigiza
gia ili waondoke gari iligoma kuondoka. Hila za
kifundi zilimwisha dereva yule bila ya mafaniko.
Gari iligoma kabisa kuondoka na baada ya
purukushani ikazima kabisa.
Balaa!
Wakashuka wote na dereva akalala chini ya
uvunguwagari kuangalia hitilifu, lakini hakuliona
tatizo. Akaingia tena ndani ya gari peke yake huku
wengine wakimsubiri nje wakati akijaribu
kuendesha. Alipojaribu kuliwasha likawaka.
Alipoliingizia gia likakubali na kuondoka, wote
wakafurahi. Baada ya gari kusimama
wakalisogelea na kuingia ndani ya gari kwa ajili ya
safari.
Walipoingia tu, mchezo ukawa uleule gari likatia
mgomo tena. Ndipo dereva akageuka mbogo
baada ya kugundua kuwa watu hawa hawakuwa
wa kawaida. Akawateremsha pamoja na mgonjwa
wao licha ya maombi ya huruma kutoka kwao.
Alipowateremsha tu gari likakubali tena,
akaliwasha na kulitia gia..akawachia vumbi tu.
Mama Kaguba alilia kwa uchungu, japo haikufaa
kitu. Wakarejea kwenye teksi yao na kusubiri
kadari ya Mungu tu iwakute maana hawakuwa na
namna nyingine.

***ITAENDELEA***
 
SEHEMU YA SABA

Mama Kaguba alilia kwa uchungu, japo haikufaa
kitu. Wakarejea kwenye teksi yao na kusubiri
kadari ya Mungu tu iwakute maana hawakuwa na
namna nyingine.
Walikaa pale bila ya kupata msaada mpaka jioni
ikawakuta wakiwa palepale huku hofu, mchoko na
njaa vikizidi kuwashambulia. Ndipo ghafla
wakatokea vijana wawili waliovaa nguo chafu na
chakavu wakiwa wanakusanya kuni.
“Habari zenu jamani?” Kungurume aliwasalimu
vijana wale baada ya kuteremka kwenye gari na
kuwasogelea. Akiwa na dada yake kwa pembeni.
“Nzuri tu…” walijibu vijana wale.
“Jamani samahani tunahitaji msaada wenu…sisi
tumeharibikiwa na gari na tupo na mgonjwa aliye
mahututi sasa tunaomba tafadhali mtudaidie
jamani?”
“Mnakwenda wapi na huyo mgonjwa wenu?”
“Tunampeleka kwa mganga mmoja hivi anaitwa
Babu Gao.” Jibu hilo la Kungurume likawafanya
vijana wale waangaliane kwa udadisi.
“Dereva wenu yuko wapi?” Aliuliza mmoja kati ya
vijana wale wawili.
“Dereva aliteremka ili kuangalia hiyo hitilafu
iliyotokea, cha ajabu hatukumuona tena akawa
ametoweka.” Jibu hili alilitoa mama Kaguba, japo
inaonekana alimkera kaka yake kwa kusema jambo
hilo ambalo lingeweza kuwatisha na kuwaacha na
maswali mengi zaidi badala ya kuwapatia msaada.
“Mnh!” aliguna kijana mmoja.
“Nd’o yuleee?” kijana mwingine akamsaili
mwenziye ambaye alitikisa kichwa kuashiria
kukubali alichoulizwa.
“Iko hivi jamani…” Alianza kuongea kijana
aliyekuwa na upanga mkononi mwake. “…Sisi ni
vijana wa huyo Babu Gao mnayemfuata, huku
tulikuja kusanya kuni na kuwinda kitoweo lakini
muda mfupi tu uliopita tumekutana na kijana
mmoja amevaa kofia nyekundu akatuambia kuwa
amepotezana na wenziye na kwamba yeye ni
dereva teksi…itakuwa nd’o huyo eeh?” Safari hii
sasa ikawa zamu ya Kungurume na Mama Kaguba
kutazamana kwa mshangao.
Hii ndiyo faida ya kuwa mkweli maana kama
Mama Kaguba angedaganya basi pengine vijana
wale wasingejua kisanga hicho kuwa kinahusiana
na huyo kijana waliyemuona.
“Nd’o huyohuyo alikuwa amevaa kapelo
nyekundu.” Jibu la hilo kutoka kwa Mama Kaguba
likamfanya kijana mmoja atoke mbio akielekea
porini kujaribu kumtafuta huyo dereva waliyekutana
naye.
“Huyu mgonjwa wenu atakuwa amerogwa vibaya
sana…” Alianza kuongea kijana aliyebaki na akina
Mama Kaguba wakati mwenziye amekimbia mle
porini. “…maana si ninyi tu, bali wengi wakiwa
wanakuja kwa Babu hupotea ghafla au
kuharibikiwa safari mpaka wanaamua kurejea huko
mjini. Ila ondoeni shaka hata kama gari itaharibika
basi tutambeba mgonjwa wenu kwenye miti mpaka
tutamfikisha kwa Babu, na hata hapa tulipo bila
shaka Babu atakuwa amekwisha tuona kupitia
‘Tivii’ yake ya asili.”
“Yaani hata hatuamini kama tumepona aisee,
ahsanteni sana. Kwahiyo ninyi ni wajukuu kabisa
wa Babu Gao?”
“Naam, mi’ ni mjukuu wake kabisa, mtoto wa wa
mwanaye. Ila huyo aliyekimbilia huko porini ye’ ni
Kanumba(msaidizi’ mganga) wake.
Wakiwa wanaendelea kupashana habari, ndipo yule
aliyekimbilia porini akarejea akiwa na yule dereva
teksi. Maongezi yakafa kwanza! Hapakuwa na haja
ya kupiga soga tena, wakaingia kwenye teksi kisha
yule Kanumba akatoa dawa fulani na kuimwagia
teksi…na kumuamuru dereva awashe gari.
Kama mchezo wa kuigiza vile, gari ikakubali na
safari ikaanza. Ndani ya teksi walibanana wote.
Akina Kungurume na mgonjwa wao, pamoja na
wale vijana wa Babu Gao.
Kumbe wala hawakuwa mbali sana na nyumbani
kwa Babu Gao kwani muda mfupi wa safari
waliwasili na kumkuta Babu gao akiwa amejipinda
na shughuli ya kutengeneza mipini ya majembe.
Wakateremka kutoka garini na kumsogelea Babu
Gao, cha ajabu Babu aliendelea na shughuli zake
kama hajawaona wageni licha ya muungurumo wa
gari yao kuvuma tangu wanaingia eneo lile, hali
hiyo iliwashangaza si tu akina mama Kaguba, bali
hata wale vijana wake walihisi kitu.
“Babu shikamoo!” Mama Kaguba na Kungurume
walimsalimu Babu Gao.
“Marahaba,” aliitikia salaam ile Babu Gao huku
akishindwa hata kukitaabisha kichwa chake japo tu
kuwatazama.
“Habari za hapa?” Mama Kaguba alisaili kwa
fadhaa.
“Nzuri.” Babu aliendelea kujibu ki-mkato.
“Babu tumekuja na mgonjwa yumo ndani ya gari…
ni mjomba Mtandi amepoteza fahamu kabisa.”
“Sasa?”
“Tumekuja kwako Babu tunaomba msaada wako!”
“Amepotezea wapi fahamu?” alisaili Babu Gao.
“Tangu nyumbani…ilikuwa hivi alikuwa akitu…”
Kabla mama Kaguba hajamalizia kauli yake
akakatizwa na Babu Gao.
“Sasa fahamu amezipotezea huko kwenu halafu
mnakuja kuzitafutia kwangu! Mi’ siwezi kuzipata
naomba muondoke haraka tafadhali nina kazi
nyingi za kufanya.”
Heeh…!
“Babu siye ni wajukuu zako, au umetusahau?”
“Sina wajukuu kama ninyi…na kama ni wateja
wangu ni kwamba sihitaji kufanya kazi nanyi
kabisa jamani mwende au mpaka niwafanyie kitu
kibaya?”
Laiti kama mzee Mtandi angekuwa na fahamu
angetambua ukweli wa kile alichokisikia kwa binti
Sambayu akimueleza Kaguba kuwa wamemtisha
na hata kutaka kumuhonga Babu Gao ili aache
kufuatilia kesi hiyo hivyo yawezekana mganga
huyu amesalimu amri.
Babu Gao alikuwa amebadilika kabisa na kuwa
kama hajui lolote kuhusu wageni wale. Kama
haitoshi Babu akanyua uso wake ili awakaripie
vijana wake tabia za kuokota watu huko na
kuwaleta pale kwake. Alipoinua sura yake tu kabla
hajawakaripia vijana wake akakutanisha macho
yake na nyuso zilichoka na kukata tamaa kabisa
kutoka kwa Kungurume na Mama Kaguba.
Waswahili wanasema wao kuwa Ukitaka kumuua
Nyani, usimwangalie usoni…utamuonea huruma.
Hivyo ndivyo ilivyokua kwa Babu Gao alijikuta
akishusha pumzi za huruma. Badala ya kukaripia
kama alivyokusudia, badala yake akawaambia
vijana wake waondoke ili abakai na wageni wake.
Vijana wakaondoka!
“Sikilizeni jamani…jambo lenu ni kubwa sana na
limenielemea kiasi cha kutishia maisha yangu…”
Alianza kuongea Babu Gao baada ya kuweka
pembeni zile zana zake alizokuwa akizitengeneza.
Akawaelezea kwa kirefu ugumu wa suala lao lile,
akawapasha habari jinsi alivyofuatwa na kutishiwa
maisha yake na wafuasi wa Kaguba na mambo
mengine mengi tu.
Mjadala ulikuwa mpana sana. Akina mama Kaguba
walimlilia babu na kusaga meno ili awasaidie
mpaka hatimaye Babu Gao akalegea. Akawaambia
wamteremshe mgonjwa kutoka ndani ya gari kisha
wamuingize ndani. Vijana wakaitwa kusaidia zoezi
lile.
Baada ya kukamilisha zoezi hilo, Kungurume
akamlipa dereva teksi na kumwacha aende zake
kwani kwa mujibu wa mganga, wao walipaswa
kulala palepale. Kuwafahamisha nyumbani kwao
haikuwa tabu kwani tangu walipofika kwa Babu
hapo mtandao ulikuwa ukifanya kazi.

***Haya!
ITAENDELEA...
 
SEHEMU YA NANE

Baada ya kukamilisha zoezi hilo, Kungurume
akamlipa dereva teksi na kumwacha aende zake
kwani kwa mujibu wa mganga, wao walipaswa
kulala palepale. Kuwafahamisha nyumbani kwao
haikuwa tabu kwani tangu walipofika kwa Babu
hapo mtandao ulikuwa ukifanya kazi.

******
Babu Gao akarejea katika ule ukarimu wake wa
kawaida na wa kila siku. Akawakirimu chakula
wageni wake, akawapa maji ya kuoga huku yeye
akazianza sarakasi zake za kumtibu mzee Mtandi
aliyekuwa hajarejewa na fahamu muda wote ule.
Tiba ilikuwa kubwa na ngumu sana, ilichukuwa
muda mrefu mpaka giza la usiku likaingia, na hapo
Babu Gao akawaandalia wageni wake sehemu ya
kulala. Walipolala, yeye akaendelea na patashika
yake.

***
“Jamani kazi ni ngumu sana kama nilivyokuambien
i tangu jana…” Babu Gao aliwaambia akina mama
Kaguba baada ya kumka asubuhi. “…Huyu bwana
kuna siri kubwa sana aliigundua kuhusiana na hao
wachawi wenu, bahati mbaya alipokuwa
akiwaelezeni ninyi hakujua kuwa nyumba ile si
salama kujadili vitu hatari kama vile…mle ndani
kuna wachawi kila kona…”
“Lakini Babu wakati mjomba anatuhadithia habari
hiyo mpaka ikamkuta hali hii, tulikuwa tumewatoa
nje watu wote wasiohusika.” Mama Kaguba
alidakia.
“Una uhakika gani kuwa kati yenu mliokuwa pale
sebuleni hakuna mchawi? Kwani ninyi mlitegemea
kuwa yule mtoto mdogo Kaguba angeweza kuwa
mchawi?” alisaili kwa umakini Babu Gao.
“Mnh! Kwahiyo kuna mtu kati yetu kule nyumbani
ni mchawi?” Alihoji kungurume.
“Sina maana hiyo, nilitaka tu kukuonesheni kuwa
hamko makini na jambo hili kwakuwa hamuujui
uchawi ninyi…iko hivi sasa, siku ile mlipokuwa
mnaongea mambo haya mle ndani palikuwa na
Paka amejilaza kwenye kiti, basi yule hakua Paka
asilani!”
“Ama!” Alimaka Kungurume huku akivuta
kumbukumbu ya siku ile.
“Alikuwa ni mwanaadamu yule aliyejibadili na kuwa
kama Paka japo miaka yote mmekuwa mkiamini
kuwa ni Paka wa kufugwa ila hayati Masonganya
alikuwa akimtamua kama mtumishi wake, na muda
mrefu huwa anawafatilia mambo yenu. Sasa
aliposikia habari ile mbaya akatoka nje na kwenda
kumpa taarifa Kaguba aliyekuwa akicheza nje na
wenziwe’ Kaguba naye haraka akawasilisha taarifa
ile kwa Binti Sambayu kwa njia wazijuazo wenyewe
ndipo likatumwa pigo lile lilomfanya mjomba wenu
awe hivi…ila tutajitahidi sana kuhakikisha
anapona.”
“Tutashukuru sana Babu.”
“Vizuri!”
“Unajua nini Babu…” Kungurume alianza kuongea
huku akitembeza macho yake katika chumba kile
cha uganga. “…sisi hata hatukujua ni kipi hicho
ambacho mjomba alikigundua toka kwa hao
wachawi kwani alipofikia tu kwenye pointi hiyo
nd’o akaanguka, sasa we’ unaweza kututajia hicho
alichokigundua?” Swali hilo likamfanya Babu Gao
apikiche viganja vya mikono yake na kisha
kuifumbata mikono yake kifuani.
Kimya kikatawala.
“Siwezi kusema uongo kabisa katika hili, ni
kwamba sijabahatika kukijua hicho kitu. Hata haya
machache niliyowahabarisha nimeyapata kwa
ufundi wangu wa hali ya juu, niliingia kichwani
mwa mjomba wenu na kuanza kuzisoma fikra zake
lakini habari niliyoipata ni ile kama mliyokuwa nayo
ninyi, yaani niliishia palepale alipoanguka tu.
Nadhani leo atazinduka na tutakwenda kufanya
kafara kubwa makaburini ambapo tukimaliza
atatuhabarisha yeye mwenyewe.
***
Asubuhi yote, na mchana kutwa Babu Gao alikuwa
akishughulika na jambo lile zito mpaka kwenye saa
kumi alasiri ndipo mzee Mtandi akarejewa na
fahamu. Ilikuwa ni kazi nzito, kazi ya kutibu huku
akipambana na nguvu za wachawi zilizokuwa
zikimshambulia mara kwa mara kiasi cha
kumvurugia kabisa kazi yake. Baada ya Mzee
Mtandi kuzinduka akaachwa apumzike, kisha
baadaye akapewa chakula na kupelekwa kuoga
akiwa amebebwa. Afya yake haikuwa mbaya sana
japo tatizo kubwa alilokuwa nalo ni kutoweza
kutembea mwenyewe pamoja na kupoteza
kumbukumbu…hakuwa na kumbukumbu zozote za
kulichotokea. Hilo Babu Gayo alilitarajia.
Saa moja magharib msafara wa kwenda
makaburini ukaanza. Kungurume, Mama Kaguba,
Babu Gao na Kanumba wake wakiwa wamembeba
mzee Mtandi wakaongozana kuelekea makaburini
ambapo zindiko kubwa liliratibiwa kufanyika.
“Tukifika makaburini hatutoruhusiwa kuongea
chochote labda kama nitawaelekeza kufanya
hivyo,. Sawa?” Aliunguruma Babu Gao.
“Ndiyo!” “…Tawire.” Walijibu.
“Kuna kazi ndogo tu kama ya dakika kumi hivi
tutaifanyia juu ya kaburi. Tukifika we’ bwana
Mtandi tutakuwekea kigoda juu ya Kaburi kisha
utaketi, tutakupa kinu kitakachokuwa na dawa
ndani yake, utakishikilia kwa mikono yako miwili
halafu mimi nitatwanga dawa itakayokuwa humo
kwenye kinu…” Walikuwa wakimsikiliza kwa kina
Babu Gao akitoa maelekezo maana walijua
wakifika huko makaburini hawatopata nafasi ya
kuongea kama walivyopewa hadhari mapema.
“…Nikishamaliza kutwanga tu dawa utainuka na
kutoka hapo kaburini kisha dawa hiyo
tutaichanganya kwenye kinu na sote tutaioga na
kuinywa. Hapo tutakuwa tumemaliza kazi yetu.”
Alihitimisha Babu Gao na kuruhusu maswali kwa
ambaye hajaelewa, hapakuwa na swali.
Wakatembea mpaka wakawasili katika viwanja vya
makaburi. Japo alikuwa amebebwa, mzee Mtandi
alisikia na kuelewa maelekezo yote yaliyotolewa na
Babu Gao.
Viwanja vya makaburi vilikuwa kimya kabisa,
upepo ukiiyumbisha miti kadhaa iliyopandwa kwa
kulizunguka eneo hilo kiasi cha kuyaangusha
majani dhaifu yaliyolegea. Wakati huo giza
lilikwishaanza kutanda na kufanya eneo hili la
makaburini kutisha haswa!
Wakaingia na kwenda mpaka katikati ya makaburi,
Babu Gao akachagua kaburi moja lilionesha kuwa
si la muda mrefu sana tangu lihifadhi mtu ndani
yake. Haraka Kanumba wa Babu akaweka kigoda
juu ya Kaburi hilo sambamba na Kinu chenye dawa
kisha akarudi hatua moja nyuma. Babu Gao
akasaidiana na Kungurume kumnyanyua mzee
Mtandi na kumkalisha juu ya kigoda kile juu ya
kaburi. Baada ya kuketi, mzee Mtandi akakishika
kinu kwa mikono yake miwili na hapohapo Babu
Gao akiwa amesimama kwa karibu japo yeye
hakupanda juu ya kaburi, akainua juu mchi wake
wa kutwangia na kuanza kuongea maneno yake ya
kiganga. Wakati huo Mama Kaguba, Kungurume,
na yule Kanumba walikuwa wamesimama kwa
kulizunguka kaburi.
Baada ya Babu kumaliza kuongea tu maneno yake,
akaanza kutwanga dawa iliyomo ndani ya kinu
kilichoshikiliwa na mzee Mtandi huku akiimba
nyimbo kwa lugha ya kiha.
Ghafla wakati Babu Gao akitwanga dawa ile
kikaibuka kizaazaa kilichowafanya wote wataharuki
mpaka Babu Gao mwenyewe.
Ilikuwa ni wakati Babu Gao akitwanga ile dawa,
ndipo Kaburi lililokaliwa na mzee Mtandi
lilipoachama kama mamba, na wote wakashuhudia
Mzee Mtandi aliyekuwa ameketi kwenye Kigoda
akizama na kupotelea ndani ya kaburi pamoja na
kinu chake kisha kaburi likajifunga.
Mama Kaguba alijikuta amemshikila shati kwa
nguvu kaka yake hofu kuu ikimkumba, wakati huo
Kanumba naye alikuwa amehamanika na
kumuangalia Babu Gao aliyebaki na mchi wake
mkononi asijue cha kufanya.
Ghafla!
Wakaanza kusikia kukurukakara na vurugu
vikitokea ndani ya kaburi aliliozama mzee Mtandi.
Ilikuwa ni kama vile uchukue dumu kubwa halafu
uliwekee mawe madogo na kuanza kulitikisa kwa
nguvu ndivyo zile vurugu mle kaburini
zilivyozizima.
“YALAAAH…UWIIIII NAKUFAAA JAMANI!” Sauti ya
mzee Mtandi ilisikika ikitokea mle kaburini licha ya
kuwa kaburi lilikuwa limejifunga. Babu Gao
uzalendo ukamshinda, akautupa mwichi wake na
kutaka kukimbia ndipo haraka Kungurume
akamrukia na kumkwida.
“Unataka kukimbia wapi?” Kungurume alibwata.
“Tuondokeni jamani hii si hali ya kawaida,” alijibu
Babu Gao. Kabla Kungurume hajajibu lolote ndipo
tena mkanda ukaendelea. Kaburi likajapasua
katikati halafu katikahali isiyokuwa ya kawaida,
mzee Mtandi akarushwa kwa nguvu kutokea mle
kaburini na kwenda angani, yeye kule, kigoda na
kinu huko. Kisha akatua chini kama kifurushi.
Kitokeo cha hapo mzee Mtandi akainuka na kuanza
kutimua mbio kali, kufikia hapo sasa akina
Kungurume pamoja na mganga wao nao
wakatimka.
Mgonjwa aliyekuja amebebwa, mara ghafla
ameondoka akikimbia kama amefungwa mota
miguuni. Chezea kifo wewe!!!
Walitimka kwa kasi ya ajabu mpaka nje ya viwanja
vile vya makaburi ambapo hawakumuona kabisa
mzee Mtandi, hawakujua amepitia njia gani.
Kutokana na hali ile ya kuogofya hawakuendelea
kupoteza muda, wakaendelea kukimbia na kuelekea
nyumbani kwa Babu Gao.

***Heeeeh!
 
SEHEMU YA TISA


Walitimka kwa kasi ya ajabu mpaka nje ya viwanja
vile vya makaburi ambapo hawakumuona kabisa
mzee Mtandi, hawakujua amepitia njia gani.
Kutokana na hali ile ya kuogofya hawakuendelea
kupoteza muda, wakaendelea kukimbia na kuelekea
nyumbani kwa Babu Gao.
“Poleni jamani, nini hasa kilichotokea maana
nimeshangaa kuona mgonjwa amerudi mbio na
kupitiliza mpaka chumbani.” Mke wa Babu Gao
aliwapokea akina Babu Gao pamoja na Kungurume
ambao nao waliingia hapo nyumbani kwa kasi ya
ajabu. Hakuna aliyemjibu mama yule zaidi ya
kuendelea kutweta kwa mchoko na kihoro, japo
hawakupumzika baada ya kusikia kuwa mgonjwa
yuko ndani. Wote wakafuatana na kuingia
chumbani kwa mgonjwa.
Wakamkuta mzee Mtandi akiwa amelala kitandani
hoi bin taabani…hana hali, hana kauli. Yaani
mgonjwa aliyekuja nyumbani huku akikimbia ghafla
amekuwa hoi asiyeweza hata kuinua mkono acha
kusimama!
Kungurume kila alipokumbuka jinsi Babu Gao
alivyotaka kuwakimbia alitamani hata amnase
kelbu lakini akahofia kuvuruga mambo. Wakaanza
kumhudumia mzee Mtandi. Mpaka kwenye saa nne
usiku hali haikuwa imetengemaa ikawabidi waingie
tu kulala. Hakuna aliyelala zaidi ya kuhesabu paa
tu.
Wakiwa bado wamejilaza vitandani mwao ghafla
wakamsikia mtu akipita nje ya nyumba huko
ambapo baada ya kusikia akipiga ngoma kisha
akinena kwa sauti kubwa. “TANZIA…TANZIA…
TANZIA Familia ya bwana GAO aliye mganga
kiboko inasikitika kuwatangazia kifo cha mteja
wake bwana mtandi Bin Kalukalange kilichotokea
usiku wa kuamkia leo, maziko yatafanyikia Kibondo
mjini.”
Tangazo hilo liliwafikia kila mmoja mahala
alipolala…hofu mpya ikaibuka hasa kwa akina
Kungurume ambao kioja cha namna hiyo
kilishapata kuwakumba kwa ndugu yao Bi
Nyanzala. Wote wakainuka baada ya tangazo hilo
kuisha na kuingia chumbani kwa mzee Mtandi.
Loohsalale!
Mzee Mtandi alikuwa amefariki. Kilio kikaibuka
hapohapo. Babu Gao akajitahidi kuwatuliza ili
ajaribu kuangalia kwenye ‘bainokyula’ yake…na
hata alipopiga ramli zake zilimthibitishia kuwa
mzee Mtandi amekwishaaga dunia. Simu
zikapigwa mjini kwa ndugu ambao nao baada ya
kuangua vilio vikubwa vilivyokusanya majirani,
walijipanga wakakodi gari na kuufuata mwili wa
marehemu pamoja na akina mama Kaguba.

********
“…hii siyo bure, kuna jambo zito humu ndani. Na
wasipokuwa makini watatikitia kama utitiri…”
aliongea Bi mkubwa mmoja aliyehudhuria msibani
hapo kwa hayati Masonganya.
“Haswa! Maana ndani ya muda mfupi tu
wamekufa watu watu. Alianza Bi Masonganya,
akafuatia Nyanzala, na sasa mjomba wao bwana
Mtandi…haiwezekani.” Waliungana mikono akina
mama hao.
“Aaah kwa Mungu madogo hayo, si ajabu kufa
watu watatu kutoka katika familia moja…Mungu
hata akitaka kuwamaliza nchi nzima kwa sekunde
hashindwi kamwe!” alijibu dada mwingine huku
‘akiwabyeda’ wenziye.
“We’ mtoto mdogo huna ujuacho kaa kimya!”
Wakati mjadala mzima ukuiendelea huko uani kwa
akina mama, upande wa mbele wa nyumba
wanaume nao walikuwa wakizungumzia jambo
hilohilo mpaka walipokatizwa na gari iliyokwenda
kufuata maiti. Ilikuwa ikirejea huku imewasha taa
ikiwa ni ishara kuwa wamebeba maiti. Wanaume
wakasimama mpaka Gari ilipoegeshwa,
wakaisogelea na kusaidiana kuupokea mwili wa
hayati Mtandi.
Muda wa mazishi ulipangwa kuwa ni saa kumi
alasiri ya siku itakayofuata ili kuwasubirisha
watoto wawili wa marehemu waishio Kigoma mjini.
“Ebyomunyumba tebi totolwa,” Alisema Kungurume
kuwaambia dada zake kwa kutumia lugha ileile ya
marehemu mjomba wao. Naye akiwa na maana
ileile kuwa wasiyaweke hadharani mambo yao.

***
Siku iliyofuata majira ya saa tano asubuhi
waliwasili watoto wawili wa marehemu ambao ni
Lubambi na Ilumbi…pamoja nao waliandamana na
Nyembo. Wafiwa walitoka kuwapokea ndugu zao
hao huku wakilia lakini baada ya akina Ilumbi
kuingia ndani tu sura za akina mama Kaguba pale
nyumbani zikawabadilika kutoka kwenye huzuni na
simanzi ya kufiwa na kuwa hasira ya Nongwa,
hapakuwa na mazungumzo yoyote zaidi ya
kupotezeana tu. Tatizo kubwa likiwa ni Nyembo.
Nyembo pia ni mtoto wa hayati Bi Masonganya
hivyo ni ndugu yao na akina mama Kaguba japo
tofauti yao ni moja tu, wakati wao wanamwita Bi
Masonganya mama, huyu Nyembo yeye anamuita
Baba. Naama Bi Masonganya ni baba yake kabisa
na Nyembo, na hivyo ni miongoni mwa vimbwanga
vya hayati Bi Masonganya.
Watoto wote wa Bi Masonganya walimchukulia
Nyembo kama ni kielelezo cha uchawi uliokubuhu
wa mama yao kiasi cha kuwafanya waoneshewe
vidole kila wakatizapo wakiwa na Nyembo.
Wakamchukia sana kijana yule kiasi cha
kumuanzishia mizozo na ghasia za kila aina mpaka
hayati bwana Mtandi alipoamua kumchukuwa na
kwenda kuishi naye Kigoma mjini baada ya
kuombwa kufanya hivyo na dada yake. Hiyo ikawa
ni neema kubwa kwa Nyembo kwani alinusurika
kulelewa kichawi na pia akiwa huko alibahatika
kusomeshwa mpaka kidato cha sita na mzee
Mtandi, tofauti na nduguze walioishia darasa la
nne na wengine la saba tu.

***
Kwa kawaida ya genge la wachawi wa pale
Kibondo ni kwamba ni lazima kwa kiongozi wao
mkuu kuwa na mke, hivyo ilipolazimu kumsimika
ukuu huo hayati Bi Masonganya, ililazimu pia
apewe mke japo naye ni mwanamke. Mke huyu
alipaswa kumfanyia Bi Masonganya kila ambalo
mke humfanyia mumewe japo tendo kuu bila shaka
lisingewezekana kwakuwa wote ni jinsia moja.
Haikuwa taabu kumpata mke kwani mmoja wa
wachawi aitwaye bwana Kalombola alimtoa binti
yake pekee kwa heshma kubwa ili aoelewe na
mkuu wake huyo mpya. Binti huyo aliitwa
Masunga.
Maisha yakaendelea huku bi Masonganya akiwa ni
mume wa Bi Masunga, na wakati huohuo akiwa ni
mke wa bwana Muhonge ambaye ndiye baba yao
na akina Kungurume. Ilimlazimu Bi Masonganya
kumchukua huyo mkewe na kuishi naye nyumbani
kwake kitu ambacho kilipekea usiri ulioligubika
jambo hilo kuvuja, ming’ono ikashamiri kwa
majirani na hatimaye wilaya nzima na baadaye
habari zikamfikia bwana Muhonge kuwa mkewe
naye ni mume wa mtu. Ikawa ni balaa kubwa,
mzozo na magomvi yaliibuka kwa kasi na hicho
nd’o kilichopelekea kifo cha kutatanisha kwa
bwana Muhonge. Hapo ndipo Bi Masonganya
alipojinafasi na kujitandaza na mkewe huyo bila
kificho…kila mtu akaamini sasa.
Miezi sita ya ndoa hiyo ya ajabu, hatimaye Bi
Masunga akapata ujauzito, haikueleweka kirahisi
nini ambacho Bi Masonganya alichomtenda Bi
Masunga mpaka kushika ujauzito ule. Kama
aliyeitegemea hali ile, Bi Masonganya kila siku
akawa anamuosha na kumfukiza madawa ya kila
aina Masunga mpaka zilipotimu siku zake za
kujifungua. Na alipojifungua, Laahaullah mtoto
alitoka kafanana kila kitu na Bi Masonganya(Baba
yake), yaani mpaka kucha. Tukio hilo la ajabu
lilizagaa karibu kila kona ya Kibondo kiasi cha
kumfanya mtoto aliyezaliwa(Nyembo) kuwa mfano
wa kivutio cha watalii wa ndani(wambea). Nyembo
alikuwa vizuri tu huku akipata malezi kama
wapatayo nduguze wengine aliowakuta japo kwake
yeye Bi Masonganya alikuwa ni Baba.
Hicho ndicho kilichowafanya watoto wa Bi
Masonganya kumchukia Nyembo na kugombana
naye mara nyingi mpaka mama Nyembo akawa
anaingilia na hatimaye kusababisha ugomvi ule
kuwa mkubwa zaidi. Bi Masunga alifariki Nyembo
alipokuwa na umri wa miaka mitano na hapo ndipo
ilipomlazimu Bi Masonganya amuombe kaka yake,
mzee Mtandi amchukue ili kunusuru vurugu
zilizokuwa zikiendelea kuota makucha. Nyembo
akahamishiwa Kigoma, huko aliishi na mzee Mtandi
mwenyewe pamoja na watoto wake kwa raha
mustarehe hata akasahau habari za Kibondo.
Ilipomlazimu mara mojamoja kwenda kumsalimu Bi
Masonganya alikwenda japo hakukaa muda mrefu,
na siku zote alizokaa huko muda mwingi aliutumia
akiwa ndani tu na mama yake, kitu kilichowazidish
ia hofu nduguze kuwa atakuwa anarithishwa
uchawi tu…na hicho ndicho kilichozidi kupalilia
uadui wao.

ITAENDELEA...
 
SEHEMU YA KUMI

Ilipomlazimu mara mojamoja kwenda kumsalimu Bi
Masonganya alikwenda japo hakukaa muda mrefu,
na siku zote alizokaa huko muda mwingi aliutumia
akiwa ndani tu na mama yake, kitu kilichowazidish
ia hofu nduguze kuwa atakuwa anarithishwa
uchawi tu…na hicho ndicho kilichozidi kupalilia
uadui wao.

***
Sasa leo amekuja tena Kibondo kwakuwa mzee
Mtandi amefariki, na makubaliano ni kwamba
angezikiwa palepale Kibondo hivyo ni lazima aje
amzike baba yake mdogo(mjomba).
“Ilumbi…” Aliita Bi Chakupewa ambaye ni dada
yake na mama Kaguba, kisha akaaendelea kuongea
kabla hajaitikiwa. “…Nadhani we’ si’ mgeni wa
mambo ya humu ndani, sasa imekuaje tena
unatuletea hiki kituko?” Alihitimisha Chakupewa
huku akimsonta Nyembo kwa kidole chake.
Wanafamilia wote wakajikuta wametazamana.
“Ulitaka asije kumzika mzazi wake aliyemlea kisa
magomvi yenu?” alijibu Ilumbi na kukazia tena “…
nachojua mimi, Nyembo ni ndugu yetu fullstop…
kama kuna makosa waliwahi kufanya wazazi wake
basi sisi hayatuhusu kama yasivyomuhusu yeye.”
“Nakwambia hivi Ilumbi kama udugu leo utauzika,
ila huyu Nyembo humu ndani hakai labda
mkamtafutie sehemu nyingine ya kulala. Angalia
huko alipoingia tu majirani wakaanza
kumzungumza, mnasababisha familia yetu
ionekane ya kichawi, hivi tutaishi vipi na jamii yetu
jamani? Alibwata mama Kaguba.
“Sasa unatutishia kuvunja udugu? Aliyekuambia si’
tunashida na udugu nani? Udugu wenyewe huu wa
nazi kukutania pakachani, acha upumbavu wako
wewe…” Safari hii alibwata Lubambi, mtoto wa
kiume marehemu. “…Iko hivi, aliyekufa ni baba yetu
sisi japonanyi ni mjomba wenu. Sasa kama
hamtaki tushiriki sote pamoja na Nyembo wala
tusibabaishane tunaichukua maiti na kwenda
kuizikia kwetu, kama ni uwezo nasi’ pia tuko fiti!”
Majibu hayo ya Lubambi nd’o kama yalichochea
vurugu, ikawa ni majibizano, majigambo na kila
aina ya upuuzi mpaka baadaye kabisa
walipouingilia ugomvi ule wazee wengine kutoka
katika familia hiyo ambapo hekma na busara zao
ziliwatuliza ndugu wale na kuwapatanisha. Maneno
ya waze yaliwaingia sana akina mama Kaguba
hasa pale waliposisitizwa kuwa Nyembo hakuwa
mwenye hatia kamwe kwa kosa lililofanywa na
wazazi huko nyuma, wakalainika ukizingatia hata
ile hofu yao kuwa Nyembo alikuwa akikabidhiwa
uchawi na marehemu Masonganya ilikwishapotea
baada ya kupata ithibati mpya kuwa kama ni
uchawi alikabidhiwa mtoto wao wenyewe, Kaguba.
Kufikia hapo kidogo amani ikarejea na shughuli za
maziko zikaendelea kupangiliwa.
Suluhu yao ikawa ni pigo kwa kambi ya akina
Kaguba waliokuwa wakiombea mzozo ule uwe
mkubwa ili maiti iondolewe mle ndani ili Kaguba
apate nafasi ya kuingia kule ufuoni akakichimbue
kile kibuyu kinachomzuia kutoka nje ya nyumba
kwenda kuwanga.
Saa kumi Alasiri baada ya kufanyika visomo vya
dua maalum na sala kwa maiti, hatimaye jeneza la
mzee Mtandi likabebwa na wanaume na kuelekea
makaburini kuzika. Wanawake walibaki nyumbani
wakilisindikiza kwa macho jeneza lile. Hakika kifo
kile kiliwachoma na kuwaingia sana.
Hiyo nd’o ikawa safari ya mwisho ya bwana
Mtandi.

***
Saa tisa usiku, kundi kubwa la wachawi
likiongozwa na Binti Sambayu lilikusanyika kwa
kulizunguka kaburi alilozikwa hayati Mtandi,
wakiwa watupu kama walivyozaliwa. Ngoma na
nyimbo za kichawi zilirindima kisawasawa, kila
mmoja alijiachia atakavyo bila ya kujali ni athari
gani atakayoacha kutokana na kubinuka akiwa
mtupu mbele ya wenziye ambao wengine ni wa
jinsia tofauti na yake. Mbali ya kuserebuka nyimbo
hizo pia kulikuwa na vinywaji na vitoweo murua,
Damu na nyama za watu, pamoja na pombe kali
vilihusika.
“Jamani mida inayoyoma, sasa tutekeleze
kilichotuleta ili tutawanyike…karibu mkuu!”
Aliongea Bi mkubwa mmoja ambaye alitapakaa
vumbi kali ya makaburini kutokana mtindo wa
kugaagaa wakati alipokuwa akiserebuka.
Alipomaliza tu kuongea, wachawi wote wakaketi
chini na hapo ndipo akasimama Binti Sambayu na
kuanza kuongea.
“Bila kupoteza muda napenda kuwapa salamu
kutoka kwa mkuu wetu Kaguba anasema yuko
pamoja nasi na kwamba siku si nyingi atajumuika
nasi na kutatua matatizo yetu yote…” kufikia hapo
vigeregere vikazimama, kisha akaendelea. “…
pamoja na hayo ni kwamba tulikuwa tuwe na
mazoezi makubwa mawili hapa leo. Moja ni
kumkata rasmi ulimi Nyanzala ili aingizwe katika
daftari letu la kudumu la misukule, na pili ni
kumfukua bwana Mtandi na kumzindika kabla ya
siku yake ya kukatwa ulimi. Ila kutokana na
maagizo toka kwa mkuu Kaguba ni kwamba
hatutomkata ulimi leo Nyanzala mpaka
atakapokuja mwenyewe hivyo tutabakiwa na suala
hili moja tu la kumfukua huyu bwana mjuaji!”
Alipomaliza tu kusema maneno hayo binti
Sambayu mara kijana mmoja aliyekuwa
amejihifadhi kichawi chini ya miembe akaibukia
akiwa amemshika mkono Nyanzala na
kumkabidhisha kwa wachawi wale. Nyanzala
aliyekuwa amevishwa kijigauni chepesi huku
miguuni akiwa peku kama bata, alikuwa
akitetemeka kama mtoto mwenye homa.
Baada ya Nyanzala kuwekwa chini, sasa
wakalisogelea Kaburi la hayati bwana Mtandi na
kuanza kubinuka tena mahepe yao. Dakika chache
tu Binti Sambayu akakipiga kwa nguvu chungu
cheusi juu ya kaburi lile na hapohapo kaburi
likapasuka na kuachia kijinjia chembamba.
Macho ya Nyanzala aliyekuwa ameketi jirani
kabisa, yalishuhudia kupitia katika ufa huo
uliopasuka hapo kaburini akichomoza maiti
aliyevaa sanda nyeupe. Kutokana na upenyo huo
finyu hapo kaburini, maiti ilikuwa ikichomoza kwa
tabu sana mpaka takribani dakika tano maiti ikawa
juu ya kaburi.
Muda wote huo wale wachawi walikuwa
wakiendelea kuimba kwa shangwe huku wakicheza
na kufurahia tukio hilo. Maiti ile haikuwa maiti ki-
ukweli maana ilipomwagiwa dawa fulani kutoka
katika kibuyu kidogo cha binti Sambayu hapohapo
ikainuka. Alikuwa ni Mzee Mtandi.
Mara macho ya Nyanzala yakakutana na yale ya
mjomba’ake mzee Mtandi. japo wote walikuwa
kama wapumbavu tu kwa jinsi walivyopumbazwa
akili na madawa. Nyanzala akaanza kulia japo bila
ya kutoa sauti.
Wakati mzee Mtandi akiwa amesimama kama
mlevi wa dawa za kulevya, akashituliwa kwa
kumwagiwa maji ya baridi yakifuatiwa na mijeredi
ya nguvu! Akashituka kutokana na maumivu yale,
na sasa akili zikawa zimeanza kumreja…hicho nd’o
walichokuwa wakikitaka wale Wachawi.
Kumzindua!
Kwa kawaida Wachawi wale wakishamfufua mtu,
humfanyia madawa yao pamoja na kumshitua kwa
maji ya baridi na mijeredi ili kuiamsha akili yake
ambayo ilidorora mchana kutwa tangu afukiwe
kaburini na ndugu zake wakiamini amekwishakufa,
kisha zoezi linalofuata ni kumfanyisha mazoezi.
Huwa wao wanasimama na msukule wao karibu
na kaburi alilofukuliwa kisha wanamuamuru
akimbie mpaka sehemu waliyoweka alama yao
halafu anarejea tena mpaka walipo wao…hufanya
hivyo kwa takribani mizunguko mitano kabla
hawajamzuia na kuondoka naye mpaka nyumbani
atakapofikishiwa kwa shughuli nyinge zaidi. Hivyo
na mzee Mtandi naye akaamriwa aanze kukimbia
kama ilivyo desturi!
***
Katika usiku huo mkubwa wakati wachawi
wakifanya vitu vyao kule makaburini, huku
nyumbani nako watu walikuwa wamelala isipokuwa
Nyembo pekee aliyekuwa amejiegesha katika
godoro lake aliloliweka juu ya turubai kubwa
lilitandikwa chumbani humo. Kilichomfanya awe
macho mpaka muda ule alikuwa akihangaika
kuchimbua pale kilipochimbiwa kile kibuyu cha
maangamizi cha hayati Masonganya,
kilichomchelewesha na kumkawiza kukifikia ni hofu
ya kushitukiwa na nduguze ambao baadhi yao
walikuwa wamelala humohumo chumbani.
Hakutaka kabisa kuonekana.
Aliendelea kuchimbua taratibu na kwa umakini wa
hali ya juu mpaka alipokifikia kile kibuyu. Alipofikia
hapo akaacha kidogo zoezi hilo. Akaingiza mkono
katika mfuko wa koti lake akatoa majani ya
‘Vibumbasi’ akayasambaza vizuri mikononi mwake
na kisha akaingiza mkono katika kijishimo
alichokichimba na kukitoa kile kibuyu.
Alipohitimisha tu zoezi lile, haraka akatoka mle
chumbani akiwa na kibuyu chake mkononi,
akaelekea na mpaka uani kisha akaingia chooni
ambako alianza kufanya kitu kikubwa kuliko umri
wake.

***MNh! Kitu gani hicho?
 

Attachments

  • 1422640805069.jpg
    1422640805069.jpg
    39 KB · Views: 290
SEHEMU YA MWISHO - Part 1

Alipohitimisha tu zoezi lile, haraka akatoka mle
chumbani akiwa na kibuyu chake mkononi,
akaelekea na mpaka uani kisha akaingia chooni
ambako alianza kufanya kitu kikubwa kuliko umri
wake.
Hatua zote anazozipitia Nyembo, tangu kukifukua
kibuyu, na kukibeba tena kwa ustadi wa kujikinga
na majani ya vibumbasi na kukimbilia nacho
chooni alizipata kupitia maelezo yaliyoandikwa na
bwana Mtandi katika kijitabu chake cha
kumbukumbu(Diary). Mchana kutwa wakati ndugu
wakishughulika na mambo makubwa zaidi
kimuonekano hapo msibani, Nyembo alikuwa
makini akisoma kitabu hicho cha kumbukumbu
ambapo mbali ya mambo mengine ikiwemo
madeni, ndipo akakumbana na siri nzito ambayo
mzee Mtandi aliisikia kutoka kwa Kaguba na Binti
Sambayu na kuiandika humo kabla hajakutwa na
ile hali ya sintofahamu wakati akiwasimulia akina
Kungurume bahati na majani hayoya vibumbasi
aliyakuta humo kwenye begi. Tabia hii ya
kujisomeasomea taarifa muhimu, Nyembo
alijizoesha kupitia huko shuleni alikokuwa anasoma
na pia alijifunza kupitia kwa mzee Mtandi.
“Akkhhhhh….OHHHHKH KHAAA NAKUFAAAAAAAAA.
” Sauti ya Kaguba ilivuma kwa kasi kutokea
chumbani alikolala. Ilikuwa ni kama mashetani
fulani yaliyompanda kichwani. bila shaka ni
kutokana na kitendo kilichofanywa na Nyembo
kuingia chooni na kile Kibuyu. Watu wote
wakaamka kwa mshituko.
“HAAGHHAAAAAAA HATARIIIIIIIIII…CHOOOONI.
NIFUNGULIENIIII NIKAUUUE.” Kaguba aliendelea
kulalama kwa hasira kiasi cha kuwafanya wakubwa
wote waingiwe na hofu na kihoro cha kujua nini
kipo huko chooni.
Wote waliamka na kujumuika pamoja isipokuwa
Nyembo tu nd’o hakuonekana alikokwenda, hofu
mpya ikawakabili.

****
Kule makaburini nako mambo yalikuwa yakiendelea
kama yalivyopangwa, tayari mzee Mtandi
alikwishaanza kufanyishwa mazoezi na tayari
alikuwa amekimbia karibu mzunguko wa pili.
Wakati mzee Mtandi akikimbia mzunguko wa tatu,
wachawi walishangaa ghafla lilipotokea jambo
fulani lisilo la kawaida, pale ambapo mzee Mtandi
badala aishie kwenye uzio wa makaburi ambako
ndiko alipokuwa amewekewa alama ya kuishia
katika mizunguko yote anayokimbia, na alifanya
hivyo tangu mwanzo, sasa alipitiliza kwa kasi ya
ajabu mpaka nje kabisa ya uga wa makaburi
ambako kuna barabara inakatiza. Kama haitoshi
mzee Mtandi akiwa katika kasi ya ajabu
alitokomea gizani kabisa.
Wachawi wote wakajua kilichotokea kuwa mzee
Saadallah amewakimbia, haikuwa kitu cha kawaida
kwa msukule wao ambaye wameshammwagia
dawa na kumpunguza akili atoweke kwa mtindo
ule. Bila shaka kuna nguvu ya ziada imetumika!
“Haiwezekani…kuna namna hapa. MKIMBIZENIIIII,”
Alliongea kwa mshituko na mashaka Binti
Sambayu.
“Mkuu ungemuangilia kwenye kioo chako kwanza
maana sisi hatumuoni kwa upeo wetu!” alijibu
kijana yule aliyemleta Nyanzala. Wakati mjadala
ukiendelea ndipo ghafla tena ilipowadhihirikia hali
mbaya zaidi kwao, ilikwa ni kama vile wamewekwa
ndani ya boksi halafu mara wabinuliwe juu chini,
mara kulia na kushoto. Waliyumbishwa bila
kujielewa mpaka wakawa kama walevi au
wanaojisikia ‘kizunguzungu’ huku wengine
wakicheua nyama na damu za watu walizokula na
kunywa. Nyanzala naye kama aliyezinduliwa
kutoka usingizi akajikuta akili za kibinaadamu
zikimrejea naye akatimua mbio kali kama mjomba
wake, hakuna mchawi hata mmoja aliyeweza
kumuangalia Nyamizi akitoweka kwa jinsi
walivyokuwa wakiona maluweluwe ya kubinuliwa
bila kujielewa.
***
“We’ Kaguba una nini lakini?” Alisaili Bi
Chakupewa.
“Mamaaa na-ku-faa…nasikia kizunguzungu
mamaaa!” Sasa Kaguba alianza kuongea, na mara
akaanza kutapika. Kutokana na vimbwanga vya
mtoto huyu kila mmoja akajua labda pengine
alikuwa akijaribu kufanya ‘mchezo’ ndipo
akakutana na dawa zilizozindikwa.
“Ulikuwa unafanya nini lakini we’ mtoto?” Mama
Kaguba naye alihoji kwa woga.
“Mama nakufaaaa aakkkhh…mjomba Nyembo
anatuuwa.” Aliendelea kulalama Kaguba.
Baada ya Kaguba kumtaja Nyembo, ndipo kila mtu
akawa kama aliyefungukiwa na kitu kichwani kwani
muda wote wa tukio hilo, Nyembo hakuwemo mle
ndani.
“Jamani kwani Nyembo yuko wapi?” Alisaili Ilumbi.
“Tuwaulizeni ninyi mliyelala naye huko ufuoni!”
alijibu Kungurume.
“YU-KO CHO-O-NI ANATAKA KUNIMALIZAAA
AKKHH Uhuaakh!” Kaguba alijibu haraka huku
akitoa milio ya ajabu isiyoeleweka kabisa. Haraka
wote wakatoka mpaka uani ambako giza nene
lililokuwa limetanda. Wakawasha taa na kuelekea
mpaka huko chooni.
Hamad!
Wakakamkuta Nyembo akiwa amesimama katikati
ya choo huku mikono yake miwili ikiwa imeshika
kile kibuyu kilichozungushiwa shanga nyingi kwa
juu huku kwa ndani kukiwa na vitu vya ajabu na
kuogofya!
“Ilumbi mnaonaa? Mnaonaa? Si’ tuliwaambia sisi
kuwa huyu Nyembo si mtu mzuri mkawa
mnamtetea!?” Alibwata kwa ghadhabu Mama
Kaguba. Akina Ilumbi nao wakajikuta wakiduwaa tu
na kumkodolea macho Nyembo ambaye alikuwa
akikizungusha kile kibuyu chini juu, juu chini, mara
kulia. Mara kushoto. Hakuna aliyeelewa
akifanyacho zaidi ya kumuona kuwa ni mchawi tu.
“Nyembo unafanya nini huku chooni saa hizi na
hicho kibuyu?” Lubambi alimsaili Nyembo kwa
kihoro na woga.
“Unamuuliza anafanya nini wakati unamwona
anawanga kabisa hapo, au unataka akuambie
anasali?” Alidakia Kungurume.
“Embu tulieni ninyi msiwe kama majuha…ningekuw
a nawanga sasa inakuaje huyo mtoto wenu
ambaye ndiye mkubwa wa wachawi apige kelele
kiasi hicho?” Alijibu kwa kujiamini Nyembo kiasi
cha kuwafanya wote mle chooni wazidi kubutwaika.
Baada ya hapo Nyembo akaendelea kukizungusha
kile Kibuyu chake, na hapohapo wakaanza
kumsikia Kaguba akilia kwa sauti huku
akiweweseka kama awali. Kufikia hapo sasa mama
Kaguba chango la uzazi likamshituka akajikuta
uzalendo ukimshinda akamvaa Nyembo ili
amnyang’anye hicho kibuyu. Wakaenda mweleka
mpaka chini, ikawa ni patashika ya haja!
Wakati vurugu hiyo ikiendelea mara ghafla
kikawakumba kioja kikubwa na cha nguvu kuliko
hicho cha kumkuta Nyembo akihangaika na Kibuyu
huko chooni. Wakati baadhi wakiwa chooni, kuna
wengine walibaki wamesimama uani. Sasa hao
nd’o walianzisha vurugu na kelele zilizowatoa wote
kule chooni.
“UWIIIIIII JAMANIII BABU MTANDI HUYOOO,”
Alipiga kelele Kilanga, mtoto mdogo wa kike wa
Kungurume, waliokuwa uani hapo wote
wakamshuhudia mzee Mtandi akiingia ndani kwa
kasi. Kusikia kuwa mzee Mtandi akitajwa
kuonekana, kikazuka kimuhemuhe cha hali ya juu.
Wakasambaana wote na kukimbilia ndani ambako
mzee Mtandi naye akaingia. Japo Nyembo
alitegemea kutokea kwa jambo zito kutokana na
maelezo yaliyoandikwa kitaalamu kwenye kile
kitabu cha kumbukumbu lakini naye kihoro
kikamkumba, akajikuta akitimka na kuelekea ndani
huku kile kibuyu akikiacha kule chooni kilipoanguka
tangu alipokumbwa na mama Kaguba kilimponyoka
na kuanguka chini.
“WEEE LUBAMBI USIINGIE HUKO, MJOMBA ND’O
AMEINGIA HUKO!” Chakupewa alimhadhari
Lubambi asiingie chumbani ambako mzee Mtandi
ameingia. Japo Lubambi alitaka kumuona kama ni
kweli baba yake lakini hofu iliyomvaa ilimsukuma
na kujikuta akikimbilia kule waliposimama
nduguze. Haikuwa jambo jepesi kumwona mzazi
wako aliyekufa na ukahakikisha mmemzika halafu
ghafla atokee tena. Si rahisi hata kidogo.
Mara tu baada ya Nyembo naye kuingia ndani,
hakutaka kupoteza muda, akawasogelea ndugu
zake ambao walijikuta wakipiga kelele za
kumuogopa wakimwona tu kama mchawi.
“Acheni upuuzi ninyi, nilichokuwa nakifanya huko
chooni nd’o kimemrejesha mzee Mtandi, sikutaka
kuwaambia mapema kwakuwa tungeharibu
mpango mzima na yangetokea kama yaliyotokea
wakati mzee Mtandi alipokuwa akiwasimulia ninyi
alichokigundua…” Aliongea Nyembo kwa kujiamini
kama ilivyo kawaida yake japo ndiyo kabisa alizidi
kuwachanganya nduguze ambao hawakumwelewa
kwanini alijua kuwa mzee Mtandi aliyekufa na
kuzikwa kuwa angerejea? Na wapi alikipata kile
kibuyu kilichofanya Kaguba awe anapiga kelele.
Akaendelea Nyembo. “…haya tujivisheni ujasiri,
tuingie chumbani tukajaribu kumtuliza mzee
Mtandi ili tuzungumze naye na endap…” Kabla
Nyembo hajafikisha neno lake mwisho kikazuka
kizazaa kipya na cha kuogofya zaidi.
Mlango wao wa kutokea uani ulisukumwa kwa
nguvu, na hapohapo wote wakamshuhudia
msichana akiingia kwa kasi kama anayekimbizwa.
Wote kwa pamoja walimshuhudia na kumfahamu,
alikuwa ni Nyanzala.
“UWIIIIIIII JAMANI TUNAKUFAAA..NYANZALAAA!”
Alipiga kelele za woga mama Kaguba, huku
akisaidiwa na nduguze wengine akiwemo Ilumbi,
Chakupewa, na wajukuu. Hakika ilikuwa ni siku ya
ajabu sana kwao, hakuna aliyeelewa kama
anoyaona kweli matukio yale ya ajabu au anaota.
Nyanzala naye akajikuta akiwaogopa nduguze
waliokuwa wametaharuki kwa kupiga makelele
huku wakiparamia meza na viti vilivyokuwapo
sebule hapo. Akajikuta akikimbilia chumbani
ambako ndiko alikokimbilia mzee Mtandi!

***Makubwa!
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA MWISHO - Part 2

Nyanzala naye akajikuta akiwaogopa nduguze
waliokuwa wametaharuki kwa kupiga makelele
huku wakiparamia meza na viti vilivyokuwapo
sebule hapo. Akajikuta akikimbilia chumbani
ambako ndiko alikokimbilia mzee Mtandi!
Kelele kali za akina mama Kaguba ziliweza kuvuma
sana kutokana na hali ya utulivu wa usiku mnene
kama ule kiasi cha kuwaamsha majirani ambao
baadhi wenye ujasiri walitoka na kuja kujumuika
nao kujua kilichotokea huku wale wenzangu na
mimi wakiishia kuchungulia madirishani mwao tu
kama njiwa manga. Majirani walizidi kumiminika,
na hapo ndipo walipokutana na kioja kile cha
mwaka, kwamba watu wawili kutoka katika familia
moja waliokufa na kuzikwa kabisa eti leo
wamefufuka na kurudi nyumbani, tena kwa
kufuatana.
Ilikuwa ni mtafutano.
Wakati hayo yakiendelea, Kaguba alikuwa ametulia
kimya, macho yakiwa yamembadilika na kuwa
mithili ya Paka. Alikuwa akiona mbali sana,
aliwaona wachawi wenzake wakiwa wametaharuki
ovyo baada ya kuhangaishwa sana kutokana na
mchezo uliokuwa ukifanywa na Nyembo katika kile
kibuyu. Sasa walikuwa wamepata ahueni tangu
kibuyu kilipoachwa peke yake chooni, wakawa
kama mazezeta hivi wasioelewa kilichowakumba,
na baada ya Binti Sambayu kupiga ramli yake
kupitia kibuyu akagundua yaliyowakuta,
akawaamuru wafuasi wake wote watawanyike,
wakawa wanatimka mbio kuelekea majumbani
huku yeye(Binti Sambayu) akifanza maarifa.
‘Kibuyu kipo chooni, kimbia haraka kakichukue na
umuangamize huyo Nyembo haraka, halafu
uwapoteze hao akina Nyanzala kabla hawajasema
chochote, nasi tuko njiani tunakuja hukohuko
vinginevyo tutakufa sote.’ Sauti ya Binti Sambayu
aliyekuwa akikimbia ilimjia waziwazi kichwani
Kaguba ikimtaka kukiwahi kibuyu kule chooni.
Hakuna aliyeisikiasauti ile zaidi ya Kaguba
mwenyewe.
‘Sawa’ Kaguba naye alijibu kwa kutuma hisia zake
moja kwa moja kwa Binti Sambayu. Kisha Kaguba
akakata mawasiliano hayo ya ki-hisia na kuanza
kutoka pale alipokuwa ameketi.
Alipofika sebuleni, Kaguba aliwaangalia
harakaharaka wazazi wake waliokuwa bado
wametaharuki kIsha kwa kasi ya kustaajabisha
akaanza kuelekea ulipo mlango wa kutokea nje ili
akakiwahi kibuyu chake. Haraka Nyembo akahisi
kitu cha hatari, damu ikamsisimka akajikuta
akiacha kuzungumza na nduguze, na kumuangilia
Kaguba ambaye alikuwa ameshakaribia kutoka nje.
Haraka, na kwa kasi ya umeme Kungurume
akatoka mbio ili amzuie Kaguba asitoke nje, lakini
alikwishamchelewa. Kaguba alikuwa
amekwishatoka uani.

******
Japo Kaguba alikwishatoka uani kabla ya kufikiwa
na Nyembo, lakini hakupata nafasi ya kuufikia
mlango wa chooni, Nyembo akawa ameshamfikia
na kumkumba kama mchezo wa mieleka. Kaguba
akaanguka chini na kuanza kugaagaa huku akilia
kwa sauti kiasi cha kuwapa hofu wakubwa kule
ndani ambao wote wakatoka kwa kasi ili wajue
Nyembo amemtenda nini. Walipotoka hawakuona
kilichotokea, zaidi ya kumwona Kaguba
akihangaika pale chini karibu na mlango wa
kuingilia chooni. Majirani waliojumuika walizidi
kuchanganywa na mchezo ule unaondelea kutukia!
Wakati Nyembo akiwa mle msalani akakiona kile
Kibuyu kikiwa palepale kilipoangukia, lakini alisita
kukigusa baada ya kukumbuka maelezo
aliyoyakuta kwenye kile kitabu kilichoandikwa na
mzee Mtandi ambaye sasa haijulikani aitwe hayati,
msukule, ama maiti wa zamani! Kilichomsitisha
Nyembo ni ni yale majani ya ‘Vibumbasi’…hakuwa
nayo maana yalisambaa ovyo wakati wa ile
mpishempishe. Kichwa kikamvurugika asijue la
kufanye. Kumbukumbu zikamjia kuwa kuna majani
kiasi aliyabakiza kwenye begi la mzee Mtandi kule
chumbani, lakini sasa angewezaje kutoka mle
maliwatoni na kumwacha Kaguba pale mlangoni
akiwa peke yake, yaani amwachie fisi bucha?
Haiwezekani.
Ambacho Nyembo hakukijua ni kwamba, kadiri
anavyopoteza muda kufikiria nini chakufanya
ndivyo genge la wachawi lilivyokuwa likizidi kuja
kwa kasi katika nyumba ile ili kukiwahi kibuyu
chao! Na kweli walibakiza kama mitaa miwili tu
kufika hapo.
Baada ya tafakuri ya muda, Nyembo akaamua
kutoka mpaka pale uani. Tayari uwanja ulifurika
uamati wa watu, majirani na ndugu. Wote
wakamlaki kwa macho tofautitofauti, wapo
waliomchukulia kama shujaa, na wapo waliohisi
labda naye ni mchawi tu. Hakujali!
“Nahitaji haraka majani ya vibumbasi yapo ndani
ya Begi la mzee Mtandi!” Maneno ya Nyembo
yakawafanya watu watazamane maana majani
hayo ni mashuhuri kwa mambo ya kishirikina tu
japo akina Kungurume wakakumbuka kauli ya
mzee Mtandi muda mfupi kabla hajakumbwa na
yale maswaibu, alipata kuwatamkia habari za
majani hayo, pia kauli hiyo ilimfanya Kaguba
amtazame kwa tahadhari sana Nyembo maana
kusikia anahitaji majani yale kukampa jibu kuwa
mtu huyo anaelewa hatua kwa hatua za kukitwaa
kibuyu na hata kutishia uchawi wao. Lakini
angefanyaje sasa? Akaanza kuizungusha akili yake.
“Ilumbi…au Lubambi, hebu nichukulie haraka hayo
majani kwenye begi ndani, Laa sivyo sote hapa
tutaangamizwa sasa hivi, nataka nikichukuwe
Kibuyu ila sasa sipaswi kukigusa bila ya majani
hayo,” Alisisitiza Nyembo baada ya kuona kama
haeleweki hivi. Lakini bado haikusaidia kitu ilikuwa
kazi bure tu, sawa tu na kumpiga konzi kinyago.
Kauli hiyo ya Nyembo ilipenya dirishani, na kuingia
mpaka chumbani, chini ya uvungu wa kitanda
walipojificha Nyamizi na mjomba wake. Sauti ya
Nyembo haikuwa ngeni masikioni mwa mzee
Mtandi hivyo Kauli hiyo ikamzindua na kumpa
ishara fulani, ishara ya hatari kuwa Kibuyu tayari
kipo chini ya himaya ya Nyembo na kwamba
anahitaji ‘vibumbasi’ vya kushikia. Kwa jinsi
anavyomjua Nyembo kwa utamaduni wake wa
kusomasoma hivyo hakupoteza muda kujiuliza
kuwa ametoa wapi taarifa za kibuyu kile hatari
maana alimtambua fika kuwa atakuwa alisoma tu
kumbukumbu alizoacha ameziandika kwenye kile
kijitabu chake. Na kwakuwa alitambua utata wa
jambo hilo hivyo ilimdhihirikia kuwa ingekuwa ni
vigumu kwa wengine kumuelewa. Akachomoka
tokea chini ya uvungu kama mshale, haraka
akasimama na kuanza kuangaza huku na kule,
akaliona begi lake likiwa limewekwa juu ya stuli,
akalisogelea na kulifungua.
Baada ya kulifungua na kupekuwapekuwa
akayatambua majani ambayo ni yeye mwenyewe
ndiye aliyeyaweka mle, yalibaki kidogo sana kiasi
cha kumpa jibu kuwa yalitumika baadhi. Akili ya
kibinaadamu ikaanza kumjia, akajuwa tu hata
kuponyoka kwao kule makaburini bila shaka
kulitokana na jitihada zilizofanywa pale
Nyumbani…bila shaka na Nyembo. Akayachukua
yale majani na kuanza kutoka nayo nje haraka.
Alipotoa uso wake tu pale uani, Loosalale uwanja
wote ulivurugika, kelele za taharuki kutoka kwa
majirani zikazizima, kila mmoja akiamini kuwa
mzee Mtandi alikwishakufa, vije tena awepo pale.
Ndugu nao utadhani nd’o wanamuona mzee wao
huyo kwa maraya kwanza, maana nao waliungana
na majirani wenzao na kukimbia ovyo. Wote
wakaelekea ulipo mlango mkubwa wa kuingilia na
kutokea uani ili watawanyike…na walipoukaribia tu
mlango, ndipo kilipozuka tena kizaazaa kipya na
cha kipekee!
Wakiwa hapo mlnango ndipo wakakutana uso kwa
macho na kundi kubwa la watu zaidi ya kumi.
Wengine wakiwa watupu kama walivyozaliwa huku
wengine wakiwa wamejivisha vibwaya vidogo
vilivyositiri sehemu nyeti tu za maungo yao, watu
hao wakiwa wamejipaka pemba nyekundu na
nyeupe katika miili yao, ukijumlisha na vumbi
zilizowatapakaa nd’o kabisa walizidi kutisha. Watu
hao ndiyo wale wachawi waliokuwa wakiserebuka
kule makaburini kabla mzee Mtandi na Nyanzala
kuwaponyoka na kufuatiwa na patashika
iliyowavuruga kabisa. Hawakuwa japo na chembe
ya aibu, maana akili zao zilikwishavurugika hivyo
kwao wao, Kibuyu nd’o kilikuwa cha muhimu kuliko
kitu chochote.
Hakuna aliyethubutu kuendelea kutoka nje, wote
waliokuwa wakimkimbia mzee Mtandi wakiamini
kuwa msukule umewatokea, wakajikuta wakipiga
kelele kwa nguvu huku wakirejea tena kulekule
walipotokea, ilikuwa ni bora kukumbana na mzee
Mtandi kuliko kuvaana na genge hili la wachawi
waliopagawa. Cha ajabu mzee waliporejea huku
uani hawakumwona tena mzee Mtandi ila
walikumbana na kioja kingine kilichowafanya
wachanganyikiwe zaidi. Walimshuhudia Nyanzala
akiwa anatokea mlemle ndani alikotokea mzee
Mtandi, japo yeye(Nyanzala) alionesha hofu na
woga wa haliya juu, alikuwa akitetemeka tu na
kuhema juujuu.
Taharuki mpya ikaibuka ikiwa ni kukimbia ovyo tu
bila muelekeo huku wakipamiana na kwenda
mieleka mpaka chini. Nyanzala alipowashuhudia
wale wachawi wakiingia kwa tambo mle ndani
akakimbia kwa kasi na kurejea kule chumbani
ambako alishindwa kubaki peke yake kwa woga
uliomvaa baada ya mzee Mtandi kutoka.
Licha ya Pemba na vumbi vilivyowatapakaa wale
wachawi, ila wote walitambulika kwa sababu ni
wakaazi wa eneo hilo na huwa wanafahamika kwa
michezo yao hiyo ya ingawaje hawakuwahi
kukamatwa!

****Mnh! Kaazi Kwel, Kwel!
 
SEHEMU YA MWISHO

Licha ya Pemba na vumbi vilivyowatapakaa wale
wachawi, ila wote walitambulika kwa sababu ni
wakaazi wa eneo hilo na huwa wanafahamika kwa
michezo yao hiyo ya ingawaje hawakuwahi
kukamatwa!
Hakuna hata mchawi mmoja aliyekuwa na mpango
na Nyanzala, wote walikatiza kona mbele ya banda
litumikalo kuanikia dagaa wakielekea sasa kule
msalani.
Kule msalani nako, mambo yalikwishawiva. Mzee
Mtandii aliamua kuifanya kazi mwenyewe, aliingia
moja kwa moja msalani akifuatiwa na Nyembo,
akiwa na ‘vibumbasi’ vyake mkononi, akakitwaa
Kibuyu kile na baada ya manuizi tu akaanza kazi
ya kukizungusha huku akikipuliza kama firimbi.
Laahaulah!
Hakuna hata mchawi mmoja aliyepiga hata hatua
moja tangu kibuyu kilipoanza kuzungushwa.
Walipamiana na kutupwa ovyo, wale huku, hawa
kule. Vilio vyao vya kichawi vikaunguruma mle
auani huku wakitapatapa kutafuta msaada.
Iliwachukua muda mrefu wakihangaika hata
majirani pamoja na wanafamilia waliokuwa
wametawanyika, sasa wakarejea kushuhudia
mtanange ule. Walikuwa wakilia kwa uchungu,
fedheha, na kukata tamaa huku wakiomboleza
kutaka msaada.
Wakati mzee Mtandi akiendelea kucheza na kile
Kibuyu, ndipo Nyembo akatoka sasa huko msalani
na kuwakuta wachawi wale waliokuwa
wamezungukwa na kundi la watu, wakiendelea
kutapatapa kama wagonjwa walio taabani bin
Sambamaji.
Baada ya dakika kama kumi za kutapatapa pale
chini, ghafla wale wachawi wakajihisi ahueni
kidogo. Taabu zikawatoka kiasi, wakawa
wanatweta tu huku wanaangaliana wenyewe kwa
wenyewe. Vurugu na zogo kutoka kwa wakaazi
waliozidi kumiminika pale vilitishia usalama wao
maana kila mtu alikuwa akisema lake na kupanga
hukumu yake dhidi yao.
“KAA CHINI MWANGA MKUBWA WE!” Nyembo
alibwata huku akiwa amemtole macho Binti
Sambayu aliyekuwa amesimama akitaka kukimbia.
Binti sambayu alihisi kurejewa na nguvu hivyo
akaamini muda wa kutoweka umewadia. Haikuwa
hivyo. Hakujua kuwa ahueni ile imetokana na
Nyembo kumwambia mzee Mtandi kuwa aache
kidogo kuzungusha kile Kibuyu ili sasa aseme nao,
sasa kutokana na ujuaji wa Binti Sambayu ikambidi
Nyembo aliyekuwa amewasimamia wale wachawi
pale uani ampe ishara nyingine mzee Mtandi akiwa
kule msalani ili aendeleze kutoa kiminyo, naye bila
ajizi akaianza tena kazi ile iliyozua tabu kwa
wachawi wale. Walitaabika vilivyo, inaonekana
kiminyo kiliwazidia mpaka baadhi wakaanza
kutapika, huku wengine wakitokwa na haja kubwa
na ndogo palepale ikiwa ni ishara mbaya kwa
mchawi yeyote akikamatwa. Ishara ya kifo!
Kama haitoshi Nyembo akachukua mijedeli na
kuwagawia wananchi wenye hasira kali kisha
wakaanza kucharaza viboko vya nguvu, Wachawi
walihangaika na kulia mpaka wakabaki hoi ndipo
Nyembo akamwambia mzee Mtandi aache kidogo
kazi yake. Akawasogelea karibu wale wachawi na
kuwamwagia maji ya baridi kutoka katika ndoo
aliyotoka nayo mle msalani, kisha sasa akaanza
kusemanao kwa utulivu na umakini.
”Leo mkifanya mchezo mtakufa hapahapa…cha
msingi ili mpate msamaha ni lazima mtueleze kila
kitu, kila siri na kila mchezo mliokwishawahi
kuufanya hapa wilayani kwetu na kwingineko…
Mmenielewa?” Alibweka tena Nyembo.
Wakamuitikia kwa vichwa tu huku nyuso zao
wakiziinamisha chini kwa fadhaa. “…Kwanza
kabisa nataka mtueleze kwanini mliwachukua
kichawi akina Nyanzala na mzee Mtandi. Pili
mtutajie watu wote mliowahi kuwaua na tatu
mtueleze jinsi mlivyokuwa mkifanya kazi zenu za
kichawi hatua kwa hatua, Sawa?” Nyembo
alitamba. Muda huo akina mama Kaguba.
Kungurume, Ilumbi, na wengine walikwishajongea
eneo la tukio, wakiwa nyuma ya Nyembo
wakimwona kama mkombozi wao licha ya kuwa
mwanzo walimbeza na kumdhihaki.
“Simama juu we’ Binti Sambayu utoe maelezo!”
Alifoka Nyembo, na hapohapo akasimama Binti
Sambayu na kuanza kutoa maelezo huku umati
wote ukiwa kimya!

SEHEMU YA KUMI
“Mimi ni kweli mchawi wa siku nyingi ila
sikupenda kuwa mchawi jamani, nilirithishwa tu na
hayati Bi…”
“NITAKUADHIBU TENA WEWE? SITAKI STORI
HAPA, NATAKA UJIBU MASWALI YANGU
NILIYOKUULIZA.” Alifoka Nyembo na kumfanya
Binti Sambayu aanze kuelezea mambo mazito
yawahusuyo wachawi wa hapo Kibondo na sehemu
kadhaa wanazohusiana nazo kikazi.
“…Sisi ni wachawi ambao tulirithishwa tu uchawi
kutoka kwa wazazi, mababu, na mabibi zetu.
Uchawi wetu uko chini ya mzimu mkubwa uitwao
GULUGUJA, Tumefunzwa na kukuzwa katika
tamaduni za kichawi mpaka tukafuzu. Wengi wetu
tuliingizwa humu tungali watoto wadogo japo kuna
baadhi walishawishiwa na kuingizwa katika kikundi
chetu cha uchawi wakiwa watu wazima…” Umati
mkubwa uliofurika uani kwa hayati masonganya
uliokuwa kimya ukisikiliza, ulishitushwa na ujio wa
ghafla katika usiku ule wa mzee mmoja ambaye
baadhi walimtambua na baadhi wakiwa
hawajamtambua. Cha ajabu wakati mzee huyo
alipoingia tu mle uani, hapohapo binti Sambayu
akaanza kulia kwa sauti ya hofu na uchungu na
kuwafanya wengi kuogopa.
Mzee yule bila ya kusalimiana na yeyote, akakatiza
katikati ya watu, akamsogea binti Sambayu na
kumnyang’anya kibuyu kidogo alichokua
amekishikilia kisha akaingiza mkono kwenye
kikapu chake cha rangi ya kaki kilichoathiriwa na
uchafu mpaka kikaonekana ni cheusi, akakiweka
kile Kibuyu na kisha akatoa kitu kama mkufu hivi
uliosukwa kwa ukindu, akamvisha binti Sambayu
shingoni. Baada ya hapo akarejea mpaka
alipokuwa amesimama bwana Kungurume na
kumpa mkono huku akimsalimu. Alikuwa ni Babu
Gao.
“Msiogope jamani nimemvisha kitu kinachoitwa
Mkanyafe yaani mkufu wa kifo, endapo atadiriki
kusema uongo basi ataangamia na kufa hapahapa
yeye na wafuasi wake wote waliopo hapa na
waliopo huko majumbani mwao, kuna mambo
mengi na ya ajabu ambayo anapaswa kuyaongea
huyu mchawi…mimi nimetembea usiku huu kwa
miguu kutokea huko kwangu mbali ili kuja kushiriki
katika kuuona mwisho wao hawa watu wabaya.”
Babu Gao aliongea kwa sauti yake kavu na ya
kukoroma kisha akamuashiria Binti Sambayu
aendelee. Naam binti Sambayu akasimulia historia
yao ya kuingia kwenye uchawi na namna
wanavyoendesha shughuli zao hatua kwa hatua.
“Ndani ya hiki kibuyu kuna nini hasa kinachofanya
kiwe na nguvu na uwezo mkubwa kiasi hiki?”
Nyembo alimsaili binti Sambayu baada ya kutoa
historia yao ambayo haikuwa na umuhimu mkubwa
sana.
“Humo kuna dawa za mitishamba tu
zilizochanganywa na vitu vingine tofautitaofauti.”
“Ni vitu gani hivyo?”
“Aaa…hu.. ku..na nywele, mkaa na..” Kabla binti
Sambayu hajafikisha neno lake mwisho watu
walimshangaa akianza kuhangaika na kutapatapa
huku mikono yake akiipeleka shingoni kujaribu
kuuzuia ule Mkanyafe uliokuwa ukimkaba mpaka
akashindwa kuhema na kuanza kukoroma.
Alikoroma huku udenda ukimtoka na macho
yakimlegea mfano wa mtu anaye karibia kufa.
“We’ si nimekukanya kusema uongo? Sasa
unataka kufa si’ ndiyo eeh?” Babu Gao alimfokea
binti Sambayu ambaye sasa hakua hata na uwezo
wa kujibu zaidi ya kunyanyua mikono yake huku na
kule kutaka msaada. Haraka Babu Gao
akamsogelea na kufanya cha kufanya mpaka
mkufu ule ukalegeza.
“Narudia tena, ukithubutu kusema uongo hapa leo
utakufa…eleza ukweli wa kila kitu,” Alibwata Babu
Gao. Watu walijikuta wakishangilia kwa tukio lile
lililowafanya sasa waamini kuwa Wachawi
wampatikana. Kufikia hapo sasa binti Sambayu
akaamua kusema kila kitu kuhusiana na uchawi
wao akihofia kuuawa na mkufu wa Babu Gao.
“…Naomba msituue jamani, ninaahidi kuwa
hatutarudia tena mchzo huu wa uchawi, tumekoma
jamani. Nitaelea…nitaeleza kila kitu…” Alilalama
binti Sambayu huku akilia na kuendelea. “…ndani
ya Kibuyu hicho kuna mchanganyiko wa vitu vingi
sana. Kuna mafuta ya watu, ngozi za maalbino,
nyongo za koboko na za simba, kitovu cha mtoto
mchanga, moyo wa kondoo, utumbo wa
mwanamke mjamzito…”
“Vitu vyote hivyo huwa mnavipataje?” alidakia
Nyembo.
“…Huwa tunwaua kwa hila watu tuwatakao,
tukishawaua ndipo usiku huwa tunawachoma na
kuwakamua mafuta yao, kama maiti ni ya
mjamzito huwa tunampasua tumbo tunamkata
utumbo wake, na kama ni ya mtoto huwa
tunachukua kitovu chake. Pia huwa tunazifukua
maiti za albino na kuchuna ngozi zao, hao Koboko
na Simba huwa tunawatega kichawi ambapo
tukishawakamata huwa tunachukua vitu kadhaa
ndani ya miili yao huku wakiwa hai…”
“Lengo la vitu vyote hivyo ni nini hasa?” Alisaili
tena Nyembo akiwa amewasimamia wale wachawi
na mijeledi yake.
”…utumbo wa mwanamke mjamzito huwa
tunauchanganya na madawa ya kienyeji kisha
tunafukia katika njia panda basi hapo kama kuna
mjamzito tuliyemkusudia, ataumwa uchungu na
kuhangaika bila kuzaa mpaka atafariki. Na hizo
nyongo za Koboko na Simba mara nyingi huwa
tunazitumia kuwasukumizia hasira watu tuwatakao
ambao hushindwa kujizuia na kujikuta wakifanya
mambo wasiyoyatarajia kama vile kuwa na nguvu
za ajabu na kumpiga mtu mpaka kumuua, au
kujinyonga mwenyewe nk. Kitovu cha mtoto
mchanga huwa tunakichangaya na majani
yatumikayo kupikia mboga ya mlenda kisha
tunamnuizia mtu tumtakaye ambapo baada ya
kukizika hicho kitovu katika kaburi la mlemavu
yeyote aliyepata kufariki, huku kwenu huyo
tuliyemfanyia hivyo ataanza kuumwa sana na
kukonda mfano wa muathirika wa Ukimwi, na hata
mkienda kumpima hospitali huonekana na ugonjwa
huo kumbe Laa!”
“Hebu tutajie majina ya watu mliowahi kuwauwa
hapa Kibondo, pia ututajie namna ya vifo
mlivyowaua…” Babu Gao alichombezaswali hilo
akiwa na lengo maalum la kuwafanya wakaazi
walichukulie lile tatizo kuwa si tu la akina mama
Kaguba, bali ni la kwao wote. Alikuwa na uhakika
kuwa wapo watakaouguswa na simulizi chafu za
binti Sambayu. Na kweli hapo ndipo kazaazaa
kilipoanza maana binti Sambayu alianza kutaja
majina ya watu waliokufa zamani na siku za
karibuni kwa vifo vya aina kwa aina. Baadhi ya
waliotajwa kuuawa kwa ajali barabarani, magonjwa
kama Ukimwi, vifo vya uzazi nk ndugu zao
walikuwapo hapo eneo la tukio. Wapo waliolia kwa
uchungu na wapo walioishia kutetemeka kwa hofu
na kwa hasira, ndipo wakajitokeza wananchi
wachache wenye ghadhabu na kuanza
kuwashambulia kwa mawe na mikoma wachawi
wale kiasi cha kuvuruga mjadala ule mtamu.
Wakati kichapo kikiendelea, ghafla wakaingia
askari polisi pamoja waliokuwa wamearifiwa juu ya
tukio hilo la ajabu. Walipofika tu wakaanza
kuwatawanya wananchi waliokuwa wakiendelea
kuwasulubu wale wachawi, kisha baada ya utulivu
kurejea, wakabaki na watuhumiwa wa Uchawi
pamoja na wahanga wa tukio hilo pamoja na mzee
Mtandi aliyetolewa kule chooni alipokuwa
amesimama na Kibuyu chake ambapo walifanya
nao mahojiano ya awali na kuamua kuwachukua
na kwenda nao kituoni kwa ajili ya mahojiano
zaidi. Pamoja na Wachawi, ndani ya gari ya Polisi
waliingia akina Mzee Mtandi, Nyanzala na
Kugurume.
Mara tu baada ya Polisi kuondoka, Babu Gao
alikichukua kile kibuyu, akakifanya alivyojua na
kukilipua moto. Kilipiga mlipuko mkali kama bomu
kabla ya kuanza kuteketea mpaka kikaisha chote.
Wakati Kibuyu kikiteketea, Wachawi wote
waliokuwa ndani ya gari ya Polisi waliteketea na
kufa wote. Cha ajabu kuna baadhi ya watu
waliokuwa majumbani mwao, nao waliteketea
kama ilivyokuwa kwa wale wachawi hivyo kudhihiri
kuwa nao walikuwa ni wachawi tu japo siku ile
hawakutoka kwenda kuwanga.
Huo ukawa mwisho wa Wachawi wote wa wilayani
hapo.
Siku mbili baadaye baada ya Polisi kujiridhisha na
kilichotokea huku wakiendelea na uchunguzi,
waliwachia akina Nyamizi na mzee Mtandi ambao
walirejea kwenye jamii yao wakiwa na mengi ya
kusimulia familia zao.

TAMATI.
 
duh Kibondo na uchawi. mtunzi anataka kusema uchawi umekwishaa. we bado kuna uchawi ndo maana wilaya haiendelei ile
 
Back
Top Bottom