Riwaya: Sala ya Sarah

Riwaya: Sala ya Sarah

RIWAYA : SALA YA SARAH

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA HAMSINI NA TATU.

ENDELEA..................

Askari walizidi kusogelea mlango wa sebule ya Sarah huku mikononi wakiwa silaha nzito. Ila kabla hawajaufikia mlango, mlango ulifunguliwa na akatoka babu yake Sarah na kutembea kuelekea getini,

"Mikono juu" Askari mmoja aliongea kwa amri ila babu yake Sarah hakuonesha kujali, alizidi kupiga hatua kuelekea getini,

"weka mikono juu mzee, ina maana husikii?" Yule Askari aliuliza ila safari hii aliipaza sauti yake huku akiamini atamuogopesha mzee yule, ila wala yule mzee hajateteleka, alizidi kupiga hatua kulisogelea geti. Askari yule akaona anafanyiwa dharau kubwa sana, ikambidi atoke kasi kumuelekea mzee, alipofika alimpiga kikumbo na yule mzee akaanguka chini, kisha yule askari akamgeuza yule mzee tumbo chini, mgongo juu na akaichukua mikono ya yule mzee na kuifunga pingu, kisha akamnyanyua,

"wewe si unajifanya jeuri" Askari aliuliza huku akimsukuma yule mzee na kutoka nae nje ya geti,

"sasa wewe vipi? Mbona mmemkamata msamalia mwema?" Polisi ambaye alikuwa kiongozi wa msafara wa polisi aliuliza na kumfanya yule askari aliyemshika mzee ashangae,

"ametoka ndani, tumempa amri amekataa kutii" Askari aliongea,

"huyu ndiye aliyetupigia simu na kutupa taharifa za kuwepo muharifu hapa, alafu sio mara moja, mara zote huyu ndiye anayetupa taharifa za muharifu" Kiongozi wa kikosi kile aliongea na kumfanya babu yake Sarah asikie uchungu kwa mara ya kwanza juu ya kauli ile, kwa kuwa aliijua alikuwa anamchoma mjukuu wake,

"mfungue pingu hiyo" Kiongozi wa kikosi alitoa amri kisha askari akatii na kumfungua pingu mzee,

"mmechelewa mbona, yule binti ameshaondoka tayari" Babu yake Sarah aliongea huku akimuangalia kiongozi wa kikosi kile,

"dah, ameelekea upande gani?" Kiongozi wa kikosi aliuliza,

"sijui, kwa kuwa mimi nilikuwa ndani, sikuweza kujua ameelekea uelekeo gani?" Babu yake Sarah alijibu na kumfanya kipindi hicho Sajenti Minja alikuwa anafika, askari wote wakampigia saluti akiwemo kiongozi wa kikosi kile cha polisi.

"mmefanikiwa kumkamata?" Sajenti Minja aliuliza huku akisimama jirani na babu yake Sarah,

"mzee anadai ameshaondoka" Kiongozi wa kikosi alijibu,

"hawa wazembe sana, nimewapigia simu muda mrefu ila ndio wamekuja sasa hivi, sijui wanamuogopa yule mwanamke?" Babu yake Sarah aliongea huku akijifanya amekasirika,

"Dokta Pendo yupo ndani?" Sajenti Minja alimuuliza babu yake Sarah,

"ndio, yupo" Babu yake Sarah alijibu,

"chukua kikosi chako na uondoke, mmeshakosea, mnapopigiwa simu mnatakiwa mfike kwa wakati" Sajenti Minja aliongea kwa amri kwa maana alihisi kama Dokta Pendo yupo ndani, basi hata Sarah atakuwa ndani.

Baada ya Sajenti Minja kutoa amri, wale askari walijilusanya na kuondoka zao huku baadhi ya askari wakilalamika chini chini kwa kitendo cha Sajenti Minja cha kuingilia kazi yao na mwisho akawafukuza bila kuwapa uhuru wa kufanya upekuzi kwenye nyumba ya Sarah.

Sajenti Minja alisimama mlangoni pale getini mpaka alipohakikisha gari ya polisi imepotea machoni mwake, kisha Sajenti Minja akaingia moja kwa moja mpaka sebuleni na kumkuta Sarah na dokta Pendo wakiwa wamekaa, kwanza wote walishtuka mara baada ya mlango kifunguliwa.

"vipi, upo salama?" Sajenti Minja aliuliza huku akichuchumaa kwenye miguu ya Dokta Pendo na wakati huo babu yake Sarah nae alikuwa akiingia ndani,

"ndio umekuja kumkamata Sarah?" Dokta Pendo aliuliza huku akimuangalia Sajenti Minja,

"wameshaondoka" Babu yake Sarah alijibu,

"kwanini ulimchukua Dokta Pendo hotelini bila kunipa taharifa?" Sajenti Minja aliuliza huku akimgeukia Sarah ambaye muda wote alikuwa kimya kwa maana alikata tamaa mara baada ya polisi kuizunguka nyumba yake, na aliamua atulie tu sebuleni huku akisubiri litakalomkuta, kwa hiyo babu yake aliposema askari wameondoka, ulikuwa muujuza mkubwa sana kwa Sarah.

"wewe si nimekuuliza? Unaniletea kiburi" Sajenti Minja aliuliza kwa hasira huku akimtazama Sarah,

"taratibu basi, kwani yeye kumchukua Dokta Pendo hotelini kuna ubaya gani, hawa si ni marafiki? au wewe unataka kuvunja ushoga wao?" Babu yake Sarah alijibu na kumfanya Sajenti Minja ashtuke, hakutegemea kama yule mzee anaweza kumtetea Sarah, Sajenti Minja akamgeukia mzee huku sura yake ikionesha mshangao wa wazi,

"siongei na wewe mzee, alafu leo mbona unamtetea sana Sarah, si alikuwa adui yako huyu, nasikia hata hawa askari niliowafukuza uliwaita wewe?" Sajenti Minja aliuliza huku akicheka na Dokta Pendo nae alikuwa akicheka ila kwa kujificha jificha,

"bwana wewe, binadamu tumeumbwa kukosea" Babu yake Sarah alijibu huku akiwa anaangalia chini,

"sasa Sarah itabidi twende kituoni, kwani ile kesi bado inaendelea na pia kumbuka kuwa una kesi nyingine ya mauaji, siku ile unatoroshwa kuna askari alikuwa" Sajenti Minja aliongea,

"na wewe nawe, kila kitu polisi, yaani kitu kidogo polisi, utadhani ulizaliwa uko?" Dokta Pendo aliongea huku akionekana hajapenda maongezi ya Sajenti Minja,

"hata mimi anamiudhi, Sarah mjukuu wangu uwe unachagua marafiki, sasa huyu mtu umemtoa wapi?" Babu yake Sarah huku akiwa anamuangalia Sajenti Minja kwa hasira na kumfanya Sajenti Minja acheke,

"Sarah huyu mzee ni babu yako, sitaki unijibu hilo, ila ninachokifanya kujua ni kuwa je, Taita ni mjomba wako?" Sajenti Minja aliuliza huku akimtazama Sarah,

"sio mjomba wake" Babu yake Sarah alijibu na kumfanya Sajenti Minja amuangalie,

.

"mzee kumbuka wewe ndiye uliyeniambia kuwa mwanao alimuoa dada yake Taita, na mwanao ndiye baba yake Sarah, sasa kwa nini unakanusha swali langu, au hujui kuwa huyu Sarah ndiye yule mjukuu wako anayeishi uingereza?" Sajenti Minja alimuuliza babu yake Sarah huku akijua kuwa babu yake Sarah atashangaa,

"ndio unanitambulisha au? Mbona najua muda mrefu tu kuwa huyu ni mjukuu wangu" Babu yake Sarah alijibu na kumfanya Dokta Pendo aangue kicheko,

"mzee miyeyusho kweli. Sarah hujanijibu, Taita ni mjomba wako?" Sajenti Minja alirudia swali lake,

"ndio, ni mjomba wangu?" Sarah alijibu, Sajenti Minja akatingisha kichwa kukubaliaba na Sarah,

"kuna kitu kimoja unanificha, wewe ni mpiganaji mzuri sana, wa ngumi na mtumiaji mzuri sana wa silaha, je haya mafunzo umeyapata wapi?" Sajenti Minja aliuliza na kumfanya Sarah ashushe pumzi nzito,

"Mimi ni mwanajeshi" Sarah alitoa jibu lililomshangaza kila mtu ndani mule,

"wa kambi gani?" Sajenti Minja aliuliza huku akificha mshangao wake,

"sio wa hapa, mimi ni raia wa uingereza" Sarah alijibu na kumfanya Sajenti Minja akumbuke kitu, alikumbuka let lile tukio la kupambana na mwanamke ndani ya ile nyumba iliyoungua na akakumbuka zile risasi mbili alizoziokota na kuzifanyia uchunguzi na kugundua kuwa zinatumiwa na jeshi la uingereza,

"kuna matukio mengi sana umeyafanya, yakiwemo ya utekaji, je ni vibaya nikikutia hatiani?" Sajenti Minja aliuliza,

"na wewe nawe unaona sifa kuwatia watu ndani" Dokta Pendo aliongea,

"nyie kaeni kimya, hapa ni mimi na Sarah tu" Sajenti Minja aliongea kwa ukali na kufanya Dokta Pendo atulie,

"unataka kuniweka hatiani? Ni sawa, ila naomba muda kidogo" Sarah aliongea kwa kujiamini,

"muda? Muda wa nini, unatakiwa uondoke na mimi muda huu" Sajenti Minja aliongea,

"ngoja nikuambie kitu, yaani wewe hapo ulipo, huwezi kunifanya chochote hata nikiamua kutokwenda polisi, na nilivyokuomba muda nimetumia busara tu, kwa hiyo niache nikamilishe mambo yangu kwanza" Sarah alijibu,

"unatupangia kazi sio, kumbuka hapa sio uingereza" Sajenti Minja aliongea,

"angalia chini ya meza" Sarah aliongea na kumfanya Sajenti Minja achungulie chini ya meza, na kipindi hicho babu yake Sarah nae alitaka kuchungulia ila Sarah alimzuia.

Sajenti Minja alipochungulia aliona mabomu mawili chini ya meza, Sajenti Minja akarudi taratibu kwenye kiti,

"ningekuwa mkorofi, ni muda sana ungekuwa umeshakufa, eidha kwa ulichokiona chini ya meza, au siku ile ulipotuona na dokta Pendo kwa mara ya kwanza, maana nilikushambulia ukapoteza fahamu, ila nikakuacha, elewa sipo hapa kumdhuru mtu, nipo hapa kudili na wanyama" Sarah aliongea ila Sajenti Minja alikuwa na wasiwasi kutokana na alichokiona,

"naomba niondoke" Sajenti Minja aliongea huku akiinuka,

"afadhali, nenda tu baba" Babu yake Sarah aliongea ila Sajenti Minja hakuongea kitu, Sajenti Minja akaondoka huku akitafakari neno ka Sarah alilosema anadili na wanyama.

"kwani uko chini ya meza kuna nini, mbona Minja alivyochungulia amekuwa mpole?" Dokta Pendo aliuliza,

"chungulia" Sarah aliongea huku akitabasamu na kumfanya babu yake achungulie, kidogo akimbie,

"hayana madhara, nimeweka kutisha watu tu" Sarah aliongea huku akiinuka katika kiti,

"shoga nirudishe hotelini" Dokta Pendo aliongea,

"nitakurudisha jioni, ngoja tule tushibe, nitakurudisha jioni ninapoenda kumalizana na Harry" Sarah aliongea huku akipotelea chumbani.

*******************

Mishale ya usiku, Trigger na Vin walikuwa ndani ya geti la Harry, na chini alikuwa mlinzi wa geti ambaye kwa muonekano wa haraka ilionekana amepoteza maisha au amepoteza fahamu,

"twende ndani, huyu tayari" Vin aliongea huku wakielekea ndani, walipofika hawakugonga hodi, wakasukuma mlango na kuingia, wakamkuta mke wa Harry akiwa na watoto wake,

"vipi shem, mbona unatutisha kwa namna ulivyoingia?" Mke wa Harry aliongea huku akitabasamu,

"jamaa tumemkuta?" Trigger aliuliza bila kujibu swali la mke wa Harry,

"ametoka, aliniambia anaweza asirudi leo" mke wa Harry alijibu,

"alikwambia anapoenda?" Vin aliuliza,


"hapana, kwani vipi? mbona mnanitisha?" mke wa Harry aliuliza,

"Harry amemuua Taita, kwa hiyo anatafutwa" Vin aliongea huku akimtazama mke wa Harry ambaye alikuwa amekamata mdomo kwa mshtuko,

"tupo hapa kulipa kisasi" Trigger aliongea na kumshangaza zaidi mke wa Harry,

"kivipi?" Mke wa Harry aliuliza huku machozi yakimtoka,

"maliza mchezo, Harry atakuwa amekimbia nchini tayari" Vin aliongea kwa sauti ndogo iliyomfikia vyema Trigger, Trigger akachomoa bastola yake na kuwamiminia risasi familia ya Harry, hakuna aliyebaki hai, wote walikufa,

"sasa wewe wahi Kiwanja cha ndege ukaangalie kama utamuona Harry, acha mimi niendelee kusubiri hapa, huenda atarudi" Vin alimwambia Trigger,

"poa mkuu" Trigger aliongea kisha akatoka zake nje na kuondoka zake.

Kipindi Trigger anaondoka, ndicho kipindi Sarah alikuwa anaingia ndani kwa kupitia ukuta, alivyotua tu ndani akaangaza macho na kuweza kuuona mwili wa mlinzi ukiwa umelala, Sarah akajua kuna uvamizi ulifanyika muda uliopita, Sarah akapata wasiwasi huku akiamini huenda ni Aisha ndio mvamizi.

Sarah akaufikia mlango wa sebuleni na kuingia, ila alichokiona ndicho kilichomstua, aliikuta miili ya watu ikiwa imelala na imetapakaa damu, macho ya Sarah yaliangukia kwenye mwili wa mtoto mdogo wa kike, kipenzi chake,

"princess!!" Sarah aliongea huku akiukimbilia mwili ya yule mtoto, alipoufikia akaubeba na kuutingisha huku akilia, alikuwa na uchungu sana, alilia huku akiamini huu mchezo umefanywa na Aisha,

"umekuja kumuua Harry au umekuja kumtuma?" Vin aliingia pale sebuleni huku akiongea maneno hayo na kumfanya Sarah ashtuke,

"ni nani aliyemuua huyu mtoto?" Sarah aliuliza kanakwamba hakuona maiti nyingine hapo sebuleni,

"na wewe unamfuata uko alipo muda si mrefu" Vin aliongea huku akiichomoa bastola yake na kufanya Sarah aamini kuwa huyu ndiye aliyefanya mauaji hayo, Sarah akachomoa kisu na kumrushia Vin, Vin akayumba kidogo kwa lengo la kukikwepa kile kisu, Vin alipokaa sawa alishuhudia teke kali likiupiga mkono wake na kufanya aiangushe bastola yake. Vin akagundua kuwa kiumbe anayepambana nae ana kasi ya ajabu sana. Vin akaamua kutumia mbinu za kujiami, yaani awe anapigana huku anarudi nyuma, Sarah akaligundua hilo, kwa kasi ile ile Sarah aliruka teke jingine kali, Vin akapiga hatua moja nyuma na Sarah akamkosa, Sarah akatua mbele ya Vin, Vin akaachia ngumi kali, Sarah akaidaka kisha Sarah nae akaachia ngumi kali, ikampata Vin usoni, Vin akaanza kuona nyota nyota, Sarah akatumia mwanya huo na kumpiga ngumi nyingi za haraka haraka, Vin akaenda chini,

Vin akajiinua na sarakasi nyepesi, akaokota pasi iliyokuwa hapo sebuleni na kumtupia Sarah, Sarah akakwepa, Vin akachukua king'amuzi na kumrushia Sarah, Sarah akainama, alipoinuka akakutana na ngumi ya Vin ikiwa imemlenga uso, Sarah akaidaka na kuunyongorota mkono wa Vin na kumfanya Sarah awe nyuma ya Vin huku akiwa ameushika mkono wa Vin kwa nyuma,

"nakuua mshenzi wewe ili kuilipa damu ya huyu malaika uliyemuua bila ya sababu" Sarah aliongea kwa hasira huku akiichomoa bastola yake, Vin alikuwa hana la kufanya, alibanwa vibaya sana.

Wakati Sarah akiwa amemshika namna ile Vin, Sarah kuna kitu alikiona kwenye mkono wa Vin, kilimshtua Sarah, aliona madoa mawili meusi kwenye mkono au Vin, tena yapo eneo lile lile kama lililopo doa lake, Sarah akajikuta amepoteza ujasiri wa kumfyatulia risasi Vin,

"Sebastian" Sarah aliita huku akimuachia Vin, Vin akashanga, ila hakutaka kujali Sarah anachofanya, Vin akamtupia ngumi nzito Sarah, Sarah hakuizuia ingawa alikuwa na uwezo wa kujikinga, ngumi ile ikatua kwenye pua ya Sarah, Vin akarusha ngumi nyingine, Sarah akamdaka mkono,

"Sebastian mimi ni dada yako, usinipige" Sarah aliongea kwa upole huku akimuachia mkono Vin, Vin akaona Sarah kama amechanganyikiwa, Vin akarusha teke na Sarah akaudaka mguu wa Vin na kumsukuma chini, Vin akadondoka

"Mimi ni dada yako, tusipigane" Sarah aliongea kwa ukali ila Vin hakuna alichojua, Vin akainuka na meza ya kioo na kumtupia Sarah, Sarah akakwepa na sasa Sarah akaamua aondoke, aliona akiendelea kukaa pale, Vin atamjeruhi na yeye hakutaka kupigana na mdogo wake.

"nitakutafuta Seba" Sarah aliongea na kisha akaanza kuondoka kwa mwendo wa taratibu bila hata kuangalia nyuma, alivurugwa akili kwa kumgundua mdogo wake.

Wakati Sarah akiondoka bila wasiwasi wowote, Vin aliimkimbilia bastola yake na kuiokota, aliamini muda huo ndio muda wa kutekeleza ahadi aliyompa baba yake (Taita).

Wakiwa wameachana umbali wa hatua kumi tu, Vin alimnyooshea Sarah bastola, ubaya Sarah hakuwa na habari na alikuwa akiendelea kutembea tu kuelekea nje.

Vin akatoa tabasamu la ushindi, hakujua anayetaka kumuua ni dada yake, Vin akiwa amelenga usawa wa kichwa cha Sarah, Vin alimfyatulia Sarah risasi, na kisha Sarah akaanguka chini................

**********ITAENDELEA**********

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA HAMSINI NA NNE.

ENDELEA..................

Sarah hakuanguka chini, ila alijitupa chini baada ya kumuona mtu akija kwa mbele yake katika mlango wa sebuleni huku akiwa ameelekeza bunduki ndani, huyo mtu ambaye ni mlinzi wa nyumba ya Harry ndiye aliyefyatua hiyo risasi, Sarah akaiona na kujitupa chini, na kitendo kile cha yule mlinzi kumfyatulia risasi Sarah, kilifanya shabaha ya Vin iyumbe na vin akajikuta mkono umemtetemeka na kufyatua risasi bila malengo na kumkosa Sarah. Vin baada ya kumkosa Sarah kutokana na kusikia mlio mwingine wa risasi, alijikuta nae akijitupa nyuma ya kochi na kujificha.

Sarah alipojitupa chini, alibiringita huku risasi zikimfuata mpaka kwenye kochi jingine, Sarah alipofika nyuma ya kochi akageuka na kufyatua risasi iliyovunja taa, sebuleni kukawa giza. Kila mtu sasa akakaa kimya wakitegeana nani ataanza kutoka ili awe ndio chambo.

Sarah akaingiza mkono mfukoni na kutoa sarafu, akairusha katikati ya sebule, sarafu ilipotua chini tu, zilipigwa risasi mfululizo kutoka kwa mlinzi na Vin, risasi zote zilielekea sehemu sarafu ilipo, Sarah akatabasamu na kujua ni wapi walipo maadui zake. Sarah akasogeza kochi alilokuwa amekaa kwa nyuma, akasikia risasi zikipiga lile kochi, ila aliona zote zikitoka kwa mlinzi, kwa upande wa Vin alisikia bastola ikifyatuliwa ila haikutoa risasi, Sarah akajua kuwa Vin amemaliza risasi, sasa akaamua kuwa makini na mlinzi tu.

Sarah kwa kasi ya ajabu aliinuka nyuma ya kochi na kupiga risasi mfululizo kuelekea mlangoni, akasikia mlinzi akipiga kelele na kisha akasikia kishindo cha mtu kuanguka. Sarah akatoka mpaka nje na kumkuta mlinzi akiwa anagalagala huku ameushika mkono wake na gobole lake likiwa pembeni. Sarah akamsogelea na kuliokota lile gobole na kulitupa mbali na mlinzi,

"pole" Sarah aliongea kwa huruma huku akimuangalia mlinzi ambaye hakujibu kitu zaidi ya kulia kwa maumivu.

Sarah akarudi mpaka kwenye mlango wa sebuleni na kuchungulia,

"fanya uondoke haraka kabla polisi hawajafika, huyu mlinzi hawezi kutumia bunduki tena" Sarah aliongea kwa sauti kubwa kiasi iliyomfikia Vin, kisha kwa njia ile ile aliyokuja nayo ndio njia ile ile aliyoondoka nayo, alipitia ukuta na kuondoka zake huku akiwa bado anamfikiria Vin kutokana na zile alama alizoziona nyuma ya mkono wa Vin.

Huku nae Vin alitoka nyuma ya kochi kwa tahadhari, hakutaka kuamini maneno ya Sarah kuwa eneo lile lipo salama. Vin alitoka kwa uangalifu mkubwa mpaka alipomuona mlinzi akiwa chini analia na mkono ukiwa umejaa dumu.

Vin akatoka kwa kukimbia mpaka nje ya geti na kuingia kwenye gari lake, akaliondoa kwa kasi huku nae akijiuliza yule mwanamke ni nani? Na kwanini amuite Sebastian? Na kwa nini hajamuua wakati alikuwa na uwezo wa kumuua? na kwanini amuite mdogo wake.

Vin alijiuliza, hakutaka kupuuza lile tukio, alipanga kulifuatilia.

*******************

Harry alirejea nyumbani kwake, aliingia getini na kukuta mlinzi hayupo, alipotupia macho kwenye madirisha ya sebuleni, aliona giza, kwa maana hiyo taa zilikuwa zimezimwa, Harry akapata wasiwasi kidogo. Akaanza kupiga hatua kuelekea kwenye mlango wa sebuleni huku mapigo ya moyo yakipiga kwa kasi, Harry akazidi kupiga hatua kuelekea mlangoni, ila kabla hajaufikia mlango, alimuona mlinzi akiwa amelala chini huku akilia na ameushika mkono wake ukiwa umejaa damu, hapo Harry alizidi kupata hofu juu ya kilichotokea,

"kuna nini kimetokea?" Harry alimuuliza mlinzi,

"Trigger alikuja na kunifunga kamba, sijui hata nini kimetokea huko ndani, maana wakati nataka kuingia nimepigwa risasi ya mkono na mwanamke na kisha amekimbia" Mlinzi alitoa maelezo yaliyomchanganya Harry,

"Mimi sikuelewi, huyo mwanamke alikuja na Trigger?" Harry aliuliza kwa wasiwasi huku akijiuliza huyo mwanamke ni nani ambaye alikuja na Trigger?

"Trigger alikuja na yule Jamaa mrefu mweusi ambaye anapenda kuvaa suti, huyu mwanamke sijajua hata muda alioingia" Mlinzi aliongea ila bado Harry hakumuelewa, alichoelewa ni huyo jamaa anayependa kuvaa suti, alijua ni Vin, hapo utumbo wa Harry ukacheza akahisi tumbo limemvuruga,. Hakutaka tena kumsikiliza mlinzi, aliamua aingie mwenyewe ndani ili aone kilichotokea,. Alipoingia ndani alipeleka mkono kwenye switch ya ukutani ili awashe taa ya sebuleni, ila aligundua switch ipo "on" yaani imewashwa, akaamua awashe tochi ya simu yake, tochi ilipowaka alijikuta akiumulika mwili wa mwanamke ukiwa umelala sebuleni, akashtuka na kummulika usoni yule mwanamke, akajikuta nguvu zinataka kumuishia, alikuwa ni mke wake na alikuwa na jeraha risasi kubwa kwenye paji la uso,

"Jane, jane, janet" Harry alimuita mke wake huku akimsogelea, ila kabla hajamfikia alijikwaa kwenye mwili wa mtoto na kujikuta akadondoka chini, akauangalia ule mwili na kugundua ni wa mtoto wake wa kiume, Harry akatoa chozi la uchungu,

"Harrison, Harrison, Princess yupo wapi?" Harry aliuliza huku akiwa ameukumbatia mwili wa mwanae wa kiume aitwae Harrison.

Harry alilia sana huku akiwa ameukumbatia mwili huo wa mwanae ambaye nae alikuwa na jeraha la risasi kwenye paji lake la uso,

"princess yupo wapi?" Harry alilia huku kamasi zikimtoka, ubaya ni kuwa hayo maswali alikuwa akiziuliza maiti, Harry akainuka na simu yake mkononi, akauona mguu wa mtoto ukiwa nyuma ya kochi, Harry akakimbilia na kumkuta mwanae princess akiwa amelala huku macho yakiwa wazi, Harry,

"nisameheni wanangu, mmehukumiwa kwa makosa ya baba yenu" Harry aliongea kwa uchungu huku akilia, alilia sana, mwisho akaamka na kusimama, akacheka, hakikuwa kicheko cha furaha,

"maisha yangu yote ndani ya dunia kumbe nilipangiwa kufanywa hivi?" Harry alijiuliza huku akicheka,

"ila sikupangiwa, inawezekana nilijipangia kuishi hivi" Harry aliongea kisha akacheka na kuanza kutoka nje huku akicheka na machozi yakimtoka,

"umeshapiga simu polisi?" Mlinzi alimuuliza,

"polisi!!?" Harry aliuliza kisha akacheka, na kumfanya mlinzi ahisi bosi wake amechanganyikiwa,

"wataharifu polisi" Mlinzi aliongea huku akiwa anamtazama Harry,

"wakija ndio watarudisha uhai wa familia yangu?" Harry aliuliza huku akimtupia simu mlinzi, kisha Harry akaelekea nje ya geti na kuondoka zake huku akicheka na kumuacha mlinzi akishangaa tu. Baada ya Harry kuondoka, mlinzi akaiokota simu na kupiga namba za msaada kituo cha polisi kuwataharifu juu ya tukio lililotokea.

***************

Sajenti Minja alifika kwenye nyumba ya Harry akiwa ameambatana na askari kadhaa pamoja na waandishi wa habari.

Sajenti Minja alipofika kwanza aliingia ndani na kukagua maiti kwa kutumia tochi walizoenda nazo, baada ya hapo wakatoa nafasi kwa wapiga picha wachukue picha.

Baada ya hapo miili ilipakiwa kwenye gari na kupelekwa kwenye kuhifadhiwa hospitali. Sajenti Minja aliondoka na mlinzi wa Harry kwenda kumuhoji.

Walifika kituoni na kisha Sajenti Minja akamuongoza mlinzi mpaka ofisini kwake na kumkaribisha kiti, kisha akammiminia kahawa kwenye kikombe kilichopo juu ya meza,

"ni nini kilitokea kabla ya mauaji?" Sajenti Minja alianza na hilo swali,

"swali sijalielewa" Mlinzi alijibu,

"ooh sawa, je unatambua ya kuwa wewe ni muhusika wa kwanza wa yale mauaji?" Sajenti Minja alibadili swali,

"hapana, mimi sihusiki kwa lolote na ndio maana niliwapigia simu" Mlinzi alijibu kwa uoga,

"kama wewe uhusiki, je unaweza kututajia muhusika?" Sajenti Minja aliuliza,

"sitokuwa na uhakika, ila kuna rafiki yake Harry aliingia na kunipiga nikapoteza fahamu, huyo ndiyo namuhisi ni muhusika, aliingia ndani na mwenzake" Mlinzi alijibu,

"anaitwa nani?" Sajenti Minja aliuliza tena,

"Trigger, namfahamu kwa jina hilo, ila yule mwenzake aliyeongozana nae simjui jina, namjua sura tu" Mlinzi alijibu,

"baada ya wao kuingia ndani ni nini kilifuata?" Sajenti Minja aliuliza,

"kwa kuwa nilipoteza fahamu sikujua kilichotokea, ila fahamu ziliponirejea niliamua niingie sebuleni na nikamkuta yule kijana aliyeingia na Trigger, alikuwa na mwanamke ndani" Mlinzi alijibu,

"Alafu?" Sajenti Minja aliuliza

"nilijaribu kuwashambulia ila walitumia akili, walivunja taa za sebuleni na kisha wakatumia mbinu hiyo kunishambulia na kunipiga mkono" Mlinzi alijibu,

"huyo mwanamke ulifanikiwa kumuona sura yake?" Sajenti Minja aliuliza,

"hapana, kwa maana macho aliyaacha wazi, ila Kuanzia puani kushuka chini alijiziba na kitambaa". Mlinzi aliongea na kumfanya Sajenti Minja atambue kuwa mwanamke huyo ni Sarah, kwa maana wamekutana mara kadhaa akiwa amejifunga hivyo.

"Baba wa familia amepata taharifa?" Sajenti Minja aliuliza,

"alikuja na ameona kilichotokea, ila ameondoka akiwa anacheka, itakuwa amechanganyikiwa" Mlinzi aliongea na kumfanya Sajenti Minja ashangae,

"anacheka? Hajasema kitu chochote?" Sajenti Minja aliuliza,

"kwa muonekano wa haraka ilionekana amechanganyikiwa, hakuwa katika hali nzuri" Mlinzi aliongea,

"umejaribu kumpigia simu?" Sajenti Minja aliuliza,

"simu niliotumia kuwapigia ni simu yake, alinipa baada ya kumwambia awapigie nyinyi, kwa maana hiyo uko alipo hana simu" Mlinzi aliongea kwa utulivu,

"sawa mzee, itabidi uende hospitali, alafu urudi ulale kituoni" Sajenti Minja alimwambia mlinzi,

"kituoni tena, ila mimi sina kosa" Mlinzi aliongea kwa kulalamika,

"haimaanishi una kosa, ila tunafanya hivyo kwa ajili ya usalama wako" Sajenti Minja aliongea kisha akamuita askari ambaye alimpa maagizo ya kumpeleka mlinzi hospitali na baada ya matibabu arudishwe selo.

Baada ya askari yule kutoka na mlinzi, Sajenti Minja alibaki peke yake ofisini,

"Sarah ameiangamiza familia ya huyu bwana, kwanini?" Sajenti Minja alijiuliza,

"na huyo Trigger ni nani?" Sajenti Minja aliendelea kujiuliza bila kupata jibu, mwisho akaamua aondoke aende Kulala ili apumzishe akili.

Sajenti Minja akatoka na kuingia kwenye gari yake na kuiondoa kwa mwendo wa wastani.

********************

Usiku ule Vin alirudi ndani ya chumba chake ndani ya Vin hotel huku mawazo juu ya kuponea kifo mikononi mwa Sarah yakiwa yamemkaa kichwani.

Vin akafungua friji na kutoa soda, akaimiminia kwenye bilauri na kuinywa taratibu, kisha akasimama na kuvua koti la suti, akaliweka ndani ya kabati,

"Alafu mwisho amemjeruhi mlinzi na kuniambia nikimbie kabla polisi hawajafika, huyu mwanamke ni nani? au anataka kuniteka akili ili baadae anitumie?" Vin aliwaza huku akijitupa kwenye kochi lililopo ndani ya chumba hicho.

Vin alitamani kwenda hospitali muda huo ili amueleze kilichotokea, ila alihofu muda huo ingekuwa ngumu kupewa ruhusa ya kuingia hospitali kwa kuwa muda ulikuwa umeenda sana.

"eti dada yangu, dada gani shetani?" Vin aliendelea kujiuliza na muda huo mlango wa chumba chake uligongwa. Akainuka na kwenda kufungua, alimkuta Trigger akiwa amesimama mlangoni,

"pita ndani, vipi umefanikiwa kumpata Harry?" Vin alimuuliza Trigger,

"hapana, nimezunguka sana nimemkosa" Trigger alijibu,.

"atapatikana tu" Vin aliongea huku akikaa vizuri kwenye kochi,

"hata nyumbani hajarudi, au hukukaa sana?" Trigger aliuliza,

"alikuja Sarah aisee" Vin aliongea kwa upole,

"umemmaliza? au nini kimetokea?" Trigger aliuliza kwa shahuku ya kutaka kujua,

"Tumepambana sana, ila mwisho wa siku alinizidi uwezo na kuniwekea bastola kichwani, ila ghafla akawa mpole na kuniita mimi mdogo wake" Vin aliongea kwa sauti tulivu na kumfanya Trigger ashtuke,

"Alafu?" Trigger akauliza,

"ebu Trigger kuwa muwazi, Sarah ni nani?" Vin aliuliza kwa utulivu,

"yule ni shetani, anatakiwa kufa" Trigger aliongea huku akiwa ana wasiwasi,

"amesema mimi ni mdogo wake na kweli ameshindwa kuniua ingawa alikuwa na uwezo wa kufanya hivyo. Je mimi ni mdogo wake kweli?" Vin aliuliza huku mkono ukiwa shavuni, ila Trigger alisita kujibu, alihisi Vin kuna kitu amekijua,

"aisee tutaonana kesho" Trigger aliongea huku akiinuka kwenye kiti,

"hujanijibu wewe, Sarah ni dada yangu?' Vin aliuliza huku akiwa amemshika mkono Trigger, Trigger akasimama na kumgeukia Vin, kisha Trigger akafikiri kwa muda,

"ndio, Sarah ni dada yako" Trigger alijibu na kumfanya Vin ashtuke..................

************ITAENDELEA***********

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA HAMSINI NA TANO.

ENDELEA..................

"Dada yangu? Kivipi?" Vin aliuliza kwa mshangao,

"kwa sisi watanzania mwanamke yoyote anaweza kuwa dada yako, hiyo ndiyo maana yangu" Trigger alijibu,

"kwa hiyo sina unasaba nae?" Vin aliuliza,

"unasaba utoke wapi na wakati wewe umezaliwa marekani na unaishi uko, kama ungekuwa na ndugu yako si baba yako angekuambia? Muda mwingine utumie akili bwana" Trigger aliongea kumshawaishi Vin,

"unaweza kwenda" Vin aliongea huku akiuachia mkono wa Trigger,

"lakini umenielewa, si ndio?" Trigger aliuliza,

"nenda Kaka, si umeshanijibu?" Vin aliongea kwa ukali na kumfanya Trigger aondoke huku akitabasamu, ila pia alikuwa na wasiwasi na kitendo cha Vin kuhoji unasaba wake na Sarah.

****************

Sarah alifika nyumbani kwake huku akiwa na uchungu sana, kitu ambacho kilimpa uchungu ni kile kitendo cha kukuta familia ya Harry yote imekufa,

"kwanini Vin ameua watu wasio na hatia?" Sarah aliongea kwa uchungu huku akilia,

"Sarah mama, vipi mbona unalia?" Babu yake aliuliza huku akiingia sebuleni kutoka chumbani kwake,

"babu nimemuona Sebastian mdogo wangu, ila naona amekuwa katili sana" Sarah alitoa habari ya kushangaza kwa babu yake,

"umemuona wapi na umejuaje huyo ni ndugu yako?" Babu yake Sarah aliuliza,

"si zile alama ulizonielekeza, nimeona anazo mbili sehemu kama ilipo ya kwangu" Sarah aliongea kwa uchungu,

"ebu mchunguze tena, maana utotoni kwenu uliwahi kumuunguza na uji, kwa hiyo ana baka la moto mgongoni, ebu kamchunguze" Babu yake Sarah aliongea kwa udadisi,

"nitafanya hivyo, ila yule ni yeye tu, nakumbuka sana siku ile Taita anachoma nyumba yetu, alituchukua mimi na Seba na kutupakia kwenye gari lake, ila baadae Harry akamshauri anishushe mimi na kunirudisha ndani, kisha wao wakabaki na Seba. Na ndio maana mwili wa Seba hakuonekana baada ya nyumba kuungua na hakuna aliyejua huo mwili ni wapi ulipo?" Sarah aliongea na kufanya babu yake atingishe kichwa kuonesha amekubaliana nae,

"au nipeleke nikamuone" Babu yake Sarah aliongea,

"sipajui anapokaa, alafu hata nikikupeleka bado hatokujua" Sarah aliongea,

"sasa utafanyaje ili akujue? " Babu yake Sarah aliuliza,

"dunia ya leo imeendelea, tutatumia hata sayansi" Sarah alijibu,

"mama lakini angalia mapambano hayo, usije ukapoteza uhai" Babu yake Sarah alimuonya,

"mzee, kusanya nguo zako zote muhimu, kesho tunahama hapa" Sarah aliongea huku akiinuka kwenye kochi na kuingia ndani na kumuacha babu yake akiwa anashangaa maamuzi ya ghafla ya mjukuu wake.

******************

Asubuhi ya leo Sajenti Minja aliamkia ofisini kwake, alipofika alifungua makabrasha yanayohusu kesi ya Sarah, akayapitia na mwisho akaona atafute chanzo cha ugomvi wa Taita na Sarah.

"sasa kama Sarah ana ugomvi na Taita, na kwanini aende akaiteketeza familia ya Harry jana? Huyo Harry ni nani?. Sarah ana hatia, na nikiendelea kumlegezea kamba anaweza kufanya mauaji ya kutisha sana" Sajenti Minja aliongea peke yake huku akiifunga kabrasha la kesi ya Sarah, kisha akainuka na kutoka mpaka eneo ilipo kaunta ya polisi,

"chukua askari watano na gari, hakikisha wanabeba bunduki zenye risasi, alafu nifuateni" Sajenti Minja alitoa agizo kwa askari aliyemkuta hapo, kisha Sajenti Minja akaelekea kwenye gari yake na kuingia, akawa anasubiri agizo lake litimizwe.

Baada ya dakika tano, gari ya polisi ilikuwa tayari imeshajaa askari waliokuwa na silaha, Sajenti Minja akawasha gari yake na kuiondoa, huku nyuma gari ya polisi ilikuwa ikimfuata.

Walitembea kwa mwendo wa muda kidogo, kisha Sajenti Minja akaisimamisha gari yake mbele ya geti la nyumba ya Sarah, na ile gari ya polisi ikasimama ikasimama. Sajenti Minja akatelemka, na kupatwa mshangao, alikuta geti la nyumba ya Sarah likiwa na kufuri, akasogelea jirani na geti na kuchungulia,

"askari wawili nifuateni" Sajenti Minja aliongea kisha akarudi nyuma hatua mbili na kukimbia kwa kasi kuelekea getini, alipofika aliruka na kukamata geti kwa juu kisha akajivuta na kuangukia ndani ya geti.

Askari wakabaki nje wakiwa wanashangaa namna mkuu wao alivyoingia ndani, hawakuwahi kudhaii kama anajua kufanya vitu kama hivyo, walijua ni mzembe tu,

"nyie mnafanya nini uko nje, ingieni" Sajenti Minja aliongea kwa ukali na kufanya wale askari wa nje wagutuke, na wao wakaingia ndani kwa mtindo huo huo alitumia Sajenti Minja.

Sajenti Minja alikuta gari ya Sarah ikiwa imeegeshwa ndani, alipojaribu kufungua mlango akakuta imefungwa, akaanza kuelekea moja kwa moja kwenye mlango wa sebuleni, napo akakuta kumefungwa na kufuri kubwa, Sajenti Minja akaishika ile kufuri na kuutingisha, kisha akazunguka upande wa nyuma wa nyumba na kukuta kufuri nyingine.

Sajenti Minja akatoa simu yake mfukoni na kujaribu kupiga namba ya Sarah, ikawa haipatikani, akatabasamu,

"tuondokeni" Sajenti Minja akaongea kisha akaanza kuondoka na kufanya askari wengine wakamfuata, walipofika getini wakatoka kwa mtindo ule ule walioingia nao, walipofika nje Sajenti Minja akawaruhusu askari wengine waondoke, kisha yeye akaingia kwenye gari yake na kuliondoa kwa mwendo wa haraka.

Safari ya Sajenti Minja iliishia katika hotel ambayo alikuwa anakaa Dokta Pendo, alifika na kwenda moja kwa moja mpaka kwenye chumba cha Dokta Pendo. Alipofika mlangoni aligonga hodi, lakini hakujibiwa, akarudia tena lakini bado hakukuwa na jibu,

"anaoga au?" Sajenti Minja alijiuliza huku akirudia tena kupiga hodi, lakini hakuna aliyejibu, akaamua asukume mlango ila ulionekana umefungwa. Sajenti Minja akatoa simu na kupiga namba ya Dokta Pendo, haikupatikana, Sajenti Minja akarudisha simu mfukoni kisha akaamua arudi mpaka mapokezi,

"samahani dada, yule binti wa chumba namba kumi na tisa ametoka?" Sajenti Minja alimuuliza Muhudumu,

"yule aliyevunjika miguu?" Muhudumu naye akauliza,

"huyo huyo" Sajenti Minja akajibu,

"ameondoka na yule dada ambaye anakujaga hapa, yule mwenye nywele ndefu" Muhudumu aliongea na kufanya Sajenti Minja aelewe huyo dada ni Sarah,

"wameondoka muda gani?" Sajenti Minja aliuliza,

"mapema sana, saa kumi na mbili asubuhi" Muhudumu alijibu,

"sawa basi, ngoja nikuachie namba yangu, wakirudi utanipigia" Sajenti Minja aliongea huku akiitoa simu yake mfukoni,

"wakirudi? Yaani wameondoka moja kwa moja na funguo wamerudisha, na deni lote amelipia yule dada" Muhudumu alijibu na kumfanya Sajenti Minja ashtuke,

"sawa" Sajenti Minja aliongea na kutoka zake nje huku akiwaza ni wapi Sarah alipoelekea na Dokta Pendo?

Sajenti Minja aliingia ndani ya gari yake na kuondoka huku akiwa hajui ni wapi ataanzia kumtafuta Sarah.

*******************

Mtaa mmoja wa uswahilini sana, anaonekana Harry nyakati za usiku akiwa amevaa suti yake nyeupe, haikuwa safi kama anavyokuwa kila siku, suti ilikuwa chafu sana, tokea siku ya tukio la familia yake kuuawa, Harry hakuwahi kubadili nguo.

Harry hakuwa na viatu, mguu mmoja ulikuwa na soksi moja nyeusi na mguu wa pili haukuwa na kitu, ulikuwa peku.

Harry alitembea mwendo wake wa haraka haraka huku akiongea na kucheka peke yake, hakuwa na akili timilifu, akili zake ziliyumba kutokana na familia yake kuteketea yote kwa wakati mmoja.

Safari ya Harry iliishia chini ya daraja ambalo chini yake hakukuwa na maji mengi yakipita, ila kulikuwa na uchafu kiasi, Harry alivyofika alivuta mabox kadhaa aliyokuwa ameyachomeka ukutani na kuyatandika chini, kisha akalalia huku akiongea peke yake.

Wakati akiwa amelala hapo, alihisi mtu akimgusa mgongoni,

"leo sijalala upande wako, usinisumbue" Harry aliongea kwa ukali kisha akacheka, ila bado alihisi mtu akimgusa tu, Harry akageuka kwa hasira na sura yake ikakutana na Sarah,

"mwisho umekuwa hivi, elimu yako imeishia hapo" Sarah aliongea kwa sauti ndogo huku akimtazama Harry. Harry akanyanyuka na kukaa,

"Sarah umekuja, umekuja kuniua?" Harry aliuliza na kisha akacheka kwa sauti kubwa,

"ukitaka kufa utakufa, hukumbuki ahadi niliyokuambia hawali, kuwa sitokuua mpaka utakapotaka?" Sarah aliuliza na kutabasamu,

"utanichoma moto?" Harry aliuliza huku akicheka,

"hapana, moto utachomwa akhera" Sarah aliongea na kutabasamu,

"nani alikuonesha nilipo? Je familia yangu imezikwa vizuri kwa heshima?" Harry aliuliza huku machozi yakimtoka,

"hakuna aliyenionesha ulipo, kuhusu familia yako ni kwamba wamezikwa, wamezikwa vizuri tu, ni vizuri ukienda kuyaona makaburi yao" Sarah aliongea kwa huruma baada ya kuona machozi ya Harry,

"Sarah, Taita amenigeuka, amemtuma Trigger auwe familia yangu, na vin nae ameshiriki" Harry aliongea kwa uchungu,

"malipo ya kazi uliyomfanyia ni hayo" Sarah alijibu,

"je unahitaji nikusaidie kwenye kesi yako?" Harry aliuliza,

"bado nahitaji msaada wako" Sarah aliongea,

"hakuna mahakama itayokubali kusikiliza ushahidi wa kichaa, mimi ni kichaa Sarah, najijua" Harry aliongea na kufuta machozi,

"wewe malaya upo huku, ni vizuri nimewakuta wote" ilikuwa sauti ya Vin, alitokea ghafla na kumuelekezea Sarah bastola, Harry akaangusha kicheko,

"muue, muue tu" Harry aliongea huku akicheka na Sarah nae hakuwa na la kufanya,

"usaliti umekufanya umekuwa kichaa" Vin aliongea kwa hasira huku akimtazama Harry,

"kichaa ni nani kati yangu na yako?" Harry aliuliza huku akicheka,

"mpumbavu wewe, unajiona mzima?" Vin alimuuliza Harry huku bastola yake ikiwa bado amemuelekezea Sarah,

"Sarah muangilie huyu, msamehe kwa kuwa hana akili timamu" Harry aliongea huku akimtazama Sarah,

"wewe bwabwaja hapo ukimaliza nikufumue ubongo wewe pamoja na huyu malaya" Vin aliongea kwa dharau huku akitabasamu,

"Dada yako unamuita malaya? Ndio maana nakuita kichaa" Harry aliongea na kucheka na kumfanya Vin ashangae,

"Seba mimi ni dada yako, ukweli anajua huyu na Taita" Sarah aliongea kwa upole huku akimuangalia Vin,

"Dada yangu kwa maana ya mtoto wa shangazi yangu, Baba alishaniambia ukweli, ila undugu haupo tena kwa kuwa umemuua mama yangu" Vin aliongea kwa hasira,

"majinuni wewe, bila mimi hata wewe ungekufa, mimi ndiye niliyetoa wazo la wewe kuondolewa kwenye moto, vinginevyo wewe, mama yako na baba yako wote mngekuwa marehemu" Harry aliongea na kucheka kwa nguvu,

"una maana gani?" Vin aliuliza,

"Baba yako na mama yako wameshakufa, Taita ndiye aliyewaua kwa moto na kisha akakulea wewe kwa kuwa hakuwa na uwezo wa kuzaa" Harry alijibu na kumfanya Sarah machozi yamtoke baada ya kauli ya Harry na kuamini sasa kuwa Sebastian mdogo wake ndiyo huyo Vin,

"mnanichezea akili nyinyi wajinga" Vin aliongea kwa hasira,

"wewe ni mdogo wangu, na kukuhakikishia tu kwa kutokukuua siku ile nyumbani kwa Harry, na pia kingine ni kwamba una baka mgongoni, baka la moto, nilikuunguza na uji wakati tukiwa watoto" Sarah aliongea na kumfanya Vin ashtuke, ni kweli ana baka mgongoni, hakuna mtu aliyewahi kuliona hilo baka, uwa analificha sana kwa maana mwanajeshi wa marekani hutakiwi kuwa na kovu lolote mwilini, kwa hiyo hujitahidi sana kulificha kovu lake.

"Taita ni mbwa tu, anakutumia na mwisho wa siku atakuua kama alivyokutuma uniue" Harry aliongea huku akicheka,

"kama huamini twende tukapime DNA, wewe ni msomi najua unajua DNA haiongopi" Sarah aliongea huku akimuangalia Vin aliyekuwa bado ameshika bastola,

"hapana, msiniletee maigizo" Vin aliongea huku akili yake na maneno yake vikianza kupingana.

Sarah akachomoa bomba la sindano kutoka kwenye mfuko wa nguo yake, kisha akajichoma kwenye mshipa mkubwa wa mkononi na kuvuta damu, baada ya hapo akachomoa bomba la sindano na kulifunga kwa juu, kisha akamtupia Vin,

"utachunguza kwa muda wako" Sarah aliongea na kisha akageuka kwa lengo la kuondoka,

"ukipiga hatua nakuua" Vin alimtahadharisha Sarah,

"mjinga kweli, muue tu, muue dada yako ili Taita awe shujaa na wewe uwe umemalizia kizazi chako kwa upumbavu wako" Harry aliongea huku akimtazama Vin,

"kama uliweza kuua watu wanne wa familia moja, sitoshangaa ukiniua mimi mtu mmoja" Sarah aliongea na kuanza kuondoka taratibu bila kujali bastola aliyoelekezewa na Vin,

"Sarah, nadhani nimekusaidia kwa mara ya kwanza leo, nimeongea ukweli mbele ya mdogo wako, sijasema ukweli ili unisamehe, nimeongea ukweli kwa kuwa sitaki huyu Vin afuate njia niliyopita mimi kwa Taita. Vin kama umeua familia yangu ni sawa, umeniua mimi pia, nimekusamehe kwa kuwa umelipa kisasi cha mimi kushiriki mauaji ya wazazi wako wewe na Sarah" Harry aliongea huku machozi yakimtoka, ila hakuacha kucheka.

"usiongee upuuzi wa kunivuruga akili, nitakuua wewe" Vin aliongea kwa hasira huku akimgeuzia bastola Harry,

"siogopi kufa, sioni sababu ya kuishi sasa, maisha yangu yameshaisha, natamani sana kufa, sihitaji kuishi tena. Bora nife nikaiombe radhi familia yangu kwa maana wamekufa kwa upumbavu wangu" Harry aliongea kwa uchungu, hakuwa akicheka tena alikuwa akilia,

"kwa hiyo unataka kufa?" Vin aliuliza huku huruma ikianza kumuingia,

"Niue kama unaweza, sihitaji kuishi" Harry alijibu huku akilia, ila bila mtu yoyote kutegemea, Sarah kwa kasi ya ajabu alitoa bastola yake na kumfyatulia Harry risasi mbili za kichwa, Harry akafa pale pale, na huo ndio ukawa mwisho wake.

Vin akapigwa na butwaa huku akiwa haelewi ni kwanini Sarah amefanya vile.

Sarah akageuka na kuanza kuondoka taratibu huku Vin akiwa anamuangalia na bastola yake ikiwa mkononi.........

**********ITAENDELEA***********

the Legend☆
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom