SEHEMU YA 21
ILIPOISHIA:
“Tunaenda kuvamia benki?” nilijiuliza nikiwa ni kama siamini. Aliendelea kutuchorea mchongo mzima unavyotakiwa kufanyika, na akasema hatutaenda wote, bali watachaguliwa wachache kati yetu watakaoungana na Kikosi A kwa ajili ya kazi hiyo. Moyoni nikawa namuomba Mungu nisiwe miongoni mwa watakaochaguliwa.
SASA ENDELEA...
“Kila mmoja akae tayari, muda wa kuondoka utakapofika mtatangaziwa waliochaguliwa,” alisema Bosi Mute wakati akikamilisha kutupa mchongo wa kazi hiyo. Aliondoka na kutuacha mle ndani, tukawa tunatazamana, kila mmoja akiwa kimya kabisa.
Basi baadaye tulitoka na kila mmoja akaendelea na kazi yake maana licha ya kazi hiyo, kila mtu alikuwa na kitengo chake, mimi nikaelekea kule kwenye kazi yangu ya kuosha magari. Kulikuwa na magari kama matatu hivi yaliyoingia jana yake, basi nikavaa nguo za kazi na kuanza kuyaosha huku mawazo kibao yakiendelea kupita ndani ya kichwa changu.
Ilipofika kama saa tisa hivi za mchana, magari mawili, Toyota Noah, yote yakiwa na rangi nyeusi na vioo vya tinted, yaliwasili na kuingia pale ndani. Nikaona pilikapilika zimeanza, nikajua sasa mambo yamewiva.
Kila mtu aliacha alichokuwa anakifanya na kuanza kuangalia ni nini kinachoendelea, nilimuona Bonta akiwakusanya wale wenzake ambao wote walikuwa wakubwa kwetu. Wakaingia kwenye chumba cha mikutano, sijui walikuwa wakijadiliana nini lakini muda mfupi baadaye, tulianza kuitwa mmojammoja.
Na mimi nilipoitwa, niliacha kila kitu na harakaharaka nikaelekea kwenye kile chumba cha mikutano huku mapigo ya moyo yakinienda mbio kwelikweli. Nilipofika, niliwakuta wenzangu watatu ambao tulikuwa pamoja kwenye Kikosi B, kwa hiyo na mimi nikawa wa nne.
Muda mfupi baadaye, yaliletwa masanduku mawili, yakawekwa pale mezani na Bonta akatuambia kila mmoja anatakiwa kuanza kujiandaa. Masanduku yalifunguliwa, la kwanza lilikuwa na nguo vikiwemo viatu kama vile wanavyovaa wanajeshi na makoti marefu meusi, na lile lingine lilikuwa na bunduki.
Tukaambiwa kila mtu achague vitu vinavyomfaa, tukawa tunatetemeka kwelikweli. Walianza akina Bonta, wakachukua vya kwao, ikafika zamu yetu. Hakukuwa na muda wa kupoteza, kwa hiyo kila mtu alichukua vitu vyake na tukaanza kubadilisha mlemle ndani kama tulivyokuwa tukipewa maelekezo.
Muda mfupi baadaye, kila mmoja alikuwa ameshavaa, kiukweli nguo hizo zilitubadilisha kabisa, sasa tukawa kwenye mwonekano wa kijambazi kwelikweli. Tulipewa pia kofia na miwani myeusi, baada ya kumaliza, Bosi Mute alikuja na kuanza kutukagua mmoja baada ya mwingine.
Ni kama alijua jinsi sisi ambao ndiyo ilikuwa mara yetu ya kwanza tulivyokuwa na hofu, akawa anatutoa hofu na kutuambia tunatakiwa kujiamini. Akaendelea kutupa mchoro wa jinsi kazi inavyotakiwa kufanyika na mwisho akatuambia kwamba Jombi ndiye atakayekuwa kiongozi wa msafara.
Sikuwa namjua sana huyo Jombi zaidi ya kuwa namuona mara mojamoja pale kambini. Alikuwa ni kipande cha mtu, amekwenda hewani halafu ‘amepasuka’ kwelikweli kutokana na mazoezi. Muda wote macho yake yalikuwa mekundu kama ‘nyanya’ na sikumbuki kama nimewahi kumuona akitabasamu au kucheka tangu nianze kumuona.
Kila mmoja alikabidhiwa bunduki yake, wale wakubwa wakachukua mbilimbili, bunduki kubwa na bastola, sisi tukapewa mojamoja. Baada ya hapo, tulitengeneza kama duara hivi, Bosi Mute akiwa katikati, akawa anaendelea kututoa hofu na kusisitiza kwamba anatuamini na hatuwezi kumuangusha.
Baada ya hapo, tulishikana mikono wote kwa pamoja kisha tukagongesheana ngumi na harakaharaka tulitoka kule nje, yale magari yalikuwa yamesogezwa mpaka mlangoni, tukaingia kwa makundi mawili, kila moja likiwa na mchanganyiko wa wakubwa wawili na wadogo wawili. Ukichanganya na madereva, kila gari lilikuwa na watu watano, safari ikaanza.
Tulitoka kwa mwendo wa kasi huku watu wote wakiwa wanatutazama, tukaingia barabarani na magari yakawa yanakimbia kwa kasi kubwa sana. Sikuwa nawajua madereva ni akina nani lakini walionesha kuwa ni wazoefu sana.
Safari yetu iliishia kwenye mtaa mmoja wenye pilikapilika nyingi, eneo ambalo baadaye nilikuja kulitambua kwamba ni Tandika. Tulisimama kwenye barabara ya vumbi ya mtaa huo, mita chache kutoka kwenye barabara ya lami.
Dakika chache baadaye, tuliona yale magari yanayotumika kubebea fedha na kuzisambaza kwenye benki mbalimbali, likipita kwenye barabara ya lami huku nyuma likiwa linasindikizwa na gari la polisi. Kwa wanaoyajua magari ya kubebea pesa watakuwa wanaelewa vizuri, lilikuwa ni kama Hiace ndogo lakini likiwa limezibwa pande zote.
Harakaharaka madereva walipeana ‘signal’, lile gari la mbele ambalo ndiyo nililokuwa nimepanda mimi, likaondoka kwa kasi na kuingia kwenye barabara ya lami, tukawa tunalifuata lile gari lililobeba fedha na lile gari jingine, liligeuza na kupita mtaa wa pili, sikuelewa linaelekea wapi.
Kulikuwa na magari mengine kadhaa katikati yetu, dereva akawa anajaribu kuyapita kwa fujo, mwisho likabakia gari moja mbele yetu, kisha gari la polisi halafu ndiyo lile gari lililobeba fedha.
Jombi ambaye tulikuwa naye kwenye gari moja, alitoa ishara kwamba kila mmoja ajiandae kwa kazi, huku nikitetemeka, niliitoa bunduki yangu niliyokuwa nimeivaa shingoni na kuificha ndani ya koti refu, nikaishika vizuri na kutoa ‘safety lock’, tayari kwa chochote.
“Gari litakaposimama tu, tunawaangusha kwanza hawa waliopo kwenye gari la polisi, wewe na wewe mtabaki kutoa back-up, hakikisha yeyote anayesogea mnamuangusha,” aisema Jombi huku akinioneshea mimi na yule mwenzangu, tukatazamana huku kijasho chembamba kikiwa kinatutoka.
Lile gari la lilikatiza na kuingia upande wa kulia, gari la polisi nalo likafuatia. Dereva wetu alipunguza mwendo kidogo, akalitoa gari barabarani, tukashuhudia yote mawili yakienda na kusimama nje ya tawi dogo la benki. Askari waliwahi kushuka, wakawatawanya watu wote waliokuwa nje ya ile benki.
Kulikuwa na skari kama sita hivi, wote wakiwa na silaha lakini pia kulikuwa na askari wengine kwenye lile gari lenye fedha ambao wao walivaa nguo za tofauti, tukawaona pia walinzi wa ile benki wakiungana nao kuhakikisha hakuna kinachoharibika.
Hata kabla ya tukio lenyewe, nilishajua kwamba hatuwezi kufanikisha tunachoenda kukifanya kwa sababu kwa hesabu za harakaharaka, wao walikuwa wengi kuliko sisi.
Kumbe dereva alikuwa anasubiri tu maelekezo, Jombi alipotoa ishara tu, dereva alikanyaga mafuta kwa nguvu kisha akakata kona na kuelekea pale wale askari walipokuwa wametanda.
Wakati wale askari wakishtuka na kuelekezea mitutu yao kwenye gari letu, lile gari jingine lilitokea upande wa pili, kwa kasi ileile, kwa hiyo wakawa ni kama wamepatwa na kiwewe, ndani ya sekunde chache tu, wote tulikuwa tumeshashuka kwenye magari yote mawili kwa staili ya kikomando kama tulivyofundishwa kule porini, tukawa tumewazunguka wale polisi na walinzi.
Jombi ndiye aliyekuwa wa kwanza kufyatua risasi, na ya kwanza ilimlenga mmoja kati ya wale askari, tena kichwani! Akadondoka chini kama mzigo, kilichofuata baada ya hapo ilikuwa ni kama uwanja wa vita.
Tuliwafyatulia mvua ya risasi kutoka pande mbili, nao wakawa wanajibu mapigo lakini kwa kuwa tulikuwa tumewazunguka, tuliwazidi ujanja. Ndani ya sekunde chache tu, watu wote walikuwa chini, si polisi, si walinzi, watu waliokuwa jirani wakawa wanakimbia huku wakipiga kelele, kila mmoja akiokoa maisha yake.
Kama tulivyoelekezwa, mimi na yule mwenzangu tulibaki kama ‘back-up’ kuhakikisha hakuna mtu anayesogea kwenye eneo la tukio, Jombi, Bonta na wengine kutoka kwenye lile gari, wakakimbilia mpaka kwenye lile gari huku wakiendelea kufyatua risasi.
Kwa kuwa tayari gari lilishakuwa limefunguliwa na sanduku la fedha kutolewa, hawakupata shida, wakaanza kusaidiana kuliburuza huku risasi zikiendelea kurindima.
Dereva wa lile gari letu alilisogeza mpaka pale karibu na lile sanduku kwa kasi mithili ya magari ya mashindano, Akina Jombi wakalibeba lile sanduku lililoonekana kuwa zito kwelikweli na kuliingiza ndani ya gari. Waliingia ndani ya gari na dereva akaondoka kwa kasi kubwa, sekunde chache tu baadaye tayari walishaingia barabarani.
Kimbembe kikabakia kwetu sisi wawili tuliobaki kutoa ‘back-up’ kama tulivyoelekezwa, lile gari la pili lilikuwa limepaki kama mita hamsini hivi kutoka pale tulipokuwepo, kwa hiyo ilikuwa ni lazima tulikimbilie haraka iwezekanavyo na kuungana na wale wenzetu wawili ambao nao walibaki kama ‘back-up’, kibaya ni kwamba wote tulikuwa ni kutoka Kikosi B.
Tukiwa tunalikimbilia kwa tahadhari kubwa huku tukifyatua ovyo risasi, tulishtukia magari mengine mawili ya polisi yakiingia kwa kasi ya kimbunga, askari wengi wakaruka kabla hata hayajasimama na kuanza kutufyatulia risasi kama mvua.
Je, nini kitafuatia?
Sent using
Jamii Forums mobile app