Riwaya: Niacheni nikufuru

Riwaya: Niacheni nikufuru

SIMULIZI: NIACHENI NIKUFURU.

MTUNZI: FAHAD MUSSA

EMAIL: fahadmussa55@gmail.com


UTANGULIZI

Usinishangae kwa haya niyasemayo, usinishangae kwa haya niyaandikayo. Ndio, usinishangae. Sijaandika haya nikiwa nimelewa, sijaandika haya nikiwa usingizini, bali ninayaandika haya nikiwa na akili zangu timamu bila kushurutishwa na mtu. Nayasema haya kwa herufi kubwa, "NIACHENI NIKUFURU". Ndio, narudia "NIACHENI NIKUFURU".

Niite Singu kama ninavyofahamika na wengi hapa mtaani. Ila kama utahitaji utambulisho wangu kamili basi niite "JOHNSON ALFREDY NZAGAMBA", msukuma halisi kutoka Maswa mkoani Simiyu. Japo kwa sasa nipo Dodoma kikazi ila sitoacha kupakumbuka kwetu. Ninapakumbuka Seng'wa kama kijiji nilichozaliwa. Kijiji kilichonipa mengi mazuri, ila pia kimenipa Jinamizi la kutisha lililonitesa kwa takribani miaka 10. Jinamizi hilo si jingine, bali ni "JACKLINE", mwanamke nimchukiae kupita wanawake wote duniani. Mwanamke shetani na katili asiye na utu!!!!!!


****SEHEMU YA KWANZA****

Saa kumi jioni, nipo zangu Baa. Baa iliyo takribani nusu kilomita kufika kwangu ninapoishi. Ni umbali mfupi sana usiohitaji hata baiskeli kufika hapo nikitokea nyumbani, nyumba ya Bwana Singu kama ninavyojulikana na wengi. Wimbo wa msanii Christian Bella aliomshirikisha Ommy Dimpoz ujulikanao kama "Nani kama mama" ndio ulikuwa unasikika kutoka kwenye spika mbili chakavu zilizokosa matunzo, na zenyewe bila hiyana wala manung'uniko zilishindana kutoa sauti.
Nikiwa nimekaa kwenye kiti huku nabugia bia yangu ya tatu tangu niingie kwenye ile baa, akili yangu ilitekwa na ule wimbo. "Eti nani kama mama, yani hawa wasanii wamekosa kabisa vya kuimba hadi wawasifie wanawake?, wanawasifia wanawake kwa kipi?, ni hawa hawa wanaoenda kuchepuka nje ya ndoa na kukubambikia mtoto makusudi pasipo wewe mwanaume kujua?. Au mimi ndo sielewi tofauti ya mama na mwanamke?. Aaaah, waende zao huko, wanajifanya kutuzalia watoto kumbe ni mashetani tu, hahahahaha," niliutafakari ule wimbo huku nikijitahidi kuuchambua nini haswa madhumuni ya muimbaji. Ila nikaona kuzidi kuuchambua ni kujiumiza tu kichwa pasipo na sababu ya msingi. Huu wimbo ulishaniharibia "mood" yangu kabisa ya kuendelea kubaki pale. Nikamuita muhudumu ili nilipie vinywaji nilivyokunywa. Alipokuja nikampatia elfu kumi na kusubiria chenchi yangu, cha ajabu huyu muhudumu akajifanya kunichekea chekea huku akiniomba nimnunulie bia kwa ile chenchi iliyobaki. "Wewe mwanamke, sinaga mazoea na jinsia ya kike mimi, nenda kaombe kwa wengine ila sio kwangu. Niletee haraka chenchi yangu niondoke", niliongea kwa sauti ya kilevi huku nimekunja ndita. Yule muhudumu akaondoka kwa hasira huku amebetua mdomo wake kama tetea aliyenusurika kupandwa na koo. Sikulijali hilo, nilichohitaji muda ule ni chenchi yangu tu. Na kweli, baada ya dakika zisizozidi nne akaniletea chenchi yangu nami nikaondoka kuelekea nyumbani.

"Sijui niseme nipo 'single' au niseme nimeoa, nashindwa kuelewa nijitambulishe vipi kwenu, maana huu ni mwezi wa tisa tangu nimtie machoni mwanamke anayefahamika kama mke wangu (Sina uhakika kama kweli natakiwa kumuita mke ama la ijapokuwa nilifunga nae ndoa). "Mama Glory,ni pepo lipi limekukumba wewe mwanamke?, ni raha ipi unayoipata huko ulipo hadi ukaamua kunitelekeza mimi na mtoto?. Haikutosha kuondoka peke yako, ukaamua kunitilia na sumu kwenye chai ili nipotee kwenye huu uso wa dunia. Kwanini ulitaka kuniua mama Glory?, kwanini ulifanya vile Jackline?, kwanin.........", nilijikuta natoa machozi peke yangu pale sebuleni huku nikiwa nimekaa kwenye sofa zenye kupamba sebule yangu. Nikajaribu kuwasha japo luninga ili niondoe msongo wa mawazo ila nayo ndo kwanza ikazidi kunikera. Nyimbo ya 'Super woman' iliyoimbwa na msanii wa marekani ajulikanae kama Alicia keys ndo ulikuwa unasikika. "Kwa u-super upi walionao hawa viumbe?, au u-super wa kuwasababishia waume zao vilema vya maisha?", niliwaza kichwani, nikaamua kuzima luninga yangu nikaelekea chumbani kulala kwani saa yangu ilionesha ni saa tatu na robo usiku. Sikujisumbua kutafuta chakula, tumbo langu ni la kijeshi, hata nikipitiliza siku nzima bila kula wala halilalamiki. Lishapitia maumivu mengi kushinda haya ya kukaa na njaa. Na maumivu yote hayo yalisababishwa na huyu shetani mtu ajulikanae kama Jackline au 'MamaGlory'.

MIAKA ISHIRINI ILIYOPITA.SIMIYU TANZANIA

"Sisi kama wana nzengo wa eneo hili, tukishirikiana na ndugu wa karibu wa Bwana Mabula tumejadiliana mengi katika kikao hiki na wote kwa pamoja tumeazimia kuwa maeneo yote aliyokuwa anamiliki Bwana Mabula Nzagamba yatakuwa chini ya usimamizi wa mdogo wake, ajulikanae kama Kashinje Nzagamba. Vipi, kuna mwenye pingamizi?",mwenyekiti alimaliza kwa kuuliza swali huku akiiangalia hadhira yake. Hakuna aliyeonekana kupinga hoja ile. "Basi nafunga kikao hiki mpaka wakati mwingine tena. Kama kutakuwa na chochote kitakachoendelea tutazidi kupeana taarifa", mwenyekiti alifunga kikao na wote walioshiriki kikao kile wakaanza kutawanyika kuelekea makwao.
Mama Singu, mke wa mzee Mabula ni miongoni mwa waliokuwepo katika kikao kile na ni miongoni mwa watu waliofurahishwa na maamuzi yale, kwani mumewe 'Bwana Mabula' alikuwa ni mdhaifu kitandani kwa takribani miaka miwili sasa. Ugonjwa wa kiharusi ulikuwa umeshambulia sehemu kubwa ya mwili wake na kumfanya ashindwe hata kuinua unyoya wa kuku, sembuse kuihudumia familia yake?. Na kama tujuavyo, rasilimali kubwa kijijini ni ardhi, pasipo kulima utateseka sana.
"Singuuuu, we singuuu", mama aliniita muda mfupi baada ya kurejea kutoka kikaoni. "Naaam, nakuja", niliitika huku nikikimbia mkuku mkuku kuelekea kule sauti ilipotokea. Nilimkuta mama sebuleni akiwa amesimama na bamdogo, nikawaamkia kisha nikamsikiliza mama alichoniitia. "Natoka na baba yako mdogo, kuna sehemu tunaelekea. Naweza nikachelewa kurudi au nisirudi kabisa siku hii ya leo, kwahiyo kuwa makini na baba yako. Akiamka tu umpatie zile dawa zake. Pia usisahau kukaa nae karibu, akichafua mazingira usafishe,si unaijua hali yake?", mama alinipa maagizo huku akinikazia macho. "Ndio nimeelewa, nitakuwa makini", nilimjibu. Akaniaga na kutokomea na bamdogo, sikujua wapi walipoelekea ila ninachokumbuka ni kwamba zilipita siku mbili tangu aondoke pale nyumbani, ndipo akarejea.

*Mama Singu alienda wapi na Bamdogo?
*Vipi kuhusu hali ya Baba?
USIKOSE SEHEMU IJAYO.KILA SIKU ZA WIKI ITAKUWA INAPATIKANA HAPA HAPA





Sent using Jamii Forums mobile app
 
Habarini wakuu, nitakuwa hapa kuwaletea simulizi hii "Niacheni nikufuru" mpaka pale itakapoisha. Yote itaishia hapahapa Jukwaani.

Kila siku nitakuwa naachia kipande kimoja kulingana na maelekezo kutoka kwa mwandishi.

NB: RIWAYA HII HAIUZWI.INATOLEWA BURE

Sent using Jamii Forums mobile app
Ikiisha naomba uni tag asee...
Arosto siiwezi
 
SIMULIZI: NIACHENI NIKUFURU

MTUNZI: FAHAD MUSSA

EMAIL: fahadmussa55@gmail.com


********PENDEKEZO/ USHAURI*******


Natoa ushauri huu wa bure kwa kuwa mimi JOHNSON ni muhanga wa hili tatizo.
Huu usemi wa "NANI KAMA MAMA" au "MAMA NI MUNGU WA PILI" naomba utumike kwa vigezo maalumu. Huu usemi usiwahusu hawa 'manungayembe'.



*****SEHEMU YA PILI******

Je, umewahi kusikia au kumshuhudia mtu fulani tajiri mwenye kusaidia masikini, wagonjwa na hata wenye shida mbalimbali?. Na watu hawaachi kumsifia huyu tajiri kwa huruma na msaada anaoutoa katika jamii. Ila upande wa pili wa shilingi wa huyu tajiri ni jambazi sugu aliyekubuhu na muuzaji wa madawa ya kulevya. Ni kiumbe mwenye kuumiza upande fulani ila ni mwenye kufariji upande tofauti na ule anaouumiza. Basi nakupa 'Home work', nenda kalitafakari hilo. Sikulazimishi kuamini ninachoamini mimi wala wewe usinilazimishe niamini unachokiamini wewe, hiyari ni yako, kuyanywa ama kuyamwaga. Niite 'JOHNSON ALFREDY NZAGAMBA'.

Endelea..............................

Mimi ni mtoto wa mwisho katika familia ya Bibi na Bwana Mabula na umri wangu ni miaka 30 kwa sasa. Nimetanguliwa na kaka zangu wawili 'Luhende' na 'Ngasa' ambao hao walianza kujitegemea ningali bado mtoto mdogo.
Kwahiyo siku ambayo mama aliondoka na bamdogo katika safari isiyojulikana, ndio siku niliyoweza kukaa na baba na kusimuliwa mambo mengi sana. Niliyajua hata mambo ambayo sikupaswa kuyajua katika umri ule. Baba akaanza kunieleza huku bado akiwa amejilaza kitandani.
...................."Singu mwanangu, ya dunia ni makubwa kushinda ukubwa wa dunia yenyewe. Najua bado ni mtoto ila ipo siku isiyo na jina utayakumbuka haya ninayokueleza hapa. Mama yako anakupenda sana, na anapenda mafanikio yako, lakini hanipendi mimi", baba aliongea kwa tabu huku akijitahidi kutafuta pumzi na kuendelea kunisimulia. "Nashindwa kuelewa ni kosa lipi kubwa nililomkosea hadi ananifanyia haya. Najua katika umri wote nilioishi na mama yako kuna kipindi huwa tunapishana maneno na muda mwingine kununiana hata wiki nzima au miezi, ila bado tuliendelea kuwa wamoja. Ni uchungu moyoni kukueleza kuwa wewe si mtoto wangu wa kukuzaa, baba yako mzazi ni mzee Ombeni", baba aliposema hivyo akanyamaza kidogo huku akiniacha na bumbuwazi. Kwa umri wangu wa miaka kumi ilitosha kabisa kuelewa nini baba anamaanisha. Na mzee Ombeni namfahamu vizuri, ni mwenyekiti wetu wa kijiji. Sio siri nilishangaa sana ila nikashindwa niongee nini. Baba aliendelea kuzungumza, "Wanakijiji wote wanalijua hilo na hata sura yako unafanana kila kitu na mzee Ombeni. Mke wangu alichepukia kwa mzee Ombeni na kuniletea huu ujauzito pasi na mimi kujua", baba akashindwa kuendelea kuongea, akawa analia na mimi nikawa na jukumu la kum'bembeleza. Tulishindwa kuendelea na mazungumzo, baba alisema niingie jikoni nimchemshie uji apashe tumbo joto. Huo ndio ulikuwa mwisho wa maongezi yetu kwa siku ile. Niliingia jikoni, nikamuandalia baba yangu uji, hatimae nikaelekea chumbani kwake na kuanza kumnywesha.Hakuwa na nguvu za kunywa peke yake, mwili wote ulikuwa umepooza isipokuwa mguu mmoja tu wa kushoto.

Sio siri, nimefanana sana na mzee 'Ombeni', na pia nimewahi kusikia zaidi ya mara nne watu wakisema kuwa mimi ni mtoto wa mzee Ombeni, ila sikutilia maanani kauli zao, baba niliyemjua mimi ni Mzee Mabula tu. Ila leo kwa masikio yangu nathibitishiwa ya kwamba mimi ni mtoto wa mzee Ombeni. Hapo ndipo nikaanza kukumbuka hata baadhi ya matukio ya nyuma niliyowahi kufanyiwa na mzee Ombeni. Kuna siku alinikuta machungani nachunga ng'ombe, alinifuata hadi nilipo akasema ameongea na mama kuhusu shule, inabidi nihame nikasome shule yenye hadhi kuishinda ile ya kijiji. Anapenda nisome kwa bidii bila usumbufu wowote. Na kweli, baada ya mwezi mmoja nikafanyiwa uhamisho na kuamia shule ya mtu binafsi yenye gharama kubwa kuishinda ile ya kijiji na mzee Ombeni ndie aliyekuwa akinilipia ada na mahitaji yote ya shule. Na pia nimewahi kumsikia mama akinisisitiza sana nimpende mzee Ombeni na nije kumsaidia mbeleni nitakapofanikiwa, kwa kuwa ana roho ya huruma na upendo juu yangu. Sikujua mama alimaanisha nini, mimi niliitikia tu.

Mpenzi msomaji, kwa miaka yangu hii 30 niliyonayo hivi sasa ninaposimulia kisa hiki, na kwa mengi niliyopitia, nimegundua kwamba, mwanamke ni sawa na tajiri muovu, anasaidia upande mmoja na kuugandamiza upande mwingine. Kwahiyo, kwa mtazamo wangu mimi JOHNSON NZAGAMBA, siwezi nikamsifia sana mwanamke eti kisa yupo tayari kufa kwa ajili ya mwanae. Hujiulizi ni mangapi anayafanya ya kuumiza upande wa pili pasipo huruma?. Wanaume wangapi wanalea watoto wasio wao?, wanaume wangapi wamegeuzwa tu vivuli katika ndoa zao?. Siri zote zipo kifuani kwa mwanamke. Dunia isivyo na aibu, inadiliki kusema eti 'nani kama mama'. Labda waseme 'nani kama mama mwenye hofu ya mungu na asiyeweza kudanganya kwa mumewe'.
Hawa wamama wa kidijitali hawana sifa ya kuitwa "Mungu wa pili", wala hawana sifa ya kuitwa 'Mungu wa duniani'. labda tuwaite "shetani wa pili". Neno langu si sheria, likufaalo lichukue na likuchukizalo niachie. Ila usithubutu kunishawishi eti nibadili fikra zangu, TUTAGOMBANA.

Ule usiku sikuweza kulala vizuri, niliwaza sana. Hata asubuhi palipokucha niliona aibu kusimama mbele ya baba. Nilijiona kama mgeni ndani ya nyumba niliyoizoea na mgeni pia mbele ya baba niliyemzoea. Ila ningefanya nini kingine zaidi ya kutulia tu?.Basi mchana ukapita na giza likachukua nafasi yake. Nakumbuka ilikuwa ni baada ya kuchemsha michembe (Viazi vitamu vilivyomenywa na kukaushwa, hutumika haswa kipindi cha kiangazi. Ni chakula maarufu sana kule kwetu usukumani). Nilipakua chakula cha kunitosha, nikala. Baada ya kumaliza kula nilimuandalia na baba na kuanza kumlisha. Hapo sasa ndipo kizaa zaa kingine kilifata. Kumbe, kaka Luhende ni mtoto wa bamdogo. Yani bamdogo amezaa na mama yangu mzazi. Sikujua kwanini baba aliamua kunieleza yote yale. Akanieleza kuwa, hata hii safari ya mama aliyoenda na bamdogo kusikojulikana, ni safari ya wapenzi wapendanao, sio safari ya mtu na shemejie. Hata baba hakuagwa na mama kama anatoka. Bali taarifa ya mama kuondoka ni mimi nilimpatia baba.

TUKUTANE TENA KESHO PANAPO MAJAALIWA.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Habarini wakuu, nitakuwa hapa kuwaletea simulizi hii "Niacheni nikufuru" mpaka pale itakapoisha. Yote itaishia hapahapa Jukwaani.

Kila siku nitakuwa naachia kipande kimoja kulingana na maelekezo kutoka kwa mwandishi.

NB: RIWAYA HII HAIUZWI.INATOLEWA BURE

Sent using Jamii Forums mobile app
Karibu sana naona member since may 2020 ila una vitu adimu keep it up humu kuna kila aina ya watu kuwa mvumilivu utapongezwa,utakejeriwa,utadhihakiwa kuwa na busara ukishindwa kumjibu mtu vzr basi kaa kimya hata km kakutukana maana hujui huyo unaemjibu ni nani na mtakutana wapi yangu ni hayo karibu sana na kila la kheri mkuu!

Sent using Jamii Forums mobile app
 
RIWAYA: NIACHENI NIKUFURU

MTUNZI: FAHAD MUSSA

EMAIL: fahadmussa55@gmail.com


*****SEHEMU YA TATU*****

Ya Ngoswe mpe Ngoswe, na ya Mazoea muachie Mazoea. Ni miaka ishirini sasa imepita tangu tumzike Baba. Sitaki kukumbuka tena ya Baba na Mama, maana hata mimi sasa ninayo mengi tu yaliyonisibu, tena yanaweza kuwa makubwa kushinda yale yaliyomtokea Baba. Ila nikutoe hofu tu mpenzi msomaji, mama yangu bado mzima wa afya ingawa amezeeka sana sahizi, wajukuu ndio wanaomfariji. Nami kila ninapopata muda siachi kwenda kijijini kumtembelea huyu mama yangu kipenzi.


MIAKA KADHAA ILIYOPITA

Ni likizo yangu ya kwanza kuipata tangu niajiriwe miezi michache iliyopita kama Ofisa rasilimali watu katika halmashauri ya wilaya ya Chemba mkoani Dodoma. Ni likizo hii ndio iliyoharibu kila kitu katika maisha yangu. Ni likizo hii ndio niliyoitumia kwenda kijijini kwetu kulibeba Jini Jackline na kuja nalo mjini. Yes, sijakosea, "Jackline au Mama Glory" ni jini haswa, limeninyonya hadi mifupa baada ya damu kuisha.

Nilidhani ndoa ni 'kuvaa shera na suti' na kucheza kwaito ukumbini huku tukilishana keki, kumbe ndoa ni zaidi ya maumivu ya pilipili machoni. Shahada yangu ya "Usimamizi wa Rasilimali watu" niliyoipata chuo kikuu cha Makerere Uganda, nyumba niliyopewa na ofisi, gari na mshahara wa kukizi mahitaji yangu vilinitia jeuri nikajiona muda wa kuoa umetimia. Sikujua kwamba "MWANA KULITAKA, MWANA KULIPATA". Hakika nimelipata.


*******KIJIJINI SENG'WA********

........."Jack, nakupa hongera kipenzi changu kwa kuwa mvumilivu kwa kipindi chote hiki tangu ningali chuo hadi sasa nimeajiriwa, hongera sana", niliongea kwa sauti ndogo ya mahaba huku nikibinya binya matiti malaini ya malaika wangu Jackline, tukiwa watupu ndani ya chumba changu.

......"Usijali Singu, kuwa mvumilivu ni jukumu langu, nakupenda sana ndio maana nikaamua kukutunzia tunda lako.Mimi ni wako peke yako, na itabaki kuwa hivyo. Nakupenda pia laazizi wangu".Jack alinijibu kwa sauti yake laini huku akipapasa papasa ndevu zangu zilizochongwa kwa mpangilio maalumu.

........"Hii harusi ikishapita tu, naomba tukimbilie kwetuuuu tukajenge familia. Kuishi kibachela nimechoka, kila siku nakula mgahawani chakula kibovu wakati mpishi wangu upo hapa", niliongea kwa sauti ya manung'uniko huku nikigusa gusa kiuno chake kilaini.

......."Kuhusu hilo ondoa shaka mume wangu, hata mimi naogopa unavyokula huko hotelini wanaweza wakakutilia limbwata mwisho wa siku umsahau mkeo bureee", Jackline alinijibu kwa sauti yake ya kudeka iliyonifanya nisichoke kumsikiliza kila anapoongea.

Hatukuendelea kuongea tena, bali sauti za kitanda na Godoro ndizo zilizochukua nafasi kwa purukushani tulizokuwa tunazifanya pale kitandani. Hakika ni furaha iliyoje kuwa karibu na mtu umpendae, nae awe anakupenda. Hakika Jack ni miongoni mwa wasichana wachache sana wenye kupenda kujiweka "smart" na kuendana na ukisasa, tofauti na mabinti wengine pale kijijini ambao muda wote ukikutana nao ni wachafu, kuanzia nguo hadi ngozi. Hata kwa uzuri wa sura na shepu, Jack wangu hakuwa na mpinzani pale kijijini. Weupe wake wa ngozi ndo kabisaaa ulinivutia, kama mnavyojua sisi wasukuma tunavyopenda mabinti weupe. Ni heri usiwe na meno ila uwe mweupe tu basi inatosha, wakukuoa watajazana kwenu hadi ukimbie mwenyewe.
Tulimaliza kuvunja amri ya sita, na hatimae nikamsindikiza kurudi kwao nami nikarudi nyumbani.

Baada ya wiki mbili, harusi kubwa ilifanyika pale kijijini, Mimi JOHNSON ALFREDY NZAGAMBA nikamuoa rasmi JACKLINE KASHINJE. Harusi ilifana sio siri, wenye kula walikula na wenye kulewa walilewa. Baada ya wiki moja za kukamilisha taratibu za kimila na kupokea baraka za wazazi, safari ya kurudi mjini ikaanza.

.........................................................................................

SHAIRI KWA JACK WANGU

Kama kupenda ni dhambi, niacheni niitende.
Sina shida ya maombi, motoni acha niende
Nipo radhi niwe zombi, au nife kama mende
Kwa Jack naweka kambi, niacheni nimpende

Kama kupenda ni kosa, wala musijisumbue
Kwa Jack nimeshanasa, sitaki muninasue
Kama zigo la kutesa, niache musinitue
Ole ataye mgusa, nipo radhi nimuue.
...........................**************...........................


Hilo ni shairi nililomtungia Jack wangu siku chache kabla hatujafunga ndoa. Ila leo hii ukiniambia nichague kimoja kati ya "kunyongwa" au "Kuliimba hili shairi", basi mimi nitachagua kunyongwa, kuliko kuimba huu ujinga niliouandikaga siku chache kabla ya harusi yangu na yule pepo mchafu "Jacline".

Naweza kukiri kwamba mwaka wa kwanza wa ndoa yetu na Jackline ulikuwa ni mwaka furaha sana. Tuliishi kwa upendo na amani. Najua kuna kupishana maneno ya hapa na pale ila mwisho wa siku tulielewana. Nilifanikiwa kujenga nyumba yangu ndani ya miaka miwili tangu nianze kazi, na pia hata ofisi nilihamishwa kutoka wilaya ya Chemba hadi makao makuu ya mkoa "Manispaa ya Dodoma. Hapa sasa ndipo mambo yakaanza kubadilika.

Mimi si mtu wa kujichanganya sana na watu, nina marafiki wachache sana tangu nihamie hapa makao makuu. Rafiki yangu mkubwa ni Idris na Godfrey. Hawa ndio watu ninaoweza kukaa nao na kuzungumza mambo mbalimbali kuhusiana na kazi zetu na stori nyingine nyingi ingawa kicheo nimewapita, mimi ni Boss wao.
Godfrey, kama nilivyo mimi nae ameoa na ana watoto wawili, mimi bado sijabahatika kupata mtoto. Ila Idris yeye hajaoa ingawa anaishi na mpenzi wake "Roida", ni mwaka wa tatu tangu waanzishe mahusiano.

Siku ya Jumapili ya mwisho wa mwezi nilimualika nyumbani, Idris na mpenzi wake "Roida" ili tupate kujumuika kwa pamoja katika chakula cha mchana na kuzungumza mawili matatu kama marafiki na majirani.

.........."Shem samahani, unaweza kuturuhusu tuondoke na 'mamito' ili akapajue kwetu, maana kila mara unakuja wewe tu alafu misez hata hapajui", ilikuwa ni sauti ya Roida wakati wa kuagana akiniomba nimruhusu Jackline waondoke pamoja nae kuelekea kwao ili akapajue.

........."Usijali shemeji yangu, nyie nendeni tu hamna tatizo. Huwa nasahau kuja nae kwenu kisa mambo mengi kichwani yamenitinga, ni kweli ukisemacho.Ni muhimu akapafahamu munapoishi ili siku likitokea la kutokea iwe rahisi kuwasiliana", nilimjibu Roida huku tukiwa tunafungua lango la geti kuu kutoka nje.

.............."Wanawake bhana, yani hapa Roida ndo kafurahi mwenyewe ulimvyomruhusu aondoke na shemeji", akadakia Idris huku akimpigapiga Roida vikofi vya utani mgongoni.

............."Hahahahaha, ndo hivyo. Sitaki mwanamke mwenzangu ajifungie ndani tu wakati hata kwetu hapajui", alijibu Roida huku wakipanda kwenye gari lao 'TOYOTA Harrier New model'.

Jackline nae aliagana na mumewe na kumuahidi kuwa hatochelewa kurudi, hatimae akaingia garini na Idris akalitoa gari kuliingiza barabarani.


NYUMBANI KWA IDRIS

................"Roida, fanya basi kama nilivyokuelekeza, nahitaji kulala na Jack hata sahizi kama itawezekana", ilikuwa ni sauti ya Idris akimsisitiza Roida. Wawili hao wakiwa chumbani huku Jackline wakimuacha sebleni akiangalia luninga.

........."Usijali Iddy, Jack ushamnasa. Ngoja niende sebuleni nikaweke mambo sawa alafu nitakuja kukushtua", Roida alijibu huku akiinuka na kufungua mlango kuelekea sebuleni alipo Jackline.

*Roida na Idris wana mipango gani ya siri?. Je, hawa sio wapenzi?

USIKOSE SEHEMU IJAYO.


















Sent using Jamii Forums mobile app
 
RIWAYA: NIACHENI NIKUFURU

MTUNZI: FAHAD MUSSA

EMAIL: fahadmussa55@gmail.com


*****SEHEMU YA TATU*****

Ya Ngoswe mpe Ngoswe, na ya Mazoea muachie Mazoea. Ni miaka ishirini sasa imepita tangu tumzike Baba. Sitaki kukumbuka tena ya Baba na Mama, maana hata mimi sasa ninayo mengi tu yaliyonisibu, tena yanaweza kuwa makubwa kushinda yale yaliyomtokea Baba. Ila nikutoe hofu tu mpenzi msomaji, mama yangu bado mzima wa afya ingawa amezeeka sana sahizi, wajukuu ndio wanaomfariji. Nami kila ninapopata muda siachi kwenda kijijini kumtembelea huyu mama yangu kipenzi.


MIAKA KADHAA ILIYOPITA

Ni likizo yangu ya kwanza kuipata tangu niajiriwe miezi michache iliyopita kama Ofisa rasilimali watu katika halmashauri ya wilaya ya Chemba mkoani Dodoma. Ni likizo hii ndio iliyoharibu kila kitu katika maisha yangu. Ni likizo hii ndio niliyoitumia kwenda kijijini kwetu kulibeba Jini Jackline na kuja nalo mjini. Yes, sijakosea, "Jackline au Mama Glory" ni jini haswa, limeninyonya hadi mifupa baada ya damu kuisha.

Nilidhani ndoa ni 'kuvaa shera na suti' na kucheza kwaito ukumbini huku tukilishana keki, kumbe ndoa ni zaidi ya maumivu ya pilipili machoni. Shahada yangu ya "Usimamizi wa Rasilimali watu" niliyoipata chuo kikuu cha Makerere Uganda, nyumba niliyopewa na ofisi, gari na mshahara wa kukizi mahitaji yangu vilinitia jeuri nikajiona muda wa kuoa umetimia. Sikujua kwamba "MWANA KULITAKA, MWANA KULIPATA". Hakika nimelipata.


*******KIJIJINI SENG'WA********

........."Jack, nakupa hongera kipenzi changu kwa kuwa mvumilivu kwa kipindi chote hiki tangu ningali chuo hadi sasa nimeajiriwa, hongera sana", niliongea kwa sauti ndogo ya mahaba huku nikibinya binya matiti malaini ya malaika wangu Jackline, tukiwa watupu ndani ya chumba changu.

......"Usijali Singu, kuwa mvumilivu ni jukumu langu, nakupenda sana ndio maana nikaamua kukutunzia tunda lako.Mimi ni wako peke yako, na itabaki kuwa hivyo. Nakupenda pia laazizi wangu".Jack alinijibu kwa sauti yake laini huku akipapasa papasa ndevu zangu zilizochongwa kwa mpangilio maalumu.

........"Hii harusi ikishapita tu, naomba tukimbilie kwetuuuu tukajenge familia. Kuishi kibachela nimechoka, kila siku nakula mgahawani chakula kibovu wakati mpishi wangu upo hapa", niliongea kwa sauti ya manung'uniko huku nikigusa gusa kiuno chake kilaini.

......."Kuhusu hilo ondoa shaka mume wangu, hata mimi naogopa unavyokula huko hotelini wanaweza wakakutilia limbwata mwisho wa siku umsahau mkeo bureee", Jackline alinijibu kwa sauti yake ya kudeka iliyonifanya nisichoke kumsikiliza kila anapoongea.

Hatukuendelea kuongea tena, bali sauti za kitanda na Godoro ndizo zilizochukua nafasi kwa purukushani tulizokuwa tunazifanya pale kitandani. Hakika ni furaha iliyoje kuwa karibu na mtu umpendae, nae awe anakupenda. Hakika Jack ni miongoni mwa wasichana wachache sana wenye kupenda kujiweka "smart" na kuendana na ukisasa, tofauti na mabinti wengine pale kijijini ambao muda wote ukikutana nao ni wachafu, kuanzia nguo hadi ngozi. Hata kwa uzuri wa sura na shepu, Jack wangu hakuwa na mpinzani pale kijijini. Weupe wake wa ngozi ndo kabisaaa ulinivutia, kama mnavyojua sisi wasukuma tunavyopenda mabinti weupe. Ni heri usiwe na meno ila uwe mweupe tu basi inatosha, wakukuoa watajazana kwenu hadi ukimbie mwenyewe.
Tulimaliza kuvunja amri ya sita, na hatimae nikamsindikiza kurudi kwao nami nikarudi nyumbani.

Baada ya wiki mbili, harusi kubwa ilifanyika pale kijijini, Mimi JOHNSON ALFREDY NZAGAMBA nikamuoa rasmi JACKLINE KASHINJE. Harusi ilifana sio siri, wenye kula walikula na wenye kulewa walilewa. Baada ya wiki moja za kukamilisha taratibu za kimila na kupokea baraka za wazazi, safari ya kurudi mjini ikaanza.

.........................................................................................

SHAIRI KWA JACK WANGU

Kama kupenda ni dhambi, niacheni niitende.
Sina shida ya maombi, motoni acha niende
Nipo radhi niwe zombi, au nife kama mende
Kwa Jack naweka kambi, niacheni nimpende

Kama kupenda ni kosa, wala musijisumbue
Kwa Jack nimeshanasa, sitaki muninasue
Kama zigo la kutesa, niache musinitue
Ole ataye mgusa, nipo radhi nimuue.
...........................**************...........................


Hilo ni shairi nililomtungia Jack wangu siku chache kabla hatujafunga ndoa. Ila leo hii ukiniambia nichague kimoja kati ya "kunyongwa" au "Kuliimba hili shairi", basi mimi nitachagua kunyongwa, kuliko kuimba huu ujinga niliouandikaga siku chache kabla ya harusi yangu na yule pepo mchafu "Jacline".

Naweza kukiri kwamba mwaka wa kwanza wa ndoa yetu na Jackline ulikuwa ni mwaka furaha sana. Tuliishi kwa upendo na amani. Najua kuna kupishana maneno ya hapa na pale ila mwisho wa siku tulielewana. Nilifanikiwa kujenga nyumba yangu ndani ya miaka miwili tangu nianze kazi, na pia hata ofisi nilihamishwa kutoka wilaya ya Chemba hadi makao makuu ya mkoa "Manispaa ya Dodoma. Hapa sasa ndipo mambo yakaanza kubadilika.

Mimi si mtu wa kujichanganya sana na watu, nina marafiki wachache sana tangu nihamie hapa makao makuu. Rafiki yangu mkubwa ni Idris na Godfrey. Hawa ndio watu ninaoweza kukaa nao na kuzungumza mambo mbalimbali kuhusiana na kazi zetu na stori nyingine nyingi ingawa kicheo nimewapita, mimi ni Boss wao.
Godfrey, kama nilivyo mimi nae ameoa na ana watoto wawili, mimi bado sijabahatika kupata mtoto. Ila Idris yeye hajaoa ingawa anaishi na mpenzi wake "Roida", ni mwaka wa tatu tangu waanzishe mahusiano.

Siku ya Jumapili ya mwisho wa mwezi nilimualika nyumbani, Idris na mpenzi wake "Roida" ili tupate kujumuika kwa pamoja katika chakula cha mchana na kuzungumza mawili matatu kama marafiki na majirani.

.........."Shem samahani, unaweza kuturuhusu tuondoke na 'mamito' ili akapajue kwetu, maana kila mara unakuja wewe tu alafu misez hata hapajui", ilikuwa ni sauti ya Roida wakati wa kuagana akiniomba nimruhusu Jackline waondoke pamoja nae kuelekea kwao ili akapajue.

........."Usijali shemeji yangu, nyie nendeni tu hamna tatizo. Huwa nasahau kuja nae kwenu kisa mambo mengi kichwani yamenitinga, ni kweli ukisemacho.Ni muhimu akapafahamu munapoishi ili siku likitokea la kutokea iwe rahisi kuwasiliana", nilimjibu Roida huku tukiwa tunafungua lango la geti kuu kutoka nje.

.............."Wanawake bhana, yani hapa Roida ndo kafurahi mwenyewe ulimvyomruhusu aondoke na shemeji", akadakia Idris huku akimpigapiga Roida vikofi vya utani mgongoni.

............."Hahahahaha, ndo hivyo. Sitaki mwanamke mwenzangu ajifungie ndani tu wakati hata kwetu hapajui", alijibu Roida huku wakipanda kwenye gari lao 'TOYOTA Harrier New model'.

Jackline nae aliagana na mumewe na kumuahidi kuwa hatochelewa kurudi, hatimae akaingia garini na Idris akalitoa gari kuliingiza barabarani.


NYUMBANI KWA IDRIS

................"Roida, fanya basi kama nilivyokuelekeza, nahitaji kulala na Jack hata sahizi kama itawezekana", ilikuwa ni sauti ya Idris akimsisitiza Roida. Wawili hao wakiwa chumbani huku Jackline wakimuacha sebleni akiangalia luninga.

........."Usijali Iddy, Jack ushamnasa. Ngoja niende sebuleni nikaweke mambo sawa alafu nitakuja kukushtua", Roida alijibu huku akiinuka na kufungua mlango kuelekea sebuleni alipo Jackline.

*Roida na Idris wana mipango gani ya siri?. Je, hawa sio wapenzi?

USIKOSE SEHEMU IJAYO.


















Sent using Jamii Forums mobile app
Imetulia sana.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom