Riwaya mpya: Mbwa wa geti

Riwaya mpya: Mbwa wa geti

Kudo

JF-Expert Member
Joined
Nov 2, 2017
Posts
1,821
Reaction score
6,122
Baada ya kuimaliza riwaya ya UKURASA WA GAIDI,huku tukielekea mwisho wa riwaya ya SAUTI YA MTUTU,Ni wasaa mwingine kukuletea MBWA WA GETI.

Riwaya hii nitaanza rasimi kuiweka hapa keshokutwa,saa kumi na mbili jioni na saa moja ahsubuhi kila siku.

Karibuni tuwe sote hapa hapa jukwaani.

Asalaam Kudo
 
RIWAYA: MBWA WA GETI
Na Bahati Mwamba
Simu 0758573660

Upande aliokuwa amesimama,tayari ulikuwa umeanza kuifikiwa na maji ,na hakutaka kabisa maji yale yamguse,alijitahidi kila namna kusimama kwenye kingo za njia ile ili kuyakwepa maji yale yaliokuwa yakitiririka kwa kasi na kutoa harufu kali iliokuwa ni adhabu tosha kwenye pua zake,tayari harufu ya maji yale ilikuwa imeanza kumuathiri katika mfumo wa fahamu zake,harufu ile ilikuwa imeanza kumlevya huku kichwa kikiwa kinamuuma na pua zilianza kutoa majimaji mepesi.
Hakutaka kuanguka kwenye yale maji maana aliamini kabisa hayakuwa salama kabisa,na hata alipotaka kuyaingia bado macho yake yalipata kushuhudia kile ambacho hakutaka kabisa kukiona,yalokuwa yanapitisha viungo vya binadamu.
Akili yake ilikwama hasa alipoona kichwa cha mtu kikielea,huku ubongo wake ukiwa upo nje na macho kodo,kuashiria mtu yule kabla hajakatwa kichwa aliona au alipitia mateso makali sana kabla mwili wake haujatenganishwa vipande vipande.
Alitamani kutapika,lakini tumbo halikuwa na kitu,njaa ilimsumbua,kichwa kilimuuma,pua zilianza kuziba na mwili haukuwa na nguvu japo ya kupiga hata hatua moja kutoka pale alipokuwa amesimama.
Akili yake ilifanya kazi kwa shida,lakini nafsi yake haikutaka imwache afe kizembe,nafsi ilimpa nguvu za kuendelea kupigania uhai wake kwenye lile pango.
Akili yake haikuwaza kitu kingine zaidi ya mwanae,hapo nguvu zikaurudia mwili wake,akayatazama maji yale yaliokuwa yanatiririka kwa kasi,akaona hayakuwa maji tu,yalikuwa ni maji yaliochanganyika na damu.
Miguu yake ilianza kufikiwa na maji yale,haraka akaruka juu na kuidaka mizizi iliokuwa imening’inia ndani ya njia ya pango lile na wazo la kuitumia kama ndio njia ya kupita bila kuyagusa maji yale ikamwijia na hakuwa na budi kuendelea kuikamata mizizi ile huku sasa akianza kuelekea kule maji yale yalipokuwa yanaelekea.
Baada ya mwendo mrefu kidogo huku akiwa bado anaitumia mizizi ile kama kamba ya kumvusha mle pangoni ,mikono ilianza kumsaliti ili asitimize adhima yake hiyo,mikono ilianza kuchoka kwa kuwa alikuwa amening’inia muda mrefu na bado hakuona kama kutakuwa na mwisho wa pango lile.
Alitamani kuachia mizizi ile ili akanyage ndani ya maji yale lakin nafsi yake ilimkataza,na hakuwa na la kufanya zaidi ya kuendelea kutembea huku akiwa amejishikiza na mizizi na Kama ungelitokea nyuma yake basi ungehisi ni nyani anaetembea kwa kudaka mzizi mmoja hadi mwingine.
Mikono yake ilianza kutetemeka,na hata mwili ulikuwa umeshachoka kupita maelezo na kichwa bado kilizidi kumuuma na pua bado zilikuwa zinazidi kupokea harufu kali ya maji yale ambayo hayakuwa ya uozo ila ilikuwa ni harufu kama ya acid flani ambayo hakuelewa ilitokana na nini ama ni acid ya namna gani.
Ilikuwa ni lazima ajiokoea lakini viungo vya mwili vilimsaliti,havikutaka tena kumpa ushirikiano,na akaamua kutulia tu pale alipokuwa huku macho yake yakiyatizama maji yale yaliokuwa yanatiririsha viungo vya binadamu kwa wingi sana,vingine aliona ni vya watoto na vingine vya wanawake na vingine vya wanaume.
Watu gani hawa wasio na huruma alijisemea ndani ya nafsi yake.
Mzizi aliokuwa ameshiria alisikia ukitikisika,mwanzo hakutilia shaka lakini mzizi ule ulizidi kutikisika katika namna ya ajabu na hapo akili yake ikamtuma atazame juu.
Kwa tabu sana akapata kuona kule kwenye shina mzizi ule kuna kitu kilijitikisa,kilikuwa ni kiumbe hai kilichokuwa kimeweka hifadhi pale.
“nyoka!!” alijisemea na haraka akataka kushika mzizi uliokuwa mbele yake lakini huko nako akapata kuona viumbe hai wengine,walikuwa ni popo wakubwa mithili ya mwewe wakiwa wameninginia na kwa uzoefu wake alikiri alikuwa hajapata kuwaona popo wa aina ile tangu anazaliwa hadi kufika umri wake aliokuwa nao wakati huo.
Mwili ulijaa hofu ya kushambuliwa na nyoka,lakini pia ya kushambuliwa na popo wale wakubwa,lakini aliona bora popo kuliko sumu ya nyoka.
Haraka mkono wake ukadaka mzizi wa mbele yake na kisha akafanya kudaka ya mwingine na alipotizama nyuma alipata kuona joka lile likijiachia kutoka kwenye kuta ya pango lile na kuanza kufuata ulekeo aliokuwapo,lakini si joka tu hata popo walianza kuruka huku na huko na hapo akafanya jitihada za kusonga mbele,lakini jitihada zake zilikuwa zinakwamishwaa na popo waliokuwa wameanza kuweka wingu jeusi mbele yake,walikuwa popo wengi sana na wakubwa na walikuwa wakitoa milio ya ajabu ajabu.
Alianza kupokea adha ya kupigwa na mbawa za popo wale na kitendo bila kutarajia akaona wale popo wanamshambulia yule nyoka kwa kumdonoa donoa.
Joka lile likashindwa kustahimili maumivu,likajitupa ndani ya maji na hapo ndipo aliona kile kilichokuwa kinamuogopesha kuyakanyaga maji yale.
Lile joka lilianza kuwa kama linaungua na kuanza kukatika vipande vipande,akiwa ameduwaa akashangaa kujikuta akianza kupokea maumivu ya kudonolewa na wale popo huku wakimpiga na mbawa zao,alipitia mateso makali ya kusulubiwa na popo wale na hapo mikono yake ilikuwa ikifanya jitihada za kupokezana kuwapangua popo wale huku kila akipata nafasi alikuwa akihama mzizi mmoja kwenda mwingine,hadi akafanikiwa kutoka eneo lile la wale popo lakini damu ilikuwa ikitoka mwili mzima kutokana na kunyofolewa nyama kwenye baadhi ya sehemu za mwili wake.
Alikuwa akipumua kama mtu alietoka kukimbia mbio za maratoni,na alipotizama chini hakuyaona maji yale wala hakuwa akisikia kelele zake.
Akajiachia kutoka juu ya pango lile na kudondoka chini huku akihema na alikuwa anajaribu kukabiliana na maumivu ya vidonda vyake.
Kwa kuwa alikuwa amechoka sana hakutaka kujua kama alipo ni salama au la akaamua kujipumzisha hapohapo na hapo akili yake ikamrudisha saa chache nyuma kabla hajakutana na adha ile.

Like,coment ili kila ikitoka upate notification

Tukutane jioni
 
Tupo pamoja bro, kazi zako nazipenda sana kwa jinsi ulivyo mjuzi wa kazi za kijajusi.!! Hongera sana@kudo900
 
Riwaya : Mbwa wa Geti
Na Bahati Mwamba


hapohapo na hapo akili yake ikamrudisha saa chache nyuma kabla hajakutana na adha ile.
Ilikuwa hivi
Alishushwa chini kama kiroba,ni baada ya kuwekwa kichwa chini,miguu juu kwa zaidi ya siku mbili,huku macho yake yakiwa yapo gizani kwa sababu ya kufungwa na kitambaa usoni.
Licha ya kushushwa,chini lakini katu hawakumfungua mikono iliokuwa imefungwa nyuma kwa kutumia kamba ngumu.
Akiwa hivyo akasikia sauti za watu zikiongea na punde akanyanyuliwa na kukalizwa chini kama mtoto mdogo,huku macho yake yakiingiwa nuru baada ya kutolewa kitambaa.
Macho yake yalipata kuona watu Kama sita hivi wakiwa wamesimama wima mbele yake na bunduki zao mikononi,hawakuonekana kuwa kama watu wa kimasihara,mikono yao ilijazia nyama,na vifua vyao vilikuwa vimetuna mithilia ya wacheza mieleka nchini marekani.
Aliwatizama tena watu wale mbele yake,lakini macho yake hayakupeleka idadi ile kama ilivyo,bali ikaongeza idadi nyingine ya watu zaidi ya watano wakiwa wamefungwa kwenye viti huku wakionekana dhahiri wakiwa zoofu kwa mateso ama njaa waliokuwa nayo watu wale.
Macho yake yakatamani kuona zaidi pale ndani,akageuza shingo yake kushoto na kisha kulia na hapo akakutana na idadi nyingine ya watu wakiwa wamefungwa kwa kuninginizwa kichwa chini miguu juu,huku wakiwa wanapepea to kwenye kamba zile zilizokuwa zimefungwa juu kwenye dali na pale walipokuwa palionesha kuwa kama ni godauni flani kutokana na ukubwa wa jengo lile.
Akashusha pumzi nyingi na kuzivuta, hapo pua zake zikakutana na harufu ya uozo wa kitu na akili ikamwambia uozo huo upo hapo hapo ndani,akatambaza tena macho yake.
Kutoka pale alipokaa akaona kwa mbele yake kuna mzoga,mzoga wa mtu aliekufa na funza walikuwa wanamtambaa mwilini mwake.
Akatamani kutapika,ila tumbo likamsaliti likaunguruma kwa njaa,na koo lilikuwa limekauka na lilihitaji maji,akameza mate,kisha akawatazama wale watu waliokuwa wamesimama mbele yake,ambao walikuwa na afya nzuri kuliko watu waliokuwa mle kama mateka,watu wale hawakuonekana kujali na ndo kwanza walitoa kicheko,kicheko cha kejeli,kejeli ya wazi kabisa ikautesa moyo wake,akatamani afunguliwe zile kamba na awaoneshe shuguli lakini nafasi hiyo haikutokea kabisa.
*****
Lango la godauni ile likafunguliwa na akiwa sasa amekalishwa kwenye kiti na kufungwa kama wale watu wengine aliowaona,akapata kushuhudia mtu mmoja akiingia na nyuma akiwa amezungukwa na walinzi kama saba hivi.
Mtu yule alimfahamu,alimfahamu kwa sababu alikuwa ni kijana mwenzie na alikuwa ni kijana mwenye pesa chafu mjini Dodoma.
Alimfahamu kwa kuwa alikuwa ni mume mwenzie,alimfahamu kwa kuwa alikuwa amefanikiwa kumpokonya mwanamke wake na alifanikiwa kuisambaratisha familia yake.
Uchungu ulimkaa kooni,akatamani kumvamia na kumsushia makonde,lakini hakuweza alikuwa na njaa na pia alikuwa amefungwa sawia kwenye kiti kwa kamba imara na wagungaji walijua kazi yao.
Alimuona kijana yule akizidi kumkaribia huku usoni akiwa ameweka tababasamu la dhihaka,tabasamu bandia,tabasamu la kidhalimu.
“Zedi Wimba,huna jipya komando wa zamani,huna jipya ndugu yangu ,na jilaumu kwa kiherehere chako,unataka mke mzuri wakati pesa huna,eeh hebu kuwa makini siku nyingine,kuna namba za kurukia ila si hii niliovaa mimi.
Zedi Wimba alimtizama kijana huyu aliekuwa akiongea kwa tambo ,huku akiwa kasimama mbele yake mikono mfukoni,alimtizama bila japo kupata sauti ya kuunguruma mbele yake,uchungu ulikitawala kinywa chake na akabaki kumtizama tu bwana yule mwenye tambo za ajabu.
“Zedi nitakunyanyasa wewe na familia yako,nitakunyanyasa Kama ulivyomnyanyasa baba yangu hadi ukampa umauti,Zedi hustahili kuishi ila kabla sijakuua lazima uyaone mateso ya damu yako,kisha ujue vile inauma…”
Zedi akimtizama tena kijana yule,alikuwa anaongea kwa kujiamini,lakini kicho fanya amtizame tena ni vile kusikia akimlaumu kwa mauji ya baba yake,na hapo swali likamjia kichwani mwake
Ina maana si mapenzi tena,kumbe ni kisasi,sasa mbona amezunguka sana,na baba yake ni yupi
Aliona hawezi kujiuliza wakati wa kumjibu yupo mbele yake,akaamua kumuuliza
Baba yako ni nani,na kwanini usiniue mimi tu ukaamua kuitesa na familia yangu?
Kijana yule akacheka kicheko cha dharau kisha akamwinamia kama anabembeleza mtoto akasema
“Baba yangu ni Ibra Mbaya,yule uliemuua miaka sita nyuma,na ukadhani yameisha ulijidanganya Zedi.
Naitwa Kabah Mbaya,ni mtoto wa pekee wa hayati Ibra Mbaya…”
Baada ya maelezo hayo mafupi Zedi akabaki mdomo wazi,alimjua Ibra,alimjua kwa unyama wake ila hakujua kama Ibra aliacha damu kama yake,damu ya maovu.
Zedi akatulia tuli juu ya kiti na aliona hatari ilio mbele yake kwa kuingia mikononi mwa mtu kama yule.
Hakujua kama yote yanamkuta kwa sababu ya kisasi yeye alijua ni Vita,vita ya mapenzi kumbe ilikuwa ni Vita alioingia bila tahadhari na matokeo yake yupo mikono isio salama.
Sesa!! Hilo jina likamwijia kichwani,akakurupukakama anaetaka kukata kamba lakini akatulizwa kwa ngumi safi iliojaa katikati ya kifua chake na kisha ikamwacha akiugulia maumivu.
Sesa lilikuwa jina la mtoto wake wa kiume,mtoto wa pekee kwake mke wake.
Zedi machozi yalianza kushuka kwenye mashavu yake,hakujua hali ya mwanae,hakujua yupo na nani wakati huo.
Kabah akimtizama kwa dharau kisha akatema mate sakafuni na kwa ishara akaashiria mlinzi wake mmoja ampe bakora aliokuwa ameweka kiunoni,baada ya kupewa akaanza kumchapa Zedi kama mtoto,alimchapa bila kujali anamchapa eneo gani.
Zedi alilia kwa uchungu kwa bakora zile kutoka kwa Kabah,lakini Kabah hakuonesha kujali kitu.
Kabah aliporidhika na kipigo kile,akavua shati na kuwapa vibaraka wake,kisha akaanza kurusha makonde mazito kwenye mwili wa Zedi,Zedi aligeuzwa punching bag na Kabah.
Baada ya dakika kumi za kutoa kipigo kabah alikuwa ameloa jasho mwili mzima huku Zedi akiwa anavuja damu usoni na midomo yake ilikuwa imechanika,alinyanyua uso kumtazama Kabah akaona Kabah anatabasamu,tabasamu la ushindi.
Mwiteni dokta
Kabah aliamrisha huku Zedi akiwa hajui dokta anaeitwa ni wa nini,lakini hakuwa na nguvu za kufanya lolote akaamua kusubiri kitakachojiri,huku macho yake yakiwa bado yanawatazama wale watu waliokuwa wamefungwa kama yeye wakiwa hawajiwezi.

Like,coment twende sawa
 
MBWA WA GETI

SEHEMU YA TATU
na BAHATI MWAMBA

wamefungwa kama yeye wakiwa hawajiwezi.
Zedi alitumia jicho moja lililokuwa na ahueni kutizama.
Kwa mbali alipata kuona mzungu akiwa anasekuma kitorori kidogo kilichokua na kiboksi cha vioo juu yake.
Mzungu yule alisogea hadi katikati ya watu wa Kabah na kisha akakipaki kile kitorori.
Alikuwa hajui ni nini kitafuata na alajua kabisa yanafuata mateso makali sana juu yake,lakini haikuwa hivyo.
Aliona mlinzi mmoja wa Kabah akiwaendea watu wale walikuwa wamefungwa kama yeye kwenye viti na walionekana hawajiwezi kabisa maana hata walishindwa kunyanyua vichwa vyao.
Mlinzi yule alianza kuwapigapiga makofi watu wale waliokuwa wamefungwa kwenye viti,licha ya kuwapigapiga wengi wao walishindwa kunyanyua au kuhisi maumivu ya makofi ya mlinzi yule japo walionesha wangali hai.
Mlinzi yule alimfikia mtu wa mwisho na akampiga kofi kali,jambo liliofanya mtu yule akanyanyue uso wake juu na mkumtazama mlinzi yule katili na akataka kusema kitu ila alishindwa kutokana na uzito wa mdomo wake,midomo yake ilikuwa imechanika na kuvimba,huku nyusi zake zikiwa zimetuna mithili ya nyusi za mabondia waliotwangana,kiujumla uso wake ulikuwa hautamaniki.
Bwana yule aliponyanyua kichwa chake,mlinzi akamwacha na kukifuata kitorori cha mzungu yule aliengia nacho kisha akasogea hadi karibu na mtu Yule na muda huo Zedi alikuwa anamwona dokta mzungu akiwa anavaa mipira ya mikono au gloves kwa lugha iliozoeleka.
“nakuonesha nguvu yangu,na watu kama nyinyi mtanipigia magoti siku chache zijazo” ilikuwa ni sauti ya Kabah na ilikuwa ikitoa ujumbe kumwendea Zedi na Zedi aliuhifadhi kichwani na akangojea kuona kile ambacho kingemkuta mtu yule ambae tayari dokta mzungu alikuwa ameshamfikia.
Dokta mzungu aliingiza mkono kwenye kiboksi cha vioo kilichokuwa juu ya kitorori kisha akatoa kitu kama kipaketi kidogo cha karanga japo chenyewe kilikuwa kimehifadhiwa kwenye kisilinda kama kitumikacho kwenye maabara.
Akakishika vizuri kipaketi kile kisha akakitizama na kisha kwa sauti ambayo Zedi hakuisikia na punde mlinzi mmoja akamfikia dokta yule na mkononi alibeba mfuko wa plastiki na akaukinga chini ya mikono ya dokta yule mwenye asili ya watu wa Amerika na kilichofanyika ndani ya mfuko ule Zedi hakuona japo aliamini ni jambo baya linaandaliwa.
Macho yake yalipata kuona mikono ya dokta yule ikitoka mitupu kwenye mfuko ule na haraka mlinzi yule akamvesha ule mfuko mtu yule aliekuwa amenyanyua kichwa chake juu ilihali akiwa amefungwa kwenye kiti na kilichofuata hapo Zedi alisikia makelele ya kuogofya ngome za masikio yake,na alipata kuona mtu yule akikukuruka kwa nguvu zake zote na haraka walinzi wengine wakakimbia na kwenda kumbana mtu yule huku yule aliekuwa amemvesha mfuko akiwa bado ameushika ule mfuko imara.
Makelele ya mtu yule yalikuwa ya kuogofya sana,ilionesha ni mtu aliekuwa anapitia maumivu makali sana,makelele taratibu yakaanza kupungua huku mtu yule akionekana kutatarika pale kwenye kiti kama mtu alieng’atwa na siafu kalioni.
Walinzi wale walimuachia na wakasimama mbali na mtu yule na yule aliekuwa amemvesha mfuko akautoa mfuko ule huku akifanya jitihada za kuufunga ili kilichomo kisipate kutoka.
Zedi hakustahimili kuona unyama ule mbele ya macho yake,akafumba macho asipate kuona kile alichokiona,na hata aliponyanyua macho yake bado aliendelea kuona kile alichokiona mwanzo,mwili ukamsisimka,uoga ukamjaa,machozi yakamtoka,hata lile jicho lililokuwa halioni sasa akalilazimisha kuona unyama ule uliokuwa umetendeka mbele yake.
Mtu yule alikuwa ameliwa mdomo,yaani midomo yake ilikuwa imeliwa na wadudu na ilibaki amekenua meno tu hata ufizi ulikuwa emetobolewa,ulimi pia ulikuwa nje ukiwa umenyofoka nyofoka,pua ilikuwa imeliwa pia,kitu pekee kilibakia ni macho,wadudu walikuwa wamejazana kwenye ule mdomo wakiingia na kutoka ilikuwa ni mithili ya siafu wakiwa wanakula mzoga,wadudu wale walikuwa wanakula kwa kasi ya ajabu,walikuwa wanakula mtu akiwa hai,walikuwa ni wadudu wadogo mithili ya mchwa ila hawa walikuw ni rangi ya njano wote ilisisimua kutazama hakika Zedi alikiri kuna unyama duniani lakini kama alidhani huo ndo unyama alioona alijidanganya.
Dokta yule akachukua kichupa kidogo mfano wa spray na akataka kuelekeza kule kwenye wadudu wale waliokuwa wanaushamulia ulimi wa mtu yule alioonekana uhai upo nae mbali wakati huo,lakini kabla hajatimiza jukumu lake,Kabah akawahi kumkemea na kisha akaingiza mkono wake tena kwenye kile kiboksi juu ya torori,mkono wa Kabah ukatoka na panya mkubwa aliekuwa anajibaraguza na kutoa mlio mkali wa na haraka akawekwa juu ya uso wa mtu yule na hapo tena Zedi akashindwa kuhimili kuona jambo kama lile.
Yule panya alianza kuwala wale wadudu kwa kasi ya ajabu na ndani ya dakika mbili tu alikuwa amemaliza kuwala na sasa alikuwa anaula ulimi wa yule mtu,lakini kabla hajaumaliza akaanguka chini kama mzoga.
“hii ndo tiba dunia itaihitaji kutoka kwangu na nitautawala ulimwengu hivi karibuni h…” yalikuwa ni maneno ya kabah,maneno yaliokuwa yamejaa kejeli nyingi lakini yalikuwa yaliokuwa yanamuumiza Zedi rohoni na hapo akapanga kufanya jambo lakini hakujua litafanikiwa vipi.
******
Alikuwa amebaki yeye na mateka wengine wakiwa ndani ya godauni ile huku wakiwa wanatazamana na mizoga ya watu kadhaa waliokuwa hawana uhai pale ndani,Zedi alikuwa anawaza kufanya jambo lakini hakuona kama atafanikiwa maana alikuwa amefungwa imara kwenye kiti.
******
Alikuwa amelala katikati ya maji ya baridi huku akiwa uchi wa mnyama.
Machozi yaliokuwa yakimtoka yaliishia kumezwa na maji yaliokuwa yamesambaa juu ya marumaru nyeupe iliokuwa imechangia kulipendezesha jumba lile la kifahari ambalo yeye aliliona kama ni jehanamu kwa jinsi alivyokuwa akiteseka mle ndani.
Alijinyanyua kutoka pale chini na hapo ndipo akagundua maumivu yalivyokuwa yameutawala mwili wake,akakiri na nafsi yake ya kuwa kipigo alichopigwa kilizidi vipigo vyote vya nyuma.
Lakini kuna la zaidi lililompelekea yeye akanyanyuka pale chini,ilikuwa ni kiu,si kiu ya maji,wala kiu ya pombe,hapana alihitaji kupata faraja ya akili na kuuchangamsha mwili,hakuendelea kukumbuka kipigo alichokuwa anapigwa muda mfupi uliopita,yeye alihitaji aipate kwanza furaha yake,ambayo aliamini inaweza kumsahaulisha na mateso yote ya nyumba ile.
Alijitahidi kuzipanda ngazi zilizokuwa zinaelekea vyumba vya juu,kichwa kilimuuma na mwili ulimuuma,lakini ni kama hakusikia maumivu yoyote.
Hakujali kama yupo uchi na alikuwa akimulikwa na taa kadhaa zilizokuwa zinaangaza sebule nzima na hata kwenye ngazi alizokuwapo.
Alijitahidi kupanda na hatimae akaifikia valanda kubwa iliokuwa imepambwa kwa nakshi kadhaa ukutani,hivyo hakujali maana aliviona siku nyingi,safari yake ilimfikisha hadi kwenye chumba kimoja ambacho aliamini anachokitaka kitakuwapo huko,.
Taratibu akausukuma mlango na kwa taabu akaingia ndani na akawakuta wenyeji wapya ambao hawakuwa wazoefu wa nyumba ile kumliko yeye,walikuwa wanawake wenzie wawili wakiwa wamemzunguka mwanaume mmoja.
Mwanaume huyu ndie aliekuwa mpenzi wake,lakini leo kamgeuza msukule ndani ya nyumba yake.
Hakuwajali japo alitamani kusema na wanawake wenzie ambao mmoja alikuwa yupo juu ya kijiti cha mwanume akikinyonga huku na huko huku miguno ya wizi ikiwa imetamalaki na mwanamke mwingine akiwa anachombeza kwa kilio cha tamaa ya kukikalia kijiti kile cha mwanume yule ambae muda mfupi uliopita alikuwa akimsulubu kwa mateke na ngumi mwanamke huyu alieingia dakika chache zilizopita.
Mwanamke yule alizidiwa na tamaa ya kile alichokitaka muda huo,haraka akatazama upande wa meza kubwa iliokuwa imekipamba chumba kile cha thamani .
Akapiga hatua ndefu kama za mama anaeenda kumuokoa mwanae asiungue na moto.
Akaifikia ile meza na kwa haraka akapangua vilivyokuwa juu yake,lakini hakubahatika kuona alichokitafuta,akahamia chini ya meza ile nako akaambulia patupu,akatamani kulia lakini afya haikumruhusu kulia na alitamani awavae wale mahasidi waliokuwa wanakata viuno juu ya bwana ake lakini pia afya haikumruhusu,alikuwa amechoka,mchoko wa ajabu,mchoko ambao mimi na wewe hatujawahi kuupata.
Ni kama mwendawazimu alieona chakula kitamu jalalani,akatabasamu kumbukumbu zilikuwa zimemrudia na sasa alikumbuka huko sebleni kulikuwa na akiba yake na aliiweka chini kwenye kitako cha tv,haraka akakimbia kutoka kwenye kile chumba na hata alipoitwa kwa dharau na bwana ake hakusikia. Yeye mawazo yake yalikuwa kwenye hicho kitu.
Aliziteremka ngazi kwa haraka na punde akafikia ile tv na akainyanyua kwa pupa,hola! Hakupata alichokihitaji,mwili ulimtetemeka kwa uchungu na hasira akajibwaga chini kwenye maji huku akiwa anatetemeka,hakutetemeka kwa sababu ya maji yale,la,alitetemeka kwa kukosa kile alichokihitaji na hata nguvu zikaanza kumwishia na majuto yakakitawala kichwa chake.
Mwaka mmoja nyuma alikuwa na maisha yake,ya furaha na amani,ila tamaa ziliuponza utu wake,na si utu wake tu hata mwanae mdogo wa miaka mitano alikuwa amekosa mwelekeo na kibaya zaidi hakujua kama mume wake yu hai au amekufa ..
“Tausi!!” sauti iliita mbele yake na akanyanyua uso kutazama ,mbele yake alisimama mwanaume wa kimo sawa na mumewe wa ndoa,lakini tofauti yao huyu alikuwa ni mnene wa umbo na mara nyingi alikuwa akitembea na silaha mkononi na ndie alikuwa mlinzi mkuu wa nyumba ile.
Tausi hakujali kama yu uchi mbele ya bwana yule aliesimama mbele yake,bwana ambae hakustahili japo kuona hata upaja wake,lakini leo aliona na Tausi hakuwa na namna.
Bwana yule akaingiza mkono mfukoni na kutoa kipaketi kidogo na kumrushia miguuni Tausi,kisha yeye akapiga hatua na kuondoka.
Tausi alikipaparikia kile kipaketi,alikuwa ni kama mtu alieona kisima katikati ya jangwa.
Alikikamata huku akibwabwaja maneno ya kushukuru kwa kuletewa burudani yake aliokuwa ameikatia tamaa kuipata.
Akakichana,kisha akikipeleka chote puani na kuvuta unga uliokuwamo na hata alipomaliza akakitupa chini huku sasa akili ikimrudia kwa mbali na kutoka kwene maji na kukaa juu ya sofa huku mwili wake ukupokea burudani murua na kuleta msisimko wenye raha ya ajabu,ambayo hajapata kuiona wala kuiwazia kama utakuja kuwapo duniani.

ASALAAM KUDO
 
Sawa sawa mkuu. Vipi hii utaimaliza sio?
Riwaya moja tu ndo sikuimaliza kwa sababu zilizo nje ya uwezo wangu ndugu ila zingine zote nimemaliza na nitamaliza Chief
Ukurasa wa gaidi imeisha,kikosi cha pili imeisha na sauti ya mtutu inaelekea kuisha
Soma kwa amani changamoto pekee ni bando
 
Riwaya moja tu ndo sikuimaliza kwa sababu zilizo nje ya uwezo wangu ndugu ila zingine zote nimemaliza na nitamaliza Chief
Ukurasa wa gaidi imeisha,kikosi cha pili imeisha na sauti ya mtutu inaelekea kuisha
Soma kwa amani changamoto pekee ni bando

Saaawa sawa mkuu! Pia tunakushukuru sana kwa kuamua kutuburudisha bila chenga. AMEN
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom