RIWAYA: Mary Mariam

IAmShedeOne

JF-Expert Member
Jul 2, 2015
202
382
MARY MARIAM (01)
FB_IMG_1516629622688.jpg


BEKA MFAUME

Alizaliwa nje ya ndoa. Baba yake hakuwahi kumwona ingawa aliamini yuko hai. Alisikia tu akiambiwa baba yake ni Mwarabu. Aliamini hivyo kwa sababu hata damu yake ilimdhihirishia ukweli huo. Alikuwa shombe wa Kiarabu aliyezaliwa na mama wa Kibondei mwenyeji wa Muheza mkoani Tanga kwenye Kijiji cha Lusanga. Hakuwahi kuambiwa na mama yake au babu yake aliyemlea, kuwa baba yake ni Mwarabu. Alisikia baba yake alikuwa akiitwa Mahfudh, jina ambalo halikutakiwa asilani kusikika kwenye familia yake! Alipewa jina la Mary kulirithi jina la bibi yake mzaa mama yake aliyekwishafariki miaka mingi ya nyuma. Akapewa ubini wa Goda ambalo ni jina la babu yake, kwa sababu ndiye aliyemlea.
Akaitwa Mary Goda.
Akakiri, kweli alikuwa mtoto wa haramu!

MAMA yake aliitwa Mboza. Alipata ujauzito wakati akifanya kazi za ndani, nyumbani kwa tajiri wa Kiarabu anayeitwa Mahfudh, mmiliki wa duka la rejareja kwenye mji mdogo wa Muheza kilomita chache kutoka mji wa Tanga.
Mahfudh aliishi na mkewe, naye pia ni Mwarabu waliotoka pamoja Yemen, waliofunga ndoa ya kindugu, mtu na binamu. Mkewe alikuwa mkorofi mwenye tabia ya kupayuka wakati wote, aliyesumbuliwa na wivu dhidi ya mumewe kwa hofu asije akatembea na wanawake wa Kiswahili.

Pamoja na sifa hizo za mkewe, bado Mahfudh aliweza kumrubuni Mboza, akafanikiwa kufanya naye mapenzi humohumo ndani ya nyumba bila ya mkewe kujua. Hatimaye Mboza akapata ujauzito!

Ulikuwa mshtuko uliomtingisha Mboza kujigundua ana ujauzito. Kwanza alifanya siri, akaogopa kumwambia Mahfudh. Aliogopa kwa sababu hata tajiri yake, naye alikuwa mkorofi. Alihofu endapo angemwambia kuwa ujauzito ni wake, asingeikubali. Ukimya wake wa kutomwambia, ukamfanya Mahfudh aendelee kufanya naye ngono huku Mboza akiambulia kuhongwa vibaba vya mchele, unga, mafuta ya kupikia, maharage na vijisenti vya hapa na pale kama kitulizo.

Ujauzito hauna siri, tumbo la Mboza likaanza kuumuka, shangazi yake akawa wa kwanza kugundua. Akamwita, akamhoji. Dakika za mwanzo za mahojiano, Mboza alikataa kujibu. Lakini alipobanwa kwa aina tofauti ya vitisho, akakiri kuwa kweli ni mjamzito. Akamtaja Mahfudh kuwa ndiye mhusika wa ujauzito huo! Taarifa zikamwendea babu yake anayeitwa mzee Goda ambaye ni mlezi wake. Naye akamwita ili kupata uhakika wa taarifa hizo. Mboza akaulizwa, akakiri yeye ni mjamzito. Akarudia kwa mara nyingine kumtaja Mahfudh kuwa mhusika na ujauzito huo!

Mzee Goda, akachukua hatua za kuwaarifu wazee wenzake. Wakakubaliana jambo hilo lisiachwe hivyohivyo. Wakachaguliwa baadhi ya wazee waende wakamwone Mahfudh kwa mazungumzo ya kina ili ijulikane hatima ya binti yao.
Ikapangwa siku, wakaenda.

******

ILIKUWA baada ya sala ya Insha inayosaliwa mapema usiku, Mahfudh alipokuwa akitoka msikitini. Wazee watatu waliokwenda kumwona, wakamwona. Wakamwangalia Mahfudh aliyekuwa akitembea peke yake, wakamfuata.
“Sheikh Mahfudh!” mmoja aliita.
Mahfudh akasikia, akageuka nyuma. Akawaona watu watatu wakimfuata. Akasimama na kuwaangalia kwa umakini. Akagundua hamjui hata mmoja.
Wakasalimiana.

“Tumeshindwa kukufuata nyumbani, suala lenyewe ni zito kidogo,” mmoja wao aliyeonekana kuwa kinara, alimwambia Mahfudh.

“Suala gani?” Mahfudh aliuliza kwa sauti iliyokosa nidhamu baada ya kuhisi wamemfuata kwa shida ya pesa.
“Inamhusu binti yetu Mboza!”

“Ana nini?”

“Ni mjamzito!”

Macho ya Mahfudh yakapepesa kwa haraka kuonyesha mshtuko. “Sasa hilo linanihusu nini?” aliuliza kwa sauti iliyoongeza kiburi. Taswira ikasomeka usoni mwake. Alikuwa ameshahisi kinachotaka kuzungumzwa!

“Mzigo ni wako!”

Mahfudh akaduwaa kwa sekunde. Alipoona wazee wale wakimwangalia machoni, akapepesa macho na kutoa kicheko kidogo cha kuigiza lakini kilichofanikiwa kuonyesha dharau.

“Hivi mna akili kweli?” alisema. “Mnakuja kunidhalilisha kwa kuniambia nimempa ujauzito binti yenu? Ndivyo alivyowaambia?”

“Ametuambia, wewe ndiye mwenye mzigo ule!”

“Kwa akili yenu mnadhani mimi ninaweza kutembea na binti yenu? Kwa kitu gani?” Mahfudh alisema huku akionekana kukosa mhimili wa kujizuia kubaki kwenye busara. “Mimi nitembee na mtu mweusi? Hakika mmejua kunidhalilisha. Si mnajua kama yeye ni kijakazi cha pale nyumbani kwangu?”
“Hilo tunalijua,” mwingine alijibu kati ya wale wazee.

“Kwa hiyo mimi nimetembea na kijakazi changu?” Mahfudh aliuliza. “Hakika mmejua kunitusi!”

“Amekutaja wewe!” mzee mwingine aliamua kujibizana na Mahfudh huku akiijenga sura ya mapambano.

“Nendeni mkamuulize vizuri ni nani aliyempa hiyo mimba! Anafikiri kunitaja mimi kumtamsaidia nini? Huku ni kunidhalilisha! Kwanza yeye Mkristo, nitatembeaje na Mkristo wakati mimi ni Mwislamu? Sitopenda habari hizi zikimfikia mke wangu. Akizisikia, zitamhuzunisha. Ni yeye ndiye mwenye kumkarimu kwa kumpa vyakula kila siku, halafu leo asikie uvundo kama huu? Amewadanganyeni! Nendeni mkambane vizuri, atawaambia ni nani aliyempa mimba hiyo. Na nyie watu wazima badala ya kufikiri, mnabebeshwa uongo na kuja kupotezeana muda. Kwa kweli mmenisikitisha!” Baada ya kusema hivyo, Mahfudh akaondoka na kuwaacha wazee hao wamepigwa na butwaa.

Baada ya kupiga hatua kadhaa, Mahfudh akageuka ghafla na kuwaangalia wale wazee. “Na sitaki kumwona tena akija nyumbani kwangu. Nimeshamfuta kazi!” alibwata na kutokomea!

Mzee Goda akapelekewa taarifa kuwa Mahfudh ameikataa mimba, akapewa na nukuu za kejeli alizozitoa. Jazba ikampanda mzee huyo, akavumilia kwa siku mbili akitafakari hatima ya binti yake huku akichemka kwa hasira kila alivyorejewa na kumbukumbu za kejeli zilizotolewa na mwarabu huyo.

Siku ya tatu mzee Goda akamwendea Mahfudh dukani kwake akiwa na bakora mkononi! Akamkuta.
“Wewe ndiye Bwana Mahfudh?” mzee Goda aliuliza kama kwamba alikuwa hamjui Mahfudh.

Mahfudh akasita kujibu haraka. Kwanza alikuwa hamjui mzee huyo. Pili, sura aliyokuwa akikabiliana nayo ilijenga shari. Wakatazamana kwa sekunde chache huku wateja wawili waliokuwepo dukani wakionekana kuvutika na tukio hilo.
“Wewe ni mgeni hapa Muheza?” Mahfudh aliuliza kwa sauti ya kijeuri kumaanisha yeye ni mtu maarufu sana hapo mjini.
“Usiniletee ufedhuli!” mzee Goda aling’aka kwa jazba. “Umesikia? Nakwambia usiniletee ufedhuli! Niambie, wewe ndiye Mahfudh?”

Macho ya Mahfudh yakaiangalia bakora iliyo mkononi mwa mzee Goda, akakiri moyoni kuwa, asipokuwa makini na mzee huyo, bakora hiyo inaweza ikamwingia mwilini.
“Ndiyo!” Mahfudh alikiri na kumwangalia mzee Goda kwa hadhari.

“Mimi ni baba yake Mboza!” mzee Goda alisema huku kidole chake gumba kikipiga kwenye kifua chake na kumtolea macho Mahfudh kama kwamba utambulisho huo uliwakilisha kila kitu.
Na kweli! Utambulisho wake ukaleta uwakilishi uliotakiwa. Mahfudh akanywea ghafla. Akawaangalia wateja waliokuwepo pale dukani. Akawaona wamevutiwa na tukio hilo.

“Nisubiri kidogo nimaliziane na hawa wateja,” Mahfudh alimwambia mzee Goda kwa sauti iliyosihi.

Mzee Goda akatulia. Mahfudh akawahudumia haraka wateja waliokuwepo na kuwamaliza. Lakini hawakuondoka!

“Sasa mnasubiri nini?” Mahfudh aliwageuzia kibao wateja wake. “Nimekwisha wahudumia, ondokeni!”
Wateja wale wakaondoka.

“Kulthum!” Mahfudh aliita kwa sauti ya juu baada ya wateja kuondoka eneo hilo.

Kulthum akaja. Alikuwa ni mkewe, aliyetembea kwa kujikokota kutokana na uzito wa mwili uliomsababisha kuumwa miguu. Wakazungumza kwa lugha ya Kiarabu. Mke wa Mahfudh akamwangalia mzee Goda, mzee Goda akayatuliza macho bila ya kupepesa kumwangalia mwanamke huyo. Mke wa Mahfudh akakwepesha macho, akendelea kuongea na mumewe, kisha Mahfudh akatoka nje na kumwacha mkewe dukani.

“Twende tukazungumze,” Mahfudh alisema kwa sauti iliyopwaya, iliyoondoka kwenye kiburi na kujenga nidhamu.
Watu hao wawili wakaongozana hadi kwenye kibanda kilichokuwa na bucha siku za nyuma iliyomilikiwa na Mahfudh. Wakasimama nyuma ya kibanda hicho kwa ajili ya kivuli, wakawa peke yao.

Mzee Goda akaenda moja kwa moja kwenye hoja yake. “Binti yangu anadai wewe ndiye uliyempa ujauzito. Unasemaje?”
Mahfudh akaruka kimanga. Akaapa kwa viapo vyote hahusiki na ujauzito huo.

“Sikiliza Mahfudh,” mzee Goda alisema huku akinyoosha bakora aliyokuwa akiitetemesha mkononi mwake ambayo ncha yake iligusa kifua cha Mahfudh huku akisema kwa msisitizo. “Sitaki kukulazimisha kuwa mimba ile ni yako kwa sababu sina ushahidi. Lakini, endapo binti yangu atajifungua mtoto mwenye damu ya Kiarabu, nakwambia Mahfudh, utamuoa Mboza unataka, hutaki! Wewe dini yako si inakuruhusu kuoa mke zaidi ya mmoja? Basi utamuoa Mboza! Labda mtoto atakayezaliwa asiwe na damu ya Kiarabu!” Baada ya kauli hiyo, mzee Goda akaondoka kwa hasira bila ya kumuaga Mahfudh.

Jeuri ya Mahfudh ikapotea, akamwangalia mzee Goda alivyokuwa akiondoka. Hakuthubutu kutamka lolote wakati mzee huyo akitokomea kwenye barabara yenye udongo mwekundu! Tishio la mzee huyo likawa limemweka mahali pagumu. Hofu ikamwingia huenda ujauzito unaozungumzwa ukawa ni wake kweli. Hata hivyo, akaliona tatizo jingine mbele yake. Asingeweza kumuoa Mboza, hata kama ujauzito huo ungekuwa ni wake! Yeye mwenyewe binafsi hakuwa tayari kumwoa mwanamke mweusi. Kwanza angeshutumiwa na familia yake, lakini hata ile iliyoko Uarabuni nayo ingemshutumu kwa kuchafua rangi ya jamii yao kwa kuingiza damu isiyotakiwa!

Pili, Mboza alikuwa dini tofauti, Mkristo! Kwao udini uliwatawala kwa kiasi kikubwa. Hiyo ingekuwa dosari nyingine! Tatu, ingekuwa aibu kwake kuzaa na mtumishi wake wa ndani, pamoja na kwamba alijiwa na fikra, hata Nabii Ibrahim alizaa na mtumishi wake, lakini kwake yeye alijiona amekwenda mbali. Yaani mtoto atakayezaliwa mwenye nasaba na mtu mweusi, ahalalishwe kuwa ni wake na jamii ikalijua hilo? Angeuweka wapi uso wake? Nne, Angejieleza vipi kwa mkewe kuwa, ni kweli mimba hiyo mhusika ni yeye! Alikiri udhaifu aliokuwa nao mbele ya Kulthum, kuwa alikuwa hana kauli kwa mkewe! Moja kwa moja akatambua, asingeweza kuukabili ugomvi utakaoanzishwa na mkewe endapo atazisikia habari hizo!

Miezi miwili iliyofuata, Mahfudh akaliuza duka lake kwa Mwarabu mwenzake raia wa Yemen. Akaichukua familia yake na kuikimbia nchi, akarudi kwao Yemen!
Huku nyuma, Mboza akajifungua mtoto wa kike, akapewa jina la Mary. Babu yake akamchukua na kumlea.
Akaitwa Mary Goda!
*****

MZEE Goda alifariki Mary akiwa na umri wa miaka kumi na moja!
Mboza ambaye alimwacha Mary mikononi mwa baba yake baada ya kumzaa, yeye ndiye aliyetaka mwanaye apewe jina la ‘Mary’ ili iwe kumbukumbu ya marehemu mama yake mwenye jina hilo ambaye naye alifariki wakati yeye Mboza akiwa mdogo. Mara baada ya kumwacha Mary mikononi mwa mzee Goda, Mboza alihamia kijiji cha Lusanga kilicho kilomita chache kutoka Muheza kwa kile alichodai, anakwenda kulima. Akaishi huko hadi kifo cha baba yake, mzee Goda kilipotokea.

Kifo hicho kikamlazimisha arudi Muheza kumchukua mwanaye, Mary baada ya kushindikana kulelewa na aliyekuwa mke wa mzee Goda. Mary akapelekwa kijijini Lusanga kuanza maisha mapya akiwa na mama yake. Huko ndiko tofauti ya maisha ilikoanza kwa mtoto huyo.

Maisha ya Muheza alikolelewa na babu yake yalikuwa ya kijukuu, pamoja na kwamba hayakuwa yenye kipato kizuri, lakini yalikuwa ya kawaida. Alikuwa akila milo yote mitatu na alikuwa na furaha wakati wote. Kuletwa kwake Lusanga, kukabadilisha taswira yote ya maisha hayo aliyokuwa akiishi nayo Mji wa Muheza.

Akiwa Lusanga, Mary alipambana na sulubu za maisha zilizoandamwa na umaskini uliokithiri na mfumo wa maisha alioukuta. Mama yake ambaye alishaathirika na tabia ya ulevi uliopindukia wa kunywa pombe za kienyeji hasa pombe ya mnazi, aliishi na bwana ambaye naye alikuwa mwathirika wa ulevi huo uliopitiliza ambaye ndiye angekuwa ni baba yake!
Baba yake huyo aliitwa Mgaya, mwenye kazi ya ugemaji wa pombe ya mnazi iliyokuwa ikimpatia kipato duni. Yeye akawa kichwa cha kuangalia maisha ya familia hiyo ya watu watatu. Biashara ya ugemaji pombe na kisha baadaye kupelekwa kuuzwa kwa wateja, haikuwa yake. Yeye aliajiriwa na mmiliki wa kitalu cha minazi inayogemwa tembo hilo. Pamoja na kugema, lakini pia akawa na kazi ya usambazaji kwenye vilabu tofauti vya kuuzia pombe hiyo kwa kutumia baiskeli. Kipato kilichopatikana kutokana na ajira hiyo hakikutosheleza mahitaji ya nyumbani. Na ili kujiongezea kipato, ikamlazimu kuhifadhi nyumbani baadhi ya pombe na kuiuza kwa wateja wachache ambao ni majirani.

Akiwa amehamia shule ya msingi iliyopo hapo Lusanga baada ya kutoka Muheza ambako alikuwa na uwezo mzuri wa masomo, Mary aliendelea kuwa mmoja wa wanafunzi wanaofanya vyema shuleni, akishika namba za juu, kuanzia moja hadi tatu katika mitihani ya shule aliyokuwa akiifanya. Lakini kadri siku zilivyokuwa zikienda, hali ngumu ya maisha iliyopo nyumbani kwao, ukawa ni mtihani mwingine kwake.

Ulevi uliokithiri wa wazazi wake ukawafanya kukosa umakini wa kukijali kipaji chake. Badala yake, Mary akawa anatumika kama jembe la kufanya kazi zote za hapo nyumbani. Siku zote alizokuwa akitoka shule hakuwahi kukuta amewekewa chakula. Hali hiyo ilimlazimu awe anajipikia mwenyewe ugali endapo atakuta mboga. Na endapo hakutakuwa na mboga, aliishia kupika uji na wakati mwingine aliunywa bila ya sukari.
Siku zote alienda shule bila ya pesa mkononi, kama hiyo haikutosha, pia alikuwa akiondoka bila ya kifungua kinywa. Aliishi kwa kudoea vitafunwa vilivyonunuliwa au kuletwa na wanafunzi wenzake. Baadhi ya siku, wanafunzi wakawa wanamkwepa na kumsimanga kwa kebehi zilizohusisha tabia za ulevi wa wazazi wake. Mary akakosa uthubutu wa kujibu kwa sababu ni ukweli aliokuwa akiuona!

Siku zote alipambana na sulubu ya kuchota maji kwenye bomba lililokuwa umbali wa mita mia moja au zaidi kutoka nyumbani kwao. Sare zake za shule alizotoka nazo Muheza, zikaendelea kuchakaa, zikakosa mbadala. Shati la sare yake hiyo likapoteza mwonekano, likakaribia kufanana na bendeji huku kola yake ikiwa na mwonekano wa chandarua.

Akawa mpishi wa kila siku wa chakula cha usiku. Siku zote ikawa ni ugali na mboga ya majani aina ya mchunga au dagaa kavu la chukuchuku. Pamoja na kutumika kote huko, bado alitakiwa na wazazi wake kusaidia kuwauzia wateja pombe hapo nyumbani. Kitendo hicho kikamfanya agombane na wateja mara kwa mara waliokuwa wakipenda kumtomasa mwili wake. Ingawa alivilalamikia vitendo hivyo kwa wazazi wake, bado alikosa msaada wa kutetewa kutoka kwao.

Wazazi wake wakawa wanavichukulia vitendo vya kutomaswa mwili binti yao, ni kama sehemu ya kukomaa kwake kuelekea utu uzima. Hakuna aliyejali au kutafakari kama binti yao huyo alihitaji muda wa kufanya kazi za shule zilizotakiwa kufanywa nyumbani. Mzunguko huo wa kukosa utulivu wa akili ukaathiri uwezo wake wa masomo darasani. Maendeleo yake ya shule yakaporomoka na kuwa mabaya. Walimu wakataka kujua chanzo cha maendeleo yake kuwa mabaya. Wakagundua ni mazingira mabovu yaliyopo nyumbani kwao ndiyo chanzo cha matokeo mabaya. Nao wakashindwa kumsaidia kwa sababu wazazi wake hawakuwa waelewa pamoja na kuitwa na uongozi wa shule zaidi ya mara moja, lakini hawakuwa msaada. Mary akaachwa kama mshumaa unaoteketea!

Mtihani wa Taifa wa darasa la saba ulipowadia, yeye akiwa ni mmoja wa watahiniwa, shule yao ikafaulisha wanafunzi tisa, jina la Mary Goda likiwa halimo!

*******

MATOKEO hayo yalimwumiza Mary baada ya kwenda kuyasoma. Akarudi nyumbani na kumfuata mama yake huku akilia kwa lengo la kutaka kumfahamisha.
Mama yake akamwangalia kwa mshangao. “Kinachokuliza?” alimuuliza mwanaye.

“Mama nimefeli!” Mary alisema mara moja na kuangusha kilio cha wazi.

“Huko kufeli ndiyo ulie?” mama yake alihoji kwa kejeli. “Hebu niondokee! Kwanza maji yameisha humu ndani, fanya ukachote badala ya kunililia kama mimi ndiye niliyekufelisha!”
Likawa pigo jingine kwake!

Akiwa anayafikiria maisha anayoendelea kuishi nayo hapo, Mary akawa anajiuliza karibu kila siku kama hayo ndiyo yatakuwa aina ya maisha atakayoishi nayo kwa wakati wote wa uhai wake? Akakifikiria kijumba anachokaa. Kibanda, mbavu za mbwa. Chumba chake hakikuwa na dirisha, nuru iliyokuwemo ilipatikana kupitia mwanga wa jua uliofanya miali iliyopenya kwenye matobo yaliyosheheni kwenye kuta za kibanda hicho. Ndani ya chumba chake hakukuwa na kabati wala sanduku. Kamba ya katani iliyokatiza kutoka ukuta hadi ukuta, ndiyo iliyochukua nafasi ya kuhifadhi viguo vyake vilivyoning’inia na kuonekana kama malapulapu yaliyowekwa kwa mafungu.

Akiwa amejilaza kwenye kitanda chake cha kamba kisicho na godoro huku nguo kuukuu zilizotandazwa katikati ya kitanda na kuwa sehemu ya godoro, Mary alikuwa akilia kwa uchungu kutokana na kukosa kuchaguliwa kujiunga na masomo ya elimu ya sekondari. Akiwa katika hali hiyo, huko nje akawa anamsikia mama yake akimzungumzia kwa wateja waliokuja kunywa pombe kuhusu kutochaguliwa kwake kwenda sekondari. Alikuwa akizungumzia kwa furaha kama vile jambo hilo lilikuwa la kawaida. Na wakati mwingine akawa anabeza hata tukio la kulia kwake!

Kauli za aina hiyo zikaendelea na kumpa hitimisho ni namna gani suala lake la elimu lilivyokuwa halipewi kipaumbele na wazazi wake. Hali hiyo ikamrudishia kumbukumbu ya malezi aliyoyapata kutoka kwa babu yake na maisha anayoishi hapo na wazazi wake hao wawili. Yalikuwa maisha ya aina mbili tofauti. Siku zote babu yake alikuwa akimwonyesha upendo kwa kumhimiza kwenda shule. Walikuwa wakikaa pamoja wakizungumza, kucheka na kutaniana. Mambo ambayo kwake yakabaki kama historia isiyosahaulika.

Alimshuhudia mama yake akikosa upendo na yeye. Alimwona akijali ulevi na kumthamini mumewe. Kati yao hakuna aliyekuwa akimjali. Kuanzia kutoendelea kwake shule wala kujali hatima yake itakavyokuwa. Matokeo ya shule yaliyotoka, yakawa yamezimisha matumaini yake yote. Hakuijua hatima yake na kila kitu kilikuwa kiza mbele yake!

Pamoja na kuamini hivyo, lakini kulikuwa na kitu kilichokuwa kikimwambia, hayo siyo maisha unayotakiwa uishi. Hakujua kwa nini alijiwa na hisia hizo mara kwa mara. Pamoja na kuwa na msukumo huo wa matamaini asiyoyaona, ukweli ukawa uko palepale. Mji wa Muheza na kijiji cha Lusanga anachoishi, ndiyo ulimwengu pekee anaoujua!

Kukoma kwa maisha ya kwenda shule, kukamwingiza kwenye maisha mapya. Maisha ya kuamka kila asubuhi, kufanya usafi wa nyumbani na kuandaa mazingira ya wateja kuja kunywa pombe, huku yeye na mama yake wakishirikiana kuuza! Shughuli hiyo ya kuuza pombe, ikamfanya kila siku inayoingia agombane na wateja waliokuwa hawachoki wala kukoma kumtongoza kwa lugha rahisi na za kipuuzi. Wapo walioahidi kumwoa na wengine walidiriki kumrubuni kwa vijipesa vyao huku wakimshawishi ajifunze kunywa pombe, wakiamini kwa kufanya hivyo, ingekuwa njia rahisi kwao kumpata wakati akishalewa. Vitendo hivyo vikamwingiza baba yake kugombana na wateja hao.

Kumwona baba yake akimtetea kukampa nafuu ya kutopata bughudha za mara kwa mara, lakini pia kukamwezesha kuwajibu jeuri wale wote waliojaribu kumtomasa sehemu tofauti za mwili wake. Hata hivyo, laiti Mary angeijua sababu ya baba yake kumlinda, kamwe asingejiona yupo salama ndani ya nyumba hiyo!

***
 
MARY MARIAM (02)

BEKA MFAUME

Kumwona baba yake akimtetea kukampa nafuu ya kutopata bughudha za mara kwa mara, lakini pia kukamwezesha kuwajibu jeuri wale wote waliojaribu kumtomasa sehemu tofauti za mwili wake. Hata hivyo, laiti Mary angeijua sababu ya baba yake kumlinda, kamwe asingejiona yupo salama ndani ya nyumba hiyo!

*******
WIVU ndiyo uliomsumbua baba yake. Wivu uliotokana na umbile la kike lilivyokuwa likichanua kadri umri ulivyokuwa ukienda. Umbile la Mary lilichanua kila kukicha, likajijenga vizuri kifuani, likafanya mzunguko wa matiti yaliyoumuka na kuwa magumu kwa kukosa mgandamizo wa kulaliwa. Chuchu zake zilisimama, zikawa mfano wa ncha za madafu yaliyomenywa. Lakini pia, ubapa wa tumbo lake uliimarisha mwelekeo wa utiririkaji ulioambaa hadi kwenye nyonga zilizojitanua na kujenga mzunguko uliobinua sehemu zake za nyuma. Ukaweka mviringo wenye mvuto wa kimahaba huku mapaja yake yenye kujitanua yakihimiza mvuto wa mapenzi na kufuatiwa na miguu yenye siha iliyojitosheleza. Umbile hilo likahitimishwa na sura ya mvuto yenye mchanganyiko wa damu ya Kibantu na Kiarabu.

Umbile hilo likawa linamtesa na kumshawishi Mgaya aingie kwenye ugomvi na wateja wake karibu kila siku. Mwanzo wa wivu ukaanzia hapo! Matamanio ya kumtamani binti yake yakaongezwa nguvu na tabia za walevi wasiochoka kumtongoza! Kadri siku zilivyoenda, ndivyo alivyozidi kumtamani Mary.

Umbo la Mary likaendelea kujenga ukomavu na kuingiza usugu kwenye akili ya Mgaya. Wakati mwingine hali hiyo ikawa inamfanya baba yake huyo awe anazubaa na kuelea kwenye fikra za kujiona akifanya mapenzi na binti yake huyo. Msongo huo uliojikita kwenye mapenzi ukamwingiza kwenye ndoto za usiku, akawa anaota akifanya mapenzi na Mary!

Uathirikaji wa tamaa ya kufanya ngono dhidi ya binti yake ukaendelea kujenga himaya kwenye kichwa chake. Kikwazo kikawa ni kumshawishi Mary akubali kufanya naye mapenzi kwa siri bila ya mama yake kujua. Hakuhofia kukataliwa. Alichohofu ni Mary kumkataa kisha akaenda kumshtaki kwa mama yake! Alikuwa na uhakika mkewe akilijua hilo, hapo nyumbani patachimbika!

Aliujua vizuri wivu wa mkewe ambaye hugeuka kuwa na akili za kinyama anaposhikwa na hali hiyo. Huweza akafanya lolote baya bila ya kujali athari za baadaye. Pamoja na hadhari aliyojipa, lakini haikupunguza nguvu ya ushawishi wa kufanya mapenzi na binti yake huyo. Hali hiyo ikageuka kuwa gonjwa sugu lililoanza kujitengeneza kwenye mishipa yake ya fahamu. Ikazidishwa na Mary mwenyewe aliyekuwa akivaa khanga moja wakati akienda kuoga.

Alikuwa akiitumia khanga hiyo kama taulo kukausha maji yatakayobaki mwilini mwake baada ya kuoga, lakini si kwa kujifuta. Bali kwa kuivaa. Hali hiyo ikawa inaifanya khanga ishike kwenye mwili wake ikiwa imelowa maji wakati akitoka kuoga. Muda huo wa kwenda kuoga ukawa ni tatizo kwa Mgaya. Kila alivyokuwa akimwona akienda kuoga, Mgaya hata kama angekuwa na shughuli nzito ya kiasi gani anayoifanya, angeisitisha na kwenda kutafuta eneo ambalo lingemwezesha kumwona vizuri Mary wakati akitoka.

Hali hiyo ikaendelea kumtesa, lakini ikimliwaza kwa staili ya aina yake wakati akiwa anamwangalia Mary katika khanga moja iliyolowana maji na kujinasa kwenye mwili wa binti huyo anayetembea huku maeneo ya nyama za makalio yake ikitingishika. Tukio la aina hiyo likawa linauweka moyo wake uende kwa mapigo ya kasi na kuwa kama anayechanganyikiwa. Mfumo unaoratibu ndani ya ubongo wake ukaanza kuathirika na kumwondoa taratibu kwenye ustaarabu.

Athari za kisaikolojia zikajitokeza. Akawa anakariri matukio hayo anayomwona akitoka kuoga. Akayabeba na kuzihifadhi kumbukumbu hizo na kuingia nazo maliwatoni wakati akienda kuoga. Huko huchukua muda kwa kujichua huku kumbukumbu za kumwona Mary akiwa ndani ya khanga moja ikiwa ni kichocheo cha kukamilisha tendo hilo. Angalau kwake ikawa sehemu ya kuridhika kumpata Mary kwa njia mbadala!

Tabia hiyo akaiendeleza kila alipojisikia kukitenda kitendo hicho. Hatimaye akaingiwa na uelewa kuwa, anachokifanya ni sawa na kujidanganya. Baada ya siku kadhaa akaona atafute njia nyingine itakayomwezesha kumpata Mary mwenyewe! Akaanzisha mbinu ya kumpa Mary baadhi ya pesa zinazopatikana kwenye mauzo ya pombe inayouzwa hapo nyumbani.

Haikuwa pesa ya maana, lakini pesa ni pesa. Mara ya kwanza, Mary akazipokea kwa mshangao kwa sababu haijawahi kutokea hata siku moja kupewa pesa na baba yake huyo na kumwambia ni zake. Pamoja na mshangao uliomkuta, katu haikumwingia akilini kuwa baba yake alikuwa na lake jambo!

Pesa alizopewa akaanza kujinunulia nguo chache za mitumba na jozi moja ya viatu. Katika mwendelezo huo, siku moja akapewa kiwango kikubwa cha pesa kuliko ilivyokuwa awali. Tukio hilo likamshtua. Akaanza kujiuliza, inakuwaje baba yake awe anampa pesa za matumizi aliyoambiwa ni yake binafsi wakati siku zote maisha ya hapo nyumbani huwa hayana uhakika wa kula milo mitatu kwa siku? Akashindwa kupata jibu la haraka.

Siku ikafika, swali lake likapata jibu. Chanzo kilianzia baada ya kutokuwepo pombe ya kuuza hapo nyumbani. Kutokuwepo kwa pombe kumpa nafasi mama yake kwenda Muheza. Aliaga na kuahidi angerudi baadaye jioni. Muda mfupi baada ya mama yake kuondoka, baba yake aliyekuwa kwenye chumba kinachotumiwa kuuza pombe, akamwita Mary.

“Ulishawahi kumwambia mama yako kuwa nakupa pesa?” Mgaya alimuuliza Mary baada ya kuingia.

Mary akakataa. “Sijawahi kumwambia!” alisema.
“Ulivyofanya ni vizuri. Usiwe unamwambia, hii ni siri ya mimi na wewe.”

Kwa mara ya kwanza Mary akaigundua nia ya Mgaya kumpa pesa zile! Ugunduzi huo ukampa usumbufu kwa saa kadhaa kwa siku ile. Nia ya baba yake ilimkera na kumuudhi. Akakusudia pindi mama yake atakaporudi, alipeleke shtaka hilo kwake. Palepale akaijenga taswira ya mambo yatakavyokuwa baada ya kuyapeleka mashtaka hayo. Akaliona vurugu litakaloibuka kati ya wazazi wake hao wawili. Aliijua akili ya mama yake, hazimtoshi! Alikwisha shuhudia mara kadhaa mama yake akimtukana Mgaya hadharani, kwa matusi mazito yasiyofaa kutamkwa na mama mwenye binti wa umri wake. Lakini pia alishawaona mara mbili wakipigana hadharani bila aibu, wakiparurana kama wanyama. Hapo ndipo hofu mpya ilipomwingia. Akalifikiria upya kusudio lake. Akakiri kulipeleka shtaka hilo ni sawa na kutaka kijiji kizima kijue alitongozwa na baba yake!
Kusudio hilo akalifuta!

*******

MAMA yake alirudi jioni, akamkuta Mary akiwa peke yake nyumbani. Akalalamika njaa. Mary akampikia chakula. Akala. Mara baada ya kumaliza kula, akaaga kuwa anatoka tena.

“Unakwenda wapi?” Mary alimuuliza.

Namfuata baba yako!”

“Wapi?”

“Kilabuni. Najua atakuwepo huko.”

“Mbona kiza kimeanza kuingia? Si ungemsubiri tu, atarudi.”

“Baba yako nisipomfuata, hatorudi sasa hivi.”

Mama yake akatoka!
Wakapishana na Mgaya! Mama katokea huku, baba kaingilia kule!

“Mama yako amerudi?” Mgaya alimuuliza Mary aliyekuwa akisafisha taa ya kandili. Harufu ya pombe ikasikika kutoka kinywani kwake.

Mary akayakwepesha macho yake yasikutane na ya Mgaya. “Amesharudi, amekufuata hukohuko!” alisema kwa haraka kisha akaondoka eneo la uani alilokuwa akisafishia kandili. Uwepo wao wawili pekee hapo nyumbani ulishaanza kumtia hofu.

“Hukohuko wapi?” Mgaya aliuliza mgongoni kwa Mary aliyekuwa akielekea ukumbini.

“Sijui!” Mary alijibu bila ya kusimama huku sauti yake ikijenga aina ya kiburi iliyochanganyika na woga.

Akiwa ukumbini, Mary akaiwasha kandili na kuipeleka chumbani kwa wazazi wake. Mara baada kuingia chumbani, baba yake aliyekuwa amesimama kwenye mlango wa uani, akachomoka kumuwahi Mary kabla hajatoka.

Akiwa anajiandaa kutaka kutoka chumbani kwa wazazi wake, Mary akasikia mchakato kwa nyuma yake. Akageuka kwa kasi kuangalia huku akiiweka dhana kwa baba yake kuingia humo. Kweli, akamwona baba yake akiwa amesimama huku akimwangalia. Mary machale yakamcheza, akataka kutoka. Mgaya akaufunga mlango!
Kengele ya hatari ikavuma kichwani kwa Mary!

“Usiogope!” Mgaya alisema na kujichekesha kihayawani. “Mama yako hawezi kuja mpaka mimi nimfuate. Kwa hiyo hapa tuko wenyewe tu, mimi na wewe!”

Mary hakujibu, alikuwa amesimama kama aliyegandishwa na uso ulimbadilika. Alinuna!

Mgaya akamsogelea na kujaribu kuutomasa mwili wake. “Mama yako hawezi kujua, itakuwa siri yetu mimi na wewe. Wewe sema chochote unachotaka mimi nitakupa.” alisema.

Mary akaanza kuhangaika kuipangua mikono ya baba yake kila alipojaribu kumtomasa huku akiutafuta upenyo wa kukimbia. Kadri Mary alivyotaka kutoka chumbani, ndivyo Mgaya alivyozidi kumzuia. Hatimaye, Mary akaamua kupiga kelele kuomba msaada. Mgaya bila ya kufikiri mara mbili akaachia kofi lililompata Mary shavuni, akatoa kilio cha maumivu!

Kofi alilopigwa likamchanganya. Akapiga kelele nyingine! Kabla kelele zake hazijaongezeka, mkono wa Mgaya ukamkamata shingoni. Ukamkaba kwa nguvu zote. Mary akapigania maisha yake kujaribu kujitoa kwenye mikono hiyo. Jitihada zake zikaishia kuhangaika kwa kupapasa kwenye mkono uliomkaba shingoni ambao haukuonyesha dalili yoyote ya kuachia. Mary akaanza kukosa pumzi. Akajiona anaishiwa nguvu kwa kasi. Ghafla mkono uliomkaba ukamwachia.

Badala ya kuendelea kupigana, Mary akainama huku akijishika shingoni akitafuta pumzi iliyokuwa imeanza kupotea. Mkono wa Mgaya ukaja kumshika tena, safari hii kwenye kwapa. Mkono mwingine ukajikita kwenye kwapa jingine, kisha ikaanza kumvuta. Mary akaanza tena harakati za kujitoa, lakini kadri alivyokuwa akihangaika kujitoa, ndivyo Mgaya alivyomudu kumvuta zaidi kuelekea kitandani!
“Ukipiga kelele nakuua!” Mgaya alionya.

Pamoja na kutishiwa maisha yake, Mary hakukubali. Akaendelea kupiga kelele. Akanyamazishwa kwa kupigwa na kitu nyuma ya kisogo chake. Hakujua nini kilichompiga, lakini nguvu ya kitu kilichompiga ikampunguzia uwezo wa kuendelea kupigana. Mgaya akamvuta hadi kitandani. Akataka kumpandisha, Mary akarudisha uhai. Akaanza upya kupambana. Mgaya akainama ghafla, akaizungusha mikono yake mapajani kwa Mary. Na kwa kitendo cha haraka, akaibana miguu ya Mary na kumwinua, akamuweka begani na kumtupa kitandani.

Mary hakutulia pale kitandani baada ya kuangukia. Akajigeuza kwa wepesi na kujiweka chali kama paka anayeshambuliwa. Akamwona Mgaya akiufungua mkanda wa suruali yake kujiandaa kumwingilia. Hata hivyo, Mgaya baada ya kumwona Mary amejigeuza, akasitisha kuendelea kufungua mkanda. Akamvamia Mary kwa juu. Bila ya kutarajia akakutana na teke lililomwingia katikati ya kifua!
Mgaya akaugulia maumivu. Teke alilopigwa na Mary lilimuumiza, likamtia hasira. Kilichoendelea hapo ni mfano wa paka wanaopigana. Mary akawa anapigana na kunguruma kama chui huku akiitupa hewani miguu yake kumzuia Mgaya asimlalie juu. Akaanza kupiga kelele kuwa anabakwa! Mgaya akaingiwa hofu. Kelele za Mary zilimtisha kuwa zingeweza kufika mbali na kusikiwa na majirani. Akamzaba Mary makofi mawili ya usoni!

“Kelele!” Mgaya alifoka.

Mary akahisi uso wake ukiwaka moto wa makofi yale mawili aliyopigwa. Nguvu ya makofi iliyotumika na lile karipio alilopewa la kutakiwa anyamaze, vikampumbaza. Juhudi za kujitetea zikapotea, nguvu zikamwishia, miguu ikanyong’onyea. Akashindwa kuitupa hewani kama awali. Akazubaa kama aliyekuwa hajajua alipigwa na nini!

Mgaya akaivua kwa nguvu nguo ya ndani ya Mary kisha akamwingilia kwa nguvu kiasi cha Mary kupiga tena kelele. Mkono wake ukaenda kutua kwenye kinywa cha Mary na kukiziba. Mgaya akaendelea kutumia nguvu zake kujiridhisha kimwili huku harufu ya jasho lake na lile la pombe ya mnazi aliyokunywa vikitawala kutoa harufu kali humo chumbani!
*****

MARY alilia kimyakimya akiwa amejikunja kitandani huku magoti yakiwa yamegusana na kifua chake. Alikuwa amerudi chumbani kwake baada ya baba yake kumfukuza kutoka mle chumbani huku akitoa onyo kwa Mary kuwa, asithubutu kulieleza tukio hilo kwa mama yake, vinginevyo angemuua!

Akiwa anajisikia baridi kwa woga uliokuwa bado umemtawala, Mary akamsikia baba yake akitoka. Hali ya kuchanganyikiwa ikazidi kumtawala. Alijiona hana pa kwenda kushtaki tukio hilo alilotendwa. Mtu pekee angeweza kumshtakia ni mama yake, lakini hakuwa na imani naye. Alijua asingeweza kuchukua hatua ya maana zaidi ya kuishia kugombana na Mgaya, kisha baadaye wangeelewana na pengine madai yake yangechukuliwa ni ya uongo. Lakini pia, kama angeichukua hatua hiyo ya kumshtakia mama yake, mama yake asingelichukulia kistaarabu tukio hilo. Angebwatuzana na Mgaya hadharani na kijiji chote kingejua amebakwa!

Taarifa za tukio hilo zingesambaa hadi Muheza na jina lake lingetajwa kila kona, popote pale angepita angenyooshewa kidole na kuonekana kichekesho. Alimchukulia mama yake kuwa si mtu wa kukabidhiwa uzito wa kesi kama hiyo kutokana na kuathirika kwake kiulevi kiasi cha kumfanya awe na akili za kipumbavu muda wote. Lakini la pili, Mary aliiona athari endapo angelikalia kimya jambo hilo. Ukimya wake ungemwezesha Mgaya afikirie ameogopa kuuawa kama alivyomwonya. Akaamini, hali hiyo ingetoa mwanya mwingine kuendelea kumbaka!

Akiwa bado amejikunyata kitandani na kiza cha usiku kimeshatawala, ghafla aliwasikia wazazi wake wakiingia. Akashtuka! Akajiinua na kukaa. Woga ulikuwa haujamwondoka. Akawasikiliza kwa makini, wote walikuwa wakizungumza kwa sauti za kilevi

“Mary!” mama yake aliita kutoka ukumbini.
Mary akaitikia kwa sauti iliyonyongea.

Mama yake akaingia moja kwa moja hadi chumbani na kumkuta Mary amejikunyata kitandani.

“Wewe unaumwa?” mama yake alimuuliza.

Kabla hajajibu, Mary akamwona Mgaya amesimama mlangoni akiwaangalia. Akatikisa kichwa kukataa kuwa haumwi. Ghafla akasina kuonyesha alikuwa akilia.

“Hili toto jinga!” mama yake alibwata. “Sasa unalia nini? Si nimekuuliza kama unaumwa na umekataa?”

“Analia nini?” Mgaya aliuliza kutoka mlangoni.

“Twen’zetu!” mama yake alimwambia Mgaya huku akitoka na kumsukuma kidogo ili apite mlangoni. “Achana na mpumbavu!”

“Siyo vizuri kumsema hivyo!” Mgaya alisema huku akijiondoa mlangoni.

“Hili toto limezidi ujinga! Babu yake alimdekeza sana alipokuwa akimlea. Ujinga wake hukohuko alikokuwa na babu yake, siyo hapa!”

Wakamwacha Mary akiugulia.
Usingizi ukapaa! Kumbukumbu ya kubakwa ikaendelea kufanya mzunguko kichwani kwake na kumtesa. Kuna wakati, japo mama yake alitoka kumkebehi, lakini alijikuta akiingiwa na ushawishi wa kumwita ili amweleze yaliyomfika. Hata hivyo, dharau aliyoonyeshwa na mama yake iliendelea kumuumiza na kukiri kuwa, huyo asingekuwa mtetezi wake!

Usiku kwake ukawa mrefu, akaendelea kukosa usingizi huku akikosa kuijua hatima yake itakapofika asubuhi. Akawa anapitisha na kupangua maamuzi aliyodhani angestahili kuyafanya. Uamuzi wake wa kwanza alifikiria kujiua, kisha akawaza kutoroka. Wazo la kutoroka akaliafiki, kikwazo kikawa ni wapi angeenda? Hakuwa na sehemu nyingine anayoijua zaidi ya hapo Lusanga na mjini Muheza! Lakini pia, asingeweza kukimbilia Muheza. Babu yake mzee Goda na kipenzi chake alishafariki, lakini pia, asingeweza kukimbilia kwa bibi yake aliyemlea kwa sababu bibi yake huyo alikuwa haelewani na mama yake kwa kutuhumiana uchawi na ndiyo sababu iliyotumika asiendelee kuishi mjini Muheza baada ya babu kufariki.

Akaufikiria tena uamuzi wa kujiua baada ya kugundua hana pa kukimbilia. Uamuzi huo ungekuwa ni wa manufaa zaidi kuliko angeendelea kuishi chini ya ulezi wa baba atakayeendelea kumbaka! Akiwa kwenye hisia za kujiona dunia inamzonga, ghafla akahisi kama aliyesikia sauti ya mwanamke anayelia. Akatulia na kujenga usikivu na umakini. Akaisikia tena sauti hiyo! Safari hii kwa uhakika zaidi. Akaitambua! Ilikuwa sauti ya mama yake iliyokuwa ikilia kwa namna isiyo ya msiba au janga lolote. Bali ilikuwa ikiomboleza katika mawimbi ya kimahaba.

Yesu wangu! Mary alijikuta akipata ganzi mwilini baada ya kugundua kinachofanyika. Akaganda kama aliyegandishwa! Akatambua wanachokifanya wazazi wake! Sauti ya mama yake ikawa wazi masikioni mwake! Taswira ya kumwona Mgaya akiwa kwenye tendo hilo ikamjia, lakini si kwa kumwona akiwa kwenye mwili wa mama yake, bali ni alivyokuwa akimbaka yeye!
Mary akasaga meno kwa hasira!
Asubuhi kabla hakujakucha vizuri, Mary akatoroka kwao!

*******

AKIWA amesimama kituoni kwenye barabara kuu inayoelekea Korogwe asubuhi na mapema, begani akiwa na begi alilokuwa akilitumia shule ambalo lilibeba nguo zake chache, Mary alilipungia basi lililokuwa likija, likasimama. Akapanda.

Aliupitisha uamuzi wa kutoroka baada ya kukumbuka ana ndugu yake anayeishi Mji wa Korogwe. Hakuujua unasaba wao wa kindugu kwa undani, lakini alijua ni ndugu yake. Alishawahi kumwona mara kadhaa wakati akiishi Muheza, akija akitokea Korogwe na kufikia nyumbani kwa babu yake. Alikuwa ni mwanamke na walimwita ‘anti Stella.’

Akiwa ndani ya basi akielekea Korogwe, Mary alimudu kulipa nauli kwa kutumia pesa alizokuwa akipewa na Mgaya. Akionekana kuwa mtulivu ndani ya basi alilopanda, akiwa amekaa kwenye kiti kinachokalisha idadi ya abiria watatu yeye akiwa katikati, hiyo ilikuwa ni safari yake ya kwanza kusafiri kwa basi kwa safari ndefu itakayomchukua takribani saa moja. Mara yake ya kwanza kupanda basi na kusafiri ilikuwa siku alipochukuliwa na mama yake kuhamishiwa Lusanga. Siku hiyo alipanda basi kutoka Muheza na kuteremkia Lusanga, safari ambayo ilimchukua chini ya dakika kumi kuhitimisha safari hiyo.

ITAENDELEA...
 
MARY MARIAM (03)
BEKA MFAUME
Akiwa ndani ya basi akielekea Korogwe, Mary alimudu kulipa nauli kwa kutumia pesa alizokuwa akipewa na Mgaya. Akionekana kuwa mtulivu ndani ya basi alilopanda, akiwa amekaa kwenye kiti kinachokalisha idadi ya abiria watatu yeye akiwa katikati, hiyo ilikuwa ni safari yake ya kwanza kusafiri kwa basi kwa safari ndefu itakayomchukua takribani saa moja. Mara yake ya kwanza kupanda basi na kusafiri ilikuwa siku alipochukuliwa na mama yake kuhamishiwa Lusanga. Siku hiyo alipanda basi kutoka Muheza na kuteremkia Lusanga, safari ambayo ilimchukua chini ya dakika kumi kuhitimisha safari hiyo.
Akiwa ndani ya basi amekosa utulivu kichwani, muda mwingi aliutumia kuangalia nje kupitia dirisha la ubavuni kwake lililokuwa jirani na abiria mwenzake. Alikuwa akishangaa mandhari ya milima aliyokuwa akiiona kama inayotembea kutokana na basi lilivyokuwa likienda na vijiji alivyokuwa akivipita. Mandhari hiyo ilikuwa kama maajabu kwake, akawa kama anayeonyeshwa rasmi umbile la dunia lilivyo.
Pamoja na kuwepo kwenye hali ya kuishangaa dunia anayoishuhudia, hofu yake ilijikita zaidi kule anakokwenda. Mji aliokuwa akienda alikuwa hajawahi kufika. Wasiwasi wa kutokuwa na uhakika wa kumpata ndugu yake anayemfuata ukazidi kumpa shinikizo. Vikwazo vyenye mashaka navyo vilizidi kumzunguka. Kwanza alikuwa hajui anakoishi ndugu yake anayemfuata huko Korogwe. Pili, alikuwa akijua kuwa anafanya kazi baa, lakini hakuijua baa yenyewe ilipo na wala jina la baa! Tatizo jingine lililomwongezea hofu ni kutoujua mji wa Korogwe. Alishawahi kusikia tu, mji wa Korogwe ni mkubwa kuliko Muheza. Ni mji wenye watu wengi, majengo mazuri na starehe nyingi. Pamoja na vikwazo hivyo, bado aliamini Mungu angeonyesha uwezo wa kufanikisha kumpata mwenyeji wake.
Ishara ya kuwa anaingia mji wa Korogwe ilianza kujitokeza kupitia kwenye mabango ya kibiashara yaliyokuwa barabarani na kwenye majengo yakitangaza biashara huku jina la Korogwe likihusishwa karibu kwenye kila bango la matangazo. Macho yake yakiwa yametulia kuangalia nje wakati wote, Mary alishuhudia kuona mtitiriko wa majengo ya kupendeza kuliko ilivyokuwa Muheza. Hofu ya kuwa yupo kwenye mji mkubwa ikawa dhahiri usoni kwake!
Basi alilopanda likafika stendi, abiria wanaoshukia kituo hicho wakaanza kuteremka.
“Abiria wa Korogwe, hapa ndiyo mwisho wa safari yenu!” kondakta wa basi alisema.
Akionekana kama anayebabaika huku akiwa bado ameikalia siti, Mary aliinua kichwa akawa anachungulia nje na kisha ndani ya basi kama vile aliyepotewa na mtu aliyetarajia kumwona.
“We’ unashukia wapi?” abiria aliyekaa naye alimuuliza.
“Nashukia Korogwe,” Mary alijibu.
“Hapa ndiyo Korogwe!”
Kauli ya abiria mwenzake ikamzindua. Mary akajitoa kwenye kiti na kupiga hatua za haraka kuwahi kutoka wakati basi likipiga resi za kutaka kuondoka.
Mara baada ya kuteremka, Mary alijiona amesimama eneo la stendi akiwa amezungukwa na nyumba zilizosheheni biashara tofauti. Watu wenye silka tofauti wakienda na kurudi, wengine wakipiga kelele za kubishania mambo tofauti kama ya mpira na siasa, na baadhi wakiitia abiria waende kwenye mabasi yao. Alikuwa yupo kwenye dunia mpya! Akaamini, kwa wingi kama huo wa watu, angeweza kumwona ndugu yake anayemtafuta.
Baada ya dakika kadhaa ya mwelemeo wa kushangaa, hali ya kukata tamaa ya kutomwona ndugu yake eneo hilo ikawa inamnyemelea. Suluhisho mbadala likamjia. Ushawishi wa kuingia barabarani na kumuulizia kwa watu ukamwingia! Lakini kabla ya kulitekeleza wazo hilo, njaa nayo ikawa ni tatizo kwa upande wake. Asingeweza kuzunguka barabarani akiwa hajanywa chai. Akayaangalia magenge ya mamantilie yaliyopo eneo hilo. Akalifuata moja.
“Nikuletee nini?” mamantilie alimuuliza Mary aliyekuwa amekaa kwenye benchi.
“Chai na chapati bei gani?” Mary aliuliza badala ya kuagiza huku akionyesha dalili zote kuwa anatoka kijijini.
Mamantilie akataja bei, kisha akamwangalia vizuri Mary wakati akisubiri kuagizwa. Wakati akimwangalia Mary, akashangazwa na uzuri anaouona kwa binti huyo. Akashangaa kumwona akitaka kula hapo gengeni tena kwa kuanza na kuuliza bei ya vyakula.
“Naomba uniletee chai na chapati mbili,” Mary aliagiza.
Mamantilie akamhudumia Mary, baadaye akarudi kwenye eneo lake la kusubiri wateja na kuendelea kumwangalia msichana huyo. Ujio wa Mary hapo gengeni, ulimfanya asiamini kama binti huyo alikosa mtu wa kumhudumia. Alimwona ni msichana mwenye vigezo vya uzuri wa kustahili mwanamume kumuweka nyumbani. Akashangazwa na mwonekano anaomwona nao. Mwonekano wa kukosa matunzo mazuri.
Akiwa katika kuusanifu vizuri uzuri wa msichana huyo, mamantilie akawa kama anayeitafuta dosari iliyomfanya binti huyo akose mwanamume wa kumtunza. Mchanganyiko wa damu mbili tofauti aliouona katika mwonekano wa Mary, ulimdhihirishia kuwa, msichana huyo alizaliwa kwa mbegu za jamii mbili tofauti. Alikiri binti binti huyo alijaaliwa umbo la kike lenye mvuto, mwenye nywele nzuri na ndefu, lakini zilizokosa huduma sahihi ya saluni. Kwa uzuri huo, akashindwa kukijua kilichomsibu msichana huyo kuogopa hadi kutaka kwanza kuijua bei ya chai na chapati mbili kabla hajaagiza, ilhali magenge ya mamantilie ndiyo yenye bei ya chini kuliko sehemu nyingine zinazouzwa chakula! Hakuamini msichana mzuri kama huyo angekosa hela hata ya kujiamini kula gengeni!
Wakati Mary akiendelea na kifungua kinywa chake, alionekana kukosa utulivu. Kila mara aligeuka kuwaangalia watu waliokuwa wakipita pande tofauti zinazolizunguka genge hilo. Kitendo hicho kikamshangaza yule mamantilie. Hatimaye akashindwa kuvumilia!
“Wewe ni mgeni hapa Korogwe?” mamantilie alimuuliza Mary.
“Ndiyo,” Mary alijibu.
“Unatokea wapi?”
“Lusanga.”
“Unaelekea wapi? Au ndiyo umekuja?”
“Nimekuja kwa ndugu yangu,” Mary alijibu.
“Ahaa,” mamantilie alisema na wakati huohuo akamwona mteja wake mwingine akiwa amesimama kutaka kulipa baada ya kumaliza kula. Akaachana na Mary, akaenda kupokea pesa kwa mteja wake, kisha akaviondoa vyombo vilivyotumika na mteja huyo na kuviweka kwenye sufuria. Akarudi alipokaa awali.
“Lakini bado sijamwona,” Mary alimwongelesha mamantilie baada ya kumwona amerudi.
Mamantilie aliyekuwa ameinama akihesabu pesa alizokuwa akiziandaa kuzifunga kwenye fundo la ncha ya kitenge alichokifungua kiunoni mwake, aliuinua uso wake na kumwangalia Mary.
“Unaongea na mimi?” alimuuliza Mary huku akizifunga pesa kwenye fundo na kisha akamalizia kwa kujifunga kitenge kiunoni.
“Nasema, ndugu yangu mwenyewe bado sijamwona!” Mary aliirudia kauli yake kwa unyonge.
“Nyumbani kwake umemkosa?” mamantilie aliuliza.
“Kwake sikujui!”
Yule mamantilie kwanza alizubaa huku akimwangalia Mary kama vile hakuamini alichosikia. “Eti nini?” hatimaye aliuliza..
“Kwake sipajui!” Mary alirudia tena kauli yake na alizungumza kama vile alichokizungumza hakikuwa cha ajabu.
Akiwa bado hajajiondoa kwenye mshangao uliomkumba, mamantilie alimwangalia Mary kama asiyeamini anayoyakisikia yanatoka kinywani kwa msichana huyo.
“Anafanya kazi wapi?” aliuliza.
“Baa.”
“Baa ipi?”
“Sijui jina lake.”
Mungu wangu! Safari hii mamantilie alijikuta akishindwa kujibu haraka. Akajiuliza kama msichana anayezungumza naye ana matatizo ya akili?
“Hata kama huijui jina lake,” mamantilie alisema tena. “Baa yenyewe iko maeneo gani?”
“Wala sijui!” Mary alijibu kirahisi.
“Mh!” mamantilie aliguna. Akatamani mteja wake huyo amalize chai na aondoke.
Baada ya kimya, mamantilie alijikuta akishindwa kuendelea kuwa kimya. “Sasa utampataje?” alimuuliza Mary huku akimwangalia.
“Nitamtafuta.”
“Anaitwaje? Au jina lake nalo hulijui?”
“Anti Stella.”
“Stella nani?”
“Ubini wake nimeusahau, lakini ni ndugu yangu! Watu wengine wanamwita mama Saimon.”
“Wewe ni mwenyeji hapa Korogwe?” sauti ya mamantilie ilibadilika wakati akiuliza hivyo.
Mary akatikisa kichwa kukataa “Nimekuja leo!” alijibu.
Mamamantilie akapigwa na butwaa. Kisha akasema, “Ninachokwambia mdogo wangu,” safari hii ukavu wa sauti yake ukawa wazi. “Huyo ndugu yako huwezi ukampata kama hukujui kwake au jina la hiyo baa anayofanya kazi. Panda basi urudi Lusanga! Ukisema umtafute kwa kumuulizia barabarani, utaangukia kwenye mikono ya mateja wanaovuta unga, bangi na vibaka, kisha watakufanya vibaya. Panda basi, rudi kwenu!”
Woga ukamvaa Mary, akaduwaa kumwangalia mamantilie bila ya kusema lolote.
Mamantilie akataka kumuuliza Mary kama nauli ya kurudi Lusanga anayo, lakini akaona swali hilo lingemwingiza kuubeba mzigo wa hasara wa kumlipia nauli mtu asiyemhusu. Badala ya kumuuliza swali hilo, akaamua kudai hela ya chakula alichomhudumia Mary!
Mary akalipa.
“Nenda kapande basi urudi kwenu Lusanga!” mamantilie alimsisitiza Mary huku akizifunga kwenye kitenge pesa alizopewa.
Mary aliishiwa nguvu, akasimama. Akaonyesha kutojua aelekee wapi baada ya kuondoka hapo. Mamantilie kwa kuhofia asije akaombwa msaada wowote na huyo binti, akaamua kuzuga kuendelea na shughuli nyingine wakati Mary anaondoka.
Mary aliondoka kwa mwendo wa taratibu, mamantilie akamwangalia. Uzuri wa msichana huyo aliamini ungekuwa kishawishi kikubwa kwa wahuni kumbaka. Huruma ikamwingia tena, akataka amwite ili amuulize kama anayo 20
nauli ya kurudi Lusanga. Akasita kumwita baada ya kukumbuka biashara yake asubuhi hiyo ilikuwa bado haijachanganya. Akabaki anamwangalia huku akimsikitikia.
Mary alirudi eneo la kusubiri usafiri. Alibakiwa na akiba ndogo ya hela ambayo ingetosha kuwa nauli ya kumrudisha Lusanga au kumpa mlo mmoja tu, kisha angebakiwa na pesa ambayo isingeweza kununua chochote au kumpeleka popote.
Akatambua anawajibika afanye uamuzi wowote badala ya kuendelea kusimama hapo stendi. Pamoja na kwamba hakujua ni uamuzi upi alitakiwa kuutoa, lakini kamwe hakuwa tayari kurudi tena Lusanga!
Nitakwenda wapi? alijiuliza. Akawaza kurudi Muheza. Akamkumbuka bibi yake aliyekuwa mke wa babu yake. Aliamini huyo pekee ndiye angeweza kulitatua tatizo lake la kumpata anti Stella. Ni yeye ndiye angempa anwani kamili ya anakoishi na anakofanya kazi, lakini pia angeambiwa hata na ubini wake!
Kile kitisho alichopewa na mamantilie kuwa mji huo una wahuni kiliendelea kumchanganya na kujikuta akiharakisha kuupitisha uamuzi wa kwenda Muheza. Woga huo ulimfanya ajione anachelewa kuondoka hapo stendi kutokana na kutokuwepo kwa basi linalokwenda Tanga kupitia Muheza. Kuchelewa kufika kwa mabasi hayo yanayoelekea Tanga kukamwongezea taharuki.
Ingawa tishio alilohadharishwa nalo kuhusu wahuni wenye kutumia dawa za kulevya na vibaka lilimtisha, lakini hakuwa mgeni na makundi ya aina hiyo. Hata Muheza na Lusanga walikuwepo. Tofauti aliyokuwa akiiona ni kuwa, wahuni wa Muheza na Lusanga alikuwa akiwajua kwa sura na wengine kwa majina na alijua namna ya kujiepusha nao. Lakini wahuni alioambiwa hapa alikuwa hawajui, hali hiyo ikampa hadhari kwa kila kijana aliyemwona akikatiza mbele yake kutomwamini. Akawa makini kutosimama karibu na vijana wa kiume ambao hawakukaa kisafari.
Akiwa katika hadhari hiyo, ghafla akatokea kijana wa kiume aliyekuwa akimjia kwa mbele. Moyo wake ukashtuka baada ya kugundua alikuwa akimfuata yeye. Woga ukamwingia. Akamwangalia kwa macho yaliyotaharuki kijana huyo huku akili yake ikikataa kutoa uamuzi wa nini cha kufanya. Akamwona yule kijana akitabasamu huku akizidi kumkaribia. Mary akaingiwa na hisia sura anayoiangalia siyo ngeni kwake, lakini hakukumbuka ni wapi alipowahi kumwona. Hata hivyo, hisia hizo hazikumfanya amchangamkie kijana huyo. Akabaki anamwangalia kwa macho yenye wasiwasi bila kurudisha tabasamu alilokuwa akipewa.
“Mary!” yule kijana alisema na kisha kusimama mbele yake.
Mary hakujibu, akili yake ilikuwa kama iliyopigwa ganzi! Uso wa yule kijana ukanywea baada ya kutojibiwa.
“Wewe siyo Mary Goda?” yule kijana aliuliza.
“Ndiye,” Mary alijibu lakini uchangamfu ukiwa mbali. Woga wa kukutana na wahuni ulikuwa bado ukicheza kwenye akili yake pamoja na kwamba alikuwa na uhakika sura ya huyo kijana alishawahi kuiona mahali.
“Hunikumbuki?”
Swali hilo likamfanya Mary amwangalie kijana huyo kwa makini kujitahidi kutaka kumtambua.
“Naitwa Nassoro!” kijana alisema na kutabasamu tena.
Mary akawa anamwangalia na kukwepesha macho.
“Bado hujanikumbuka?” kijana alisisitiza kutambuliwa. “Ah, Mary,” alisema kwa kuhamanika. “Tumesoma shule moja ya msingi Lusanga! Wakati mimi nikimaliza darasa la saba, wewe ulikuwa la tano. Hunikumbuki?”
Uso wa Mary ukakunjuka, tabasamu likajiunda na macho yake kung’ara. “Unajua nilikuwa najiuliza, hivi nilikuona wapi?” alisema.
Sura zilizojaa tabasamu za vijana hao wawili zikashamiri ucheshi walipokuwa wakikumbushana stori za shule. Wakati wakiwa kwenye mazungumzo, Mary bila ya kutarajia akaangalia upande lilipo genge la mamantilie alilolitumia kunywa chai. Akamwona yule mamantilie aliyemhudumia akiwa amezubaa kumwangalia. Mary akampungia mkono, kitendo kile kikamfanya Nassoro akageuka kumwangalia mamantilie, akamwona akirudishia kivivu kumpungia Mary.
“Ndiyo unafika au unaondoka?” Nassoro aliuliza huku akiliangalia begi lililokuwa likining’inia ubavuni mwa Mary.
“Nimekuja leo kumtafuta anti yangu. Nimemkosa. Nimeamua kurudi nyumbani,” Mary alisema.
“Umemkosa kivipi? Amesafiri?”
“Nimeshindwa kupajua anakoishi.”
“Ulitarajia angekusubiri hapa stendi?”
“Niliamua tu mwenyewe kuja kumtafuta. Sikumwambia kama nakuja. Nimemkosa na sasa narudi!”
“Ulimtafuta wapi na wapi?”
“Nimewauliza watu, wakaniambia hawamjui. Nimeamua kurudi!”
“Kwa hiyo unaamua kuondoka bila ya kumwona?”
“Nitamwonea wapi?”
“Kwani wewe ulivyoamua kuja ulitarajia ungempatia wapi?”
“Nilitaka kumtafuta kwenye baa, ndiko anakofanya kazi.”
Uso wa Nassoro ukapigwa na butwaa. Akauliza kwa sauti yenye mshangao, “Kwenye baa?”
“Si ndiko anakofanya kazi!”
“Ulikwenda ukamkosa?”
“Wala sikwenda!”
“Kwa nini?”
“Baa yenyewe pia siijui!”
Nassoro akainamisha uso wake chini kwa sekunde chache kabla hajauinua kumwangalia Mary usoni. “Unasema kweli au unatania Mary?” aliuliza.
“Khaa! Kwa nini nitanie?”Mary alijibu kiwepesi.
“Kwa hiyo umeridhika urudi bila ya kumwona?”
“Sasa ningefanya nini? Hapa Korogwe sina ndugu yeyote wa kusema ningeanzia kwenda kwake kisha baadaye ndiyo nianze kumtafuta mwenyeji wangu.”
“Nataka nikuulize swali Mary?” Nassoro aliuliza akiwa makini usoni.
“Uliza.”
“Huyo ndugu yako una umuhimu naye wa kumwona?”
Mary akafanya tabasamu dogo. “Ningesumbuka kuja mpaka huku?” aliuliza.
“Kwa hiyo ulikuwa na umuhimu wa kumwona?”
“Ndiyo maana yake!”
“Upo tayari twende nyumbani ukaliweke begi lako, kisha tuanze kumtafuta?”
Dhumuni lake la kutoroka halikuwa kuja kuangukia kwenye mikono ya mwanamume ili amweleze matatizo yake yaliyomtoa Lusanga, Mary alijionya. Onyo hilo likamuweka njiapanda na karibisho alilopewa. Akajiuliza kama karibisho analopewa limelenga kumsaidia kwa dhati kumtafuta ndugu yake au ulikuwa mwanzo wa kuingizwa kwenye mambo ya mapenzi kama sehemu ya kusaidiwa kumpata ndugu yake huyo. Akili yake ikawa inapambana na mambo mawili kwa wakati mmoja. Alikubali karibisho alilopewa? Au alikatae na aendelee na uamuzi wake wa awali wa kwenda Muheza kupata taarifa kamili za Stella na kisha arudi tena Korogwe?
Akiwa anawaza kwa kasi, Mary aliirudisha akili yake Lusanga. Kwa muda huo angekuwa anatafutwa, na taarifa za kupotea kwake zingekuwa zimeshasambazwa. Akahofu zingekuwa zimefika hadi Muheza! Kwa maana nyingine, kwenda Muheza kungewafanya wazazi wake wapewe taarifa za kuonekana kwake Muheza, lakini pia, mwendelezo wake wa kurudi tena Korogwe ungejulikana kuwa amekimbilia huko baada ya kuomba anwani kamili ya Stella kutoka kwa bibi yake! Hilo halikuwa lengo lake, alichokuwa akitaka ni wazazi wake wasijue yeye yuko wapi. Alitaka iwe hivyo kama sehemu ya kuwaadhibu! Kutokana na fikra hizo, akaliona suala la kwenda Muheza lingetoa mwanya kwa wazazi wake kujua mahali alikokimbilia!
Mary akamwangalia Nassoro aliyekuwa akisubiri jibu.
“Sawa!” Mary alimkubalia Nassoro.
*****
MARY alikaribishwa chumbani kwa Nassoro. Kilikuwa chumba nadhifu kwa daraja lake, kilichosheheni samani zote kwenye chumba kimoja. Kuanzia kitanda cha futi tano, makochi matatu, kabati dogo la nguo na jingine la vyombo na seti ya runinga. Chumba hicho, kwa Mary kilionekana kama aliyeingia chumba cha hoteli yenye hadhi ya nyota tano. Hakuwahi kulala au kuingia kwenye chumba cha aina hiyo. Kwa mtazamo wa haraka alijikuta akitamani kuishi na mwanamume mwenye chumba kama hicho.
Nassoro ndiye aliyemkumbusha Mary kuhusu safari ya kwenda kumtafuta Stella baada ya Mary kujisahau kama kulikuwepo na safari iliyokuwa imewaleta hapo. Wakaliacha begi chumbani, wakatoka. Shughuli ya kumtafuta Stella ikaanza. Haikuwa shughuli ndogo, iliwachukua hadi mchana kuhangaika kwenye baa zilizopo eneo la Manundu. Baa zikawa nyingi kuliko uwezo wa kuzizungukia. Na kote walikofika, kila waliyemuulizia, hakuna aliyemjua Stella!
“Itabidi tule chakula na kupumzika kidogo, kisha tuanze tena kumtafuta,” Nassoro alisema wakiwa kwenye moja ya baa waliyomuulizia Stella.
“Mi’ nimeshachoka, sitaendelea kumtafuta!” Mary alisema baada ya kukaa kwenye kiti cha baa.
“Unaweza kumtafuta hata kesho ukitaka!” Nassoro alisema kwa lengo la kuitupa karata ya kumbakisha Mary hapo Korogwe.
“Nimtafute hata kesho?” Mary aliuliza akijifanya kushangaa. Aliamua kucheza na akili ya Nassoro.
“Ndiyo. Ikiwa umechoka kama unavyodai, kipi kingine cha kufanya kama si kupumzika? Pumzika hadi kesho! Au unataka kurudi Lusanga kisha kesho upande tena basi la kuja huku kwa ajili ya kumtafuta upya?”
“Si nimekwambia hapa Korogwe sina ndugu?”
Nassoro akajiinamia. Alipouinua uso wake, akamwona Mary akimwangalia.
“Unaweza ukalala kwangu!” Nassoro alitupa karata mezani.
Vijana hao wawili wakaangaliana usoni. Nassoro akisubiri jibu, Mary akizuga kutafakari.
Kwa Mary ilikuwa bahati iliyojitokeza. Alikuwa tayari kwenda kulala kwa Nassoro, na alikuwa tayari kumridhisha kufanya naye mapenzi, kitu ambacho alijua Nassoro ndicho anachokihitaji. Lakini lengo lake halikuwa hilo, lengo lake ni kutorudi Lusanga! Hofu iliyokuwa ikimwandama ni kuhusu hiyo kesho endapo watamkosa tena Stella. Itakuwa ndiyo safari ya kurudi Lusanga? alijiuliza. Alishaingiwa na wasiwasi huenda zoezi la kumtafuta Stella lisifanikiwe. Nitafanya nini endapo sitompata? Hapo ndipo palipokuwa pakimuumiza kichwa. Asingeweza kumwomba Nassoro waendelee kuishi pamoja, alikuwa na uhakika asingeeleweka!
“Nahofia usije ukaniletea matatizo,” Mary alijibu.
“Matatizo kama?” Nassoro aliuliza akiwa makini na swali lake, alikuwa bado hajamwelewa vizuri Mary na swali lake.
“Hivi nikifanyiwa fujo usiku, nitakwenda wapi?” Mary aliuliza.
Nassoro akamwelewa Mary!
“Hilo haliwezi likatokea! Nassoro alimhakikishia Mary.
“Sawa,” Mary aliitikia. Hakuwa na chaguo. Asingeweza kuendelea kutumia Lugha ya kumzungusha wakati alihitaji hifadhi kama hiyo ilimradi asirudi Lusanga.
Waliagiza chips na kuku. Mary hakukumbuka kama alishawahi kula mlo kamilifu wa chakula hicho katika maisha yake.
“Agizia bia!” Nassoro alimwambia Mary.
“Situmii pombe,” Mary alijibu.
Nassoro akaagiza bia na soda kwa ajili ya Mary. Wakatumia muda mwingi wa mazungumzo yao kukumbushana kuhusu shule. Waliwazungumza walimu, wanafunzi na baadhi ya vijana wanaoishi Lusanga
 
MARY MARIAM (04)
BEKA MFAUME.
Nassoro akaagiza bia na soda kwa ajili ya Mary. Wakatumia muda mwingi wa mazungumzo yao kukumbushana kuhusu shule. Waliwazungumza walimu, wanafunzi na baadhi ya vijana wanaoishi Lusanga.
“Hujakuja muda mrefu Lusanga.” Mary alisema bila ya kumwangalia machoni Nassoro.
“Ni kweli, nina muda mrefu sijafika huko. Tokea nilivyomaliza darasa la saba nadhani niliwahi kuja kama mara mbili hivi, lakini tokea kaka yangu ambaye nilikuwa nikiishi naye kule afariki, sijarudi tena.”
“Umekuwa mkubwa!” Mary alisema na kutabasamu. “Ni tofauti na ulivyokuwa umemaliza darasa la saba. Kipindi kile ulikuwa ukionekana mdogomdogo.”
Kauli hiyo ikawapatia fursa ya kutaniana, huku kila mmoja akimwambia mwenzake ndiye aliyekuwa mdogo wakati wakiwa shule.
Mara baada ya kuondoka baa, wakaongozana hadi anapoishi Nassoro. Walipofika, walimkuta mama mtu mzima amekaa nje barazani mwa nyumba hiyo akisoma gazeti. Wakamsalimia.
“Shangazi,” Nassoro alimwita yule mama. Kisha akaendelea, “Huyu ni rafiki yangu tulisoma pamoja shule ya msingi, anaitwa Mary.”
Mama yule akiwa amevua miwani ya kusomea na kuishika mkononi alijenga uso uliochangamka na kumwambia Mary, “Karibu mwanangu.”
Mary akaitikia kwa kushukuru.
“Mary,” Nassoro alisema akiwa amemgeukia Mary. “Huyu ni mama yetu na ndiye mwenye nyumba hii,” alimtambulisha Mary. “Wote tunamwita anti Salome. Kwa hiyo na wewe mwite hivyo. Lakini yeye anaishi Dar es Salaam, amekuja kututembelea wanawe.”
Mary na mwanamke aliyetambulishwa kwa jina la anti Salome wakazungumza hili na lile pale nje wakati Nassoro akiwa ameshatangulia kuingia ndani. Baadaye Mary akaaga. Akaenda moja kwa moja chumbani kwa Nassoro.
“Ni kweli yule ndiye mwenye nyumba wenu?” Mary alimuuliza Nassoro baada ya kuingia.
“Ndiyo. Kwani vipi?”
“Anaonekana ana roho nzuri.”
“Ana watoto wake wakubwa. Wa kike anaishi Dar es Salaam. Nasikia ameolewa na mtu mwenye pesa. Mtoto wake mwingine ni mwanamume, yeye anaishi hapahapa Korogwe ni daktari na anamiliki hospitali yake mwenyewe.”
Mchana huo, Mary na Nassoro kwa mara ya kwanza wakafanya mapenzi.
*****
Giza lilipoingia, wakatoka pamoja. Nassoro akawa mwenyeji wa kumtembeza Mary katika Mji wa Korogwe. Katika matembezi yao, Nassoro akampeleka tena Mary eneo la stendi ili kuyaona mabadiliko ya mandhari yake yanavyokuwa wakati wa usiku. Eneo lote akaliona limezungukwa na miali ya taa kuonyesha biashara zilizokuwa zikiendelea eneo hilo. Ukawa kama mji mpya uliojitokeza. Walipotoka hapo, kwa mara nyingine wakaelekea baa. Wakala nyamachoma huku Nassoro akishushia kwa bia na mwenzake kwa soda.
Walirudi nyumbani saa tano usiku. Kwa mara nyingine tena, wakafanya mapenzi.
******
UKURASA mpya wa maisha ya Mary ukaanzia hapo.
Hakuwahi kufurahia maisha ya mapenzi yenye uhuru kama ilivyomtokea usiku uliopita. Kitendo cha kuzunguka na Nassoro na kukatiza kwenye mitaa huku wakiwa bega kwa bega na wakati mwingine kufanyiana utani wa hapa na pale kwa kupigana vibega vya kusutana kimapenzi na kujiamini kuzungumza katika wigo mpana wa lugha yenye kuonyesha upendo, ilikuwa ni sehemu ya hazina ya furaha aliyokuwa ameikosa kwa miaka yote. Hali hiyo ikamfanya amwone Nassoro kama mgunduzi aliyekuja kuivumbua hazina ya mapenzi iliyojificha moyoni mwake!
Alikuwa hajawahi kutekwa na nguvu ya mapenzi kutoka kwa mwanamume kama alivyoweza kutekwa na Nassoro. Ukawa kama ufunuo uliokuja kumtambulisha kuwa, Nassoro ndiye mwenye haki ya kustahili awe chaguo lake. Aliukumbuka usiku huo walivyoupitisha wakiwa kitandani kwa mazungumzo ya furaha iliyowapeleka kutoa vicheko vya usiku.
Hata hivyo, hadi kufikia kulala, Mary hakuizungumza sababu iliyomfanya aje Korogwe!
*****
Nassoro ndiye aliyewahi kuamka asubuhi akimwacha Mary kitandani. Akaenda kuoga. Alivyorudi akajiandaa kwa ajili ya kwenda kazini.
“Hivi yule baba yako wa kambo bado yupo?” Nassoro aliuliza ghafla wakati akifunga vishikizo vya shati.
Lilikuwa swali ambalo Mary hakutarajia kuulizwa. Kwa sekunde fulani hakuonekana kama angelijibu swali hilo. Kumbukumbu ya kubakwa na baba yake huyo ikamrudia, ikamteka mawazo na kuufanya muda huo utumiwe na Nassoro aliyekuwa akisubiri jibu kumwangalia.
“Mary!” Nassoro aliita kwa upole kwa lengo la kumshtua Mary aliyepotea kimawazo.
Akawa hakushtuka baada ya kuitwa. Aligeuka taratibu kumwangalia Nassoro, lakini sura yake ikabaki kwenye hali ileile ya kuwa mbali kimawazo.
“Yupo!” Mary alijibu kwa sauti iliyopwaya.
Nassoro akafanya mshangao mdogo usoni huku akiendelea kumwangalia Mary. Akahisi huenda mwenzake huyo hakupenda kuulizwa habari za baba yake.
“Ameacha ulevi?” Nassoro aliuliza tena.
“Atakufa nao!” Mary alijibu kwa sauti yenye hasira. “Yeye na mkewe!”
Safari hii Nassoro akaonyesha mshangao wa wazi. “Unamaanisha mama yako?” aliuliza katika hali ya kushtuka.
“Ndiyo. Si unajua kama mama yangu naye ni mlevi wa kutupwa?” safari hii Mary alimudu kuirudisha sauti yake katika hali ya kawaida.
“Najua. Ndiyo maana jana ulinishangaza uliponiambia hunywi pombe! Sikukuamini. Pale kwenu si palikuwa panauzwa pombe ya mnazi?”
“Mpaka leo panauzwa!”
“Halafu nilisikia hata wewe ulikuwa ukiuza?”
Nassoro alisema na kuyatuliza macho yake kumwangalia Mary.
“Walikuwa wakinilazimisha!” Mary alijibu bila ya kumwangalia Nassoro na macho yake bado yalionyesha kuwa mbali kimawazo.
“Kwa hiyo, unauza halafu hunywi?”
“Huamini?”
“Ni vigumu kuamini.”
Mary hakujibu palepale. Alionekana akiwaza, kisha kama aliyelazimishwa akasema, “Kama ungeendelea kukaa na mimi, ungenijua nilivyo!”
“Ni wewe tu mwenyewe,” Nassoro alisema. “Kwani ukiendelea kukaa hapa kuna ubaya gani? Ni nani asiyetaka kukaa na kitu cha nguvu cha aina yako!”
Kama yangekuwa ni matokeo ya mtihani, Mary angekurupuka kwa furaha, lakini si kwa hilo. Jibu la Nassoro lilimfanya asiamini alichokisikia! Kitu pekee alichoweza kukifanya ni kumshukuru Mungu kimoyomoyo kwa kumkubalia dua lake la kutorudi Lusanga.
Kabla ya kuondoka, Nassoro alimwachia Mary pesa ya matumizi, akamwelekeza bucha na genge lililokuwa jirani na baadhi ya vitu vingine vilivyopo hapo nyumbani kama vyombo vya kupikia na vinginevyo.
“Maeneo mengine ya kununua mahitaji unaweza ukamuuliza anti Salome.”
Nassoro aliaga angerudi usiku. Alipoondoka, hakugusia lolote kuhusu kurudi Lusanga wala suala la Stella.
Ndoto ya kutorudi Lusanga, ikaanza kuwa kweli kwa Maryi!
******
MARY aliamka kutoka kitandani na kufanya usafi wa chumba. Alifagia na kupiga deki, akavipanga vitu vidogo vidogo kwa mpangilio mzuri. Alihifadhi vizuri mswaki, dawa ya meno akaisogeza kwa kuiweka karibu na alipouweka mswaki baada ya kuona umewekwa karibu na ilipowekwa sumu ya panya. Chumba alikipanga upya, akakitoa kwenye sura ya ukapera na kukiweka katika mtazamo unaoonyesha kuna mwanamke anayeishi humo ndani. Katika harakati za kuingia na kutoka, Mary akaanza kukutana na wapangaji wengine wa nyumba hiyo na kusalimiana nao. Wapo walionyesha kumshangaa kutokana na kumwona akiwa na shughuli nyingi za humo ndani zilizomwonyesha hakuwa mwondokaji wa karibuni.
Akaonana na anti Salome kwa mara nyingine.
Mara baada ya kuandaa kifungua kinywa, Mary alimtengea anti Salome kwa kumpelekea chumbani kwake. Kitendo hicho kisichotarajiwa na anti Salome, kilimfanya mama huyo amshukuru Mary.
“Leo usipike mchana, mimi nitapika,” Mary alimwambia anti Salome. “Sasa hivi natoka naenda buchani, na Nassoro ameniagiza kama sehemu siijui, nikuulize wewe.”
“Usijali mwanangu, we’ njoo uniulize,” anti Salome alimhakikishia.
Kati ya mambo yaliyoulizwa na Mary mchana huo, ni jambo moja tu ndilo lililompa picha anti Salome kumwelewa vizuri Mary ni msichana wa aina gani. Ni pale Mary alipomwita chumbani kwa Nassoro na kumwomba amwonyeshe namna ya kuwasha runinga na namna ya kuitumia. Lakini pia, Mary hakuuficha ulimbukeni wake mbele ya anti Salome alipokuwa akitabasamu wakati wote wa kuiangalia runinga.
Kwake ilikuwa ni sehemu ya maisha aliyokuwa akiyakosa!
Ilipofika usiku majira ya saa tatu, Nassoro alirudi. Aliufungua mlango wa chumba chake taratibu bila ya kupiga hodi, akamkuta Mary anaangalia runinga. Akamwangalia kwa jicho la mara moja, lililotoa ujumbe uliomshtua Mary. Palepale baada ya kuangaliwa vile, Mary akahisi kuna jambo limekwenda sivyo! Amani ikamwondoka! Nassor akaingia pasipo kumsalimia, ukawa mshtuko mwingine kwa Mary.
Akiwa hayupo kwenye sura ya upendo tofauti na alivyoondoka asubuhi, Nassoro aliinama na kuichukua rimoti iliyokuwa kwenye kochi kandoni na alipokaa Mary. Akaizima runinga! Kitendo hicho kikamfanya Mary ainue uso kumwangalia Nassoro aliyekuwa amesimama akiwa bado na rimoti huku amejikamata kiuno kwa mikono yote miwili. Wakaangaliana usoni! Uso wa Nassoro ulikuwa umenuna, makali ya macho yake yalimwangalia Mary kwa hasira. Mary akaukwepeshe uso wake, kisha akaanza kuvisugua vidole kuonyesha taharuki ikichukua nafasi yake.
Mary alijawa na hofu, hakujua kilichotokea, lakini pia alishindwa kuuliza. Alimwona Nassoro kama mwokozi wake aliyekuja kumwokoa. Akaogopa asimuudhi kwa kumuuliza swali litakaloendelea kumkasirisha. Akaamua aendelee kuwa kimya, akimsubiri Nassoro aseme kilichomuudhi, kisha angeichukua nafasi hiyo kuomba msamaha hata kama angetuhumiwa kwa kosa ambalo hakulifanya. Alishakuwa mtumwa!
“Mary,” Nassoro aliita taratibu tofauti na sura yake ilivyoonekana. Pengine hakuona umuhimu wa kufoka kwa sababu ujumbe atakaoutoa ungekuwa ni mfupi na wenye kueleweka.
Mary akainua uso wenye macho yaliyokwishatah
aruki. Akamwangalia Nassoro kwa sura iliyoomba huruma kabla hata hajalifahamu kosa lake.
“Nataka utoke humu ndani, sasa hivi!” Nassoro alisema huku akiendelea kumwangalia Mary usoni.
Kauli hiyo ikasikika kwenye masikio ya Mary kama radi, akapigwa na butwaa kama vile alikuwa hajaelewa alichoambiwa!
“Hujanisikia?” Nassoro alimuuliza Mary huku akiendelea kumwangalia usoni.
Mary hakujibu, kauli ilishapotea kinywani mwake!
“Nakuomba uondoke hapa kwangu!” Nassoro aliirudia kauli yake, safari hii ikaonyesha msisitizo.
“Usiku huu nitakwenda wapi Nassoro?” Mary aliuliza kwa sauti iliyokata tamaa. “Si unajua hapa Korogwe sina mahali pengine pa kwenda?”
“Hilo halinihusu! Ninachotaka uondoke sasa hivi!”
“Nassoro, kwa nini unanifanyia hivi? Si ungeniambia tokea asubuhi ningeweza kuondoka. Sasa hivi nitapata usafiri gani wa kunirudisha kwetu?” Mary alisema na wakati huohuo machozi yakang’aa kwenye mboni zake.
“Unataka kuondoka kwa hiari yako au nikuondoe kwa nguvu?” sauti ya Nassoro ilipanda kwa jazba.
Mary akaogopa! Akasimama kutii amri aliyopewa na kuonekana kuwa tayari kuondoka. Lakini ghafla akajiuliza, nikiondoka hapa nielekee wapi? Akachanganyikiwa! Akamwangalia Nassoro kwa uso uliolowa machozi na kutoa taswira ya kuomba huruma kimyakimya.
Nassoro akaupitisha mkono wake katikati ya kwapa la Mary na kumgeuzia upande lilipo begi lake.
“Chukua begi lako na uondoke!” Nassoro alisema huku akimwonyesha Mary begi lilipo.
Mary akaliangalia begi lake lililokuwa halina nguo. Nguo zake alishazitoa akazipanga kabatini wakati wa asubuhi alipokuwa akifanya usafi kwa kuamini alishapata mahali pa kuishi.
“Nguo zangu zipo kabatini ngoja nizichukue,” Mary alisema kwa sauti ndogo iliyohamanika.
“Na nguo zako ulishaweka kabatini kwa kujiona hapa umeshafika? Ulidhani mimi bwege wa kuweza kuishi na malaya?”
Mary hakujibu ingawa hakujua kwa nini aliitwa malaya. Aliliendea kabati na kulifungua, akaingiza mikono yake kabatini, badala ya kutoa nguo zake akaonekana kusita, kisha akawa amepigwa na butwaa. Akavuta pumzi kubwa kama aliyepaliwa na maji. Alikuwa ameshindwa kuudhibiti uvumilivu wa kulia kimyakimya! Sauti ya kilio iliyokosa mhimili wa kuizuia ikamtoka kwa nguvu na kisha akaidhibiti tena kwa kuilazimisha isitoe sauti. Akaanza kulia kwa sauti ya chini na mwili wake kutikisika kwa kwikwi zilizoandamana na machozi.
“Haloo!” Nassoro aliita kwa jazba. “Unajua unanipotezea muda wangu!” alifoka.
“Naondoka Nassoro!” Mary alisema kwa sauti yenye kitetemeshi cha kilio.
Akavitoa viguo vyake vichache na kuvikamata kwa mpigo, akavikumbatia kwa mkono mmoja na ule mwingine ukafunga kabati. Akarudi kwenye begi na kupiga magoti, akaziingiza nguo zake kwenye begi bila utaratibu wa kuzipanga. Akazishindilia mara moja, akavuta zipu na kulifunga. Badala ya kuinuka, akamwangalia Nassoro kwa macho yanayobubujika machozi, akatamani kumuuliza, kwa nini unanifukuza? Lakini alishindwa baada ya kujiona hana haki ya kuuliza. Aulize kama nani?
“Niruhusu nilale mpaka kesho asubuhi ili niweze kupata usafiri wa kunirudisha Lusanga,” Mary aliomba huku sauti yake ikifanya kitetemeshi cha kukabiliana na kudhalilishwa. “Usiku huu, mimi nitakwenda wapi? Tafadhali Nassoro, nionee huruma!”
Huruma ilikuwa mbali kwa Nassoro. Subira ikamwondoka, akapiga hatua zilizojaa shari hadi alipokuwa Mary amepiga magoti. Akamkamata kwenye bega na kumwinua kwa nguvu, kisha akamsukuma mlangoni huku akifoka kwa sauti yenye jazba, “Nimekwambia toka!”
Nguvu aliyoitumia Nassoro ilikuwa kubwa, ikamkokota Mary hadi kwenye mlango na kujibamiza. Akanguka kifudifudi kisha akatulia kimya pale alipoangukia. Akawa kama mfu huku begi likiwa limeangukia ubavuni kwake.
Palepale Nassoro akaingiwa na hofu kuwa, ameua! Akanywea, akasimama huku akimwangalia Mary. Ukimya uliojitokeza kwa Mary ukamfanya ajikune nywele za kisogoni na kuanza kujiuliza, afanye nini kama atakuwa ameua?
Ghafla, Mary akaonekana kuzinduka baada ya sauti yake kusikika ikiita, “Nassoro!”
Nassoro akajikuta akipata ahueni baada ya kumsikia Mary akiita. Hata hivyo hakuitikia kutokana na kigugumizi kilichomkumba kuwa, ameua!
“Nassoro!” Mary aliita tena akiwa palepale alipolala.
“Unasemaje?” Nassoro aliitikia kijeuri baada ya kuwa na uhakika alikuwa hakuua.
“Nimekufanyia kosa gani mpaka unaniumiza hivi? Na kwa nini uniite malaya? Au ni kwa sababu ya kukukubali kirahisi?”
Zilipita sekunde kadhaa bila Nassoro kujibu. Sehemu ya mwonekano wa macho yake kulionekana huruma, lakini upande wa pili wa mwonekano kulionekana hasira.
“Kama usingekuwa malaya usingeweza kuniambukiza gonoria!” Nassoro alisema na kuonekana kufadhaika ghafla. “Sijui kama nina usalama tena! Oh, Mungu wangu!” Akajishika kisogoni kwa mikono yote miwili kama aliyechanganyikiwa. “Sijui kama hujaniambukiza Ukimwi!”
Kauli ya Nassoro ikaupasua moyo wa Mary! Akahisi nguvu zikimwishia! Alikuwa kama amefunguliwa pazia la kuiona tena picha ya kubakwa alikofanyiwa na baba yake. Akamwona jinsi alivyokuwa juu ya mwili wake akijitosheleza tamaa yake. Kila kitu kikawa wazi kwake! Alikuwa ameambukizwa ugonjwa huo na baba yake! Akaubana mdomo pale alipolala, akasaga meno kwa uchungu, akahofu ameshaathirika!
Nitamjibu nini Nassoro? alijiuliza. Nijitetee kuwa nimebakwa na baba yangu? Na ndiyo sababu iliyonikimbiza kuikimbia Lusanga? Aliamini halikuwa kosa lake kumwambukiza Nassoro kwa sababu alikuwa hajui kama ameambukizwa. Aliamini angekuwa amepata sababu ya kumweleza Nassoro ukweli huo, lakini kwa upande wa pili bado isingesaidia kumbakisha aendelee kuishi hapo kwa Nassoro.
“Nisamehe Nassoro,” Mary alisema kwa sauti iliyokata tamaa. Alijiona akikosa utetezi mwingine wa kujieleza nao zaidi ya huo wa kuomba msamaha. “Naondoka, lakini naomba unisamehe hadi kwa Mungu!” Baada ya kusema hivyo Mary alisimama na kulichukua begi lake.
Nassoro hakujibu, badala yake alimwangalia Mary alivyokuwa akitoka. Akawa kama aliyekuwa akilisimamia zoezi la kuhakikisha Mary anaondoka. Baada ya Mary kutoka, naye akapiga hatua kutaka kutoka ili amshuhudie anavyoondoka. Akiwa mlangoni, akashangaa kumwona Mary akigeuza na kurudi tena mle chumbani. Nassoro akaganda na sura yake kuinunisha ghafla. Akataka kumuuliza kinachomrudisha, lakini akawahiwa!
“Samahani Nassoro,” Mary alisema bila ya kusimama huku akimkwepa Nassoro ili kupata nafasi ya kuingia tena chumbani. Akaendelea, “Kuna kitu changu nimekisahau ndani, nakwenda kukichukua.”
Nassoro akaingiwa na kigugumizi. Akabakia kumsindikiza Mary kwa macho hadi chumbani alikoingia na kumwona akiinama na kuchukua kitu ambacho hakukiona, kisha akamwona akikitia kwenye mfuko wa pembeni wa begi alilolibeba.
Wakati Mary akiwa anatoka, Nassoro akasogea zaidi kutoa uwazi pale mlangoni aliposimama ili Mary apite bila ya miili yao kugusana. Pale mlangoni kabla ya kutoka kulikuwa na ndoo iliyokuwa na maji ya kunywa, Mary akasimama. Akainama na kuchukua glasi iliyokuwa juu ya ndoo, kisha akaufunua mfuniko na kuchota maji.
“Glasi yako utaikuta uani kwenye karo,” Mary alisema wakati akimpita Nassoro. “Natokea mlango wa uani!”
Nassoro hakujibu. Alimwacha Mary hadi alipofika uani, kisha naye alirudi chumbani kwake. Akatoa kutoka mfukoni mwa suruali yake dawa za kutibu kisonono na kuchukua tembe mbili ili ameze. Akiwa kwenye mwelekeo wa kuifuata ndoo yenye maji, akaikumbuka glasi iliyochukuliwa na Mary. Akalaani kwa usumbufu anaopewa wa kwenda kabatini kuchukua glasi nyingine. Wakati akiifungua kabati huku akiendelea kulaani, akakifikiria kitendo cha Mary kuichukua glasi na kutoka nayo. Hakuona umuhimu wa Mary wa kuondoka na glasi ile yenye maji kwa sababu angeweza kuyanywa maji palepale na kuirudisha glasi kwenye ndoo na kisha angeondoka zake, tena kwa kupitia mlango wa mbele. Akalaani kwa mara nyingine kupewa usumbufu utakaomfanya aende uani kuifuata na kuirudisha glasi yake.
Ghafla pasipo kutarajia, kumbukumbu ya kumwona Mary akiinama na kuchukua kitu mle chumbani ikajirudia. Alifuata nini? alijiuliza. Akaanza kuunganisha hatua moja kwa nyingine kuhusu kitendo cha Mary kurudi chumbani. Alichukua nini? Na kwa nini amekwenda kunywea maji uani? Kwa nini aamue kutokea uwani wakati njia rahisi ya kutokea iko mlango wa mbele? Nassoro akaanza kuingiwa na mashaka baada ya kuhisi vitendo hivyo kama vilikuwa na mpangilio fulani.
Akaikumbuka sumu ya panya iliyokuwemo mle chumbani!
******
AKAKUMBUKA alivyoinunua siku iliyopita kwenye duka lililopo jirani na hapo nyumbani ikiwa kwenye kipakiti kidogo na kuileta humo chumbani ili baadaye ampelekee mama yake anayeishi kijijini, kilometa chache kutoka hapo Korogwe. Palepale Nassoro akakurupuka alipokuwa amesimama. Akaenda sehemu aliyokuwa ameiweka sumu ile. Ikawa kama alivyotarajia. Haikuwepo! Atakuwa ameichukua? alijiuliza. Mbona alivyorudi hakuja hapa? Palepale akayatazama mabadiliko ya mle chumbani. Chumba kilikuwa kimepangwa upya. Akahisi Mary aliihamisha sumu hiyo kutoka pahali pa awali alipokuwa ameiweka. Akaamini, alipokuwa amemwona Mary akiinama wakati akirudi chumbani kufuata alichodai amekisahau, alikuwa ameirudia sumu ile sehemu aliyokuwa ameihamishia!
Ameichukua!
Akiwa ametaharuki, Nassoro alitoka kwa kasi chumbani kwake. Akakutana na anti Salome ukumbini. Anti Salome akaiona taharuki aliyoivaa Nassoro usoni.
“Vipi?” anti Salome alimuuliza Nassoro.
“Subiri!” Nassoro alijibu kama mtu aliyepandwa na mzuka, akampita kwa kasi mwanamke huyo kuelekea uwani.
Anti Salome akaganda kwa mshangao na kuangalia uani alikokwenda Nassoro.
Nassoro akaiona glasi juu ya karo kama alivyoahidiwa na Mary, kisha akaiona pakiti ya sumu ya panya ikiwa pembeni. Akaichukua pakiti ile na kuiangalia. Akaiona imekatwa kwa kuvutwa upande mmoja wa ncha kama iliyochanwa na meno. Akaiangalia glasi, ilikuwa tupu! Lakini ndani kulikuwa na matone ya maji kuonyesha ilitumika.
Mungu wangu! Nassoro alihamanika peke yake na kugeuka kwa kasi kutaka kukimbilia nje kupitia mlango wa uani. Ghafla akamwona anti Salome akitokea mlango mkubwa wa nyumba unaotokea uani.
“Nassoro mwanangu, kuna nini?” anti Salome aliuliza na kuonyesha taharuki usoni mwake.
“Anti nifuate, Mary amekunywa sumu!” Nassoro akatoka kama mshale kupitia mlango wa uani.
***ITAENDELEA
KWA ANAYETAKA KUISOMA HADITHI YOTE HII KWA MKUPUO, TAFADHALI INGIA PLAYSTORE UI-DOWNLOAD APP YA Uwaridi ( UWARIDI APP)
 
MARY MARIAM (05)
BEKA MFAUME
Anti Salome akaganda kwa mshangao na kuangalia uani alikokwenda Nassoro.
Nassoro akaiona glasi juu ya karo kama alivyoahidiwa na Mary, kisha akaiona pakiti ya sumu ya panya ikiwa pembeni. Akaichukua pakiti ile na kuiangalia. Akaiona imekatwa kwa kuvutwa upande mmoja wa ncha kama iliyochanwa na meno. Akaiangalia glasi, ilikuwa tupu! Lakini ndani kulikuwa na matone ya maji kuonyesha ilitumika.
Mungu wangu! Nassoro alihamanika peke yake na kugeuka kwa kasi kutaka kukimbilia nje kupitia mlango wa uani. Ghafla akamwona anti Salome akitokea mlango mkubwa wa nyumba unaotokea uani.
“Nassoro mwanangu, kuna nini?” anti Salome aliuliza na kuonyesha taharuki usoni mwake.
“Anti nifuate, Mary amekunywa sumu!” Nassoro akatoka kama mshale kupitia mlango wa uani.
******
“JESUS!” anti Salome alisema na kuanza kumfuata Nassoro. Kwa kuwa alishakuwa na umri mkubwa, hakuweza kuendana na kasi ya Nassoro aliyekuwa amemwacha kwa hatua za mbali.
Nassoro alimwona Mary akiwa umbali wa mita zisizopungua thelathini akiwa na begi lake begani akitembea kwa mwendo wa kawaida kama vile hakuna alichokifanya nyuma yake, Nassoro akaongeza kasi ya mbio.
“Mary!” aliita.
Mary aligeuka nyuma, alivyomwona Nassoro akimkimbilia, naye akaongeza kasi ya mwendo na baadaye kukimbia. Kasi ya Nassoro ilikuwa kubwa, akamfikia Mary, akamvamia na kumkamata.
“Nassoro niache!” Mary alisema na kujikakamua kujitoa mikononi mwa Nassoro. “Naomba uniache!”
“Sikuachi!” Nassoro alisema huku akihema na kujaribu kumbeba Mary. “Siwezi kukuacha ujiue!”
“Nitakayekufa ni mimi, wewe inakuhusu nini? Wacha tu nife!” Mary alisema huku akiendelea kulazimisha kujitoa.
Wote wawili wakaanguka chini, Nassoro akawa juu, Mary akawa chini. Ikawa nafasi nzuri kwa Nassoro kumdhibiti Mary. Purukushani yao ikawavutia watu wachache wa mtaani waliokuwepo. Wakaanza kuwasogelea.
Anti Salome naye akawasili. “Jamani nyie watoto hebu tulieni kwanza!” alisema kujaribu kuwatuliza.
“Anti Salome nunua maziwa hapo dukani uje nayo haraka, huyu amekunywa sumu!” Nassoro alisema na kuonekana kuchanganyikiwa huku akiendelea kumdhibiti Mary.
Awali, watu waliokuwepo walidhani ni ugomvi wa kimapenzi, lakini wakashtuka baada ya kumsikia Nassoro akitoa sababu ya kudai maziwa yanunuliwe.
“Nani kanywa sumu?” mmoja wa vijana wa pale mtaani anayemfahamu Nassoro aliuliza.
“Huyu msichana!” Nassoro alijibu kwa sauti iliyolalamika.
Kauli hiyo ikamfanya kijana aliyeuliza swali kumkimbilia anti Salome aliyekuwa dukani akiwa tayari ameyanunua maziwa. Kijana yule akamnyang’anya anti Salome maziwa, akarudi kwa kasi walipokuwepo Nassoro na Mary. Wakaongezeka vijana wengine wawili wakamdhibiti Mary.
Harakati za huduma ya kwanza za kumnywesha kwa nguvu Mary maziwa, zikaanza. Awali Mary alikuwa akikataa kwa kubana mdomo, lakini alipozidiwa nguvu, akauachia. Ilichukua muda mfupi maziwa kufanya kazi. Mary alitapika mfululizo hadi akawa hoi. Hekaheka ya kutafuta teksi ikafanyika. Ikapatikana! Nassoro na yule kijana aliyeonekana kuwa na ukaribu naye wakambeba Mary na kuingia naye kiti cha nyuma kwenye teksi iliyowasili. Anti Salome naye akaingia kiti cha mbele cha abiria.
“Tupeleke Magunga Hospitali!” Nassoro alimwambia dereva wa teksi.
Dereva akaiondoa teksi kuielekeza iliko Hospitali ya Magunga.
“Tusiende Magunga!” anti Salome alisema ghafla. “Geuza gari tumpeleke hospitali ya Usambara!”
“Kwa nini?” Nassoro aliuliza na kuonekana bado amechanganyikiwa na tukio hilo kiasi cha kusahau kama hospitali iliyotajwa ilikuwa ikimilikiwa na mtoto wa kiume wa anti Salome.
Anti Salome akionekana mtulivu, aligeuka na kumwangalia dereva wa teksi. “Twende Usambara!” alisema.
Dereva akageuza gari na kuelekea hospitali ya Usambara. Wakati huohuo, anti Salome akampigia simu mtoto wake.
“Marahaba Dokta,” alisema. Alipenda kumwita mwanaye kwa jina lake la kitaaluma. “Uko zamu? Nina emergency kidogo…nakuja na binti mmoja amekunywa sumu ya panya…aah, mambo ya vijana mwanangu, lakini tumewahi kumnywesha maziwa muda mfupi baada ya kuinywa…ndiyo ametapika. Sawa tupo njiani tunakuja na gari.”
Hospitali ya Usambara ipo kwenye barabara inayoelekea Old Korogwe, ina ghorofa mbili na eneo la kulaza wagonjwa. Walipofika, moja kwa moja walikwenda kumwona daktari bila ya kufuata taratibu za awali. Mary akawahiwa kupewa matibabu na baadaye kulazwa.
Anti Salome na mwanaye ambaye ndiye daktari aliyemhudumia Mary, walichukua muda kuzungumza peke yao, kisha anti Salome alitoka na kuungana na Nassoro akiwa na mwenzake. Wakarudi nyumbani wakimwacha Mary hospitali.
Wakiwa wamesharudi nyumbani, anti Salome akamtaka Nassoro amweleze sababu ya Mary kutaka kujiua. Nassoro akaeleza mkasa mzima, tokea alivyoonana na Mary stendi na kumsaidia kumtafuta ndugu yake ambaye walimkosa. Baada ya hapo, wakaangukia kufanya mapenzi na ndipo alipojigundua ameambukizwa kisonono!
“Sikuwa na njia nyingine anti, isipokuwa kumfukuza! Nassoro alisema. “Mwenzangu akaamua kunywa sumu!”
“Hiyo siyo sababu ya kunywa sumu!” anti Salome alisema. “Kulala kwako usiku mmoja hakuwezi kuwa sababu ya kutaka kujiua, na wala mapenzi yenu ya saa chache iwe sababu ya kutaka kujiua!”
Hata mimi hilo limenishangaza anti!” Nassoro alisema. “Labda ni kweli alikuwa hana pahali pa kwenda, huenda ndiyo sababu iliyomfanya anywe sumu.”
“Maamuzi ya kujiua hayafanywi kirahisi hivyo!” anti Salome alisema na kumwangalia Nassoro. “Naomba kesho usiende hospitali, niache mimi niende. Nataka kuzungumza naye!”
Nassoro akakubaliana na wazo hilo.
“Mara nyingine kesi za mtu aliyetaka kujiua usizipeleke kwenye hospitali za serikali,” anti Salome alisema. “Hospitali inaripoti kesi hizo polisi na serikali inamshtaki raia kwa kutaka kujiua.”
“Anti hilo nalijua,” Nassoro alisema. “Lakini nilikuwa nimechanganyikiwa. Sikupata muda wa kutafakari.”
“Kwa hiyo uwe mwangalifu.”
******
ALIMKUTA mhudumu wa kike akimalizia kumuwekea Mary chupa nyingine ya dripu.
“Anaendelea vizuri,” mhudumu alimwambia anti Salome aliyefika hapo hospitali mapema asubuhi. Alikuwa akimjua mama huyo kuwa ndiye mama mzazi wa bosi wake.
“Ninaweza nikazungumza naye?” anti Salome aliuliza.
“Unaweza.”
Mhudumu akatoka. Anti Salome akaenda kwenye kiti kilichokuwa mkabala na kitanda alicholala Mary, akakaa.
“Unajisikiaje?” anti Salome alimuuliza Mary huku akijiweka sawa alipokaa.
Akionyesha kutahayari, Mary alijibu, “Sijambo anti,” kisha aliamkia.
Baada ya kuitikia amkio alilopewa, anti Salome akasema, “Nassoro alikuwa aje, nimemzuia. Nataka kwanza kuzungumza na wewe!”
Mary hakujibu, lakini pia hakumwangalia anti Salome.
“Nassoro ameniambia, alikufukuza kwa sababu ulimwambukiza kisonono. Hizo habari ni kweli?”
Zilipita sekunde kadhaa bila ya Mary kujibu. Macho yake kwa ndani yakawa yanameremeta, yalikuwa machozi. Ghafla akaikamata shuka na kujifuta machoni, kisha akasina kama mwenye kamasi.
“Mary mwanangu,” anti Salome alisema kwa upole. “Naomba unieleze kama ni kweli ili daktari akupe matibabu ya huo ugonjwa.”
Kama vile asiyependa kulizungumzia hilo tukio, Mary akaubana mdomo kujizuia kulia. “Inawezekana ikawa hivyo!” alisema na kujifuta tena machoni.
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Inawezekana nikawa nimeambukizwa,” Mary alisema na kuendelea kukwepa kumwangalia anti Salome.
Anti Salome akaonekana kutatizika na kauli ya Mary. Akazidisha umakini kumwangalia. “Nani aliyekuambukiza?” aliuliza.
Mary hakujibu!
Anti Salome akawa na mashaka huenda Mary ni kati ya wasichana wanaoweza kutembea na wanaume hata watatu kwa siku mradi apate pesa ya kujikimu na maisha. Akauona ugumu uliopo kwa msichana huyo kuweza kumtambua mtu aliyemwambukiza. Akaamua kughairi kutoendelea kumhoji jambo hilo.
“Baba!” Mary alisema ghafla.
Kwanza anti Salome hakuamini kama alisikia vizuri, lakini pia hakuwa na uhakika kama kuisikia kauli hiyo ilimaanisha Mary alikuwa akizungumza na yeye.
“Umesema nani?” anti Salome aliuliza huku akimwangalia Mary.
“Baba,” Mary alijibu.
“Amefanya nini?”
“Ndiye aliyeniambukiza.”
Kauli hiyo ikamchanganya anti Salome. Akakunja uso na kumwangalia Mary. “Ulikuwa ukitembea na baba yako?” aliuliza.
Mary akatikisa kichwa kwa haraka kukataa. Akaonekana kuwa na hisia kali za kuumizwa na kumbukumbu. Akabana mdomo na kutikisa tena kichwa, safari hii kwa hisia kali zaidi. Anti Salome akawa anamwangalia katika hali iliyomjengea hisia kuwa, binti huyo yupo kwenye matatizo ya akili.
Mary akaikamata shuka kwa mikono yake yote miwili, akaitia mdomoni na kuing’ata.. “Alinibaka!” alisema kwa sauti yenye kitetemeshi cha kilio.
“Mungu wangu!” anti Salome alihamanika. “Huyo ni baba yako mzazi?” aliuliza.
“Hapana! Ni baba wa kufikia!”
Anti Salome akavuta pumzi na kuibana kifuani. “Unaishi na nani?” aliuliza.
“Na wote, yeye na mama yangu.”
“Mama yako anajua kama umebakwa?”
“Hajui.”
“Ni tabia yake kukubaka?”
“Majuzi ndiyo ilikuwa mara ya kwanza!”
“Kwa nini hukumwambia mama yako?”
“Asingenisaidia!”
Anti Salome alijikuta akishusha pumzi kwa nguvu. “Baba yako mzazi yuko wapi?” aliuliza.
“Sina baba!”
“Una maana gani?”
“Simjui baba yangu, watu wanasema yuko Uarabuni.”
Anti Salome akakipiga kimya cha muda mfupi, kisha akasema, “Mary, unaweza ukaniambia historia ya maisha yako hadi unabakwa na huyo unayemsema ni baba yako?”
Mary akatikisa kichwa kukubali.
Dakika chache zilizofuata, anti Salome alijikuta akiisikiliza historia ya binti huyo inayohusu maisha yake hadi siku alivyojikuta akiangukia kwenye mikono ya Nassoro.
MIAKA MITANO BAADAYE
DAR ES SALAAM
MARY alikuwa amesimama akiwa ameegemea mnazi uliopo ufukweni mwa Coco Beach uliopo Oysterbay jijini Dar es Salaam. Usoni alikuwa amevaa miwani ya jua, maungoni mwake alivaa blauzi yenye kitambaa chepesi iliyoshonwa bila ya madoido ya kukera na ilikuwa ikipeperushwa na upepo mkali wa bahari. Chini ya blauzi hiyo alivaa suruali ya jinzi iliyomkaa vyema na kumshika kwenye mapaja. Ikalionyesha umbile lake zuri kuanzia nyonga hadi visiginoni. Yeyote angemwona, hata kama angekuwa ni mwanamke mwenzake, asingeridhika kuendelea na safari yake bila ya kugeuka na kumwangalia kwa mara ya pili kuhakikisha uzuri aliouona.
Mary alikuwa akiiangalia baharini wakati jua la alasiri likiyoyomea magharibi mwa dunia. Ingawa alikuwa peke yake, lakini kamwe isingekuingia kwenye fikra alikuwa amekuja peke yake kwenye eneo hilo. Eneo lote la fukwe lilionekana kuwa tulivu kutokana na kutokuwa siku ya mwishoni mwa wiki wala sikukuu. Watu na magari machache ndivyo vilivyoonekana kwenye uwanda huo wenye mandhari ya kupendeza yenye mchanga mweupe. Watu wachache walionekana wakiogelea baharini na wengine wakiwa wamekaa pembezoni mwa fukwe huku baadhi wakiwa kwenye mgahawa wa Coco Beach.
Utulivu uliokuwepo hapo uliifanya akili ya Mary ielee juu ya bahari anayoiangalia, ikatekwa na mawimbi yanayotoa povu kutokana na upepo mkali. Tukio hilo likawa kama sehemu ya kioo alichokuwa akiyaangalia matukio yaliyomtokea miaka mitano nyuma.
Alikuwa akiikumbuka siku alipokuwa na anti na Salome kwenye Hospitali ya Usambara ya mjini Korogwe, ikiwa ni siku ya pili tokea alivyokunywa sumu kutaka kujiua na kuletwa kwenye hospitali hiyo. Siku hiyo ndiyo iliyobadilisha maisha yake kwa ujumla!
Ilikuwa ni baada ya kumwelezea anti Salome historia ya maisha yake na jinsi tukio la kubakwa na baba yake lilivyomlazimisha atoroke kutoka kijijini kwao Lusanga na kukimbilia Korogwe kulikomkutanisha na mama huyo. Na baada ya maelezo hayo yaliyomsimumua anti Salome, ndipo mwanamke huyo alipopata wazo la kumchukua kuja naye jijini Dar es Salaam!
“Kesho kutwa narudi zangu Dar es Salaam,” Mary alikumbuka alivyoambiwa na anti Salome. “Kama upo tayari kwenda kufanya kazi za ndani, basi twende pamoja Dar es Salaam!”
Ni kauli iliyotamkwa kirahisi, lakini haikuondoka kirahisi. Mary akaipokea kwa kutamka kuwa yupo tayari kwenda Dar es salaam kuliko kurudi kijijini Lusanga! Siku iliyofuata akatolewa hospitali na kuwa mikononi mwa anti Salome. Hakurudishwa tena nyumbani kwa Nassoro, akapelekwa kwa mtu ambaye anti Salome alidai ni rafiki yake. Akakaa huko kwa siku moja zaidi. Siku iliyofuata akiwa na anti Salome, Mary akasafirishwa rasmi kuletwa Dar es Salaam.
Kamwe haitoisahau siku hiyo!
******
SIKU za mwanzoni akiwa katika maisha mapya ya Dar es Salaam, Mary aliendelea kuumizwa na kumbukumbu za Nassoro. Alikiri kwenye nafsi yake alivyokuwa amempenda kijana huyo aliyeishi naye kwenye dimbwi la mahaba kwa saa chache. Alikuwa ni mwanamume wake wa kwanza kumpenda! Ndiye aliyemwingiza kwenye ufahamu wa kujua thamani ya kupenda, lakini akawa ni huyohuyo aliyemtoa kwenye thamani hiyo!
Alikumbuka alivyokuwa akiangaliwa na Nassoro walipokuwa kwenye baa za Korogwe wakifurahia kujuana kwao. Macho ya Nassoro yalionyesha dalili zote kuwa, alikuwa akimhitaji. Na yeye pasipo matarajio ya kukutana na kijana huyo, akajiona kuwa mikononi mwa Nassoro angekuwa ameua ndege wawili kwa jiwe moja. Kwanza, ilikuwa ni hifadhi aliyokuwa akiihitaji. Pili, aliipata hifadhi hiyo kwa mtu aliyemkubali moyoni mwake!
Kitendo cha kufukuzwa na Nassoro usiku ule kilimuumiza kila alipokikumbuka. Ilikuwa ni moja ya ukatili alioshuhudia akifanyiwa katika maisha yake. Ingawa hakutaka kumlaumu sana Nassoro kutokana na kutoujua upande wa pili wa yeye alivyoupata ugonjwa huo, lakini bado alijiona hakustahili kufanyiwa uamuzi ule wa kufukuzwa usiku wakati Nassoro alikuwa akijua, hakuwa na mtu yeyote aliyemjua pale Korogwe Zaidi yake!
Hilo nalo likawa tukio jingine ambalo aliamini asingelisahau kwenye maisha yake!
Akiwa anaishi nyumbani kwa anti Salome jijini Dar es salaam, Mary alifanya kazi za ndani kwa miezi kadhaa hadi siku alipoelezwa na mlezi wake huyo, kwamba amempatia kazi sehemu nyingine kwa mfanyabiashara tajiri Mtanzania mwenye asili ya Kiarabu aliyeitwa Mohamed Alawiy.
Akahama nyumbani kwa anti Salome na kwenda katika ajira rasmi ya kazi za ndani, nyumbani kwa mfanyabiashara huyo tajiri. Kuanza kazi nyumbani kwa tajiri mpya ndiyo ukawa mwanzo wa kupoteza jina lake la Mary. Wenyeji wake wakawa wanamwita kwa jina la Mariam. Mabadiliko hayo ya kubadilishwa jina yalitokana na sababu ndogo tu, kwa kuwa naye alikuwa na asili ya Uarabu, asili iliyolingana na matajiri zake waliokuwa waumini wa dini ya Kiislamu kulimfanya aonekane ni mmoja wa wana familia hiyo, badala ya mtumishi wa ndani!
Tajiri aliyemwajiri Mary, mzee Mohamed Alawiy aliishi akiwa na mkewe na watoto watatu, mmoja wa kiume na wawili wa kike. Mtoto wake wa kiume aliyeitwa Hamdun aliondoka kwenda kazini Jeddah, Saudi Arabia baada ya siku chache tokea Mary alipoajiriwa kwenye nyumba hiyo. Watoto wake wa kike, walikuwa wakisoma kwenye shule ya sekondari ya binafsi. Pamoja na kusoma kwenye shule ghali yenye walimu wazuri, lakini baba yao alimleta mwalimu nyumbani kila jioni kwa ajili ya kuwafundisha mabinti zake hao.
Mary alijenga uhusiano mzuri na familia hiyo hasa mabinti wa mzee huyo. Ukaribu huo ukawafanya waugundue uwezo wa akili aliokuwa nao Mary. Na katika hali isiyo ya kawaida, mabinti hao wakamshawishi Mary awe anasoma masomo ya jioni ili kuendeleza elimu yake iliyoishia darasa la saba. Mary akakubali. Mabinti hao wakamwambia mama yao kuhusu jambo hilo, mama yao naye akamwambia mumewe. Hatimaye ushawishi huo ukakubaliwa na mzee Alawiy. Mary akajiunga na masomo ya sekondari ya kusoma kidato cha kwanza na cha pili kwa mwaka mmoja na kuendelea kwa mfumo huo kwa kidato cha tatu na nne. Akasajiliwa shuleni kwa jina la Mariam badala ya Mary.
Baada ya mwaka wa kwanza wa kuhitimu kidato cha kwanza na cha pili, mwaka uliofuata akaumalizia kwa kusoma kidato cha tatu na cha nne. Mary akapata cheti cha elimu iliyoishia kidato cha nne. Familia ya tajiri huyo ikamwondoa Mary kutoka kwenye utumishi wa kazi za ndani, nafasi yake ikachukuliwa na mtumishi mpya mwanamke wa kibantu asiye na nasaba nao.
Kwa kuwa alimaliza shule akiwa na matokeo mazuri, Mary akaomba ajiunge na Chuo cha Biashara, familia hiyo ikakubali kumlipia gharama za masomo yake.
Maisha ya Mary yalibadilika hatua kwa hatua. Akawa siyo yule Mary aliyeishi Lusanga, wala siyo yule aliyechukuliwa na kuzama kirahisi kwenye penzi la Nassoro. Alikuwa Mary mpya mwenye jina jipya la Mariam, lakini aliyebaki kwenye dini yake ya Ukristo ambayo kwa kipindi chote tokea ahamie kufanya kazi nyumbani kwa tajiri huyo, hakuwahi kwenda kanisani. Wasiomjua, wakaamini ni ndugu wa damu katika familia hiyo.
Jina la Mariam likamzoea, marafiki na wanafunzi wenzake wakamjua kwa jina hilo. Siku moja Hajra binti mkubwa wa mzee Alawiy akamshawishi Mary abadili dini aingie kwenye Uislamu, naye kwa wepesi Mary akajibu, “Kama siuoni umuhimu wa kwenda kanisani, kwa nini nijiingize kwenye mzigo mwingine?”
Jibu hilo likamfanya Hajra asizungumzie tena ushawishi wa kutaka kumbadilisha dini Mary!
Mary alikiri moyoni maisha yake yamepitia katika bahati asiyoitarajia. Kuna kipindi alikuwa akikaa na kuzikumbuka shida na dhiki alizokumbana nazo wakati akiishi Lusanga. Yalikuwa ni maisha tofauti na anayoishi sasa. Maisha aliyokuwa akiishi Lusanga yalimfanya ayaangalie maisha ya kifahari kama kitu kigeni, na wala kutoyajua ni kitu gani. Lakini mabadiliko yaliyomkumba, aliyaona kama ndoto iliyomjia usingizini, akaota ana maisha mazuri, akajikuta akiamka akiishi ndani ya maisha yaliyozungukwa na raha za kifahari! Ni maisha yaliyomtengeneza, akitoka hatua hii kwenda nyingine. Yakamuweka kwenye sifa ya kutukuzwa uzuri wake wenye asili, uliojitokeza na kuchanua kama waridi, uzuri ambao sasa unamuweka kwenye kero za kutakiwa kimapenzi na wanaume wenye madaraja ya juu kimaisha!
Alipewa sifa ya ugumu, kuwakataa wanaume! Baadhi ya wanaume walianza kuhofu alikuwa na kasoro kwenye mwili wake, ikaonekana ndiyo sababu ya kuwaogopa wanaume ili wasiione. Vinginevyo, asingewakataa wanaume wenye nafasi zao kimaisha, ilhali pacha wa mwanamke mzuri ni mwanamume mwenye pesa!
Ni kweli alikuwa na kasoro! Lakini haikuwa ile iliyowekewa dhana kwenye mwili wake. Kasoro ilikuwa ipo kwenye fikra zake ambako ndiko kulikokuwa na kovu lililomwathiri kisaikolojia. Kovu lililowekwa na Nassoro ndani ya saa chache la penzi lao! Nassoro ndiye mwasisi aliyemtengeneza asiwapende wanaume. Kila mwanamume alimwangalia kwa mfano huo akimfananisha na nyoka, kuwaona wote wana sumu ileile! Hakuwaamini, kwa hiyo hakuwa na haraka nao!
Wengi walimfuata wakiwa na vishawishi tofauti, lakini havikuonekana kuuyumbisha msimamo wake! Wanaume waliokuwa wakimfuata waliweza kumpa uzoefu wa kuwazoea kwa kuzungumza na kucheka nao, lakini hatimaye akawa anawakataa huku akitabasamu. Baadhi yao wakamwita, Smiling killer. Akiwa kwenye msimamo huo aliouamini kwamba tayari anao, ndipo kirusi kisichotarajiwa kikachomoza na kuanza kuwa jinamizi kwake!
Mtoto wa kiume wa mzee Alawiy!
****KAMA UNADHANI HADITHI INAELEKEA MWISHO, UMEKOSEA! NDO KWAAANZA INAANZA; NI TAMU NA YENYE KUSISIMUA MNO. KUISOMA YOTE PAKUA APP YA UWAIDI (UWARIDI APP) UBURUDIKE NA KUELIMIKA.

Ndugu zangu nimepewa ruhusa ya kuleta sehemu tano pekee
Samahani kwa usumbufu wowote
Nijatihidi kuleta riwaya itakayofika hadi mwisho
 
riwaya tamu yenye kufunza na kusisimua japo pia inahuzunisha
beka mfaume umedhihirisha pasipo shaka namna ulivyo nguli katika uandishi
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom