Kanungila Karim
JF-Expert Member
- Apr 29, 2016
- 20,746
- 25,637
- Thread starter
- #21
RIWAYA: KIROBA CHEUSI
MTUNZI: LAURA PETTIE
SEHEMU YA TANO.......
ILIPOISHIA:
Aliliona bwawa la mikakati yao likinyemelewa na ruba.
Alihamanika. Alipepesa macho kutazama kule alikotoka. Pamoja na kuwepo kwa mwanga wa taa toka nyumba hii na ile. Bado giza dogo lililokuwepo katikati ya barabara hii iliyokuwa kimya, lilimchezesha kwata. Ujasiri wa kurudi alikotoka ulichanja mbuga na kutokomea.
Sasa?
INAENDELEA:
4
MORENA alikata shauri kusonga mbele. Kwa wahaka aliokuwa nao, asingeweza kurudi pale alipokuwa amesimama mwanzo. Aliangaza akizitazama zile njia nne kwa awamu. Kibaridi cha usiku nacho kilimpuliza na kuiparaza ngozi mpaka utumbo. Kuna majuto yalipita haraka kichwani mwake, yalipita kwa kasi mno kiasi cha kumtaja Mungu na asimweleze alilotaka amfanyie.
Akaamua tu kukamata njia iliyokuwa mbele yake, akiwa amejikumbatia, mkono wa kulia ukiwa na viatu vyake huku ule wa kushoto ukiwa na simu yake. Akaivuka njia panda, akiwa yeye na kivuli chake. Alitembea tu na asijue aendako.
Si kwamba hakuzoea kuwa nje usiku kama huu. La hasha! Katika mikikimikiki yake ya kujiuza alikwishazunguka nje usiku mnene zaidi ya huu.
Vingunguti, Buguruni, Yombo ama Kariakoo hii saa saba kasorobo usiku, pilika pilika za hapa na pale zingetosha kumfanya akae mahali aagize hata mchemsho wa miguu ya kuku kusukumia wasaa. Ila huu mtaa alioibukia ulikuwa kimya mno, kimya kupitiliza.
Hatua kadhaa mbele akamwona mtu kwenye moja ya mageti yaliyokuwa mbele yake. Kwa haraka haraka akahisi ni mlinzi. Mkombozi!
Alimkimbilia. Akasimama mbele yake wakati mlinzi yule naye akiacha kuingia ndani na kusimama kizingitini. Alimtazama Morena juu chini.
“Kaka yangu n’na shida!” Alianza kujieleza.
Ile hali ya kuhema ilifanya mabega yake yapande na kushuka kiasi cha kuonekana wazi kuwa alikuwa katika hali ya taharuki. Yule mwanaume getini, alimtazama Morena kwa mashaka kisha akatazama kule alikotokea. Ni dhahiri alitaka kuhakiki kwanza kama Morena alikuwa yu mtu mwema, ama pengine kujiridhisha kuwa hakuwa ameongozana na mtu mwingine yeyote.
Morena alimeza mate kwa taabu akiwa kimya. Huenda aliomba dua amri ya kuendelea kujieleza itoke na kumhakikishia usalama wake. Yule mwanaume akamkunjia uso.
“Shida gani?” Alisaili kwa sauti kali. Alifunga geti, akasimama kumwelekea bibie.
Morena aliomba hifadhi ya muda hata pale ndani ya geti ili aweze kuwasiliana na ndugu yake kwa usalama.
Yule mwanaume hakumwelewa. Alimtandika maswali ya haraka haraka ambayo Morena alijitahidi kuyajibu ili tu apate hifadhi aliyoihitaji. Uongo na ukweli vikichanganywa kuitafuta huruma. Akaipata.
Alipopewa stuli ili aketi hapo getini kwa ndani, Morena alipata amani ya kumpigia simu Fatumata. Ghadhabu na hofu vilikumbatiana wakati akisubiri simu yake ipokelewe.
Simu iliita hadi kukatika. Aliitoa sikioni. Akaitazama kwa hasira.
Yule mwanaume alimtazama kana kwamba alitaka kuthibitisha kuwa Morena hakuwa mwongo. Akaipiga tena simu ya Fatumata safari hii akimwomba Mungu simu ipokelewe. Ikaita kwa sekunde tatu nne.
Kimya!
Alisubiri kidogo tena.
Kimya!
Alihisi ile ilikuwa siku ya kufa nyani, kila mti pruuu mpaka maka. Akainua macho. Alimtazama yule mlinzi, ambaye naye alikuwa anamtazama kwa umakini.
“Hapokei simu!” Alitamka kwa huzuni akinyanyua mabega juu na kuyashusha.
“Sasa?” Mlinzi alimtupia swali kwa sauti ya kuhimiza jibu.
Morena akatapatapa. Kwa nini? Hakuwa na pesa yoyote ya maana zaidi ya shilingi elfu mbili alizokuwa amezitia kwenye sidiria. Makubaliano yao yalikuwa teksi ije impitie pale alipokuwa akiisubiri mwanzo kisha impeleke huko pa kusubiria kuuchukua mzigo halafu imrudishe nyumbani. Si hivi mambo yalivyoonekana kuparaganyika ghafla!
Hasira zilimshika maradufu. Hakuwa na namba ya Daudi Chochoro ambaye pengine angemsaidia kujua kinachoendelea. Akahisi kudhalilika na kusumbuka kwa tamaa ya pesa za haraka. Wakati akiwaza cha kumjibu yule mlinzi. Simu yake ikaita, alikuwa Fatumata.
Moyo ukafunguka haraka, hata kabla ya mwito wa simu ile kuchanganyia akaipokea.
“Mpuuzi wewe na huyo Uchochoro wako!” Alisonya. “Hivi mnadhani mie kipande cha mti kukaa hapa nawangojea kiama na msiniambie mko wapi?”
Morena hakuwa na muda wa kumsikiliza Fatumata aliyekuwa akiongea wakati Morena akigomba. “Mie mgeni huku halafu hamnambii kinachoendelea mkitegemea nini? Nimekoswa koswa kisu cha utumbo we’ unalalana tu uko…”
Alisonya msonyo mrefu zaidi wa kilo za kutosha kiasi cha kumfanya mlinzi atabasamu.
“Sipajui hapa… niendeje?... Mwenzangu mwisho usiku huu nitokezee Matombo Morogoro bure kwa kukatiza katiza… Kwa hiyo?” Morena aliuliza akiinama kidogo na kuanza kuvaa viatu vyake. Ni kama vile sasa alipata suluhisho la namna ya kuondoka pale.
Alipomaliza kuongea na Fatumata, alinyanyuka. Alimshukuru yule mlinzi. Aliitoa ile elfu mbili yake aliyokuwa nayo. Alimpatia mlinzi. Kwa uungwana wake, mlinzi akaikataa akidai kumsitiri pale ilikuwa ihsani tu.
Huenda alishikwa na imani vile alivyoitoa hela pekee toka kwenye kitambaa kidogo kilichokuwa kwenye sidiria. Wakazungumza mawili matatu. Mlinzi akavunja kanuni za ulinzi. Alimsindikiza Morena mpaka karibu na ile njia panda. Dakika tatu tu, mwanga wa gari ukaonekana ukikata kona kuja eneo lile.
Morena akashukuru. Wakaagana.
“Unajua una mishe ya hatari halafu unachukua gari bovu, la kazi gani mzee?” Morena alinung’unika wakati akiingia kwenye teksi ya Daudi Chochoro baada ya kuelezwa sababu ya kuchelewa kwake.
Daudi alikuwa mtu mzima wa makamo. Mvi lukuki zilizompatia shikamoo nyingi za hiari. Huo utu uzima wake ndiyo uliopelekea Morena amfanyie staha ya kutomporomoshea maneno ya shombo. Vinginevyo, njia nzima angeipata pata.
Kwa ule umri wake, ilimpasa kuwa nyumbani akiogelea kwenye bahari ya usingizi wa raha. Tena, baada ya uchovu wa kucheza na wajukuu kutwa nzima. Lakini, uhalisia wa maisha ulimpiga ngwara matata sana. Nazo shida za dunia hii zikampora yote yampasayo.
Alikuwa barabarani usiku huu akitafuta senti za ziada. Senti za kupeleka mkono kinywani kwake na kwa familia yake kubwa ya wana na wajukuu. Familia iliyomtegemea yeye kwa kila kitu.
“Magari hayana muamana mwanangu!” Mzee Daudi alijitetea akitabasamu. Tabasamu lililovaa uchovu wa kutwa nzima. Mwendo wa gari ukaongezeka.
***Hii safari ya kukifuata Kiroba inazidi kuwa ndefu aisee!
MTUNZI: LAURA PETTIE
SEHEMU YA TANO.......
ILIPOISHIA:
Aliliona bwawa la mikakati yao likinyemelewa na ruba.
Alihamanika. Alipepesa macho kutazama kule alikotoka. Pamoja na kuwepo kwa mwanga wa taa toka nyumba hii na ile. Bado giza dogo lililokuwepo katikati ya barabara hii iliyokuwa kimya, lilimchezesha kwata. Ujasiri wa kurudi alikotoka ulichanja mbuga na kutokomea.
Sasa?
INAENDELEA:
4
MORENA alikata shauri kusonga mbele. Kwa wahaka aliokuwa nao, asingeweza kurudi pale alipokuwa amesimama mwanzo. Aliangaza akizitazama zile njia nne kwa awamu. Kibaridi cha usiku nacho kilimpuliza na kuiparaza ngozi mpaka utumbo. Kuna majuto yalipita haraka kichwani mwake, yalipita kwa kasi mno kiasi cha kumtaja Mungu na asimweleze alilotaka amfanyie.
Akaamua tu kukamata njia iliyokuwa mbele yake, akiwa amejikumbatia, mkono wa kulia ukiwa na viatu vyake huku ule wa kushoto ukiwa na simu yake. Akaivuka njia panda, akiwa yeye na kivuli chake. Alitembea tu na asijue aendako.
Si kwamba hakuzoea kuwa nje usiku kama huu. La hasha! Katika mikikimikiki yake ya kujiuza alikwishazunguka nje usiku mnene zaidi ya huu.
Vingunguti, Buguruni, Yombo ama Kariakoo hii saa saba kasorobo usiku, pilika pilika za hapa na pale zingetosha kumfanya akae mahali aagize hata mchemsho wa miguu ya kuku kusukumia wasaa. Ila huu mtaa alioibukia ulikuwa kimya mno, kimya kupitiliza.
Hatua kadhaa mbele akamwona mtu kwenye moja ya mageti yaliyokuwa mbele yake. Kwa haraka haraka akahisi ni mlinzi. Mkombozi!
Alimkimbilia. Akasimama mbele yake wakati mlinzi yule naye akiacha kuingia ndani na kusimama kizingitini. Alimtazama Morena juu chini.
“Kaka yangu n’na shida!” Alianza kujieleza.
Ile hali ya kuhema ilifanya mabega yake yapande na kushuka kiasi cha kuonekana wazi kuwa alikuwa katika hali ya taharuki. Yule mwanaume getini, alimtazama Morena kwa mashaka kisha akatazama kule alikotokea. Ni dhahiri alitaka kuhakiki kwanza kama Morena alikuwa yu mtu mwema, ama pengine kujiridhisha kuwa hakuwa ameongozana na mtu mwingine yeyote.
Morena alimeza mate kwa taabu akiwa kimya. Huenda aliomba dua amri ya kuendelea kujieleza itoke na kumhakikishia usalama wake. Yule mwanaume akamkunjia uso.
“Shida gani?” Alisaili kwa sauti kali. Alifunga geti, akasimama kumwelekea bibie.
Morena aliomba hifadhi ya muda hata pale ndani ya geti ili aweze kuwasiliana na ndugu yake kwa usalama.
Yule mwanaume hakumwelewa. Alimtandika maswali ya haraka haraka ambayo Morena alijitahidi kuyajibu ili tu apate hifadhi aliyoihitaji. Uongo na ukweli vikichanganywa kuitafuta huruma. Akaipata.
Alipopewa stuli ili aketi hapo getini kwa ndani, Morena alipata amani ya kumpigia simu Fatumata. Ghadhabu na hofu vilikumbatiana wakati akisubiri simu yake ipokelewe.
Simu iliita hadi kukatika. Aliitoa sikioni. Akaitazama kwa hasira.
Yule mwanaume alimtazama kana kwamba alitaka kuthibitisha kuwa Morena hakuwa mwongo. Akaipiga tena simu ya Fatumata safari hii akimwomba Mungu simu ipokelewe. Ikaita kwa sekunde tatu nne.
Kimya!
Alisubiri kidogo tena.
Kimya!
Alihisi ile ilikuwa siku ya kufa nyani, kila mti pruuu mpaka maka. Akainua macho. Alimtazama yule mlinzi, ambaye naye alikuwa anamtazama kwa umakini.
“Hapokei simu!” Alitamka kwa huzuni akinyanyua mabega juu na kuyashusha.
“Sasa?” Mlinzi alimtupia swali kwa sauti ya kuhimiza jibu.
Morena akatapatapa. Kwa nini? Hakuwa na pesa yoyote ya maana zaidi ya shilingi elfu mbili alizokuwa amezitia kwenye sidiria. Makubaliano yao yalikuwa teksi ije impitie pale alipokuwa akiisubiri mwanzo kisha impeleke huko pa kusubiria kuuchukua mzigo halafu imrudishe nyumbani. Si hivi mambo yalivyoonekana kuparaganyika ghafla!
Hasira zilimshika maradufu. Hakuwa na namba ya Daudi Chochoro ambaye pengine angemsaidia kujua kinachoendelea. Akahisi kudhalilika na kusumbuka kwa tamaa ya pesa za haraka. Wakati akiwaza cha kumjibu yule mlinzi. Simu yake ikaita, alikuwa Fatumata.
Moyo ukafunguka haraka, hata kabla ya mwito wa simu ile kuchanganyia akaipokea.
“Mpuuzi wewe na huyo Uchochoro wako!” Alisonya. “Hivi mnadhani mie kipande cha mti kukaa hapa nawangojea kiama na msiniambie mko wapi?”
Morena hakuwa na muda wa kumsikiliza Fatumata aliyekuwa akiongea wakati Morena akigomba. “Mie mgeni huku halafu hamnambii kinachoendelea mkitegemea nini? Nimekoswa koswa kisu cha utumbo we’ unalalana tu uko…”
Alisonya msonyo mrefu zaidi wa kilo za kutosha kiasi cha kumfanya mlinzi atabasamu.
“Sipajui hapa… niendeje?... Mwenzangu mwisho usiku huu nitokezee Matombo Morogoro bure kwa kukatiza katiza… Kwa hiyo?” Morena aliuliza akiinama kidogo na kuanza kuvaa viatu vyake. Ni kama vile sasa alipata suluhisho la namna ya kuondoka pale.
Alipomaliza kuongea na Fatumata, alinyanyuka. Alimshukuru yule mlinzi. Aliitoa ile elfu mbili yake aliyokuwa nayo. Alimpatia mlinzi. Kwa uungwana wake, mlinzi akaikataa akidai kumsitiri pale ilikuwa ihsani tu.
Huenda alishikwa na imani vile alivyoitoa hela pekee toka kwenye kitambaa kidogo kilichokuwa kwenye sidiria. Wakazungumza mawili matatu. Mlinzi akavunja kanuni za ulinzi. Alimsindikiza Morena mpaka karibu na ile njia panda. Dakika tatu tu, mwanga wa gari ukaonekana ukikata kona kuja eneo lile.
Morena akashukuru. Wakaagana.
“Unajua una mishe ya hatari halafu unachukua gari bovu, la kazi gani mzee?” Morena alinung’unika wakati akiingia kwenye teksi ya Daudi Chochoro baada ya kuelezwa sababu ya kuchelewa kwake.
Daudi alikuwa mtu mzima wa makamo. Mvi lukuki zilizompatia shikamoo nyingi za hiari. Huo utu uzima wake ndiyo uliopelekea Morena amfanyie staha ya kutomporomoshea maneno ya shombo. Vinginevyo, njia nzima angeipata pata.
Kwa ule umri wake, ilimpasa kuwa nyumbani akiogelea kwenye bahari ya usingizi wa raha. Tena, baada ya uchovu wa kucheza na wajukuu kutwa nzima. Lakini, uhalisia wa maisha ulimpiga ngwara matata sana. Nazo shida za dunia hii zikampora yote yampasayo.
Alikuwa barabarani usiku huu akitafuta senti za ziada. Senti za kupeleka mkono kinywani kwake na kwa familia yake kubwa ya wana na wajukuu. Familia iliyomtegemea yeye kwa kila kitu.
“Magari hayana muamana mwanangu!” Mzee Daudi alijitetea akitabasamu. Tabasamu lililovaa uchovu wa kutwa nzima. Mwendo wa gari ukaongezeka.
***Hii safari ya kukifuata Kiroba inazidi kuwa ndefu aisee!