Riwaya: Bondia

Riwaya: Bondia

RIWAYA: BONDIA
MTUNZI: HUSSEIN ISSA TUWA


SEHEMU YA MWISHOO


Kabla mwamuzi hajapitisha uamuzi, iwapo pambano liendelee au lisiendelee, Deus alijiengemeza kwenye kamba na kuziacha zimsukume mbele kwa kasi naye akaenda mzima mzima huku akiachia ukelele wa ghadhabu ilhali akimsukumia Roman konde la mkono wa kulia.
Roman alimuona Deus akimwendea na ngumi ya mkono wa kulia huku miguu ikimuishia nguvu, na ndipo aliporuka mbele haraka kumfuata yule mpinzani wake bazazi, mkono wake wa kushoto ukiwa juu kabisa hewani, kisha akaushusha na kuuzungusha kutokea chini na kumshindilia konde zito sana kwenye upande wa kichwa chake chini kidogo ya jicho lake la kulia.
Deus alienda chini kama mzigo, kinga ya meno iliyokuwa kinywani mwake ikimtoka na kusambaratika mpaka nje ya ulingo.
Roman alirudi nyuma na kusimama kwenye kona ya neutral, akiiacha kona yake, huku akimtazama mpinzani wake kwa makini. Deus alijiinua na kubaki akiwa amepiga magoti na ameshika sakafu kwa mikono yake, akajiinua wima, akayumba kulia na kushoto, kisha akaenda chini mzima mzima na kuanguka chali kwa kishindo.
Ukumbi ulilipuka kwa shangwe na hoi hoi zisizo kifani.
Roman alibaki akimtazama mpinzani wake akiwa ametulia chali pale sakafuni, damu ikimtoka puani na mdomoni. Mwamuzi alimsogelea Deus na kuanza kumhesabia na ilipofika tano bila ya Deus kutikisika, watazamaji nao wakawa wanahesabu pamoja naye.
"SITA...SABA...NANE...TISA...KUMIIIIII....!"
Ukumbi ulilipuka kwa hoi hoi na nderemo, jina la Roman likitamkwa kila kona ya ukumbi ule. Mwamuzi ulimuinua Roman mkono juu kumtangaza mshindi, na mara baada ya kufanya hivyo alimgeukia Deus aliyelala pale chini, kisha akawaashiria wahudumu walete machela.
Roman alibaki akiwa anatweta ilhali ameinua juu mkono wake wa kushoto kwa ishara ya ushindi huku akimtazama adui yake aliyelala pale chini. Machozi yalikuwa yakimtiririka na alikuwa akigeuka huku na huko kuwatafuta Dan, Mark na Kate, lakini kwa namna ya ajabu alikuwa hawaoni.
Sasa ulingo ulikuwa umevamiwa na baadhi ya watu wa kambi ya Deus walioenda kumtazama mtu wao aliyelala taabani pale chini. Kocha wake alimvua glovu na mikono yake ikabaki na zile bandeji mabondia wanazozifunga mikononi mwao kabla ya kuvaa glovu za kupigania.
Macho ya Roman yakaangukia kwa Inspekta Fatma aliyekuwa amepiga magoti nje ya ulingo huku akimtazama kwa fadhaa na masikitiko makubwa.
Walitazamana...
Huku nyuma Deus alijaribu kujiinua lakini alishindwa. Watu wachache walikuwa wamemzonga pale chini lakini bado akili yake iligoma kabisa kukubali kuwa alikuwa amebwagwa chini na Roman. Aligeuza uso wake uliomvimba na kumuona Roman akiranda kibabe pale ulingoni huku akiwa ameinua juu mkono wake, na ghadhabu zikamzonga. Alihisi maumivu yasiyo ya kawaida kichwani...ndani ya kichwa chake, na kwa mara ya kwanza akabaini kuwa amekuwa akisikia mvumo mzito masikioni mwake tangu alipojigundua kuwa alikuwa ameagushwa chini na Roman.
Ina maana huu ndio mwisho wangu kweli?
Alijisukuma na kuinuka kwa kujishikilia kwenye kamba za pale ulingoni na baadhi ya watu wake wakamsaidia kuinuka.
Nimevuliwa ubingwa na Roman!
"Tulia tu Deus, tulia. Pambano limeisha hili...tumeshindwa kaka!" Mmoja wa watu wa kambi yake alimwambia, bila ya kujua kuwa Deus hakuwa akisikia lolote zaidi ya ule mvumo mzito masikioni mwake.
Alijishikilia kwenye stuli iliyowekwa pale kwenye kona yake kwa ajili ya kupumzikia mwisho wa raundi, na hata pale alipojishikilia kwenye stuli ile, aliona tone la damu nzito kutoka puani kwake likiangukia pale kwenye ile stuli.
Yaani Roman ndio amenifanya hivi kweli?
Aligeuka kule alipokuwa Roman na kuona kuwa alikuwa hatua chache tu kutoka pale alipokuwa, akiwa amemgeuzia mgongo na amezibwa kidogo na watu. Kwa nguvu alizobakiwa nazo zilizosukumwa na ghadhabu ya hali ya juu aliikwapua ile stuli na kuwasukuma wale watu waliomkinga Roman huku akimwendea kwa hasira...
Roman alikuwa anaanza kuhamisha macho yake kutoka kwa Inspekta Fatma ili awasake akina Kate, wakati alipoona uso wa yule Inspekta ukibadilika na kuwa wa taharuki, macho yakimtumbuka na kinywa kikimtanuka bila ya sauti kumtoka. Pamoja na badiliko lile alilolishuhudia katika uso wa Inspekta Fatma alisikia sauti ya Kate ikiita kwa wahka kutoka nyuma yake.
"Roomaaaaaan!"
Wito wa Kate ulikuja nukta moja tu kabla ya ule wa Inspekta Fatma ambaye hapo naye alipiga ukelele wa hamaniko huku akimuoneshea kwa mkono wake nyuma yake.
"Angaliaaaaaaa!"
Haraka Roman aligeuka nyuma yake...
La Haula!
Alijikuta uso kwa uso na Deus aliyekuwa amefinyanga uso kwa ghadhabu huku akiwa ameinua juu ile stuli kwa mkono wake wa kulia, na aliona wazi kuwa ile stuli ilikuwa inamshukia kichwani...
Deus hakuwa akisikia mayowe ya watu waliokuwa wakipiga kelele kutahadharisha juu ya kile alichokuwa akikifanya, na aliishusha kwa nguvu sana ile stuli kichwani kwa Roman aliyekuwa ameegemea kamba pale ulingoni bila ya namna yoyote ya kujiokoa...
Kate, Dan na Mark Tonto waliokuwa upande wa pili wa ulingo waliachia vilio vya fadhaa huku wakishuhudia kiwetewete kilichokuwa kinatokea.
Bila ya kuhama hata kidogo kutoka pale alipokuwa amesimama, Roman alijipindua kutokea kiunoni kwenda juu na kulalia kulia kwake huku akiwa ameegemea kamba za ulingo, na pigo baya la Deus likakikosa kichwa chake na kumpunyua juu kidogo ya unyusi wake wa kushoto, na hapohapo, bila ya kufikiri wala kupanga, Roman akajigeuza kulalia kushoto huku sumbwi lake la kushoto likichomoka kwa nguvu yenye msukumo wa ajabu na kumshindilia Deus kwa upper cut nzito sana iliyojikita sawia chini ya kidevu na kumnyanyua hewani mzima mzima kabla ya kumbwaga tena sakafuni kama mgomba.
E Bwana we!
Ukumbi sasa ulilipuka kwa yowe moja kubwa la pamoja, ambalo halikuwa la kushangilia bali na la mshituko, au mastaajabu, au mshangao.
Kisha kimya kikatanda ukumbi mzima wakati Kate, Dan na Mark wakivamia ulingo na kwenda kumzingira Roman aliyebaki akiwa ameegemea kamba huku mikono yake ameiinua kibondia katika ile honour stance, tayari kuendelea na pambano kama lipo.
Kate alishindwa kujizuia na kumkumbatia Roman pale pale ulingoni. Roman naye akamkumbatia huku ukweli wa kile kilichotokea pale ukimfunukia wazi akilini mwake.
"Oh, Roman! Alitaka kukuua yule Roman!" Kate alibwabwaja, na Roman hakuwa na jibu, kwani alihisi donge kubwa likiwa limemkaba kooni.
Watu wengine pamoja na watoaji huduma ya kwanza walimkibilia Deus aliyekuwa amelala chali pale kwenye sakafu ya ulingo ule huku damu ikitambaa taratibu pale sakafuni kutokea sehemu kwenye kichwa chake. Wale watoa huduma ya kwanza waliweka machela kando ya Deus pale ulingoni na kumchunguza kwa muda, kisha mmoja akamgeukia mwamuzi kwa macho yaliyohamanika.
"Amekufa huyu refa!" Alisema kwa wahka mkubwa.
Mwamuzi alibaki akiwa amekodoa macho. Bado alikuwa hajaelewa kilichotokea, kwani yeye tayari alishamaliza pambano, na yale yaliyotokea baada ya kumalizika kwa lile pambano hakujua ayapokee vipi.
Roman aliisikia ile kauli ya yule mtoa huduma ya kwanza, na alifumba macho huku akimeza funda kubwa la mate kondoa lile donge lililomkaa kooni.
"Nimelipiza kifo chako Rachel...sasa unaweza kutulia kwa amani huko uliko mdogo wangu...rest in peace." Alinong'ona peke yake huku akiwa amemkumbatia Kate kwa mkono mmoja, ilhali kwa ule mwingine akiwa amenyoosha ngumi yake juu, jina lake likitajwa kwa shangwe kutoka kila kona ya ukumbi ule.
Rooman...Koooga!
Rooman...Kooogga!
Roooman...Kooogga...!
Hatua chahe pale ulingoni, Mark Tonto alikuwa akimtazama yule rafiki yake aliyetimiza azma aliyojiwekea tangu akiwa gerezani, na hakuweza kuzuia machozi kumtiririka. Moja kwa moja alikutana na macho ya Inspekta Fatma aliyekuwa akimtazama kwa macho yenye mchanganyiko wa fadhaa na kutoamini, naye akakwepesha macho yake na kujichanganya na akina Dihenga na Kate, pamoja na kundi la mashabiki waliovamia ulingo na kumbeba Roman juu juu.
Roman aliinua juu ngumi yake huku akibubujikwa na machozi.
"Nimelipiza kifo chako Rachel...nimelipiza mdogo wangu...kama nilivyokuahidi!" Alijisemea mwenyewe wakati akiushuhudia mwili wa bingwa wa zamani Deusdelity Macha akitolewa ulingoni ukiwa kwenye machela.
Saa moja baadaye dunia na umma wa watanzania walitangaziwa kuwa bondia Deusdelity Macha alifariki dunia akiwa ulingoni baada ya kupigwa na mpinzani wake wakati akitetea ubingwa wake wa dunia katika uzito wa Super Middle, dhidi ya bingwa mpya wa dunia wa uzito ule, Roman Kogga.


KIHITIMISHO


Upepo mwanana ulikuwa ukivuma na kupeperusha majani yaliyozagaa katika lile eneo la makaburi. Ilikuwa asubuhi tulivu na hali ya hewa ilikuwa ikitishia mvua, japo ki-jua chepesi cha asubuhi inayokimbilia kwenye mchana kilikuwa kikionekana. Hii iliwafanya wakaazi wa jiji la Dar kuongeza kasi ya mbio katika harakati zao za kimaisha kutimiza yaliyo muhimu kabla mvua haijaanguka na kuwavurugia mipango yao.
Kaburi lilikuwa limejengewa vizuri kwa marumaru ghali, na msalaba uliokuwa kwenye kichwa cha kaburi lile ulikuwa umesimama wima na imara, nao ukiwa umetengenezwa kwa marumaru. Kwenye kichwa cha kaburi lile, kibati cha shaba kilichojengewa pale kaburini na kuwekea kioo juu yake kilimnadi wazi yule marehemu aliyelala usingizi wa milele ndani ya kaburi lile.


Rachel Kogga
Dada uliyependwa kwa dhati.
Uliishi, ukadhulumiwa, ukalipiziwa.
Pumzika kwa amani.


Chini ya maneno yale, paliandikwa tarehe ambayo marehemu Rachel Kogga alizaliwa na ile ambayo aliiaga dunia .
Kate, Mark Tonto na Dan Dihenga walikuwa wamesimama nje ya gari la Dan walilokuja nalo pale makaburini wakimtazama Roman aliyekuwa amesimama mbele ya lile kaburi.
Alikuwa amevaa suruali ya jeans na viatu vya raba aina ya Reebok, ilhali jaketi ghali la kimazoezi lililoandikwa jina lake mgongoni likiwa limeificha fulana nyepesi nyeusi iliyomshika vizuri mwilini.
Hata pale walipokuwa wakiendelea kumtazama akiwa amesimama namna ile, akina Kate walimuona Roman akiichutama na kuweka shada jipya la maua juu ya lile kaburi.
Kwa pale alipokuwa, Roman alibaki akiwa amechutama mbele ya lile kaburi kwa muda akilitazama lile shada la maua aliloliweka juu ya lile kaburi la dada yake. Kaburi ambalo siku alipotoka gerezani alilikuta likiwa halijajengewa na limemong'onyoka ilhali msalaba uliokuwa kichwani kwa lile kaburi ukiwa umelalia upande.
Baada ya muda, alitabasamu kidogo.
"Okay dada yangu...najihisi kuwa kuwa sasa uko katika amani huko uliko...kwani nami najihisi amani ambayo sikuwa nayo kabisa hapo awali. Nimetimiza azma yangu dada...nimelipiza kifo chako." Aliongea kwa sauti ya chini.
Aliinuka na kubaki akiwa amesimama kama alivyokuwa hapo mwanzo, bado akilitazama lile kaburi.
"Pumzika salama dada yangu...pumzika mdogo wangu...wewe ndiye ulikuwa mrithi wangu pekee hapa duniani. Najua kuwa sasa haupo nami tena, na nimebaki peke yangu my sister, lakini usijali...nadhani sitakuwa hivyo kwa muda mrefu sana!" Alisema tena kwa sauti ya chini, kisha lile tabasamu likatanuka zaidi pale usoni kwake naye akageuka na kuanza kurudi kule kwa akina Kate waliokuwa wakimsubiri.
Hatua chache kabla ya kulifikia gari la Dan na wale wenzake alisita kidogo.
Kutokea upande wa pili wa barabara alimuona Inspekta Fatma akiteremka kutoka kwenye gari ambalo hakuwahi kuliona kabla, akiwa katika mavazi yake rasmi ya kiaskari hali usoni akiwa amebandika miwani yake ya jua, na ile kofia yake ya kiaskari akiwa ameifumbata kwapani.
Roman aliuma midomo na kuendelea na hatua zake. Akina Kate waliona jinsi alivyosita na wote wakageuka kule alipokuwa akitazama na ndipo walipomuona yule askari.
"Oh! Huyu naye! Hivi anamtakia nini Roman lakini?" Kate alilalama.
"Hana lolote la kumdhuru Roman...nadhani Romani atammudu tu..." Mark Tonto alisema wakati Inspekta Fatma akifika pale walipokuwana kuwasilimia.
Ni Dan pekee ndiye aliyeijibu salamu yake.
Lakini Fatma alikuwa ameelekeza macho yake kwa Roman aliyekuwa anafika eneo lile.
"Hongera kwa ushindi Roman...u-bingwa wa dunia sasa wewe...hongera kwa hilo." Alimwambia huku akimtazama moja kwa moja usoni.
Roman aliachia tabasamu la upande mmoja.
"Ahsante Fatma. Je, niko chini ya ulinzi kwa kuchukua ubingwa huo?" Roman alimjibu na kumuuliza.
"No, Roman. Hauko chini ya ulinzi na wala sikuja kwa shari..."
"Good to know that...je nawe una marehemu wako uliyekuja kumzuru hapa makaburini? Ajabu umechagua muda ambao na mimi nilikuwa nakuja kumzuru marehemu wangu hapa makaburini!" Roman alimwambia huku akimtazama.
Fatma alicheka kidogo, kisha akatoa miwani kutoka usoni kwake na kumtazama moja kwa moja usoni.
"Nahitaji kuongea nawe tena Roman..."
"Utaongea lolote ulitakalo kwangu mbele ya hawa wenzangu hapa Fatma, sina maongezi ya faragha nawe mimi!"
"Na hivyo ndivyo nilivyokuwa nataka. Sikujua nitawapata wapi, lakini nilidhani kuwa baada ya ushindi wako wa jana usiku, leo ungekuja huku...sikuwa nimekosea. Je tunaweza kwenda sehemu tukakaa na kuongea labda?" Fatma alisema na kuuliza.
"No, nadhani hapa panatosha Fatma, kwani sikuwa nimepanga kutumia muda mwingi sana kuongea nawe...ni nini utakacho?" Roman alimjibu kwa ukavu.
Fatma alitikisa kichwa kwa masikitiko na kutazama chini kwa muda, kisha akainua uso wake kuwatembezea wote pale macho yake.
"Very well! Ni kwamba nilitaka kukwambia mbele ya hawa wenzako kuwa usinichukie na kuniwekea kinyongo kwa namna nilivyokuwa najaribu kukusihi usiendelee na pambano lako na Deus..." Fatma alianza kujieleza, lakini hapo Roman alimkatisha.
"Marehemu Deus, unamaanisha!"
"Oh, yes..sawa...marehemu Deus." Fatma alikubaliana naye kwa mshangao, kwani aliona wazi kuwa Roman hakusikitishwa na kifo cha yule bondia mwenzanke, ingawa alijua kuwa alikuwa ni adui yake.
"Kwa hiyo ulikuwa unataka kuniambia nisikuwekee kinyongo...sawa. Sikuwekei kinyongo...kuna kingine?"
"Roman, sisi sote hapa twajua kuwa we' hukuingia kwenye hizi ndondi safari hii kwa ajili ya upenzi wako kwenye huu mchezo, bali uliona ndondi ndio njia pekee ya wewe kumuua Deus kwa makusudi bila ya kuchukuliwa hatua yoyote. Kwa hiyo mbele ya macho yangu wewe ulikuwa ni muuaji tu kama wengine Roman..."Fatma alimwambia, na Kate akaguna kisha akasonya kwa jazba, Roman akamuashiria atulie.
"Nyinyi nyote na nani afande? Mi sikujua lolote kuwa Roman alikuwa amedhamiria kumuua Deus ulingoni makusudi!" Mark Tonto alidakia.
"Hata mi sikujua!" Kate naye akadakia.
"Ah, hata mimi! Mi' nijuavyo ni kwamba mabondia wakishapanda ulingoni lolote linaweza kutokea! Angeweza kuwa ni Roman ndiye aliyeaga dunia pale ulingoni ile jana! Au sio? We' ulikuwa na garantii gani kuwa ni Roman ndiye angetoka mshindi na Deus ndiye ambaye angeaga dunia ile jana?" Dan anaye alimchachamalia Fatma, ambaye alitikisa kichwa kwa kukata tamaa.
"Isitoshe afande, kama ni hivyo mbona basi sijakamatwa na kupeleka gerezani kusubiri hukumu?" Roman naye alimuuliza huku uso wake akiufanya kuwa wa mtu asiyejua lolote kabisa hapa duniani.
Fatma alitabasamu.
"Najua kuwa huwezi kushitakiwa kwa hilo Roman, kwa kuwa mbele ya jamii inajulikana wazi kuwa Deus amekufa katika michezo, hivyo we' huna kosa, ila..."
"There you are! Kumbe unajua kuwa kifo cha kwenye michezo hakina hatia sasa ya nini kupotezeana muda, Fatma? Siye tuna safari zetu dada...can we go now?" Roman alidakia huku akimcheka yule afande.
Fatma aliuma meno kwa hasira.
"Lakini ukweli unabaki pale pale, Roman. Kuwa sote tunajua kuwa wewe ulikuwa umedhamiria kumuua Deus ulingoni toka mwanzo! Na ni kutokana na kujua hilo ndio maana nilikuwa najaribu kukuzuia. Nilikuwa na mashaka kuwa ukisharuhusu chuki yako ikufanye uue, utakuwa mtu mwingine kabisa. Lakini sasa nimeona kuwa kumbe hilo halikupi taabu..." Alisema kwa uchungu.
"Halimpi taabu ndiyo. Sasa kwa nini wewe likupe taabu?" Kate alimjia juu. Fatma alimtazama na akatamani amtandike makofi, lakini akaona atapoteza lengo la ujio wake pale.
"Okay sio ishu. Nilitaka kuja kuweka wazi sababu za mimi kujaribu kumzuia Roman wakati ule, basi. Kama nimeeleweka basi mi' itanitosha!" Alisema kuwa hasira.
"Haya umeeleweka bibie...unaweza kwenda sasa!" Kate alimjibu kwa jazba. Fatma alimtazama tena kwa macho makali. Akataka kumpa majibu yake, lakini akaghairi. Akamgeukia Roman, ambaye naye akampa yaliyo moyoni mwake.
"Hivi wewe ulishakaa ukajiuliza kuwa huenda Deus alidhamiria kutotoka hai bila ya mkanda ile jana, afande?" Alimchachamalia, na Fatma akapigwa butwaa.
"Kivipi? Kwamba alitaka umuue?"
"Wewe ulitupa taulo ulingoni ili kusimamisha pambano, sio? Yeye akalipiga teke na kulitupia nje, tena wakati nimeshampeleka chini kwa mara ya kwanza!. Hilo linakwambia nini, eenh?"
Fatma hakuwa na jibu, alibaki akimtazama kwa mastaajabu, na Roman akaendelea;
"Mimi nilimwambia aachane na mpambano ule wakati tuko pale ulingoni, wakati huo nimeshampeleka chini kwa mara ya pili...alinisikia? Hapana! Alitaka tu kuendelea wakati anajua wazi kuwa nina historia ya kuua watu ulingoni, kwa nini?"
Dah! Fatma alibaki amebutwaika.
"Okay Roman...lakini pamoja na yote hayo niliyosema hapo mwanzo, pia nilikuwa nimekuja kukutaka radhi kwa makwazo yote niliyokusababaishia, kwani pamoja na hiyo hisia yangu ya siku zote hizo dhidi yako, jana ilinithibitikia pale pambanoni kuwaDeus naye kwa namna moja au nyingine alijiletea kile kifo mwenyewe."
"Si ndicho ninachokwambia hapa, Inspekta?"
"Watu wote waliona kuwa Deus alikuwa ameamua kutumia stuli kukupiga nayo...wakati pambano rasmi lilikuwa limekwisha. Ulichokifanya hatimaye kinakuwa ni kuua bila kukusudia, au kwa kujitetea, au vyovyote iwavyo...lakini haiwi mauaji ya kukusudia tena. Na ndio maana nikaona nina wajibu wa kuja kukutaka radhi na... na kukutakia maisha mema nikiwa na matumain kuwa hilo halitakusumbua maishani."
"Mi nitakuwa okay tu Inspekta, usijali." Roman alimwambia kwa upole.
Kimya kilitanda kidogo, kisha Fatma akamuuliza.
"Sawa basi...kwa hiyo sasa umechukua ubingwa...itabidi uendelee kuutetea ulingoni huo. Utafanyaje?"
Roman alicheka.
"Nitaendelea kuutetea tu ulingoni, afande. Na natumai hutanibughudhi tena juu ya hili?" Alimwambia. Fatma alitikisa kichwa kwa kustaajabia jinsi Roman alivyolichukulia kirahisi lile swala.
"Okay Roman. Basi nakutakia kila la kheri, ingawa ningekuwa na amani zaidi iwapo ungeachana kabisa na mambo ya ndondi. Sipendi kuona watu wakiaga dunia ulingoni!" Fatma alimwambia huku akimpa mkono.
Roman alimtazama kwa muda bila ya kufanya bidii ya kuupokea ule mkono. Kisha akatabasamu.
"Labda nitafanya hivyo iwapo tu utachangia kwenye harusi yangu!" Alimwambia huku akiupokea ule mkono wa yule afande.
Fatma alitumbua macho kwa mshangao. Alimtazama Kate, na kumgeukia Roman, na kumgeukia tena Kate ambaye sasa alikuwa akitabasamu.
"Ah, Roman! Kama hilo ndio litakufanya uache ndondi, basi hata milioni moja n'tachangia ndugu yangu!" Alisema huku akicheka kwa furaha, na wote walicheka kwa sauti huku wakipeana mikono wa yule Inspekta mtata.




*




MWISHOOOO!!!!

Wahusika gani kwenye riwaya ungependa wawe marafiki halisi...!


ROMAN
davidson689 Toplady ram BPM Sangomwile Mamamercy jonnie_vincy mbalu byb sac mlyn VAN HEIST nrango mangimezamuuza ubuyu Jullie ZIgunga Mojaculbby mugaru
 
Kwa adhabu aliyoipata Deus iwe fundisho kwa wote wenye tabia kama yake. Adhabu aliyoipat inamtosha bazazi huyu.
Kimsingi nimemchukia hata sitakwenda kwenye mazishi yake japo nitahudhuria harusi ya Roman. Nasubiri kadi ya mchango tu.
Sasa Casuit turudi kwenye roho mkononi.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom