Riwaya - Balaa

SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA SABINI NA SABA

Walipoingia tu ndani ya chumba chake, Daniel Mwaseba alimkaribisha Tano kutoka kundi la Six Killers.

"Karibu sana rafiki yangu, haya sasa kwa hiyari yako naomba unambie unaitwa nani?"
"Kunileta hapa haimaanishi kwamba mimi ni mateka yako, eti kwamba nitakwambia chochote unachojisikia kuniuliza" kwa mara ya kwanza Tano alijibu huku mdomo wake akiubetua kijeuri kwenda juu.
"Hahaha kumbe nawe jeuri" Daniel Mwaseba alikuwa anacheka huku akimtazama kwa umakini Tano.

Ilikuwa ni kitendo bila kuchelewa, Daniel Mwaseba alirusha teke la haraka lililotua katika goti la Tano, goti lilelile lililojeruhiwa na daktari makini kabisa, Dokta Yusha. Tano alipiga ukelele mkali sana kutokana na maumivu aliyoyapata katika goti, kutokana na pigo lile la teke toka kwa Daniel Mwaseba.

"Sipendi kukutesa kijana, naomba unambie kila nitakachokuuliza" Daniel Mwaseba aliongea maneno hayo yakienda sambamba na ngumi mbili nzito zilizompata barabara Tano katika shavu lake la kulia. Ngumi hizo zilileta athari kwa Tano, Damu zilikuwa zinamchuruzika mdomoni.

"Utasema husemi?"
"Nitasema" Tano alijibu huku akitema rundo la damu.
"Safi sana kijana"
"Unaitwa nani?"
"Tano"
"Tano nani?"
"Tano wa Six killers"
"Sijakuelewa"
"Naitwa Tano wa Six killers"
"Six killers ndio nini?"

Tano alikaa kimya.
Daniel Mwaseba alipatwa na hasira juu ya ukimya wa Tano, alirusha ngumi ya nguvu iliyotua katikati ya mdomo wa Tano, ngumi iliyorudisha jibu, meno mawili ya Tano yalidondoka sakafuni.

"Six killers ndio nini?" Daniel aliuliza kwa ukali!

Tano aliona hana ujanja, ilimpasa afanye kitu ili aweze kujiokoa katika mdomo wa kifo! Kwa nguvu zake zote Tano alisimama. Ingawa alisikia maumivu makali kwenye goti lakini alisimama. Alirusha teke la nguvu lililomkosa Daniel Mwaseba kidogo sana. Bila wepesi wa Daniel Mwaseba kulikwepa teke lile angepata madhara makubwa sana.
Tano aliyebadirika na kuwa kama mzimu alirusha ngumi ya nguvu iliyompata Daniel Mwaseba katika bega la kushoto. Tano alikuwa amechachamaa, alikuwa anataka kufa na mtu. Daniel nae akajipanga vyema sasa...

ITAENDELEA MUNGU AKIPENDA
 
SIMULIZI: BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA SABINI NA NANE

Tano wa Six Killers alikwenda mzima mzima kumvaa Daniel Mwaseba. Daniel Mwaseba alimuona vizuri sana, alikuwa ameshajipanga vizuri kimapambano, Daniel alisogea pembeni kidogo, Tano alipita moja kwa moja kwa kasi kubwa sana na kwenda kuuvaa ukuta.
Ebwana ee!
Alijigonga vibaya sana usoni. Dakika hiyohiyo uso wa Tano ulivimba na kutoa kitu kiitwacho nundu katikati ya paji lake la uso! Tano alipata maumivu yasiyo na kifani, alitumia nguvu nyingi sana kwenda kumvaa Daniel Mwaseba.
Tano wa six killers hakuweza kustahamili maumivu aliyokuwa anayapata, alianguka chini mzimamzima.
Danielle Mwaseba hakumuonea huruma kabisa. Sasa angalau kidogo alishayajua madhara ya Tano. Hakutaka kumpa mwanya wa kufanya chochote. Alimfata kwa teke la nguvu palepale chini alikokuwa amelala. Teke la kiume lililotua barabara katika kifua cha Tano, Tano alitoa mguno hafifu wa maumivu na kuanza kutoa madonge mazito ya damu mdomoni.
"Nakufaa"
Tano alisema kwa sauti dhaifu, ama hakika alikuwa amepatikana hasa.
Daniel Mwaseba alimjibu, alimjibu kwa teke kali sana la uso. Daniel alikuwa na huruma sana kwa raia wema. Lakini kwa bahati mbaya hakuwa na huruma kabisa kwa wahalifu kama Tano.
Uso mzima wa Tano ulitapakaa damu. Tano alijikusanya pale chini, akijitahidi kuvuta pumzi zake za mwisho. Daniel Mwaseba aliinama pale chini alipokuwa amejipweteka Tano, alimshika koromea kwa mkono wake wa kulia. Tano macho yalimtoka pima!, Daniel Mwaseba alimkaba kiasi kwamba alishindwa hata kumeza mate, ama kumeza damu ambazo ndizo zilikuwepo mdomoni mwake.
"Six killers ni nini?" Daniel Mwaseba aliuliza kwa nguvu akiwa anaangaliana na Tano.
"Hata nisi-po-kwambia uta-ni-fanya n-ini, mi-mi ni mfu ta-ya-ri, nifa-nye utakacho si-kwa-mbii ki-tu"
Daniel Mwaseba akajua yule jamaa amegoma kusema. Alimwacha pale, akasogea kwenye kabati lililokuwa ukutani, akafungua na kutoa mkoba wake. Alitoa kamba za katani, kamba alizotumia kumfunga vizuri sana Tano miguuni na mikononi, hakutaka kumuua, alitaka kujua vitu kwanza toka kwa yule jamaa. Alimwacha kamfunga vizuri tano na kutoka nje ya kile chumba. Hakwenda mbali sana Daniel, alijibana sehemu akiangalia kitatokea nini pale mlangoni.
Kwa jinsi Tano alivyofungwa kamba zile na kwa hali aliyokuwa nayo, mimi na wewe tusingeweza kufungua zile kamba. Lakini Tano wa Six killers hakuwa mimi na wewe. Tano alikuwa nunda kweli. Tano alikuwa mjuaji, Tano alikuwa jambazi mahiri, Tano alikuwa mbabe, Tano alikuwa mtemi. Tano alikuwa sugu!

Daniel Mwaseba akiwa amejibanza katika mpenyo katika korido ya nyumba ile ya kulala wageni alishangaa kuuona mlango wa chumba chake ukifunguliwa na mtu kutokea ndani...

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA
 
Dah.... hapa nitarudi tar 10 itakua imesogeasogea kama sio kuisha.
 
SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU: 0757 633010

SEHEMU YA SABINI NA TISA

Daniel Mwaseba hakutegemea kabisa kitendo kile. Yeye alikuwa anategemea kama mlango ule utafunguliwa basi mtu atatokea nje, licha ya kumnyang'anya bastola yule jamaa lakini hakumnyang'anya simu. Alimuachia simu makusudi ili awapigie simu watu wake, ili Daniel aweze kuwafahamu ama kuwakamata. Kumuacha na simu ulikuwa mtego. Lakini Daniel Mwaseba hakutegemea kabisa kama mtu aliyemwacha mle ndani ataweza kufungua mlango ule. Kwanza alimwacha akiwa amemchakaza kisawasawa, pili alimwacha kamfunga kamba barabara mikononi na miguuni pia ule mlango aliufunga kwa funguo. Cha kushangaza pamoja na yote hayo Tano alikuwa anafungua mlango, ila kwa bahati mbaya mlango ulikuwa ukishuhudiwa na macho mawili ya Daniel Mwaseba.

Kwa mwendo wa taratibu Daniel alisogea hadi pale mlangoni. Tano alivyomaliza tu kufungua mlango alikutana na Daniel Mwaseba! Wakawa wanatazama na macho kwa macho.

"Wewe ni shujaa, umeweza kufungua huu mlango ukiwa katika hali hiyo"

Tano hakusema kitu, alikuwa anamwangalia Daniel kwa jicho la chuki.
Ghafla, Daniel alirusha guu lake lililompata Tano tumboni na kumrudisha mle ndani. Tano alianguka chali sakafuni huku akitoa tusi kubwa la nguoni. Lakini tusi lile haikusaidia kitu. Daniel Mwaseba aliruka juu hewani, na kuwa anashuka chini kwa miguu yake yote miwili. Tano alifumbua macho kwa nguvu akiwa pale chini, kwa uoni wake hafifu uliotokana na uso kujaa damu hadi kwenye macho, alimuona Daniel Mwaseba akiwa angani, akiteremka pale alipolala, akajua lile ni pigo la kifo!
Na Tano hakuwa tayari kufa. Kwa nguvu zake za mwisho Tano alijisogeza pale chini ingawa kwa shida sana.

E bwana eeee!

Daniel Mwaseba alishuka chini kwa nguvu na kutua sakafuni! Alikuwa kamkosa Tano pale chini. Daniel Mwaseba alipata maumivu makali sana ya miguu.
Ilikuwa Balaa!
Daniel alikaa sakafuni akiugulia maumivu, huku Tano nae akiwa amelala pale chini. Wote wakiwa hoi kwa maumivu. Lakini cha kushangaza Tano wa Six killers ndiye alikuwa wa kwanza kuinuka pale chini....

ITAENDELEA MUNGU AKIPENDA
 
SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA THEMANINI

Tano alikuwa anaenda taratibu kumfata Daniel Mwaseba pale chini alipokuwa amelala. Ngoma sasa ilikuwa imemgeukia Daniel, tena imemgeukia kwa kasi sana! Tano alikuwa anatisha kama Nsyuka!
Tano Nsyuka alinyanyua guu lake baya la kulia juu, saizi ya kimo cha mbuzi akawa analirudisha kwa kasi kuelekea katika kifua cha mwanaume, Daniel Mwaseba, Tano Nsyuka alikuwa anautumia mguu uleule alioumia vibaya sana gotini. Labda Tano alishikwa na ganzi katika mguu ulipewa jeraha na Dokta Yusha, maana hakusikia kabisa maumivu ya ule mguu wake mbovu. Akiwa amelala pale chini Daniel Mwaseba aliuona vizuri sana mguu ule. Ulivyokuwa unashushwa, kwa kasi ya haraka alinyoosha mikono yake yote miwili na kuudaka mguu ule mbovu, Daniel Mwaseba aliuzungusha kwa nguvu zake zote. Mguu mbovu wa Tano uliteguka aisee!
Tano alianguka chini akigalagala na kulia mithili ya mtoto mdogo. Alikuwa anasikia maumivu yasiyo na mfano. Daniel Mwaseba akiwa na ghadhabu aliruka juu na kushuka chini, aliukanyaga tena mguu mbovu wa Tano palepale kwenye kifuti.
Tano alilia kilugha cha kwao....

"Six killers nd'o nini?" Tano alimwangalia Daniel Mwaseba kwa hasira sana. Alijitahidi kukusanya mate ya kutosha mdomoni, ingawa kwa shida lakini aliyapata. Aliyerusha mate yale yote yaliyokuwa yamechanganyika na damu! Yalitua katikati ya paji la Daniel Mwaseba. Mate yenye mchanganyiko wa damu mbaya! Kitendo kile cha kijeuri kilizidi kumuuzi Daniel Mwaseba. Sasa alipandwa na hasira mithili ya kifaru. Hakujiangaisha kabisa kuyafuta yale mate yenye damu ya Tano. Alirudisha kichwa chake nyuma, kwa nguvu zake zote alikipigisha kichwa chake katika kichwa cha Tano.
Kilikuwa kichwa kweli!
Kichwa kilichomwacha Tano akipiga kelele mithili ya mtu aliyefiwa na baba yake mzazi. Kichwa kilichomwacha Daniel Mwaseba akiwa nae katapakaa damu usoni. Damu alizozitoa toka katika sura ya Tano.

Ghafla! Mlango wa kile chumba ulifunguliwa kwa nguvu! Watu watatu kila mmoja akiwa na bunduki mkononi walikuwa wanawaoneshea midomo ya bunduki zao kwa Tano wa Six Killers na mpelelezi mahiri nchini Tanzania, Daniel Mwaseba!

Balaa!

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA
 
Ndo mana sipendi stori za hivi bora nisubiriage ifike mwisho
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…