Kauli nyingine za ajabu inabidi ziwekwe kwenye mzingo sahihi. Hii kusema "kazi ya kupambana na rushwa/wizi ni ya watu wote" inakuwa na maana tu pale serikali yenye vyombo na nyenzo za kutekeleza sheria inapofanya kazi yake. Kama serikali haina nia wala mpango wa kudhibiti rushwa, inabakia kuwa kauli ya kujikosha na kugawa lawama kwa umma wote. Hivi kuna mwananchi au kikundi binafsi cha wananchi kinachoweza kuchukua hatua ya kumkamata fisadi na kumpitisha kwenye mchakato wa mashtaka?
Majina ya wala rushwa yameshatajwa sana na mengine kwa ushahidi unaofikirisha. Ni juu ya serikali kutumia vyombo vyake rasmi kuchunguza, kuthibitisha madai na kuendesha mashtaka. Tunachoshuhudia ni kuzidi kusema "wataje basi" - mara ngapi?; "ni jukumu letu sote" - how? Halafu kwa nini serikali isubiri kutajiwa majina - tena kwa ushahidi unaotoka hukohuko serikalini? Bajeti za CID, PCCB, TISS, AG ni za kazi gani kama ni "kazi ya wote" bila kuainishwa?
Kwa upande mwingine wananchi wakiendesha harakati za kufichua ufisadi, serikali imekuwa mstari wa mbele kupambana na wanaoongoza na wanaoshiriki harakati hizo kuliko kuzishughulikia kama inavyotegemewa. Ikitokea vyombo vya dola vikatesa, kudhuru au kuua wanaoshiriki kufichua ufisadi au ikitokea watu wakapoteza ajira, nyadhfa kwa sababu hizo basi utasikia adha hizo zisingewakuta kama wasingekubali "kuponzwa" na walioongoza harakati. Haisemwi kwamba walikosea kufuatilia wizi/ufisadi huo; wala kwamba serikali na vyombo vya dola vimekiuka kanuni za utawala bora au haki za binadamu; bali, "ungetulia nyumbani kwako au ukakaa kimya kwenye dawati lako hayo yote yasingekukuta"! Kama huko sio kuendesha utawala wa kinafiki na hofu ni nini tena hapo.