Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,316
- 33,125
Aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu
Aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu (63), amedai mahakamani kuwa aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa (wakati huo ), Rais Jakaya Kikwete, alipotembelea nchini humo alifanya mazungumzo na mmiliki wa jengo la ubalozi kabla halijanunuliwa ambaye alimweleza kuwa ununuzi wake utakuwa na mikataba miwili kwa kuwa linauzwa kwa bei nafuu.
Mahalu anayekabiliwa na kesi ya kuisababishia serikali hasara ya Euro 2,065,827.60, alidai kuwa Kikwete alikagua jengo hilo na kuona kuwa linafaa kwa ajili ya ofisi ya ubalozi wa nchi hiyo ambapo alimuahidi mmiliki kufanya malipo ya awali kabla ya mwisho wa mwaka 2001.
Alitoa ushahidi wake mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi, Illivin Mgeta, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam.
Akiongozwa na wakili wa utetezi, Mabere Marando, alidai kuwa kulikuwa na nakala halisi mbili na mikataba ya ununuzi wa jengo hilo na kwamba kwa mujibu wa sheria za Italia, majengo yanayouzwa kwa bei nafuu yalikuwa na mikataba miwili. Alidai kuwa Desemba, 2001, Rais Kikwete alikwenda na alikutana naye pamoja na mmiliki wa jengo hilo.
Kabla Kikwete hajafanya mazungumzo na mmiliki wa jengo hilo, mtoto wa mwanamke huyo Albelto alimzungusha waziri kwenye jengo hilo ambapo alikiri kwamba ni zuri na linafaa kwa ajili ya ofisi za ubalozi.
Katika mazungumzo hayo, Kikwete alimuuliza mmiliki kwa sababu gani kuna mikataba miwili ya ununuzi wa jengo hilo ambapo alijibiwa kuwa ni sheria za nchi hiyo kwa majengo yanayouzwa kwa bei nafuu lazima kuwe na mikataba miwili, alidai Mahalu.
Aliongeza: Waziri alivyofafanuliwa hivyo, alicheka na alimuahidi kwamba atahakikisha malipo ya awali yanafanyika kabla ya mwisho wa mwaka 2001, nilimsikia akimpigia simu Katibu Mkuu wa wizara hiyo akimuagiza atume pesa kwa ajili ya malipo ya awali na papo hapo alinitaka nitakapopata fedha hizo nifanye malipo ya awali mara moja kabla halijanunuliwa na mtu mwingine, alidai Mahalu.
Awali akiongozwa na wakili wa utetezi, Alex Mgongolwa, Mahalu alidai kuwa alifanya mawasiliano kwa njia ya barua na Katibu Mkuu wa Wizara akimjulisha kupatikana majengo matano kwa ajili ofisi za ubalozi wa Tanzania nchini humo.
Hata hivyo, Juni 11, mwaka 2001 alipokea barua kutoka kwa ofisa wa wizara ya Utumishi S. Mlay kwa niaba ya Katibu Mkuu ikimweleza kuwa wizara iko tayari kutuma mthamini wa majengo mara atakapofanikiwa kupata jengo linalofaa.
Aidha, Juni 28, mwaka 2001 alimuandikia barua Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje akimweleza kuhusu kupatikana kwa majengo matano. Julai 2, mwaka 2001 alipokea barua pepe kutoka kwa Mlay kwa niaba ya wizara ikimtaka kuwasilisha gharama za ununuzi wa majengo nilikamilisha taratibu zote za ununuzi ikiwemo na kuomba msamaha wa kodi katika ununuzi huo. Kesi hiyo inaendelea kusikilizwa utetezi wa Mahalu leo.
CHANZO: NIPASHE