hivi polisi kazi yao kutoa kibali au kutoa ulinzi katika mikutano nadhani hapa kuna umbumbumbu wa uelewa!
Sheria ya Vyama Vingi inaruhusu viongozi wa vyama vilivyosajiliwa kufanya mikutano na wananchi. Havihitaji kibali cha Polisi, bali chini ya Kanuni zilizotungwa kwa mujibu wa Sheria ya Polisi, Polisi wanahitaji taarifa ya masaa 48 kabla ya mkutano wa hadhara, ili waweza kuleta ulinzi mahali panapofanyika mkutano. Nasema haya kwa uhakika kutokana na uzoefu wangu, na nikiwa ni Muasisi wa Chadema.
Inaonekana sasa Polisi wanaegemea "taarifa za ki-intelligensia" ili kuzuiya vyama vya upinzani visifanye mikutano: eti taarifa zinaashiria kutakuwa vurugu na uvunjifu wa amani. Hivi hawa Polisi wataibeba CCM mpaka lini? Hata wao wenyewe wanaweza kufanya fujo na kuanza vurugu mahali mkutano unapofanyika ili kuthibitisha kwamba taarifa zao za "intelligensia" zilikuwa sahihi! Tunaanza kutoa sababu za kipuuzi sana!
Ningetaka kushauri serikali ya Jakaya Kikwete ipime kwa makini zaidi maono na maslahi ya Watanzania wa leo. Wengi wameonyesha kuchoshwa na mienendo ya viongozi wengi wa CCM na Serikali. Hawa viongozi hawahitaji ushahidi zaidi ya jinsi kura zilivyopigwa wakati wa Uchaguzi Mkuu huu uliopita. Watanzania wamechoka na uongozi wa CCM. Wanataka mabadiliko.
Nimefarijika kidogo kuona juzi kwamba hata Waziri Mkuu amekubali hoja yetu kwamba Katiba ya Tanzania inahitaji tathmini ya kina. Kama ni hivyo, basi ni vema umma ukaanza mapema kujadili hadharani mambo yanayopaswa kuzingatiwa katika mjadala wa marekebesho ya Katiba. Hayo ndiyo madhumuni ya msingi ya mikutano mingi ya Chadema inayoandaliwa sasa. Viongozi kama IGP Mwema aandae maofisa wake ili waone vyama vya upinzani vinaongozwa na Watanzania wanaojali maslahi ya taifa pia.
Hivi visingizio vya taarifa za kiintellijensia za uvunjifu wa amani na vurugu vikome. Elimu ya Uraia mwema itolewe kwa Polisi na watumishi wengine wa serikali, kwamba Upinzani wa kidemokrasia utaboresha maendeleo ya nchi kwa faida ya vijana wa Polisi na watu wote wa Tanzania. Hilo lieleweke hasa kwa Polisi.