Penzi lililo sababisha umauti

Penzi lililo sababisha umauti

Madame S

JF-Expert Member
Joined
Mar 4, 2015
Posts
17,190
Reaction score
34,526
JUMA HIZA
PENZI LILILOSABABISHA MAUTI-01
Based on True Story.
0712988278

Niliamua kufunga pingu za maisha na Julieth kwasababu alikuwa ni mwanamke niliyempenda sana. Alikidhi kila aina ya vigezo ambavyo nilikuwa nikivihitaji kwa mwanamke hasa yule ambaye nilitarajia kufunga naye pingu za maisha.
Nakumbuka alivumilia mambo mengi sana, wakati wa mateso, huzuni na hata wakati mwingine wa furaha bado alikuwa na mimi. Sikutaka kumpoteza katika maisha yangu nilihakikisha naitimza ahadi yangu niliyomuahidi ya kumuoa.
Julieth alijaaliwa uzuri wa sura ya kitoto, macho makubwa legevu ya kurembuwa, umbo namba nane lililokuwa linawapagawisha wanaume wengi waliyokuwa wakimtazama kwa macho ya matamanio.
Nilikuwa nikipata kesi lukuki za wanaume ambao walikuwa wakimsumbua lakini wote hawakuweza kupata nafasi. Julieth alikuwa akinipenda sana, hakutaka kufanya kitu kibaya ambacho kingeweza kunigharimu maisha yangu. Alikuwa akizijali sana hisia zangu.
“Dominick mpenzi mimi siwezi kukusaliti nakupenda sana na ninakuahidi hutojutia kunipenda katika maisha yako,” yalikuwa ni maneno ya Julieth aliyokuwa akipenda kuniambia, wakati huo kichwa chake alikuwa amekilaza kifuani mwangu.
Nilizidi kumuamini sana Julieth na hii ndiyo sababu iliyonipelekea mpaka nikaamua kumkabidhi dhamana ya moyo wangu, moyo ambao sikumbuki kama uliwahi kupenda hapo kabla. Ilikuwa ndiyo mara yangu ya kwanza kupenda na niliangukia mikononi mwa Julieth, mwanamke niliyekuwa nikimfananisha na kito cha thamani ambacho niliahidi kukitunza mpaka pale mwisho wa pumzi zangu utakapofika. Nilimpenda sana Julieth Mushi.
Ingawa maneno ya Mama yangu, ndugu na marafiki hayakuwa mbali kipindi ambacho nilikuwa nataka kumuoa Julieth lakini hayakufanya niache kufanya kile ambacho nilidhamiria kwa wakati ule, kwa kuwa niliamini sisi ndiyo tulikuwa tumependana kwa dhati itokayo moyoni basi maneno ya watu hayakuweza kusitisha kile tulichokuwa tumepanga.
Kazi yangu ya ufundi wa simu niliyokuwa nikiifanya katika ofisi yangu ndogo iliyokuwepo mtaa wa Kariakoo ukijumlisha na Julieth ambaye hakuwa na kazi yoyote ilichangia kuzalisha maneno mengi kila kukicha, wengi wao hawakutaka kuamini kama kweli nilikuwa naoa tena nilikuwa naenda kumuoa mwanamke ambaye hakuwa amesoma wala hakuwa na kazi yoyote, katika maisha yake ya kielimu alibahatika kusoma mpaka darasa la saba tu!. Ugumu wa maisha ndiyo uliyochangia Julieth kutoendelea na elimu yake ya sekondari, wazazi wake hawakuwa na uwezo wa kuendelea kumsomesha. Huo ndiyo ulikuwa mwisho wa elimu yake. Hakika nilichekwa sana, nilitukanwa kila aina ya tusi lakini katu sikutaka kuwasikiliza, nilisimamia katika kile nilichokuwa nakiamini.
“Nakupenda sana Julieth wangu,” nilimwambia Julieth huku nikimtazama kwa macho ya huba, alionekana kuwa mpole sana.
“Sawa unanipenda Dominick lakini Mama yako anaonekana kutonipenda, utawezaje kuishi na mimi?” aliniuliza Julieth swali lililokuwa na maana kubwa sana, ni kweli mama yangu alionekana kutompenda lakini sikutaka hilo liendelee kuwa tatizo litakalosababisha kuvunjika kwa uhusiano wetu.
“Julieth mimi ndiyo niliyokupenda Mama yangu asiwe kikwazo cha kukufanya utokwe na imani ya mapenzi yangu,” nilimwambia.
“Hata kama Dominick lakini nitawezaje kuishi na Mama yako na wakati hanipendi?”
“Julieth mpenzi wangu naomba uniamini kuwa nakupenda kwa dhati wala usiwe na wasiwasi wowote kuhusu Mama yangu usijali nitaongea naye na kila kitu kitakuwa sawa” nilimwambia maneno ambayo yalionekana kumuingia vyema, alikuwa ni muelewa sana.
****
Maneno ya Mama yangu bado yaliendelea kuwa tatizo katika mapenzi yangu kila siku nilikuwa nikigombana na Mama yangu kuhusu Julieth mwanamke ambaye alionekana kuwa takataka, hakuwa na kazi yoyote hivyo kila kitu kwake kilionekana kuwa kibaya. Mama yangu alikuwa akimsema sana Julieth, alinidharau kwa maamuzi ambayo nilikuwa nimeyachukua.
“Dominick mwanangu hivi una akili kweli wewe, utaendaje kumuoa mwanamke ambaye hana kazi wala nini” aliniambia Mama yangu huku akionekana kukasirishwa na kitendo nilichokuwa nimekifanya.
“Lakini mama nampenda sana,” nilimjibu huku nikimtazama usoni, alionekana kuwa na hasira mno.
“Utampendaje mwanamke ambaye hana mbele wala nyuma. Mwanangu wewe mwenyewe embu angalia kazi unayoifanya halafu bado unaenda kuoa mwanamke ambaye hana maisha hivi unafikiri maisha yako yatakuwaje?” aliniuliza Mama.
“Mama mapenzi hayaangalii kazi nzuri wala maisha mazuri bali moyo ndiyo unaopenda na moyo ukipenda kamwe huwezi kuukataza uache kupenda,” nilimjibu huku nikiwa nimeyaelekeza macho yangu chini, sikutaka kumtazama Mama yangu usoni. Nilimuonea haya.
“Ati! nini! Unasamaje Dominick? Mimi na marehemu Baba yako hatukupendana kama unavyosema bali ni wazazi wetu waliamua kutuchagulia na kwa wakati ule Baba yako alikuwa na maisha mazuri tu! Sasa huo unaouita moyo hapa sijui ni moyo wa aina gani?”
“Mama ni moyo wa mapenzi na ukishapenda umependa kweli wala huwezi kuubadilisha. Nampenda sana Julieth na yeye ndiye mwanamke wa ndoto zangu,” nilimwambia.
Bado niliendelea kuushikilia msimamo wangu wa kumpenda Julieth mwanamke niliyekuwa nampenda kuliko kitu chochote kile wala siwezi kuficha kitu katika hilo.
Ingawa Mama yangu alionekana kutokukubaliana na mimi kumuoa Julieth lakini ilifikia kipindi akaamua kukubali hapa ni baada ya kuniona nimezidi kuwa kin’gang’anizi.
Hatimaye Dominick mimi niliyezaliwa miaka ishirini na Saba iliyopita nikaamua kufunga ndoa rasmi na Julieth na huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa kuhama maisha ya nyumbani, nikayaanza maisha mapya ya ndoa yangu. Maisha ambayo kiukweli mwanzo yalianza kama hadithi nzuri ya kimapenzi lakini kadri siku zilivyokuwa zikisonga mbele hadithi hiyo iliweza kubadilika na kuwa miongoni mwa hadithi za kutisha ambayo iliweza kuniacha na uadui mkubwa sana dhidi ya viumbe ambavyo vimefanya niishi maisha ya kutoitamani kesho yangu.
****
Nilikuwa nikiishi Magomeni mtaa wa Mwinyimkuu, nilifanikiwa kupanga nyumba yenye vyumba viwili. Maisha ya ndoa yalionekana kuwa mazuri sana, yalibadili mfumo mzima wa maisha yangu ukitofautisha na mfumo ule wa maisha tegemezi niliyokuwa nikiishi nyumbani kwetu Kimara kwa Mama Dominick.
Mke wangu Julieth alikuwa ni zaidi ya mke mwema kwangu, hakukuwa na tofauti yoyote katika maisha yetu ya ndoa, kila siku nilizidi kujifunza mambo mengi sana hususani yale ya ndoa.
Nilijifunza juu ya uvumilivu, upendo, upole na busara katika kufanya maamuzi. Vitu hivi ndiyo ngao ambayo niliitumia katika kuishi vizuri na ndoa yangu.
Japo kazi yangu ya ufundi simu haikuwa ikiniingizia kipato kikubwa lakini hiyo haikuwa sababu ya kunifanya nishindwe kuwa mwaminifu wa ndoa yangu, nilikuwa mwaminifu haswaa wala siongopi ninapoyasema haya. Nayamaamisha kutoka katika kitako cha moyo wangu.
Julieth alikuwa ndiye mshauri wangu, alikuwa akinishauri mambo mengi sana hata yale ambayo nilikuwa siyafahamu pia aliweza kunijuza. Alikuwa na kipaji cha kuniongoza vyema katika maisha yangu, hakupenda kuona naanguka kimaisha hivyo kila kitu kilichokuwa kikiendelea katika maisha yangu yeye alikuwa ndiye rubani wangu, alikuwa akiniongoza. Hakika elimu yake ya darasa la saba aliitumia katika dhana ya kipekee sana wala sikutaka kuamini.
“Mume wangu pole na kazi,” aliniambia Julieth wakati ambao nilikuwa nimerudi nyumbani, ilikuwa ni majira ya jioni.
“Asante sana mke wangu,” nilimwambia kisha kabla sijakaa kwenye kochi alinipokea kwa kumbato na kunivua begi lililokuwa mgongo mwangu, lilikuwa ni begi lenye vifaa vyangu muhimu vya kazi.
Upendo ulitawala katika maisha yangu, nilihisi kupendwa sana na hii ndiyo sababu iliyopelekea nikazidi kuyasahau yale matusi na maneno ya kejeli niliyokuwa nikiambiwa na ndugu pamoja na marafiki zangu juu ya Julieth mke wangu, walikuwa wakimsema kuwa alikuwa ni mwanamke ambaye hakuwa amesoma.
Kwa upendo aliyokuwa akinionyesha Julieth kwa kweli nilimchukulia kuwa kama zaidi ya msomi, sikuhitaji msomi mwingine ukimtoa Julieth pambo la moyo wangu, furaha ya maisha yangu.
“Nakupenda sana Julieth wangu,” kinywa changu hakikuacha kumkumbusha maneno haya kila siku, ilikuwa ni desturi yangu. Haikuweza kupita siku bila kumsifia Julieth kutokana na uzuri aliyokuwa nao, nakumbuka kuna baadhi ya sifa nilikuwa nikiongezea chumvi. Hahaha! Ila wanasema yote haya ni mapenzi tu! mapenzi yanahitaji mambo mengi sana yanayoleta furaha ila chunga shubiri isije ingia katika mapenzi yako, utatamani dunia igeuke miguu juu kichwa chini, hutatamani kupenda tena.
“Wewe ndiye mwanamke wa maisha yangu, nakufananisha na kila kitu ninachokihitaji katika maisha yangu. Sijutii kukuchagua katika maisha yangu. Naomba utambue kuwa wewe ni zaidi ya kiungo muhimu katika mwili wangu,” nilimwambia maneno ambayo yalijawa na ushawishi wa utamu wa mapenzi ya dhati .
“Dominick nakupenda pia mume wangu,” aliniambia Julieth.
Maisha yetu yalitawaliwa na furaha sana, utamu wa maisha ya ndoa ukanifanya nisahau kabisa shida nilizokuwa nazo, nikazidi kunawiri japo maisha hayakuwa mazuri sana lakini kiupande wa pili wa sarafu wale waliokuwa wakinitazama walikiri kuwa hakika ndoa ilinipenda.
“Aisee Dominick umebadilika kabisa ndugu yangu,” aliniambia Chrispine rafiki yangu ambaye urafiki wetu ulikuwa kama ndugu, nilikuwa nikisaidiana naye mambo mengi sana, hata katika suala hili la mimi kumuoa Julieth alihakikisha anasimama kidedea mpaka nafanikiwa kumuoa. Alikuwa akifanya kazi katika duka la kuuza Compact Disk (Cd) Kariakoo.
“Ah! Wapi wewe acha mambo yako, huoni jinsi nilivyokondeana hivi?” nilimuuliza swali la kiutani huku kicheko kikishika hatamu yake, nilikuwa nikicheka kwa wakati huo.
“Sasa unacheka nini wakati nakwambia ukweli,” aliniambia Chrispine huku akinitazama, nikazidi kucheka sana.

Je, ni nini kitaendelea?
 
JUMA HIZA
PENZI LILILOSABABISHA MAUTI-02
Based on True Story.
0712988278

ILIPOISHIA......

“Ah! Wapi wewe acha mambo yako, huoni jinsi nilivyokondeana hivi?” nilimuuliza swali la kiutani huku kicheko kikishika hatamu yake, nilikuwa nikicheka kwa wakati huo.
“Sasa unacheka nini wakati nakwambia ukweli,” aliniambia Chrispine huku akinitazama, nikazidi kucheka sana.

SONGA NAYO.....

“Hahaha! Shemeji yako anafanya kazi yake bhana,” nilimwambia maneno ambayo yakamfanya atokwe na tabasamu pana.
“Naam! Hilo ndiyo neno ambalo nilikuwa nataka kulisikia kutoka kwako,” aliniambia.
“Hii ndiyo kazi ya shemeji yako.”
“Hata mimi naona ndugu yangu unapendeza tu!”
“Hahahaha!”
Kila neno alilokuwa akilizungumza Chrispine lilikuwa likinichekesha sana, nilizoea kuzungumza naye kwa utani.
Alipenda kuona nikiishi maisha mazuri ya ndoa yangu, hakupenda kuona nikinyanyasika na mapenzi naweza kusema alikuwa ni mtu ambaye alikuwa akinipa somo kubwa kuhusu maisha ya ndoa.
Katika maisha yake aliwahi kubahatika kuoa lakini kutokana na mkasa uliyowahi kumtokea hakuweza kuendelea kuishi na mke wake, waliachana.
Aliwafahamu sana wanawake, alifahamu kila kitu kuhusu wanawake na hata kipindi ambapo nilikuwa nikiambiwa na watu kuwa nimuache Julieth nikamuoe mwanamke mwingine hakuweza kukubaliana nalo.
Kwa maisha ya furaha ambayo alikuwa akiona nikiishi baada ya kuoa hakika alifurahi sana, sikumbuki kama kuna neno baya ambalo aliwahi kuniambia ila ninachokikumbuka mimi aliwahi kuniambia kuwa nimuheshimu sana mke wangu.
“Inabidi umuheshimu sana mke wako Dominick, usikubali hata siku moja katika maisha yako itokee ukamuudhi, utakuwa umefanya makosa makubwa sana, jitahidi atamani kuwa na wewe kila siku za uhai wake,” aliniambia Chrispine siku moja tulipokuwa kwenye mgahawa mmoja mtaa wa Kariakoo tukipata chakula cha mchana, alionekana kuwa na mengi sana ya kuniambia siku hiyo.
“Nimekuelewa sana ndugu yangu,” nilimwambia huku nikikitikisa kicha changu kumuonyesha kuwa nilimuelewa sana.
“Unajua wanawake ni viumbe wa ajabu sana, mimi napenda kuwaita sometime jua sometime mvua,” aliniambia maneno aliyoyafumba.
“Kwanini?” nilimuuliza.
“Hawatabiriki yani unaweza ukahisi ni jua kumbe ni mvua aisee,” aliniambia maneno ambayo yalikuwa na fumbo ndani yake, sikuweza kulifumbua kwa haraka, ikabidi nimuulize kuwa alikuwa na maana gani hasa, wakati huo alikuwa akicheka.
“Sasa hapo ni lipi usilolielewa Dominick?”
“Umesema jua mara mvua sijui unamaanisha nini?”
“Inabidi utumie akili nyingi sana kuishi na hawa viumbe aisee hawachelewi kukupa kovu la maisha,” aliniambia Chrispine huku akikipigapiga kijiko katika sahani, alikuwa akitabasamu, sikujua tabasamu lake lilimaanisha nini hasa, nikamuuliza tena.
“Kuna nini?”
“Mkeo anakupenda sana.”
“Ndiyo nalifahamu hilo.”
“Basi jitahidi kuishi naye vizuri ila usiombe wale waliyokutabiria mabaya yakakutokea kweli utahisi dunia imekuelemea.”
“Sawa nimekuelewa.”
“Mpende sana mkeo Dominick naamini wewe ni mpambanaji, pigania penzi lako, pigania ndoa yako usikubali kumpoteza mkeo kwa maneno ya ndugu na marafiki,” aliniambia kisha akanyamaza kidogo halafu akaendelea tena kuzungumza.
“Kuna kitu kimoja inabidi ujifunze,” aliniambia.
“Kitu gani hicho?” nilimuuliza.
“Ishi maisha ya kumpenda kila mtu,” aliniambia Chrispine.
Maneno ya Chrispine yalizidi kunijenga sana, yalikuwa yakiniimarisha vyema, nilisimama imara na ndoa yangu ambayo kila siku nilikuwa nikiifurahia.
Nakumbuka Mama yangu hakuwa akimpenda Julieth hata kidogo hapo awali lakini kupitia maneno na ushauri wa Chrispine niliweza kuutumia katika kumfanya Mama yangu akampenda Julieth, sikumbuki kama ni kweli alimpenda ama la lakini ninachokikumbuka alikuwa akimpenda, yale maneno mabaya aliyokuwa akiyasema kuhusu Julieth yalimuisha.
Ukurasa wa maisha ya ndoa yangu ulikuwa ni wa aina yake, tuliishi kwa upendo sana na mke wangu, alijivunia kuwa na mimi hata mimi pia nilijivunia kuwa na yeye maishani, alikuwa ni hakimu wa moyo wangu, kila kitu ambacho alikuwa akiamua nilikifuata bila kupinga, waliokuwa wakinitazama waliniambia kuwa nimelogwa. Sikutaka kuyapa nafasi maneno yao yatanitawale, nilichokuwa nikikitazama kwa wakati ule ni maisha mazuri yaliyogubikwa na amani niliyokuwa nikiishi na mke wangu.
“Siamini kama Mama yako amekubali kabisa mimi kuolewa na wewe,” aliniambia Julieth siku moja usiku tulipokuwa kitandani.
“Inabidi uamini sasa Mama yangu anakupenda sana,” nilimwambia huku nikimbusu katika paji la uso wake, alitabasamu kisha nikaitumia mikono yangu vyema katika kumpapasa mgongoni mwake, alikuwa na mwili laini sana uliyonisisimua kimapenzi.
“Furaha yangu sasa naweza kusema imerudi,” aliniambia Julieth kwa sauti ya chini, ilikuwa na utulivu wa aina yake.
“Kwani ilienda wapi?” nilimuuliza kiuchokozi, akatabasamu wakati huo nilikuwa nikiendelea kumpapasa.
“Umeshaanza vituko vyako,” aliniambia.
Haikuchukua dakika nyingi mwisho nikajikuta tayari nimeshazipandisha hisia za Julieth, alionekana kuweweseka kimapenzi, alikuwa akihangaika katika kifua changu. Sikumbuki ni nini kilitokea ila nilishangaa Julieth akiwa juu yangu tena akiwa uchi wa mnyama, kitendo kilichofuata hapo ilikuwa ni kufanya mapenzi usiku kucha.
Mchezo huo haukukoma tuliendelea kila siku, Julieth alinisifu kuwa katika maisha yake hakuwahi kumpata mwanaume ambaye alikuwa akimfikisha safari yake kama nilivyokuwa nikifanya mimi, hilo lilizidi kunifanya nijione kuwa hodari hasa katika mchezo ule ambao ndiyo kama silaha ya ndoa.
“Sitokuacha mume wangu kipenzi,” aliniambia Julieth siku moja tulipomaliza kufanya mapenzi.
“Hata mimi siwezi kukuacha wewe ndiyo hodari wa raha zangu,” nilimwambia.
“Naomba ujiheshimu sana mume wangu, jilinde siku hizi maradhi ni mengi sana,” aliniambia Julieth kwa sauti ya kipole, alikuwa akideka.
“Najiheshimu sana Mke wangu wala usiwe na mashaka katika hilo mumeo ni mwaminifu sana,” nilimwambia.
“Nitafurahi sana kama ni kweli hayo uyasemayo mume wangu.”
“Kama usiponiamini mimi ni nani mwingine ambaye utamuamini?” nilimuuliza.
“Nakuamini Mume wangu,” alinijibu.
“Nakupenda sana,” nilimwambia.
“Nakupenda pia mume wangu,” aliniambia.
Maisha yetu yaliendelea mpaka pale siku moja Julieth aliponiambia kuwa alikuwa ni mjamzito, taarifa hizo ziliweza kunifurahisha sana, nikahisi kuitimiza ndoto ya maisha yangu, ilikuwa ni ndoto ya kupata mtoto.
“Mke wangu unasema kweli?” nilimuuliza mke wangu huku nikionekana kutoamini kabisa, nilihisi alikuwa akinitania.
“Ndiyo mume wangu nina ujauzito wako,” alinijibu Julieth huku uso wake ukiunda tabasamu pana.
“Siamini kwa kweli, unaujauzito?” nilimuuliza tena safari hii nilisimama na kwenda kumkumbatia kwa furaha, nilipokuwa nimemkumbatia sikuacha kumwambia kuwa nilimpenda sana na kwa zawadi ile aliyokuwa amenipa katika maisha yangu ilinifanya nizidi kumpenda sana. Niliahidi kuongeza mapenzi.
“Huu ujauzito una muda gani?”
“Mwezi mmoja.”
“Asante mke wangu, umeitimiza ndoto yangu.”
“Ndoto yako?”
“Ndiyo.”
“Ndoto gani?”
“Kwa muda mrefu nilikuwa nikitamani siku moja kuitwa baba, sikujua itakuwa ni siku gani lakini katika hili la leo ulilonifanyia katika maisha yangu kwa kweli nashindwa nikushukuru vipi ila nakuahidi kuwa nitakupenda sana na nitakutunza maisha yako yote, nitapigania uwepo wako katika maisha yangu,” nilimwambia.
Wakati wa furaha ukazidi kutawala maisha yangu, maisha ya ndoa yangu, nilizidi kumpenda sana mke wangu kwa maana yeye ndiye alikuwa mwanamke wangu wa kwanza kumpenda katika maisha yangu na vilevile ndiye alikuwa mwanamke wangu wa kwanza kunipa taarifa za ujauzito wangu. Moyo wangu ulikuwa katika furaha kubwa sana.
“Siamini, siamini Julieth,” nilijiambia maneno haya nilipokuwa peke yangu chumbani, wakati huo nilikuwa nimejilaza kitandani huku nikiukunjakunja mto. Hakika nilijiona kuwa kidume tena kidume haswaa.

Je, ni nini kitaendelea?
 
JUMA HIZA
PENZI LILILOSABABISHA MAUTI-03
Based on True Story.
0712988278

ILIPOISHIA.....

“Siamini, siamini Julieth,” nilijiambia maneno haya nilipokuwa peke yangu chumbani, wakati huo nilikuwa nimejilaza kitandani huku nikiukunjakunja mto. Hakika nilijiona kuwa kidume tena kidume haswaa.

SONGA NAYO......

Nilikumbuka kumwambia Mama yangu juu ya habari zile za ujauzito wa Julieth, alionekana kufurahishwa na taarifa hizo. Hakuacha pia kunihusia juu ya maisha mapya ya familia ambayo nilikuwa natarajia kwenda kuyaanza.
“Dominick mwanangu hongera ila jiandae kwa maisha mapya ya familia unayokwenda kuyaanza,” aliniambia Mama nilipokuwa nikizungumza naye kwenye simu.
“Asante Mama ila hata hivyo najiandaa najua sasa tunakwenda kuongezeka katika familia yangu,” nilimwambia Mama kisha nikajichekesha kwa makusudi kabisa ajabu Mama yangu alikuwa kimya, hakunionyesha hali yoyote ya kuniunga mkono.
“Ila Dominick mwanangu kuna jambo nataka kukueleza,” aliniambia Mama kwa sauti ya chini.
“Jambo gani hilo mama?” nilimuuliza.
“Ni kuhusu huyo mke wako,’ alinijibu.
“Amefanyaje tena?”
“Hajafanya kitu ila hivi ni kweli kabisa umefurahia mkeo kukubebea ujauzito wako?”
“Ndiyo Mama kwani kuna ubaya?”
“Hakuna ubaya ila nahisi kama unaenda kujibebesha mizigo.”
“Najibebesha mizigo kivipi Mama mbona sijakuelewa?”
“Huyo unayemuita mkeo hana kazi yoyote anakutegemea wewe umfanyie kila kitu bado hapohapo anakuletea mtoto hivi huoni kuwa hiyo ni mizigo unajibebesha?”
“Hapana Mama usiseme hivyo huyu ni mke wangu na suala la mimi kumuhudumia ni wajibu wangu mbona sioni kama kuna tatizo hapo?”
“Dominick mwanangu wewe bado ni mtoto kwangu na utabaki kuwa mtoto siku zote, kwa macho ya haraka unaweza kusema sio tatizo lakini kiukweli ni tatizo tena ni tatizo kubwa sana, unakwenda kubeba majukumu mazito mwanangu.”
“Sasa Mama unanishauri nifanyaje?”
“Hapo cha kukushauri mwanangu mrudishe kwao aende kwanza kuilea mimba mpaka pale atakapojifungua ndiyo arudi nyumbani wakati huo utakuwa umeshamuandalia mazingira mazuri ya kumlea mtoto wenu.”
“ Hapana Mama siwezi kufanya hivyo.”
“Dominick mwanangu nakuonea huruma,” aliniambia Mama kwa sauti iliyoonyesha kuwa na masikitiko makubwa sana.
Niliamua kuyakatisha mazungumzo kwa kumdanganya kuwa salio nililokuwa nimejiunga lilikuwa limeisha hivyo muda wowote simu ingeweza kukatika. Naam! Haikuchukua sekunde chache kisha niliweza kukata simu, niliamua kufanya hivyo kwa kuwa sikutaka kuzungumza na Mama yangu kwa wakati huo, maneno yake yalionekana kunikwaza moyoni.
Sikupenda kumuona mtu yoyote akimzungumzia vibaya mke wangu, nilihakikisha nasimama imara katika kuipigania ndoa yangu. Sijui ni nini kilitokea mpaka Mama yangu akabadilisha mawazo yake, alikuwa akimchukia tena mke wangu. Nilipokuwa nikiendelea kutafakari juu ya chuki iliyojipandikiza upya kwa Mama yangu dhidi ya mke wangu Julieth ghafla! simu yangu iliingia ujumbe mfupi. Nilipoufungua na kuusoma ulikuwa ni ujumbe kutoka kwa Mama yangu, alikuwa ameniandikia hivi,
“MWANANGU NAONA UMELOGWA SASA YANI HUTAKI KABISA KUNISIKILIZA MIMI MAMA YAKO NILIYEKUZAA SIJUI UTAMSIKILIZA NANI MWINGINE AU UNATAKA MIZIMU YA BABA YAKO IFUFUKE IJE IKUAMBIE NDIYO UTAELEWA?”
Nilipomaliza kuusoma ujumbe huo hakika ulionekana kunitisha sana, sikutaka kumjibu lolote kwa maana niliamini fika hata kama ningeamua kumjibu lolote kama swali la kumuuliza majibu yangekuwa ni yaleyale.
Kichwa changu bado kiliendelea kutawaliwa na mawazo lukuki, nilizidi kuwaza na kuwazua, kupanga na kupangua lakini mpaka kufikia wakati huo sikujua ni nini nilitakiwa kufanya. Kila nililokuwa nikiliwaza lilizidi kuniumiza kichwa changu, nilipagawa.
Bado wimbi la mawazo liliendelea kuvuma katika upeo wa fikra zangu, nilizidi kuwaza mambo mengi sana kuhusu ndoa yangu ambayo tayari ilikuwa imeingia dosari.
“Kwanini mama unanifanyia haya, kwanini hutaki kufurahia maisha ya ndoa yangu?” nilijiuliza wakati huo mikono yangu ilikuwa imeshikilia picha iliyokuwa ndani ya fremu, ilikuwa ni picha yangu na mke wangu tuliyopiga siku ya ndoa yetu. Macho yangu yaliitazama lile vazi la shela alilokuwa amevaa mke wangu kisha na mimi nikiwa katika vazi la suti adhimu, tulikuwa tumekumbatiana huku furaha ikiwa imetutawala.
Machozi hayakuwa mbali kwa wakati huo, yakaanza kunidondoka tone moja kisha tone la pili na haikuchukua sekunde kadhaa kusababisha mvua ya machozi ya uchungu iliyoninyeshea kutiririka mashavuni mwangu, nilikuwa nikilia kwa wakati huo.
Mama yangu alikuwa kikwazo cha furaha ya ndoa yangu, kila kitu kilichokuwa kikiendelea alionekana kuwa nacho kinyume, alikikosoa.
“Nimekukosea nini mimi Mama kwanini hutaki kuniunga mkono katika hili, kwanini hutaki kushiriki furaha ya maisha yangu au nimefanya makosa kukueleza taarifa za ujauzito wa mke wangu?”
Kila swali nililokuwa nikijiuliza halikuweza kupata majibu zaidi machozi ndiyo yaliyokuwa yameshika hatamu yake, yalizidi kunitiririka mashavuni bila kuyafuta.
Wakati ule ambao nilikuwa nimeishikilia picha huku machozi yakiendelea kunidondoka ghafla! mke wangu Julieth akatokea, alinikuta nikilia.
“Mume wangu kuna nini kimetokea?” aliniuliza Julieth kwa sauti iliyogubikwa na upole wa hali ya juu, alionekana kushangazwa na hali aliyonikuta nayo kwa wakati ule.
“Hakuna kitu,” nilimjibu huku nikiyafuta machozi yangu kisha nikairudisha ile picha ukutani.
“Hakuna kitu na wakati nimekukuta unalia?” aliniuliza huku akionekana kutoelewa lolote lile.
Naam! Ni kweli alikuwa hajui lolote lililokuwa limetokea hata hivyo sikutaka kumuweka wazi, niliamua kumficha ukweli, niliamua kufanya hivyo ni kutokana na hali ambayo alikuwa nayo.
“Hakuna kitu nipo sawa,” nilimwambia kisha nikajaribu kutengeneza tabasamu pana katika uso wangu, nilifanikiwa kutabasamu.
“Mbona unalia?” aliniuliza wakati huo alinisogelea kisha akaanza kunifuta machozi kupitia viganja vyake, nilipomtazama alionekana kuonyeshwa kuguswa na tukio lile japo hakuwa akijua ni nini hasa kilichokuwa kimetokea.
“Nimemkumbuka marehemu baba yangu laiti kama angekuwepo naamini hata yeye angefurahia kwa tukio hili lililotokea, angefurahi kuwa babu mtarajiwa,” nilimwambia maneno ya uongo ambayo yalijitunga ghafla! kichwani. Muonekano wangu wa majonzi ukichanganya na hayo maneno niliyomwambia yakasaini ukweli ambao alikuwa akiutaka kuufahamu japo ulikuwa ni ukweli wa kutunga.
“Mume wangu usiseme hivyo utakufuru,” aliniambia huku akionekana kuniamini kabisa ila ni kama alikuwa akiwaza kitu na mara baada ya kukiwaza akaamua kuniambia.
“Halafu nimesahau kukwambia,” aliniambia huku akionekana kufurahi.
“Umesahau kuniambia nini?” nilimuuliza huku nikimtazama, wakati huo machozi yalikuwa yamekoma kunidondoka.
“Nimeongea na mama,” alinijibu.
“Mama yupi?” nilimuuliza.
“Kwani wewe una mama wangapi?” aliniuliza.
“Wawili,” nilimjibu.
“Yupi na yupi?” aliniuliza tena swali ambali likanifanya nitabasamu.
“Mama Julieth na Mama Dominick mzaa chema, sasa sijui wewe umeongea na mama yupi hapo?” nilimjibu kwa kumuuliza swali.
“Nimeongea na Mama Dominick,” alinijibu.
“Anasemaje?” nilimuuliza.
“Amefurahi tu! kusikia kuwa nina ujauzito ila ameniambia kuna zawadi anataka kunipa.”
“Zawadi gani tena.”
“Hata sijui mume wangu ila amefurahi huyo,” aliniambia Julieth huku uso wake ukiwa katika tabasamu pana, tabasamu ambalo likazidi kuniweka katika bumbuwazi, kichwani likanijia swali. Lilikuwa ni swali juu ya huyo Mama Dominick ambaye alikuwa akiniambia alifurahishwa na taarifa hizo kiasi kwamba ikafikia wakati wa kutaka kumpa zawadi.
Ni zawadi gani hiyo ambayo anataka kumpa mke wangu?
Na je huo upendo anaouzungumzia mpaka akafurahishwa na taarifa za ujauzito wake ulitokea wapi?
Nikazidi kuwa katika kizungumkuti, sikujua ni nini kilichokuwa kinakwenda kutokea katika ndoa yangu. Nikakumbuka yale maneno aliyoniambia Mama yangu pamoja na ule ujumbe alinitumia, vilikuwa ni vitu viwili tofauti na yale maneno ya Julieth aliyokuwa akiniambia kwa wakati huo.
“Unasema umeongea na Mama Dominick, Mama yangu!” nilimuuliza Julieth huku nikionekana kushangazwa na maneno yake.
“Ndiyo nimeonge na Mama yako,” alinijibu huku akionekana kutokuwa na tatizo lolote, alikuwa akijiamini na jibu lake.
“Vipi na Mama yako pia umemwambia?”
“Ndiyo niliwaambia wote ila kwa ufupi hakuna tatizo lolote mume wangu.”
“Una uhakika?”
“Ndiyo mbona umeshangaa?” aliniuliza.
“Hapana hakuna kitu,” nilimjibu.
Nilizidi kuwa katika fumbo zito, nisijue ningeweza kulifumbua vipi kwani tayari akili yangu ilikuwa imechoka. Nikazidi kubaki kujiuliza maswali lukuki ambayo hayakuweza kupata majibu, kiufupi nilitawaliwa na mawazo.
“Ina maana Mama yangu alikuwa akinitania au?” nikajiuliza tena hapo nilikuwa nikijichekesha kama mwendawazimu, sikutaka kumuonyesha tofauti yoyote mke wangu.

Je, ni nini kitaendelea?
 
JUMA HIZA
PENZI LILILOSABABISHA MAUTI-04
Based on True Story.
0712988278

ILIPOISHIA.....

Nikazidi kubaki kujiuliza maswali lukuki ambayo hayakuweza kupata majibu, kiufupi nilitawaliwa na mawazo.
“Ina maana Mama yangu alikuwa akinitania au?” nikajiuliza tena hapo nilikuwa nikijichekesha kama mwendawazimu, sikutaka kumuonyesha tofauti yoyote mke wangu.

SONGA NAYO....

Maisha yaliendelea huku nikiendelea kubaki na siri moyoni mwangu, ilikuwa ni siri ile ya maneno aliyoniambia Mama yangu, aliniambia kuwa sikutakiwa kuendelea kuishi na mke wangu hasa katika kipindi kile cha ujauzito hivyo nilitakiwa kumrudisha nyumba kwao kwa ajili ya kuilea mimba mpaka pale ambapo angeweza kujifungua ndiyo nilitakiwa kumrudisha na kuendelea kuishi naye. Hilo lilizidi kuniumiza sana akili yangu.
Dominick mimi fundi simu wa Kariakoo sikushindwa kutafuta pesa ya kuweza kuihudumia mimba, sasa kwanini Mama yangu aniambie nilitakiwa kumrudisha kwao, kwani ameona nini?
Lilipotoka swali hilo likajitunga swali lingine basi ikawa ni tafarani tu! nikazidi kujiona kuwa mjinga wa kuendelea kuificha siri ambayo mwisho wa siku ningeweza kuzikwa nayo.
Baada ya wiki moja kupita niliamua kumueleza ukweli mke wangu, nilimuelezea kila kitu kilichokuwa kimetokea, sikutaka kumficha lolote, nilimwambia kwa kuwa nilimuamini, alikuwa ni msikivu hivyo sikutegemea tofauti yoyote ambayo ingeweza kujitokeza.
“Mume wangu,” aliniita mara baada ya kumuelezea kila kitu tulipokuwa nyumbani.
“Naam,” nilimuitikia huku nikimtazama, hakuonekana kubadilika kwa lolote lile, sura yake ya kitoto bado iliendelea kuwa katika vazi lake la upole.
“Mama ameongea kitu cha umuhimu sana,” aliniambia Julieth kwa sauti ya upole.
“Cha umuhimu kivipi?” nilimuuliza.
“Ameona mbali,” alinijibu.
“Kivipi?”
“Wewe hautaweza kunihudumia kwa kila kitu, kuna vingine utashindwa wakati utakapokuwa kazini ni bora niende nyumbani tu! kule watakuwa karibu sana na mimi hasa katika hiki kipindi cha ujauzito wangu.”
“Kwahiyo unataka kuniambia umekubaliana na Mama mkwe wako?”
“Ndiyo tena ameongea kitu cha umuhimu sana,” aliniambia Julieth huku akionekana kuwa sawa, hakuonyesha kukasirika kwa lolote lile.
Nilijaribu kumkatalia lakini lilipokuja suala la king’ang’anizi kwa kweli nilishindwa, Julieth hakutaka kuona wazo la Mama yangu ninalipuzia.
“Mama ni mama Dominick embu tusimpuuzie yeye ni mtu mzima,” aliniambia Julieth.
“Lakini mke wangu.”
“Hakuna cha lakini, kilichobaki hapo wewe nipe nauli niende nyumbani,” aliniambia Julieth.
****
Baada ya siku ya tatu kupita niliamua kwenda kumkatia tiketi ya basi Ubungo mke wangu ambapo siku iliyofuata alitakiwa kusafiri kwenda mkoani Kilimanjaro na basi la KIMOTKO.
Ilikuwa ni moja kati ya safari iliyoniacha katika wakati wa maumivu sana, nilimzoea sana mke wangu, alikuwa ndiyo kila kitu katika maisha yangu.
Hatimaye siku ya safari ikawadia, Julieth mke wangu akaweza kusafiri kuelekea nyumbani kwao Kilimanjaro. Nakumbuka nilipokuwa Ubungo nikimuaga machozi yalikuwa yakinilengalenga mwisho yakaanza kunibubujika.
“Nakupenda sana mke wangu, nitakukumbuka sana,” nilimwambia nilipokuwa nikimuaga.
“Hata mimi nitakukumbuka sana mume wangu, huwezi kuamini yani natamani nisiondoke lakini sina jinsi acha niende nikailee mimba yako nikirudi nitakuletea furaha ya maisha yako,” aliniambia Julieth maneno aliyoyatamka kwa hisia. Nilishindwa kujizuia nikaamua kumkumbatia, akatulia vyema katika kumbato langu.
“Niambie kitu kimoja kabla hujaondoka,” nilimwambia nilipokuwa nimekumbatiana nae.
“Nakupenda sana na ninakuahidi nitamlea vizuri mwanao,” aliniambia huku akilipapasa tumbo lake. Nilimtoa katika lile kumbato kwa wakati huo muda wa kuondoka basi ulikuwa umefika. Nikamsindikiza kwa zawadi ya mabusu huku moyoni nikiahidi kumtunzia thamani yake kama mke wangu wa ndoa.
****
Nilianza kuyaamini maneno ya Mama yangu, niliamini alikuwa sahihi kuniambia maneno yale ya kunikaripia. Hakika nilijiona kuwa mjinga sana hasa kwa kujaribu kupingana na maneno ya Mama yangu, Mama aliyeniweka miezi tisa tumboni mwake kisha akanizaa kwa uchungu.
Nilihisi kuwa mkosaji na niliamua kwenda kumuomba msamaha kwa yale yote yaliyokuwa yametokea. Alinisamehe lakini ulikuwa ni msamaha wa masharti.
Alikuwa amenitafutia mwanamke mwingine ambaye alihitaji nimuoe haraka iwezekanavyo na kila kitu alikuwa ameshakiandaa kama maandalizi ya kumuoa mwanamke huyo ambaye alijulikana kwa jina la Evelyne.
Hakutaka kunipa nafasi ya kujielezea lolote kwa wakati huo alipokuwa akinieleza kuhusu Evelyne, alijua fika nisingeweza kukubali kirahisi hivyo aliamua kutumia cheo chake kama Mama katika kunikandamiza.
“Dominick ukitaka nikusamehe na haya yote yaishe yani nisiwe na kinyongo chochote basi kubali umuoe Evelyne, roho yangu itaridhika,” aliniambia Mama kwa msisitizo.
Nilikuwa katika wakati mgumu sana ndugu msomaji, nilihisi kuchanganyikiwa baada ya kuambiwa maneno hayo. Nikamkumbuka mke wangu ambaye alisafiri siku chache zilizopita pamoja na ahadi zangu nilizomuahidi, nilimuahidi mambo mengi sana lakini kubwa ilikuwa ni kumtunzia thamani yake ya ndoa kama mke wangu halali, sikutaka kumfanyia lolote baya ambalo baadae lingeweza kumpa maumivu makali mno, nilizithamini mno hisia zake, niliuthamini uwepo wake katika maisha yangu.
Nilianza kuona ahadi zangu zikiteketea moja baada ya nyingine, msamaha wa Mama yangu wenye masharti ndani yake kwa kweli ulizidi kuniweka katika wakati wa mawazo, nilikuwa nikiwaza mambo mengi sana lakini hakukuwa na kitu nilichowahi kuking’amua.
“Mama kumbuka lakini nina mke na tayari ana ujauzito wangu,” nilimwambia Mama maneno yaliyomfanya abadilike, alikuwa amekasirika.
“Mke wako mimi simtambui,” alisema Mama huku akiwa katika mnuno usiyomithilika.
“Mama,” nilimuita.
“Hakuna cha Mama hapa ninachotaka ni ukubali kumuoa Evelyne,” aliniambia Mama.
“Nimuoe kivipi Mama na wakati tayari nina mke wangu,” nilimjibu.
“Dominick umekuwa mwanangu yani unanijibu kama mwanao, naona umekuwa sasa baba, umekuwaeeeh,” aliniambia Mama huku akinipigia makofi ya kunidhihaki. Eti! Alikuwa akinipongeza kwa ukuaji wangu mpaka nimefikia hatua namjibu ninavyojisikia.
“Hapana Mama sio kama nakujibu ninavyojisikia lakini waka…” nilimjibu lakini kabla sijamaliza sentensi yangu ghafla! alinikata kauli.
“Lakini nini?” aliniuliza.
“Nampenda sana Mke wangu,” nilimjibu.
“Hivi ni nini unachoking’ang’ania kwa huyo mwanamke au amekupa nini mwanangu. Mimi nahisi sio bure kuna kitu hapa yule mwanamke atakuwa amekuloga,” aliniambia Mama huku akionekana kuithibitisha kauli yake kana kwamba alimuoma mke wangu wakati akiniloga.
Haikuwa kazi rahisi hata kidogo katika kunibadilisha mawazo yangu ya kumpenda Julieth kisha yakabadilika na kuwa chuki, nimchukie Julieth mwanamke wa maisha yangu. Hakika hiyo ilikuwa ni ndoto tena ndoto ya kufikirika kamwe isingeweza kutimia abadani.
Evelyne alikuwa ni msichana mrembo aliyejaaliwa kila sifa za kumshawishi mwanaume rijali. Sikutaka kulijali lile wowowo lake kubwa atembeapo nyuma alikuwa akiacha lawama wala sikutaka kuijali ile elimu yake pamoja na kazi aliyokuwa nayo, nilichokuwa najali kwa wakati huo ni uwepo wa Julieth wangu, mama wa mwanangu mtarajiwa. Sijui aliingia vipi mkataba na Mama yangu mpaka akaamini kuwa ningeweza kumuoa.
Hilo lilikuwa ni jambo gumu sana, sikutaka kukubali kirahisi japo Mama yangu aliniambia kuwa asingeweza kunisamehe lakini haikuwa tatizo kwangu, niliendelea kubaki na msimamo wangu, sikutaka kukubaliana na jambo lile kwani kwa kukubali kwangu kungeweza kusababisha maumivu kwa mwanamke ambaye alikuwa akinipenda sana.
“Naomba unisamehe Mama, siwezi kufanya hivyo,” nilimwambia Mama yangu.
“Huwezi nini Dominick na wakati nimeshakwambia msahau kuhusu huyo mke wako,” aliniambia Mama.
“Mama kwanini unashiriki kuiangamiza ndoa yangu?” nilimuuliza.
“Unasemaje?” aliniuliza kwa ghadhabu.
“Mama kwanini unataka nimuache mke wangu?” nilimuuliza swali ambalo lilionekana kumkera sana, alikasirishwa mno na ni hapo ambapo hakutaka kuniona, aliamua kunifukuza na kuniambia nisimtafute tena katika maisha yake, nisimjue tena akazidi kwenda mbali akaniambia nitafute Mama mwingine ambaye angeweza kuyafurahia maisha ya ndoa yangu. Mama yangu alitokea akanichukia. Kuna kipindi niliwaza kuwa kama kweli yule alikuwa ni Mama yangu mzazi aliyenizaa sasa kwanini anichukie kiasi kile? Nilijiuliza swali ambalo sikuweza kupata jibu. Ndoa yangu ambayo aliikubali mwanzoni na kuipa baraka zote leo aliikataa na kuanza kunitafutia mwanamke mwingine, nikazidi kuwa katika maumivu makali mno, kuna wakati nilihisi wenda nilikuwa nikiigiza katika moja ya sinema ya kusikitisha na muda wowote muongozaji wa sinema hiyo angeweza kuniambia neno “Cut,” na hivyo ningesimama lakini haikuwa hivyo, nilikuwa katika maisha halisi, maisha ya changamoto niliyokuwa nikipitia ya ndoa yangu.

Je, ni nini kitaendelea?
 
JUMA HIZA
PENZI LILILOSABABISHA MAUTI-05
Based on True Story.
0712988278

ILIPOISHIA.....

Ndoa yangu ambayo aliikubali mwanzoni na kuipa baraka zote leo aliikataa na kuanza kunitafutia mwanamke mwingine, nikazidi kuwa katika maumivu makali mno, kuna wakati nilihisi wenda nilikuwa nikiigiza katika moja ya sinema ya kusikitisha na muda wowote muongozaji wa sinema hiyo angeweza kuniambia neno “Cut,” na hivyo ningesimama lakini haikuwa hivyo, nilikuwa katika maisha halisi, maisha ya changamoto niliyokuwa nikipitia ya ndoa yangu.

SONGA NAYO.....

Niliamua kumuita Chrispine katika ofisi yangu kisha nikamsimulia mkasa mzima uliyokuwa umetokea na lile tukio zima la Mama yangu kunifukuza na kuniambia kuwa nitafute Mama mwingine ambaye angeweza kuifurahia ndoa yangu.
“Unajua bado nipo njia panda,” aliniambia Chrispine huku akionekana kuchanganyikiwa, wakati huo nilikuwa nikitengeneza simu ya mteja ambayo ilikuwa na tatizo la kubadilisha Screen.
“Upo njia panda kivipi?” nilimuuliza.
“Kwani Mama yako anachokitaka hasa ni nini?” aliniuliza.
“Anataka nimuoe Evelyne,” nilimjibu.
“Duh! Ndugu yangu kweli hapo upo katika wakati mgumu ila kuna kitu itabidi nikushauri.”
“Kitu gani?”
“Kuwa na maamuzi, unajua sifa kubwa ya mwanaume sio kula au kunyanyua vyuma hapana bali ni kuwa na maamuzi tu! maamuzi ndiyo yatakayoweza kukufanya ukabiliane na matatizo yote hayo yanayokuandama katika maisha yako,” aliniambia Chrispine.
Kwa kweli sikuwa tayari kumsaliti mke wangu, sikutaka kukubaliana na Mama yangu katika mpango wake wa kunishawishi nimuoe Evelyne mwanamke aliyenichagulia na kudai kuwa ndiye alikuwa chaguo sahihi la maisha yangu. Akili yangu haikutaka kukubaliana na hilo kabisa na kila nilipojaribu kulitafakari bado liliendelea kuniumiza tu! sikutaka kuamini kama zile zama za kuchaguliana mke au mume bado zilikuwepo.
Ama kweli wenye maneno yao waliposema kuwa kuwa uyaone hawakukosea, hakika nilikuwa katika ukubwa wa kuyaona maajabu yasiyosimulika.
Yote yaliyokuwa yametokea niliamua kuyachukulia kuwa kama changamoto za kimaisha ambazo mtu yoyote anaweza kukumbana nazo hata hivyo sikutaka kuonyesha kukata tamaa, niliendelea kuipigania ndoa yangu.
Sikuacha kuwasiliana na mke wangu kipindi alipokuwa nyumbani kwao akiendelea kuilea mimba, kila nilipomkumbuka nilimpigia simu na kuzungumza mambo mawili matatu kuhusu maisha yetu nay a mtoto ambaye tulikuwa tunatarajia kumpata, nilizungumza na wazazi wake pamoja na ndugu zake ambao walionekana kunipenda sana, hakukuwa na tofauti yoyote katika mazungumzo yetu na mara zote nilipozungumza nao sikuacha kuwaambia kuwa nilikuwa nikiwapenda sana na waendelee kumtunza mke wangu, kauli yangu hiyo kwao ilikuwa ni kituko, iliwaacha na kicheko kikubwa sana. Nakumbuka ndugu zake wengine walikuwa wakiniambia Julieth alikuwa amepata mume.
Maneno ya ndugu zake mke wangu pamoja na upendo wao ndiyo ulinifanya nizidi kusahau yale matatizo yaliyokuwa yakiniandama, kuna wakati sikutaka kuyakumbuka kabisa.
Naikumbuka ile sauti ya mke wangu Julieth iliyokuwa na upole uliyopitiliza, alipokuwa akizungumza na mimi sikujutia, nilitamani muda wa maongezi usiishe haraka kwani alikuwa akinifariji sana.
“Usijali mume wangu ni muda mchache umebakia nitakuzalia mwanao,” aliniambia mke wangu kwa sauti legevu iliyoniacha katika weweseko la kimapenzi.
“Natamani sana mwanangu awe ni wa kiume,” nilimjibu huku nikiivuta pumzi nzito na kuiachia kwa pupa.
“Kwanini umependa awe wa kiume na asiwe wa kike?” aliniuliza Mke wangu.
“Kwasababu nataka nimuite jina la marehemu baba yangu,” nilimwambia.
“Jamani mimi nataka awe wa kike,” aliniambia.
“Akiwa wakike sitakuwa na rafiki hapo.”
“Kwahiyo wewe unataka rafiki?”
“Hahaha! Ndiyo ili nicheze naye na fujo zote anifanyie mimi.”
h“Kwani akiwa wakike hataweza kufanya hivyo?”
“Muda wote atakuwa kwa mama yake huo muda wa kucheza naye nitaupata wapi,” nilimwambia mke wangu maneno yaliyomfanya akacheka sana.
Hakuacha kuniambia kuwa katika maisha yake alikuwa akijivunia kuwa na mimi, nilikuwa nikimfanya awe ni mtu wa kutabasamu kila wakati. Maneno yangu, vituko vyangu vya kwenye simu vilimfanya kila mara anitafute, kuna wakati alinipigia simu kisha akaniambia kuwa ananipenda sana, nikatabasamu halafu na mimi nikamjibu kuwa nampenda pia, jibu hilo likamfanya afurahi sana, wakati huo nilikuwa katika ofisi yangu nikiendelea kuzitibu simu mbovu za wateja wangu.
****
Baada ya miezi tisa kutimia Julieth alifanikiwa kujifungua mtoto wa kike ambaye niliamua kumuita jina la Glory. Nilimpongeza sana mke wangu kwa zawadi ile ambayo alikuwa amenipatia katika maisha yangu, nilimwambia kila aina ya maneno mazuri siku hiyo.
“Yani mke wangu siamini, hivi ni kweli leo naitwa baba?” nilimuuliza Mke wangu nilipokuwa nikizungumza naye kwenye simu, wakati huo alikuwa bado yupo hospitalini.
“Ndiyo mume wangu amini sasa hivi unaitwa baba,” alinijibu mke wangu kwa sauti iliyokuwa na furaha.
“Asante mke wangu ila pia pole najua umeumia kwa ajili yangu, nakupenda sana laazizi wangu,” nilimwambia.
“Asante mume wangu,” alinijibu kisha na huo ndiyo ulikuwa mwisho wa mazungumzo yetu.
Nilitawaliwa na furaha sana, sikutaka kuamini kama kweli nilikuwa naitwa baba kwa wakati ule. Huo ulikuwa ni ukweli ambao ulizidi kuniweka katika wakati wa furaha muda wote, sikutaka kuamini kwa kweli.
“Dominick, Dominick unaitwa baba,” nilijiambia kisha nikaanza kucheka kama mwendawazimu.
Japo ilikuwa imepita miezi mingi tangu Mama yangu aliponifukuza nyumbani kwake na kuniambia kuwa nisimtambue lakini sikuacha kumpigia simu na kumueleza tarifa zile, alionekana kuzipuuzia kisha hakutaka kubaki kimya akaniambia kuwa namba ile niione kuwa kama kituo cha polisi, nisiizoee. Alifika mbali akaanza kumtukana mke wangu pamoja na mwanangu, malaika ambaye alikuwa hajui lolote kuhusu baba wala bibi katika hii dunia.
Nilizidi kushangazwa na matusi aliyokuwa akiyatoa Mama yangu dhidi ya mke wangu na mwanangu, nikajiuliza juu ya makosa ambayo walikuwa wameyafanya mpaka wakafikia hatua ya kutukanwa, hakukuwa na kosa lolote bali lilikuwa ni gubu la Mama yangu.
“Mama mbona unanitukania mke wangu na mwanangu kwani wamekukosea nini?” nilimuuliza Mama yangu baada ya matusi kumkoma.
Hakunijibu lolote mwisho akaamua kunikatia simu, kitendo kile kikaniweka katika hali ya sintofahamu, chuki alizokuwa nazo Mama yangu zikazidi kunishangaza. Nikajiuliza kama kweli yule alikuwa ni Mama yangu mzazi sasa kwanini anifanyie yale au hakuthamini uwepo wangu kama mtoto wake. Inamaana hakutaka kujua lolote kuhusu mwanaye, ukimya wangu wa miezi yote niliyokaa kimya tangu pale aliponifukuza hakutaka kujua lolote, hakutaka kunisikiliza japo kwa sekunde kadhaa ambazo ningezitumia vyema kuzungumza naye.
Niliguna mara baada ya kukatiwa simu kwa wakati ule, nilihisi kukosea namba, akilini nikajiambia kuwa labda yule hakuwa Mama yangu mzazi hivyo nikarudia kuitazama ile namba vyema. Naam! Ilikuwa ni namba ya Mama yangu Mzazi, sikutaka kuamini kama bado alikuwa na chuki na mke wangu tena chuki zake zilipitiliza kiasi kwamba akawa anamchukia na mwanangu ambaye hakuwa na hatia yoyote. Nilijaribu kumpigia simu kwa mara nyingine lakini haikupolewa mwisho akaamua kunizimia kabisa simu, ikawa haipatikani.
Sikutaka tena kuishughulisha akili yangu kuendelea kuwaza mambo ambayo yalikuwa yanaendelea kuniumiza kwa wakati ule ambao nilikuwa katika furaha, niliamua kuyaacha kama yalivyo na kama tatizo alikuwa ni Mama yangu nilipanga kutomsumbua tena kwa kumpigia simu wala kumtafuta kwa njia yoyote ile kama alivyokuwa akitaka nifanye. Nilifahamu fika kwa kuendelea kumsumbua ningezidi kujitafutia matatizo mengine.
****
Baada ya kupita miezi mitatu niliowaomba wazazi wa mke wangu niweze kumrudisha mke wangu na mwanangu kisha maisha yetu yaendelee kama kawaida. Hawakuonekana kunipinga kwa lolote, walinikubalia ombi langu kisha wakaniruhusu nimchukue mke wangu.
Baada ya kufanikiwa kumrudisha mke wangu pamoja na mwanangu nyumbani maisha yaliendelea vizuri, nilikuwa nikifanya kazi yangu ya ufundi simu huku nikitegemea kipato nilichokuwa nikikipata kiniwezeshe kuilea familia yangu ambayo ilikuwa imeongezeka.
Nilimpenda sana mwanangu Glory ambaye kila nilipomtazama kwa mbali nilikuwa nikiiona taswira ya Mama yangu mzazi, alifanana sana Mama Dominick.
Maisha yaliendelea huku mwanangu naye akizidi kukua vyema. Bado niliendelea kumficha mke wangu juu ya kile kilichokuwa kimetokea kwa Mama yangu lakini ni kama vile nilikuwa nikijaribu kuificha siri ambayo tayari ilikuwa ikifahamika na wengi, nilijidanganya.
Siku moja mke wangu aliniuliza swali ambalo liliniweka katika wakati mgumu sana wa kuweza kulijibu. Aliniuliza juu ya ukimya aliyokuwa nao Mama yangu pamoja na tukio la kutokuja kumuona mjuu wake. Lilikuwa ni swali gumu ambalo liliniwia vigumu kutoa jibu kwa uharaka, nilibaki kimya huku nikiendelea kumtazama usoni kana kwamba sikuwa nimemsikia swali alilokuwa ameniuliza.
“Mume wangu,” aliniita.
“Naam,” nilimuitikia.
“Mbona Mama yako hataki kuja kumuona mjuu wake?” aliniuliza.
“Labda itakuwa ni ubize wake lakini atakuja kumuona usijali,” nilimjibu kwa kumdanganya uwongo ambao haukuwa na mashiko hata kidogo.
“Ubize inamaana ndiyo akose hata nafasi ya kuja kumuona halafu mbona nikimpigia simu hapokei kuna nini?” aliniuliza tena akinitazama kwa macho yaliyogubikwa na kila aina ya wasiwasi.
“Hapokei?” nikamuuliza huku nikijifanya kushangazwa.
“Vipi kwani wewe ulizungumza naye?”
“Ndiyo na tena aliniambia atakuja kumuona mtoto,” nilimwambia huku nikijitahidi kutomuonyesha tofauti yoyote ambayo ilikuwa imetokea na mwisho aliweza kuniamini, akaridhika na maneno yangu.

Je, ni nini kitaendelea?
 
JUMA HIZA
PENZI LILILOSABABISHA MAUTI-06
Based on True Story.
0712988278

ILIPOISHIA.....

“Hapokei?” nikamuuliza huku nikijifanya kushangazwa.
“Vipi kwani wewe ulizungumza naye?”
“Ndiyo na tena aliniambia atakuja kumuona mtoto,” nilimwambia huku nikijitahidi kutomuonyesha tofauti yoyote ambayo ilikuwa imetokea na mwisho aliweza kuniamini, akaridhika na maneno yangu.

SONGA NAYO......

Maisha yaliendelea huku kila siku swali likiwa ni lile lile kuhusu Mama yangu, kwa kweli kuna kipindi nilikwazika moyoni hasa baada ya mke wangu kuzidi kung’ang’ania ujio wa Mama yangu. Kuna kipindi tulikuwa tukiingia katika ugomvi na sababu kubwa ilikuwa ni Mama yangu. Mke wangu alikuwa hajui ni kitu kilichokuwa kikiendelea, kuna wakati nikatamani nimueleze ukweli wa kile kilichokuwa kimetokea lakini nafsi yangu ilisita nikahisi ningeweza kuzua ugomvi ambao kwa kweli ningeshindwa kuuamua.
Kuendelea kuwaza na kujiuliza maswali lukuki bila kupata majibu yake ni sawasawa na kuteka maji katika tenga. Niliamua kumueleza Chrispine kuhusu janga lile lililokuwa limeikumba ndoa yangu kiasi kwamba kuna kipindi furaha ilikuwa ikitoweka kabisa.
“Unajua kuna kitu kimoja unakosea Dominick,” aliniambia Chrispine huku akionekana kunisikitikia.
“Nakosea nini sasa?” nilimuuliza.
“Julieth kwani ni nani yako?” aliniuliza swali ambalo jibu lake lilikuwa wazi kabisa, nilihisi kama alikuwa akinikejeli.
“Ni mke wangu inamaana hujui?” nilimjibu kwa kumuuliza swali.
“Nafahamu ila inawezekana ukawa umesahau kuwa Julieth ni mkeo ukahisi labda ni mpenzi wako,” aliniambia maneno yaliyoniacha njia panda.
“Una maana gani?” nilimuuliza.
“Kwa ninavyojua mimi mpaka mnaamua kuishi kama mke na mume katika ndoa basi maana nyie ni kitu kimoja sasa kutakuwa kuna maana gani ya ndoa wakati matatizo yako unayafanya kuwa siri usiyotaka hata mkeo kufahamu au unataka kuniambia unaamini katika ule msemo wa kipumbavu eti! Changu ni changu?” aliniuliza.
“Hapana sio kama naficha lakini,” nilimwambia lakini kabla sijamaliza akanikata kauli.
“Lakini nini?”
“Namjua vizuri mke wangu, sitaki kumuumiza.
“Kuna vitu vya kuficha lakini si kama hili, mueleze ukweli mkeo ili aweze kujua ni cha kufanya wakati mwingine unaweza ukaona upo sahihi kuficha lakini baadae itakuja kukugharimu maisha ohoo,” aliniambia Chrispine maneno yaliyokuwa na maana kubwa sana.
Nilijiona kuwa sahihi kwa kile nilichokuwa nikikifanya, kumficha mke wangu ukweli wa jambo lile, niliamua kuuvunja ukimya nikapanga kumueleza mke wangu ukweli wote uliyokuwa umetokea mpaka kufikia hatua Mama yangu kunitafutia mwanamke mwingine ambaye alinilazimisha nimuoe, kwa kweli sikujua nilitakiwa nianzie wapi kumuelezea mke wangu ambaye alikuwa hafahamu lolote.
Nilikuwa nimepanga kumueleza ukweli mke wangu wala sikutaka tena kumficha, maneno ya Chrispine yaliiingia vilivyo mpaka nikajiona kuwa nilikosea. Nilianza kwa kumuomba msamaha kwa kosa nililokuwa nimelifanya, akaonekana kushangazwa na msamaha wangu, alinitazama kama mtu aliyekuwa katika mshangao wa kuitazama sinema ya kutisha. Nilifahamu nilikuwa nimemuacha njia panda hasa baada ya kumuomba msamaha wa kosa ambalo sikulikiri mbele yake.
“Unaniomba msamaha kwani umenikosea nini mume wangu?” aliniuliza huku akiendelea kunishangaa, sikutaka kumuacha aendelee kuwa katika mshangao ule sajari na hali ya sintofahamu iliyokuwa imemkumba ghafla! nikaamua kumuelezea kila kitu kilichokuwa kimetokea.
Hakutaka kuamini hata kidogo kwa kile nilichokuwa nikimueleza kuhusu Mama yangu na mambo aliyokuwa akinifanyia, akabaki akiwa ameyatoa macho yake mithili ya mtu aliyekuwa katika kabali nzito baada ya kusikia kuwa nilitafutiwa mwanamke ambaye nililazimishwa nimuoe kipindi kile ambacho alikuwa nyumbani kwao akiilea mimba.
Kama ilivyokuwa kawaida yake machozi hayakuwa mbali, yalianza kumdondoka huku midomo yake ikionekana kumchezacheza, alikuwa na maneno ya kuniambia lakini yalikwamishwa na kilio kilichomkumba ghafla! Nikapata kazi ya kumbembeleza mpaka pale alipotulia ndipo alipoweza kuzungumza.
“Dominick kwanini mama yako ananichukia kiasi hiki nimemkosea nini mimi?” aliniuliza kwa sauti dhaifu iliyokaribisha kilio kingine, akaanza kulia tena, nikamsihi anyamaze huku nikimfuta machozi yake.
“Dominick hivi nimemkosea nini mimi mama yako?” aliniuliza huku machozi yakiendelea kumbubujika mashavuni mwake. Nilipomtazama alinisikitisha mno, nikajikuta maumivu yakianza kunichoma katika moyo wangu.
“Hapana mke wangu usiseme hivyo,” nilimwambia kwa kumkataza, sikujua hata nilikuwa namkataza nini wakati ukweli nilikuwa tayari nimeshamueleza.
“Dominick mama yako hanipendi, hampendi hata huyu mwanao hivi unafikiri tutaishi vipi?” aliniuliza huku machozi yakiwa yamemjaa katika macho yake.
“Julieth mke wangu najua Mama yangu hakupendi lakini mimi ndiye ninayekupenda hivyo naomba usijisikie kuwa mnyonge, umesikia mke wangu,” nilimwambia lakini hakunijibu lolote, alibaki kuwa kimya huku akiwa ameyaelekeza macho yake chini, machozi bado yalikuwa yanaendelea kumbubujika.
Haikuchukua sekunde chache akainua kichwa chake kisha akanitazama, maneno yangu yalionekana kumuumiza sana.
“Dominick najuta hata kumzaa huyu mtoto,” aliniambia huku akiyafuta machozi yake.
“Mke wangu ndiyo maneno gani hayo unanayoniambia kwanini hutaki kuwa mwelewa, nimekwambia usijali lolote,” nilimwambia.
“Hivi kwa haya yote uliyonieleza bado niendelee kuishi na wewe kweli au unasubiri mama yako aje aniue ndiyo ufurahi?”
“Julieth mke wangu.”
“Naomba uniache,” aliniambia huku akionekana kujawa na hasira, hakutaka hata nizungumze lolotr, hakuwa tayari kunisikiliza tena.
Nilianza kujilaumu kwa uamuzi ule niliyokuwa nimeuchukua wa kumueleza ukweli mke wangu, moyo wangu ukaanza kumchukia Chrispine, nilimuona kuwa kama adui mwingine wa ndoa yangu yani ushauri kwa wake badala uiokoe ndoa yangu ndiyo kwanza ulienda kuiharibu na kwa wakati ule nilikuwa katika ugomvi na mke wangu.
Nilijitahidi kuomba msamaha lakini hakukuwa na msamaha, nilichukiwa ghafla! na mke wangu hata ile furaha ambayo ilikuwa imetawala katika maisha yetu ikapotea, hakukuwa na aman tena.
“Kwanini hutaki kunielewa mke wangu?” nilimuuliza wakati huo nilikuwa nimepiga magoti.
“Nikuelewe nini Dominick we nenda kamuoe huyo mwanamke aliyekutafutia mama yako,” aliniambia huku hasira pamoja na wivu vikiwa vimemtawala.
“Nakupenda wewe mke wangu huyo mwanamke kama ningekuwa nina nia ya kumuoa ningemuoa tangu ulipokuwa nyumbani lakini sikuwa tayari kufanya hivyo, nakupenda mke wangu,” nilimwambia.
“Nimesema Dominick naomba uniachee,” aliniambia.
“Kumbuka tuna mtoto hivi kama tukianza kugombana wakati huu unafikiri mtoto atakuwa katika misingi ipi?”
“Dominick sitaki kukugombanishe na Mama yako nende ukamuoe huyo mwanamke ili umridhishe mimi niache na maisha yangu.”
“Hiyo ndoto isiyoweza kutimia, siwezi kukuacha wala siwezi kuruhusu ukapotea katika maisha yangu, wewe ni mke wangu tafadhali naomba unielewe.”
“Nikuelewe nini?”
“Nakupenda.”
“Na mama yako je?”
“Mama yangu asikuumize kichwa, sisi tuishi maisha yetu kama yeye hataki basi ila sisi ndiyo tumependana na tayari tupo katika ndoa hivyo hawezi kufanya lolote,” nilimwambia.
“Niahidi,” aliniambia hapa alikuwa tayari ameshaacha kulia.
“Sitokuacha kamwe katika maisha yangu mpaka mwishi wa pumzi zangu,” nilimwambia.
“Kweli?” aliniuliza.
“Namaanisha,” nilimwambia.
Tuliendelea na Maisha yetu huku huku mawazo ya mama yakiendelea kufutika, sikutaka Mama yangu aendelee kuwa kikwazo cha ndoa yangu, nilifanya kila niwezalo ilimradi ndoa yangu iendelee kuwa salama.
Baada ya kupita mwaka mmoja nilihisi kuwa na kila sababu ya kubadilisha kazi, majukumu yaliongezeka na kama unavyojua tena swala la kulea mtoto siyo kazi ya mzahamzaha. Pale Kariakoo nilipokuwa nikifanya kazi yangu ya ufundi simu haikuwa ikinilipa sana kama hapo awali, maisha yalibadilika na kila siku ilikuwa ni afadhali ya jana.
Kuna kipindi tulikuwa tukishindia uji siku nzima huku pesa niliyokuwa nikifanikiwa kuipata nilikuwa nikiichanga kwa ajili ya kulipa kodi ya chumba. Maisha yalikuwa magumu sana, ukichanganya na uwepo wa mtoto tuliyekuwa naye ndiyo kwanza kichwa kilizidi kuniuma.

Je, ni nini kitaendelea?
 
JUMA HIZA
PENZI LILILOSABABISHA MAUTI-07
Based on True Story.
0712988278

ILIPOISHIA.....

Kuna kipindi tulikuwa tukishindia uji siku nzima huku pesa niliyokuwa nikifanikiwa kuipata nilikuwa nikiichanga kwa ajili ya kulipa kodi ya chumba. Maisha yalikuwa magumu sana, ukichanganya na uwepo wa mtoto tuliyekuwa naye ndiyo kwanza kichwa kilizidi kuniuma.

SONGA NAYO.....

Nilimueleza mke wangu juu ya mpango wangu wa kubadilisha kazi akaonekana kuniunga mkono lakini pia hakuacha kunishauri,
“Kwanini usiangalie kazi ambayo inalipa ndiyo uifanye?” aliniuliza.
“Ni kazi gani hiyo?” nilimuuliza.
“Kuna biashara nimeifikiria,”aliniambia.
“Biashara gani hiyo?”
“Kwanini usifanye biashara ya kuuza mitumba nasikia inalipa,” aliniambia mke wangu.
Kwa kweli biashara hiyo ya kuuza mitumba ilionekana kuniingia akilini, nilitabasamu baada ya kusikia hivyo, sikuacha kumshukuru mke wangu ambaye ndiye aliyenipa wazo lile, hakutaka kunishukuru zaidi aliniambia kuwa lile lilikuwa ni jukumu lake kama mke kuhakikisha nafanikiwa katika maisha.
“Hivi mtaji wake ni shilingi ngapi?” nilimuuliza.
“Inategemea na uwezo wetu ila kwa kuanza itabidi ukanunue mzigo pale Ilala sokoni kwa bei rahisi halafu utakuwa unaenda kuwauza wateja mitaani mpaka pale ambapo tutapata mtaji kisha na sisi tutakuwa tukinunua kwa jumla na kuziuza kwa upana,” aliniambia mke wangu maneno ambayo niliyapitisha katika serikali ya ubongo wangu.
****
Niliamua kufanya rasmi biashara ya kuuza nguo za mitumba mitaani, biashara ambayo ilifanya watu wengi wanishangae kipindi ambapo nilikuwa nikianza hata rafiki yangu Chrispine alinishangaa sana na kuniona kuwa nilifanya maamuzi ya kukurupuka bila kuhitaji ushauri.
Kama walivyosema wahenga kuwa katika wengi kuna mengi pia ndivyo ilivyonitokea kipindi ambapo naanza kufanya biashara yangu ya kuuza nguo za mitumba mitaani.
Nilianza kusikia maneno ya watu wakisema kuwa nilifilisika kiasi kwamba niliamua kuacha kazi yangu ya ufundi simu Kariakoo nikawa muuza mitumba. Kila mtu alikuwa na lake la kusema.
Miongoni mwa maneno ambayo siwezi kuyasahau katika maisha yangu nayakumbuka mpaka leo katika kumbukumbu zangu ni siku moja nilisikia watu wakinizungumzia vibaya, walikuwa wakisema kuwa nililogwa na mke wangu ambaye alikuwa hana kazi yoyote Ati! Limbwata la mke wangu ndiyo lilikuwa linaniongoza niende kufeli katika maisha yangu ili tuwe sawa.
Maneno hayo yaliniumiza sana moyoni, sijui ni kwanini ila nilishangaa nikikosa uvumilivu, machozi yakaanza kunidondoka mfululizo. Nilikuwa nikilia machozi yaliyochanganyika na maumivu yaliyo ndani ya moyo wangu.
Siku moja majira ya usiku niliamua kumueleza mke wangu juu ya maneno niliyoyasikia kwa watu wakitusema vibaya lakini mke wangu mimi aliyeumbwa na upole, roho yake iliyochanganyika na ustahimilivu hakuacha kunena japo maneno ya kishujaa akiniambia mimi mume wake ambaye uvumilivu ulikuwa tayari umeshanishinda, kama ni maji basi yalikuwa yamenifika kooni.
“Mume wangu najua sio wote watakao tupenda kuna wengine watatuchukia hata hivyo hutakiwi kukata tama kumbuka tuna mtoto na anatutegemea kwa kila kitu, mimi sina kazi yoyote mume wangu angalau wewe umepata nafasi hii ya kuuza mitumba basi ifanye kwa bidii ili baadae izae matunda,” aliniambia mke wangu wakati huo alikuwa akiandaa chakula mezani, alikuwa amepika ugali na mboga ya kisamvu.
“Miongoni mwa vitu ambavyo najivunia katika maisha yangu ni kuwa na wewe katika maisha yangu, sijuitii kukuita mke wangu kwani kila ninapolitamka neno hili linanipa picha halisi ya mwanamke sahihi aliyeumbwa kwa ajili ya maisha yangu,” nilimwambia huku nikimtazama alipokuwa akininawisha mikono tayari kwa kula chakula alichokiandaa usiku ule.
“Ni wajibu wangu kama mkeo kuhakikisha nakuwa mstari wa mbele kutetea hitaji la moyo wako, kutetea ndoto yako na kuhakikisha kila ulilolipanga nakuwa nyuma yako kwa kila hali mpaka litimie,” aliniambia alipomaliza kuninawasha mikono kisha na nikampokea jagi pamoja na lile beseni dogo aliloninawishika, nikamnawisha.
“Asante mume wangu,” aliniambia mara baada ya kumaliza kumnawisha mikono yake, akaketi chini kisha tukaanza kula kwa pamoja, nilianza kwa kumlisha tonge moja, akacheka wakati huo mtoto wetu alikuwa ameshalala.
“Glory ameshiba kweli?” nilimuuliza mke wangu nilipomkumbuka mwanangu.
“Ndiyo nilimnywesha uji, ameshiba sana,” alinijibu mke wangu kisha tukaendelea na zoezi letu la kula ugali na mboga ya kisamvu iliyopikwa ikapikika.
Kila nilipokuwa nikimtazama Julieth usoni nilizidi kuiona taswira ya mwanamke mvumilivu ambaye alivumilia mambo mengi sana japo kuna kipindi alionekana kuchoka na kukata tamaa lakini hiyo haikuwa sababu ya kufanya mapenzi yetu yafutike, ndoa yetu ivunjike, hilo lilikuwa ni jambo gumu mno kuweza kutokea.
Niliendelea na biashara yangu mpaka pale ambapo nilifanikiwa kupata mtaji uliyoniwezesha na mimi kununua mabeli nikawa nauza kwa jumla jumla. Ilikuwa ni hatua nzuri niliyoipiga katika biashara yangu hiyo ukilinganisha na mwanzo ambapo nilipoanza.
“Hivi umewezaje kufanya haya yote?” lilikuwa ni swali la Chrispine huku akionekana kutoamini kwa hatua niliyokuwa nimefikia katika biashara yangu ya kuuza mitumba. Alikuwa bado akiendelea kuuza Cd katika duka lake Kariakoo, kwa upande wake biashara ilionekana kuwa ngumu mno.
“Ni mipango ndugu yangu,” nilimwambia.
“Mipango ipi tena wakati naona sasa hivi mambo yako sio mabaya,” aliniambia Chrispine huku akicheka.
“Kwa kweli mimi sikuwahi kuamini kama nitafanikiwa kufika hadi huku ila yote haya shemeji yako ndiyo kafanya mpaka yametimia,” nilimwambia kisha akaonekana kama kutoelewa lolote, nikaamua kumuelewesha kwa kirefu, akaonekana kuvutiwa na biashara ile niliyokuwa nikiifanya.
“Itabidi na mimi nianze kuuza mitumba aisee kule biashara imekuwa ngumu,” aliniambia Chrispine maneno ambayo alionekana kuyamaanisha kwa kila kitu.
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa kufanya biashara ya kuuza mitumba na Chrispine, aliamua kuniongezea mtaji na sasa tukawa kitu kimoja, tukaamua kufungua duka la pamoja Kariakoo, tukawa tunauza na kununua kwa wingi. Biashara ikaonekana kukuwa kila siku na tulikuwa tunapata faida kubwa sana.
Baada ya kupita miaka mitano biashara ya kuuza mitumba ilikuwa imetupa mafanikio makubwa sana. Nilikuwa nimefanikiwa kufungua duka langu la nguo pia niliamua kumfungulia mke wangu saluni ya kike pamoja na mgahawa na biashara zote hizo nilimuweka yeye ndiyo aongeze. Julieth alifurahi sana hakutaka kuamini kama kweli na yeye alikuwa anaitwa boss.
Wakati huo Mtoto wetu Glory alikuwa na umri wa miaka saba na tayari alikuwa ameshaanza kusoma darasa la kwanza katika shule ya msingi ya Ali Hassan Mwinyi.
“Jamani Dominick mume wangu nakupenda sana,” aliniambia huku akiwa amenikumbatia kwa furaha nilipomueleza kuwa biashara zote alitakiwa aziongeze.
“Nakupenda pia mke wangu,” nilimwambia kisha nikambusu shingoni.
Nakumbuka mpaka kufikia wakati huo nilikuwa nimefanikiwa kununua kiwanja maeneo ya Vikindu na nilikuwa katika mipango ya kuanza kujenga, sikutaka kumwambia mke wangu kwa haraka, nilipanga kumfanyia Surprise kama wazungu wanavyosema.
Baada ya miezi kadhaa kupita huku biashara zikiendelea kupamba moto mke wangu alianza kuonekana kuhitaji kitu katika maisha yake, kuna kitu alionekana kukisubiri kwa muda mrefu sana na hakikuweza kutimia, aliamini kwa wakati ule ndiyo ulikuwa muda muafaka wa yeye kunieleza ili niweze kumtimizia.
Alitamani sana kuwa mwandishi wa habari, ndoto yake kubwa ilikuwa ni siku moja kuwa mwandishi wa habari mkubwa sana hapa Tanzania. Hakutaka kunificha lolote lile lililokuwa likiendelea kumuumiza moyoni mwake, alinieleza kila kitu na mipango yake ya kurudi shule ili aweze kuitimiza ndoto yake hiyo ambayo aliishi nayo kwa muda mrefu sana.
“Una uhakika utaweza kufanya vizuri?” nlimuuliza mara baada ya kunielezea malengo yake kwa wakati ule.
“Ndiyo mume wangu natamani sana kuwa mwandishi wa habari wa kidunia,” alinijibu huku akionekana kuwa na munkari kupita kawaida.
“Umepanga uanzie wapi sasa?” nilimuuliza.
“Itabidi nirudi shuleni ili nitafute cheti cha form four halafu nikajiunge na chuo kinachofundisha masomo ya uandishi wa habari,” alinijibu huku akionekana kudhamiria kufanya kweli yale aliyokuwa akinieleza.
Kwa kweli nilishindwa kumkatalia mke wangu kwa yale aliyokuwa akinieleza, maneno yake niliyachukulia kuwa kama zaidi ya taarifa muhimu ambayo nilitakiwa kuisikiliza kwa umakini na kuizingatia.
Niliamua kumkubalia kwa kila kitu alichokuwa akikihitaji kwa wakati ule kisha nikaanza kupanga mipango ya kumrudisha shule mke wangu. Niliamua kumpeleka katika elimu ya watu wazima Qualifying Test (QT) ambapo aliweza kusoma na baadae kufanikiwa kumaliza na kupata cheti cha kidato cha nne. Hiyo ilikuwa ni zaidi ya furaha kwa mke wangu, hakutaka kuamini kama alifanikiwa kusoma na kupata cheti cha kidato cha nne.
Upendo ulizidi kuongezeka pale ambapo niliamua kumpeleka chuo cha uandishi wa habari kilichojulikana kwa jina la Daresalaam school of Journalisim kilichopo Ilala. Akafanikiwa kusoma kozi ya uandishi wa habari na utangazaji kwa muda wa miaka mitatu akamaliza.
Furaha ikazidi kumtawala mke wangu ambaye alitamani sana siku moja kuonekana kwenye runinga akitangaza habari au kipindi chochote ambacho angeweza kupewa akiendeshe.
“Kuna siku utaniona kwenye runinga mkeo nikitangaza taarifa ya habari,” aliniambia Julieth tulipokuwa tukitazama taarifa ya habari.

Je, ni nini kitaendelea?
 
JUMA HIZA
PENZI LILILOSABABISHA MAUTI-08
Based on True Story.
0712988278

ILIPOISHIA.....

Furaha ikazidi kumtawala mke wangu ambaye alitamani sana siku moja kuonekana kwenye runinga akitangaza habari au kipindi chochote ambacho angeweza kupewa akiendeshe.
“Kuna siku utaniona kwenye runinga mkeo nikitangaza taarifa ya habari,” aliniambia Julieth tulipokuwa tukitazama taarifa ya habari.

SONGA NAYO....

“Usijali mke wangu tumuombe sana Mungu kwani kwa Mungu hakuna kinachoshindikana,” nilimwambia huku nikijaribu kumkumbusha uwepo wa Mungu katika maisha yetu.
“Namuomba sana Mungu azidi kutujaalia maisha mazuri pamoja na mtoto wetu aendelee kukua vyema ili siku moja ajivunie kuwa na wazazi kama sisi,” aliniambia Julieth.
“Hilo ndilo jambo la msingi mengine huwa yanakuja yenyewe,” nilimwambia.
“Ila kuna kitu nataka nikuombe mume wangu,” aliniambia Julieth huku akiwa ananitazama kwa macho ya kuniuliza nikwambie.
“Kitu gani gani hicho?” nilimuuliza huku nikijiweka tayari kusikia hicho kitu.
“Nataka unichagulie jina zuri ambalo ungependa nilitumie nitakapokuwa mtangazaji,” aliniambia.
“Mimi napenda utumie jina lako hilo hilo.”
“Hapana itabidi nibadilishe jina mume wangu ili liwavutie wengi hata nitakapokuwa natangaza wapende aina ya utangazaji wangu.”
“Unataka ujiite jina gani sasa?”
“Nataka unichagulie wewe,” aliniambia Julieth kisha nikapata kazi ya kuanza kufikiria jina ambalo ningeweza kumpa na likampendeza.
Kichwani yalianza kunijia majina ya watangazaji lukuki ambao walikuwa wakivuma sana kwa aina ya utangazaji wao hata katika majina yao yalivutia mno.
“Sasa nikuite nani?” nilimuuliza.
“Fikiria jina lolote mume wangu,” aliniambia Julieth huku akiwa umeupindisha mdomo wake kuashiria kuwa alikuwa ameanza kukasirika
“Ok ngoja nikuchagulie,” nilimwambia kisha nikanyamza kidogo nikafikiria halafu nikaendelea kuzungumza.
“Jiite basi Julie Pretyy,” nilimwambia huku nikitabasamu, nilifahamu fika nilimpa jina ambalo halikumpendeza, nikaamini hatalipenda hata kidogo. Ajabu akaonekana kulipenda, alifurahi sana kusikia hivyo.
“Ooooh! My God jina zuri sana nimelipenda mume wangu,” aliniambia Julieth mke wangu huku furaha ikiwa imemtawala.
Maisha yalibadilika kwa kiasi fulani kutoka katika maisha ya kushindia mlo mmoja kwa siku mpaka kufikia wakati ule ambapo tulikuwa tunauwezo wa kubadilisha mboga.
Kila nililoamua kulifanya kwa mke wangu niliamua kulifanya kwa moyo mmoja wala sikutaka mtu wa kunishauri lolote katika hilo. Niliamini katika mapenzi ya dhati ambayo nilikuwa nayapata kwa mke wangu, mapenzi hayo ndiyo yaliyosababisha nikaamua kumsomesha mpaka kufikia wakati akamaliza na sasa alikuwa akisubiri kupata kazi.
Alianza kuhangaika kutafuta kazi ya utangazaji katika vituo mbalimbali vya runinga na redio, kila alipokuwa akipeleka barua kwa ajili ya maombi ya kazi alikuwa akikosa, hilo likazidi kumuweka katika wakati wa mawazo, kuna kipindi alianza kukata tamaa, nikamsihi hakutakiwa kufanya hivyo kwani kila kitu kilikuwa na wakati wake hivyo asichoke kusubiri.
“Siamini kama kweli ndoto yangu itatimia,” aliniambia.
“Kwanini isitimie mke wangu muamini Mungu kila kitu kinawezekana,” nilimwambia.
“Kila ninapoenda kuomba kazi nakataliwa halafu bado unaniambia kila kina wakati wake hivi ni wakati gani huo usiyoweza kutimia.”
“Mke wangu hutakiwi kusema hivyo bali unachotakiwa ni kuwa na subira, kila kitu kitatimia,” nilimwambia.
Julieth alizidi kuhangaika kutafuta kazi huku na kule, hakuchoka na kama Mungu siku moja aliweza kupigiwa simu na namba ya simu ya mezani. Ilikuwa ni simu iliyomtaarifu kuwa alikubaliwa kufanya kazi katika kituo kituo cha habari kilichojulikana kwa jina la HIZA TV.
Taarifa hiyo ilileta furaha nyingine ndani ya nyumba bila kujua kuwa baadae nilikuwa naenda kumwaga machozi.
Hatimaye mke wangu akafanikiwa kuanza kazi katika kituo hicho cha habari cha televisheni kilichokuwa maarufu sana. Nilifurahi sana kuona nimefanikiwa kuzitimiza ndoto za mke wangu kipenzi ambazo alionekana kuishi nazo kwa muda mrefu bila kutimia, hilo likanifanya nizidi kujivunia sana wala sikuona sababu ya kuacha kumpongeza mke wangu, nikampongeza kwa kumuahidi kuwa shabiki yake namba moja hasa katika kazi yake ya utangazaji redioni pamoja kwenye televisheni.
Julieth alinishukuru sana, hakutaka kuamini kama kweli alifanikiwa kusoma na kwa wakati ule alikuwa ameanza kazi ya utangazaji. Kila alipokuwa karibu yangu alizidi kunishukuru sana.
“Hapana mke wangu hupaswi kunishukuru kiasi hicho,” nilimwambia mke wangu.
“Yani siamini mume wangu kama kweli nimekuwa mtangazaji, ndoto yangu imetimia,” aliniambia huku furaha ikionekana kutawala uso wake, alifurahi mno.
Kwa kipindi hicho mtoto wetu Glory alikuwa ameshafika darasa la tano na katika upande wa malezi bora hatukuwa nyuma, tulihakikisha tunamlea katika malezi yaliyokuwa bora, hilo naweza kujivunia kwa wakati ule, niliishi vizuri na familia yangu wala hakukuwa na tatizo lolote.
Tulikuwa bado tukiishi katika nyumba ya kupanga lakini maisha yetu yalikuwa mazuri, mahitaji yote muhimu tulikuwa tukiyapata tena kwa wakati.
Sikuacha biashara yangu ya kuuza nguo za mitumba, niliendelea kuifanya huku nikiamini kuwa ilikuwa ndiyo kazi yangu mama ambayo ilinizalishia biashara nyingine ndogo ndogo.
****
Mke wangu alikuwa ni mtangazaji wa redio na TV katika vipindi vyake pendwa alivyokuwa akiviendesha. Alipendwa sana hasa kutokana na aina ya utangazaji wake, hilo lilinifanya nijivunie sana na kujiona kuwa mtabiri ambaye nilitabiri ukweli uliyoweza kutokea katika maisha ya kweli.
Kazi yake utangazaji ikaanza kumuweka bize mke wangu mpaka akawa anakosa muda wa kusimamia biashara alizokuwa akiziongoza hapo awali. Ikabidi nisaidiane nae katika kuziongoza biashara hizo wala hakukuwa na tatizo lolote lile.
Niliamini majukumu ya kikazi aliyonayo ndiyo yaliyokuwa yakimsababisha mpaka akawa anakosa muda wa kufuatilia biashara.
“Mume wangu usione nakuwa mzembe kufuatilia biashara siku hizi nakuwa bize sana,” aliniambia Julieth huku akionekana kutingwa na majukumu ya kikazi.
“Mke wangu naelewa hali uliyokuwa nayo kwasasa wala usijali,” nilimwambia.
“Nafurahi mume wangu kwa kunielewa,” aliniambia.
Hakukuwa na mtu niliyekuwa namuamini kama mke wangu, nilimuamini kupita kawaida wala sikuwa tayari kuona anatokea mtu anakuja kuuvunja uaminifu huo. Nilimpenda sana na pia nilimuheshimu kwa kila kitu.
Katika kumbukumbu zangu sikumbuki kama kuna siku niliwahi kumsaliti mke wangu wala kuwa na chembechembe zozote za kutaka kumsaliti, nilijiheshimu sana na ndoa yangu niliyokuwa naipenda kuliko kitu chochote kile.
Uaminifu niliyokuwa nao kwa mke wangu ulimshangaza mpaka Chrispine japo yeye ndiye aliyekuwa mtu wangu wa karibu wa kunishauri mambo mengi sana kuhusu ndoa yangu.
“Dominick kama ikitokea siku watu wakaamua kutoa tuzo za uaminifu basi katika wanaume kumi bora wewe huwezi kukosekana,” aliniambia Chrispine huku akionekana kutabasamu.
“Kwanini unasema hivyo?” nilimuuliza.
“Sijui nikwambie nini ili kiukweli wewe ni muaminifu sana na ndoa yako,” aliniambia.
“Ni kweli unajua unapoamua kuingia katika ndoa inabidi ukubali kuacha mambo yote ambayo hutakiwi kuyafanya wakati ukiwa ndani ya ndoa,” nilimwambia.
“Julieth kapata mume aisee,” aliniambia Chrispine maneno ambayo yakatufanya wote tukacheka.
Siku hiyo tulizungumza mambo mengi sana kuhusu maisha, ndoa, biashara ila lilipofikia suala la Chrispine kumsifia mke wangu juu ya kazi yake ya utangazaji aliyokuwa akiifanya pamoja na changamoto ambazo angeweza kukutana nazo kidogo nilianza kuingiwa na wasiwasi lakini baada ya dakika kadhaa kupita ule wasiwasi uliniondoka.

Je, ni nini kitaendelea?
 
JUMA HIZA
PENZI LILILOSABABISHA MAUTI-09
Based on True Story.
0712988278

ILIPOISHIA....

Siku hiyo tulizungumza mambo mengi sana kuhusu maisha, ndoa, biashara ila lilipofikia suala la Chrispine kumsifia mke wangu juu ya kazi yake ya utangazaji aliyokuwa akiifanya pamoja na changamoto ambazo angeweza kukutana nazo kidogo nilianza kuingiwa na wasiwasi lakini baada ya dakika kadhaa kupita ule wasiwasi uliniondoka.

SONGA NAYO.....

“Mbona kama umesita kidogo?” aliniuliza Chrispine.
“Hapana,” nilimjibu.
“Ila inabidi uwe makini sana na mkeo unajua hawa viumbe hawakawi kubadilika sasa hivi ameshakuwa mtangazaji wa tv na redio, anakutana na watu wengi maarufu na wenye uwezo wa kifedha zaidi yako, inabidi uwe makini sana usipoangalia unaweza kuja kuyadondosha machozi baadae halafu ukakosa wa kukufuta,” aliniambia Chrispine.
Sikutaka kuyachukulia maneno ya Chrispine kuwa kama ya kufikirika na kwamba yasingeweza kutokea kwa mke wangu, kwa kipindi kile ambapo alikuwa akinieleza kuhusu changamoto ambazo angeweza kukutana nazo mke wangu pamoja na aina ya watu mashuhuri aliyokuwa akikutana nao nilianza kuingiwa na wasiwasi, niliamini kuna ukweli ambao ulikuwa ukiishi katika maisha ya mke wangu ambapo kwa muda mfupi tangu alipoianza kazi yake ya utangazaji nilianza kuyaona mabadiliko makubwa sana.
Alianza kuchelewa kurudi nyumbani na kila nilipokuwa nikimuuliza alinijibu kuwa alipangiwa ratiba ya kutangaza usiku redioni jibu ambalo likanifanya nikubali bila kipingamizi chochote.
Nakumbuka kuna kipindi nilikuwa nikimsikiliza mke wangu redioni alipokuwa akitangaza na hata wakati mwengine kwenye Tv, nilijikuta nikianza kuwa mpenzi wa kusikiliza redio na kufuatilia vipindi vilivyokuwa vikirushwa kwenye Tv na yote sababu alikuwa ni mke wangu.
Nilizidi kumuamini mke wangu hata ule wasiwasi wangu ambao ulikuwa umeanza kuniingia moyoni ukaanza kupotea, sikutaka kumuonyesha mke wangu tofauti yoyote, niliamua kuyapuuzia mawazo yote mabaya niliyokuwa nikimuwazia mke wangu.
“Dominick mume wangu ni nini hivyo embu punguza wivu,” nilijiambia kisha nikajipiga kofi kuashiria kuwa nilikuwa katika mawazo ya kijinga.
Nilimuamini mke wangu kwa kuwa hakukuwa na sinema iliyokuwa ikiendelea nyuma ya pazia ambayo sikuwa nikiifahamu, alikuwa akinieleza ukweli wa kila kitu kilichokuwa kikiendelea katika maisha yake.
Ukweli wake aliyokuwa akinieleza juu ya wanaume waliyokuwa wakimsumbua ofisini ukanifanya nizidi kumuamini kabisa. Nikawa nakesha kumuombea kwa Mwenyezi Mungu azidi kumlinda na pepo baya la ngono ambalo lingeweza kumuingia. Sikuwa tayari kupokea maumivu ya usaliti moyoni.
“Mume wangu niamini nakupenda sana na ndiyo maana nakueleza ukweli,” aliniambia Julieth.
“Nakuamini sana mke wangu kuhusu hilo ondoa shaka kabisa,” nilimwambia huku nikiwa msisitizo wa maneno yangu.
“Mkeo ni mzuri sana eti na ndiyo maana nasumbuliwa na wengi ila mimi najiheshimu na kujilinda mume wangu,” aliniambia Julieth. Maneno yake ya upole yaliyoandamana na maana ya kile alichokuwa akinieleza yalizidi kuniteka vilivyo.
Alipoanza kubadilisha mavazi yake ya heshima na kuvaa nguo fupi nilimuuliza lakini hakukuwa na jibu lingine alilonijibu zaidi ya kuniambia kuwa kazi yake ilimuhitaji awe katika mavazi yale ili azidi kuwavutia mashabiki wakipende kipindi chake. Sikutaka kujifanya mjuaji sana, niliamua kumuacha kama alivyo maadam aliniambia kuwa ananipenda na kuniheshimu basi hiyo ndiyo ilikuwa ngao niliyoishikilia siku zote.
Sasa kama alikuwa akinipenda kulikuwa kuna sababu gani za kutomuamini? Hilo ndiyo swali kubwa lililonijia katika kichwa changu, sikuwa na jibu kamili zaidi ndiyo kwanza nilizidisha mapenzi kwa mke wangu.
Baada ya kupita miezi kadhaa siku moja majira ya usiku mke wangu alirudi nyumbani akiwa na gari aina ya Land cruiser Prado lenye rangi nyeusi. Nilibaki katika mshangao mara baada ya kumuona mke wangu. Sikushangazwa na uzuri wa mke wangu ambao kila siku ulizidi kuongezeka bali kitu kilichonishangaza ni aina ya gari alilokuja nalo. Nikakadiria hesabu ya miezi aliyokuwa nayo tangu alipoanza kazi yake ya utangazaji, alikuwa na miezi mitatu tu.
“Yaani ndani ya miezi mitatu ndiyo anunue gari lenye thamani kubwa kiasi hiki?” nilijiuliza swali ambalo jibu lake alikuwa nalo mtu mmoja tu! alikuwa ni mke wangu. Sikutaka kupoteza muda niliamua kumuuliza.
“Hili gari umetoa wapi?” nilimuuliza mara baada ya kushuka kwenye gari, nikashangazwa na kioja kingine. Ilikuwa ni udereva wake.
“Unajua kuendesha gari siku hizi?” nilimuuliza tena na sasa yalikuwa ni maswali mawili aliyotakiwa kuyajibu.
“Hee! Mume wangu hata salamu,” aliniambia huku akionekana kujiamini.
“Nimekuuliza hili gari umetoa wapi?” nilimuuliza.
“Nimehongwa,” alinijibu kwa dharau.
“Unasemaje?” nilimuuliza kwa ghadhabu.
“Unataka nikujibu nini wewe mwanaume,” aliniambia maneno ambayo yalinishangaza sana.
Kwa sinema aliyonionyesha Julieth ni dhahiri alikuwa amebadilika, sikutaka kuamini kile nilichokuwa nikikishuhudia, nilimtazama mara mbilimbili huku nisijue ni nini nilitakiwa nifanye.
Aliponiambia maneno yale hakutaka kuendelea kuzungumza na mimi, aliongoza moja kwa moja mpaka ndani. Niliendelea kushangazwa na sinema niliyokuwa nikiendelea kuishuhudia, nikalitazama lile gari hakika lilinifanya nibaki katika wakati wa maswali yaliyokosa majibu.
“Ni nini hiki kinachotokea katika maisha yangu?” nilijiuliza kimoyomoyo kisha sikupata jibu lolote zaidi nilizidi kupandwa na hasira na nilijiapiza kuwa liwalo na liwe.
Niliingia ndani huku hasira zikiwa zimenitawala kichwani mwangu, nikamkumbuka mwanangu Glory ambaye alikuwa tayari ameshalala, sikutaka kufanya vituko vyovyote mbele yake hata vya kuigiza, niliamua kufanya hivyo ni kutokana na malezi bora ambayo nilipanga kumpa, sikutaka niwe chanzo cha kuyaharibi maisha yake kwa kumuathiri kisaikolojia.
Licha ya kuwa hasira zilikuwa zimenitawala lakini sikuwa na budi ya kuzipunguza, nakumbuka nilipanga kumpiga Julieth lakini nilishindwa kufanya hivyo. Nilipoingia chumbani nilimkuta tayari ameshalala tena usingizi haswaa! nikajiuliza iliwezekanaje huo usingizi ukampata kwa dakika chache ambazo alikuwa ameingia ndani tena sidhani kama hata kuoga alikuwa ameoga. Tukio hilo lilizidi kuniudhi.
“Mke wangu,” nilimuita lakini hakuitika, nikanyamaza kama muda wa sekunde tano halafu nikamuita tena ndipo hapo alipoweza kuitika.
“Unasemaje mimi nataka kulala nimechoka,” aliniambia maneno ambayo yalinizidi kunikwaza sana moyoni.

Je, ni nini kitaendelea?
 
JUMA HIZA
PENZI LILILOSABABISHA MAUTI-10
Based on True Story.
0712988278

ILIPOISHIA....

“Mke wangu,” nilimuita lakini hakuitika, nikanyamaza kama muda wa sekunde tano halafu nikamuita tena ndipo hapo alipoweza kuitika.
“Unasemaje mimi nataka kulala nimechoka,” aliniambia maneno ambayo yalinizidi kunikwaza sana moyoni.

SONGA NAYO.....

“Unasemaje?” nilimuuliza.
“Sitaki usumbufu nataka kulala nimechoka,” aliniambia kwa sauti ya dharau maneno ambayo yalizidi kunichoma moyoni mwangu. Siwezi kusema ni maumivu kiasi gani ambayo nilikuwa nikiyapata kwa wakati huo ni kama vile kulikuwa na msomaji ambaye alikuwa akinisimulia simulizi nzuri ya kimapenzi na kwa wakati ule alikuwa ameufikia ukurasa uliyobeba maumivu makali mno.
Nilivumilia mambo mengi sana na bado niliendelea kuyavumilia, naweza kusema kati ya wanaume waliyokuwa na mapenzi ya dhati kwa wake zao basi nilikuwa miongoni mwao. Licha ya mateso yote niliyokuwa nikipitia bado niliendelea kuvumilia huku nikijipa moyo yalikuwa na mwisho wake. Siku hiyo ikapita.
****
Siku iliyofuata majira ya asubuhi mara baada ya Glory kwenda shuleni niliamua kumuuliza mke wangu kwa kile kilichokuwa kimetokea siku iliyopita.
“Bado siamini kama umeninunia mke wangu hivi ni nini kimetokea?” nilimuuliza.
“Huamini nini sasa?” aliniuliza.
“Mbona jana nakuuliza kuhusu gari ulilokuja nalo hujanijibu lolote?”
“Unajua wewe ni mwanaume wa ajabu sana yani nakushangaa Dominick badala ya kunipa pole mkeo narudi kutoka kazini wewe una kazi ya kuulizia gari nimetoa wapi hivi umesahau kuwa mkeo sasa hivi nafanya kazi?” aliniuliza.
“Julieth mke wangu mbona mapema sana yani miezi mitati tu! umeshanunua gari?”
“Ni kitu gani ambacho unashindwa kukiamini hapo au unataka nizungumze lugha ipi ili uweze kunielewa.”
“Jana unakumbuka nilipokuuliza ulinijibuje?”
“Ndiyo nakumbuka.”
“Kwanini ulinijibu vile?”
“Unajua uliniudhi sana wewe hujui tu!” aliniambia Julieth kisha nikashindwa kuelewa ni kitu gani ambacho nilimuudhi.
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa kuchanganywa na mapenzi, mapenzi yalikuwa yakinipeleka puta, nilishindwa kuamua lolote kwa mke wangu, alikuwa ameiteka nafasi kubwa sana.
Nilimkumbuka Mama yangu ambaye mpaka kufikia kipindi hicho sikuwa nafahamu lolote kuhusu yeye. Tangu alipoweza kunifukuza nyumbani kwake na kuniambia kuwa nisimtafute kwa namna yoyote huku sababu kubwa ikiwa ni mke wangu kwa kweli sikuweza kumtafuta.
Nilikaa miaka mingi sana bila kuwasiliana na Mama yangu, nilifanya yote hayo nikiamini Mama yangu alikuwa na makosa. Kitendo cha kumchukia Mke wangu na kudai kuwa hakuwa mwanamke sahihi katika maisha yangu hakika kilinifanya nimchukie sana.
Nilimchukia mara baada ya kupata ushauri wa rafiki yangu Chrispine. Maneno yake yalinifanya nijione kuwa bora zaidi ya kila kitu na sikutakiwa kumsikiliza Mama yangu kwa lolote lile ambalo alikuwa akiniambia.
“Hivi nimefanya ujinga gani mimi?” yalikuwa ni majuto kwangu, nilianza kuona thamani ya maneno ya Mama yangu, Mama Dominick ambaye alikuwa ni mjane.
Kwa kipindi cha miaka yote hiyo sikufahamu ni nini kilichokuwa kikiendelea katika maisha yake, nilimsusa kwa kiasi kikubwa sana na kwa kile kilichokuwa kimetokea katika ndoa yangu nilianza kuukumbuka uwepo wake, niliamini alikuwa na maneno mengi sana ya kunieleza mimi mwanaye.
“Nataka nijiandae niende zangu kazini,” aliniambia Julieth kisha akafanya kama alivyoniambia.
Bado nilizidi kuwa katika kiza kinene na sikujua ni nini kilichokuwa kikiendelea nyuma ya pazia.
“Julieth embu naomba tuzungumze kuhusu hili suala kabla hujaondoka,” nilimwambia alipomaliza kujiandaa na kwa wakati huo alikuwa anataka kuondoka.
“Nina haraka zangu please naomba tutazungumza nikirudi,” aliniambia huku akiitazama saa yake ya mkononi kuashiria alikuwa amechelewa.
“Dakika chache nipe ili niweze kuzungumza na wewe,” nilimwambia.
“Kwa sasa sina muda huo nina haraka labda tufanye kesho,” aliniambia.
“Kwanini hutaki kunisikiliza.”
“Sio sitaki tatizo lako sio muelewa,” aliniambia kisha akaondoka bila hata kuniaga.
****
Mateso ambayo nilikuwa nikiyapata kwa kweli siwezi kuyasimulia, nilianza kuwa mvivu katika kufanya kazi zangu hata katika biashara ya kuuza mitumba nilianza kuwa mtu wa kupata hasara kila kukicha, hilo lilimshangaza Chrispine ambaye yeye kwa wakati huo mambo yake yalikuwa mazuri tu.
“Una nini wewe?” aliniuliza siku moja alipoanza kuona tofauti.
“Mbona nipo kawaida hakuna kitu,” nilimjibu.
“Hapana kuna kitu sio bure unajua siku hizi sikuelewi kabisa maana hata katika biashara umekuwa ni mtu wa kuambulia hasara kuna nini?”
“Chrispine.”
“Niambie.”
“Kuna vitu sivielewi kwa mke wangu.”
“Vitu gani hivyo.”
“Unajua mpaka sasa nahisi nipo njia panda.”
“Kwanini?” aliniuliza.
Nilianza kumsimulia kila kitu kilichokuwa kimetokea mpaka kufikia hatua mke wangu kumiliki gari ambalo hakuniambia lolote zaidi ya ugomvi na kunionyesha dharau.
“Ndugu yangu pole sana,” aliniambia.
“Bado sijapoa.”
“Piga moyo konde ndugu yangu.”
“Nashindwa kufanya hivyo Chris kiukweli nashindwa yani mpaka sasa sijui ni nini kinachoendelea.”
“Vipi kuhusu mwanao?”
“Hafahamu lolote na sitaki kwanza hafahamu.”
“Ndugu yangu ukisikia kua uyaone ndiyo haya, sasa hapa itabidi uanze kumchunguza mkeo ili ujue ni nini kinachomchanganya maana ukiendelea kuwaza mwisho wa siku utavuruga kila kitu.”
“Nitaanzia wapi?”
“Jifanye mjinga muache akutawale ila inabidi uishi kiakili ukiendelea kumsoma naimani mwisho wa siku utafahamu kila kitu.”
“Sijui kama nitaweza Chrispine unajua mpaka nimemkumbuka sana Mama yangu.”
“Ni lazima umkumbuke hasa kwa hili lililotokea lakini unajua wanawake ni viumbe wa ajabu sana,” aliniambia Chrispine huku akionekana kusikitishwa na kile kilichonitokea.

Je, ni nini kitaendelea?
 
JUMA HIZA
PENZI LILILOSABABISHA MAUTI-11
Based on True Story.
0712988278

ILIPOISHIA....

“Sijui kama nitaweza Chrispine unajua mpaka nimemkumbuka sana Mama yangu.”
“Ni lazima umkumbuke hasa kwa hili lililotokea lakini unajua wanawake ni viumbe wa ajabu sana,” aliniambia Chrispine huku akionekana kusikitishwa na kile kilichonitokea.

SONGA NAYO.....

Nilishindwa kuelewa ni kitu gani nilitakiwa kufanya kwa mke wangu, alibadilika ghafla! na sikufahamu ni nini kilisababisha mpaka akawa katika hali ile.
Mwanzoni nilionekana kuipenda kazi ya mke wangu kwasababu nilishikiri kwa kiasi kikubwa katika kumsomesha mpaka kufikia hatua akapata kazi na miezi mitatu kupita baada ya kupata kazi ndipo mabadiliko yalipoanza.
Niliporudi nyumbani sikuweza kupata usingizi kabisa muda wote nilikuwa nikiifikiria ndoa yangu ambayo ilikuwa imeshaingia doa. Nilimtazama mwanangu Glory kama mboni yangu muda wote yeye ndiye alikuwa mfariji wangu kwa wakati ule.
Kuna kipindi kilifika Mke wangu akaanza tabia ya kutorudi nyumbani, hilo lilizidi kuniumiza sana na nilipomuuliza siku iliyofuata aliporudi nyumbani alidai kuwa amechoka na kazi yake ya utangazaji hivyo nimuache apumzike.
Wimbi la mawazo lililoambatana na upepo wa upweke ukanipitia, nilikuwa mnyonge mithili ya mkiwa. Sikuweza kufanya kazi, sikuweza kula, sikuweza kupata usingizi muda wote nilikuwa nikimuwaza mke wangu. Ama kwa hakika ndoa iikuwa imeniweka mahali pabaya sana. Nilishindwa kuwaza na kuwazua lolote.
“Baba mbona una mawazo, una waza nini?” lilikuwa ni swali la mwanangu Glory aliloniuliza usiku mmoja ambao Mama yake hakuwa amerudi nyumbani.
“Hakuna kitu mwanangu nipo sawa, enhee! Halafu hujaniambia leo shuleni mmejifunza nini?” nilimjibu kisha nikamuuliza swali la kuzuga.
“Tumejifunza jinsi ya kumpa huduma ya kwanza mgonjwa aliyezimia.”
“Unajua ni hatua gani muhimu ambayo anatakiwa kufanyiwa?”
“Anatakiwa kupata hewa nyingi hivyo mwalimu ametufundisha inabidi tuhakikishe amepata hewa ya kutosha.”
“Vizuri sana mwanangu bila shaka umelielewa vyema somo hilo.”
“Ndiyo Baba halafu wiki ijayo tunaanza kufanya mitihani ila Baba nataka likizo niende nikamsalimie Bibi,” aliniambia Glory maneno ambayo yalinishtua sana. Kwa umri aliyokuwa nao sikutaka kuamini kama aliweza kukumbuka uwepo wa Bibi yake ambaye hakuwahi kumuona hata mara moja.
“Usijali nitakupeleka mwanangu,” nilimwambia.
Sikumaanisha kile nilichokizungumza bali niliamua kumwambia maneno hayo kama kumdanganya kwa kumridhisha ili asiendelee kunisumbua.
“Baba mbona Mama hajarudi?” aliniuliza tena swali lingine lililoniweka katika hasira kali mno, kutokana na hasira nilizokuwa nazo nikajikuta nampiga kibao mwanangu na kuanza kumtolea maneno makali ya kumfokea juu ya maswali yake yasiyokuwa na vichwa wala miguu.
Alianza kulia huku akilitaja jina la Mama yake, nikapata kazi ya kumbembeleza, hakuweza kunyamaza kirahisi na kila nilipokuwa nikijaribu kumbembeleza alizidi kulia huku akilitaja jina la Mama yake.
“Julieth kwanini unanifanyia haya lakini?” nilijiuliza kwa ghadhabu.
Usiku huo ulikuwa ni wa kilio kwa mwanangu Glory pamoja na maumivu kwa upande wangu, nilijiona kuchanganyikiwa kwa maamuzi ya kukurupuka niliyokuwa nmeyachukua. Hata nilikuwa sielewi ni nini nilichokuwa nakifanya. Siku hiyo ikapita.
****
Siku iliyofuata niliweza kumuomba msamaha mwanangu kwa kosa la kumpiga usiku wa siku iliyopita, hakuwa amenikosea bali nilikuwa katika hasira. Kwa kumdanganya ilinibidi nimpe noti ya shilingi elfu mbili nikamwambia ilikuwa ni zawadi yake na hakutakiwa kunichukia mimi Baba yake ambaye nilikuwa nampenda sana.
“Mama yuko wapi?” aliniuliza.
“Mama leo atarudi jana alibanwa na kazi halafu ameniambia akirudi atakuletea zawadi,” nilimwambia.
“Baba kweli?” aliniuliza
“Ndiyo mwanangu,” nilimjibu.
Nilimwambia ajiandae ili aweze kwenda shuleni kisha akafanya kama nilivyomwambia na baada ya kumaliza kujiandaa nilimwandalia chai akaweza kwenda shule.
Akaniacha na upweke kama ilivyokuwa kawaida yangu, nikaendelea kuiwaza ndoa yangu jinsi ilivyokuwa ikielekea mahali pabaya.
Nilimpigia simu Chrispine kisha nikamueleza kuwa sikuwa sawa kwa siku hiyo hivyo nisingeweza kutoka kwenda mahali popote pale, nikajaribu kumpa maelekezo ya kunisaidia mambo mawili matatu ya juu ya biashara zangu.
“Sawa nitafanya kama ulivyoniambia ila Dominick ndugu yangu mapenzi yasikupeleke puta kiasi hicho yani imefikia hatua mpaka kutoka unashindwa?”
“Nahisi kichwa kinaniuma Chrispine sipo sawa kabisa.”
“Ndugu yangu una matatizo makubwa embu jioni fanya tuonane tuzungumze kitu,” aliniambia Chrispine.
“Sawa,” nilimjibu kisha nikakata simu.
Tangu Chrispine aliponiambia nianze mpango wa kumfuatilia mke wangu ili niweze kufahamu ni nini kilichokuwa kinaendelea nyuma ya pazia kwa kweli nilishindwa kufanya hivyo. Niliamini kuwa endapo ningeweza kumchunguza na kufanikiwa kufahamu kitu kilichokuwa nyuma ya pazia hakika nilikuwa nikishiriki katika mpango wa kuupondaponda moyo wangu kutokana na maumivu makali ambayo ningeweza kuyapata.
Jioni ya siku hiyo mara baada ya Glory kurudi kutoka shule nilihakikisha amekula kabisa, ameandaa nguo zake za shule kisha nikaweza kumuaga huku nikimuahidi kuwa sitachelewa kurudi nyumbani.
Nilienda kukutana na Chrispine Magomeni Mikumi katika baa moja iliyojulikana kwa jina la Deluxe Bar. Tulipokutana niliagiza bia aina ya Grant’s kitendo ambacho kilimshangaza sana Chrispine. Yeye aliagiza soda na baada ya kuhudumiwa na muhudumu mazungumzo yetu yalianza.
“Unakunywa pombe siku hizi?” aliniuliza.
“Ndiyo nakunywa,” nilimjibu.
“Unajua umebadilika sana,” aliniambia.
“Nadhani unajua sababu iliyosababisha mpaka nimekuwa hivi,” nilimwambia.
“Kwanza umeanza kutekeleza kile nilichokuambia?” aliniuliza.
“Kitu gani?”
“Kumchunguza mkeo.”
“Hapana.”
“Kwanini?”
“Nimeshindwa kufanya hivyo Chris.”
“Unapoelekea ni mahali pabaya inabidi ujitoa kiume upambane mpaka ujue ni nini kilichomsibu mkeo.”
“Hivi kwa hapa nilipofikia unadhani nitaweza kweli?”
“Kwanini ushindwe Dominick ni mambo mangapi umeweza kuyafanya katika maisha yako ukayafanikisha kwanini hili jambo dogo la kumchunguza mkeo ushindwe?”
“Sitaki kufanya huo ujinga hata mara moja,” nilimwambia kwa ukali kisha nikaanza kunywa pombe kwa pupa mithili ya mtu aliyekuwa na kiu kikali, nilikunywa pombe zisizokuwa na idadi mpaka nikapoteza fahamu.

Je, ni nini kitaendelea?
 
JUMA HIZA
PENZI LILILOSABABISHA MAUTI-12
Based on True Story.
0712988278

ILIPOISHIA....

“Kwanini ushindwe Dominick ni mambo mangapi umeweza kuyafanya katika maisha yako ukayafanikisha kwanini hili jambo dogo la kumchunguza mkeo ushindwe?”
“Sitaki kufanya huo ujinga hata mara moja,” nilimwambia kwa ukali kisha nikaanza kunywa pombe kwa pupa mithili ya mtu aliyekuwa na kiu kikali, nilikunywa pombe zisizokuwa na idadi mpaka nikapoteza fahamu.

SONGA NAYO.....

Nilipata fahamu na kujikuta nipo ndani ya chumba kimoja, nilikurupuka na kushangaa mahali pale nilifikaje. Kumbukumbu zangu za mara ya mwisho nilikumbuka nilikuwa baa na Chrispine tukizungumza na baada ya hapo sikukumbuka tena kitu kilichoendelea. Kichwa kilianza kuniuma, nilipoamka nilijihisi kuwa mzito sana. Nilipokuwa nikiendelea kujiuliza maswali yalikosa majibu mara Chrispine akaingia ndani.
“Hapa nimefikaje Chrispine?” nilimuuliza Chrispine alipokuja na kukaa pembeni yangu.
“Ina maana unataka kuniambia umesahau kila kitu kilichotokea jana?” aliniuliza.
“Sikumbuki ila si tulikuwa baa?” nilimuuliza.
“Sema tulikuwa baa,” aliniambia.
“Mbona nipo hapa nyumbani kwako?”
“Ushukuru ulikuwa na mimi sijui kama ungekuwa peke yako ingekuwaje?”
“Kwanini?”
“Dominick embu acha kujitoa ufahamu ina maana unataka kuniambia umesahau kila kitu kilichotokea jana?”
“Sikumbuki kweli.”
“Ok, jana ulikunywa sana pombe mpaka ukapoteza fahamu,” aliniambia Chrispine kisha nikakumbwa na bumbuwazi.
Nilihisi kama hakukuwa na ukweli katika yale aliyokuwa akinieleza, nikabaki nikiendelea kumkodolea macho huku nisiwe na la kusema. Yaani mapenzi yalikuwa yamenichanganya mpaka nikafikia hatua ya kunywa pombe, sikutaka kuamini kabisa.
Niliingiwa na hofu nilipomkumbuka mwanangu Glory, sikujua alikuwa katika hali gani, nilikumbuka siku iliyopita nilimuahidi kutoka na kutochelewa kurudi matokeo yake niliamka katika siku nyingine tena nikiwa nje na nyumbani kwangu.
“Sijui Glory atakuwa salama?” nilimuuliza.
“Kwani ulimuacha na nani?”
“Peke yake.”
“Mama yake hakurudi?”
“Sijui kama alirudi,” nilimjibu Chris kisha akatikisa kichwa chake, alionekana kunihurumia sana, kila alipokuwa akinitazama alizidi kunionyesha sura iliyogubikwa na masikitiko makubwa.
“Dominick hivi utaendelea kuishi maisha haya mpaka lini?”
“Sijui Chris, sijui kwa kweli.”
“Unajua nahisi kama nimekukosea sana.”
“Kwanini?”
“Nakumbuka mimi ndiyo mtu ambaye nilikuwa kipaombele sana katika kukushauri na kukupigania katika mahusiano yako hata hii ndoa yako mimi ndiye niliyekushauri umuoe huyu mwanamke, najua kwa mateso unayoyapita hivi sasa ni lazima utafika muda utanichukia ni lazima unichukie maana hata huyu mwanamke amesababisha mpaka umegombana na Mama yako,” aliniambia Chris.
Maneno ya Chris yalizidi kuniumiza sana, nilikumbuka mambo mengi ambayo yalitokea katika maisha yangu, jinsi ambavyo nilipigana kiume mpaka nikahakikisha nafanikiwa kumuoa Julieth japo alisababisha mpaka nikagombana na Mama yangu lakini hilo sikutaka kujali.
Licha ya mapenzi yote ambayo nilimuonyesha na kumthamini kama mke wangu wa ndoa lakini ghafla! alikuja kubadilika. Alibadilika katika kipindi ambacho nilikuwa nampenda sana, sikutarajia kama angeweza kubadilika katika kipindi kile nilichokuwa namuhitaji zaidi.
Sikutaka kuweka mlolongo mrefu wa mazungumzo kati yangu na Chrispine, aliponiambia kuwa alikuwa akinionea huruma kwa yale yaliyokuwa yakinitokea nilimwambia asijali hivyo abaki na amani, niliamini kile kilikuwa ni kipindi cha mpito na muda wowote kingeweza kufika mwisho.
Nilimuaga Chrispine kisha nikaondoka kuelekea nyumbani kwangu, barabarani nilikuwa mwingi wa mawazo sana, kuna muda nilikuwa nikiongea peke yangu kama mwendawazimu.
Nilipofika nyumbani nje nililiona gari alilodai mke wangu kuwa ni lake, nikalitazama kwa muda wa sekunde kadhaa kisha nikaingia ndani, nikamkuta mke wangu akiwa amekaa sebuleni, alionekana kunisubiri kwa hamu kubwa sana. Wakati huo Glory alikuwa ameshaenda shule.
“Umetoka wapi?” bila hata salamu aliniuliza huku akiwa ameikunja sura yake kwa ghadhabu.
“Bila hata salamu mke wangu?” nilimuuliza kwa sauti ya upole.
“Salamu ya kazi gani sasa au itakusaidia nini, nimekuuliza umetoka wapi?” aliniuliza.
“Nimetoka kwa Chris,” nilimjibu.
“Kwa Chris?” aliniuliza.
“Ndiyo,” nilimjibu.
“Kwahiyo unataka kuniambia jana umelala huko huko?”
Kila swali nililokuwa nikimjibu mke wangu nilimjibu kwa sauti ya upendo lakini nilishagazwa na muonekano wake, alionekana kutawaliwa na hasira na yote ilisababishwa na kutorudi kwangu nyumbani, nilipomuuliza kuhusu mwanangu Glory alishindwa kunijibu alikuwa shule mwisho tukaingia katika ugomvi.
Alidai kuwa amenichoka na hivyo hakutaka kuendelea na mimi tena, kama ni ndoa basi ule ndiyo ulikuwa mwisho wake wa uvumilivu. Hakutaka kuendelea kuumiza akili yake juu ya vitu ambavyo havikuwa na msingi katika maisha yake.
Sio siri nilishangazwa na maamuzi aliyokuwa ameyachukua mke wangu, nikazidi kumuona kuwa mwanamke wa tofauti sana hasa ukilanganisha muonekano wake, kazi yake pamoja na mambo aliyokuwa akiyafanya vilikuwa ni vitu viwili tofauti.
Kwakweli nilizidi kuchanganyakiwa kutokana na uamuzi aliyokuwa ameuchukua mke wangu, nilikuwa nampenda sana japo alianza kunifanyia visa lakini sikutaka kuupunguza upendo niliyokuwa nao kwake. Kwa wakati ule ambapo alikuwa ameniambia amenichoka na kutaka tuachane nilijaribu kumsihi asichukue maamuzi hayo kwani tayari tulikuwa tumejaaliwa kupata mtoto katika maisha yetu na alikuwa akitutegemea kwa kila kitu, sikutaka Glory apoteze muelekeo wa maisha yake baada ya kuachana kwetu, nikajaribu kumsihi mara mbilimbili asichukue uamuzi huo mgumu ambao ungeweza kumuathiri kisaikolojia.

Je, ni nini kitaendelea?
 
JUMA HIZA
PENZI LILILOSABABISHA MAUTI-13
Based on True Story.
0712988278

ILIPOISHIA....

Kwa wakati ule ambapo alikuwa ameniambia amenichoka na kutaka tuachane nilijaribu kumsihi asichukue maamuzi hayo kwani tayari tulikuwa tumejaaliwa kupata mtoto katika maisha yetu na alikuwa akitutegemea kwa kila kitu, sikutaka Glory apoteze muelekeo wa maisha yake baada ya kuachana kwetu, nikajaribu kumsihi mara mbilimbili asichukue uamuzi huo mgumu ambao ungeweza kumuathiri kisaikolojia.

SONGA NAYO......

“Tafadhali mke wangu naomba usichukue uamuzi huo, mimi bado nakupenda sasa kwanini unataka kunipa hukumu nisiyoistahili?” nilimuuliza kwa sauti ya kulalamika, nilikuwa nikiyalalamikia mapenzi ya mke wangu na kwa wakati huo hakuonekana kujali, alikuwa amenikinai.
“Sitaki Dominick naomba tuachane nimekuchoka,” aliniambia huku akinionyesha hasira za waziwazi.
Kuna wazo lilinijia kichwani na nilihitajika kulifanyia kazi kwa wakati huo ili kuinusuru ndoa yangu ambayo ilikuwa inaendea kuangamia.
MSAMAHA hili ndilo wazo lililonijia kichwani kwa wakati huo, nilichoamua kukifanya ni kuanza kumuomba msamaha mke wangu. Niliamua kufanya hivyo ilimradi amani ya mapenzi yetu ya ndoa irejee kama hapo awali lakini naweza kusema haikuwa kama nilivyodhani.
****
Huo ndiyo ukawa mwanzo wa kuyapokea maumivu mengine yaliyouumiza moyo wangu wa mapenzi, Julieth aligeuka kuwa ncha ya kisu kikali na kisha akawa ananichomachoma moyoni mwangu. Nilikuwa nikiyapokea maumivu makali ambayo sikuyatarajia katika maisha yangu. Hatimaye ya mapenzi niliyoyafananisha na simulizi nzuri ya kimapenzi iliweza kugeuka kuwa simulizi ya kusikitisha.
Kipindi ambacho Julieth alikuwa amebadilika na kuwa mbogo ndani ya nyumba nilianza kuyasikia maneno ya chinichini ya watu wakisema alikuwa akitembea na wanaume mbalimbali wenye pesa ambao ndiyo walikuwa wakimuhonga magari pamoja na pesa.
Sikutaka kuamini macho yangu pale nilipoziona picha za Julieth mitandaoni akiwa kitandani na mwanamuziki maarufu wa nyimbo za bongo fleva aliyekuwa akijulikana kwa jina la Gibson David lakini jina la kisanii alikuwa akitumia “G Malove”.
Nilihisi kuchanganyikiwa baada ya kusikia Julieth alikuwa katika mahusiano ya kimapenzi na Gibson na kibaya zaidi alikuwa ana ujauzito wake. Maumivu hayakuishia hapo tu, Mwanamuziki huyo alimpangia nyumba pamoja na kumfungulia biashara mbalimbali mke wangu.
Kilichokuwa kimetokea katika maisha yangu kilimsikitisha sana rafiki yangu Chrispine, alinionea huruma sana kutokana na madhila niliyokuwa nimeyapata.
Hakutaka kuamini kama Dominick niliyekuwa nikiishi maisha ya kuifurahia ndoa yangu wakati huo nilikuwa nikiteseka, nikinyanyasika, nikiumizwa na ndoa yangu.
Ulifika wakati nilikosa mtetezi wa kunitetea si kwa Chrispine tu! bali hata kwa upande wa Mama yangu mzazi hatukuwa na mawasiliano mazuri, tuligombana na sababu kubwa alikuwa ni mke wangu.
“Hutakiwi kuendelea kuwa mnyonge inabidi ufanye maamuzi katika hili,” aliniambia Chrispine.
“Hivi kweli mke wangu anaweza akanifanyia unyama huu?” nilimwambia Chrispine kisha nikamuuliza swali ambalo lilinifanya nidondokwe na machozi, nilikumbuka mambo mengi niliyowahi kuyafanya kwa mke wangu lakini yalionekana kuwa ni bure, hayakuwa na faida yoyote kwa wakati huo.
“Najisikia vibaya sana ndugu yangu najua unapitia katika wakati wa maumivu kiasi gani lakini huna budi kukubaliana na hali halisi, yule mwanamke ni muuaji kweli, hana utu kabisa,” aliniambia Chrispine.
“Lakini angeniambia mapema kuwa amenichoka, nimewekeza dhamana ya upendo, uvumilivu na kujitoa lakini mwisho wa siku amekuja kunilipa maumivu, amenilipa dharau nadharaulika mimi kila kona, naonekana labda pengine simridhishi mke wangu na ndiyo sababu amenisaliti,” nilimwambia Chrispine huku machozi yakiendelea kunibubujika mashavuni mwangu.
“Usiseme hivyo,” aliniambia Chrispine.
“Kwanini anasahau wema wangu wote niliyomtendea katika maisha yake, kwanini anasahau kwamba tuna mtoto mdogo ambaye anatutegemea, kwanini anachukua kunipa hukumu hii? Anasahau kuwa yeye ndiyo chanzo cha mimi kugombana na Mama yangu, kwanini amesahau mapema kiasi hiki?” nilimuuliza Chrispine huku nikiendelea kudondokwa na machozi mfululizo.
Nililia sana, niliumia mno wala maumivu yangu sidhani kama kulikuwa kuna mtu wa kuyatibu kwa wakati ule. Nilitokea nikayachukia mapenzi, nikayawekea uadui mkubwa mno.
Niliyekuwa namsikia akiyasifia mapenzi nilimuona kuwa kipofu asiyeona mbele ni kitu gani kilichokuwa kinakwenda kumtokea, mimi nilikuwa mfano bora wa kuwasimulia yale yaliyowahi kunikuta katika maisha yangu, nilikuwa kipofu wa mapenzi.
Nakumbuka nyumba niliyopanga kujenga kisirisiri, ilinishinda mwisho wa siku nikaamua kuiuza.
****
Baada ya mambo yote hayo kutokea katika maisha yangu niliamua kwenda nyumbani kwa Mama yangu kwa lengo kwa kuomba msamaha. Nilichokutana nacho baada ya kwenda nyumbani kwa Mama yangu huku nikiwa na mwanangu ni kaburi ambalo niliambiwa alizikwa hapo miaka miwili iliyopita.
Kiukweli sikutaka kuamini kwa kile nilichokuwa nikielezwa na majirani, nilihisi kuchanganyikiwa, hakukuwa na kitu kingine zaidi ya machozi ya uchungu, nilimlilia Mama yangu ambaye alikufa bila kusema neno lolote na mimi, alikufa huku akiwa ananichukia, niliumia mno.
****
Niliporudi nyumbani kwangu sikuonekana kuwa mwenye furaha hata kidogo, nilikuwa mnyonge sana na kila wakati taswira ya kaburi la Mama yangu ilikuwa ikinijia kichwani.
Sijui niseme nini ila naweza kusema nilichanganyikiwa na kila nililokuwa nalifanya haikuwa ni akili yangu kwa wakati huo.
Usiku wa siku hiyo mke wangu hakurudi tena nyumbani, nikabaki nikitabasamu huku nikiamini alikuwa na huyo mwanamuziki wake.

“Kwako Chrispine,

Najua utashtushwa na aina ya maamuzi ambayo nimeamua kuyachukua, sina maana kwamba nimeshindwa kuyavumilia hapana ila imebidi iwe hivi.
Najisikia kufanya mauaji na sitaki kusabababisha mauaji kwa damu isiyokuwa na hatia. Najiona nikielekea mahali pabaya sana na hakuna wakunisaidia.
Nimeteseka sana katika kupigania maisha ya mke wangu lakini mwisho wake amekuja kunilipa zawadi ya maumivu, amenipa jeraha la mapenzi na sijui kama nitaweza kupona.
Najua nitaishangaza dunia kwa maamuzi yangu haya ninayokwenda kuyachukua lakini kabla sijayachukua naomba uyafanyie kazi haya nitakayokuandikia.
Hakikisha unasimamia vyema biashara zangu, hakikisha unabaki na mwanangu Glory, naamini ninamuacha katika mikono salama.
Nachukua maamuzi ya kujiua lakini nitakapokufa hakikisha nazikwa pembeni na kaburi la Mama yangu pengine kwa kufanya hivyo nitapata wasaa wa kuzungumza naye na kumuomba msamaha kwa mara nyingine. Atanisamehe.
Maiti yangu chonde tafadhali hakikisha mke wangu haisogelei, sitaki tukio hili litokee katika msiba wangu kwa maana yeye ndiyo chanzo cha yote haya na kama utapata bahati ya kuisoma barua hii basi usiache kumwambia mke wangu kuwa nakufa huku nikiwa namchukia sana.”
Ilikuwa ni barua iliyoambatana na simulizi ya maisha aliyoiandika Marehemu Dominick, kila mtu alisikitishwa na kifo chake alichokisababisha mwenyewe.
Aliamua kujiua kwa kujichoma na kisu tumboni. Kifo chake kilisababishwa na MAPENZI.
MWISHO.
 
Mapenzi ukiyaendekeza yanakupelekesha.hadithi nzuri ila sikupenda kuamua mwisho kujiua. Unajikomoa mwenyewe
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom