Njia nyembamba (Simulizi mpya by SteveMollel)

*Njia nyembamba -- 23*



*Mtunzi: SteveMollel














Kone hakuwa na la kusema, akabeba mafaili, yeye pamoja na Rose wakatoka kwenye gari la Amadu na kwenda kwenye usafiri waliokuwa nao. Wakajiweka ndani na kuwa na maongezi mafupi kabla hawajatia moto chombo.


"Kone, hawa watu wanatisha," alisema Rose. "Kwa muda gani na kivipi wameweza kufanya haya?"
"Sina jibu, Rose, ila ninawaamini," alijibu Kone. "Wana utashi mkubwa wa kazi. Wana ujuzi wa kufanya kazi zao vizuri sana. Bila shaka wakidhamiria hili litafanikiwa."
"Utaungana nao?"
"Sijajua bado. Ila pia sina sababu ya kunifanya nisijiunge nao. Nafikiri nitapata jibu mujarab nikipitia haya mafaili."
"Natamani uyapitie pamoja nami, kama hautojali lakini."
"Hamna shida, mimi mwenyewe ningependekeza iwe hivyo."
"Tutafanya hilo zoezi lini?"
"Tufanye kesho mapema. Leo hii acha nirudi kwa mke wangu, atakuwa ananingoja."
"Naomba basi unipitishe nyumbani."
"Bila shaka."


Kone akampitisha Rose kwenye makazi yake kisha akaelekea nyumbani. Akamkuta mkewe na watoto wameketi mahala pa kulia chakula. Mwanamke alikuwa amevalia gauni jepesi rangi ya bluu, nywele zake zilikuwa zimefumwa vema kuthibitisha ametoka saluni.


Kone akaketi na kuungana na familia. Muda mfupi watoto wakaondoka kwenda kupumzika na kuwaacha wazazi peke yao mezani.


"Haki umependeza," Kone aliwasilisha pongezi zake kwa mkewe. Mke, bi Fatma, akatabasamu kifupi.
"Ahsante mpenzi," akajibu na kuendelea kula. Punde akamtazama mumewe kama mtu aliyekumbuka jambo.
"Umesikia kilichotokea Guinea?" Akauliza. Kone akatikisa kichwa akiubinua mdomo.
"Hapana, kuna nini?" Akauliza upesi. Macho ya bi Fatma yalikuwa yanaonyesha habarize si njema, na hilo likapelekesha puta moyo wa Kone kwa muda.
"Nimeona kwenye taarifa ya habari muda si mrefu, mke wa marehemu Raisi ameuawa."


Kone akakunja usowe.


"Mama Angela?"
"Ndio. Ameuawa kwa kupigwa risasi ya kichwa na watu wasiojulikana."
"Kuna madai yotote wameyaeleza juu yake?"
"Hapana." Bi Fatma akatikisa kichwa. "Nilichosikia cha ziada ni kwamba alikuwa amepanga kugombea kiti alichokiacha mumewe."
"Kupitia chama gani?"
"Hicho hicho cha mumewe. Alishaanza kampeni na mipango ya chini kwa chini kusaka kiti hicho. Inasemekana ni chama ndicho kilimshawishi agombee."


Kone akatekwa na mawazo. Kwanini mauaji hayo yatokee? Kuna nini nyuma ya pazia? Hili jambo linaweza likasisimua kulipuka kwa vita. Hakupata hamu ya kula tena.


Akachoropoa simu yake afanye mawasiliano, akakuta ujumbe. Alishangaa umeingia muda gani kwani hakupata kuusikia wala kuuhisi. Alitazama kiooni akaona namba ngeni aliyoing'amua ni ya Amadu. Haraka akafungua ujumbe huo.


"Kadiri tutakavyokawia, ndivyo mauaji yatakavyotokea," ujumbe ulisomeka hivyo. Haraka, Kone akauitikia ujumbe huo kwa kuuliza:
"Unawajua waliohusika na tukio hilo?"


Punde akajibiwa: "Pitia mafaili niliyokupa."


"Vipi mpenzi, kuna tatizo?" Bi Fatma aliuliza. Kone akapachika tabasamu usoni mwake upesi.
"Hamna tatizo, mpenzi."
"Unandanganya."
"Kweli hamna tatizo."
"Tafadhali, usianze kuwaza na kuwazua ya Guinea."
"Usijali, mpenzi. Sitafanya hivyo."


Bi Fatma akanyanyuka na kumpoka mumewe simu. Akaiweka mezani na kisha akamkalia mapajani kama vile mwanaume apandavyo bodaboda.


"Leo zamu yangu," akasema bi Fatma. "Leo zamu yangu na mimi unifikirie, na utibu matatizo yangu."


Kone akatabasamu. Akamnyanyua mkewe na kumpeleka kitandani. Akamvua nguo na kumpeleka bafuni. Walipotoka wakarejea tena kitandani.


Mwanaume akajitutumua kumfurahisha mkewe. Alimshika na kumgusa kila kona tata ya mwili. Alisimamia huduma yake kadiri ya uwezowe, ila bado maji yakazidi unga. Hakuweza.


Akili yake haikuwa kitandani, bali Guinea. Kila alipojitahidi kuihamisha ilishindikana. Alikuwa anawaza mambo lukuki, muhimu na nyeti.


Akajilaza pembeni akitazama dari.
"Nini shida, Kone?" Bi Fatma aliuliza. Aliweka mkono wake juu ya kifua cha mumewe.
"Siko sawa, kuna mambo yananitatiza," Kone akajibu. Akashusha pumzi mdefu kisha akailaza mikono yake na kuilalia kama mto.
"Niambie basi nini kinakusumbua."


Kone akaona huo ni wasaa wa yeye kueleza kinaganaga. Endapo angesema ni kuhusu Guinea, kifupi hivyo, basi Fatma angekasirika kwani aliomba siku hiyo apewe zamu.


"Unamkumbuka Amadu - yule jamaa niliyekuwa nakuambia kuhusu Sierra Leone?"
"Yule aliyewahi kuwa kwenye kundi la waasi?"
"Ndio. Leo nilikutana naye baada ya muda mrefu sana. Kuna baadhi ya vitu aliniambia, na vina mahusiano na kifo hiki cha mke marehemu Raisi."


Kone akamwambia mkewe kuhusu mafaili, ila hakuthubutu kumueleza kwamba naye alikuwa anahitajika kwenye vita hiyo, aliona kitasababisha mkewe akose amani na furaha.


"Kesho nitayapitia vizuri hayo mafaili. Kuna mambo kedekede yatakuwa yameainishwa, nyeti na yenye tija. Haya mambo ni makubwa."
"Kone, lakini haya mambo yasitufanye tukasahau ndoa yetu," akashauri bi Fatma.
"Nitajitahidi mpenzi." Kone akajibu na kisha akazima taa.

***

"Ndio hapa," sauti ikasema ndani ya gari kubwa, Land Cruiser, lenye vioo vyeusi. Mara wakashuka wanaume wawili ambao hawakuwa wanaonekana vema kutokana na giza.
"Kwa sasa bado atakuwa hajawasili," Mmoja akasema akitazama saa yake ya mkononi.
"Kwahiyo sasa?" Mwingine akauliza.
"Twende tukaketi pale," mwenzake akajibu na kuongezea; "Nadhani hatutokaa muda mrefu."


Wakajongea mahali fulani palipokuwa pametulia. Palikuwa na viti na meza kadhaa. Muziki laini ulikuwa unapigwa. Hapakuonekana mtu yeyote akiwa hapo japokuwa ni usiku, pengine ni kwasababu ilikuwa ni siku ya kazi ama usalama haukuwa unaridhisha.


Wakaketi na mara mhudumu akaja. Wanaume hawa walikuwa wapya usoni. Walikuwa wamejazwa na ndevu wakivalia shati na suruali za kitambaa. Nyuso zao zilikuwa pole, makini.


Mhudumu alikuwa mwanaume mrefu aliyekuwa hajavalia vema. Shati lake jeupe lilikuwa limejikunja, na suruali yake nyeusi ya kitambaa ilikuwa ina vumbi vumbi.


"Naweza nikawasaidia?" Akauliza mhudumu.
"Tuletee maji makubwa," mwanaume mmoja akaagiza. Uso wake ulikuwa na vidotidoti na macho yake yalikuwa makubwa.


Mhudumu aliondoka kwenda kufuata alichoagizwa. Akawaacha wanaume wale peke yao.


"Endapo kama leo hatutampata, hatutaeleweka," akasema mwa aume mmoja.
"Ni kweli unachosema lakini tutafanyaje sasa. Ni kama vile jamaa huyu amejua janja yetu."
"Kabisa. Amekuwa sio wa kutulia eneo moja. Hili litakuwa eneo la tatu sasa, tunamuenendea na hatumpati. Tukimkosa hapa, sijajua tutampatia wapi tena."


Kukawa kimya kidogo. Wote macho yao yalikuwa yanatazama jengo fulani walilotegemea kumuonea mlengwa wao hapo.


Mlengwa huyu hakuwa mwingine bali bwana Richard. Mwanaume aliyeagizwa kuuawa na Talib baada ya kupewa maneno chokonozi na Rauli kuhusishwa na kifo cha Freeman.


Lakini jambo hili linageuka na kuwa mtihani mgumu. Mwanaume huyu amekuwa adimu mno kupatikana tofauti na ilivyodhaniwa kabisa. Amekuwa akihamahama makazi. Amekuwa si mtu wa kuonekanaonekana, na haya yalianza punde tu baada ya kifo cha Freeman, mwanzilishi wa oparesheni mwanzo, kati na mwisho ambayo haikufanikiwa kupiga hata hatua moja.


Kifo hicho kilimfamya Richard ahisi usalama wake utakuwa hatiani. Na kweli hisia hizi zikamlipa fadhila.


Wanaume hawa wawili walikuwa wamezunguka na sasa walikomea kwenye eneo la tatu kwa idadi. Kote huko walipeleleza na kuweka kajikambi ka' masaa lakini hawakuvuna kitu. Kwenye nyonga zao walikuwa wamebebelea bunduki ndogo, agizo walilopewa ni kuua tu!


Mhudumu alirejea akiwa amebebelea maji makubwa. Aliwagawia wateja wake kisha akachukua pesa na kuondoka. Wamaume wale wakajihudumia wakiendelea kungoja.


Wakiwa katika hilo zoezi, mhudumu aliwatazama, na katika hali ya umakini, akaingia ndani ya chumba kidogo kinachotunza vinywaji. Akatoa simu ndogo mfukoni mwake kisha akapiga.


"Halo! ... wengine wapo hapa, njoeni upesi!" Alinong'oneza. Alipomaliza, akarudisha simu mfukoni mwake kisha akatafuta mahali alipokuwa na fursa ya kuwaona wateja wake.


Haikupita muda mrefu wanaume wale wawili wakamuona mtu akijongea karibu na jengo walilokuwa wanalitazama. Haraka wakamalizia vinywaji vyao na kunyanyuka upesi. Wakaelekea kule walipoona jambo.


Wakachomoa bunduki zao na kuzikabia mikononi. Wakatembea haraka mno wakihakikisha macho yao hayabanduki kutazama mlango wa jengo wanaloliendea.


Huku nyuma mhudumu alitoka, akawa anatazama wanaume hao wakienenda. Wakati huo akiwa ameshikilia simu mkononi anaongea na watu kuwaelekeza.


Wanaume wale wakafika karibu na eneo husika. Wakajibanza mahali wasionekane. Walitazamana kupeana ishara, mmoja akaenda nyuma mwingine akabakia mbele.


Walifanya mambo hayo katika ukimya mno. Miguu yao haikuwa inatoa sauti na ilhali walitembea na kukimbia. Hii ilikuwa nafasi yao ya kumaliza kazi iliyowasumbua kwa muda, na hawakutaka kuichezea, maana walijua gharama yake.


Wakatulia kwa dakika kama mbili, kimya. Mara mlio wa risasi unavuma. Mlio huu ulitokea nyuma ya jengo. Mwanaume yule aliyekuwa mbele ya jengo akashtuka, hakujua hiyo risasi aliifyatua nani. Akapata hofu.


Alijaribu kusogea, mara akapunyuliwa na risasi ya sikio. Akashika sikio lake kwa maumivu. Hakukaa vema, risasi zikarushwa kumfuata kama mvua. Hakujua zinatokea wapi. Akajikuta anakimbia kuokoa uhai wake.


Akakimbia kufuata gari walilokuja nalo. Akafungua mlango na kuzama ndani. Kabla hajatia moto chombo, chuma cha risasi kikapasua dirisha la gari na kutoboa kichwa chake. Akafa papo hapo!


Dakika nne mbele, wakajongea wanaume kumi wakiwa wamebebelea bunduki. Miongoni mwa hawa wanaume kuna nyuso mbili tunazozifahamu. Nyuso hizi tulishawahi ziona kwenye mauaji ya Freeman.


Lakini zaidi yumo na yule mhudumu. Kumbe naye alikuwa ni miongoni mwa hawa watu na ndio aliokuwa anawasiliana nao. Kundi la waandamanaji waasi!


"Tutawaangamiza wote hawa!" Alisema mmoja. "Wanadhani wakiwaingiza watu wao mtaani hatutuwafahamu!"


Loh! Mpango wa Rauli ulianza kufeli.


Kuangamiza kikundi cha waandamanaji wa kiasi kwa kutumia wapelelezi mitaani, ilishaanza kubumburukiwa. Bahati haikuwa kwa wanaume hawa wawili wapelelezi, wakiwa wanamfuatilia Richard wakajikuta wanazama mikononi ya wauaji wengine.


Waandamanaji walikuwa wauaji. Wauaji wenye juzi na mtandao mpana. Hapakuwa salama kabisa.


Richard, akiwa hajui kama mapambano yaliyotukia yalikuwa yanamhusu yeye, akatoka ndani ya jengo lake. Akachungulia kama kuna watu. Alipoona ni shwari, akatoka upesi na kukimbia!




***

☆Steve
 
*NJIA NYEMBAMBA -- 24*







Majira ya saa nne asubuhi:


Pembezoni mwa barabara kuu ya lami, Kone na Rose wanakutana. Walikuwa na miadi hapo.


Kone alikuwa amebebelea begi kubwa la mkono mmoja. Rangi ya begi hili ilikuwa nyekundu. Alikuwa amevalia shati la mikono mirefu alilolikunja mikono pamoja na suruali nyeusi ya kadeti na raba nyeusi.


Rose alikuwa amejivesha suruali ya kubana, tisheti ya njano na viatu vyeusi vya kuchomeka. Nywele zake alikuwa amezibana vema, usoni akipaka wanja pekee.


Walibadilishana matabasamu, kisha pasipo kuongea wakaanza kujongea wakielekea kaskazini mwa barabara. Walitembea kidogo kabla hawajafika kwenye makazi ya Rose.


"Ungefika usingenikuta," Rose akasema akitabasamu.
"Ndio maana nikaamua kujiongeza, nikaona nikupigie simu kwanza."
"Umefanya jambo jema sana."
"Ila Rose hauogopi kutembea huko nje, tena ukiwa wazi hivyo?"
"Sina sababu ya kuogopa, Kone. Serikali kwa sasa ipo bize ikihaha kupambana na waandamanaji. Hawana muda nami."


Kone akatabasamu. Aliketi, Rose akaingia ndani kumletea sharubati baridi ya machungwa.


"Usiku huu ulikuwa mgumu sana kwangu," Kone alisema akiweka glasi mezani. "Sikulala kabisa, si umesikia juu ya kifo cha mke wa Raisi?"
"Ndio, nimesikia!" Rose alijibu akitoa macho ya staajabu. "Nani kamuua?"
"Majibu yapo humu." Kone akaonyeshea begi alilokuja nalo. "Tukipitia hizi faili, tutapata kujua ama kupata mwanga."


Wakiwa wanakunywa sharubati, wakaanza kukagua mafaili kwa kina, wakianza na la nyumbani: Guinea. Mcheza kwao hutunzwa, walisema waswahili. Macho yao yalizama ndani ya karatasi wakisoma maelezo.


Kitu cha kwanza kukiona kilikuwa ni picha ya marehemu Raisi. Picha hiyo ilikuwa pana, ilimuonyesha Raisi akiwa anatabasamu akikunjia mikono yake kifuani. Chini ya picha hiyo yaliandikwa maneno machache:


'Mtuhumiwa namba moja wa chuki za kikabila.'


Tuhuma hizi zilikuwa mpya mbele ya Kone na hata Rose. Siku zote hawakuwahi kumtuhumu Raisi wao kuwa daraja la chuki hatari za kimakabila. Walitazamana kwa macho ya pazo, kisha kwa sauti, Kone akasoma:
"Kwa takribani miaka miwili sasa tangu Raisi wa Guinea, akiwa kiongozi wa kundi la POWER lenye fanisi ya kuhakikisha kabila la Fula ama Fulani wanakuwa na kubakia madarakani.


Ndani ya mwaka wake wa kwanza kama Raisi, na pia kama kiongozi wa POWER, alisababisha mauaji ya wanaume wawili kwa majina Robert Diallo na Bala Musa. Robert alikuwa anafanya kazi huko Addis Ababa, Ethiopia Umoja wa mataifa Afrika, na Bala Mussa alikuwa akifanya kazi serikalini kama katibu mkuu wa wizara ya usalama na ulinzi.


Robert Diallo aliuawa kwa kupigwa risasi ya kifua na watu waliotuhumiwa kuwa majambazi. Lakini mazingira ya tukio hilo yanaonyesha watu hawa hawakuwa majambazi bali walitumwa kummaliza mtu huyu.


Ndani ya siku hiyo, tarehe 12 January mwaka juzi, majira ya saa nne usiku, Robert Diallo akiwa nyumbani, wanaume watatu walimvamia. Walikatisha uhai wake pasipo kuchukua chochote kile. Walipotea na hakukuwa na uchunguzi wala ufuatiliaji wowote uliofanyika ukizingatia nafasi kubwa aliyokuwa nayo huyo mhanga.


Mhanga wa pili, Bala Mussa, huyu aliuawa kwa kisingizio cha ajali. Akiwa ndani ya gari lake kurudi nyumbani, aligongwa na gari kubwa semi trella lililoacha njia yake na kumparamia. Inasemekana ni ajali ila kiuhalisia haikuwa hivyo.


Dereva alilaghai kwamba tairi lilipasuka hivyo akashindwa kumudu chombo, ila halikuwa kweli. Dereva huyu hakudhurika hata kiungo kimoja ukilinganisha na uharibifu wa gari lake ulivyotokea. Lakini zaidi hakuchukuliwa hatua zozote, ikiwemo kushtakiwa.


Dereva huyu ndiye tumembana, akatupa maelezo ya kweli. Tulimmaliza maana kama angeliendelea kuwa hai, basi angeliweza kusambaza habari juu yetu.


Tulifanya ukaguzi ndani ya nyumba yake, tukakuta kinyago cheusi chenye umbo la simba na bunduki aina ya SMG. Vitu hivi ndivyo vilisadikika kutumiwa na majambazi waliomuua Robert Diallo.


Mbali na hapo, Raisi wa Guinea akiongoza kundi lake la POWER, walikuwa wanakutana mara mbili ndani ya miezi sita. Wakijadili namna ya kuimarisha kabila lao na nguvu yao. Lakini pia wakifanya mambo katika namna ya kuficha kucha. Raisi hakuacha kuteua watu wa kabila zingine, lakini akifanya hivyo alihakikisha kwanza mtu huyo hatokuwa na madhara. Ama basi ni mtu wa karibu anayemjua nyendo.


Hili linajionyesha kwa rafiki yake mkubwa aitwaye Suma Yakuba, afisa wa ikulu, ambaye amefanikiwa kupumbaza umma juu ya ukabila wa serikali.


Uteuzi huu wa Yakuba haukuwa wa kukurupuka, la hasha, bali uliopangwa. Raisi alisoma na Yakuba shule moja tokea hatua ya awali mpaka walipokuja kutengana elimu ya juu. Huko kote walikuwa ni marafiki wa kutupwa.


Kwa lengo la kulaghai macho ya wananchi, Raisi akaufanya uteuzi wa Yakuba kuwa wa kwanza kabisa kabla ya yote. Tukio hilo likavuta hisia za watu kwa mtu wa kabila 'A' kumteua wa kabila 'Be' kwa kipaumbele namna hiyo.


Baada ya hapo kombe lilifunikwa, mwanakharamu akapita.


Endapo Raisi huyu angeendelea kuvuta hewa ya dunia, kusingewahi kuwa salama ndani ya Guinea. Watu wa Malinke wasingewahi kuwa salama salmini.


Sasa ameenda, ila POWER imebaki. Kundi hili kwa sasa limekaliwa na kiongozi mpya kwa jina Saikou Boubacar. Mtu huyu ni hatari sana kuliko aliyepita kwani hamini kwenye kula na kipofu.


Dalili ya hatari ilionekana kwenye msiba wa Raisi. Saikou Boubacar akiongozana na wenzake watatu hawakumpa mkono wa pole bwana Yakuba. Walimruka na kwenda kusalimu wengine. Pia wakajitenga wakiketi eneo lao la peke yao.


Bila shaka kwa minajili hii, tutaweza kushuhudia mauaji na uvunjifu mkubwa wa haki za binadamu siku za usoni. Endapo bwana huyu na kundile hawataangamizwa."


Kone aliweka kitu hapo kwa kushusha pumzi ndefu na kutazamana na Rose. Walilowanisha koo zao kwa sharubati kabla hajaendelea na kurasa ya pili ambapo kulikuwa kuna picha kadhaa za Saikou Boubacar, Yakuba na wahusika wengine wa kundi la POWER.


Zaidi ya hizo picha kukiwa na vipande vya magazeti vikonyesha picha ya Saikou Boubacar akikataa mkono wa Yakuba. Picha zingine zikimuonyesha Yakuba akiwa na marehemu Raisi maeneo kadha wa kadha matabasamu yakipendezesha nyuso zao.


Picha zingine za magazeti zikionyesha mabaki ya matukio ya ajali ya Bala Musa na mauaji ya bwana Diallo. Pia maelezo kadhaa ya mashahidi wa matukio.


"Ngoma hii ngumu," Rose akasema akitikisa kichwa.
"Ni kweli," Kone akaunga mkono hoja. "Ni kubwa kuliko ionekanavyo mbele ya macho ya kawaida. Kuna mizizi ya kukatwa, mti huu umekomaa."
"Nikuongezee kinywaji?" Rose alimhamishia Kone kwenye ulimwengu mwingine. Mwanaume huyo hakujua hata kama sharubati imeisha kwenye glasi. Alitazama glasi akaiona tupu, akatikisa kichwa akitabasamu.

"Nitashukuru."


Rose akanyanyuka na kwenda kwenye jokofu. Akafungua na kumimina sharubati baridi aliyomletea Kone mara moja.


"Karibu."
"Ahsante, Rose."


Kone akanywa fundo moja la nguvu.


"Unatengeneza mwenyewe hizi?" Akauliza punde aliposhushia glasi mezani.
"Ndio, natengeneza mwenyewe," Rose akajibu na kisha akauliza: "Vipi, umeipenda?"
"Sana, una mkono wa jikoni kweli."
"Ahsante, Kone."
"Na pia una mkono wa kutoa, maana yale matunda uliyojaza kwenye jokofu si mchezo."


Rose akaangua kicheko.


"Umejuaje kama kuna matunda mule?"
"Umesahau kitu cha kwanza kuniomba wakati tukiwa tunakuja eneo hili?"


Rose akajaribu kukumbuka. Mara akaangua kicheko.


"Nakumbuka. Nilikuomba unipe pesa ninunulie matunda."
"Na leo tumekutana ukielekea wapi?"
"Kuchukua matunda." Rose akaangua kicheko tena. "Acha bana mambo yako!"
"Walaa! Mie nimesema tu."
"Unadhani basi nayanunua hayo matunda?" Rose aliuliza. Kabla hajajibiwa, akaongezea: "Unamkumbuka yule mzee tuliyemuona siku ile gengeni?"
"Yap!"
"Hunipa matunda bure."
"Bure?" Kone alitoa macho.
"Ndio, bure." Rose akajibu akirembua macho. "Nadhani Kone umesahau ni namna gani nilivyo mzuri."


Wakacheka kwa pamoja.


"Na kweli nimesahau. Ila umuonee huruma mzee wa watu."
"Nani kasema? Mpaka nihakikishe amemaliza mtaji wote. Ujinga kaupalilia mwenyewe na maji ya tamaa."
"Ila usijali, hii kazi itatuondoa hili eneo muda si mrefu. Bila shaka babu wa watu atadumisha genge angalau."


Wakacheka. Waliacha maongezi hayo wakarejea kwenye zoezi lao la kusoma faili waliloliacha kiporo kwa vidakika kadhaa. Walijivesha nyuso za kazi na macho ya umakini.


Sasa ndani ya faili hili walikuwa wanamtazama pande lingine la jibaba, kwa jina Sisawo. Picha ya mwanaume huyo ilikuwa kubwa ikiwa imepigwa nyakati za jioni. Mandhari ya picha hiyo yalikuwa ya siri.


Chini ya picha hiyo kulikuwa kuna maandishi machache yakisomeka: "Sisawo, nguzo ya damu ya Mandinka."


Baada ya maneno hayo yalifuatia maneno yaliyokolezwa uweusi: *Tageti ya kwanza kabisa ya kuangamizwa ndani ya Guinea.*


Picha ilikuwa moja tu ya mwanaume huyo. Japokuwa ilikuwa kubwa lakini bado haikuwa anaonekana vizuri, ila angalau ingeweza kumkumbusha mtu endapo angemuona mhusika huko njiani, kama angemtazama vema.


Kwenye picha hiyo Sisawo alikuwa amevalia kofia kubwa 'cowboy' nyeusi. Alikula suti ya rangi ya kahawia na alikuwa anaingia mlangoni mwa mahala fulani palipokuwa panapendeza machoni.


Mahala hapo palikuwa mithili ya hoteli ama mgahawa mkubwa.


"Yani hadi Sisawo?" Alistaajabu Kone. "Huwezi mdhania kabisa!"
"Huyu si ndiye yule anayesaidia watoto yatima na wazee?" Aliuliza Rose.
"Ndiyo yeye!" Kone akajibu.
"Ina maana naye anahusika na joto la Guinea?"
"Bila shaka ndiyo maana yupo humu."


Kone akaanza kusoma maelezo ya mwanaume huyo;
"Mwanaume huyu mfanyabiashara mkubwa ndani na nje ya Guinea, ndiye tageti ya kwanza kwenye mauaji. Anafadhili jeshi la kikabila ambalo linapewa mafunzo ya kijeshi na kumiliki silaha za kisasa kabisa.


Jeshi hili lina watu toka nchi mbalimbali, ila kigezo kikiwa kikuu kikiwa kimoja; lazima mtu huyo awe ni wa kabila lao. Huko mazoezini atafundwa ukakamavu, kuua na uvumilivu. Wanatolewa utu na kupandikizwa chuki dhidi ya wengine, lakini pia kiu ya kuua.


Tulifanikiwa kumpandikiza mtu wetu kwenye jeshi hilo akakusanya taarifa kadhaa muhimu. Kiongozi na ratiba zao za mashambulizi. Lakini pia sauti ya Sisawo ikiwahamasisha wanaume hao wajitoe sadaka kwa ajili ya kabila lao.


Endapo mauaji yoyote ya watu wa jamii ya Fulani yakijiri, basi ni hawa watu ndiyo wanahusika. Watawamaliza wale wote wanaoonekana wana ushawishi mbele za watu, na tishio kwa kabila lao."


Kone aliweka nukta hapo akamtazama Rose.


"Ina maana hawa ndiyo wamemuua mke wa Raisi?"
"Inawezekana," Rose akajibu na kisha kuuliza: "ila kwanini wamuue mama wa watu?"
"Inasemekana ndiye alikuwa mgombea mteule wa kuwania nafasi ya uraisi kwa kupitia chama cha mumewe."
"Ndiyo wamuue?"
"Inawezekana kuna kitu walikiona kwake, hawawezi wakamuua tu. Aidha waliona kuna hatari ambayo mwanamke huyu anaweza kuwasababishia."


Kone aliacha kupekuwa faili akaingia mtandaoni kupitia simu yake. Aliandika jina la mwanamama huyo na kusachi. Taarifa lukuki zikaja. Alipembua taarifa hizo kwa dakika kama kumi, kisha akasema:
"Sasa nimepata mwanga."
"Niambie," Rose akadakia.
"Katibu mkuu wa chama ndiye alimshawishi mama huyu kugombea. Waliamini ana mvuto kwa jamii, lakini haswa kwa wanawake wenzake ambao walimuona shujaa kwa kusimama mbele ya hadhira na kutema maovu aliyokuwa anafanya mumewe.


Waliamini ni mwanamke shupavu ambaye anaweza kuvunja mfumo dume. Hivyo kupata ushawishi wake ni kuwapata wanawake, kupata wanawake ni kupata kura. Siku zote wanawake ndiyo wapigaji kura, wanaume waongeaji tu."





****


☆Steve
 
*NJIA NYEMBAMBA --- 25*


*Mtunzi: SteveMollel*








Iliwachukua lisaa kumaliza kusoma faili la Guinea, ikawachukua tena lisaa limoja kulipitia la Sierra Leone, wakapumzika. Mambo yalikuwa mengi na hatari zaidi. Kila karatasi waliyoifungua ilikuwa na mambo mazito kuliko ya awali. Mambo yaliyowaacha mdomo wazi.


Kama kuna somo kuu walilolipata kwa kupitia nyaraka hizo, basi ni kutoamini yale tu macho yako yanachoona. Ulimwengu ni zaidi ya hapo. Kuna mambo mengi yapo ardhini, kama usiposhika jembe ukalima basi maisha yako yote utaishia kusema dunia ni milima na mabonde.


Walikunywa kahawa nyepesi wakati wakingojea maakuli jikoni yaliyokuwa yanaandaliwa na mkono wa Rose. Walisindikiza subira yao kwa soga za hapa na pale, walipomaliza kula wakaendelea na zoezi.


Simu ya Kone iliita, ila hakuna aliyetambua kwani ilikuwa imewekwa mfumo wa kimya. Si chini ya mara tano simu hiyo iliita. Kone alikuja kulitambua hilo baadae baada ya kumaliza kupitia kila jambo mafailini. Alikuwa ni mkewe amuita.


Alijaribu kumtafuta, salio likawa halijitoshelezi. Njia pekee aliyoiona sahihi ikawa ni kuondoka kwenda nyumbani.


"Inanipasa niende," alimwambia Rose.
"Kwahiyo vipi sasa?" Rose akauliza. "Tunaamua nini juu ya haya?" Alinyooshea mkono wake kwenye mafaili.
"Tutakuja kuongea baadae, Rose."
"Una uhakika tunaweza tukaongea baadae? Muda si rafiki, na sidhani kama Amadu atakuwa na uvumilivu wa kiasi hicho," alisisitizia Rose. Kone akashusha pumzi ndefu.


Pengine angemwambia mwanamke huyo juu ya mkewe, angemuelewa. Ila hakutaka kufanya hivyo, aliweka siri. Alipima hoja ya Rose akaona ina mashiko. Hakukuwa na muda wa kusubiri tena, basi akajikuta anaamua kuketi. Kama moto basi ni moto na si vuguvugu.


"Unaamua hili?" Aliuliza Kone akimtazama Rose machoni.
"Ndiyo, naamua. Kwa akili zangu zote tena nikiwa timamu," Rose akajibu kwa kujiamini.
"Kila mtu anajua kazi hii ni ngumu na hatari, ila hakuna wa kuifanya zaidi yetu," Kone alisema na kuongezea: "Ni sisi tu ndio tunangojewa ili mapambano yaanze. Kwahiyo kama nikimtaarifu Amadu, basi anaweza kutuambia tuanze mapambano mara moja. Hatujajua angelipendekeza iwe nchi gani ila inaweza ikawa yeyote ile, kwahiyo tunahitaji kujiandaa."
"Ni kweli. Ila huoni kama ingekuwa vizuri kumwambia kwanza Amadu ili basi kama kujiandaa tujiandae kwa mujibu wa mpango? Bila shaka mipango haiwezi kufanana, na hata maandalizi yake pia."
"Umeongea la maana," Amadu akaunga mkono hoja. Alifanya mpango akaongeza salio simuni kisha akamtumia ujumbe Amadu;
"Tumeridhia kufanya kazi."
"Kwanini usimpigie?" Rose akauliza.
"Namba yake haipatikani," Kone akamjibu. "Nimejaribu mara kadhaa nikashindwa kumpata. Ni ujumbe tu ndiyo unaenda. Uzuri anajibu haraka."


Kweli, ndani ya muda mfupi ujumbe unaingia kwenye simu ya Kone. Kone anaufungua na kuusoma kwanguvu Rose asikie.


"Leo, majira ya saa tano usiku, kuna kazi ya kufanya ndani ya Sierra Leone. Ni kazi ya mauaji, takribani kilomita sitini na tano toka yalipo makazi yenu. Mtuhumiwa namba tano."


Walirejelea kwenye mafaili yao kumtazama mtuhumiwa namba tano. Alikuwa ni mwanaume mrefu mpana. Mpenzi wa vileo na kuhudhuria kumbi za starehe.


"Nitakuja kukupitia baadae," akasema Kone. Rose akatikisa kichwa.
"Bila shaka ntakukuta umeshajiandaa," Kone akaongezea. Rose akatikisa tena kichwa. Kone akaaga aende sasa.



***
***



"Hatujampata, mkuu," Alisema Rauli ndani ya kijikao kidogo cha dharura alichoketi na Talib. Walikuwa ikulu ndani ya kajichumba kadogo ka mkutano.
"Rauli," Talib aliita. "Hauna ambacho umefanikiwa kufanya?" Akauliza.


Rauli alipepesa macho mdomo ukibanwa na kigugumizi. "Ki ... kip - o, mkuu."
"Kipi?"
"Nimeweka maajenti wangu mtaani, wanafanya skauti ya kuwatafuta waandamanaji."
"Mpaka sasa wamekamata wangapi?"
"Bado, mkuu. Wana ..."
"Wao wameua maajenti wako wangapi?"
"Watano."


Talib akatabasamu.


"Mkuu, hali si nzuri. Waandamanaji hawa wamekuwa wakimshuku mtu yeyote mgeni ndani ya maeneo yao," alijitetea Rauli.
"Kwahiyo kama ni hivyo?" Talib aliuliza. "Rauli, ndio maana nikakupa hiyo kazi. Ukae na utazame namna ya kuwapoteza watu hawa.

Unavyokuja na kuniambia njia yako imefeli, unadhani nina muda wa kusikiliza huo upuuzi wako?"


Rauli akatikisa kichwa.


"Ulitaka nini ulichokiainisha kwenye mipango yako nikakunyima?"
"Hamna, mkuu."
"Sasa unaniletea porojo gani hapa?"


Talib akasimama. Alipiga kofi meza akifoka:
"Toka! Ukirudi hapa pasipo kuniletea cha maana, nitakumaliza mbwa wewe."


Rauli alisimama, akaenda akitazama chini. Alijihisi vibaya, lakini pia alijihisi amekosewa. Aliminya lips akienenda na kujipaki kwenye gari lake, mercedes benz jeupe toleo la zamani, akatoka ikulu.


Baadae ilikuja kuripotiwa mwanaume huyu amejiua kwa kujinyonga. Ilikuwa ni punde baada ya kuonana na wenzake na kuwaambia hawezi tena kazi. Hawakumuelewa, labda kwasababu hakusema sana.



---



Waswahili husema mzaa janga hula na wa kwao. Na hakika hawakukosea. Msiba haukosi ndugu.


Wakati Sierra Leone kukifukuta, Al Saed anafikishiwa habari mbaya kabisa inayomharibia siku. Anahabarishwa watumishi wake wameuawa, ni Rambo pekee ndiye alibaki hai, tena akiwa majeruhi hohehahe.


Taarifa hizo zilimkuta akiwa anakula chakula cha mchana. Hamu ya kula ilikoma punde akaharakisha hospitali kumuona Rambo apate kumuelezea kilichosibu. Isingelikuwa ni mkuu wa nchi, asingeliruhusiwa kumuona mhanga kwa kuambiwa ampe muda wa mapumziko. Zaidi, uso wake uliwaogopesha wauguzi kwani ulikuwa umefura na kughafirika vya kutosha.


Hatua zake alizotupa zingekufanya umpishe njia pasipo kuombwa.


Alijikuta anapigwa ganzi ya mwili alipomuona Rambo akiwa amejilaza kitandani. Alijihisi mwili umepoteza nguvu, magoti yanagongana. Alipata joto la mwili upesi, akaona nguo zinambana. Alitamani hata kuzivua.


Kwake Rambo kulala kitandani halikuwa jambo dogo hata kidogo, ilikuwa ni ishara ya kushindwa. Ishara ya kuzidiwa. Atafanyaje sasa ilhali wanaume aliowategemea wamalize kazi, wamemalizwa kabla ya kazi?


Uso wote wa Rambo ulikuwa mwekundu, jicho moja lilivimba rangi ya zambarau. Mkono wake wa kuume ulikuwa umevunjwa. Kichwa kilikuwa kimezungushwa plasta nzito kana kwamba mti umeungwa usianguke. Mguu wa kushoto haukuwepo, wa kulia ukiwa umevunjika.


Alitia imani. Ungeweza sema amekufa.


Al Saed alimsogelea karibu zaidi, akashika kitanda. Aliita kwa sauti ya chini, mara tatu, mara Rambo akafungua jicho, lile lililokuwa na afadhali, la kushoto. Nalo lilikuwa limevijilia damu. Hakumudu kuliangaza kwa muda, akalifumba.


"Mkuu," aliitika kwa shida.
"Nini kimetokea, Rambo?" Al Saed akauliza. "Nini kimewakumba?"
"Tuli ... va- miwa, mkuu," alijibu Rambo kwa shida. Alikohoa mara mbili kisha akaendelea: "Tulipang - a vizuri tu ... vizuri ... Tulipo,anza kusha ... mbulia, mabomu mata...tu ya -liru - shwa mbele yetu." Rambo akaweka kituo. Alivuta kwanza hewa, mara kwa mara akiugulia maumivu.
"Baa ... da ya ha-po, sikumbuki cho-cho-te zaidi ... zaidi ya make - lele ya wenzangu na make... le, le ya risasi. Nasha ... nga .. aa nimefika ... je hapa hai."


Akaweka kituo kirefu.


Ilikuwa ni habari ya kuwahiwa kabla hujawahi; pale ujanja wako unapokuwa ujinga mbele ya adui. Kikosi cha wanaume hawa, wakina Rambo, walitanguliwa hatua tatu mbele kimaamuzi. Kila walichokuwa wanafanya kilishatarajiwa tayari, na kikapangiwa namna ya kukikomesha.


Wakiwa wamepashwa habari na mateka wao, kiongozi wa kamati ya ulinzi na mjumbe wake, walivamia maeneo yale matatu elekezi. Walipovamia eneo moja, hawakukuta kitu, na la pili pia, hivyo basi wakajua la tatu ndilo lenyewe hivyo nguvu zikatiwa hapo.


Ambacho hawakukijua ni kwamba, maadui zao nao walikuwa wameshalitambua hilo, kwani taarifa za uvamizi wa maeneo mawili ya nyuma walishazipata toka kwa maajenti wao. Hivyo basi, wakajipanga.


Wakina Rambo walikuta eneo kimya kama vile hamna watu. Walikuja eneoni hapo kwa miguu. Walisogelea jengo hilo kwa kunyatia, na kwa uangalifu.


Lilikuwa ni jengo la kisasa kubwa la ghorofa, halikuwa limemaliziwa plasta. Kwa nje kulikuwa kuna bustani kubwa likizingira, pamoja na matofali kadhaa.


Rambo na wenzake wakiwa wanasogea, kuna wanaume wanne waliokuwa wanawatazama, wakiwa wamekaa chumba cha juu. Walipofika eneo la karibu zaidi, wanaume wale wakatazamana, kisha wakapeana ishara. Mmoja akatoa mabomu kwenye kamfuko cheusi kalichokuwepo kando. Akayachomoa pini na kuyarusha kwa mkupuo.


Yakiwa hewani, wengine wakashikilia bunduki zao tayari kwa mashambulizi.


Kufumba na kufumbua, mabomu yakatua miguuni mwa wakina Rambo. Hakika wakatoa macho kwa mshangao. Roho zilikuwa mikononi sasa. Walikutana uso kwa uso na kifo.


"Kimbia!" Mmoja wao alifoka. Kila mtu alijaribu kujiepusha na adha ya kifo kwa kutumia miguuye, ila hawakufika hata hatua mbili, mabomu yakajitusu na kuwarushia mbali.


Kilichomnusuru Rambo, ni kutulia tuli baada mlipuko huo, alikuwa amepoteza fahamu. Wenzake waliokuwa wanagugumia kwa maumivu, walishushiwa mvua ya risasi, na kisha wahusika wakahepa.


Ni baada ya masaa matatu, ndipo wakaja waokozi na kubeba miili ya Rambo na wenzake. Walikuwa ni wanajeshi watano waliobebelea silaha. Walipekua nyumba wakapata maganda lukuki ya risasi.


Walidhani Rambo amekufa pia. Isingekuwa hekima za mfanyakazi wa mochwari, basi alikuwa anatiwa kwenye jokofu kama wenzake waliotiwa humo pasipo kupata huduma yoyote.



***



"Twende basi tukale, mpenzi," Kone alimwambia Fatma aliyekua amejilaza kitandani. Ni majira ya saa mbili usiku sasa na takribani dakika za kutosha.


Macho ya Fatma yalikuwa mekundu. Alilaza kichwa chake juu ya mkono. Alikuwa amegeuzia uso wake ukutani asimwangalie mumewe. Hakutaka kabisa kuongea na mwanaume huyo tokea aliporudi toka kwa Rose.


"Mke wangu, utakaa hivyo mpaka lini? Niambie basi kosa langu ni nini."
"Kone, kama hujui kosa lako, huna haja ya kuomba msamaha," alisema Fatma kwa mara ya kwanza. "We nenda kale, mimi utanikuta hapahapa!"
"Siwezi nikaenda pasipo wewe. Watoto watajisikiaje?"


Kimya.


"Fatma," Kone akaita tena. Aliongea zaidi na zaidi ila Fatma hakusema tena chochote, mwishowe akaamua kwenda kula mwenyewe. Aliwadanganya watoto mama anajisikia vibaya. Watoto walikula wakaenda zao, wakamuacha baba peke yake mezani.
Baada ya muda mfupi, Kone anajipepesa kutafuta simu mfukoni. Hakupata kitu. Alitazama mezani na maeneo ya karibu, napo hakupata kitu. Moja kwa moja akajua atakuwa ameiacha chumbani.


Alijinyanyua akaenda chumbani taratibu. Alimkuta mkewe akiwa anatumia simu hiyo, akipekua ujumbe. Aliishia kumtazama akimngojea amalize. Bado macho ya mwanamke huyo yalikuwa mekundu.


Alimaliza upekuzi, akaiweka simu kando na kugeukia ukutani. Kone hakuichukua simu hiyo, akamtazama mkewe kwa muda wa kama dakika nne pasipo kusema jambo. Alikuwa anatafakari mambo lukuki kichwani.


Alimgusa mkewe bega, akimuita. Fatma hakuitikia.


"Samahani, mke wangu. Nimejua kosa langu. Nilipitiwa, hakika nilisahau kabisa. Ila kesho, naapa, nitakupeleka kwenye ile nyumba ukaione."
"Kesho?" Fatma aliuliza na kisha akaguna. Aligeuza shingo yake akamtazama mumewe. "Unadhani tutakaa hapa mpaka lini? Kila uchwao tuwe tunatoa pesa kulipia nyumba, chakula. Mpaka lini? Uliliona hili halina maana, ukalipuuzia. Umeona ya Guinea na Rose ni ya maana zaidi kuliko familia yako?"


Fatma aliongea kama chiriku. Kone alikaa kimya kusikiliza. Mwanamke huyo alipochoka, akajilalia zake, akimalizia kwa kusema:
"Safari njema ya mauaji."


Kone alishusha pumzi ndefu akiegemeza mgongo wake ukutani. Aliendelea kutafakari mambo kadha wa kadha wakati muda ukisonga. Yalipofika majira ya saa nne, alichukua simu yake akampigia Rose.


"Vipi tayari?"
"Ndio, nakungoja wewe."
"Poa, nakuja."



***

☆Steve
 
Back
Top Bottom