Njia nyembamba (Simulizi mpya by SteveMollel)

Njia nyembamba (Simulizi mpya by SteveMollel)

Tutajua tu anakotoa hii stori sidhani kama anatunga yeye


Sent using Jamii Forums mobile app
Sasa mzee wangu ningekuwa natoa sehemu si ndo ningekuwa nazimwaga hapa daily. Au wewe ndo una mpango wa kuichukua? Anyways naandika hii simuliz kwa mikono na akili yangu mwenyewe ma ndiyo maana kuna muda najikuta nakosa muda wa kuiendeleza maana mpaka nikae na kuandika.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
*Njia nyembamba -- 20*



*Mtunzi; SteveMollel*










Bado siku haikuwa imeisha. Jua lilikuwa linaelekea kuzama anga likiwa jekundu kwa kufifia. Ndege walikuwa wanajirudisha viotani, na baadhi ya watu pia wakijirudisha kwenye maskani zao.


Kulikuwa ni tulivu sana juu ya uso wa Liberia. Tulivu haswa isiyo na shari. Na pengine kuna waliodhani tulivu hiyo ingeendelea kudumu. Bahati mbaya walikosea. Tulivu hii ilikuwa inawindwa, na muda mchache mbeleni ilikuwa inaelekea kuvunjwa.


Wanaume wawili waliokuwa wamevalia vinyago vyeusi, waliwasili karibu na nyumba ndogo kimipango iliyokuwa imezibwa kwa uzio wa bati. Nyumba hiyo ilikuwa ni ya rangi ya bluu iliyofifia. Ilikuwa na kibaraza kidogo chakavu kinachomkaribisha mgeni mlangoni.


Wanaume hao waliovalia vinyago, walitazamana, wakatikisa vichwa. Migongoni mwao walikuwa wamebebelea vibegi vidogo tusivyojua vina nini. Walisukumiza mlango mdogo wa geti ukafunguka, wakazama ndani.


Hawakufika mbali, mara wanashtuliwa na sauti kali ya mlio wa mbwa. Alikuwa ni mbwa mkubwa mweusi upande wao wa kushoto. Masikio yake yalikuwa yamesimama kama kidaka mawimbi. Sauti yake kubwa na nzito ilifoka kwa wingi. Alibweka akiwa amesimama, na akitazama mlangoni.


Wanaume hawa hawakumuona mbwa huyu kabla ingali walipembua mazingira. Labda kwasababu ya uweusi wa mnyama huyo na uhaba wa mwanga hapo nje. Kulikuwa kuna taa moja tu. Mwanga wake ulikuwa mkali ila haukutosha kumulika eneo lote vema.


Ilibidi haraka maamuzi yafanywe. Mwanaume mmoja alipeleka mkono wake pajani, mara akachomoa kisu alichokitupa kwa ustadi kumfuata mbwa, kisu kikazama kifuani mwa mnyama huyo na kumwangusha chini. Kukawa kimya.


Haraka mbwa alihamishwa toka eneo la wazi, halafu wanaume hao wakajongea kuufuata mlango. Wakiwa wanajisogeza, walisikia sauti ya vishindo vya miguu inakuja mlangoni. Haraka wakabana ukutani.


"Nimemsikia bobby anabweka!" Sauti ya mtoto wa kiume ilivuma.


Mlango ulifunguliwa, kikachomoza kichwa cha mvulana. Kwa makidirio alikuwa na miaka saba. Macho yake yalikuwa makubwa, alivalia jezi nyekundu ya mpira. Aliangaza macho yake kumtafuta mbwa, mara akadakwa na kuzibwa mdomo kwanguvu.


"Shhhh! ... tulia!" Aliamriwa kwa kunong'onezwa. Wanaume walizama ndani, mmoja akiwa amembana mtoto huyo. Sasa mikononi mwao walikuwa wamebebelea bunduki ndogo; aliyembana mtoto akiielekezea kwenye kichwa cha mateka wake huku mwenzake akiielekezea wanapoelekea.


"Chini! Chini! Lala chini!" Amri ilitolewa. Kulikuwa kuna watu watatu sebuleni: mama mmoja mtu mzima, takribani miaka sitini na kitu, akiwa na watoto wawili mapacha wa kike mwenye makadirio ya miaka kumi na mitatu.


Wote walilala chini upesi. Walishajawa na hofu juu ya uhai wao. Mikono vichwani. Mioyo ilikuwa inakimbia marathon. Mtoto yule wa kiume naye aliamriwa alale chini, haraka akatii.


"Mwenye nyumba yupo wapi?"
"Yupo kazini baba!" Aliwahi kujibu mama.
"Anarudi saa ngapi?"


Kulikuwa kimya kidogo. Jibu lilibanwa na kigugumizi. Kabla halijalazimishwa kutoka, sauti ya geti ilisikika. Wavamizi wakatazamana. Si bure akili yao iliwaambia mtu wanayemhitaji ndiye anakuja sasa, hivyo basi ilibidi wafanye kitu.


Mwanaume mrefu mweusi aliyevalia sare za jeshi la Liberia, alikuwa ameingia ndani ya eneo hilo la nyumba. Mkono wake wa kushoto ulikuwa umebebelea mfuko mweusi wa nailoni. Mwendo wake ulikuwa mkakamavu, akisafisha koo mara kwa mara kutoa ishara ya mwenye nyumba kuwasili.


Mwanaume huyu alikuwa miongoni mwa wale waliofanya oparesheni kabambe ya kutokomeza kijiji cha wanamgambo wa AMAA. Alikuwa ni msaidizi wa oparesheni hiyo ya siri iliyoleta mafanikio makubwa. Damu aliyokuwa ameimwaga kwa ajili ya nchi na kiongozi wake, sasa ilikuwa inataka kumtokea puani.


Mazingira ya nyumba yalikuwa kimya mno, kiasi akashangazwa. Ila hakutaka kujisumbua sana na hilo. Alitafakari kwa sauti;
"Wamelala au?"


Alikaribia mlangoni, kabla hajafungua mlango, akastaajabu kwa kutikisa kichwa;
"Yani hata mbwa hawajamfungulia!"


Bwana huyu hakuwaza mara mbili juu ya usalama wake na wa familia; sababu kubwa ilikuwa ni kutodhani kama ana sababu ya kufanya hivyo. Hakufikiri kama bado yupo vitani, alidhani vita imeshakwisha. Walishammaliza adui kwa milipuko ya mabomu na ncha za risasi, waliamini.


Alitengua komeo la mlango akazama ndani. Kutazama, uso kwa uso na mdomo wa bunduki.


"Karibu kaburini!" Alipokelewa kwa maneno ya shombo. Aliamriwa anyooshe mikono juu, akatii. Aliomba familia yake iachwe salama maana haina makosa, lakini hakuna aliyesumbuka kumsikiliza.


Mwanamke yule wa makamo pamoja na watoto walifungwa kamba na kuzibwa midomo. Nyenzo zilitolewa toka kwenye mabegi. Walipofungwa walifungiwa vyumbani, wanaume wale wakibakia na mwanaume waliyemfuata.



"Ukidhani umemaliza kazi, mzee?" Alisema mwanaume mmoja akichomoa pande la kisu toka begini.


Walimfunga mikono mateka wao na kumpigisha magoti. Walimbandikia pia plasta kubwa mdomoni rangi ya silva.


"Sasa mtakufa mmoja mmoja kama kuku!"
Walimkata shingo mwanaume huyo wakimchukua filamu. Baada ya hapo waliutoa mwili wake na kuutupia chumbani. Kisha wakaondoka zao.


Ni kwamba wakati tukio hilo likiwa linafanyika upande huu wa dunia, na mengine pia ya aina hiyo hiyo yalikuwa yanaendelea ndani ya muda huo huo upande mwingine wa shilingi. Wanaume hawa waliovalia vinyago vyeusi walikuwa kumi kwa idadi, na kwa mujibu wa orodha yao, watu waliotakiwa kumalizwa usiku huo ni wanajeshi watano, hivyo basi walijigawa wawili wawili kwa kila tageti.


Harakati hizo za mauaji zilifanikiwa kwa kuwamaliza wanajeshi wanne, mwanajeshi mmoja akiponea chupuchupu. Kuna aliyeuawa karibu na maeneo ya bar, mwingine akiuliwa na kutupwa misituni, na mwenginewe akimalizwa kandokando ya barabara kwa njia ya risasi. Ilitegemea na wapi mlengwa alikutwa na kikosi cha umauti.


Kwa namna moja sasa Mr. X akawa amerejesha tabasamu lake usoni, ingawa kumkosa huyo mmoja ilimuuma mno. Laiti isingelikuwa mwanajeshi huyo alipata udhuru wa ghafla wa safari, basi kwa sasa ingelikuwa simulizi tofauti. Simulizi ya ushindi mnono kwa Mr. X.


"Si mbaya, maana hata sisi hawakutumaliza wote," alisema Mr. X. Mwanaume ambaye kwa sasa alikuwa na kikosi cha watu kumi na tano pekee, wanaume alionusurika nao kwa kujilaza ndani ya mahandaki siku ya mashambulizi.


Wanaume hawa walikuwa kumi na tano, ila shughuli yao ni pevu. Walikuwa wamefundwa katika ujuzi wa kijasusi maridhawa. Walikuwa ndio wanaume pekee wanaokuwa karibu na Mr. X kwasababu ya kuaminika kwao kiimani, kiakili na kinguvu.


Japokuwa walikuwa wachache lakini walimfanya Mr. X awe na kibri. Awe na imani maradufu kwamba anaweza kuiteka Liberia na kuiweka kiganjani.


"Kesho tutashambulia sehemu nne za makutano kwa kutumia vilipuzi. Nahitaji watu si chini ya mia mbili wawe wameuawa ama kujeruhiwa. Vita yetu ndio imenza rasmi. Na hatutakoma mpaka pale tutakapokuwa tumeitwaa dola ya Liberia," alisema Mr. X.


Walianisha na kuweka bayana mipango yao ya namna ya kushambulia. Kwa siku hiyo hiyo moja ya kesho, ndani ya muda mmoja, inabidi vilipuzi vyote viwe vimeshafyatuka. Kazi hiyo ilikuwa ni lazima ifanyike, lazima ifanikiwe.



***

Kikao kilihudhuriwa na takribani watu kumi na mbili. Watu hawa walikuwa wamevalia suti nyeusi pasipo tai. Vichwa vyao vilikuwa vimefunikwa na kofia aina ya 'cow boy', wengi wakionekana wameambatana na mikongojo kama miti ya miamvuli.


Walikuwa wamechukua uwanja wa mkutano unaopatikana juu kabisa ya hoteli ndogo ya kitalii. Eneo hilo lilikuwa ni tulivu na lenye wingi wa upepo. Watu hawa, ambao kwa wingi walikuwa ni watu wazima, walikuwa na nyuso ngumu zinazotisha.


Wanaume watatu walikuwa wameketi mbele ya wenzao. Walitenganishwa na meza kubwa ndefu ya chuma. Bila shaka wanaume hawa walikuwa ni viongozi. Juu ya meza yao kulikuwa kuna vinywaji kadhaa, vyote vilikuwa vilevi. Ila hawakuwa wamekifungua chochote kile, vyote vilikuwa na mifuniko yake.


Mwanaume mmoja miongoni mwa hao watatu, alisimama na kusafisha koo lake. Watu wote walimtazama kwa umakini. Aliangaza kila pande kabla hajafungua mdomo wake na kusalimu.


"Leo tumekutana hapa kwa ajili ya kikao chetu cha pili, kama watu wa Malinke: watawala wakubwa waliowahi kutokea Afrika na duniani kwa ujumla chini ya empaya ya Mali. Lengo letu kubwa ni kutazamia wapi tulipofikia baada ya kikao cha kwanza, na pia wapi tunapotaka kuelekea. Kikao kimefunguliwa."


Baada ya maneno hayo, muongeaji aliketi, na mara anasimama mwingine wa kando. Anasalimu na kufungua kijidaftari kidogo.


"Mahudhurio yetu ya kikao kilichopita ilikuwa ni watu saba. Tulipata wasaa wa kujadili mambo kadhaa, hususan, kurudisha nguvu yetu inayoyumbayumba katika dola ya Guinea. Miongoni mwa tuliyokubaliana ikawa ni kuhakikisha kila wizara ya serikali hii mpya, itakuwa na mtu wetu. Lakini kubwa ni kwamba kumteua nani ambaye ataenda kuwa raisi wa nchi hii ya Guinea, yaani atakayesimama kugombea uraisi miezi miwili hapo mbele."


Kukawa kimya kidogo. Muongeaji alisafisha koo kana kwamba alikuwa amebanwa, kisha akaendeleza soga;
"Sasa basi kulikuwa kuna watu watatu walipendekezwa na wajumbe. Nao ni Aba, Jatoo na Sisawo. Bila shaka leo tutampata tunayemtaka ili tuanze kuainisha na kutekeleza mipango yetu ya kuhakikisha tunashika dola. Na hilo zoezi ndilo tutakaloanza nalo kwa sasa. Tutapitisha makaratasi na kila mjumbe atatia alama ya tiki kwa mteuliwa anayemuunga mkono."


Zoezi hili lilidumu kwa takribani dakika tano tu. Kura zilihesabiwa na mshindi akawekwa bayana. Alikuwa ni bwana Sisawo, pande la mtu mweusi mwenye utajiri wa ndevu kipilipili. Bwana huyu ndiye alikuwa mmiliki wa eneo hilo la hoteli ambamo mkutano ulikuwa unafanyika.


Kufuatia uchaguzi huo, wakateua pia na mawaziri kwa kila nyanja. Watu hawa walikuwa wanafanya haya katika namna ya kujiamini sana. Ni kana kwamba walikuwa tayari wameshashinda uchaguzi.


Walimaliza kila teuzi, kabla hawajaendelea zaidi, hoja ilichipuka ndani ya kikao. Mjumbe mmoja alipendekeza kufahamishwa. Aliuliza;
"Vipi kama tukishindwa uchaguzi huu, kama vile tulivyofanyiwa pambe ya ndere kwenye uchaguzi uliopita?"


Hoja hii ilizua gumzo. Msimamiaji wa kikao, alisimama na kuwaondoa shaka wajumbe juu ya jambo hilo.


"Hilo jambo halitatokea. Hilo jambo, kamwe, halitawezekana! Uchaguzi huu lazima tushinde, iwe kwa njia halali ama ya panya. Na tayari tumejizatiti kuhakikisha hilo linatokea. Hapa tunavyoongea, kuna kikundi cha vijana mia moja na hamsini wapo mafunzoni wakijiandaa. Wana mafunzo ya kutumia silaha na mapambano ya vita. Mbali na hapo, tumeshawasiliana na wenzetu waliopo Guinea Bissau, Liberia, Ivory Coast, Mali, Gambia, Burkina Faso, Sierra Leone na Senegali. Wote wapo tayari kutuunga mkono. Lakini sisi pia kama wajumbe, tuna haja ya kutumia nafasi zetu kuhakikisha hilo linawezekana."


Jibu hilo lilituliza munkari, kikao kikaendelea. Kilidumu kwa muda mfupi mbeleni kabla hakijafungwa na wajumbe kusambaa wakikubaliana kukutana baada ya majuma mawili.


Wajumbe hao walijitoa jengoni, isipokuwa Sisawo, wakajipakia kwenye magari yao ya kifahari na kupotea eneo hilo.


Ila kandokando mwa barabara kulikuwa na gari moja dogo, Suzuki Vitara. Vioo vyake vilikuwa vyeusi ti isipokuwa cha mbele atumiacho dereva kuangazia barabara. Gari hilo lilikuwa na rangi ya kijani kilichotota uweusi. Vioo vyote vilikuwa vimepandishwa juu kutokujua aliyemo ndani.


Punde gari hilo linawashwa na kushika barabara. Linatokomea. Baada ya muda mfupi, simu ya Kone inaingia ujumbe. Kone aliiwahi simu hiyo na kutazama. Namba ilikuwa mpya.


"Naomba tuonane. Ni jambo la haraka."
"Wewe nani?" Kone aliuliza kwa ujumbe.
"Mimi Amadu," akajibiwa baada ya muda mfupi. Alistaajabu. Alijaribu kupiga namba hiyo, haikupatikana. Alituma ujumbe;
"Upo wapi?"
Punde akajibiwa; "nipo kila sehemu."




****




☆Steve

Sent using Jamii Forums mobile app
 
*Njia nyembamba -- 21*


*Mtunzi: SteveMollel*








Kone akajikuta anatabasamu.


"Sasa tunakutana wapi?" Alituma ujumbe. Baada ya muda fupi akajibiwa:
"Nitakuambia karibuni. Ila itakuwa huko huko Sierra ulipo."


Akatahamaki.


"Umejuaje kama nipo Sierra?"
"Nimekwambia nipo kila sehemu, Kone," ujumbe ulimjibu punde, akabakiwa mtupu asiye na maneno. Aliaga ila hakujibiwa tena, maongezi yakawa yamekomea hapo.
"Amadu," Kone alijikuta akinong'oneza mwenyewe. Alitabasamu kabla hajaiweka simu mezani na kujinyoosha viungo. Ilikuwa ni usiku sasa wa saa moja. Alikuwa ameketi nje ya jengo pembezoni mwa bwawa kubwa la kuogelea.


Alikuwa amevalia kaptula ya bluu inayokomea magotini. Kifua chake kilikuwa wazi. Alikuwa amejilaza kwenye kajitanda kadogo chembamba chenye michoro ya mistari mistari. Alikuwa hapo kajitandani peke yake.


Eneo lilikuwa tulivu. Mbali na Kone, ni watu wawili tu ndio walikuwepo hapo, ila wakiwa mbali; walikuwa ndani ya maji wakiogelea. Hawakuonekana hata kama wanajua kama kuna mtu aitwaye Kone amejilaza.


Hata naya Kone hakuwa anawatambua uwepo wa watu hao. Japokuwa macho yake yalikuwa pale, akili yake ilikuwa ikiwandawanda huku na kule. Alikuwa anatatua baadhi ya mambo kichwani. Na mambo haya yaliongezeka maradufu alipopokea ujumbe toka kwa Amadu.


"Atakuwa yupo wapi? Anataka kuniambia nini? Mbona kanitafuta? Lazima kutakuwa kuna jambo. Tena hili jambo si haba," alitesa kichwa. Alibadili milalo mara mbili. Alikuja kung'amuliwa mawazoni na sauti ya mkewe, bi Fatma.
"Mbona umekaa hapa mwenyewe?"
"Kubadili tu mazingira mpenzi," alijibu kone akijisogeza kumpatia Fursa mkewe aketi.
"Nimekutafuta ndani. Hukuniambia kama utakuwepo huku," alilalama Fatma.
"Samahani, mpenzi," Kone akajitutumua kuomba msamaha. Alimshika mkewe mkono akimtazama usoni. Ila Fatma hakuwa anamtazama mwanaume huyo. Macho yake yalikuwa yanaangaza kuwatazama wale waliokuaa wanaogelea.


Mwanamke huyo alikuwa amevalia gauni refu jekundu. Miguuni alivalia viatu vyeusi vyepesi vya kuchomeka.


Macho ya Kone yalimjuza mkewe hayupo sawia. Alijua sababu itakuwa ni Rose tu, lakini hakutaka kuliweka hilo bayana. Aliuliza:
"Mpenzi, nini kinakutatiza?"
"Hamna kitu, nipo sawa tu," alijibu Fatma.
Kauli hii aitamkapo mwanamke, inabidi uhofie. Mwanamke akikuambia vivyo basi ujue shida ipo. Na basi kama usipoliendelea kuuliza napo pia atakuchukulia haujali, na hata mwishowe humpendi.


Kone akiwa tayari ameling'amua hilo, aliketi kitako akasogeza mdomo wake karibu na uso wa mkewe.


"Nini shida mpenzi. Naomba unishirikishe."
Kulikuwa kimya kidogo. Fatma alikuwa anatazama maji kana kwamba hajasikia kitu. Alikunjia mikono yake kifuani. Hata na mdomo alikuwa ameuvuta kidogo.


Alishusha pumzi ndefu kwa pua, kisha akaguna kidogo.


"Huyo Rose uliyesemea unaenda kumtoa, yupo wapi?" Aliuliza. Bado alikuwa anatazama kwenye maji. Kone alitabasamu kidogo alafu akamkumbatia mkewe kwa nyuma.
"Nimeshamtoa mpenzi. Sikuona hekima kumleta hapa hivyo ameweka makazi yake sehemu nyingine mbali na hapa."
"Utaenda kumuona lini?" Fatma aliwahi kuuliza haraka.
"Nadhani kesho ndio nitaenda kumuona. Nilimuacha apate kupumzika kwanza."
"Kone," Fatma aliita. Mara hii alimtazama Kone. "Hivi ni lini utaacha huu ukaribu wako na Rose?"
"Fatma mpenzi," Kone alitikisa kichwa. "Mimi na Rose tunaunganishwa na kazi tu, hamna kingine chochote. Kama ingelikuwa ni kukusaliti, ningelifanya hilo kitambo sana, tena kipindi kile tulipokuwa na mgogoro ndoani. Tafadhali naomba uniamini kwenye hili."
"Nakuamini sana, Kone,"alisema Bi Fatma. "Usidhani sikuamini, ila naogopa sana kukupoteza. Sitaweza kuishi utakaponiacha, Kone. Rose ni mwanamke mrembo sana, mjuvi na mcheshi. Ni mwanamke pekee aliye karibu na wewe."
"Mbele ya macho yangu hamna mzuri kuzidi wewe, hakuna. Nilikuona na ndio maana nikapata haja ya kukuweka ndani. Kwangu maana ya mwanamke mzuri ni wewe. Kwangu mfano halisi wa mwanamke mzuri ni wewe, Fatma wangu."


Fatma alishindwa kuzuia tabasamu usoni mwake aliposikia maneno hayo. Alimtazama mumewe kisha akamzawadia busu juu ya lips.


"Nakupenda, Kone."
"Nakupenda pia, Fatma."


Punde ...


"Ila mpenzi, fanya tuwe na makazi yetu. Nimechoka kuishi hapa hotelini. Natamani niwe napika na kuandalia familia yangu chakula," alisema Fatma kwa madeko. Alikuwa amejilaza juu ya kifua cha Kone.
"Hata mimi hilo jambo lilikuwa kichwani. Kuna nyumba moja nimeiona karibu kabisa na maeneo haya, inauzwa. Kesho tutafute muda wa kwenda kuitazama. Ukiridhia, basi tuichukue."


Fatma alijibu kwa tabasamu pana. Alimbusu mumewe shingoni mara mbili kabla hajajituliza kifuani mwa mwanaume huyo kama mtoto aliyeshiba na kubadilishwa nguo.



***

"Tayari mkuu," alisema mwanajeshi mmoja aliyekuwa amesimama kwa ukakamavu. Macho yake makubwa yalikuwa yanamtazama Al Saed aliyekuwa ameketi ndani ya ofisi yake akitafakari.


"Sawa, nakuja," alisema Al Saed, mwanajeshi akaondoka. Baada ya muda mfupi Al Saed alinyanyuka kisha akaenda chumba kingine ambapo huko alikutana na watu watatu wakiwa wamejiweka wakimngojea. Mmoja wa watu hao alikuwa ni mwanajeshi yule aliyesalimika kumalizwa na watumishi wa Mr. X.


Eneo lilikuwa limejengwa katika namna ya mkutano. Meza kubwa ndefu inayong'aa ilikuwa imetapakaa pamoja na viti vikubwa vyeusi vya kurelaksi. Viti vilikuwa takribani kumi na tano kwahiyo basi vingine vilibakiwa tupu kutokana na idadi chache ya watu.


Al Saed alijiweka kwenye kiti kikubwa kilichokuwa kinatazamwa na vingine vyote. Uso wake ulikuwa umepooza. Alitazama kwanza nyuso za watu waliokuwa wameketi kabla hajasafisha koo lake na kuongea kwa sauti ya kukoroma kana kwamba ametoka usingizini.


"Nimewaita hapa kufuatia mauaji yaliyotokea jana. Sina haja ya kuelezea zaidi kuhusu hilo tukio, hatuna muda na kila mtu analifahamu. Ningeenda moja kwa moja kwenye hoja. Nimewaita hapa kuniletea mrejesho wa nani anayehusika na haya matukio. Najua mmefanya kazi kwa muda mchache mno ila nategemea mtakuwa mmepata angalau kitu."


Al Saed aliposema maneno hayo aliweka kituo kirefu, akawatazama wanaume wawili wageni machoni.


"Johnson, Rambo nipeni majibu. Nataka kumjua ni msaliti gani anayehusika haya mauaji!" Al Saed alibamiza meza kwanguvu.


Wanaume hao wageni walitazamana, kisha mmoja, aliyekuwa amevalia miwani ya macho akawa wa kwanza kufungua mdomo. Jina lake Johnson.


"Mkuu, tangu ulipotupatia kazi ya kuwafuatilia wale watu watatu juzi siku ya tafrija, kuna baadhi ya mambo machache tuliyagundua ingawa hatukuwa tumemaliza upelelezi wetu huu. Aidha twaweza kuunganisha taarifa hizi na tukio hilo la mauaji."


Johnson alifungua faili lake rangi ya kijani iliyofifia. Macho yote yalikuwa yanamtazama akingojewa kwa hamu.


"Kwa huo muda, yaani tokea juzi usiku mpaka leo hii usiku tukija hapa kikaoni, naweza kusema kwamba naibu wa kamati ya ulinzi wa taifa, ndiye mtuhumiwa wa kwanza na mkubwa kwenye hili. Yeye akisaidiana na mjumbe wa kamati ya ulinzi. Labda kwa kupitia wao wanaweza wakatusaidia kuwajua wengineo."
"Mmejuaje kuhusu uhusika wao?" Al Saed aliuliza. Macho yake yalikuwa yamejifinyanga yakizama ndani.
"Huko ndiyo naelekea mkuu," Johnson akadokeza na kisha akaendelea; "Ile siku ya tafrija, naibu wa kamati ya ulinzi alipotoka hapa alilekea kwenye glosari kubwa hapa mjini. Hapo alikaa kwa takribani lisaa limoja. Alikuwa anakunywa mvinyo mmoja mkubwa kwa taratibu mno, na macho yake yakiwa yanasumbuka kutazama mazingira mara kwa mara kama atafutaye jambo. Kila aliyeingia eneo hilo alimtazama na kumpekua."


Johnson aliposema hayo alionyeshea picha za naibu huyo akiwa hapo glosari. Chini ya picha hizo kulikuwa kuna tarehe ya siku ambazo hizo picha zilichukuliwa.


"Naibu huyu alikuwa hapa glosari kwa ajili ya kupoteza muda tu. Hakukuwa na la msingi alilokuwa anafanya. Aidha lengo lake lilikuwa ni kupoteza watu wanaomfuatilia, kama watakuwepo. Alikuwa anataka kujihakikishia usalama wake kwanza kabla hajaendelea na oparesheni zingine."


Johnson akatoa picha zingine na kuzionyeshea. Picha hizi zilikuwa zinamuonyesha Naibu akiwa akiwa anatembea sasa kutoka glosari.


"Baada ya Naibu kumaliza mvinyo wake, alitoka glosari hapo akitumia njia ya uchochoro. Alilaghai kama anaenda chooni, lakini akakatiza kando na kuiruka fensi ndogo ya maua ya glosari. Alielekea mpaka kwenye kibanda cha simu za jumuiya kinachopatikana karibu na glosari hiyo. Aliacha gari lake kwenye parking. Na hii ndiyo inayotoa picha halisi kwamba alikuwa amefuata simu pale, na si kinywaji.


Sema maswali yanakuja, kwanini aliacha gari lake parking na kwanini alilifanya tendo hili kwa usiri hivi? Kwanini pia alikuwa anaenda kutumia simu ya jumuiya na si ya mkononi?


Yote haya ni kuhakikisha usiri. Usiri ambao ndio unazua maswali na kuzaa mashaka.


Aliongea kwenye simu kwa dakika kadhaa. Bado alikuwa anatazama tazama kuhakikisha usalama."


Johnson alitoa tena picha akaonyeshea. Zilikuwa mbili kwa idadi. Zilikuwa zinamuonyesha Naibu huyo akiwa kwenye kibanda cha simu akitazama nyuma.


Kwa namna picha hizo zilivyokuwa zimepigwa, zinaweza kukuachia maswali juu ya uweledi wa mpigaji wake. Zilipigwa katika namna ambayo ilimtoa vizuri mhusika, tena kwa usiri mkubwa mno!


"Alimaliza kuongea na simu akarejea glosari. Alikaa hapo na punde akaondoka zake kurudi nyumbani," Johnson alimalizia taarifa yake hiyo akafunga faili.
"Kama unavyojua mkuu, ni ngumu kupata taarifa za mteja anayetumia simu za vibandani. Na hili ndilo haswa lengo la Naibu kutekelezea mawasiliano yake kibandani hapo."
"Sawa sawa," Al Saed alisema akitikisa kichwa. Alishusha pumzi ndefu kabla hajauliza:
"Na vipi kuhusu huyo mjumbe?"


Hapo Rambo, mwanaume aliyeketi karibu na Johnson, akateka zamu. Alifungua faili lake rangi ya chungwa akisema:
"Mjumbe nitakayemuongelea hapa ni huyu." Rambo alionyeshea picha. Al Saed aliitazama akiendelea kuskiza.
"Mjumbe huyu kuhusika kwake kunarandana na na yule wa kwanza ambaye ni Naibu wa kamati ya ulinzi. Huyu mjumbe ndiye alikuwa mtu wa kwanza kabisa kukutana na Naibu wa kamati ya ulinzi. Alikutana naye asubuhi na mapema jana. Lakini pia baada ya matukio, yani jioni wakakutana tena. Na mpaka tunakuja kwenye kikao, wamekutana tena majira ya mchana."


Rambo alitoa picha tano akazionyeshea.


"Mara ya kwanza walikutania nyumbani kwa Naibu, kama unavyoweza kuona hapo picha ya gari la mjumbe likiingia ndani ya jengo la Naibu. Ila mara zilizofuata wamekuwa wakibadili maeneo. Wamekuwa wakikutana kwa siri, na mara ya tatu walipokutana kuna mwanaume mmoja mgeni walikuwa naye. Alikaa kwa muda mchache akaondoka,"


Rambo akaonyeshea picha.


"Huu ukaribu wa hawa watu, na vikao vyao kwa muda mchache hivi, vinasababisha mashaka na hata kutufanya tuwatuhumu kwa pamoja."


Al Saed alichukua mafaili yote, la Rambo na Johnson, akayaweka karibu naye. Alivunja kikao kwa kutoa agizo la watuhumiwa wote kutiwa nguvuni mara moja. Lakini pia akamteua mwanajeshi yule mnusurika, James Peace, kuwa msimamizi wa usalama tangu muda huo.


"James, bila shaka umehama makazi na umedumishiwa usalama maradufu. Nataka hawa washenzi waliobakia wamalizwe upesi! Chagua wanaume kumi unaowaamini, kwenye kikosi chochote kile. Hakikisha mnapanga mipango yenu na kuja kuniona. Mtashirikiana pamoja na Rambo na Johnson."


Al Saed akasimama.


"Haya, twende msibani sasa."


Wakiwa wanatoka, wanakutana na askari mwanajeshi mmoja aliyewahi kupiga saluti na kusimama kwa ukakamavu. Askari huyo mwanaume alikuwa mweusi. Uso wake ulikuwa umejaa umakini jasho likimchuruza.


"Vipi?" Al Saed alitahamaki.
"Mkuu!" Askari alipaza sauti. "Tumeshambuliwa mara nne kwa mabomu. Mji unateketea!"



****

☆Steve
 
*Njia nyembamba --- 22*



*Mtunzi: SteveMollel*










Kwa kutazama tu uso wa Al Saed ungelifahamu ni kwa namna gani habari hizo zilimgusa. Macho yalimtoka na uso ukawa mweusi kwa haraka mno. Kwa muda alichanganyikiwa akiwa hajui la kufanya. Alisaga meno akikunja ngumi.


"Sawa, tutacheza kwa mujibu wa ngoma!" Alijikuta akisema.


Mara aliamuru naibu mwenyekiti wa kamati ya ulinzi pamoja na mjumbe mtuhumiwa wauawe, tena kwa kunyongwa, punde tu baada ya kuwafanyia mahojiano. Hakutaka hata kuwatia machoni.


"James!" Aliita. "Hamna muda wa kujiandaa tena. Kakusanye watu wako na muanze oparasheni mara moja!"


Aliwatazama Rambo na Johnson, nao akawaambia:


"Unganeni na James. Malizeni wale wasaliti kisha mkakate vichwa vya hao magaidi na kuniletea hapa!"


Haraka James na wenzake wakatoka kwenda kutekeleza amri. Al Saed alirudi ndani akajiandaa na kutoka kwenda kufanya ziara maeneo yaliyorudhika na milipuko.


Loh! Ilikuwa inatisha kuona. Jiji la Monrovia lilikuwa linateketea kama moto wa kifuu. Moto mkali mkubwa ulikuwa umetawala mitaani ukitafuna majengo. Zimamoto wachache waliokuwepo hawakuweza kabisa kuumudu.


Al Saed alistaajabu sana kuona moto huo. Alihisi mwili unaishiwa nguvu. Jasho jepesi lilimteremka. Macho yake yaliweka ukungu wa machozi. Moyo ulimuenda mbio sana akipaliwa na ghadhabu kuu.


Kila eneo lilikuwa limeshikwa na vilio. Kama siyo rafiki, basi ni ndugu ama jamaa alikuwa amekwapuliwa uhai na milipuko hiyo. Wengine walilia kwa hofu juu ya kesho yao iliyoonekena ni ya kubahatisha, wakati wengine wakizirai kwa kushindwa kuhimili.


Ilikuwa ni ndani ya muda mfupi tu maisha yalikuwa yamegeuzwa juu chini, chini juu, mikono ikashika vichwa. Simanzi ilizizima.


"Ni maeneo gani haswa yalilengwa?" Aliuliza Al Saed. Alikuwa amesimama kando na afisa wa kikosi cha zimamoto na uokoaji: mwanaume mnene mweusi aliyevalia nguo za kazi.
"Jengo kuu la makutano ya biashara," alijibu afisa zimamoto. "Soko kuu na makutano ya maduka, mkuu."


Al Saed akasonya kwa masikitiko. Maeneo hayo tajwa yalikuwa ni maeneo yanayokuwa na idadi kubwa ya watu kutokana na mizunguko yake ya kibiashara. Ni maeneo ambayo ni vitega uchumi vizuri vya taifa.


Alishusha pumzi ndefu, akakamata kiuno chake akitazama anga la Liberia. Alijaribu, akilini, kukokotoa idadi ya watu watakaokuwa wamekufa na kujeruhiwa. Hakutaka hata kuuliza maana alihisi angeutoboa moyo wake.


Alishuhudia namna watu wanavyowahishwa hospitalini wakiangua kilio, ama wengine wakiwa hawajiwezi abadani.


Akiwa anaongozana na walinzi wake watatu, alitembea akikatiza mitaa. Akifariji na kutia watu matumaini. Matumaini ambayo yalikuwa kama vumbi jepesi kwenye pepo ya bahari. Macho ya wahanga yalikuwa yamebeba maumivu, na hasira.


"Sitaki kuongea chochote!" Alisema Al Saed akiwatazama waandishi wa habari waliokuwa na kiu ya kusikia neno toka kwake. Waandishi hao walijazana punde tu walipojua uwepo wa kiongozi huyo mkuu maeneo hayo.


"Kiongozi, naomba utuambie msimamo wa serikali yako kuhusiana na hili?" Ilisikika sauti moja ya mwandishi wa habari.


Al Saed alishindwa kupuuzia swali hili. Aligeuza shingo yake akamtazama mwandishi aliyeuliza.


"Msimamo wangu ni kuwaua wote waliohusika na haya mauaji," alijibu na kuongezea, "hakuna yeyote atakayetoka salama. Na wote nitawanyonga chaneli ya taifa ikionyesha mubashara."


Baada ya kusema hivyo basi kazi ikawa kwa walinzi kuwazuia waandishi kwa kuwasukumizia kando wasimbughudhi mkuu kwani hawakukaukiwa maswali, bado waliendelea kuyatiririsha.


Al Saed akipuuzia maswali hayo, alitoa simu yake mfukoni akapiga. Alikuwa anataka kuulizia oparesheni aliyoiagiza. Upande wa pili, bwana James alipokea simu hiyo mara moja!


"Tayari tumewashawatia wote nguvuni, mkuu. Tupo nao tunawahoji muda huu!" James alinguruma hewani.
"Safi sana," akasema Al Saed akitikisa kichwa. "Wabane wawatajie hao wauaji wenzao. Baada ya hapo malizeni kabisa!"
"Sawa, mkuu!"
"James, nataka mrejesho wa maana."
"Bila shaka, kiongozi. Tutafanya kila liwezekanalo."


Simu ilipokatwa, James aliwatazama walengwa wake waliokuwa wamefungwa kwenye viti: naibu mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na mjumbe wake. Watu hawa walikuwa wamelowana damu, sura zao zikitepeta kichapo.


Mkononi mwa James kulikuwa kuna spana kubwa ya chuma. Spana hiyo ilikuwa imechafuka damu. Hata mikono ya James pia ilikuwa mekundu kuashiria imeshika majeraha.


"Sasa tunaingia kwenye awamu ya pili," alisema James. Uso wake haukuwa na masikhara. Mdomo wake aliubinua katika namna ya kuonyesha kebehi.
"Unataka nini tena na nimeshakuambia?" Alilalama mjumbe kwa tabu. Macho yake yalikuwa yamevimba. Mdomo wake ulikuwa unachuruza damu, huku ngao za mashavu yake zikiwa zimejazwa majeraha.
"Hujaniambia ni wapi naweza nikawapata hawa walipuaji!" Alisema James akitikisa kichwa.
"Kwasababu sijui wapi utawapata," akajibu mjumbe. "Hawana makazi ya kudumu kwa sasa tangu makazi yao ya kule kijijini yalivyoharibiwa. Wanakaa popote pale!"


James alikuna kidevu chake. Alimtazama Naibu mwenyekiti wa kamati ya ulinzi, akamuuliza;


"Nani anafadhili hicho kikundi?"
"Sijawahi kuambiwa. Si kila kitu nafahamu kuwahusu," alisema Naibu. Uso wake ulikuwa umevujishwa damu za kutosha kukufanya upate shida kumtambua.
"Kama nilivyokuambia hapo awali, walikuwa wananitumia kwasababu ya kuhofia usalama wangu. Kama ningeliwageuka basi wangelinimaliza."
"Muongo!" Sauti ya Mjumbe ilidakia. James aliyarusha macho yake upesi kwa Mjumbe huyo.
"Wote tulifanya hii kazi kwasababu ya ahadi!"
"Ahadi gani?" Aliuliza James upesi.
"Tuliahidiwa maisha mazuri, na vyeo vinono serikalini," alijibu Mjumbe. Alikuwa anapata wasaa mgumu sana kuongea.


James alitikisa kichwa chake akisema:
"Sawa, sasa tunakaribia kumaliza zoezi letu." Alimgeukia Naibu akamwambia:
Ningependa kukupa nafasi yako ya mwisho ya uhai kwa kusema ukweli. Ni maeneo gani ninapoweza kwenda kuwatafuta hawa watu mbali na kule kijijini?"


Naibu alimtazama James kwanza. Aliona namna gani uso wa James ulivyokuwa mkavu. Alishusha macho yake chini akiyaambatanisha na pumzi ndefu. Akataja maeneo matatu anayohisi yanaweza yakawa yanakaliwa na wanamgambo wa AMAA.


Alipotoa taarifa hizo, James aligeuka malaika Israel akanyofoa roho zao akiwanyonga kwa mikono yake mwenyewe. Kisha akapiga simu kuwataarifu wenzake.

***

Ndani ya sebule ndogo yenye samani zilizopangiliwa vema. Picha kubwa ya farasi wawili; mweusi na wa kahawia ilikuwa inaning'inia ukutani. Mezani kulikuwa kuna bakuli kubwa la kioo likibebelea matunda mbalimbali.


Pembeni ya meza hiyo kulikuwa kuna makochi mawili tu ya ngozi rangi kahawia. Kila kochi likiwa limeegemea dirisha kubwa la chuma.


Sebule hiyo ilikuwa pweke, na kulikuwa kimya. Ila baada ya muda mfupi, sauti zilisikika nje ya sebule. Ilikuwa ni ya mwanaume na mwanamke. Sauti hizo zilisogea karibu na sebule na mara mlango ukafunguliwa.


Alikuwa ni Kone na Rose. Kone alikuwa amevalia kaunda suti rangi ya udongo, Rose alikuwa amejisitiri kwa kuvalia bukta ya kitenge na tisheti jeupe.


"Karibu!" Alisema Rose akitabasamu.
"Ahsante sana, Rose. Nimeshaingia sasa."


Kone aliketi, Rose akamletea kinywaji; juisi ya embe ndani ya glasi kubwa. Kone hakutaka chakula.


"Kazana kula, Rose. Umekonda sana," Kone aliteta. Rose akatabasamu.
"Kwani nimekuwa mbaya?" Aliuliza.
"Hapana, sema sijazoea kukuona hivyo. Naona kama unaumwa."


Kwa mtu ambaye hakuwa anamfahamu Rose hapo kabla, asingegundua tofauti yoyote ile kwa mwanamke huyo. Bado alikuwa mzuri na mwenye kuvutia. Hakuwa ametia kikorombwezo chochote usoni mwake, lakini aliita.


"Itabidi uzoee, Kone. Nataka kubakia hivi hivi niweze kufanya kazi yangu vizuri."
"Kazi ipi?"
"Ya kummaliza Talib! Siwezi nikamuacha hata kidogo kwa namna alivyon'tendea. Lazima nimmalize kwa mikono yangu mwenyewe!"
"Si rahisi kihivyo, Rose."
"Najua. Nitaenda na ugumu wake hivyo hivyo. Lazima nimuue, mara hii niende jela kwa kustahili!" Rose alipiga ngumi paja lake kwa msisitizo.
"Nisingependa kukupoteza, Rose," Kone alisema akimtazama mwanamke huyo machoni. "Kuna mambo makubwa na muhimu sana tunapaswa kuyatekeleza. Na mambo haya si tu kwa faida yetu bali kwa taifa zima."


Rose alimtazama Kone kwa umakini. Alikitikilia maanani kila litokalo kinywani mwa mwanaume huyo.


"Hapa tunavyoongea, Guinea ipo kwenye hali mbaya. Vita yaweza kutukia siku yoyote. Natilia mashaka sana juu ya uchaguzi huu unaokaribia, hauwezi kuisha kwa amani ... sasa nataka tukaokoe jahazi nyumbani, Rose."

"Umejuaje kuhusu haya, Kone?" Rose aliuliza, na kuongezea: "Ni kwa muda mrefu sina habari juu ya kinachoendelea huko."
"Ni habari ndefu kidogo nitakayojaribu kuifupisha ..."


Maongezi hayo hayakudumu, mara yakakatishwa na mlio wa ujumbe kwenye simu ya Kone. Mwanaume huyo alitoa simu yake mfukoni akaitazama. Alikuwa Amadu.


"Kama una muda, naomba tuonane nje ya makazi yako sasa hivi." Ujumbe ulisomeka hivyo.
"Sawa, nakuja." Kone akajibu upesi.


Rose aligundua mabadiliko kwenye uso wa mwanaume huyo. Alipata hamu ya kujua, akauliza:
"Vipi Kone kuna nini?"


Kone akamueleza juu ya Amadu.


"Tunaweza kwenda wote?" Rose aliuliza. Macho yake yalijawa na ashki. Alikuwa tayari ameshasimama.
"Ngoja kwanza," Kone akamtuliza, kisha akamtumia ujumbe Amadu juu ya ujio wake na Rose.
"Unamuamini?" Ujumbe wa Amadu uliuliza.
"Ndio, namuamini sana," Kone akajibu.
"Sawa, unaweza kuja naye." Akapewa ithibati.


Rose alijiandaa upesi kwa kuoga na kujivika suruali, kisha wakatimka na Kone kwenda mahali walipoelekezwa na Amadu wakutane. Walifika eneoni wakakuta patupu.


Amadu alikuwa ameketi kando akiwatazama. Zilipopita dakika tatu akihisi shwari, ndipo akajongea kuwafuata. Alikuwa amebebelea begi kubwa jeusi mgongoni. Alivalia tisheti jekundu, suruali nyeusi ya jeans na viatu vya wazi.


Alisalimu kisha akapendekeza wakafanyie maongezi yao ndani ya gari alilokuja nalo; Suzuki Vitara. Pendekezo hilo likaungwa mkono na wote.


"Kuna jambo nimeona ni vema nikakushirikisha Kone," alisema Amadu. Alikuwa amekaa viti vya mbele yeye na Kone wakati Rose akiketi nyuma. "Si tu kwamba kwasababu linakuhusu, bali unaweza ukatoa mchango wako mkubwa sana.


Kwa muda mrefu sasa, mimi na wenzangu tulikuwa tumetenga muda wa kuchambua mambo kwa kina kuhusu siasa za huu ukanda wetu. Na yote hiyo ni kwasababu tuliona hatuwezi tukatibu nchi moja wakati zingine zikiendelea kuumwa, kwa maana nchi hizi huambukizana, huathiriana kwa namna kubwa mno. Kwa Liberia kuwa na amani, basi Sierra na Guinea zinapaswa kuwa tulivu. Vilevile kwa Sierra na Guinea. Hakuna anayebaki salama wakati mwenzake akiwa vitani.


Tulikuja kugundua kwamba, unaweza ukawa unaipigania nchi yako ndani ya nchi jirani. Ukahangaika kusuluhisha na kumaliza migogoro yao kwa ajili ya kwako kuwe hai, kwasababu mbegu ya chuki, uhasama na ukabila huzaa mti mpana wenye matawi marefu yanayoziba mwanga wa jua. Siyo tu kwa aliyepanda, hata pia kwa majirani. Nyoka watakaokaa hapo, hawatamng'ata tu mwenye nyumba, bali pia na jirani.


Hivyo basi kuukata mti huo si kazi ya mwenyenyumba pekee, yumo pia na jirani.


Kulitambua hilo kukatupa nguvu na haja ya kusambaza watu wetu kila kona ya nchi hizi. Watu hawa kazi yao ilikuwa kuwa macho na masikio. Waone kila liendalo, wasikie kila lisemwalo. Kazi yao ilikuwa kukusanya taarifa za kutosha, za kina, ili tujue nani chanzo, nani mtekelezaji, nani funiko.


Katika hilo tukafanikiwa, kilichobakia sasa ni utekelezaji. Hapa tuongeavyo, kikundi cha THE GHOST kipo tayari muda wowote kuanza kuisaka shwari. Katika hili, ningependa tuwe pamoja.


Ila pia ningependa kukupa wasaa wa kufikiria."


Amadu alifungua begi akatoa mafaili matatu na kumkabidhi Kone. Kila faili lilikuwa lina rangi yake, na juu ya kila faili kulikuwa kuna jina la nchi moja miongoni mwa Sierra Leone, Liberia na Guinea.


"Kwenye kila faili, kuna picha na maelezo ya kila mmoja tunayetakiwa kummaliza, pia sababu na njia za kufanya hivyo. Chukua muda wako kapitie, alafu utanipa mrejesho karibuni.


Muda si mpenzi wa kweli," Amadu alihitimisha.



****


☆Steve

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Katafute ninapotoa. Ukipata leta hapa yote. Alafu mtaarifu na mtunzi kwamba namuibia. Sawa?

Sent using Jamii Forums mobile app
Tivuu achana nao bana hao wanaponda na kusoma wanaendelea kaa kimya
Sasa mzee wangu ningekuwa natoa sehemu si ndo ningekuwa nazimwaga hapa daily. Au wewe ndo una mpango wa kuichukua? Anyways naandika hii simuliz kwa mikono na akili yangu mwenyewe ma ndiyo maana kuna muda najikuta nakosa muda wa kuiendeleza maana mpaka nikae na kuandika.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Back
Top Bottom