Njia nyembamba (Simulizi mpya by SteveMollel)

Njia nyembamba (Simulizi mpya by SteveMollel)

Stevemollel naomba uweke na zile arrears kwa kipindi ulichopotea
Natanguliza shukrani

Sent from my VFD 1100 using JamiiForums mobile app
 
NJIA NYEMBAMBA --- 17




Mtunzi: SteveMollel





Taswira ya jiji la Freetown ilikuwa imefifia, halikuwa linatamanika tena. Magari yalikuwa machache na hata watu pia. Ungeweza kusema ni jangwa, ama mji wenye watu wachache kabisa juu ya uso wa dunia. Hii yote ilitokana na upungufu maradufu wa usalama nje ya milango. Bado maandamano, tena yanayoambatana na vurugu kali, yalikuwa yanaendelea kuzizima ndani ya jijii. Hakukuwa salama.

Watu kadhaa waliripotiwa kuuawa wengine wakijeruhiwa vibaya. Makundi ya watu walioongozwa na hamu kali ya kuuondoa utawala wa Talib walirandaranda huku na kule kuutafuta ushawishi. Kila mwananchi alitakiwa kuwaunga mkono la sivyo angelionjeshwa joto. Haikuwa ombi sasa kumpinga Talib, bali ni amri! Kwa yule aliyekaidi angeachwa anatiririka mito ya damu.

Ikiwa ni majira ya mchana sasa wa saa nane, ndani ya nyumba kubwa mno nyeupe inayovutia machoni, chumbani, anaonekana naibu kiongozi wa ulinzi wa taifa: Meja jenerali Edward Simon akiwa amevalia nguo za kutafutia joto. Ingawa kiyoyozi kilikuwa kinapuliza kwa wingi, bado alionekana kutotosheka.

Chumba kilikuwa kikubwa kama uwanja wa mchezo wa tenesi. Kitanda kilitapakaa kikiwa kimefunikwa na sufi laini nzito. Madirisha, mawili, yalikuwa mapana mno kiasi cha kutengenezea milango. Viti na meza, pamoja na maua feki yaliyokuwa chumbani humo, kwa macho tu, yalieleza bei yake ya kikubwa. Palikuwa pazuri mno usitamani kutoka ukiingia.

Ni siku ya tatu sasa meja jenerali huyu hajaenda ofisini kwa sababu ya usalama. Amekuwa akibakia ndani kwake tena akiwa amezungukwa na wanajeshi kadhaa waliobebelea silaha za kisasa. Mke na watoto wake wawili pia walibakia nyumbani, shule na shughuli zao zikisitishwa kwa muda usiojulikana.

Mitaani hakukuwa shwari. Wanajeshi si wengi kama wananchi. Hata kwa wingi wao silaha bado hakufui dafu. Wananchi hawana sare hivyo basi haujui yupi aliye mawindoni na yupi aliye mafichoni, yupi anataka tabasamu lako ama damu yako!

Mwanamke mnene aliyevalia taulo pekee kifuani anaingia chumbani akitokea kwenye bafu. Mwili wake umejazwa na matone matone ya maji. Kichwani amejifunika na taulo dogo jeupe kama pamba. Mwili wake rangi ya maji ya kunde wenye umbo zuri la chupa. Ila uso wake ulikuwa wa mwanamke mchanga. Alionekana mdogo asiye hata na miaka ishirini na tatu.

“Mpenzi,” mwanamke huyo aliita akijifuta kichwa na taulo. Meja akamtazama mwanamke huyo pasipo kusema jambo.

“Nahitaji kutoka mara moja leo.” Alisema mwanamke.

“Kwenda wapi?” Akawahi kuuliza Meja.

“Kwa rafiki yangu – Diana.”

“Una matatizo gani Sarah? Utaacha utoto lini wewe? Hivi niwe nakuimbia kila siku kwamba huko nje si salama?”

“Sasa mpenzi, tutakaa humu ndani mpaka lini? Si nitaongozana na walinzi? Shughuli zangu nyingi zinakwama.”

“Shughuli zipi hizo?”

Mwanamke akaguna, “basi yaishe.”

“Au unataka kwenda kwa hivyo vijana – vijana vyako huko?”

“Sasa hayo yanaingiaje hapa?”

“Nakwambia hivi, nikija kugundua unaendelea na huo ujinga wako. Nitakuua!”

Mwanamke akaguna kwa kubinua mdomowe.

Si bure kwa Meja kuhofia. Umri wake ni kama mara tatu ya binti huyu mchanga mrembo, ni wazi mwanamke huyu anaweza akawa anatafuta injini zingine huko nje zenye moto zaidi, pengine.

Mwaname alifuata kabati lake la nguo akalifungua. Lilikuwa limesheheni nguo. Akiwa anatazama ni nguo ipi inayoweza kusitiri mwili wake, mara sauti kali ya mlio wa risasi inasikika. Anashtuka! Anageuka upesi kumtazama mumewe akitumbua macho.

Meja alikuwa tayari ameshasogea dirishani kuchungulia.

“Kuna nini?” Sauti ya hofu ya mwanamke iliuliza.

Meja hakujibu, aliendelea kukazana kutazama. Ila baada ya sekunde chache aligeuka akamtazama mkewe kwa sura yenye mushkeli wa mashaka.

“Watoto wapo wapi?” Aliuliza.

“Kuna nini?” Mwanamke akajibu kwa swali. Alikuwa ameshapata woga, mikono yake ikitetemeka.

Milio ya risasi iliita tena, mara hii mara tatu kwa fujo kuu! Mwanamke alichanganyikiwa akakimbilia kufungua mlango.

“Watoto wanguu!” alipiga yowe. Alitoka chumbani haraka akakimbilia sebuleni alipoangaza na kisha haraka akaenda vyumbani, akatoka na watoto wawili wa kike. Walishika korido, wakakutana na Meja, mkononi alikuwa amebebelea bunduki ndogo.

“Nendeni chumbani mjifungie!” Aliagiza Meja, mwanamke akiongozana na watotowe wakazama chumbani na kuupiga mlango kufuli.

Meja alisogelea sebuleni. Kulikuwa kuna kelele za watu huko nje. Aliangaza macho yake upesi akaona simu ya mezani, aliikimbilia apate kupiga. Aliinyakua simu hiyo haraka akaiweka sikioni na kubofya namba kadhaa. Simu ikaita.

Makelele ya watu, yakiwa ni ya kufoka, yalizidi kuongezeka. Yalisikika yakikaribia mlango, na bado simu haikuwa imepokelewa.
Macho ya Meja yalitazama mlangoni kwa mashaka. Mkono wake uliobebelea bunduki ulielekea pia huko. Alilaani kwanini simu haipokelewi, alichanganyikiwa. Punde mlango unagongwa na mara unavunjwa!

Haikudumu muda mrefu, mwanamke aliyekuwepo chumbani, anasikia sauti ya risasi inayojibiwa na risasi nne huko sebuleni. Walikuwa ndani ya kabati yeye pamoja na wanawe wakiwa wamejikunyata kama wanaosikia baridi kali.

Sauti za kufoka na kuropoka zinaendelea. Kwa mujibu wa sauti hizo waweza sema kulikuwa kuna idadi toshelezi ya watu. Sauti hizo zinaruruma, zinasogea karibu chumbani, baada ya muda mlango unavunjwa. Hapo kabla ilisikika milango miwili ikitendwa vivyo hivyo.

“Wako wapi?” Sauti moja inauliza. Kwa kupitia ka-mwanya ka mlango wa kabati, wanaonekana wanaume kama nane hivi, watatu wakiwa wamebebelea bunduki kubwa ndefu na wengineo wakiwa wamebebelea mapanga.

“Tafuteni! Tafuteni kila sehemu!” Inatoka amri kwa mmoja wao. Wanaume hao wanagawanyika kutazama huku na huko. Punde kabati linafunguliwa, mwanamke na watoto wake wanatolewa kwa nguvu. Wanarushiwa sakafuni kama mizigo.

Taulo liliacha mwili wa mwanamke, akabakiwa mtupu: mbele ya watoto na wageni wake wa lazima.

“Naam! Wewe si miongoni mwa wale wanaokula jasho letu, sasa leo utaliwa wewe!” alisema mwanaume mtoa amri. Macho yake yalikuwa yameshatepeta uchu.

Pasipo kujali kama kuna watoto, alivua suruali. Mwanamke alilia, pamoja na watoto pia wakiomba mama yao aachwe, hawakusikilizwa. Mbele ya macho ya watoto, mama akabakwa kwa zamu mpaka alipopoteza fahamu.

Wanaume walimaliza haja zao, wakammaliza mwanamke huyo na watoto wake kwa kuwakatakata mapanga. Palitapakaa damu kana kwamba machinjioni. Viungo vilitenganishwa mwili ukipasuliwa kama kuni.

Watu hawa hawakuwa hata na lepe la huruma. Waliwakata binadamu wenzao kana kwamba wanamkata mnyama. Walipomaliza wakatokomea.


***


NDANI YA KUNDI LA WHATSAPP …


“Tukutane wote kwenye mazishi ya Bernard pasipo kukosa.”

“Tutafika kumpumzisha mpambanaji mwenzetu.”

“Nani anayefuata kwa sasa baada ya yule mbwa tuliyempeleka jehanamu?”

“Tutalitazamia hilo siku za usoni.”

“Unajua haya mambo yanahitaji utulivu na mipango.”

“Ni kweli.”

“Kweli, tusije tukaingia mkenge.”

“Unachokisema ni sahihi.”

“Ila tutampata mwingine mwenye mwanamke mtamu kama yule malaya?”

Viwanasesere vya kufurahi vinatumwa kwa wingi kundini.

“Aisee yule mwanamke ni mzuri bwana. Hata tukimkuta mwingine ni bibi, tuwafanye tu! tena sasa hivi wakiwa wanaona tunavyowashughulikia wake zao kama wao walivyotushughulikia kwa muda wote huo.”

“Wazo zuri!”

“Tunaweza tukanogewa tukakamatwa.”

“Ni muda wa hawa watu kuumia. Hawastahili kufa hivihivi.”

“Hey, tukutane kwenye mazishi ya Bernard. Tutaongea na kupanga mengi huko.”

“Mustafa anasisitizia tusikose kufika.”

Jumbe zinaendelea kutiririka na kutiririka, mamia.


***


Mwanga wa simu ulifukuza kagiza kalichoanza kujirundika chumbani. Ilikuwa ni majira ya jioni sasa lakini chumba hakikuwa kimewashwa taa. Mwanga huu wa simu ndani ya kiza unadumu kwa sekunde kadhaa kabla ya mlio wa soketi kuita, na mara chumba kinakuwa cheupe.

Anaonekana Kone akiwa amevalia bukta fupi nyeusi ya drafti drafti. Mkononi mwake alikuwa amebebelea simu, ile iliyokuwa inatoa mwanga. Anaitazama tena simu hiyo kabla hajayarusha macho yake kwa bi Fatma aliyekuwa amejilaza kitandani.

Mwanamke huyo alikuwa amejifunika kwa nguo nyepesi iliyosadifu mwili wake vema. Alionekana amechoka, mdomo wake ulikuwa wazi akikoroma kwa mbali.

Kone aliweka namba fulani kwenye simu yake alafu akapiga, namba haipatikani. Alijaribu tena, bado majibu yalikuwa hayo hayo. Alisonya akamuamsha mkewe kwa sauti chovu.

“Bado hapatikani,” alisema. “Inabidi niende kwake sasa.” akaongezea.

“Kuwa makini sana, Kone,” alisema Fatma mwenye mang’amung’amu ya usingizi. “Inawezekana kuna kitu kikawa kimemtokea kikakuweka nawe hatarini.”

“Najua hilo, usijali. Lazima Rose atakuwa yupo shidani, hii si kawaida. Alikuwepo wakati nikimuhitaji, na sasa ni wakati wa mimi kuonyesha kujali kwangu.”

“Lakini … huoni kama unaweza kuharibu kote kote, Kone. Tutakimbilia wapi?”

Kone aliweka mkono wake begani mwa Fatma. Akamtazama katika namna ya kumuondoa hofu.

“Niachie mimi, najua cha kufanya.”

Alinyanyuka akatumia dakika kumi tu kujiandaa. Alivalia suruali nyeusi ya kadeti pamoja na tisheti nyeupe iliyofunikwa na koti kubwa refu rangi ya kaki lenye vifungo vinene. Aliaga akaondoka.

Akiwa yu njiani, ndani ya gari lake, kuelekea kwa mwanamke Rose, mawazo yanakula kichwa chake. Mwanzoni alikuwa anafikiria usalama wa Rose kwenye mikono ya mshenzi Talib, ila baadae, katika kasi ya ajabu, mawazo juu ya mkewe yalimparamia.

Usiku wa kuamkia siku hiyo haukuwa mwepesi kwake hata kidogo. Ulikuwa ni usiku wa mzozano na malumbano baina yake na mkewe. Ulikuwa ni usiku wa kukata mzizi wa fitna, kudadavuliana kwanini na sababu za mambo mbalimbali, haswa mahusiano ya Fatma na marehemu Raisi wa Guinea.

Ukweli una gharama kubwa, waliwahi sema wahenga. Japokuwa Kone aliuhitaji ukweli, ulimuumiza. Alipata kujua mambo kadhaa ambayo yaliutoboa moyo wake na kuufanya chujio. Akili yake ilitibukwa na nyongo ikapasuka.

Ni baada tu ya miaka miwili ya yeye kuwa kazini kama mhusika muhimu kwenye usalama wa taifa, alijikuta anateuliwa kuwa mtu muhimu kwa usalama wa Raisi. Maisha yalienda kasi sana. Aliaminiwa sana na Raisi akapewa kazi ambazo hakustahili, bali wale walio juuye.

Kwa muda wote huo alikuwa akiamini kazi, vyeo na mshahara wake mnono ni majibu ya kazi yake aliyoifanya kwa utashi mkubwa. Kumbe lah! Jasho na damu aliyoimwaga kwenye uwanja wa vita, huku na kule, havikuwa vishawishi hata kidogo, bali mkewe, bi Fatma.

Mkono wa Raisi uliokuwa unampapasa mkewe pindi anaposafiri, ndio huo huo uliokuwa unatia saini kwenye izimisho za mishahara na cheo chake. Hili lilikuwa chungu.

Ilikuwa ngumu kwake kuamini. Hapana. Hapana. Hapana. Alisema na moyowe. Ila Bi Fatma hakutaka kumficha, alimweka wazi. Hakuna yeyote aliyekuwa anajua mchezo huo isipokuwa mke wa Raisi aliyewahi kuwafumania siku moja wakiwa Ikulu. Na hiyo ndiyo sababu mke huyo, wa Raisi, akajiondokea.

Moyo wa Kone ukawa mgumu mno kama jiwe, aliuhisi kifuani ukiguruguta kama wataka kuchomoka. Alijizuia sana kutoa machozi siku hiyo. Alijikaza kisabuni mwanamke andelee kumwaga mboga.

"Sio kwamba nilifanya hayo kwasababu ya kazi yako tu, bali pia na usalama. Kuna kipindi alinitishia endapo nisipofanya anayoyataka, basi atateketeza familia yangu. Nilishindwa kumkwepa kila ulipokuwa unaondoka kwani alikuwa anajua ratiba zako. Ndio maana nilikuwa nakusisitizia sana ubaki nyumbani japokuwa sikuweza kukwambia haswa kwanini."

Maneno hayo yalitafuna mtima wa Kone. Aliambiwa usiku wa kuamkia siku hiyo lakini ni kana kwamba aliambiwa dakika moja tu nyuma. Aliyasikia yakiimba vizuri masikioni mwake. Yalimuumiza.

Alijitahidi kujikomboa toka kwenye mawazo hayo, ikawa ngumu. Ni mpaka pale kafoleni kepesi kalichokuwa kamemzinga kalipoanza kutembea, basi ndipo akili yake ikahamia barabarani. Alitembea mpaka karibu na jengo la Rose, ilikuwa majira ya saa tatu usiku, akarusha macho yake getini. Aliwaona wanaume watatu ndani ya jezi za jeshi wakiwa wamebebelea bunduki.

Alisogeza gari lake mbali alafu akalizima na kutoka ndani akiwa amebebelea bunduki ndogo.

Tusijue kwa namna gani, Kone anaingia ndani ya jengo pasipo walinzi kushtuka hata kope. Anazama mpaka ndani, mfanyakazi, aliyekuwa jikoni, anashtuka akiitwa kwa kunong'oneza.

"Ssshhhhh! ... ni mimi, Kone. Unanikumbuka?"

Mfanyakazi anatikisa kichwa chake kwa uoga. Haraka mwili wake ulianza kutetemeka.

"Mimi rafiki yake Rose. Hukumbuki nilishawahi kuja hapa?"

Hofu iliziba kumbukumbu ya dada wa kazi. Alifanya jitihada za ziada kumkumbuka Kone. Bahati nzuri haikuchukua muda mrefu.

"Ndio, nimekukumbuka!"

"Rose yupo wapi?" Kone aliwahi kuuliza.

Dada wa kazi alibanwa kigugumizi. Ilimbidi ashushe pumzi kwanza kabla hajateta:

"Dada amechukuliwa na wanajeshi, walisema wanampeleka jela!"

Alieleza tukio zima lilivyokuwa, Kone akaishiwa nguvu kwa upungufu wa matumaini. Ni jela gani atakayokuwa amepelekwa Rose? Hakuweza hata kubashiri. Kichwa chake kiliingia kazini upesi, punde akapata jibu, ila jibu hili lilikuwa na ukakasi: njia yake ya mafanikio ilikuwa nyembamba.

Yuko radhi kuipita?

Hakukuwa na namna sasa, ilimlazimu Kone awarudie wale walinzi getini. Kwa namna moja ama nyingine watakuwa na majibu ya maswali yake kadhaa. Alijaribu sana kulikwepa hili, ila halikuwezekana. Hiki kikombe kilikuwa chake.



***


Post sent using JamiiForums mobile app
 
*Njia nyembamba – 18*

Alirudi huko kwa utulivu na ukimya. Alichungulia nje, akaona ni shwari. Alitoka ndani ya jengo asogelee geti, lakini upesi akamuona mlinzi mmoja aliyebebelea bunduki, haraka akajificha kwenye mgongo wa mti mmojawapo uliomo humo ndani.

Alitulia hapo akimtazama mlinzi. Alingojea kidogo tu, mlinzi akasogea karibu kabisa na yeye. Upesi alimdaka akamvunja shingo pap - pap! mlinzi akadondoka chini kama zigo. Kone akalifuata geti na kuligonga mara mbili kwa konzi ya vidole vyake.

Geti lilifunguliwa, haraka Kone akamkwapua mlinzi aliyelifungua. Alimpiga shingo, kwa kutumia mgongo wa kiganja chake, katika namna ambayo ilimpiga ganzi na kumlegeza mlengwa wake. Alitoka nje ya geti upesi akawamudu wengineo kwa kuwafyatulia risasi ambazo hazikutoa sauti.

Wote aliwaingiza ndani ya geti akalifunga. Alimtwaa mlinzi wa kwanza kumkabili, alikuwa kama ametoka pigwa na shoti. Aliweka mdomo wa bunduki shingoni mwa mlinzi huyo akamuuliza:
"Rose yupo wapi?"

Mlinzi alimtazama kwa macho ya ghadhabu, akamjibu kwa pupa:
"Unaongelea nini? - Sijui nini wasema!"
"Sina muda wa kupoteza hapa na wewe, ndugu," Kone aliwaka. "Rose, mwanamke aliyekuwa anaishi humu ndani, mmempeleka wapi? Aidha unijibu au nifumue shingo yako ukawakute wenzako!"

Kone alididimizia mdomo wa bunduki shingoni mwa mlinzi. Mlinzi akagugumia kwa maumivu.

"Atakuwa alipelekwa jela!" Alinena akiukunja usowe kwa hisia za maumivu.
"Jela ipi?"
"Sijajua ni ipi - inaweza ikawa Pademba ama jela kuu ya Freetown. Huko ndio kuna wafungwa wanawake."

Kone hakuwa na haja ya kuuliza kuhusu hukumu hiyo. Alijua fika mdomo wa Talib ndio mahakama, na neno lake ni sheria. Alimmaliza mlinzi huyo aliyekuwa anaongea naye kwa kumnyonga, akimviringita shingo kama udongo wa mfinyanzi, kisha akaondoka.

Ilibidi afanye mauaji hayo kwasababu ya kulinda harakati zake. Endapo angemwacha hai mlinzi huyo basi taarifa zake juu ya msako wa Rose zingefika kwa Talib. Na basi kitumbua kingekuwa kimeingia mchanga.

Kwakuwa alishampanga dada mfanyakazi, mauaji yale ya walinzi yangeonekana yalifanywa na waandamanaji tu wenye hasira kali. Hilo ni heko kwake.

Aliondoka eneoni akiwa sasa anawaza ni namna gani atapata upenyo wa kumkomboa Rose toka kwenye mdomo wa jela. Jela ambayo hakuwa ameijua haswa ni ipi kati ya mbili zilizotajwa.


***
***

Oparesheni ya chini kwa chini ya mtawala; Al Saed, haikukoma kuvuma na kuita.

Kikosi kazi kilichokuwa kimeundwa na wanaume kumi, kikiwa tayari kimetandaza mipango yake kama vile walivyopewa maelezo na mateka, kilisogea karibu kabisa na maeneo nyeti ya kikundi cha AMAA.

Walitumia miguu wakilenga kutoonekana ama kugundulikana mapema. Miguu yao pamoja na macho vilifanya kazi kwa ufanisi mkubwa sana. Walinyata wakiangaza.

Wakiwa wanafahamu kabisa wanachokifanya, waliwaua wanaume watano waliokuwa kwenye lindo la ulinzi. Walijua fika wanaume hao walipokuwa wamejificha na hata silaha walizobebelea. Taarifa zote hizo juu yao walikuwa wamezikusanya toka kwa mateka. Ni mlinzi mmoja tu ndiye alikaribia kunusurika, ila naye domo la kifo likammeza.

Alikuwa ametoka lindoni akifuata chupa ya maji kwenye makazi yake. Alitwaa chupa hiyo na upesi akarudi kazini. Akiwa yu njiani, fahamu zake zilimtonya kuna mushkeli. Ukimya ulikuwa mkubwa mno na hata pale alipojaribu kumuita mwenzake, hakukuwa na majibu.

Kitendo chake cha kwenda kutazama usalama wa mwenzie ndiyo kikawa cha mwisho. Alivamiwa na pande la mwanaume lililompeleka chini na kumshindilia kisu cha kifua.
Kikosi kazi cha Al Saed, kwa nidhamu ya hali ya juu, kilijigawa na kukizunguka kijiji cha wanamgambo wa AMAA pasipo mtu yeyote wa ndani ya kijiji kufahamu. Wengi wa wanamgambo hao walikuwa wamelala, wachache wakiwa macho wakiusogeza usiku huo kwa vijisimulizi vya hapa na pale.

Kikosi hiki kilitega mabomu lukuki kila upande. Walijua fika kupambana na maadui zao mtu kwa mtu (man against man) wasingeliweza kufua dafu kutokana na idadi yao, na hata pia ugeni wa eneo ukizingatia ni usiku.

Baada ya kupandikiza mabomu hayo, taratibu walijiondoa eneoni. Waliyarudia magari yao wakaketi humo wakingojea muda kidogo kuyaruhusu waliyoyapandikiza yafyatuke.

Punde mwanaume mmoja anatazama saa yake ya mkononi na kutikisa kichwa.

"Tayari!" Alimwambia mwenzie aliyekuwa amebebelea kifaa cheusi kizito chenye vitufe kadhaa. Tip! Tip! Vitufe vilibonywa, na mara sauti kubwa za milipuko zikaanza kujibu kwa kishindo.

Milipuko hiyo inasababisha tetemo kubwa la ardhi. Mwanga mkali uliosababishwa na moto nao unaangaza kana kwamba umeme. Kabla vitu hivyo havijakoma, wanaume hawa wanapeana ishara na mara haraka wanatoka kwenye gari na kurudi kule kijijini mwa wanamgambo.

Walijigawa kama hapo awali. Kazi yao sasa ilikuwa ni kuwatafuta masalia, walionusurika kifo, na kuwamaliza kwa kuwashindilia risasi. Walifunua vyote vilivyokuwa vimefichwa na kuviweka bayana. Walitazama kila chochoro na chaka, hakukuwa na cha kubakiza!

Kazi hiyo ikadumu kwa dakika chache tu, kijiji kikawa kimya, mizoga ikitapakaa. Wanaume lukuki wa kikundi cha AMAA wanaachwa wakiwa maiti, wakimimina damu.
Je kazi yaisha?

Al Saed angalipumua sasa.

***
***

"Hili jambo halivumiliki hata kidogo. Ni upumbavu wa hali ya juu!" Alifoka Talib. Mishipa ya shingo ilikuwa imemsimama. Kinywa chake kilifunguka mpaka kwenye komo.

Ni punde tu toka atoke kwenye msiba wa Meja jenerali aliyeuawa na kikundi cha waandamanaji. Lakini pia tangu apewe taarifa ya mauaji ya walinzi kwenye nyumba ya Rose. Haya kwake hayakuwa mepesi kuvumilia.

"Inatosha!" Aliwaka. "Sihitaji tena kikao chochote baada ya hapa, bali utekelezaji. Nataka hawa wauaji wote wanyongwe, tena mbele ya umati: uwanja wa taifa!"

Kulikuwa kimya. Wanaume kumi na mbili waliokuwa wanamtazama, wakiwa wamevalia sare za jeshi zenye utitiri wa vyeo, walikuwa kimya na watulivu.

"Jenerali Freeman!" Talib aliita.
"Ndio mkuu!" Freeman akaitikia kwa ukakamavu. Alikuwa ni mwanaume mnene mweusi. Sare ilikuwa imembana kana kwamba inachanika dakika moja mbele.

"Nataka washenzi wote hawa ndani ya vitanzi! Umenielewa?"
"Ndio, mkuu!"
"Nakupa juma moja tu, moja! Silaha unazo, watu unao. Ukiwapata, unitaarifu. Nitakuja kuwafunga vitanzi kwa mikono yangu."
"Sawa, mkuu!"
"Kuna swali lolote?" Aliuliza Talib akiwatazama wajumbe wake kwa macho makali na ya udadisi.
Kulikuwa kimya. Pengine uoga ulitawala. Nyuso za wajumbe zilikuwa zinatazamana kana kwamba wanataka kumshitaki yeyote atakayeongea.
"Basi kama hamna maswali, tukatekeleze," alimalizia Talib kisha akaondoka zake. Mwendo wake ulikuwa wa kasi. Ilikuwa ni wazi hakuwa na hamu ya kuongea. Uso wake ulikuwa mweusi zaidi, na macho mekundu yaliyovimba.
"Sasa tunafanyaje?" Aliuliza Freeman. Hakuwa anajua cha kufanya, kwa mujibu tu wa macho yake. Ni kana kwamba mtoto anayemtafuta mamaye akafika njia panda asijue pa kuelekea.

Kwa muda kulikuwa kimya. Kila mtu alikuwa anatafakari namna ya kufanya. Baada ya kama dakika tatu za utulivu, mmoja, mwembamba maji ya kunde kwa rangi, anavunja ukimya akisema:
“Nina wazo.”
Wenzake wote wanamtazama.

“Kwanini tusiitishe mkutano wa usalama tukajumuika na hawa waandamanaji?”

Wazo hilo likawa kituko. Liliwasahaulisha watu matatizo kwa kuwaangulisha kicheko.
“Richard, we mzima kweli?” aliuliza Freeman. “Umemsikia mkuu amesemaje hapa? Anawahitaji watu hawa vitanzini, tena alivyovifuma mwenyewe, wewe unakuja kutuambia tuitishe mkutano? Tujadiliane kitu gani na hao wauaji?”
“Nadhani mngenisubiri nimalize ninachotaka kuongea,” alijitetea mtoa hoja, Richard kama alivyotambulishwa na wenzake.

“Richard, huna haja ya kumalizia,” alisema Freeman. “Mkutano hauwezekani kabisa! Hilo futa kichwani mwako. Hatuwezi kukaa meza moja na mwivi.”

Baada ya maneno hayo, Richard anafunga mdomo wake, haongei tena. Freeman akishirikiana na wenzake, ambao yeye ndiye alikuwa anawaongoza, wakapanga na kukubaliana juu ya mkakati wao. Waliupachika jina la oparesheni mwanzo, kati na mwisho.

Kwenye mkakati wao huo hakukuwa na mambo ya kubembelezana. Maeneo yaliyoripotiwa kuwa na vurugu kwa kiasi kikubwa yalitengewa nguvu ya ziada, wakikubaliana kila kijana ndani ya maeneo hayo atakamatwa, maelezo atayatolea ndani.

Wafungwa hao watawataja wenzao na mmoja baada ya mmoja atasakwa, atatiwa nguvuni na mwishowe kuuawa. Mwisho wa mpango.

“Ndani ya siku tatu tu, tunamaliza huu mchezo!” alitamba Freeman.
“Mkuu, atafurahi sana kumaliza jambo hili ndani ya muda mfupi.”
“Bila shaka, tunaweza ongezwa hata marupurupu.”

Kicheko kikajaza vifua vyao. Nyuso zilikuwa nyepesi sasa tofauti na mwanzo. Hii ndiyo nguvu ya tumaini. Japokuwa hawakuwa bado wamefanikisha, ila walitumai.

“Haki huu mpango hautafanikiwa,” alisema Richard. Sauti yake ilikuwa kama hatua za mwalimu karibu na darasa la wanafunzi wapiga kelele. Wote walinyamaza wakimtazama, kwa mshangao.

“Freeman, tuache kupeana matumaini mepesimepesi. Mnajua fika huo mpango wenu hautafanikiwa hata lepe,” alisema Richard kwa kujiamini. “Tumemfanya adui yetu aonekane mdogo sana kuliko uhalisia. Tunalifanya hili tatizo liwe dogo ili kujipa ahueni. Tunakosea.”
“Richard!” Freeman akang’aka. “Wewe ni nani wa kuchambua na kupima oparesheni zangu?” aliuliza. “Ina maana mkuu hakukuona wewe mpaka akaniteua mimi? Naona umesahau mimi ni nani kwako, ukiendelea basi nitakukumbusha katika njia ngumu.”

Kikao kilifungwa namna hiyo kila mtu akapata kuenenda katika njia yake. Makubaliano yakiwa kwamba utekelezaji wa oparesheni mwanzo, kati na mwisho utaanza moja kwa moja siku inayofuatia.

Ila basi kama kuna mahali Mungu ametupatia sie binadamu, ni kutojua ya mbele yetu, hata kwa sekunde. Mawazo na utashi wetu havina uwezo wowote wa kubashiri, haijalishi ni namna gani tulivyo werevu.

Freeman alirudi nyumbani kwake punde tu baada ya kutoka kupitia bidhaa kadhaa ndani ya duka kubwa lililopo ndani ya kambi ya jeshi. Akiwa na walinzi watatu ndani ya gari lake, anaongozana mpaka nyumbani kwake anapopokelewa na geti kubwa rangi nyekundu pamoja na walinzi watano waliovalia sare za jeshi wakibebelea mitutu.

Geti linafunguliwa anazama ndani. Walinzi wanatangulia kushuka kabla yake kwa ajili ya kutazama usalama. Freeman anaingia ndani akiwaacha walinzi wakidumisha usalama maradufu.

Hatukujua yaliyoendelea humo ndani, ila baada ya punde, kama robo saa, jambo fulani linatukia. Wanajeshi waliokuwa lindo wanabadili zamu. Gari la jeshi linalorandana muundo na fuso, lililokuwa limewabebelea wanaume sita wenye silaha, linasimama mbele ya uzio na kuwashusha wanaume watano isipokuwa dereva.

Wanaume hao wanasalimiana na wenzao wanaowapokea lindo, kisha wanashika zamu wakiwashuhudia wenzao wakiyoyoma na gari lililowaleta.

Baada ya gari kupotea kabisa lisionekane, wanaume, hao watano walioletwa na gari, wanatazamana na kupeana ishara ya macho. Geti linagongwa mara mbili, mara linafunguliwa.

Wanaume hao watano wanazama ndani ya jengo kwa mkupuo. Wanafyatua risasi kuwalenga walinzi watatu waliokuwemo ndani. Tukio hilo linadumu kwa haraka mno. Walinzi wanalazwa chini wakivuja damu. Wavamizi wanaingia ndani kwa kuvunja milango.

Punde…

“Nisameehee!”

Sauti kali ya kiume ilisikika. Bila shaka alikuwa Freeman. Mlango wa sebuleni unafunguliwa, Freeman, akiwa amevalia nguo ya ndani pekee, anarushwa nje kama zigo. Anatua kwenye sakafu kwa kukita. Anapata majeraha kadhaa ya kuchubuka mkono ukitenguka.

“Nisameheni jamani. Nisamehe!” alilia. Alitia huruma: macho yalimtoka, mdomo ukiachama. Alivuja jasho jingi. Mstari wa jasho ulijichora kwenye nguo ya ndani.
“Mtaenda mmoja baada ya mmoja!” alisema mwanaume mvamizi. Alikuwa ni yule aliyekuwa anatoa amri pia kwenye tukio la kuuawa kwa meja.
“Taratibu taratibu, mpaka tutamfikia huyo mshenzi wenu. Hamna yeyote atakayepona. Mtajua kwamba nchi hii ni ya wafanyakazi, na si viongozi waliojawa na tamaa na mapuuzo.”
“Jamani nina familia,” alijitetea Freeman. “Sihusiki na lolote kwenye mambo ya utawala. Sihusiki kabisa!”
“Na vipi kwenye mauaji? Sio wanajeshi waliokuwa wanaua watu? Mlidhani nyie ndio watu pekee mlio salama nchini, si ndio?”
“Hapana! Hapana!” Freeman alisema akikumbatisha mikono yake kama mtu anayesali. “Sijahusika na oparesheni yoyote ya kuua watu jamani. Naombeni mnisamehe.”

Alipiga magoti. Punde alijikuta yupo chini baada ya kupigwa teke zito la kichwa. Pua yake ilichuruza damu, na mdomo pia. Macho yake hayakuwa yanaona vema, ni kama vile mtu aliyekuwa amedumu gizani kwa muda mrefu alafu ghafla akahamishiwa penye mwanga, tena mkali.

Kwa mbali alikuwa anasikia namna akitukanwa matusi ya nguoni. Alivuliwa nguo yake ya ndani akabakizwa uchi. Alipigwa picha kedekede kisha akafumuliwa kichwa kwa risasi. Huo ukawa mwisho wake: muasisi wa OPARESHENI MWANZO, KATI NA MWISHO.


*Oparesheni hiyo itakufa? Talib atafanyaje akipata hizo habari? Richard alitaka sema nini? Je Mr. X kaenda na maji? Wapi The GHOST?*




****

Post sent using JamiiForums mobile app
 
Back
Top Bottom