Njia nyembamba (Simulizi mpya by SteveMollel)

Njia nyembamba -- 11

*Mtunzi: SteveMollel









Talib alirejea chumbani akajivesha nguo nyepesi kabla ya kutoka ndani na kwenda moja kwa moja kwenye sebule ya ikulu. Mlinzi wake aliwasha runinga akamtaka mkuu wake atazame yaliyokuwa yanajiri kwenye chaneli ya taifa.

Maelfu ya watu walikuwa wamejazana mitaani wakiwa wamebebelea mabango yenye ujumbe mkali dhidi ya Talib na utawala wake. Maelfu hayo ya watu walikuwa ni wafanyakazi waliokuwa wanadai malimbikizo ya pesa zao tokea miaka na miaka wakiwa sasa wamepoteza matumaini ya pesa hizo baada ya mapuuzo ya Talib.

Mitaa ilitapika; wafanyakazi hawakuwa peke yao bali pia walisaidiwa na wananchi wengine ambao nao waliona haja ya kufanya hivyo kwasababu ya hali ngumu ya kiuchumi iliyowaloweza kwenye umasikini uliokithiri. Kutokana na maandamano hayo, maduka yakafungwa na shughuli za uzalishaji zikasimama kwa muda.

‘TUNATAKA HAKI YETU!’ bango mojawapo lilisomeka hivyo, ‘MATUMBO YANATAKA CHAKULA NA SI SIMULIZI’ ‘POCHI YA SERIKALI NI YA WOTE SI YA WACHACHE’. Hayo yalikuwa baadhi tu ya maneno yaliyopachikwa kwenye mabango yaliyobebelewa na wananchi waliofurika mtaani. Mabango mengine hayakuwa na maneno bali michoro na katuni za Talib akiwa anafanya visa mbalimbali.

Sauti ilikuwa moja tu, tunataka haki yetu! Watu wote hao walikuwa wanapaza sauti hiyo kwa kuimba. Safari yao ilikuwa ni kuelekea kwenye majengo ya wizara husika wakiapa kutotoka hapo mpaka wajue hatima yao.

Talib alisaga meno yake akitazama habari hiyo yote iliyokuwa inarushwa mubashara. Alihisi kifua chake kimepata moto na wafanyakazi wanaelekea sasa kumpanda kichwani. Haraka aliwasiliana na waziri wa usalama na ulinzi, akamuuliza:

“Umepanga kufanya nini mpaka muda huu upo kimya?” Alifoka.
“Mkuu, naona wapo wengi sana. Nimeona niwaache tu kwani hawana madhara yoyote.”
“Hawana madhara!” Alitahamaki. “Wanavyonitusi na kunidhihaki unaona sawa?”
“Hapana mku …”
“Watoe mtaani mara moja, warudi majumbani mwao! Nadhani unajua namaanisha nini!”

Baada ya agizo hilo simu ikakatwa kisha Talib akaketi akiendelea kutazama runinga. Sasa alikuwa anangojea kuona utekelezaji wa agizo lake ndani ya muda mchache mbeleni.

Rose alikuja sebuleni akiwa amevalia gauni la kulalia, akaketi pembeni ya Talib. Macho yake yalitekwa na taarifa ya maandamano iliyokuwa inaonyeshwa. Wakati akitazama taarifa hiyo, alimuuliza Talib juu ya nini kinasibu huko kwenye mitaa ya Freetown. Talib akamjibu kwa jibu jepesi:

“Usijali, muda si mrefu mitaa itakuwa meupe.”

Jibu hilo lilitosha kabisa kumjuza Rose mambo yatakuwa mabaya kwa wale waandamanaji ndani ya muda mchache. Aliwaonea huruma na alianza kufanya jitihada za kuwakomboa.

“Talib, sidhani kama njia ya upanga itasaidia.”

Talib kimya. Macho yake yaliyokuwa mekundu tayari yalikuwa yanatazama runinga.

Rose alijaribu sana kuongea lakini hakupata msikilizaji. Mwishowe alichoka akaaga anaenda zake. Talib alimsindikiza mpaka kwenye gari, akamwambia maneno machache.

“Nenda kapumzike; samahani sihitaji ushauri wako kwenye hili.”

Rose hakusema kitu. Aliingia kwenye gari lake akatoka eneo hilo. Talib alijirudisha ndani akaendelea kutazama runinga. Ndani ya muda mfupi akapata kuona magari ya jeshi yakiwa yanaingia mitaani yakibebelea wanajeshi lukuki wenye silaha nzito. Wanajeshi hao walijitoa magarini wakatapakaa mitaani.

Talib akatabasamu.

Mwanajeshi mmoja aliyebebelea kipaza sauti kikubwa, alipaza sauti yake:

“Tawanyikeni mara moja. Mna dakika tatu tu za kupotea eneo hili!”

Sauti yake hiyo ilisikika vema lakini ikapuuziwa: hakuna mwandamanaji aliyesikia na kutii agizo. Bado sauti za ‘tunataka haki zetu’ ziliendelea kuvuma na kuwika.

Tangazo lilirudiwa tena kwa msisitizo. Mara hii wanajeshi walijiandaa wakiwa wamebebelea ngao za kujikinga, virungu na hata bunduki.

Dakika tatu zilipopita, wanajeshi wakaanza kutimua watu kwa kuwarushia mabomu ya machozi, kuwafyatulia risasi na kuwakung’uta kwa virungu. Watu walikimbia kama wehu kuokoa maisha yao. Kutokana na idadi yao wengine wakaangushwa chini na kukanyagwa vibaya mno.

Mamia ya watu walijeruhiwa na kuachwa barabarani wakiwa wanavuja damu, wanalia kwa maumivu makali. Wengine walikuwa wamekufa ama kuzirai huku wengine wakiwa ni majeruhi tayari lakini wanaendelea kupewa kipigo kizito kana kwamba wezi ndani ya mitaa ya kariakoo.

Sasa ilikuwa vita kamili. Waandamanaji nao wasikubali kuonewa, wakaanza kujibizana na wanajeshi kwa kurusha mawe na mabanzi. Wengine walio waovu wakawa wanapasua maduka waibe bidhaa mbalimbali na pesa taslimu. Ilikuwa fujo mno ndani ya jiji.

Baada ya lisaa limoja kukawa tulivu. Watu hawakuonekana tena mtaani bali baadhi ya magari ya jeshi yakirandaranda. Hospitali za jiji zilikuwa zimefurika mamia ya maiti na miili ya watu. Wengine walio hai na wenye majeraha ya kujikidhi walikuwa ndani ya nyumba zao wakitazama nje kwa kupitia madirishani.

Talib alikuwa ana furaha sasa, adhma yake ilikuwa imetimia ya kuwatia adabu ‘wakaidi’ kwa kuwaonyesha upande wake wa pili. Ila kwa upande mwingine, taasisi za kimataifa za kutetea haki za binadamu zilianza kubweka zikikemea hali hiyo. Video mbalimbali zilizoonyesha watu wakipigwa kinyama na kuuawa zilisambaa ulimwenguni kote. Huko mitandaoni maneno yakaanza kurushwa na vidole vikanyooshewa Sierra Leone.

Talib hakujali hata lepe. Alimpigia simu Rose akitaka arejee Ikulu lakini Rose hakupokea simu hiyo, zaidi aliizima asipatikane hewani.

“Siku yako ipo karibuni,” alisema Rose akiitazama simu yake kana kwamba anaonana na Talib. Uso wake ulikuwa umevimba kwa hasira na hata moyo wake pia.




***




Ilikuwa ni jioni iliyoelemewa na usiku. Kone alikuwa ndani ya gari dogo la magendo lilikuwa linavuka mpaka kwenda Guinea.

Gari hilo dogo lilikuwa limebananisha watu mno. Wanyama kama mbuzi, ndama na kuku nao walikuwa wamo humo ndani pamoja na binadamu. Kulikuwa kuna joto kali na harufu pia. Japokuwa madirisha yalikuwa wazi lakini hayakusaidia.

Safari hiyo iliyokuwa inafanyika kwenye barabara mbovu, ikijawa na michanga, mawe na madimbwi ya maji, ilikuwa ina matumaini ya kukamilika ndani ya masaa mawili mbele kwa abiria kuingizwa ndani ya Guinea. Na hiyo ndiyo ilikuwa safari ya mwisho mpaka tena kesho asubuhi na mapema. Kama Kone asingelipata hilo gari basi ingemlazimu avumilie tena mpaka siku inayofwata, jambo ambalo asingeliweza abadani.

Wakiwa bado hawajamaliza safari yao, ghafla walisimamishwa na wanajeshi wanne waliobebelea bunduki Ak 47. Waliamriwa wote washuke chini na kunyoosha mikono yao juu.

Abiria wote walitii, wakaacha mifugo tu ndani ya gari.

“Mnaenda wapi muda huu?” alifoka mwanajeshi mmoja mfupi.
“Tunaenda msibani, waheshimiwa,” akadakia dereva upesi.
“Mnatufanya sisi wajinga enh?” alisema mwanajeshi yule mfupi. Alimtazama Kone kwanzia juu mpaka chini, akamuuliza:
“Wewe ndiye kiongozi wao?”

Kone alifikiria mara mbili. Alimtazama dereva wa usafiri ule, dereva akamkonyeza kumpa ishara.

“Hapana, mimi siyo kiongozi wao,” alijibu Kone.
“Bali?”
“Ni mwanafamilia tu. Ni mjomba wa marehemu.”
“Oooh! Pole sana mjomba. Najua unataka sana kuwahi msibani, fanya basi mkono ucheze matairi yaende.”

Kone alishatambua nini wanajeshi wale wanataka. Alikumbuka maneno ya kondakta wa kwanza kabisa wakati anakuja nchini Sierra Leone kwa kutumia usafiri wa aina ile. Basi akaingiza mkono wake mfukoni na kutoa kiasi fulani cha pesa alichokichambua na vidole vyake, kama laki mbili hivi, akawapatia wanajeshi wale.

Mwanajeshi yule mfupi alikagua pesa hizo kisha akazitia mfukoni. Alitabasamu akimtazama Kone.

“Karibu sana na pole kwa msiba.”

Abiria walirudi ndani ya gari wakaendelea na safari yao. Kwenye majira ya saa nne usiku waliingia Guinea, Kone akipokelewa na mlinzi wake ndani ya gari. Alijiweka ndani ya chombo hicho wakatimua upesi.

Majira ya nane usiku, Kone na mlinzi wake wakawa wamewasili karibu kabisa na maeneo ambayo Kone aliambiwa na mlinzi wake kwamba ni makazi ya mwanaume aliyekuwa anamchukua mkewe, bi Fatma.

Kone alikuwa amelala hivyo mlinzi wake akamgutua toka usingizini na kunyooshea kidole jumba hilo.

“Ndiyo pale.”
Eneo hilo lilikuwa lina wanajeshi wawili waliobebelea bunduki wakitembeatembea. Palikuwa kimya mno.

Kone alishuka toka garini akasogelea eneo hilo. Haraka wanajeshi wale walitambua ujio wake huo, wakamwamuru asimame haraka na kunyoosha mikono juu akiwa huko huko mbali. Midomo ya silaha zao ilikuwa inamtazama Kone.

“Unaenda wapi!?” Mwanajeshi mmoja aliuliza. Uso wake ulikuwa umekakamaa kana kwamba kaona gaidi.

“Samahani kwa usumbufu, nimekuja kumfwata mke wangu!” Kone alipaza sauti yake kavu.

Wanajeshi walitazamana kwa mshangao kisha wakarudisha nyuso zao kwa Kone.
“Mkeo? Nani kakwambia mkeo yupo hapa!”
“Najua yupo hapa. Tafadhali naomba nionane naye, anaitwa Fatma.”

Wanajeshi hawakutaka kumsikiliza wala kumwelewa, walimfukuza Kone aondoke eneo hilo upesi. Kone alileta ubishi risasi ikapigwa kandokando yake. Alikubali kuondoka lakini akiahidi atarejea. Alijiweka ndani ya gari akaenda nyumbani kwake kupumzika.

Kesho yake asubuhi kwenye majira ya saa nne alipoamka, aliikuta simuni rekodi tatu za miito toka kwa Raisi, pamoja na ujumbe uliosomeka kwa kuuliza:
“Nani amekuambia urudi Guinea?”

Alijikuta anaghafirika, lakini pia akipatwa na maswali. Raisi amejuaje kuhusu ujio wake mapema kiasi hicho?

Kabla hajajibu ujumbe huo, mlango wa chumba chake ulifunguliwa na watu wawili waliovalia sare za polisi. Walikuwa wamebebelea bunduki ndogo mikononi mwao.

“Afisa Kone, upo chini ya ulinzi. Nyanyuka upesi twende kituoni!”

Kone alijikuta anatabasamu kwa kuchanganyikiwa. Kichwa chake kilifeli kughani mawazo kwa muda. Polisi walimsogelea na kumtia pingu, kisha wakamtwaa na kumpeleka kwenye gari ‘defender’ walilokuja nalo.

Hawakumweleza Kone juu ya kosa lake mpaka kituoni. Walimsweka rumande na kumwacha mwanaume huyo asijue la kufanya.



***




Yalikuwa yamebakia masaa manne tu kabla ya jeshi la Liberia kuvamia kijiji kinachokaliwa na wanamgambo wa AMAA. Bwana Samweli alikuwa nyumbani kwake kwa muda huo lakini akiwa karibu sana na mawasiliano na kamanda mkuu wa jeshi aliyekuwa anawasiliana vema na vikosi viwili vilivyokuwa vimetumwa kufanya oparesheni ‘tokomeza’.

Ilikuwa ni majira ya asubuhi inayojongea kabisa kuifuata mchana. Vikosi viwili vya jeshi vilikuwa vipo njiani sasa vikikaribia kuingia ndani ya kijiji hasimu kwa kutumia usafiri wa magari.

Baada ya lisaa limoja, yakiwa sasa yamekaribia zaidi, magari hayo yalijigawa yakiwa ndani ya mawasiliano. Moja lilielekea upande wa mashariki na lingine likaelekea upande wa magharibi.

“Kuweni waangalifu sana,” alisisitizia Samweli. Akiwa ndani ya suti nyeusi alikuwa ndani ya sebule yake kubwa akiwa amekunja nne safi. Simu yake ya mezani ilikuwa sikioni mdomoni akitafuna ‘bubblegum’.

Nyumba yake kubwa ilikuwa imejitenga mbali kabisa na majengo mengine. Eneo lake lilikuwa tulivu lisilo na bughudha wala purukushani za watu. Majengo machache yaliyokuwa kwa mbali nayo pia yalikuwa ni makubwa watu wakijifungia ndani ya uzio na mageti makubwa.

Baada ya muda mchache, kama dakika zisizozidi tano tangu Samweli atie neno lake la mwisho simuni, mwanaume mmoja aliyekuwa amejifunika uso kwa kinyago cheusi alitokezea ubavuni mwa ukuta wa nyumba ya waziri huyo.

Alichomoa visu viwili nyuma ya kiuno chake akavirusha kwa walinzi wawili waliokuwa wamesimama getini, visu hivyo vikawakita shingoni na kuwalaza wafu.

Haraka mwanaume huyo akajongea getini na kugonga geti mara mbili, akafunguliwa na mlinzi mwingine aliyemdaka shingo na kumvunja. Aliingiza ndani miili miwili ya wale walinzi aliowachoma kisu, akafunga geti na kwenda ndani.

Yote hayo yalifanyika kwa utulivu mno usijue kama kuna chochote kinajiri.

Mpaka bwana Samweli anaguswa bega lake la kulia, hakuwa anajua kama alivamiwa. Alitazama akamkuta mwanaume ndani ya kinyago cheusi. Mkononi mwake alikuwa amebebelea bunduki ndogo nyeusi mdomowe akiulekezea kwenye kichwa cha Samweli.

“Haraka batilisha mpango wako kabla sijakutoa roho!” Sauti nzito ilinguruma ndani ya kinyago.


***





☆Steve
 
Njia nyembamba -- 12

Mtunzi: StevwMollel






“Haraka batilisha mpango wako kabla sijakutoa roho!” Sauti nzito ilinguruma ndani ya kinyago.

Macho ya Samweli yalitoka kana kwamba vipande vya matango. Moyo wake ulilipuka na pumzi ilianza kukimbia. Ni kwa namna gani mwanaume huyo alizama ndani pasipo yeye kujua? Hakupata majibu. Ama ni jini! Anataka nini kwangu?

Hofu ilikamata uso wa Samweli na mwili wake ukaanza kujibu mapigo kwa kutetemeka mithili ya kifaranga aliyenyewa na mvua.

“Wewe nani?”
“Huna haja ya kujua. Nimesema batilisha mpango wako haraka!” mvamizi aliongea akinyooshea mdomo wa bunduki kwenye simu ya mezani.

Haraka Samweli akanyanyua simu na kuiweka sikioni.

“Ukifanya jambo lolote la kipumbavu nitatoboa kichwa chako!” Alitisha mvamizi. Bwana Samweli aliita namba ya mkuu wa jeshi, ilipopokelewa akatoa amri ya kusitisha oparesheni ya uvamizi wa kijiji makazi cha AMAA haraka iwezekanavyo.

“Mkuu, unasitishaje mpango huu ghafla hivyo?” Aliuliza mkuu wa jeshi.
“Nimesema rudisha hivyo vikosi haraka!” Samweli akafoka kabla ya kurejesha simu mezani akiilaza kando ya kitako chake hivyo kupelekea simu hiyo kuendelea kuwa hewani.

“Tayari,” alisema Samweli akimtazama mvamizi kwa macho ya huruma. Mvamizi yule alikuwa mwerevu, alitambua janja ya Samweli. Pasipo kusema jambo, alinyooshea bunduki yake kwenye simu akampa Samweli ishara ya kuikobeka simu ile kwenye kitako chake.

Samweli alitii, akaweka simu kitakoni. Hapo ndiyo mvamizi akaongea:

“Unajifanya mjanja siyo?”

Kabla Samweli hajajibu, risasi ilitoka kwenye mdomo wa bunduki ya mvamizi ikazama ndani ya fuvu lake la kichwa. Tundu kubwa lililozuka kichwani hapo likaanza kuvuja damu pomoni, wakati huo mvamizi akitazama.

“Kapumzike jehanam!” alisema mvamizi.

Masaa manne baadae, gari nyeusi, Harrier, muundo mpya iliingia ndani ya nyumba ya bwana Samweli. Ndani yake ilikuwa imembebelea mwanamke mnene mweusi na mtoto mdogo wa kike mwenye umri wa miaka kumi kwa makadirio mepesi.

Mwanamke huyo alikuwa ni mke wa Samweli na mtoto huyo akiwa ndiye mtoto pekee wa mheshimiwa huyo.

Walistaajabu kukuta hamna mlinzi hata mmoja getini hali iliyowalazimu wafungue geti wenyewe. Waliingia ndani na hawakuwakuta walinzi vilevile. Mke alipata mashaka, akakamata mkono wa mwanaye.

Kitu cha kwanza walichokiona baada ya kuingia ndani ya sebule, kilikuwa ni kichwa cha bwana Samweli juu ya meza. Kichwa hiko kilikuwa kimetapakaa damu na kimepatapakaza damu mezani. Kiwiliwili chake kilikuwa kimelala kwenye kochi, nacho kikiwa kimechafuza damu.

Sebule ilikuwa inanuka damu!

Mke wa Samweli alipiga kelele kali wakati mwanaye akiachama mdomo kwa bumbuwazi. Alidondoka chini akizirai, mtoto pekee akibakia hajui cha kufanya bali tu kulia na kuchanganyikiwa.




***




Hilo la Samweli kuuawa na kisha kuchinjwa halikuwa siri. Baada ya takribani nusu saa habari iliwasili kwenye masikio ya kiiongozi mkuu bwana Al Saed.

Wakati huo alikuwa yu ikulu akiwa anangojea kwa hamu mrejesho wa oparesheni ya kutokomeza kijiji kinachowatunza wanamgambo wa AMAA. Ndani ya mkono wake wa kushoto alikuwa amebebelea sigara aliyokuwa anaivuta kwa zamu.

Bwana Al Saed si mvutaji wa sigara mara kwa mara isipokuwa tu pale anapokuwa ametingwa na mawazo. Tabia hii inajulikana kwa watu wake wote wa karibu. Pindi anapovuta sigara basi anakuwa katika hali tulivu na ahitaji usumbufu wowote.

Hii aliyokuwa anaivuta sasa ilikuwa ni sigara yake ya tatu tangu aanze kusubiria taarifa za oparesheni ya uvamizi wa kijiji. Alishapigiwa simu mara moja tu na bwana Samweli, na sasa ulikuwa umepita muda mrefu kabla ya kuhabarishwa nini kilichokuwa kinaendelea, ila aliamua kuvuta subira.

Simu yake ilipoita, aliwahi kuitazama, alidhani ni bwana Samweli. Alikuta ni kamishna wake wa jeshi, akapokea, akapewa taarifa ya kifo cha bwana Samweli.

Mwili wa Al Saed ulipigwa ganzi kwa muda. Sigara yake ilidondoka chini akiendelea kusikiliza. Simu ilipokata, akanyanyuka upesi na kwenda ndani ya ikulu moja kwa moja mpaka kwenye chumba chake cha mawasiliano. Alifungua tarakilishi yake mpakato akatazama barua pepe. Huko akakuta ujumbe.

Ujumbe huo ulitumwa mapema sana. Laiti kama angelitazama mapema basi asingelikuwa na haja ya kupewa taarifa ya mauaji ya Samweli na kamishna wake wa jeshi.

Picha kubwa ya kichwa cha Samweli kikiwa kimekatwa ilijaa kwenye uso wa tarakilishi. Picha hiyo ilikuwa inatisha lakini Al Saed aliitazama. Alipomaliza akasoma na ujumbe uliombatana na picha hiyo:

“Nilikwambia usithubutu kufanya jambo lolote la kijinga, ulidhani natania.” Ujumbe huo ulitoka kwa Mr. X.

“Hiyo ni rasharasha tu, Al Saed. Kadiri utakavyoendelea kufanya ujinga ndivyo utakavyoadhibiwa. Tii amri sasa!”

Al Saed alifunga tarakilishi yake kwa nguvu. Alirejea kule alipokuwa awali akawasha sigara nyingine na kuendelea kuvuta. Alivuta sigara hii kwa hisia sana. Kichwa chake kilikuwa mbali mno kwa mawazo. Aliwaza mambo mengi ambayo aliyakosea majibu. Ila mwishowe kuna mambo akakubaliana nayo na baraza lake la kichwa.

Kuna watu ndani ya serikali yake, wanaungana na kundi hili la AMAA kwani hao ndio watakuwa wamevujisha mpango huo wa siri. Alijitahidi kuchambua jambo hilo, labda linaweza likawa limeonekana huko nje, akili yake ikagoma kabisa. Aliamini kazi hiyo imesukwa na msaliti.

Hakutaka kupaparakia hiyo oparasheni, akampigia mkuu wa jeshi na kumtaka mpango huo usitishwe mpaka pale atakapotoa taarifa zaidi.

“Sawa, mkuu,” aliitikia mkuu wa jeshi. “Tayari wapo njiani kurudi.”

Magari mawili yaliyowabebelea wanajeshi yalikuwa yanarudi kwa mwendo mkali baada ya mpango wa uvamizi kusitishwa. Yalikuwa ndani ya eneo kame lenye udongo mwekundu na vichakachaka vya hapa na pale. Eneo hilo lilikuwa tajiri kwa vumbi jekundu.

Baada ya matembezi ya kilomita kadhaa ndani ya eneo hilo jekundu, madereva waliona magari matano mbele yao umbali wa kilomita kama sita. Magari hayo yalikuwa ni makuukuu ila imara yakiwa yamewabebelea watu lukuki kwa nyuma.

Baada ya kusogeleana zaidi, ndipo wanajeshi wale ndani ya magari yao mawili wakapata kutambua magari yale yalikuwa yamewabebelea wanaume wenye silaha, na tena walikuwa njiani kuwashambulia! Midomo ya bunduki zao ilikuwa imeelekezwa kwao.

Kabla wanajeshi hawajaanza kujihami kwa kushambulia, walijikuta katika matata mazito baada ya kuanza kupokea mashambulizi mazito tokea nyuma! Hawakufahamu ya kwamba nyuma yao kulikuwa kuna magari matatu yalikuwa yanawafuata. Maadui hao waliweza kutumia vizuri vumbi lililokuwa linatimuliwa na magari ya wanajeshi hao kwa kujificha dhidi ya vioo vya pembeni. Walijipanga katika mstari mmoja wakicheza na vumbi zito. Haikujulikana walijikobeka humo muda gani.

Risasi zilirushwa kwa fujo kufuata magari ymawili ya jeshi. Risasi hizo zilitokea mbele na nyuma. Wanajeshi hawakuweza kumudu mashambulizi hayo, madereva walishindwa kumudu vyombo, vikakengeuka!

Kwa uhakiki zaidi, wanaume wale waliokuwa ndani ya magari yale nane kwa idadi, waliendelea kushambulia magari ya wanajeshi wa Liberia mpaka pale yaliposhika moto na kulipuka, ndipo wakatokomea eneo hilo.




***





Ni jioni tulivu ndani ya kipande kidogo cha ardhi ya Guinea.

Ndani ya jengo kubwa jeupe lililozingwa na wanajeshi watatu getini, sebuleni, alikuwa ameketi bi Fatma; mke wa Kone. Mkononi alikuwa amebebelea glasi maridadi yenye mvinyo mwepesi rangi ya kahawia. Hali yake ya mwili ilikuwa imetengemaa sasa, majeraha usoni yalikuwa kwa mbali, labda kwasababu ya vipodozi.

Nywele zake zilikuwa zimesukwa na kufumwa vema. Mwili wake ulikuwa umefunikwa na gauni ghali la heshima. Alikuwa ananukia kama bustani. Kila kitu kilikuwa mahala pake; hakika mwanamke alipendeza. Usingeweza kudhani kama ana watoto kadhaa.

Macho yake yalikuwa yanatazama filamu ya kilatini akiwa amezama haswa. Filamu hiyo alikuwa anaishushia na kinywaji chake maridadi kabisa mkononi. Kwa muda kidogo alikuwa kwenye ulimwengu wa peke yake.

Wakati filamu hiyo ikiendelea kunguruma, mlango wa sebule ulifunguliwa akaingia mwanaume aliyevalia kanzu ndefu nyeupe na kofia nyekundu. Mwanaume huyo alikuwa mweusi na aliyejaza nyama, uso wake haukuonekana mpaka pale alipogeuza uso kuuacha mlango na kumtazama bi Fatma kwa tabasamu.

Alikuwa Raisi!

Bi Fatma alinyanyuka akamkimbilia na kumkumbatia kwa furaha. Walipeana mabusu kabla hawajaachana na kuketi. Walijuliana hali kisha wakawa wanateta hoja za ziada. Wakati huo filamu iliisha na sasa macho na akili ya bi Fatma ikawa kwa Raisi.

“Nina habari njema kwako,” alisema Raisi.

Kiu kikaonekana kwenye macho ya bi Fatma.

“Habari gani hiyo?” aliuliza bi Fatma akijilaza kwenye mapaja ya Raisi. Raisi alichezea nywele za bi Fatma akiongea:
“Kwanzia sasa hutohitaji tena kuwa na wasiwasi wala mashaka,” alidokeza Raisi. “Hivi tunavyoongea hapa, Kone yupo ndani, na hatotoka kamwe!”
Bi Fatma akakurupuka toka kwenye mapaja ya Raisi. Alitazama kwa bumbuwazi uso akiwa ameukunja.
“Unasemaje?”
“Kone yupo ndani mpenzi,” Raisi alisema kwa tabasamu. “Hatimaye sasa amenipa sababu nzuri sana ya kumweka ndani; kutotii maagizo ya mkuu wa nchi.”

Akaangua kicheko.

“Sasa tunaweza tukajivinjari tutakavyo … vipi hujafurahi?”

Macho ya bi Fatma yalikuwa mekundu. Alimtazama Raisi kwa uso wa kughafirika akisaga meno.

“Tafadhali, naomba ukamtoe,” alisema kwa sauti ya kutetemeka.

“Wewe mzima kweli?” Raisi aliuliza. “Nikamtoe nimpeleke wapi? Ina mana bado unataka kuwa naye pamoja na kukutenda yote hayo?”
“Tafadhali tafadhali, naomba ukamtoe. Akiwepo ndani watoto watapata shida mno. Nakuomba sana.”
“Siwezi kumtoa,” alisema Raisi. “Unadhani nikimtoa alafu akagundua itakuaje?”

Si bure Raisi alitilia shaka. Kone hakuwa mtu wa kumpuuza hata kidogo. Kwanza ni mtu anayejulikana kama mmoja wa maafisa weledi serikalini, watu wengi wanamtambua, huo ni mtandao. Pili, ni mwanaume aliyeumbwa kwa mafunzo ya kutumia viungo vyake kujilinda na hata kuutoa uhai wa mtu.

Rekodi yake ya jeshi si ya kubeza. Si mzuri sana kwenye habari za upelelezi ila ni mwanaume ambaye ana uwezo mkubwa sana wa kumfanya binadamu mwenzake amuogofye. Jambo hili halikuwa linajulikana sana kwasababu Kone si mtu wa maonyesho wala majigambo.

Sifa zake hizo ndizo zilimvutia Raisi na kumweka mwanaume huyo karibu akimtuma kwenye kazi zake nyeti. Kone ni mtu wa kutunza siri lakini pia mwenye kuzimudu asiyewahi kukata tamaa. Hakuna kazi aliyowahi kushindwa, labda tu kukawia.

“Nipo chini ya miguu yako. Kone hajakutenda lolote baya, astahili haya kabisa! Amejitolea sana kukufanyia kazi leo unakuja kumlipa kwa kumfunga?”

Raisi hakutaka kusikiliza, alinyanyuka akaondoka zake kuelekea chumbani.

Bi Fatma alilia na kusaga meno. Alijiona msaliti asiye na huruma. Kwa muda aliwafikiria wanae na mumewe aliyeko lupango, kifua kikajaa uchungu na hasira. Alikumbuka namna familia yake ilivyokuwa hapo awali, tabasamu na cheko. Akashindwa kuvumilia.

Ilimlazimu sasa atoroke ndani ya jengo hilo akaikute familia yake. Ndivyo roho yake ilimwambia.

Ila anatorokaje?

Alifikiria namna ya kutoroka katika jengo lenye walinzi getini, mawazo yake hayakujipa kabisa. Alikaa hapo sebuleni akiendelea kuwaza na kuwazua mpaka mishale ya saa saba usiku. Hata lepe la usingizi hakuwa nalo.

Alinyanyuka akafuata dirisha akatazama nje. Aliona wanajeshi wawili wakiwa wanateta na bunduki zao mabegani. Kwa namna walivyokuwa wamesimama hapo usingeweza kudhani kama Raisi yupo ndani. Bila shaka yale yalikuwa ni makazi ya siri ya Raisi. Hata vyombo vya usafiri vilivyokuwemo ndani havikuonyesha kama ni vya mtu mkubwa kiasi hicho.

Bi Fatma alienda mlangoni mwa chumba alimoingia Raisi, akaita kwa sauti ya chini. Hakukuwa na majibu. Aliporidhia kwamba Raisi hasikii, alitoka ndani ya nyumba kwa kutembea taratibu. Alifungua mlango akatazama usalama, akaona unaridhisha.

Alizunguka nyuma ya nyumba kwenda ukutani akidhamiria kuruka. Ila kabla hajafanya hivyo, alihisi kuna mtu anamsogelea. Bila kutazama, haraka akapandisha gauni lake juu na kushusha kufuli yake chini.

Mapaja yake yote yalikuwa wazi. Gauni lake alilolinyanyua lilikomea chini kidogo mwa makalio.

Sauti ya mwanaume akisafisha koo ilisikika, bi Fatma akaigiza kujifunika kwa aibu. Alikuwa ni mwanajeshi mlinzi aliyebebelea bunduki akisogea kwa tahadhari, lakini tayari picha ya mapaja ya bi Fatma ikiwa kichwani.

“Kuna tatizo lolote mama?” aliuliza.
“Hapana,” akajibu Fatma kwa sauti ya puani. “Kwani kuna tatizo afande?” akauliza kichokozi.

Akili yake yote ilikuwa inaifikiria bunduki ya mwanajeshi ni kwa namna gani ataitia mkononi.



****


Kuna nini kwenye mahusiano ya Raisi na bi Fatma?


Nini hatma ya Kone lupango?





☆Steve
 
Rais mhuni sana,ila naiona njia yake ya kupinduliwa na kone.

Sasa siera mapinduzi, Liberia mapinduzi na Guinea napo mapinduzi yananukia
 
tivu sante
kweli kikulacho kinguoni mwako huyu raisi anamtuma kone makazi magumu kumbe ajivinjari na mkewe
halaf massawe ulisema raisi atakua anamkula huyo mwanamke
Nakuona mke mweee maeneo muhimu hku
 
Back
Top Bottom