Njia nyembamba (Simulizi mpya by SteveMollel)

Njia nyembamba (Simulizi mpya by SteveMollel)

Hizi ndizo riwaya za kusoma mtoto wa kiume,sio dume zima unakesha kusoma eti "MAHABA CHUMBANI"
Stupid
 
Njia nyembamba --- 09


Mtunzi; SteveMollel







Si punde nyingi taarifa inamfikia Al Saed kwa njia ya barua pepe. Kwa muda huo hakuwa na habari yoyote na aidha alikuwa anangojea habari njema ya kuteketezwa kwa ‘kijikundi’ cha AMAA, wapumbavu waliokuwa wameanza kumchezea sharubu.



Alikuwa amekaa kwenye uwanda wa nyumba yake, ikulu, macho yake ndani ya miwani yakiwa yanatembelea baadhi ya mikataba iliyokuwa mbele yake, mikataba iliyokuwa inahusisha nyanja mbalimbali za kimaendeleo mathalani uvuvi, ukulima na madini. Macho yake yalikuwa yamezama ndani ya makaratasini akiwa amebeba tahadhari kubwa. Lakini ghafla anashikwa begani na kutibuliwa utulivu huo.
“Kuna ujumbe wako, mkuu.” Alikuwa ni mtumishi wake aliyevalia suti nyeusi akitamka.
“Kutoka kwa nani?” aliuliza Al Saed akiendelea na kazi yake ya kupekua mikataba.
“Mr X,” akajibu mtumishi.
Moyo wa Al Saed ukapasuka. Alivua miwani yake akamtazama mtumishiwe.
“Una uhakika?”
Uso wake ulitambaliwa na puzo la shaka. Hata kabla hajajibiwa alionekana kupata jibu la swali alilouliza.
“Ndio, mkuu. Umeingia sasa hivi!”
Al Saed alipandisha kichwa chake juu kabla hajamruhusu mtumishi wake aende zake. Alibakia kitini kwa muda kidogo akitafakari na kubashiri nini ambalo Mr. X atakuwa amelituma. Kwa namna moja kubwa aliona si alama njema kupokea ujumbe toka kwa Mr. X kwanza kabla ya ujumbe toka kwa Samweli.
Alishusha pumzi ndefu akaenda ndani. Alimkuta mtumishi wake yupo karibu na tarakilishi yake mpakato, akaivuta na kutazama. Loh! Hakukuta maneno yoyote bali picha; picha za kutisha na kusisimua; picha za vichwa vitatu visivyo na viwiliwili!
Kama vile aliyemtumia picha hizo alijua ya kwamba Al Saed yupo hewani, mara ujumbe mfupi unaingia. Al Saed bado alikuwa kwenye pumbazo la kujiuliza zile picha azitazamazo ni za nani na kwanini ametumiwa. Alishtushwa na ujumbe huo, haraka akarusha macho yake kuusoma:
“Hiyo ni salamu kwako kafiri, usithubutu kufanya jambo lolote la kipumbavu.”
Al Saed alidadavua ujumbe huo kwa dakika moja, haraka akampigia simu Samweli na kumjuza. Habari hiyo ikapokelewa kwa mshangao; Samweli hakutegemea kama ingalikuwa rahisi kwa makachero wake anaowaamini kumalizwa namna hiyo. Ilimlazimu sasa kuchukulia jambo hilo kwa namna tofauti; kwa namna nzito na kwa umakini zaidi.
Hawakuongea sana, simu ikakatwa. Al Saed aliendelea kutazama picha alizotumiwa kwa takribani dakika tatu. Kila alipojaribu kutuma ujumbe wa kumjibu Mr. X, ujumbe haukwenda. Uligoma na kumtaka aweke kwanza anwani ndipo apate kutuma. Al Saed akaishia kughafirika na kutoka ndani.
Miwani sasa ilibidi ibadilishwe, pasi na shaka. Jambo lilikuwa kubwa kuliko walivyodhania, lakini pengine bado lilikuwa kubwa kuliko ambavyo bado wanadhania.
Wafuasi wa AMAA, si kwamba walikuwepo ndani ya kile kijiji kidogo tu, walikuwa wametapakaa maeneo yote ya karibu na eneo hilo wakiwa wamejihami kwa silaha nzito lakini pia wakiwa wamejiweka katika mazingira ya kujificha vya kutosha kiasi cha kutoonekana kwa wepesi.
Kijiji kizima kilikuwa kina mahesabu kamili ya wanamgambo hao wa kikundi cha AMAA. Hiyo ndiyo ilikuwa ngome yao na hivyo basi kila namna iendeleayo humo walikuwa wanaifahamu. Kila mwanakijiji alikuwa ni mhusika wa kikundi hicho aidha kwa njia moto ama vuguvugu. Kila mgeni aliyeingia humo alitazamwa kwa ukaribu akifuatiliwa nyendo haswa.
Shaka kwa makachero wawili wa Samweli lilikuwa ni la kawaida hapo awali. Hata wenyeji wao hawakuwa wameng’amua lolote la kugutusha. Ila pale gari la Samweli lilipotua maeneo hayo, ndipo mambo yakaanza kuwa uchi.
Walifwata nini ndani ya lile gari? Kwanini gari halikuja ndani ya kijiji? Nani yupo ndani ya gari? Hapo ukakasi ukaanza. Japokuwa makachero hao na mkuu wao, bwana Samweli, walidhani wapo wenyewe baada ya kukiacha kijiji kilomita kadhaa, ukweli ni kwamba kulikuwa kuna watu watatu ambao walikuwa wanatazama gari hilo na darubini kali.
Lakini kama kuna kosa kubwa ambalo makachero hao walilifanya basi ni kwenda msikitini siku hiyo hiyo baada ya kuonana na mkuu wao. Mbona siku zote hawakwenda na ingali walikuwemo ndani ya kijiji? Mosi. Pili, walitolea wapi kanzu mpya wakati hali yao ya kimaisha ilionekana ni duni? Walijichimbia kaburi. Jicho la karibu lililokuwa linawatazama likageuka kuwa upanga uliokula vichwa vyao.

***

Agizo la Raisi ni amri. Japokuwa kishingo upande, Kone alijiandaa kwenda Sierra Leone kutimiza alichotumwa. Yeye ni nani abishane na Raisi?
Macho yake yalikuwa yamevimba. Uso wake ulikuwa na uchovu. Ulikuwa ni muda wa jioni akiwa tayari ameshakata tiketi ya ndege ya kumtwaa masaa manne mbele. Alioga kisha akachukua mashati mawili aliyoyatupia kwenye gari. Alijiveka viatu vyeusi vya ngozi vilivyokuwa vinang’aa, akamwita mlinzi na kutoka naye garini.
Hawakuongea neno lolote mpaka pale walipokaribia uwanja wa ndege. Kone alikuwa mwingi wa mawazo. Alisonya kwanza kabla hajasema kwa uchovu:
“Nadhani unakumbuka niliyokwambia.”
Mlinzi akatikisa kichwa chake kukubali.
“Ndio, kiongozi. Nakumbuka.”
Kukawa kimya tena mpaka wanaingia eneo la uwanja wa ndege.
“Nakuamini,” alisema Kone. “Natumai hautoniangusha.”
“Sitakuangusha kiongozi wangu.” Mlinzi akasema kwa kujiamini.
Kone alivuta begi fulani dogo toka viti vya nyuma, akalipakia mashati yale mawili kisha akashuka akienda ndani ya uwanja. Mlinzi alijisogeza kwenye kiti cha dereva, akatia moto gari apate kutimka. Alirudisha nyuma gari, ila kabla hajaondoka alisikia gari likipigwa kwa nyuma. Alitazama kwa kutumia vioo vya pembeni, akamwona Kone!
“Hakuna safari!” Kone aliwaka akiwa dirishani mwa gari. “Safari zote za kwenda Sierra Leone zimesitishwa mpaka pale taarifa itakapotolewa.”
Mlinzi akaachama kwa mshangao.
“Kumbe taarifa ilitolewa masaa kadhaa hapo nyuma, sikutazama simu!”
Kone alitabasamu. Mlinzi alikuwa anamtazama mwanaume huyo kwa macho ya duwazo, na kwa namna fulani alihisi Kone anaweza akawa amechanganyikiwa.
“Kwanini safari zimesitishwa?” Mlinzi aliuliza.
“Ni kwasababu za kidiplomasia. Hakuna mahusiano mazuri kati ya Sierra Leone na Guinea kwa sasa. Hawatutaki nchini mwao!”
Gari lilitoka uwanja wa ndege mlinzi akiendesha. Kone alimpigia simu Raisi akamjulisha kuhusu jambo la Sierra Leone. Raisi kwa utulivu akaagiza kwa sauti yake nzito:
“Ni lazima leo uende Sierra Leone kwa namna yoyote ile, Kone.”
Uso wa Kone ukawa mweusi.
Raisi alikata simu. Baada ya robo saa akapiga tena kumpa maagizo Kone. Alimtaka aelekee mashariki kusini kuukuta mpaka uwatenganishao na Sierra Leone. Huko atakuta usafiri utakaomwingiza ndani ya nchi hiyo kimagendo.
Haikujalisha Kone alikuwa amekwazika namna gani, gari liligeuza mwelekeo kutii amri ya Raisi. Baada ya masaa matano wakawa wamefika panapotakiwa. Kone alikuta gari aina ya van rangi ya bluu iliyokoza. Lilikuwa limechoka mno na lilikuwa linakaribia kujaza watu, hohehahe kwa hali, lipate kutimka.
Ndani ya gari kulikuwa kuna wanyama mathalani kuku, mbuzi na ndama. Lakini pia lilikuwa limejaa joto na uvundo. Sura za watu waliomo humo zilikuwa zinarandana kwa ukata na kuchakaa.
Kabla ya Kone kupanda humo, alimuuliza kondakta:
“Kuna usalama wa kufika Sierra Leone?”
Kondakta alimtazama kwa mshangao.
“Ndio mara yako ya kwanza kwenda Sierra?”
“Hapana,” akajibu Kone. “Ila ndiyo mara ya kwanza kutumia usafiri huu.”
Kondakta akatabasamu.
“Usijali, usalama upo. Ila bila shaka utatusaidia endapo tukikamatwa na wanajeshi.” Alisema akimtazama Kone. Bila shaka alimwona ni wa tofauti.
“Kivipi?”
“Usijali, ni kuwahonga tu. Ukiwapatia kitu kidogo basi wanaturuhusu. Huwa tunafanya hivyo mara kwa mara endapo wakishikwa na njaa.”
Kone alitikisa kichwa chake kwa masikitiko. Alitazama lile gari analoeleka kupanda, akajikuta akitokwa jasho. Aliagana na Mlinzi wake kisha akajitweka ndani ya gari hilo mbanano, na punde safari ikaanza.
Ni umbali mfupi tu tokea pale safari ilipoanzia mpaka ndani ya Sierra Leone, ila kwa mujibu wa gari lile ambalo lilikuwa linasimama na kubustiwa, ama kutiwa maji ndio lipate kwenda, wakatumia masaa manne kuingia.
Ilikuwa ni usiku sasa. Kone alilazimika kutafuta mahali pa kulala. Alikosa kabisa sehemu nzuri akaishia kulala kwenye nyumba fulani iliyochoka mno, akipewa hifadhi na mzee mmoja mkarimu. Alipata chakula hapo na kukabidhiwa mkeka autumie kama kitanda. Mazingira hayo yalimwia vigumu lakini hakuwa na namna zaidi ya kukabiliana nayo.
Mwenyeji wake alimwambia mahali hapo huwa panatembelewa mara kwa mara na wanajeshi kwasababu ya kukaa karibu na mpaka, hivyo basi asiwe mtembezi. Akatii.
Alimpigia simu Rose, akawa hapatikani. Wakati akiendelea bado kumtafuta mwanamke huyo alijikuta akipitiwa na usingizi mzito kutokana na uchovu mkali. Alikuja kuamka saa kumi na mbili asubuhi ambapo aliaga na kufanya mpango wa kuitafuta Freetown.
Akiwa njiani alimpigia simu Mlinzi, simu ikaita mara tatu pasipo kupokelewa. Aliachana na hilo zoezi lakini haikupita muda mrefu, simu ya Rose ikaingia. Alipokea na kumtaka mwanamke huyo waonane ndani ya jiji la Freetown baada ya masaa kadhaa, Rose akaridhia.
Mwanamke huyo alikuwa ndani ya hoteli kubwa wakila raha na Talib. Ilimpasa aende chooni kuwasiliana na Kone kwasababu za usalama. Alimwomba Talib muda wa kwenda kupumzika nyumbani kwake, Talib pasipo na kinyongo akamruhusu. Alijiweka kwenye gari lake, akiendesha yeye mwenyewe, akaenda mpaka nyumbani kwake.
Alioga na kujivesha nguo maridadi kabla tena hajatoka nyumbani kwake, na mazingira yasiyomjuza, akaelekea mahali fulani ufukweni mwa bahari. Miwani yake kubwa ya macho na nywele nyingi za bandia zilimfanya asijulikane kama ni katibu mkuu wa nchi, bali mwanamke fulani aliye kwenye starehe zake.
Ilikuwa imebakia kama nusu saa tu, Kone atinge ndani ya Freetown. Alikuwa amesinzia kwenye kiti cha basi akiwa ameegemea kioo cha dirisha. Alikuwa amechoka, ungeweza kumwona kwa macho tu. Mdomo wake ulikuwa umeachama akikoroma kwa mbali.
Simu yake iliita mara nne, hakusikia. Alikuja kugundua hilo aliposhuka toka kwenye basi baada ya kushtuliwa na kondakta kuwa basi limefika mwisho. Kioo cha simu yake kilimjuza Mlinzi alimtafuta mara zote hizo. Pasipo kujivunga, akaamua kumpigia.
“Amekuja leo kumjulia hali,” Alisema Mlinzi.
“Lile lile gari?”
“Ndio, amekuja leo asubuhi na mapema, sijui amejuaje kama shemeji yupo hapa.”
“Umemfuatilia?”
“Ndio! Nimemfuatilia mpaka nyumba aliyoingia.”
“Safi sana. Umefanya kazi nzuri!”
“Lakini kiongozi kuna jambo kidogo.”
“Niambie.”
“Kwenye nyumba ambayo gari hilo limeingia, kuna ulinzi mkali mno. Ni ngumu hata kusogea karibu; inaonekana huyu jamaa ni mtu mzito serikalini.”
Kone akanyamaza kwa muda. Alijaribu kuvuta picha ya huyo mtu kichwani kumbukumbu zake zikagoma kabisa kuunga mkono hoja kwamba anamjua. Ni mtu gani mzito kwenye serikali hii ya Guinea asipate kumjua? Aliwaza.

***
Liberia: ndani ya chumba chenye mwanga hafifu.
Walikuwemo watu watatu ndani ya chumba kimoja msikitini. Nyuso zao hazikuwa zinaonekana vema kutokana na uhafifu wa mwanga. Wawili walikuwa wamevalia kanzu nyeusi na mmoja pekee ndiye alivalia kanzu nyeupe. Walikuwa wameketi chini wakitengeneza umbo la pembe tatu.
Kulikuwa ni kimya usidhani kama kuna watu.
“Nadhani maelezo yote umeshayapata,” alisema mwanaume mmoja ndani ya kanzu nyeusi. Sauti yake ilikuwa nzito na ya kukwaruza. “Wewe ndiye umeteuliwa kufanya sadaka hii, utasaidiana na mwenzako hapo. Ni muda sasa wa dunia kujua uwepo wetu rasmi.”
Baada ya kusema hayo, mwanaume huyo alipeleka mkono wake wa kuume upande wa kushoto nyuma kwake, akavuta begi fulani kubwa. Alilisogeza karibu na yule pekee aliyevaa kanzu nyeupe akisema:
“Kila kitu mnachohitaji kipo humo. Kila kitu mnachohitaji kwenye kufanya kazi yako hii takatifu.”
Pasipo kuhakikisha kama yasemwayo ni kweli, yule mwanaume aliyevaa kanzu nyeupe alilitwaa begi akatikisa kichwa chake.
“Tutafanikiwa kama vile Mungu apendavyo.”
Wenzake wakatikisa kichwa na kumwekea viganja kwenye bega lake la kulia.
Asubuhi na mapema, gari dogo jekundu Toyota Starlet linatoka kijijini hapo likiwa limebebelea wanaume wawili. Wote wamevalia kiraia. Macho yao makubwa yanaangaza na nyuso zao zimejawa tahadhari.
Kwa mwendokasi wa wastani gari hilo lilitembea. Mpaka kufikia karibu na jioni, walikuwa tayari wameingia ndani ya jiji la Monrovia. Walikodisha chumba cha malipo nafuu wapate kumpuzikia hapo. Walikula chakula cha kawaida na kuswali kabla ya kulala.
Asubuhi ya mapema, waliamka wakaswali. Mmoja, mweusi kuliko mwenzake, alivua nguo zake akibakiwa na nguo ya ndani pekee, mwenzake akaanza kumfunga ‘kikoti’ cheusi alichokitoa ndani ya begi, kisha akamfunga na mkanda mnene mweusi kiunoni. Baada ya hapo akahakikisha kama vitu hivyo vimekaa vema. Aliporidhika, alimvesha mwenzake kanzu yake na kumkabidhi rimoti ndogo.
Walitazamana wakawekeana viganja kwenye mabega yao ya kulia na kutikisa vichwa vyao. Kisha wakatoka ndani kuendea gari.





***




☆Steve
 
*Njia nyembamba -- 10*


Mtunzi: SteveMollel







Kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2008, jiji la Monrovia lilikuwa lina watu takribani milioni moja na kumi elfu mia tisa sabini. Ni jiji lenye watu wengi zaidi nchini humo likiwa na pilikapilika za hapa na pale za kibiashara. Lakini biashara hizi zikiwa nyingi ni za umachinga watu wakitandaza bidhaa chini na kungojea wateja.
Ndani ya jiji hilo kuna masoko makubwa mawili ambazo ndaniye ndimo watu wa nchi hiyo hupata bidhaa nyingi toka nje ya nchi hiyo, ama twaweza kuziita bidhaa za kimagharibi. Watu hujazana humo haswa kipindi cha mwisho wa juma.
Huu muda sasa ulikuwa ni mwisho wa juma na watu walikuwa wamejazana vya kutosha ndani ya masoko hayo mawili kama ilivyo ada wakinunua bidhaa mbalimbali. Nje ya soko mojawapo kati ya hayo mawili, lilisimama gari lililowabebelea wanaume wale wawili waliotoka kwenye nyumba ya wageni.
Mwanaume yule aliyejikoki kwa kujazwa mambo lukuki ndani ya kanzu, alitoka ndani ya gari hilo na kuendea ndani ya soko. Mwendo wake ulikuwa wa taratibu na uso wake haukuonyesha shaka lolote.
Mwenzake alimtazama akiyoyoma ndani ya soko, kisha akawasha gari na kutoka eneo la karibu na soko hilo. Alikwenda umbali wa kama nusu kilomita kisha akalituamisha gari hapo na kurusha macho yake kutazama soko lile lililommeza mwenzake.
Baada ya dakika kama tano, mtikisiko mkubwa wa ardhi ukavuma ukiambatana na sauti kubwa ya mlipuko. Soko aliloingia yule mwanaume lilishika moto mkubwa na sauti za yowe zikateka jiji! Ilikuwa mvurugano watu waliosalimika wakikimbia na kukanyagana. Wengine wakivuja damu nyingi maeneo mbalimbali ya miili yao.
Mwanaume yule ndani ya gari alitabasamu kabla hajakanyaga pedeli za mafuta kuondoka eneo hilo.
“Tayari, yamekwisha,” aliwataarifu wenzake kwa kutumia simu.




***




Haraka vyombo vya habari vya kitaifa na kimataifa vikarusha tukio hilo la mlipuko wa soko kubwa ndani ya jiji la Monrovia, Liberia. Watu wapatao themanini na tano waliripotiwa kufia papo hapo, huku wengine kama arobaini na kitu wakiwa ni majeruhi.
Damu zilitapakaa ndani ya soko hilo ambalo liligeuzwa sehemu ya maombolezo ndani ya muda mfupi mno!
AL Saed aliyekuwa anatazama tukio hilo runingani alijikuta anasinyaa moyo, macho yake yakimtoka pima. Kama vile tamthilia utamuni alipata kutazama. Mkono wake wa kuume uliunda ngumi na mdomo wake ukasaga meno. Alijiona yumo matatani, na hatua ya haraka inabidi ichukuliwe kuzuia upumbavu huo.
Hakuna wengine zaidi ya AMAA! Aling’aka. Alishangazwa ni kwa namna gani watu hao wanavyolazimisha taifa kugeuzwa kuwa la kidini kwa kuua watu wasio na hatia. Ni uslamu gani huo wanaousimamia? Hapana, hawa watakuwa wana ajenda ya siri; watakuwa wana ajenda binafsi mbali ya pumbazo la dini!
Upesi Al Saed alimpigia simu Samweli na kumtaka aje ikulu. Ndani ya muda mfupi, yeye na Samweli wakawa wamo kwenye chumba cha majadiliano wakiteta mustakabali wa usalama wa nchi.
“Kama tukiendelea kutochukua hatua, watatumaliza,” alisema Samweli akiwa ametoa macho ya ukali.
Mwanaume huyo ahusikaye na usalama hakuona tena kama kuna haja ya kujiuliza mara mbilimbili kuhusu kuvamia na kuharibu kijiji kizima kinachotuhumiwa kufadhili kikundi cha wanamgambo wa AMAA. Jambo hili kwake lilikuwa jema lakini kwa Al Saed bado lilikuwa la ukakasi.
“Hakuna njia ya kuwamaliza hawa wanamgambo pasipo kuwaua hata na wananchi wasio na hatia kijijini hapo?”
“Mkuu ni bora tukaua watu hamsini kwa ajili ya kuokoa taifa zima,” alishauri Samweli. “Endapo kama tukifiria hivyo basi ni wazi hakuna siku tutakuja kuchukua maamuzi. Kijiji kile hakiingiliki kwa urahisi. Muda haungoji na watazidi kukua zaidi.”
“Kwahiyo unashauri tuwaangamize kwa njia gani?”
“Tutume jeshi likawatawanyishe.”
“Mawazo yako ni mema, ila yasitawaliwe na papara. Hatujajua wamejipangaje hawa watu haswa baada ya kufanya tukio hili kubwa. Inabidi kutazama nyendo zako vema kabla ya kuzamisha kichwa.”
Maongezi hayo yalidumu kwa muda wa nusu saa: wakakubaliana Samweli aendeshe operesheni hiyo ‘tokomeza’ baada ya siku mbili za upembuzi yakinifu. Samweli akamuaga kiongozi wake kisha akaenda kukutana na viongozi wa juu wa jeshi kuwajulisha kuhusu mpango huo kabambe. Alitaka vikosi viwili vya jeshi viandaliwe na kuwekwa bayana kushambulia muda wowote. Wakuu wa jeshi wakapokea taarifa hizo na kuzivalia njuga.
Lakini juu ya mpango huo kulikuwa kuna msisitizo wa siri na umakini mkubwa kwani kushindwa kwa mpango huo kutasababisha hali iwe mbaya zaidi. Halikuwa jaribio bali tendo litakalorudisha nchi kwenye mikono ‘salama’ tena.
Lakini kauli kumbuzi ya Mr. X bado ilikuwa inarandaranda ndani ya kichwa cha Al Saed. Kwa namna moja ilikuwa inamuogopesha na kumfanya afikirie jambo hilo mbele yake mara nne nne.
“Hiyo ni salamu kwako kafiri, usithubutu kufanya jambo lolote la kipumbavu.”
Jambo lake hili la ‘kipumbavu’ litafanikiwa? Lazima lifanikiwe! Alisema na moyo. Alimpigia simu Samweli akamwambia hataki taarifa yoyote ya kushindwa toka kwenye zoezi hilo.




***
***




Televisheni bado ziliendelea kuonyesha maswahibu yaliyotokea kwenye soko kubwa huko Monrovia. Saa hii, wakati wa jioni, Rose na Kone walikuwa wakitazama tukio hilo wakiwa kwenye eneo kubwa la wazi ndani ya hoteli kubwa ya kifahari.
Rose alikuwa amevalia nywele nyingi za bandia lakini pia pasipo kusahau miwani kubwa iliyotwaa zaidi ya nusu ya uso wake. Kone alikuwa amevalia shati jeupe jepesi alilolichomekea ndani ya suruali yake ya kitambaa rangi ya kahawia.
Meza yao ndogo lakini imara ilikuwa imebebelea juisi ndani ya glasi kubwa ndefu, huku Rose akiwa ameambatanisha na vitafunwa vyake avipendavyo: sambusa za nyama. Waliketi mbali kidogo na watu wachache ambao walikuwepo eneo hilo. Hata maongezi yao hayakuwa ya kusikika; yalikuwa binafsi.
“Nafasi ipo tena kubwa sana, Kone,” alisema Rose. “Sema tu tunahitajika kuwa wapole kwa sasa. Hatuwezi tukakurupuka kukwapua ukizingatia muda mchache tuliopo madarakani.”
Kone alitikisa kichwa chake akanyonya juisi mrijani.
“Kwahiyo ni kama muda gani utakuwa tayari kutimiza hilo?”
“Nipe angalau miezi mitatu.”
“Wasema? – Hapana haiwezekani, Rose!”
Kone hakuwa radhi kupoteza miezi yote mitatu, kwake huo ulikuwa ni muda mrefu sana maana wamaanisha ni muda wa kutokuwa na familia yake. Hapana! Sasa alikuwa amechoka kuzunguka nchini mwa watu na alikuwa anataka atulie kando na wanawe na hata mkewe aliye hoi.
Rose hakuwa anayaelewa hayo. Kone alimweleza mwanamke huyo kinaganaga juu ya yale yote anayoyapitia pasipo kumficha jambo. Rose akamwonea huruma sana Kone, lakini pia akashangazwa.
“Kwanini Raisi anafanya hivyo?”
Kwa muda wote huo wakati Kone alivyokuwa anaeleza, Rose alikuwa ameacha kufanya kila kitu akitazama uso wa Kone uliokuwa umesinyaa kwa msongo wa mawazo. Kwa kupitia macho ya mwanaume huyo ungelipata kuona ni namna gani moyo wake ulivyoraruriwa: namna gani mwanaume huyo alivyojeruhiwa na hisia.
“Kone, kuna kitu,” alisema Rose. Uso wake haukuwa na shaka wakati anatamka hayo. “Mi nakushauri uwe makini sana na uweke macho na masikio yako wazi muda wote. Ni lazima kutakuwa na sababu iliyomfanya Raisi akawa hivyo.”
Waliteta na hilo jambo kwa muda wa kama dakika kumi kabla Rose hajahitimisha kwa kushauri:
“Kone, rudi nyumbani ukakae na familia yako.” Yalikuwa ni maneno machache mazito. Kone alipoyapokea alivuta pumzi ndefu akanyonya juisi yake kupoza kifua.
“Sidhani kama ni rahisi kiasi hicho, Rose.”
Alihofia usalama wake. Kwa namna moja ama nyingine aliona ni bora akafanya vile atakavyo Raisi kwani akikaidi anaweza akajikuta yupo mbali zaidi na familia yake, ama kutoiona tena.
“Kone, mkeo yupo hospitalini, anakuhitaji sana muda huu. Na watoto wako je? Wataendelea kuwa wapweke mpaka lini ingali wana wazazi?”
“Natambua yote hayo, lakini unajua mimi ni unyoya tu mbele ya kauli ya Raisi. Anaweza kunipoteza ndani ya sekunde na asiwepo mtu yeyote wa kumuuliza!”
“Kwani Raisi anakuja nyumbani kwako? – Rudi nyumbani na uniachie mimi hiyo kazi yako, nitaifanya. Sidhani kama ukirudi tu basi Raisi atakuona. Kwani ana macho nchi nzima? …”
Kabla Rose hajaendelea zaidi simu yake ilimtaarifu anahitajika na Talib kwa kupitia ujumbe mfupi. Alimuaga Kone akimsisitizia afanye yale aliyomwagiza, kisha akaondoka.
Kone alimsindikiza mwanamke huyo na macho yake yaliyochoka. Alimalizia juisi yake naye akaondoka kwenda mahali alipofikia kwa ajili ya mapumziko.
Alijitupia kitandani haraka kichwa chake kikatwaliwa na mawazo ya nyumbani kwake: mkewe na watoto. Alitamani kupiga simu kuulizia huko nyumbani lakini akakumbuka alifanya jambo hilo muda si mrefu sana. Alifikiria kuhusu maneno ya Rose na ushauri wake lakini bado nafsi yake ikawa na majibizano; ilikuwa ngumu sana kwake kuamua. Aliwaza na kuwaza mpaka akalala. Alikuja kuamshwa baadae na mlio mkali wa simu. Alikuwa ni Mlinzi anamtafuta.
Kabla hajapokea alitazama saa yake mkononi, akaona ni majira ya saa sita na dakika ishirini na tatu usiku.
“Kiongozi,” sauti ya Mlinzi ilifunua mjadala. “Samahani kwa usumbufu, kuna jambo nataka nikutaarifu.”
Macho ya Kone yalikaa tenge akingojea ujumbe huo anaotaka kupewa.
“Yule jamaa amekuja leo hospitali, na amemwamishia shemeji hospitali nyingine!”
Moyo wa Kone ukapiga tuff! Alitaka aufungue mdomo kwa pupa, ila akajikuta ananyamaza baada ya kusikia sauti ya Mlinzi ikiendelea.
“Leo hii jioni alikuja akiongozana na polisi wanne, sikuweza kufanya kitu kabisa. Niliwauliza polisi wale wanampeleka wapi shemeji lakini hawakusema kitu. Hata nilipotaka kuongea na mwanaume huyo, nilizuiliwa na kukatazwa kujongea karibu kabisa!”
Betri lilikata nguvu kwenye simu ya Mlinzi, simu ikakata kwa kuzima. Kone aliwehuka na hakupata usingizi usiku wote huo. Ilipofika saa kumi na moja kasoro alipaki vitu vyake vyote akaenda kwenye kituo kikubwa cha mabasi, alikata tiketi na kujiweka kitini akiona muda hauendi kabisa!
Alimtumia ujumbe Rose:
“Nipo njiani narudi nyumbani.”





***




Wakati ujumbe wa Kone unaingia kwenye simu ya Rose, Talib ndiye alikuwa ameshikilia simu hiyo akiperuzi mtandaoni. Rose alikuwa bafuni anaoga.
Ilikuwa ni ndani ya Ikulu kwenye kitanda kikubwa chenye shuka zito jeupe na mito ya kumwaga. Chumba kilichopendeza kwa samani za haja na kuvutia. Sina haja ya kueleza sana kuhusu mahala hapa maana tayari nomino ‘Ikulu’ ilishatangulia.
Talib alivutiwa kusoma ujumbe huo kwa msukumo wa wivu. Jina la aliyetuma lilikuwa limetunzwa simuni: ‘Kone-Bro’. Aliufungua ujumbe huo akausoma kisha akamngojea Rose aje kumfafanulia.
Rose alitoka bafuni akiwa anajikausha nywele zake ndefu. Mwendo wake ulikuwa wa madaha na alienda kuketi kitandani kumkuta Talib.
“So hauendi tena?” Rose aliuliza.
Tokea majira ya asubuhi Talib alikuwa ana miadi ya kukutana na chama cha wafanyakazi ambao walikuwa wanataka kumwelezea na kumlalamikiia kuhusu madai yao sugu ambayo yamekuwa yakipuuziwa na kupigwa danadana muda nenda muda rudi, tokea utawala ule nyuma ya Kessy.
Tokea muda huo wa asubuhi, wanachama hao walikuwa kwenye uwanja mkubwa wa mkutano wakimsubiria kiongozi huyo ambaye alikuwa na Rose Ikulu akiwa hana habari yoyote.
“Siendi popote,” alijibu Talib akimwonyeshea Rose simu. “Huyu nani?”
Rose alishtuka lakini alifanikiwa kutomwonyesha Talib chochote. Aliigiza tabasamu akajibu akiendelea kufuta nywele zake.
“Jamani si unaona nimemsevu Bro. acha wivu mpenzi!”
“Hukunambia kama una kaka.”
“Yah! Sio kaka wa tumbo moja, hapana. Ni mtoto wa baba mkubwa. Sasa mpenzi n’tatambulisha familia yote?”
“Ulionana naye, leo?”
“Ndio. Nilimwacha nyumbani wakati nakuja huku.”
Waliachana na hilo jambo wakazama kwenye ulimwengu wa mahaba kwa kukumbatiana na kupeana mabusu motomoto. Kama watoto wakavutana na kuchezea mito. Walikumbushiana utoto ‘walioumisi’ na muda si mrefu hamu zikajaza bongo zao wakaanza kunyonyana ndimi wakipapasana maungo.
Rose alikuwa anatoa miguno ya haja. Uso wake ulionyesha kweli amezama, lakini hakuna anayejua kama kweli kichwani alikuwa hivyo ama alikuwa anaigiza. Hakuna mtu anayemjua vema Rose isipokuwa yeye mwenyewe. Ni muumba wake pekee ndiye anaweza kuhangaika na kichwa cha mwanamke huyo.
Wakiwa humo dimbwini mwa mahaba, mlango wa chumba hicho unagongwa taratibu mara tatu, hakuna anayesikia. Mlango unagongwa tena kwa msisitizo, Talib na Rose wanasikia sasa na kusitisha zoezi lao. Talib alikunja sura akitazama mlangoni.
“Nani?” Alipaza sauti.
“Nenda kamsikilize mpenzi.” Rose akashauri.
Talib alijifunika shuka akaenda mlangoni. Alimkuta mwanajeshi mwenye zamu ya kumlinda akiwa amesimama kwa ukakamavu.
“Mheshimiwa, kuna tatizo.”
Talib akasonya.
“Tatizo gani?”
“Tatizo kubwa, mheshimwa. Ni bora ukaenda kujionea mwenyewe.”




***




☆Steve
 
Tupia nondo

weka vitu bhana

Hizi ndizo riwaya za kusoma mtoto wa kiume,sio dume zima unakesha kusoma eti "MAHABA CHUMBANI"
Stupid

Steve njoo huku

Mbona kimya hivi, au ratiba imebadilika tena???


nadhani hadithi ishakwisha

Haya njoeni wazee. Nimewatumia ya Ijumaa na Jumamosi.




☆Steve
 
Back
Top Bottom