Njia nyembamba --- 08
Mtunzi: SteveMollel
Talib alishusha pumzi ndefu, akasema:
“Samahani Kessy. Ni wakati wangu sasa.”
Baada ya muda mfupi akiwa anamtazama Kessy ambaye sasa alikuwa marehemu, alijikuta anatabasamu. Alijihisi sasa amekuwa kipepeo toka kwenye muundo wa dudu washa. Alijihisi amekuwa mwepesi kama unyoya lakini kwa wakati huo akiwa mwenye kujawa nguvu na madaraka.
Alah! Ati Talib alikuwa amekufa. Kifua chake kilichobebelea chuki kilikua kimetuama. Ndio alikuwa amekufa. Hilo halikuwa na pingamizi tena, alienda na ngebe zake.
***
Kinyume na yalivyokuwa matarajio ya wengi, msiba wa Kessy ulidumu kwa siku mbili tu. Viongozi wachache sana waliudhuria tena toka mbali, wengi wao waliishia kutoa salamu za rambirambi ama kunyamaza kabisa ikiwemo Guinea. Lakini kilichoshangaza zaidi ni kwamba hata basi Al Saed wa Liberia naye? Hakufika! Ni wazi kulikuwa kuna jambo, hili lilitatiza raia ingawa hawakuwa wanampenda kabisa Kessy. Na kwa namna moja ama nyingine, Talib akatumia hii fursa kutimiza haja.
“Habari zenu wananachi wa taifa kubwa la Sierra Leone,” ilikuwa sauti ya Talib ikitokea kwenye spika za redio, na kwa wale wenye televisheni wakapata kumuona kabisa kiongozi huyo kwenye chaneli ya taifa akiwa amevalia sare za jeshi zilizopambwa na ‘vidudedude’ vingi vinavyong’aa. Alikuwa na uso wa tanzia lakini mkakamavu.
Watu walivutika kumwona na hata kumtazama. Kila mmoja alikuwa anataka kujua hatma ya nchi, lakini zaidi juu ya kifo cha Kessy ambacho kiligubikwa na utata na wingi wa siri. Walitumai watapata majibu ya maswali yao yaliyotuama kichwani hivyo wakaandaa macho pamoja na masikio.
Talib alijua kiu hiyo, na basi tokea alipoanza kuhororoja akawa anakuna pale panapowasha. Lakini si kwa kucha kama vile ambavyo wasikilizaji na watazamaji walidhani, bali kwa chuma! Alijaza uongo na pumba za kulaghai akiwa anajimiminia sifa kedekede. Ila zaidi alijenga uhasama baina ya nchi yake na mataifa mengine, haswa jirani.
“Inasikitisha sana kusema ya kwamba, kiongozi wetu mkuu aliuawa na rafiki yake kabisa, bwana Al Saed, ambaye alimtilia sumu walipoonana mara ya mwisho katika jiji la Freetown kwa ajili ya kujadili mambo kadha wa kadha ya maendeleo. Na kwa matokeo yake, jirani yetu huyo ameona aibu hata kufika kwenye msiba, amebakia kujificha nyumbani kwake. Inashangaza sana hili maana hamna taarifa rejeshi yoyote inayoonyesha kama walikuwa na mtofautiano wa mawazo.”
Hapa kwa wale waliokuwa mbali na vyombo vya taarifa ya habari wakajisogeza karibu zaidi. Lilikuwa linasisimua hili.
“Inasononesha kuona pia hata jirani yetu, Guinea, nao wameamua kuonyesha unafki wao hadharani kwa kutojihusisha kwa namna yoyote kwenye msiba wa kiongozi wetu. Ni vema, na tunampongeza kwa kuweka wazi ngozi yake ya chui. Lakini aishi akifahamu ya kwamba atakapobanwa na kiu, ni sisi wa karibu ndio tutakaomhudumia.”
Hakukomea hapo, akajinadi mbele ya wananchi.
“Wale waliodhani ya kwamba Sierra Leone itatetereka baada ya kumuua kiongozi wetu, basi wamejidanganya, tena sana. Nataka kuwahakikishia wananchi wote wa Sierra Leone usalama wa kuaminika kabisa, nchi yetu haitotetereka kwa namna yoyote ile, wala hakuna yeyote atakayehatarisha usalama wetu. Tumejipanga kwenye mipaka yetu yote na tupo tayari kwa wakati wowote kumwaga damu kwa ajili ya nchi yetu.”
Hapo uso wake ulionekana kusahau tanzia, ukachanua tabasamu kwa mbali. Ni kwa mtazamaji makini ndiye angeligundua hilo.
“Kwanzia sasa nchi itakuwa chini ya wizara ya ulinzi, na ningechukua hii fursa kutangaza safu mpya ya uongozi. Naamini kabisa kwa kushirikiana na hawa watu tutahakikisha ufanisi kwenye kuendesha nchi yetu.”
Sasa hapo akashindwa kuzuia kabisa tambazo la furaha kwenye paji lake la uso. Aliwataja watu kumi na mbili akiwagawia nyadhifa mbalimbali, watu hao wote wakitokea kwenye jeshi la Sierra Leone. Lakini kaba hajafunga mjadala huo wa madaraka, akamtaja na bibie Rose. Haikuwashangaza wanachi kwani hawakuwa wanamjua Rose, ila lilimshangaza Rose mwenyewe. Karibia litoe moyo wake nje ya kifua!
Katibu mkuu wa nchi! Si cheo kidogo. Rose alijihisi kichwa chake ni chepesi kulinganisha na majukumu aliyotwikwa. Lakini bado tabasamu lilimjaa usoni, pia na hofu ndaniye.
Alitaka kumshirikisha mtu furaha yake hiyo, na hakuwepo yeyote isipokuwa Kone. Alimtafuta mwanaume huyo simuni lakini hakumpata, mpaka pale alipojaribu mara tatu. Kiu chake kilikuwa kikubwa na hakuweza kutunza furaha yake kifuani.
“Unasema kweli?” Aliuliza Kone. Sauti yake ilikuwa ya kukoroma usipate shida kujua ametoka usingizini.
Rose alijinasibu juu ya bahati yake hiyo, lakini hakuchukua muda mrefu akagundua Kone hakuwa sawa. Mwanaume huyo alikuwa anajitahidi kuficha hali yake, ila haikutosha kumfanya Rose asing’amue kuwa mwanaume huyo yu matatizoni.
“Mke wangu yupo hospitali. Sijisikii vizuri kabisa, maisha yangu yapo mrama,” alieleza Kone. Macho yake yalikuwa mekundu. Hakuwa nadhifu kabisa.
Rose alimpatia pole. Alikata simu baada ya kuona Talib anampigia, lakini aliahidi kumtafuta tena Kone baada ya kumaliza kuongea.
Hivyo akatimiza ahadi baada ya dakika tatu.
“Amesema tutaapishwa keshokutwa. Nadhani kesho nitakuja kukuona huko Guinea lakini itakuwa siri sana. sitaki afahamu kabisa kama nina mahusiano na Guinea,” Rose alisema. Kone aliafiki mpango huo.
“Najua una mawazo fulanifulani kichwani. Si salama kuongelea kwenye simu bali uso kwa uso,” aliendelea kueleza Rose. Napo Kone akaafiki na simu ikakatwa.
Alirudisha simu mfukoni mwake akashika tama. Alikuwa kwenye hospitali kubwa kwa ajili ya kumjulia hali mkewe. Nafsi yake ilikuwa inajuta kwanini alimshushia kipondo bi Fatma kiasi kile. Alijuta kwanini hakuweza kumudu hasira zake. Alijiona mpumbavu, na baba asiyestahili. Lakini alikuwa na maswali mengi kichwani juu ya Fatma. Alikuwa anataka majibu, bahati mbaya hakuwepo pale kumjibu.
Aliwaza na kuwazua. Aliona ana haja ya kwenda kwa Raisi kumpa taarifa juu ya kifo cha Kessy. Ndio, aliona hilo ni sahihi kwa muda huo. Alifikicha macho yake akasimama.
Usiku mzima hakuwa amelala vema kutokana na mbu wa hospitali. Muda pekee aliopata wa kulala ilikuwa ni pale alipoegemea kiganja chake cha mkono wa kuume ama kushoto. Hakuweza pia kufanya hivyo kwa muda mrefu, zaidi dakika tano.
Alipopiga hatua tatu tu, simu yake iliita; alikuwa ni Raisi. Aliipokea simu hiyo haraka akaiweka sikioni.
“Ndio nilikuwa nina mpango wa kuja huko, mheshimiwa.” Aliikarimu simu kwa maneno hayo. Raisi alisafisha koo lake, akasema:
“Nahitaji uende Sierra Leone haraka iwezekanavyo.” Sauti ilikuwa kavu na usingehitaji kuelezewa kujua ya kwamba ilimaanisha kile kilichotamkwa.
“Huu ndio muda wa wewe kutazama fursa ya kutimiza kile tulichokiazimia kabla serikali hii haijatengemaa,” aliendelea kusema Raisi.
Kone alitabasamu, kisha naye akasema:
“Hakuna shida mkuu. Ila hatuna haja ya haraka kwa sasa kwani Rose, yule mdada niliyekuwa naye pamoja, ni mmoja wa watu walioteuliwa, tena kuwa katibu mkuu wa nchi! Hivyo hatuna tena haja ya papara.”
“Rose anihusu, Kone. Wewe ndiye mwenye hii kazi na si mwinginewe,” alisema Raisi. Kone tabasamu likajiminya.
“Nimesema haraka iwezekanavyo. Nadhani tumeelewana,” Raisi alisema kisha simu ikakata.
Kone alikosa cha kufanya kwa muda wa dakika mbili; alikuwa amesimama kama mnara. Alishika kiuno akitazama chini. Mwishowe alirudi kwenye viti vya hospitali akaketi na kushika tama.
Mwanaume ameumbwa mateso, lakini aliona sasa yamezidi. Aliona sasa ulimwengu unamuonea. Awali alikuwa anatamani Kessy afe basi amalize kazi, tayari amekufa, bado tena yaja kazi nyingine! Kufa kwa Kessy kwake kulikuwa kuna maana sana, si kwamba Raisi wake atapata anachokitaka, la hasha! Bali atapata muda wa kuketi na familia yake.
Sasa nayo ndoto yake ilikuwa inayoyoma. Alihisi moyo wake unasagwa kuwa chapati. Kama isingelikuwa jicho la mwanaume ni gumu kupokea chozi, basi angelikuwa tayari ameshabubujika. Alimfikiria mkewe na hali yake ile. Aliwafikiria wanawe na hivi hawana mzazi wa kuwatazama. Alikumbuka sauti ya mkewe ikimuonya dhidi ya mpango huo awali kabisa. Akajikuta anasaga meno.
Alibadilisha kila aina ya tama akachoka. Alizinduliwa na mtetemo wa ujumbe mfupi kwenye simu yake. Alitoa simu yake akatazama. Ulikuwa ni ujumbe toka kwa Raisi. Kone alitikisa kichwa akiufungua apate kuusoma.
“Pesa tayari imeshaingizwa kwenye akaunti yako. Fanya ulichoagizwa.”
Ujumbe ulisomeka hivyo.
Kwa hasira, Kone alibamiza simu sakafuni.
***
Ndani ya Toyota Prado nyeusi yenye vioo visivyoonyesha ndani.
Samweli, msimamizi mkuu wa ulinzi Liberia, alikuwa pamoja na wanaume wawili waliovalia kiraia. Wanaume hao walikuwa wanamtazama Samweli kwa umakini akiwapa maelezo juu ya nini cha kufanya. Walikuwa ndani ya eneo lijulikanalo kama Pleebo, ndani ya kata kubwa ya Maryland, kusini mwa nchi ya Liberia. Eneo ambalo kwa mujibu wa msimamizi wa ulinzi, bwana Samweli, lilikuwa linahisiwa kuwafadhili kundi changa la AMAA – Alwaqt min ajil alttaharrur.
Walitakiwa kuwa waangalifu sana kwenye eneo hilo lenye udongo mwekundu ndio maana wakachukua hatua kadhaa kuficha uhalisia wao. Usingeweza kudhani kama ndani ya gari hilo lililokuwa limechafuka matope kuna mtu mkubwa kama Samweli, lakini pia usingeweza kudhani kama wale wanaume wawili waliokuwa wanamtazama na kumsikiliza Samweli, walikuwa ni makachero. Sio tu kwamba walivalia kiraia, hapana. Walikuwa pia wachafu kama wengi waishio maeneo hayo.
Kuna mahali wamepahisi panaweza pakawa kitovu cha kikundi hicho. Wanaume hao wawili baada ya kuketi kwa siri eneo hilo huku wakiwa wanapeleleza kwa macho ya upande, waligundua mahali hapo pa siri. Ni mahali ambapo si watu wote huingia, isipokuwa ijumaa tu kwa ajili ya sala; ni mahali palipojitenga mbali kidogo na makazi ya watu; ni mahali ambapo nje yake kuna wanaume wawili wanaopalinda, na wanaume hao hubadilishwa kila baada ya siku moja na kuja wapya.
Hakuna mwenye taarifa kamili kuna nini ndani ya eneo hilo, na kabla ya kuchukua hatua yoyote dhidi ya eneo hilo ndipo makachero hao waliamua kuonana na mkuu wao awapatie amri.
“Ni lazima kwanza tuwe na uhakika kabla ya kuchukua hatua,” alisema Samweli kwa msisitizo. “Leo ni ijumaa na muda si mrefu …” akatazama saa yake mkononi, “muda si mrefu wataanza sala. Kwahiyo basi mtumie hiyo fursa kusali humo na mpekenyue kuna nini.”
Hiyo ikawa imeeleweka. Wanaume hao wawili walishuka toka kwenye gari, Samweli akaondoka. Walikuwa mbali na mji kwa sababu za usalama, kwahiyo kurudi kwenye makazi walilazimika kutembea kama lisaa limoja.
Walimaliza lisaa hilo wakaingia ndani ya mji, lakini kila mtu kwa upande wake. Walifikia kwenye makazi yao ya kuzugia, kila mmoja akiwa na yake, kisha wakajiandaa kwa ajili ya kwenda msikitini. Walivalia kanzu, mmoja yake ikiwa nyeusi na mwingine ikiwa nyeupe.
Adhana ililia ikawakuta wakiwa njiani kwenda msikitini. Walifika mlangoni wakakaguliwa kama wana silaha, ilipothibitika wapo safi, wakaruhusiwa kuzama ndani kama wengineo. Waliswali ndani ya msikiti huo lakini akili yao ikiwa haipo ibadani. Walikuwa wanaperuzi kutazamataza mazingira katika namna ya siri.
Kulikuwa kuna holi kubwa la kuswalia walipokuwa wamejazana watu kama hamsini na kitu hivi, wote walikuwa wanaume. Wanawake walikuwa kwa upande wa pili huko, nyuma ya mwongoza ibada aliyekuwa upande wa kaskazini mwa holi. Upande wa kusini mwa holi kulikuwa kuna milango miwili iliyokuwa imefungwa. Zaidi ya hapo hakukuwa na lolote la kukufanya uwaze kuna nini mule ndani.
Sasa kwanini kulikuwa kunalindwa? Tena na watu wabadilishwao kila baada ya muda fulani?
Maswali hayo yaliwafanya makachero wale wawili waendeleze macho yao ya upekuzi. Baadae wakati ibada yaelekea ukingoni, kachero mmoja akagundua kitu pale alipokuwa amekanyaga. Palikuwa pamefunikwa na zulia jekundu na hivyo basi ukadhania ni sakafu, ila kachero huyo alipopakanyaga mara mbili na kisigino chake aligundua chini ya hapo apakanyagapo pana uwazi. Huweza ikawa ni handaki!
Alijivunga na hakufanya kitu mpaka ibada yakwisha. Akiongozana na mwenzake, walijipanga katika mstari wa wanaotoka ndani, lakini walipofika mlangoni wakasimamishwa na wanaume wanne waliokuwepo mlangoni. Walikuwa na nyuso za kughafirika. Macho yao yalikuwa makali ambayo yangekufanya uhofie. Mmoja alikuwa ana asili ya kiarabu, wenzake watatu wakiwa weusi kama mie na wewe.
Kwa ishara yule mwarabu akaonyesha uelekeo wa kusini. Mkono wake wa kuume ulikuwa umeshikilia bunduki kubwa iliyokuwa ndani ya kanzu. Kwa kuhofia usalama wao, makachero wale wawili wakatii amri. Walisindikizwa na wanaume hao wanne mpaka ndani ya chumba kimoja upande wa kusini mwa holi.
Mlango ulifungwa tusijue nini kilichoendelea humo ndani. Ila baada ya kama robo saa, damu nzito ilichuruzika ikitokea chini ya mlango.
***
☆Steve
Sent from my SM-J110F using
JamiiForums mobile app