Ni mtihani mzito kwa JK leo

Mtu wa Pwani

JF-Expert Member
Dec 26, 2006
4,184
671
Ni mtihani mzito kwa JK leo

jk.jpg
*Baraza kuibua au kuzamisha matumaini ya Watanzania

Na Mwandishi Wetu

RAIS Jakaya Kikwete leo anakabiliwa na mtihani mwingine mgumu katika kipindi cha miaka miwili tangu serikali yake iingie madarakani Desemba mwaka 2005.

Mtihani huo unafuatia hatua yake ya wiki iliyopita kuvunja Baraza la Mawaziri ambapo leo anatarajiwa kutangaza jipya litakalokuwa chini ya Waziri Mkuu mpya, Bw. Mizengo Pinda aliyeteuliwa na kuapishwa Jumamosi iliyopita mjini Dodoma.

Tangu ilipoingia madarakani mwaka 2005,Serikali ya Rais Kikwete imekuwa ikiandamwa na vilio vya wananchi wengi hususan katika suala la kuanguka kwa uchumi huku mfumuko wa bei ukichochea kupanda kwa bei za bidhaa mbalimbali madukani.

Baadhi ya watu wamekuwa wakihusisha hali hiyo na ufanisi mdogo wa baraza hilo huku baadhi ya wananchi wakishinikiza kupunguzwa kwa ukumbwa wake sambamba na kuvunjwa kwa baadhi ya wizara ili kupunguza mzigo wa matumizi ya serikali.

Wachunguzi wa mambo ya siasa wameliambia gazeti hili kuwa baraza jipya la mawaziri ni mtihani mwingine mgumu katika utawala wa Rais Kikwete kwani litaibua ama kuzamisha kabisa matumani ya wananchi wanaoendelea kukaangwa na hali ngumu ya maisha inayozidi siku hadi siku.

Aidha wachunguzi hao walisema ahadi ya Rais Kikwete ya Maisha Bora kwa Kila Mtanzania ilitegemea sana uwezo na ufanisi wa baraza lake la mawaziri lakini hadi sasa hakuna matarajio yaliyokutana katika suala hilo.

Utafiti uliofanywa hivi karibuni na Taasisi ya Utafiti wa Maendeleo Tanzania (REDET) ulibaini maoni ya watu wengi yakionesha kupoteza matumaini na baraza hilo na kwamba halimsisadii Rais Kikwete.

Tangu Rais Kikwete alipoingia madarakani mwaka 2005 na kuunda Baraza lenye wizara 29, mawaziri na naibu mawaziri 61, zimekuwepo hisia miongoni mwa watu kwamba ukubwa huo wa baraza, umetokana na uswahiba jambo linalomfanya ashindwe pia kuwawajibisha.

Pia inadaiwa kwamba baadhi ya mawaziri hao wametumikia serikali kwa muda mrefu hatua inayowafanya wananchi kuhoji kulikoni na kuwaona wakongwe hao kuwa ni kikwazo kingine katika utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi na ahadi ya Rais Kikwete ya Maisha Bora kwa kila Mtanzania.

Baadhi ya wananchi wanawaona mawaziri hao kuwa 'wamepitwa na wakati' na wanafanya kazi kwa mazoea hivyo kushindwa kumudu kasi ya Rais Kikwete na kuonekana Serikali nzima imedorora.

Kwa mtanzamo mwingine baadhi ya wananchi wanadai kuwa idadi kubwa ya mawaziri wa sasa ilitokana na kundi la Mtandano lilichangia kwa kiasi kikubwa ushindi wa Rais Kikwete katika mchakato wa uteuzi wa mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Mei mwaka 2005.

"Rais Kikwete kama anataka kuunda Baraza madhubuti asahau mambo yaliyopita hata kama kuna waliomsaidia. Uwaziri usitolewe kama zawadi au au ahsante au sababu za kihistoria, wanaochapa kazi wapewe. Tunataka watu wenye uwezo," alisema mkazi wa Kipawa, Dar es Salaam, Bw. Claud Nanyaro.

Aliendelea kusema " Watu wanaofanya kazi kwa mazoea bila kuwa wabunifu, wanachangia kumwangusha Rais Kikwete, inasikitisha Serikali kukumbwa na mtikisiko uliotokea hadi kujiuzulu Waziri Mkuu katika kipindi kifupi cha miaka miwili tu, hii ni ishara mbaya, Rais anapaswa kusuka Baraza imara la Mawaziri hata ikibidi achukue wapinzani," alishauri Bw. Nanyaro ambaye alisema ana Shahada ya Uzamili katika masuala ya Siasa na Utawala.


Wananchi wengine waliozungumza na Majira kwa nyakati tofauti wamemshauri Rais Kikwete kuepuka mawaziri wenye upeo mdogo wanaowezwa kurubuniwa na kuingia mikataba yenye utata, itakayoliingizia Taifa hasara na kuleta fedheha.

Wananchi hao walisema wana imani kubwa na Rais Kikwete na kueleza kwamba endapo ataunda baraza imara bado ana nafasi kubwa ya kutekeleza falsafa yake ya Maisha Bora kwa Kila Mtanzania.

Walisema baraza linalotangazwa leo lina umuhimu mkubwa kwa utawala wa Rais Kikwete kwani litatoa picha ya kusonga mbele ama kuzama kwa matumaini ya Watanzania hususan katika kipindi hiki ambapo wengi wameonekana kukatishwa tamaa kutokana na kupanda kwa hali ya maisha.

"Hii ni nafasi ya pekee kwa Rais Kikwete kuteua watu safi wenye sifa na uwezo, wananchi wanawajua watu wenye uwezo wa kuchapa kazi, endapo hawatapewa nafasi wakawekwa watu wenye uwalakini, matumaini ya Watanzania yatapotea hivyo huu ni mtihani mgumu kwa Rais Kikwete na CCM pia," alisema Bw. Jongo Shaaban, mkazi wa Msalato Dodoma.

Baadhi ya waliokuwa mawaziri katika baraza lililovunjwa waliliambia gazeti hili jana kuwa mustakabali wa wao kurudi au 'kutemwa' kwenye baraza hilo wanamwachia Mungu.

Mmoja wa naibu mawaziri hao, alisema kwa njia ya simu kuwa anaamini kazi aliyofanya katika wizara yake inampa matumaini makubwa ya kuteuliwa tena katika baraza jipya.

"Haya mambo tunamwachia Mungu ni magumu kutabiri lakini binafsi kazi niliyofanya ni nzuri haina kasoro, sina sababu ya kuhofia kuachwa kama ni suala la kuachwa, litakuwa mabadiliko ya kawaida lakini si kwamba nimeshindwa," alisema naibu waziri huyo kwa sharti la kutotajwa jina gazetini.

Rais Kikwete alilazimika kulivunja Baraza la Mawaziri wiki iliyopita kutokana na kujiuzulu kwa aliyekuwa Waziri Mkuu, Bw. Edward Lowassa kutokana na kashfa ya mkataba kwa kuzalisha umeme kati ya Kampuni ya Richmond Development Ltd na Shirika la Umeme Tanzania ( TANESCO).

Kufuatia hatua hiyo alimteua waziri wa zamani wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Bw. Pinda kushika nafasi hiyo na kumwapisha Jumamosi iliyopita mjini Dodoma


majira
 
Back
Top Bottom