Binafsi nahisi ni kama Tanzania kwa sasa hivi tuna wakati mgumu kuliko kipindi chochote cha uhai wa nchi hii kilichopita.
Sasa hivi wataalamu wote wa nchi hii wanakwazwa na wanasiasa ambao 100% hawana utaalam wowote. Doctor msomi na mzoefu kazini anaweza kufukuzwa kazi na mkuu wa wilaya! Ambaye hata kusoma na kuandika hajui vizuri. Ni hatari sana.
Hatari kubwa zaidi ni viongozi kujaribu kuyatumia majeshi yetu kisiasa. Hii ni hatari kubwa kuliko wao wanavyofikiri. Kama hali itaendelea hivi, basi kuna Siku haya haya majeshi yetu na yenyewe yatatamani kutawala. Hakuna atakayeweza kuyazuia.
Nchi imekosa dira kabisa. Wananchi hawajui wafanye nini! Kwa mfano. Mwaka huu wakulima wamelima nyanya na mazao ya mboga mboga kwa wingi sana. Wengi walihamasika baada ya kiongozi wetu kuwaahidi kuwa ni Tanzania ya viwanda. Matokeo yake kila mkulima analia. Nyanya hazina bei na hakuna hata kiwanda kimoja cha kusindika nyanya. Zinaozea mashambani.
Wakulima wa nyanya ni kilio kila kona ya nchi hii. Sasa hivi tenga moja la nyanya ambalo lina wastani wa kilo 30 bei yake ni Tsh elfu tatu (3000) hakuna juhudi zozote za kuwaokoa hawa wakulima. Waziri anayehusika na viwanda hawezi kufanya lolote la dharura ili kuwaokoa hawa wakulima kwa sababu anaogopa bila sababu. Sasa kama hatuwezi kuhifadhi hata mazao yetu tunayolima, je ni viwanda gani tunafikiri tunaweza kumiliki?
Kila kiongozi mwenye taaluma anaogopa kufanya maamuzi kwasababu nyuma yake kuna anayemsimamia ambaye ni mwanasiasa asiye na taaluma yoyote. Yeye taaluma yake ni kutafuta sifa tu, madhara yake ni makubwa kuliko tunavyofikiri. Tusipobadilika mapema, tutakwama sana na tunastahili kukwama.