NHIF IBADILI SHERIA JUU YA WATEGEMEZI
Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya ni mpango wa Bima ya afya wa kisheria ulioanzishwa kwa Sheria ya Bunge Na.8 ya mwaka 1999 ili kuwezesha upataji wa huduma za afya kwa wanachama wakuu na wategemezi wao.
Uanachama huo ni kwa mujibu wa Sheria ya Mfuko wa Bima ya Afya Sura Na.395 TL 2015 na kanuni zake za mwaka 2002. Katika Sheria na kanuni hizo zimeweka mipaka ya wanaotakiwa kunufaika na mpango huu wa Bima ya Afya. Ambapo wanaotajwa ni mchangiaji mwenyewe na mwenza wake, watoto wa kuwazaa, kuasili au kufikia, wazazi wa mchangiaji au wakwe zake.
Sina tatizo na Sheria kwasababu Sheria ni mawazo ya watu, walikaa wakapanga utaratibu uwe hivyo na ukapitishwa ikawa Sheria. Si vibaya pia mawazo yangu haya yakakubaliwa, kupitishwa na mwishowe yakafanyika marekebisho ya Sheria Na.395 TL 2015 pamoja na kakuni zake za mwaka 2002.
Kilicho nisukuma kuandika juu ya jambo hii ni utaratibu wa mchangiaji kupangiwa wategemezi. Tatizo haliko kwenye idadi inaweza kubaki hiyo ya watu sita (6) kama ilivyo sasa, lakini Sheria isitamke kwamba ni nani na nani wanaotakiwa kuwa kwenye mpango huo, mchangiaji awe huru kuweka mtegemezi anayemtaka na sababu zake ni kama ifuatavyo.
Moja, kuna wachangiaji ambao hawana watoto wao wa kuzaa pengine hawakujaaliwa watoto kabisa, mbaya zaidi wanaweza kuwa pia hawana wazazi, lakini wachangiaji hao wanalea wadogo zao wa kuzaliwa pamoja, wanalea watoto wa ndugu zao ambao wengine wazazi wao wamefariki, wanalea bibi na babu zao pia wanafamilia wengine ambao wanawategemea kwa asilimia mia moja kama wazazi wao. Nafahamu kuna kipengele cha kuasili, lakini ukweli ni kwamba taratibu za kuasili ni ngumu sana, pia kuna wategemezi ambao kwa mujibu wa Sheria huwezi kuasili lakini wanakutegemea kwa asilimia zote.
Matharani kwenye familia X mtumishi Y ni mtoto wa kwanza kwenye familia, wazazi wao wamefariki wote, amebaki analea wadogo zake ambao hawana msaidizi mwingine yeyote zaidi yake. Lakini Sheria ya Mfuko wa Bima ya Afya haiwatambui hao wadogo zake, kwahiyo mtumishi Y anakatwa fedha kila mwezi za uanachama, anatibiwa yeye na kama ameoa na mwenza wake pekee huku akitoa tena fedha nyingi mfukoni kuwatibia nduguze.
Unajaribu kujiuliza hivi mfuko wa Bima unamaana gani kwa mtumishi ni suala la kuleta nafuu kwake au ni suala la kuchangia tu na kama ni kuchangia kwanini lisiwe suala la kila mtu ndani ya nchi lisiwe la watumishi pekee.
Nafahamu ipo hoja kwamba, masuala ya bima ukichangia si lazima unufaike wewe na kwamba unachangia wasiojiweza, hivi inaingia akilini kwamba wasiojiweza wapo ndani mwako Sheria haiwanufaishi, lakini unachangia watu wengine usiowajua, kama uzalendo ndiyo huo kwanini ni kwa watumishi wa sekta iliyo rasmi pekee, hasa watumishi wa umma walimu, wauguzi nakadhalika.
Kama nilivyotangulia kusema mwanzo kwamba, mfuko wa Bima ya Afya ni kwa mujibu wa Sheria ya Bunge Na.8 nataka niamini kuwa kuna uwezekano mkubwa kwamba waliopitisha Sheria hii haya hayawahusu ama kwasababu ya kuwa na mishahara mikubwa, kwahiyo hawaoni tabu ndugu zao wanapougua kwenda kugharamikia kwa fedha za mfukoni au pengine bima zao zimewapa uhuru wa kumtibu yeyote kwenye familia.
Nina amini jambo hili linawaumiza sana wachangiaji ambao wengi wao wana mishahara midogo wasio na marupurupu kama ya wabunge. Wengi wao wana wategemezi wengi, kutokana na kwamba waliowengi wanatoka katika familia za kawaida sana.
Ni kweli kwamba idadi ya watu sita ni ndogo kutokana na aina ya familia zetu za kiafrika, ukweli kwamba kila mtu kwenye familia hawezi kutibiwa na bima ya afya unajulikana, lakini idadi hiyo ndogo ya watu sita Sheria isitaje nani anatakiwa kuhudumiwa suala la msingi ni kuzingatia idadi ili mtumishi aamuwe yeye anayewaona ni wahitaji zaidi kuliko Sheria kuweka kizingiti kwa kutamka.
Vinginevyo naweza kuamini kwamba mpango wa bima ya afya hauna lengo la kumpa nafuu mchangiaji, badala yake itakuwa ni janja ya kuchukua fedha zao, ili kuwalipa mishahara mikubwa watumishi wa Mfuko wa Bima wenyewe na kufanyia mambo mengine ambayo yako nje ya utaratibu wa huduma ya afya.
Iko hoja kwamba tukiwaruhusu wawe huru wataweka watu ambao siyo ndugu zao, kwani hata wakiweka watu ambao siyo ndugu zao watu hao watakuwa wakenya au waganda si ni watanzania? Kama lengo ni kuchangia huduma za watanzania wasiyo jiweza kuna shida gani hata ikitokea hivyo.
Kama mahesabu yalipigwa kwamba kwa makato haya wanaostahili kupata huduma ni sita (6) kuna shida gani kila mtumishi akiwa na wategemezi wote sita au mfuko unatumia Sheria kujinufaisha kwasababu kwa Sheria jinsi ilivyo ina wazuia wachangiaji wengi wasiwe na wategemezi wanao nufaika na Bima, sasa kama lengo litakuwa hilo basi wachangiaji wanaibiwa fedha zao.
Habari njema ni kwamba hata wakiwepo sita hawawezi kuumwa kwa wakati mmoja, kwahiyo kwavyovyote vile kuna pesa nyingi zinakusanywa na hazitumiki unaweza kukuta wanufaika wa mfuko wanakaa muda mrefu bila kwenda hospitali hofu ya kukataa kuruhusu mchangiaji kuwa na wategemezi wote watano inatoka wapi?
Nafikiri ni wakati muafaka sasa marekebisho ya Sheria hii yafanyike ili kuwapa uhuru wachangiaji nani wamweke kwenye mpango wa matibabu maana ndiyo wanaofahamu nani muhitaji zaidi katika familia ili kupunguza magojwa ya visukari na presha kwa watumishi wanaotegemewa. Maana kwakweli magonjwa mengi husababishwa na kuwaza namna ya kutatua shida za familia hasa matatizo ya ugojwa ambayo hayapigi hodi.
Mara kadhaa tumesikia tuhuma mbalimbali baadhi ya watumishi wakitumia kadi zao za Bima kwenda kujichukulia madawa maduka tofautitofauti hili linawezekana pia linachangiwa na baadhi yao kuona kama wanakatwa pesa za bure, kwasababu unakuta hawana wategemezi hao kwa mujibu wa Sheria za mfuko. Kwahiyo wanaona ili waone pesa yao wanayokatwa imeenda kihalali ni kujichukulia dawa bila hata kuumwa kama fidia. Kuna wakati watu hutenda uhalifu kutokana na Sheria kandamizi kwahiyo wakati mnawashughulikia lazima mjitazame wenyewe.
Ni kweli kuwa inawezekana kabisa kwamba Sheria isipotaja nani anatakiwa kunufaika wapo wachangiaji watakaotumia nafasi hiyo pengine kuuza nafasi hizo kwa watu wengine, lakini bado jambo hilo lisiwe kikwazo kwa wachangiaji waaminifu ambao wangalipenda kuwaweka ndugu na jamaa wanaowategemea kwa kila kitu kutibiwa. Hilo laweza kuchukuliwa kama changamoto ndogo katika jambo kubwa ambalo linawaathiri wengi. Wapo watu wamelelewa na mama au baba zao wa kambo, wamewasomesha leo wanapata kazi hawawezi kuwahudumia kutumia Bima!
Natambua zipo Bima za vitu mbalimbali kama magari, nyumba, biashara na kadhalika.Wako wanaojaribu kuzifananisha bima hizi na bima ya afya kwamba bima ndivyo zilivyo, lakini kama Sheria inataja idadi ya watu kufikia sita kwanini iwe nongwa kwa kila mchangiaji kuwa nao sita? Pengine inaweza kusemwa kwamba hatujazuia kufikia idadi hiyo lakini kwa utaratibu wa kutaja nani na nani maana yake ni wazi kwamba huwo ni mkakati wa kuhakikisha hawatimii ili pesa nyingi za makato zisitumike.
Ushauri wangu.Kwa kuwa jambo hili limekuwa kero ya muda mrefu kwa wachangiaji nafikiri ili kuwapunguzia mzigo wa kuwahudumia ndugu zao ambao walipaswa kuwa kwenye mpango wa Bima, niombe mamlaka za kisheria zinazohusika ili kuifanyia marekebisho Sheria ya Mfuko wa Bima ili sasa wachangiaji wawe na uhuru wa kuchagua nani anastahili lakini idadi ibaki ileile.
Kutofanya hivyo ni kuendelea kuwaumiza wachangiaji kwa kukata fedha zao huku wakiingia tena mifukoni kulipia matibabu ya wategemezi wao ambao Sheria haiwatambui. NHIF lazima watambuwe kwamba huo ni wizi wa wazi wazi na haukubaliki kubalini kubadili Sheria ya mfuko.