Tutor B
JF-Expert Member
- Jun 11, 2011
- 9,025
- 6,617
NGUVU ZA ASILI NA NGUVU ZA AKILI.
Nguvu za akili ni ule uwezo wa kumuunganisha mtu na nguvu asili. Hakuna kitu kishindacho nguvu za asili na nguvu za asili zikiingia ndani ya mwili wa binadamu hutenda mambo makubwa na ya ajabu. Kwa hiyo nguvu za akili ni lango la kupitishia nguvu za asili ambazo zikipenya mwilini mwa binadamu huleta manufaa makubwa sana kiafya, kiakili na kimawazo.
Binadamau ameishawahi kuhisi nguvu za asili zikimwingia mwilini. Mfano, pale ambapo mtu aliwahi kuwazia jambo zuri au kitu akipendacho na akahisi msisimko wa nguvu mwilini mwake; mfano wa pili ni pale ambapo mtu anaweza akawa amelala amechoka au hata kuwa katika hali ya ugonjwa ghafla akaletewa taarifa nzuri basi ghafla nguvu zikamjia na kuruka bila kujua nguvu hizo zimetoka wapi. Basi hizi ndio nguvu za asili.
Nguvu za asili ni kwamba hutokea pindi jambo fulani linapotokea liwe la kutisha ama kufurahisha; na nguvu hizi mtu anao uwezo wa kuzitumia kwa kila jambo na akafanikiwa, kinachotakiwa ni kujua jinsi ya kuzitumia (jinsi ya kuzitumia ndo nguvu za akili). Uzuri au ubaya wengi hatujui na hata wanaozijua wengi wamefanya siri kwa manufaa yao binafsi au kundi la watu kadhaa.
Nguvu hizo huponya maradhi na kuleta ustawi wa kiakili kiafya na kimawazo. Kinachotakiwa kujua ni namna gani ya kuyatengeneza mazingira hayo yavutayo nguvu za asili ili mtu apate afya, maendeleo na amani ya kudumu.
Nguvu za asili zimeenea ulimwenguni pote na ndizo hutumika kuendesha kila kitu kinachofanyika Duniani. Nguvu hizi za asili huathiri watu na vitu. Nguvu hizi za asili hazizalishwi na binadamu hivyo kwa jina jingine tunaweza kuziita nguvu za Nje. Kinachozalishwa na binadamu ni nguvu za akili ambazo humwezesha mwanadamu huyo kuzitawala nguvu za asili.
Binadamu anao uwezo wa kuitumia nguvu hii ya nje/ya asili pale ambapo nguvu ya ndani haitoshi. Mtu yoyote akiweza kuinasa nguvu hii basi ataweza kuutendesha mwili wake chochote anachotaka. Mwanadamu anapolala usingizi huvuta nguvu za asili kwa wingi na ndio maana watu wakiamka asubuhi wanakuwa fresh. Uchovu wa jana unaisha au kupungua. Lakini nguvu za asili zinazovutwa wakati wa usingizi wa usiku hazitoshi kuendesha mwili ipasavyo zaidi ya zile zivutazwo pindi mtu anapokuwa katika hali ya utashi wa kuzipata nguvu hizi. Kifupi ni kwamba nguvu za asili humuingia mtu anapokuwa katika hali ya nusu usingizi.
Kwa kawaida mwili huchoshwa na mihangaiko ya kimaisha na akili inapohangaishwa na mawazo mabaya kama vile chuki, wivu, hasira, wasiwasi, kisirani, woga na mengine mengi yafananayo na hayo na wakati huo huo mtu huyo asipovuta nguvu za asili vya kutosha za kujikarabati mwili; huyu anakuwa kwenye hatari kubwa ya kupata maradhi ya kufisha kama vile presha, sukari, moyo, kiharusi na anaweza akawa kichaa.
Nguvu za asili huvutwa kupitia akili na akili iko katika viwango vitatu.
1. Akili ya fahamu.
Hii ni akili ya kwanza ambapo kazi zake ni kukusanya taarifa zote kupitia milango ya fahamu na huzichuja ndipo hupeleka kwenye akili namba 2 (tutaiona mbele). Akili hii hufanya mchakato wa taarifa na kama taarifa hiyo inaonyesha jambo hilo lilileta matokeo mabaya huko nyuma basi haliziruhusu taarifa hizo kuingia akili no. 2.
Halikadhalika akili hii ina uwezo wa kutumia kumbukumbu ilizozihifadhi kwenye akili no. 2 hata siku za baadae na kupata kujua jambo jema na baya. Na kwa ajili hii ndio maana kuna watu hawawezi kubadilika; wao hung'ang'ania lile lile wanalolijua kwa sababu akili namba moja haijaruhusu jambo hilo kuingia ndani zaidi. (Hapa ndipo unakuta vita za udini, siasa, ukabila n.k) Hii inamaanisha kwamba akili namba 1 iliruhusu fikra fulani kuingia kwenye akili hizo zingine na kuzitoa ikawa ngumu.
Akili ya fahamu huruhusu mambo mazuri tu kupenya na kuelekea viwango vya juu vya akili (akili hizo zingine); lakini ubaya wa akili hii ya ufahamu ikiwa jambo moja litarudiwa mara nyingi kuizonga akili hiyo basi huruhusu jambo hilo kupenya kwenye akili zingine. Ndiyo maana hata matangazo ya biashara hurudiwa mara nyingi na mwishowe hushawishi wanunuzi kuipenda bidhaa hiyo bila sababu kwa sababu imesisitizwa mara nyingi sana kwenye akili yao ya ufahamu.
Kwa hiyo tuepuke kutazama au kusikiliza mambo tusiyoyapenda kwani yakijirudia sana kwenye akili ya fahamu basi yataingia kwenye akili ya nusu fahamu na kuturudisha nyuma kimaendeleo, kiakili, kiafya hata kimawazo.
2. Akili ya nusu fahamu.
Akili hii huchanganua kila taarifa bila kujali mbaya au nzuri. Akili hii hulichanganua jambo kama lilivyo bila kuongozwa na uzoefu wa nyuma. Na hii ndio akili ambayo wagunduzi na wabunifu wengi uongozwa nayo maana wao hawaathiriwi na kupima jema wala baya (hali ya kusitasita). Akili hii huleta taswira kama za kwenye ndoto. Akili hii humpeleka mtu kujenga taswira ya kufikirika ya jambo zuri sana na akiileta kwenye mazingira halisi (ya duniani) basi jambo hilo huwa la kuvutia na kusisimua na hapa ndipo wagunduzi hujipatia heshima na umaarufu. Akili hii huchakata jambo kwa muunganiko wa maarifa yote kiasi kwamba tatizo lenyewe huwa ni sehemu ya jawabu. Kwa hiyo tofauti kuu ya akili ya fahamu na nusu fahamu ni kwamba akili ya fahamu haitoi suluhisho la tatizo bali huzuia jambo baya kuingia kwenye akili ya pili wakati akili ya nusu fahamu huchakata taarifa bila kuangalia ni mbaya au njema na pia hutatua tatizo na kulipatia jawabu. Ndiyo mana watu wanaotumia sana akili ya kwanza hawana uwezo wa kutosha wa kutatua matatizo.
3. Akili ya kutojifahamu.
Akili hii haina tofauti na usingizi fofofo ambayo humpeleka mtu kwenye ulimwengu wa vitu visivyoonekana kwa macho na ulimwengu huo ni mkubwa kiasi kwamba ulimwengu huu tunaoishi ni sawa na punje ya haradali. Huko ndiko chanzo cha vitu vyote vinavyoonekana Duniani. Japo vitu hivyo si vya kushikika wala kuonekana ni vitu katika hali ya mawazo tu. Kama tujuavyo vitu vyote huanza na wazo kabla hakijawa halisi. Basi huko ndiko penyewe. Na hapo unashauriwa kabla ya kulala basi jenga tabia ya kujiuliza swali au kitu kinachokusumbua kuwa utakitatuaje. Basi akili hii hulifanyia kazi na kukupatia jawabu siku moja. Hata kama umetafuta namna ya kufanya jambo fulani kwa muda mrefu na ukashindwa, usikate tamaa endelea kufanya zoezi la kujiuliza mara kwa mara na siku isiyo na jina utapata jawabu na utashangaa imetokeaje.
Hili ndilo jambo ambalo huwatokea wagunduzi.
Kwa leo tuishie hapa natumaini utakuwa umenielewa.