Neno La Leo: Jamii Ya Walo Wema Imsamehe Elizabeth ' Lulu' Michael

maggid

JF-Expert Member
Dec 3, 2006
1,084
1,246
Ndugu zangu,


Jana amemezikwa Steven Kanumba , kipenzi cha wengi.
Mauti ya Steven Kanumba yanatukumbusha wanadamu ukweli huu; kuwa maisha yetu hapa duniani ni mafupi sana. Hivyo, lililo jema kwetu wanadamu ni kuishi kwa kutenda yalo mema. Kuwatendea mema hata tunaodhani wametukosea, maana, tutawasaidia kujifunza kutenda mema. Na ni mwanadamu gani asiyekosea?


Na moja ya adhabu kubwa mwanadamu unaweza kuipata humu duniani kutoka kwa wanadamu wenzako ni adhabu ya kutengwa na wanadamu wenzako.


Msichana Lulu ameshapata na anaendelea kuipata sasa, adhabu kubwa sana kutoka kwa wanajamii. Adhabu ya kupewa hukumu ya mauaji na kutengwa na wengine. Lulu , ambaye ni mmoja wa waliokuwa karibu na marehemu Kanumba hata katika dakika zake za mwisho maishani, na ambaye alikuwa mpenzi wa Kanumba, hakuweza kushiriki mazishi ya mpenzi wake. Hiyo nayo ni adhabu kubwa kwa Lulu kupewa na wanadamu wenzake.


Yumkini Lulu ana mapungufu yake kama mwanadamu, lakini, kwa sasa hastahili adhabu kali hiyo kutoka kwa wanajamii. Kwa kosa ambalo hakuna aliye na hakika leo kuwa amelitenda. Ndio, Lulu aweza kuwa mwanadamu mwenye mapungufu yake mengine, lakini , hayo yasitufanye wanadamu tuwe na haraka ya kumpa hukumu isiyo ya haki. Na kwenye mienendo ya maisha, ni mwanadamu gani asiye na mapungufu?

Maana, tangu mara ile ilipofahamika, kuwa msichana Elizabeth ‘ Lulu' Michael alikuwepo kwenye mazingira ya kutokea kwa kifo cha Kanumba, basi, jamii, huku ikisaidiwa na vyombo vya habari, haraka ikapata wa kumnyoshea kidole. Na hukumu ya Lulu kutoka kwa wanajamii walo wengi ikawa imetolewa hapo. Kwamba Lulu ndiye muuaji. Kwa sasa, hukumu hiyo haiwezi ikawa ya haki mpaka pale wenye mamlaka ya kututhibitishia hilo watakapofanya hivyo.


Na hata kama ugomvi, uliotokana na wivu wa kimapenzi , wa Lulu na mpenzi wake ulipelekea mauti ya Kanumba, bado maelezo tuliyoyasikia hayamwonyeshi Lulu kuwa na dhamira ya kutaka kutenda maovu anayohukumiwa na wanajamii kuwa kayatenda. Hivyo, naye, kama mwanadamu, anastahili msamaha kutoka kwa wanajamii wengi walo wema.


Katika wakati huu mgumu sana kwa msichana Lulu, vyombo vya habari viwe mbele katika kumsaidia Lulu kama mwanadamu mwenzetu, badala ya kutumia balaa lililomkuta kama mtaji wa kuandika na kutangaza udaku wa kuuzia magazeti na kuvutia watazamaji wa runinga na wasikilizaji wa redio.


Maana, kwa adhamiriae kutumia magumu yanayomkabili msichana Lulu kuvuna, basi, hana atakachokivuna zaidi ya kuvuna dhambi.


Badala yake, media isaidie katika kutufanya wanajamii tujitafakari. Kwa vile, habari za matukio ya mahusiano yasiyo na staha na matendo ya kiuhuni yanayofanywa na baadhi ya wanajamii wakiwemo wasanii, huwa yanashabikiwa na vyombo vya habari badala ya vyombo hivyo kushiriki kukemea na kuelimisha jamii. inasikitisha, kuwa katika wakati huu, vyombo hivyo vya habari vyaweza kabisa kuwa kwenye harakati za kuandaa stori zaidi za ‘ kumning’iniza’ zaidi Lulu ambaye tayari ameshaning’inizwa hadharani.


Ndugu zangu,


Kama wanajamii, na wengine kama wazazi. Lulu anabaki kuwa ni msichana mdogo anayehitaji kusaidiwa katika wakati huu mgumu kwa maisha yake. Yumkini vyombo vya dola vinaweza vimtie au visimtie hatiani. Hivyo, kumwachia huru Lulu.


Lakini, bado hukumu ya jamii ikabaki pale pale. Hukumu ya Lulu kutengwa na jamii. Hiyo ni hukumu mbaya zaidi inayoweza kuchangia hata kuyafupisha maisha ya msichana huyu mdogo. Jamii haina faida na hukumu kama hiyo. Ni heri ikamwacha huru aende akapambane na yanayomkabili mbele yake. Ndio, akapambane na maisha haya magumu ya dunia hii bila kujisikia kutengwa na wanajamii wenzake.


Na naamini, leo kuna wengi kama mimi, wenye kufikiri hili, kuwa jamii ya walo wema imsamehe Elizabeth ‘ Lulu’ Michael.


Na hilo ni Neno La Leo.


Maggid Mjengwa
Dar es Salaam.
0788 111 765
http://mjengwablog.com
 
I have already 4gven her,now namhurumia tu,na hakika Mungu atamsamehe,lilomtokea Lulu hata wewe lingeweza tokea,na kama mzazi Lulu nitampenda,na Wanajamii wasiowaelewa watamwita Murderer,buut c kosa lao,n mawazo yao yanayopelekeshwa na media uchwara,bila kuangalia mambo kwa kina.R.ip sK,bt Lulu! Anaitaj saikolojist wa hali ya juu
 
Shukran sana mleta mada mi binafsi nshamusamehe Lulu na namuonea huruma sana huyu mtoto kwan yaliyomkuta ni mtihani mkubwa sana nawashauri wanaomlaumu lulu waache kumlaum na wamusamehe wamchukukulie kama mtoto wao au mdogo wao. Najua Kanumba alikuwa akipendwa sana lkn ndo kashatutoka cha kufanya ni kuangalia jins ya kumsaidia Lulu make kufungwa kwa luku hakuwezi kurudisha uhai wa mpendwa wetu Kanumba la msingi ni kumuombea Lulu aachiwe huru japo atakutana na mitihan mkubwa kwenye jamii yetu ukiwemo wa kuchukuliwa kama muuwaji, na kuwepo kwa Lulu nyumbn kwa kanu mba wkt kifo chake kinatokea isiwe sbb za kumchukulia Lulu kama muuaji hebu tujaribu kuukumbuka wimbo wa Hussen Machozi ule wa Kafia geto.
 
IMEANDIKWA USIHUKUMU USIJE UKAHUKUMIWA, mi ni nani basi mpaka nimuhukumu Lulu? Wacha sheria ichukue mkondo wake. REST IN PEACE KANUMBA
 
Fanyeni utafiti kubaini kama yuda iskariote alisamehewa na mungu au la. Sio mnakimbilia kutoa misamaha hata pasipohitajika msamaha.
 
Ni nani aliyekwambia Lulu ametengwa? Lulu ametengwa na Waasherati wenzanke na vyombo vya habari uchwara basi, kama akitoka akubali kumpokea Yesu uone kama wapendwa katika bwana huwa wanamtenga mwanakondoo.

Huyu anatakiwa ayakabidhi maisha yake kwa Yesu, nadhani hakukuwa na njia yoyote mbadala ya kumnyoosha huyu mtoto ndipo mungu akaamuwa kuitumia njia hii kumnyoosha huyu mtoto, sasa usikute akaja kuwa muimba Injili mzuri tu.
Nasisitiza Lulu hajatengwa wala hajahukumiwa bali ananyooshewa vidole na tabaka la wazinzi na waasherati. na hili ndilo neno langu la leo.
 
Fanyeni utafiti kubaini kama yuda iskariote alisamehewa na mungu au la. Sio mnakimbilia kutoa misamaha hata pasipohitajika msamaha.
Lulu amekukosea nini Mkuu mpaka utowe msamaha au ukatae kumsamehe?
 
Baba yetu uliye mbinguni,Jina lako litukuzwe,Ufalme wako uje,Mapenzi yako yatimizwe,hapa duniani kama huko mbinguni.Utupe leo riziki yetu.Utusamehe makosa yetu,kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu.Na usitutie majaribuni,lakini utuokoe na yule mwovu.Kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele.Amina.

*** Unawezaje kusema utusamehe makosa yetu kama nasi tunavyowasamehe waliotukosea..wakati hujasamehe bado?****

Namuhurumia kwa yale yote anayiopitia huyu mtoto sasa Mungu aendelee kumtia nguvu huko alipo na sheria ndio itaamua sasa.
 
tukimsamehe ndo kesi ya mauaji itafutwa?

mbona kuna watu kibao wako jela tena kwa kesi

za kusingiziwa hamuwaombei msamaha iweje kwa huyo

mzinzi mdogo pamoja na mwenzake aliekufa?
 
Back
Top Bottom