Ndoto ya wana Tabora, salam kwa Ismail Aden Rage....

Hossam

JF-Expert Member
Feb 10, 2011
3,538
2,155
Mimi Pangu Pakavu nimeota ndoto kwa niaba ya wana Tabora, ni ndoto niliyoota usiku wa kuamkia leo na ndoto hii ni salam kwa Rage na kumuomba afikirie upya nafasi yake ya ubunge Tabora mjini.

Nimeota ndoto vijana wa Tabora mjini wataacha kunywa gongo huko Isevya na Ng'ambo na watapata ajira lukuki pale Tabotex kiwanda cha nyuzi, na mama zao nao watajiajili kwa kjpika chakula na kuwauzia vijana hao, na hata hawa bodaboda nao watapata dili kupeleka watu Tabotex na kuwarudisha makwao.

Usiku mie nimeota, shida ya maji huko Ng'ambo na Tambukareli, na Malolo na Ntalikwa sasa itatatuliwa kwa kuchimba kisima cha kudumu kirefu katika kila kata, hapo vijana wetu watapata na fursa ya kulima mbogamboga na kujipatia soko pale Orion Tabora hotel, Frankman Hotel, George Complex, na Wilca Hotel, hii itasaidia kupunguza wimbi la vijana kujiingiza katika vitendo vya uhalifu.

Na tazama ndoto yangu ikanionyesha vijana machinga wasivyo na sehemu maalum ya kufanyia biashara kwamba ma wao sasa wamepatiwa sehemu maalum na sasa hawaungui tena na jua na machinga hao wanao umoja wao na wameshajenga na kijiofisi chao tayari kuomba msaada benki ili kupanua biashara zao.

Ole wangu mie Pangu Pakavu ambae nimeota watoto wetu huko Kipalapala, Chemchem, Mbugani, na Izimbili, kuwa sasa wanapewa hata misaada ya uniform za shule zile za bukubuku na kandambili ili waache kupekua, huduma za afya nazo zimeboreshwa, vituo vya polisi vimejengwa na sasa hakua tena hofu.

Mimi Pangu Pakavu ndoto yangu ikanichukua sana, na tazama nikaona utalii wa asili ukitangazwa kwa kasi Tabora, nikaona lile Kaburi la Mtemi Mirambo 'The Napoleon of East Africa', kule Ulyankulu sasa likihifadhiwa vizuri, nikaona Tembe la Livingstone huko Kwihara nalo likitembelewa na watalii kwa kuwa lilitangazwa, nikaona na ile subway kutoka pale bomani hadi railway station ikitangazwa sehemu ya utalii, nikaona jiwe lenye mizizi huko Magereza sasa likitangazwa kama kivutio, na nikaona vijana wengi wakiwa bize kuwaongoza watalii na kujipatia senti mbili tatu.

Mwisho wa ndoto yangu nikaona asali safi ikibubujika kutoka pale Nyuki airport road, ikiwa na lebo safi 'The Pride of Unyanyembe' na nikaona vijana kwa wazee wakipata ajira kiwandani ambapo asali huchumwa nz kupakiwa, nikaona magari elfu yakileta asali mbichi toka Sikonge na Igalula na Goweko na Urambo. Na huko asali itokako nikaona vijana kwa wazee wakichangamka kurina na kutega mizinga mingi zaidi, huku wale wanaouza asali sasa wakijenga nyumba za bati, wakinunua nguo nzuri, na wengina wakinunua hata redio na tv.

Na ndoto yangu ikanionyesha Mh Raage akiwa bize na simba s c, ambayo hata haifanyi vizuri, nikaona Raage akiwa bize na kujenga majumba huko Makokola na zaidi akiwa na mabunduki kiunoni hata wakati wa amani. Nje ya nyumba yake nikaona msururu mkubwa wa watu wakiwa na mabakuli wakiomba msaada kwake, yeye wala hana habari, gafla nikastuka toka usingizini na kujikuta nikitokwa na machozi baada kugundua kwamba hiyo ilikuwa ndoto tu.

"Ninayo imani, mimi Pangu Pakavu, kwamba siku moja wakazk wa Tabora watasimama kwa miguu yao na watafaidi mrundikano wa rasilimali zao, mkoa wa Tabora utakuwa tajiri kwa kuwa tokea zamani ulikuwa ukiitwa 'business center' na nina imani watoto wetu sasa watachagua MwanaTabora, Mnyamwezi mwenzao na mzalendo ili kuamsha matumaini yalopotea ya watu wa Tabora, hii ni imani ambayo nitaihubiri kwa kila mja wa Tabora na kila mwenye jicho la tatu''

Ni mimi,
Pangu Pakavu,
Nakusalimia.
 
Hosssam, ile kampuni yako ya u ISP bado ina -operate Tbr. siku nyingi mzee nataka kuja unifungie internet nyumbani kwangu.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom