KATIKA hali inayotia shaka na kuzusha wasiwasi kwa wakazi wa Jimbo la Igunga, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimetangaza hali ya hatari na kuagiza vijana wake waliokuwa katika kambi za mafunzo kwenda jimboni humo kwa kile kilichodaiwa kulinda amani, huku kikisema kuwa kisilaumiwe kwa yatakayotokea kuanzia sasa.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, amesema wamechoka na vurugu wanazofanyiwa na vyama vya upinzani, hususan CHADEMA, na hawapo tayari kukaa kimya wakishuhudia ukatili huo.
Alisema chama hicho kimeamua kuchukua hatua za kujilinda kwa kuwatumia vijana wake, ingawa alidai kwamba vijana hao hawataingilia kazi za Jeshi la Polisi.
Nape alisema hayo jana katika mkutano wake na waandishi wa habari, Ofisi Ndogo ya Makao Makuu, Dar es Salaam.
Katika wiki inayomalizika leo, CCM imejikuta katika mgogoro mkubwa Igunga, baada ya kutuhumiwa na CHADEMA na ikakiri kwamba inaandaa vijana katika makambi; mara kiongozi wake mwandamizi anayeongoza kampeni za CCM akafumaniwa na mke wa mtu; halafu Mkuu wa Wilaya ya Igunga, Fatma Kimario, akafumwa na vijana wa CHADEMA akifanya mkutano na wajumbe wa CCM jirani na eneo la mkutano wa CHADEMA, akaondolewa kwa nguvu.
Nape alisema CCM wamechoka kushuhudia vitendo vinavyokwenda kinyume cha sheria na maadili ya Mtanzania.
Alisema tangu Septemba 9, mwaka huu kumekuwa na matukio ya udhalilishaji yakiwamo ya kubakwa na kupigwa kwa wanachama na viongozi wa chama hicho, hali inayoashiria kuvurugwa kwa amani kunakofanywa na kikundi cha watu wachache.
Alisema: "Haiwezekani CCM tukae kimya. CCM hatuko tayari kuona viongozi wetu wakidhalilishwa. Kuna vijana wameletwa kutoka mikoa mbalimbali na CHADEMA, hivyo nasi tutatumia vijana wetu kuwalinda viongozi na chama chetu na tusije kulaumiwa kwa litakalotokea."
Alitaja matukio ya vurugu kuwa ni kumwagiwa maji yanayohisiwa kuwa tindikali kwa kijana Mussa Tesha kulikotokea Septemba 9, mwaka huu alipokuwa akibandika picha za mgombea wa CCM. Aliongeza kuwa Septemba 11, Mjumbe wa Nyumba Kumi, Michael Shija, alikatwa mapanga na kuibiwa simu na baiskeli yake.
Mbali na matukio hayo, alisema Septemba 12, Mwalimu mstaafu Francis Msalika, alivamiwa nyumbani kwake saa saba usiku na mtoto wake wa kike mwenye umri wa miaka 12 alibakwa na kutupwa katika eneo la mto.
Wabunge wa CHADEMA wakamatwa tena
Siku moja baada ya Jeshi la Polisi wilayani Igunga kuwakamata na kuwaachia wabunge wawili wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), wabunge hao jana wamekamatwa tena na kuzuiliwa kwa kile kinachodaiwa ni maagizo kutoka ngazi za juu.
Wabunge hao Slyvester Kasulumbai (Maswa Mashariki) na Suzan Kiwanga (Viti Maalumu) pamoja na Kamanda wa Baraza la Vijana (BAVICHA), Anwar Kaswega, wanashikiliwa kwa tuhuma za kumshambulia Mkuu wa Wilaya ya Igunga, Fatma Kimario, alipokuwa kwenye shughuli za kiserikali katika Kijiji cha Isakamaliwa.
Wakati Mkuu wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Makao Makuu, Naibu Kamishna wa Polisi, Issaya Mungulu, akisema kukamatwa kwa viongozi hao wa CHADEMA ni sehemu ya upelelezi wao, Mbunge wa Iramba Mashariki, Tundu Lissu (CHADEMA) alisema polisi wamekataa kuwaachia wabunge hao kwa dhamana.
Aliongeza kuwa polisi walisema wamewakamata wabunge hao baada ya kupokea maelekezo kutoka ngazi ya juu. "Sasa sijui ni nani, labda Stephen Wassira, nimempigia IGP Mwema hajapokea, nimemtumia ujumbe hajajibu. Kwa hiyo hatujui ni mkubwa gani," alisema Lissu.
Alisema wabunge hao wanatuhumiwa kumpiga DC, kumvua hijabu na kumwibia simu yenye thamani ya sh 400,000. "Nimezungumza na Mkuu wa Operesheni Mungulu, akasema watawashikilia mpaka hapo watakapowapata wengine waliokuwepo kwenye hilo kundi," alisema Lissu.
Akizungumzia tuhuma hizo, Tundu Lissu alisema kukamatwa kwa wabunge hao ni njama za kupunguza kasi ya kampeni za CHADEMA. Amesema wakati polisi na watu wote wamekisukumia chama hicho lawama, polisi hao hao wamepuuzia malalamiko yaliyotolewa na CHADEMA dhidi ya mkuu wa wilaya.
Lissu alimtuhumu mkuu wa wilaya kwa kufanya mkutano wa kampeni kwa kuwahutubia wazee maarufu, viongozi wa dini na mabalozi wa CCM ili wasiende kwenye mkutano wa hadhara wa CHADEMA uliokuwa ukihutubiwa na Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa.
Alisema kanuni za maadili ya uchaguzi zinawakataza watendaji wa serikali kama wakuu wa wilaya kujihusisha kwa namna yoyote kuingilia kampeni au kukibeba chama cha siasa na kutumia gari na muda wa serikali kufanya kampeni.
Naye Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Slaa, amesema CCM na polisi wanamlinda mkuu wa Wilaya ya Igunga ambaye anashiriki kuhujumu mikutano ya chama chake. Aliongeza kuwa polisi kama ni wakweli na watenda haki, walitakiwa kumkamata kiongozi huyo wa serikali badala ya wabunge wa CHADEMA ambao walikuwa wakipinga dhuluma wanayofanyiwa na mkuu huyo wa wilaya.
Dk. Slaa alisema sasa watazunguka nchi nzima kutangaza uovu wa polisi na wa CCM wanaofanya kazi ya kuwakandamiza viongozi wa vyama vya upinzani na kuwataka Watanzania kukikataa Chama Cha Mapinduzi.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Igunga, Fatuma Kimario, amedai kuwa alikuwa na mkutano wa ndani na viongozi wa serikali ya kijiji, ikiwa ni sehemu ya kazi za kawaida za kiserikali na kwamba hakuwa na lengo la kuingilia mkutano wa CHADEMA.
Aliwatuhumu wabunge hao kwa kumdhalilisha na kumtukana matusi ya nguoni, hali aliyodai kuwa imemfedhehesha sana.
Habari za kuaminika zinasema kuwa sakata zima la tukio hilo lilianza baada ya msafara wa CHADEMA kufika katika eneo la kampeni saa 8:00 mchana na kabla mkutano haujaanza, Meneja wa Kampeni wa chama hicho, Sylivester Kasulumbai, aliarifiwa kuwa mkuu wa wilaya hiyo alikuwa akifanya mkutano wa ndani na viongozi wa eneo hilo.
Kasulumbai baada ya kusikia taarifa hizo, aliwaongoza viongozi wenzake hadi katika ofisi ya mtendaji wa kata kulikokuwa kunafanyika mkutano huo ambapo walihoji aliko mkuu huyo wa wilaya.
FFU wenye silaha watanda
Wakati Nape akitangaza hali hiyo, mjini Igunga, idadi kubwa ya askari polisi wakiwamo wale wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) wametanda kila kona ya mjini hapa. Askari hao wakiwa wamevalia rasmi mavazi ya kazi, siku nzima ya jana walikuwa wakizunguka katika mitaa ya mji wa Igunga wakiwa na magari yao na yale yanayobeba maji ya kuwasha.
Kuongezeka kwa polisi hao kumewatisha wakazi wengi ambao hawakuzoea hali hiyo, jambo ambalo limelalamikiwa na CHADEMA.Hata hivyo, baadhi ya viongozi wa CUF, wameeleza kufurahishwa na ulinzi huo na wameishambulia CHADEMA kwa madai ya kuhusika na vurugu zinazotokea.
Taarifa hii imeandaliwa na Joseph Senga, Irene Mark, Mustapha Kapalata (Igunga) na Bakari Kimwanga, Shilila Mzavah (Dar es Salaam).
|
| |