BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,789
- 288,015
Mtanzania auawa kikatili Dubai
2009-03-04 10:56:04
Na Mashaka Mgeta
2009-03-04 10:56:04
Na Mashaka Mgeta
Raia wa Tanzania ameuawa kinyama kwa kutupwa katika mashine za kusaga vyakula huko Dubai, Falme za Kiarabu na mwili wake kukatwa vipande vipande.
Taarifa zilizolifikia gazeti hili zimemtaja Mtanzania huyo kwa jina la Eric William Maige ambaye wazazi wake wanaishi Gezaulole, jijini Dar es Salaam.
Marehemu Eric anadaiwa kuwa mfanyakazi wa kampuni ya Gulf Import and Export Limited wakati wa uhai wake.
Akiwa katika kampuni hiyo, taarifa zinadai kuwa Eric alikuwa msimamizi katika kitengo cha G.G Department Al-Guair Food.
Maofisa wa habari katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, hawakuwa tayari kuzungumzia kifo hicho, kutokana na kile walichokieleza kuwa kutopata taarifa hizo.
Hata hivyo, maofisa hao wamethibitisha kupata taarifa hizo kutoka kwa watu waliojitambulisha kuwa ndugu wa marehemu Eric.
Baba mzazi wa marehemu Eric, William Maige, aliliambia Nipashe jana kwa mujibu wa taarifa zilizopo, mwanae alipoteza maisha kwa kuuawa na watu waliokuwa chini yake kiutendaji.
``Mwanangu alikuwa msimamizi katika eneo lake la kazi, sasa kuna taarifa kwamba waliokuwa chini yake kimajukumu, walimtupa kwenye mashine za kusagia chakula, akafa,`` alisema.
Kwa mujibu wa Mzee Maige, taarifa hizo zilitolewa na mdogo wa marehemu Eric, Raymond Maige, anayefanya kazi katika kampuni alipokuwa marehemu.
``Tuna uhakika kwamba mtoto wetu amekufa kwa sababu taarifa za kifo chake tumezipata kutoka kwa mdogo wake aitwaye Raymond, walikuwa wote huko Dubai,`` alisema.
Alisema Raymond alifikisha taarifa nyumbani kwao kwa njia ya simu, kwamba Eric aliuawa asubuhi ya Jumatatu wiki hii.
Mzee Maige alisema kutokana na hali hiyo, familia inatafuta uwezekano wa kupata msaada utakaofanikisha kurejeshwa nyumbani kwa mabaki ya mwili wa Eric.
Alipoulizwa kwa njia ya simu jana, mmoja wa maofisa habari katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Assah Mwambene, alisema hakuna taarifa kuhusu tukio hilo.
Mwambene alitoa namba kwa ajili ya mawasiliano na Balozi Mohamed Musa aliyepo Abu Dhabi, ambapo simu moja kati mbili zilizotolewa ilikuwa inaita bila kupokewa.
Hadi tunaingia mitamboni jana jioni, jitihada za kumtafuta Balozi Musa na taarifa zaidi kuhusu mauaji hayo, zilikuwa zinaendelea.
SOURCE: Nipashe