![]()
Ama kweli siku hazigandi, alijiimbia Lady JD.
Nikikumbuka miaka ile nikiwa kijana shababi mwenye siha nzuri, kipindi hicho, mkate wa Boflo kwa mpemba ulikuwa unauzwa hela kumi. Wakati huo sijakutana na Mama Ngina, wala hawa wanangu King'asti na Asnam hawajulikani duniani nilitesa sana na vibinti.
Nakumbuka wakati huo mabinti walikuwa wanatokelezea na magauni yao ya vitambaa vya Polister, Criplin au Chirmen walivyonunua kwa washihiri, wakati huo vitamba vilikuwa vinapimwa kwa kipimo maarufu cha ZIRAA.
Nilikuwa kama Helikopter ndege isiyochagua mahali pa kutua. mambo yangu yalikuwa bambam na vijisenti mfukoni havikuwa vya kujibana, yaani nilikuwa nikimhonga mwanamke shilingi kumi atatangaza mtaa mzima. "Baba ana pesa yule kama njugu...!" Atasema kwa mashoga zake, kumbe ndio alikuwa ananipigia upatu, mabinti kuniwania.....
Sasa kiko wapi?
Mtambuzi nishageuka Simba Mzee aliyeshiba mizoga, vitoweo vinanichezea sharubu, mwenyewe nimebaki kuvikodolea macho. Nitoe wapi nguvu ya kuhiminili sarakasi za mabinti wa siku hizi ambao wanataka kugeuzwa geuzwa kama samaki kikaangoni.
Kwa bahati mbaya sana mazingira ya kazi yangu achilia mbali hapa kazini kwangu kazi ninayofanya hunikutanisha na vimwana walioumbwa wakaumbika, na kujipamba na lebasi za ulimbwende pamoja na makochokocho chungu mzima. Ukichanganya na vivazi wanavyovaa, Oh mai.........! Utashangazwa na uumbaji wa Mwenye enzi Mungu.
Kutokana na macho yangu kukaa kihayawani. Ama kweli macho ya muasherati yana hila mbaya, hivi sasa nina bahati mbaya ya kusingiziwa na mabinti kuwa nawatongoza. Yaani nikizungumza na binti yeyote hapa kazini au popote pale huishia kunisingizia eti nimemtongoza...!
Hivi sasa hapa kazini kuna vita baridi miongoni mwa mabinti wakitupiana vijembe. Si mnawajua wanawake kwa mipasho...! Hivi majuzi wawili wametiana vidole vya macho, lahaula, kesi imefika kwa Meneja Rasilimali Watu. Mara simu hiyo napigiwa, mie huyo kwa Meneja Rasilimali Watu, nikijua tunaenda kuzungumzia mambo ya mafunzo kazini. He! Nafika, nakutana na mabinti wametumbuliana macho kama kuku mitetea inayogombea Koo (Jogoo).
Kesi iko Kilingeni.......
Hivi hawa mabinti wananitafutiani...?
Jasili haachi asili, hicho ndicho nichokipata hapo kwenye red unaposema "mwenyewe nimebaki kuvikolea macho". Ni ngumu sana kuondokana na asili ndio maana mwanzo kabisa umekiri na kuweka wazi historia yako juu ya mambo hayo wakati ukiwa na nguvu ya kutosha yaani kwenye akili na mwili.
Nimeshageuka Simba mzee mchezewa sharubu, hapa inaonesha kabisa roho i radhi kutimiza matakwa ya asili lakini mwili hauko radhi hata kidogo hasa kwa kuzingatia hili "Nitoe wapi nguvu ya kuhiminili sarakasi za mabinti wa siku hizi ambao wanataka kugeuzwa geuzwa kama samaki kikaangoni."
Wakati ukuta, ukishindana nao utaumia, nafurahi kuona mtu akikubaliana na hali halisi kama ulivyofanya.
Hivi hawa mabinti wananitafutiani...?
Hawa unaweza kuta hawana kosa sana ila wanashindana na asili zilizo ndani yao wenyewe na ndani yako pia, macho yako yapokutana na wao kuna ishara fulani huisoma na hiyo ndio inawaletea shida. Waeleze huna nguvu tena za kugeuzana kama kama samaki kikaangoni, wasije poteza kazi bure kisa wewe mzee wa watu.