Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Bw. Antony Blinken anafanya ziara nchini China, ikiwa ni ziara ya kwanza ya ofisa mwandamizi wa serikali ya Marekani nchini China tangu Rais Joe Biden aingie madarakani. Ziara hii inatajwa kuwa ni ziara muhimu, lakini inayofanyika katika kipindi ambacho uhusiano kati ya China na Marekani ukiwa na mikwaruzano.
Pamoja na kuwa baadhi ya wachambuzi wanaona kuwa ziara hii haina matarajio makubwa kwa pande zote mbili, ukweli ni kwamba hii ni ziara muhimu kwa hali ya utulivu wa dunia. Kama pande hizi mbili zenye nguvu kubwa kiuchumi na kijeshi haziwezi kuwa na mawasiliano mazuri, si jambo la heri kwa dunia. Lakini pia licha ya ubabe na ujeuri wa Marekani, imefika mahali Marekani imetambua kuwa ni lazima iwasiliane na haiwezi kuiweka kando au kuikwepa China.
Tukiangalia hali halisi kiuchumi kwa sasa, tunaweza kukumbuka kuwa si muda mrefu uliopita Chansela wa Ujerumani Bw. Olaf Scholz, Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron, na mwenyekiti wa kamisheni ya Ulaya Bibi Ursla Von de Leyen, walifanya ziara nchini China, kikubwa kikiwa ni biashara na China, na maslahi ya kiuchumi ya nchi zao. Marekani imetambua kuwa kuiweka pembeni China, bila shaka ni sawa na kujihujumu yenyewe kiuchumi.
Kwenye maswala ya usalama imeonekana kuwa ni hatari kwa pande mbili kutowasiliana. Katika miezi ya hivi karibuni kumekuwa na mivutano katika eneo la bahari mashariki na kusini mwa China, mivutano ambayo kwa nyakati fulani ilionekana kuweza kuzusha hatari ya vita. Hata njia za mawasiliano kati ya majeshi ya pande hizo mbili ni kama ziliwekwa kando. Lakini pia bado kuna tofauti kubwa kati ya Marekani na China kuhusu suala la Taiwan, na hasa baada ya aliyekuwa spika wa bunge la Marekani Bibi Nancy Pelosi kutembelea Taiwan kinyume na makubaliano kati ya pande mbili, na hata kitendo cha mkuu wa kisiwa cha Taiwan kutembelea Marekani.
Kwenye upande wa diplomasia, ni wazi kuwa maswala makubwa yanayoitatiza dunia kwa sasa yanahitaji China na Marekani ziwasiliane. Iwe ni mgogoro kati ya Russia na Ukraine, au mabadiliko ya tabia nchi, na hata usimamizi wa jumla wa mambo ya duniani, bila ushirikiano kati ya China na Marekani mambo haya yanaweza kuwa na changamoto nyingi.
Katika kipindi chote tangu Rais Joe Biden aingie madarakani, China imeeleza wazi kukasirishwa na vitendo vya uchokozi vya Marekani. Lakini Marekani ilionyesha ujeuri ikidhani kwamba China itapiga magoti na kuanza kuibembeleza, lakini katika kipindi chote hicho China imekuwa kimya na kuwa na msimamo thabiti ikitambua kuwa kulinda heshima yake pamoja na maslahi sio kosa, na si jambo la kuibembeleza Marekani. Ni vizuri Marekani yenyewe imetambua kuwa haikuwa sahihi, na kwamba bila kushirikiana na China haitakuwa rahisi kwake, kwa hiyo kumtuma Bw. Blinken kufanya ziara nchini China ni hatua sahihi ya Marekani kurekebisha makosa yake.
Ukweli unabaki palepale kuwa ziara ya Bwana Blinken nchini China sio mwarobaini kwa tofauti zilizopo kati ya China na Marekani. Bado kuna tofauti za kimsingi ambazo zipo na zitaendelea kuwepo, lakini kama Marekani ikiendelea na ishara iliyotolewa na ziara ya Bwana Blinken, yaani kufanya mawasiliano na upande mwingine bila kujali tofauti zilizopo, hiyo ndio diplomasia chanya.