Kijiji cha Bwelanga kimezungukwa na Ziwa Victoria kwa pande tatu, hivyo pia kinaitwa Kijiji cha Peninsula. Kijiji hicho kiko mbali na miji, hivyo kufanya mawimbi ya televisheni kuwa duni, jambo lililoleta shida kubwa kwa wakazi huko kutazama TV. Lakini hivi karibuni shida hiyo imetatuliwa, kwani mradi wa “Wancuntong” unaofanywa na kampuni ya Kichina umepeleka vipokezi vya dijiti vya kisasa, ikiwemo antena, vipokezi vya mawimbi ya satelaiti, TV za kidijitali, projekta, na mfumo kutumia nishati ya jua, na sasa wanakijiji wanaweza kutazama TV bila malipo kupitia satelaiti.
Mradi wa “Wancuntong” ni moja ya hatua za ushirikiano kati ya China na Afrika zilizopendekezwa kwenye Mkutano wa Kilele wa Baraza la Ushirikiano kati ya China na Afrika uliofanyika mwaka 2015 huko Johannesburg nchini Afrika Kusini. Mradi huo unalenga kusakinisha vifaa vya vipokezi vya TV kwenye vijiji 10,000 vilivyoko sehemu za ndabi zaidi barani Afrika, ili kuboresha mawimbi ya televisheni. Ikiwa moja ya miradi muhimu ya ushirikiano kati ya China na Afrika, utekelezaji wa “Wancuntong” unafuatiliwa sana na pande mbalimbali. Sasa miaka sita imepita. Kutokana na jitihada kubwa, mradi huo umetekelezwa kwa mafanikio katika vijiji vya ndani zaidi katika nchi za Afrika, na kunufaisha watu wengi.
Nchini Uganda, katika awamu ya kwanza, mradi wa “Wancuntong” umekamilika katika vijiji 500, na awamu ya pili ya mradi huo pia imezinduliwa, na vifaa karibu elfu 10 vya vipokezi vya TV vitapelekwa katika vijiji 400 vilivyochaguliwa. Licha ya vifaa hivyo, China pia imetoa mafunzo kwa mafundi wenyeji 1,980, ambao watawahudumia wanavijiji katika siku za baadaye.
Nchini Kenya, mradi wa “Wancuntong” uliozinduliwa mwaka 2018 pia umeendelea vizuri, na umesakinisha vifaa katika vijiji 800 vya kaunti 47, ambapo jumla ya familia 16,000 zimenufaika.
Takwimu zinaonesha kuwa, hadi Oktoba mwaka huu, mradi wa “Wancuntong” umekamilisha kutekelezwa katika vijiji 8,612 za nchi 20 barani Afrika, na bado unaendelea kupamba moto.