Moyo Ulioonja Maumivu

Moyo Ulioonja Maumivu

SEHEMU YA 66

Asubuhi ya siku iliyofuata ilipofika, mapema sana wakaondoka hotelini na kwenda hospitalini. Walipofika, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kutaka kumuona Rachel, walihitaji kujua alikuwa akiendeleaje pale kitandani.

Walipofika na kumwangalia, alikuwa kama alivyokuwa, hakuwa na mabadiliko yoyote yale, kama mashine ya gesi ilikuwa puani kwake, alitulia huku kukiwa na dripu ambayo kazi yake ilikuwa ni kupeleka maji mwilini mwake.

Kwa kifupi pale alipokuwa alionekana kama mfu ambaye alisubiri muda wake wa kufa utimie tu.

Kila mtu aliumia kile kilichokuwa kikiendelea lakini Violeth aliumia zaidi kwa kuwa mumewe mawazo yake mengi hayakuwa hapo, yalikuwa kwa mchepuko wake ambao aliutumia pesa za matumizi siku iliyofuata.

Hakuujua usaliti wa mume wake, kwake, alimuona mwanaume aliyefaa ambaye alishirikiana naye katika kila hatua ya kumuuguza mtoto wao.

Mzigo mkubwa uliokuwa moyoni mwake alihisi hata mume wake alikuwanao huohuo kumbe haikuwa hivyo kabisa. Walikaa hospitalini, muda wote Theo alikuwa akiangalia simu yake, alitegemea kuchati na Iyanya ambaye alitakiwa kusafiri kuelekea nchini India kwa ajili ya kulala naye hotelini.

Madaktari walikuwa wakiingia na kutoka ndani ya chumba alicholazwa mtoto wao, waliwaonea huruma, waliyaona maumivu waliyokuwanayo mioyoni mwao kupitia macho yao, walijua kabisa kwamba endapo wangethubutu kuwakatisha tamaa kwa staili yoyote ile hali ingekuwa mbaya mno kwao.

“Mna uhakika Rachel atapona?” hilo lilikuwa swali alilouliza Violeth kila siku.
“Atapona tu!”
“Mna uhakika?”

“Kwa Mungu hakuna linaloshindikana,” alijibu daktari maneno ambayo yalimfariji mwanamke huyo kila siku.
Siku hiyo walishinda hapo mpaka usiku ulipoingia ambapo haraka sana Theo akamuwahisha mke wake waondoke mahali hapo na kuelekea hotelini.

Violeth hakutaka kujiuliza, alihisi labda mume wake alikuwa na jambo muhimu alihitaji kulifanya na ndiyo maana alimwambia walitakiwa kurudi hotelini haraka.

Kichwa cha mwenzake hakikuwa hapo kabisa, alitegemea kujua kilichokuwa kikiendelea kwa Iyanya, alihitaji kuwasiliana naye kwa ukaribu mno na si kama vile alivyokuwa akifanya wakati alipokuwa hapo hospitalini.
 
SEHEMU YA 67

Wakaondoka na kurudi hotelini. Walipofika tu, Theo akamwambia mke wake akamletee chakula ili wale. Kwa jinsi hali ilivyokuwa ikiendelea, hakujisikia kula kabisa.

Alimwambia Theo kwamba hakusikia njaa na tumbo lake halikuwa na hamu ya kula hata kidogo. Theo hakutaka kukubali, alimwambia mke wake kuhusu hali waliyokuwa wakipitia, walikuwa wakifikiria sana, mwili ulipoteza nguvu nyingi hivyo ilikuwa ni lazima wale chakula kingi hata kama hawakuwa na hamu ya kula.

“Mke wangu! Unajua tunapotia kwenye matatizo makubwa mno ila ni lazima tule na tushibe kwa kuwa tunapoteza nguvu nyingi sana,” alisema Theo huku akiwa karibu na mke wake huyo ambaye muda wote alionekana kuwa mpole kana kwamba alikuwa akiumwa.

“Sina hamu ya kula!” alijibu kwa sauti ya chini.
“Hata mimi pia ila ni lazima tujilazimishe mpenzi,” alisema Theo huku akimwangalia mke wake huyo.

Hakuwa na njaa bali alikuwa akitafuta njia ya kutoka ndani ya chumba hicho. Alihitaji kuwasiliana na Iyanya, alitaka kufahamu ni kitu gani kiliendelea baada ya kumtumia pesa zile.

Hakuwa na njia yoyote ya kuwasiliana na msichana huyo zaidi ya kuondoka ndani ya chumba hicho. Ajifanye anakwenda kwenye mgahawa na huko apate nafasi ya kuzungumza naye na ndiyo maana aling’ang’ania sana.

Baada ya kuona mume wake ameomba mno ale, akakubaliana naye na hivyo Theo kuelekea chini kwenda kuchukua chakula.
Moyo wake ulikuwa na furaha tele, hakuamini kama mume wake aliweza kumkubalia na kwenda huko.

Alipofika chini, kitu cha kwanza kilikuwa ni kutafuta sehemu tulivu na kuanza kuwasiliana na msichana huyo kupitia WhatsApp.
“Kwani umefikia wapi?” aliuliza kwa sauti ya kawaida.

“Nipo Afrika Kusini!”
“Afrika Kusini?” aliuliza Theo huku akionekana kushtuka, hakutegemea kabisa kusikia jibu hilo. “Ndiyo!”
“Kuna nini huko?”

“Kaka yangu amefariki! Nimewahi mazishi halafu keshokutwa nitakuja huko!” alisema msichana huyo huku kwa jinsi sauti yake ilivyosikika tu, alionekana kuwa na majonzi tele.
 
SEHEMU YA 68

Theo hakuwa na jinsi, moyo wake ulijisikia huzuni nzito lakini alitakiwa kukubaliana na kile alichoambiwa na mpenzi wake kwamba alifiwa na hivyo kwenda msibani kwa lengo la kuungana na familia yake.

Alisubiri huku akiwa na hamu tele ya kumuona Iyanya kwa mara nyingine tena. Wakati mwingine alitamani kuona kila kitu kilichotokea kilikuwa ndoto ambapo baada ya muda fulani angeshtuka na kujikuta akiwa nchini Tanzania, kitandani pamoja na msichana huyo mrembo.

Uzuri wa Violeth ulipotea kabisa machoni mwake, hakumpenda, alimzoea, alimuona kuwa mwanamke wa kawaida sana.

Alimthamini lakini hakutaka kufanya naye kitu chochote kile, na tena katika kipindi hicho ambacho mtoto wao alikuwa akiumwa, alimshukuru Mungu kwa kuwa kusingekuwa na uwezekano wa kuonana naye kimwili tena mpaka pale ambapo mtoto huyo angepona kabisa.

*** “Upo wapi?” lilikuwa swali la kwanza kwa msichana Iyanya, aliulizwa na mwanaume mmoja, bilionea mkubwa nchini Afrika Kusini.
“Tanzania!”

“Unafanya nini huko? Nimekutafuta sana, simu zako haupatikani mpaka WhatsApp. Ninataka kuonana nawe, unakumbuka kwamba kesho ni siku yake ya kuzaliwa?” aliuliza mwanaume huyo.

Iyanya alishtuka, hakuamini alichokisikia, alikuwa na mambo mengi ya kufanya kiasi kwamba hakukumbuka hilo.

Alinyamaza kwa muda, ni kama alipigwa na bumbuwazi kusikia mwanaume huyo alimwambia hivyo, alifikiria kwa sekunde kadhaa, akaligundua hilo.

“Mungu wangu! Nilisahau kabisa,” alisema Iyanya.
“Njoo Afrika Kusini haraka, nina zawadi yako kabambe,” alisema mwanaume huyo.
“Zawadi gani?”

“Wewe njoo utaikuta huku,” alisema mwanaume huyo na kukata simu.
Iyanya alitulia na kufikiria alichokuwa akiambiwa. Mwanaume ambaye alimpigia simu aliitwa Dickson Makusa, alikuwa miongoni mwa wanaume waliokuwa na pesa nchini humo.

Makusa alimpenda sana Iyanya, katika maisha yake alifanya mapenzi na wanawake wengi warembo, aliwapenda, aliwapa pesa lakini mwenye alikiri kwamba hakukuwa na msichana ambaye alimpenda kwa moyo wote kama Iyanya.
 
SEHEMU YA 69

Alijitahidi sana kumtafuta na kumuingiza mikononi mwake. Alitumia pesa, alishindwa, alitumia akili zake, alishindwa, alitumia kila kitu lakini hakufanikiwa kumpata msichana huyo mrembo.

Kila alipomuona, moyo wake ulitikisika, penzi lake lilimkimbiza kupita kawaida. Hakukata tamaa, aliendelea kumtafuta kila siku, alimsumbua kwenye simu na kumualika kwenye vyakula vya wakati tofauti lakini msichana huyo aliendelea kuweka msisitizo wake kwamba hakutaka kuwa na mwanaume huyo.

Alichokifanya ni kumnunulia zawadi nyingi-nyingi, bado Iyanya hakuingia kwenye mtego wake, alifanya mambo mengi lakini hakupata hata busu kitu kilichomuuma mno.

Baada ya kumtafuta kwa miezi zaidi ya saba ndipo alipoamua kwenda kupima afya yake katika siku maalumu ya Ukimwi Duniani. Alipokwenda na kuchukua vipimo vyake katika Hospitali ya Nelson Mandela, hakuamini alichokikuta, aliathirika kwa ugonjwa huo hatari.

Alinyong’onyea mno, hakuamini kama kweli yeye ndiye aliyeambukizwa ugonjwa huo hatari.

Kichwa chake kikawa na hasira kali, aliamini kabisa aliupata kutoka kwa msichana mmoja, hakumtambua ila aliamini msichana huyo alijua kabisa kwamba aliathirika ila alikwenda kufanya naye mapenzi makusudi na kumuambukiza.

Akawachukia wanawake, kwa kuwa aliupata kutoka kwao, naye akaahidi kuusambaza kwa wasichana mbalimbali mpaka pale ambapo angefariki dunia.

Hakutaka kumuacha Iyanya, bado aliendelea kumtafuta, kupitia msichana huyo aliamini kabisa angekwenda kuwamaliza watu wengi na ndiyo maana aliamua kwa moyo mmoja kutumia kila kitu ili kumpata.

Wakati akimpigia simu msichana huyo, aliamini angekwenda nchini Afrika Kusini na kuonana naye, hivyo alimnunulia gari kali aina ya Benz ambayo aliiagiza kutoka nchini Ujerumani.

Msichana huyo aliposikia kwamba anaitwa huko, haraka sana baada ya kutumiwa pesa na Theo, akaondoka na kuelekea huko. Alipofika, akapokelewa kwa mbwembwe uwanja wa ndege na kupelekwa hotelini.
 
SEHEMU YA 70

Marafiki zake wote waliambiwa kuhusu sherehe ambayo iliandaliwa. Alipokutana na Makusa, wakakumbatiana, mwanaume huyo akataka kumpiga romance, msichana huyo akakwepesha.

“Nimekumiss sana,” alisema Makusa huku akimwangalia Iyanya.
“Nashukuru sana!” aliitikia.

Makusa hakuwa na wasiwasi hata kidogo, aliamini kabisa kwamba mwisho wa siku msichana huyo angekubali kufanya naye mapenzi na kumuambukiza Ukimwi kama alivyofanya kwa wengine.

Siku hiyo usiku akafuatwa na gari na kupelekwa katika ukumbi wa sherehe. Alipofika huko, moyo wake ukashtuka, marafiki zake wengi walikuwepo, walifurahi kumuona na hatimaye kuanza kutambulishwa mmoja baada ya mwingine.

Moyoni mwake alikuwa na furaha sana, kitendo alichokifanya Makusa kilikuwa kikubwa sana, hakutakiwa kunyimwa tena mapenzi, alitakiwa kupewa kiuhakika kwa sababu alijitoa sana kwa sababu yake.

Hilo ndilo lilikuwa kosa, tena alipoliona gari alilonunuliwa kama zawadi, akalainika na hatimaye usiku huyo kulala na Makusa ambaye alifanya naye kwa sana kuhakikisha msichana huyo anaondoka na virusi vya Ukimwi ili naye aende akawamalize wanaume wengine waliokuwa na tamaa ya kutembea na wanawake wazuri kama alivyokuwa yeye.
“Hapa nimemuweza, sasa naye aende akawaambukize wengine.

Huu ugonjwa siwezi kufa peke yangu,” alisema Makusa huku akionekana kuwa na furaha tele, alikamilisha kwa huyo Iyanya, sasa akaendelea na safari yake ya kuwatafuta wanawake wengine waliokuwa na tamaa ya pesa na magari mazuri.
|
|
|

Je, nini kitaendelea?
 
Habari zenu humu ndani , naombeni mniombee

Na mitihani mizito sana mbele

Mtihan wa darasa la saba kaka amenambia ni mgumu sana

Maombi yenu ndugu zangu

Sent using Jamii Forums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom