SEHEMU YA 55
Moyo wa Violeth ulipoa kabisa, hakumfikiria vibaya mume wake, kila kitu kilichokuwa kimetokea kilionekana kama video, hakufikiria kusalitiwa tena, kwake, mume wake alionekana kuwa mwaminifu kuliko mtu yeyote yule.
Hakufahamu kuhusu tatizo la moyo alilokuwanalo mtoto wake, Rachel, daktari na Theo walikubaliana wamfiche juu ya suala hilo kwani waliamini kwamba angepata matatizo zaidi kama tu wangemwambia kwamba hata yule mtoto aliyekuwa amenusurika alikuwa na tatizo hilo.
Ilipofika majira ya saa tano usiku, huku akiwa macho akimsubiri mume wake aliyekuwa na mwanamke mwingine, akashtuka kuona mtoto wake akianza kulia kwa sauti.
Alishangaa, kwa jinsi alivyokuwa akilia siku hiyo ilionekana kuwa tofauti na siku nyingine, alisikika akilia kwa maumivu makali, alishtuka hivyo kumuinua na kuanza kumwangalia huku akimbembeleza.
Upumuaji wake ulikuwa tofauti, ulifanana na mtu ambaye alikuwa akikaribia kukata roho. Alichanganyikiwa, kijasho chembamba kikaanza kumtoka, alihisi akitetemeka kana kwamba yeye ndiye alikuwa akiumwa.
Haraka sana akachukua simu yake na kumpigia mume wake ili ampe taarifa juu ya kile kilichokuwa kikiendelea, simu yake haikuwa ikipatikana kitu kilichomfanya kuwa na hofu kubwa.
Alikuwa chumbani, haraka sana akatoka huku akiwa amembeba na kuelekea nje, kulikuwa na gari lakini kwa jinsi alivyochanganywa na hali ya mtoto wake, akaona kama gari lingemchelewesha hivyo kutoka nje na kuanza kukimbia huku akielekea hospitalini.
Ilikuwa ni rahisi kusema mwanamke huyo alichanganyikiwa, alikimbia pasipo kuangalia nyuma, alikuwa na nguo ya kulalia tu lakini hakutaka kujifunga hata khanga, kwake, kuyaokoa maisha yake kilikuwa kitu muhimu kuliko hata kujisitiri.
Alikuwa akikimbia huku akilia, hakutaka kuangalia umaarufu wake, angeonekanaje, kwake, kuokoa maisha ya mtoto wake kilikuwa kitu cha kwanza kabisa.