Miliki bunifu, changamoto kwa wanateknolojia tanzania

kafukugm

Member
Oct 10, 2009
11
6
Kwanza napenda kutoa shukrani zangu nyingi kwa juhudi zilizofanywa na Tume ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) pamoja na Wakala wa Usajili biashara na Utoaji leseni (BRELA) kwa kushirikiana na Shirika la Miliki Bunifu duniani (WIPO) kwa kuanzisha Kituo cha Utoaji Huduma za Ushauri na Taarifa za Miliki Bunifu (TIPASIC) kilichopo pale COSTECH.

Ni dhahiri kwamba nchi nyingi sasa zinapiga hatua kubwa za kimaendeleo na uchumi kwa kutumia mfumo mzima na mwongozo wa miliki bunifu (Intellectual Property). Miliki bunifu hupenyeza katika nyanja zote za shughuli za mtanzania ikizingatiwa kwamba Tanzani ni nchi itegemeayo tecknolojia kwa kiasi kikubwa kutoka nje.
Lakini ni mpaka lini Tanzania itakuwa tegemezi kwa karibu kila teknolojia na nyingine zikiwa ni rahisi kiasi cha kuweza kuigwa na kutengenezwa hapa hapa Tanzania? Hivi ndivyo wenzetu wa nchi zinazopiga hatua kwa kasi zilivyojiuliza na kugundua kwamba njia moja tu ya kujitegemea ni kujifunza wengine (yaani nchi nyingine kubwa) wafanyavyo kuendeleza teknolojia na uchumi. Mfumo pekee ambao huwezesha taifa moja au watu wa nchi fulani kujifunza au kuiga na kuboresha teknolojia na kuuza kwa maendeleo ya kiuchumi na teknolojia ni kutumia miliki bunifu kupitia mfumo wa Hataza (Patent System). Kwa kutolea mfano wenzetu wa Korea, Japan, Malaysia, Brazil, China, India n.k. hutumia sana mfumo wa hataza kwa maendeleo ya kiteknolojia na hatimaye uchumi.

Hii ni changamoto kubwa kwa wanasayansi na watafiti wa Tanzania. Ni wakati wa kubadilika na kuanza kujifunza teknolojia za nchi nyingine na hatimaye kuziboresha na kuzitengeneza hapa hapa nchini kwetu kwa kupitia mfumo huu wa Hataza. Kwani husemekana kwamba asilimia 80 ya taarifa za kiufundi hupatikana kwenye nyaraka za hataza tu (Patent documents).

Tanzania ni nchi iliyojaliwa kuwa na rasilimali nyingi sana ambazo huweza kutumika kama malighafi katika uzalishaji wa bidhaa mbalimbali. Pia nguvu kazi Tanzania ni ya kutosha kabisa na ni ya gharama nafuu.

Hivyo basi ni jukumu la yeyote mwenye kipaji cha ugunduzi/ubunifu au mtafiti kunufaika na matokeo ya kazi ya akili yake. Ni lazima tuzungumze kibiashara zaidi kuliko kitaaluma zaidi kama ionekanavyo sasa.

Hata wajasiriamali wetu wasipotambua umuhimu wa miliki bunifu katika kusajili na kuzitangaza biashara zao kupitia mfumo wa alama za biashara (Trade and Service Marks) itakuwa ni kupoteza mikopo na kuwalaumu kwa malipo ya shida.

Hivyo basi ninawahasa watanzania wenzangu kukitumia ipasavyo hiki kituo cha miliki bunifu (TIPASIC), ambapo huduma kwa sasa ni bure, kilochopo hapo tume ya sayansi, kijitonyama kwa kutatua matatizo yetu ya kisayansi, kiutafiti na teknolojia na kwa kuweka wazi ubunifu wetu na hatimaye kuwa na teknolojia zetu wenyewe.

Gerald Kafuku.
0784 493230
 
Back
Top Bottom