SEHEMU YA 123
Kwa kipindi kirefu kundi hilo la kigaidi likatamani kulipua Marekani. Walikumbuka jinsi walivyotumia ndege mwaka 2001, hawakutaka kuridhika hivyo kutamani kulipua tena kwani waliamini kwamba wanaonewa, walitaka kuyaondoa majeshi ya Marekani na Uingereza nchi mwao, kitu pekee kuonyesha kwamba walichukizwa na uwepo wao huko kilikuwa ni kuwalipua tu.
Hawakujua ni kwa jinsi gani wangeweza kuingia nchini Marekani. Waliwatumia watu wengi kwenda huko lakini ilishindikana, hata kabla hawajaingia nchini Marekani, walikamatwa na hivyo kufungwa katika gereza la Guantanamo.
Walijiuliza ni sababu zipi ziliwafanya kukamatwa kirahisi namna hiyo na jibu pekee walilolipata ni kwa sababu waliwatumia Waarabu wenzao.
Ili kuingiza bomu nchini Marekani ilitakiwa kumtumia Mzungu au mtu mweusi, hawakujua wangewapata vipi, kwa Wazungu ilikuwa vigumu sana lakini kwa watu weusi halikuonekana kuwa jambo gumu hata kidogo.
Wakakutana nchini Uturuki, nchi pekee barani Ulaya ambayo walikuwa wakikaa kwa usalama kwa kuwa watu wa nchi hiyo walikuwa Waarabu wenzao.
Hapo ndipo walipopanga mipango, wakawafuata watu weusi waliotaka kuingia Marekani, waliwaambia kwamba walikuwa tayari kuwasaidia lakini walipowaambia kuhusu mabomu, waliogopa.
Walipoteza watu wengi, wakaweka vikao na kuona kwamba hawakutaka kuwaambia lengo la kuingia nchini Marekani bali walitakiwa kubaki kimya, wawape mizgo ya mabomu pasipo wao wenyewe kujua.
Kitendo cha Fareed kupatikana kiliwapa uhakika kwamba mwanaume huyo angefanikiwa kuingiza mabomu nchini humo, mawasiliano yakafanyika na hivyo taarifa kupelekwa kwamba tayari kijana mmoja alikuwa amepatikana, kijana aliyekuwa na hamu ya kuingia nchini Marekani.
“Hata mimi ninao wawili huku,” alisikika kijana aliyeitwa Mohammed Mustapha, mwanaume aliyekuwa akipanga safari za kwenda nchi mbalimbali kulipua.
“Safi sana. Basi nitaomba uje kumchukua na huyu,” alisema Mzee Al Fakh.
“Haina shida.”
Fareed hakuwa na hofu, moyo wake ulifurahi mno kwa kuona kwamba hiyo ndiyo ilikuwa nafasi yake ya kuelekea nchini Marekani. Hakuhisi kama watu hao walikuwa wabaya waliotaka kumbebesha mabomu mpaka nchini MArekani.