Barca itaiweza Shakhtar leo?
Send to a friend Tuesday, 05 April 2011 20:02 0diggsdigg
BARCELONA, Hispania
WAKATI timu ya Barcelona imejiweka katika nafasi nzuri ya kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Hispania kwa mara ya tatu mfululizo, leo itakuwa na kibarua kikali wakati itakapoingia uwanjani kwa ajili ya kupambana na Shakhtar Donetsk katika mechi ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Barani Ulaya.
Kocha wa Barcelona, Pep Guardiola ameiwezsha timu hiyo kufanya vizuri tangu aanze kuifundisha timu hiyo mwaka 2008 na hivi sasa Barca ipo kwenye mwisho wa msimu ikitaka kutwaa makombe matatu.
Guardiola alichukua kazi ya kukinoa kikosi cha Barca baada ya aliyekuwa kocha wa timu hiyo Frank Rijkaard kushindwa kuipa mafanikio timu hiyo na kusimamia nidhamu ya wachezaji wa timu hiyo kuanzia kwenye vyumba vya kubadilishia nguo, pia Guardiola aliikuta timu ipo katika hatua ya kufuzu kushiriki Ligi ya Mabingwa Barani Ulaya.
Katika msimu wake wa kwanza, kocha Guardiola aliiwezesha Barca kutwaa mataji sita na mwaka jana waliweza kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Hispania na Kombe la Copa del Rey, lakini hawakuweza kutwaa ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya baada ya kutolewa na Inter Milan iliyokuwa ikifundishwa na na kocha Real Madrid hivi sasa Jose Mourinho.
Katika mechi ya ligi kuu ya Hispania waliyocheza Barca dhidi ya Villarreal na Barca kushinda bao 1-0, wachezaji wao Carles Puyol, Eric Abidal, Maxwell Pedro Rodriguez kwa sababu ya kuwa majeruhi, Xavi Hernandez pia hakucheza na Leo Messi alianza mechi hiyo akiwa benchi.
Pedro anatarajiwa atakuwepo katika mechi ya leo dhidi ya Shakhtar Donetsk, pia Messi na Maxwell wanatarajiwa kuwepo, lakini Puyol anaweza asiwepo hivyo ukuta wa Barcelona unatarajiwa kusimamiwa na Sergio Busquets na Gerard Pique.
Barca ambayo inatarajiwa kucheza pia mechi ya fainali ya Copa del Rey mwishoni mwa mwezi huu, mshambuliaji wake mahiri David Villa alidai kuwa wiki chache zijazo ni muhimu kwa mafanikio ya klabu hiyo.
"Hatua tuliyofikia sitakubali tutwae makombe mawili kati makombe matatu tunayowania, tunazo mechi ngumu mbele yetu, tunatakiwa tuifunge Shaktar Donetsk katika mechi ya kwanza tunayocheza nao katika uwanja wetu wa nyumbani ili tusiangaike tutakaporudiana nao,"alisema David Villa.
Barca inatarajia kuifunga Shaktar Donetsk kwa mara ya tisa katika Ligi ya Mabingwa Barani Ulaya na hii ikiwa ni mara ya kwanza kwa Shaktar Donetsk kucheza hatua ya robo fainali ya mashindano hayo.
Mwaka 2009, Barca iliifunga Shaktar Donetsk katika mashindano ya Uefa Super Cup, lakini mara ya mwisho zilipokutana Shaktar Donetsk na Barcelona, timu ya Shaktar Donetsk ilishinda kwa mabao 3-2.