Simba yaipa ahueni Yanga
na Dina Ismail
MABINGWA wa soka Tanzania Bara, Simba ya jijini Dar es Salaam jana ilishindwa kujiweka kwenye mazingira mazuri zaidi ya kutetea taji lake baada kuvutwa shati na Kagera Sugar na kulazimishwa sare ya bila kufungana kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.
Mchezo huo uliochezeshwa na mwamuzi Peter Mjaya wa Pwani, ulianza kwa mashambulizi ya kupokezana, ambapo dakika ya 9, Emmanuel Okwi alikosa bao baada ya shuti lake kutoka nje kidogo ya lango la Kagera Sugar.
Dakika ya 10, Wakata miwa hao wa Kagera, walijibu mapigo baada ya Steven Mazanda kupiga shuti lililogonga mwamba, kabla ya Mussa Hassan Mgosi naye shuti lake kutoka nje ya lango dakika ya 21.
Kinara wa mabao hadi hivi sasa katika ligi hiyo, Gaudance Mwaikimba shuti lake la dakika ya 24 lilitoka nje ya lango la Simba, huku kiungo Mkenya Jerry Santo naye akikosa bao baada ya kupiga shuti hafifu dakika ya 33 lililodakwa na kipa Hannington Santi alipiga shuti hafifu likaokolewa na kipa Hannington Kalwaesubula.
Mwamuzi Mjaya, alitoa kadi za njano kwa Luhende kwa kumchezea vibaya Nyoso na Themi Felix kumzonga mwamuzi na kipa Hannington kwa kupoteza muda wote wa Kagera Sugar. Hadi dakika 45 za kwanza zinamalizika hakuna timu iliyocheka na nyavu za mwenzake.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku kila timu ikifanya mashambulizi ya kupokezana, ila Simba itabidi wajilaumu zaidi, kwa wachezaji wake kukosa mabao ya wazi, wakiwamo Mgosi, Shiboli, Okwi na Santo.
Dakika ya 75, Kipa Hannington alilimwa kadi nyekundu kwa kupoteza muda dakika ya 75, hivyo kuwalazimu Kagera Sugar kumtoa mshambuliaji wake Themi Felix na kuingia kipa Msafiri Daffo kabla ya Mwaikimba kukosa penalti iliyookolewa na kipa Juma Kaseja. Hadi filimbi ya mwisho timu hizo zilitoshana nguvu kwa sare ya bila kufungana.
Kwa matokeo hayo Simba imefikisha pointi 45 huku ikiwa imebakiza mechi mbili mkononi dhidi ya Majimaji ya Songea na JKT Ruvu ya Pwani, huku wanaowanyemelea kwa karibu, Yanga wakiwa na pointi 40 ambao leo wanashuka dimbani kuvaana na Azam FC yenye pointi 37.
Simba: Juma Kaseja, Haruna Shamte, Juma Jabu ‘JJ', Juma Nyoso, Kelvin Yondan, Jerry Santo, Rashid Gumbo/ Ahmed Ali Shiboli, Patrick Ochan, Mussa Hassan Mgosi, Emmanuel Okwi na Mohammed Banka.
Kagera Sugar: Kalwaesubula Hannington, David Luhende, Said Morad, Tonny Ndollo, George Kavilla, Jumanne Hamis, Sunday Frank, Gaudance Mwaikimba, Steven Mazanda na Themi Felix/Msafiri Daffo.