Mbowe: Nchi imekwama, Kikwete kaelemewa

NGOWILE

JF-Expert Member
Sep 8, 2011
454
258
Nchi imekwama; tayari Kikwete amelemewa (1)
na
Freeman Aikaeli Mbowe
Mwenyekiti Taifa
KAMA ilivyo kawaida, ukiandika ukatoa hoja, tarajia maswali, pongezi na hata kejeli kutoka kwa wasomaji. Majibu yatategemea aliyeguswa kaguswa vipi.

Leo, nitajikita kwenye swali moja ambalo nimeulizwa.
Waungwana wamesema: "Mbowe tumekusikia na kukusoma hoja zako kuhusu mustakabali wa nchi yetu; sasa tufanye nini?
Nashukuru kwa changamoto hii. Kama Mtanzania na zaidi kama kiongozi, nina wajibu wa kuweka fikra zangu wazi. Wenye hekima na busara wazitafakari. Wenye husuda wabeze!

Mawazo yangu si msaafu. Ni fikra mbadala ambazo zinakusudia kujenga hoja mjadala.
Ninaamini wako Watanzania wengi wenye uwezo mkubwa sana wa uongozi. Lakini mfumo wetu hauwapi fursa.
Sasa si siri, nchi yetu imekwama. Ni dhahiri Rais Jakaya Kikwete amelemewa. Yeye hataki au pengine hana ujasiri wa kukiri kuwa chama anachokiongoza hakina jibu la umaskini wa Watanzania.

Taifa lolote lililokwama linahitaji mabadiliko. Mabadiliko hayo huweza kuja kwa njia mbili. Ama kwa mtindo wa kutumia nguvu, yaani mapinduzi (revolution), au kwa mtindo wa amani, yaani mageuzi (reforms).

Ni dhahiri kuwa Watanzania wanapendelea mabadiliko kwa njia ya amani, yaani ‘reforms'. Tangu tumepata uhuru, Tanzania imefanyiwa ‘majaribio' mengi sana ya kisiasa, kijamii na hata ya kiuchumi, lakini ‘majaribio' haya hayakutukwamua. Bado tumekwama.
Yako maeneo machache tuliyopiga hatua kama taifa. Lakini mafanikio machache tuliyopata hayalingani na utajiri wa asili wa nchi yetu. Aidha, hayalingani kabisa na umri wa miaka 46 ya uhuru wetu.

Ni kweli subira huvuta heri, lakini subira inapoendelea kutumbukiza taifa kwenye lindi la umaskini, subira hii hukaribisha shari!
Ni rahisi kufikiria kuwa kukwama kwetu leo ni tunda la ufisadi wa viongozi. Ni kweli hili linachangia. Tukumbushane historia kidogo.
Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliongoza taifa hili kwa miaka 25.

Alikuwa kiongozi aliyependwa sana na watu. Hakuwa fisadi na wala serikali ya awamu yake haikuwa ya kifisadi. Pamoja na uadilifu wa Mwalimu, bado nchi hii, ilikwama sana kiuchumi na hivyo kimaendeleo!


Kama taifa, tuna wajibu wa kutafakari tumekwama wapi? Ni dhahiri kuwa kutokomeza ufisadi pekee si suluhisho pekee la kuipeleka nchi yetu kwenye neema. Na wakati mwingine nimekuwa nikihoji: ‘Je, inawezekana amani yetu tunayojivunia ndiyo sababu ya kukwama kwetu?'

Sihitaji kujadili utajiri wa Tanzania. Wote tunaujua.
Katika kujadili kukwama kwetu na kupendekeza suluhisho, wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu, nilizungumza kwa nguvu kubwa mambo kadhaa.

Leo nitaanza kujadili machache ya msingi kama changamoto kwa Watanzania. Nilijenga hoja:
1.Kwamba mfumo wetu wa utawala ndiyo chimbuko la umaskini na kukwama kwetu.
2.Kwamba hata ukimleta ‘malaika' ukamweka Ikulu awe Rais wa Tanzania, kwa mfumo wetu wa utawala uliopo, lazima atakwama!
3.Kwamba utajiri wetu wa asili ndio utatumika kama chanzo cha kubomoa mshikamano wa taifa.
4.Kwamba, kwa matendo ya watawala wetu, ni wazi kwamba wamemsahau Mungu!
5.Kwamba amani yetu ni tete!

Sera iliyosikika sana wakati wa uchaguzi ni ile ijulikanayo kama sera ya majimbo. Sera hii ilikusudia (na inakusudia) kujibu hoja na hofu yetu kuwa mfumo wetu wa utawala ndio msingi wa kukwama kwetu.

Mada hii ni ndefu. Nakusudia kuijadili kwa kina na kwa mapana yake katika mfululizo wa makala kadhaa.
Niliamini niliyozungumza wakati ule. Bado nayaamini. Hatimaye, nitayaandikia kitabu, ili dira yangu ibaki kama kumbukumbu kwa vizazi vijavyo.

Kama ilivyotarajiwa kwenye ushindani wa kisiasa, wapinzani wangu wakiongozwa na mgombea wa CCM, Jakaya Kikwete, walipotosha kisha wakabeza hoja zangu, tena kwa kejeli kubwa!

Kikwete aliponda asichokielewa. Alichokuwa anawaeleza wananchi si sera ya majimbo bali ni uzushi wa CCM. Natumaini naye sasa atasoma na aelewe. Kama ninavyosema siku zote, jamaa hawa kwa propaganda ni hatari!

Katika demokrasia ya mfumo wa vyama vingi, chama cha siasa kina wajibu wa kutoa dira ya nchi. Chama kinakuwa chimbuko la fikra. Fikra hizo zinatekelezwa na serikali. Chama kinaweka misingi ya kiitikadi, serikali inatengeneza sera na kuzitekeleza.

Mageuzi yanayolikwamua taifa lolote huanzia kwenye mageuzi ya kifikra. Mageuzi ya kifikra hupatikana tu pale walio kwenye madaraka wanapotambua kwamba uongozi wa nchi ni dhamana na si miliki yao.

Ni pale tu wanapokubali ukweli kuwa rais na hata viongozi wengine wa juu peke yao hawawezi kuliletea taifa neema.
Ni pale tu watakapoheshimu kuweka mifumo mizuri itakayotoa fursa kwa wote wenye uwezo wa uongozi kupata nafasi hizo kwa misingi ya chaguzi zilizo huru na za haki.

Kikwete na timu yake waliingia madarakani bila fikra wala dira. Ndiyo sababu alikiri kuwa wale wanaotegemea mabadiliko wasahau, kwani anataka kufuata yale ya waliomtangulia kwa ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya! Waingereza wanasema ‘business as usual!' Yaani, mambo yaleyale!

Kasi mpya, nguvu mpya na ari mpya, si dira! Si itikadi! Si sera! Ni kaulimbiu. Ni vibwagizo vya uchaguzi! Ni mbwembwe! Ni sanaa.
Watu waliopewa au kujinyakulia dhamana dhidi ya watu wao wanapokosa fikra na dira zao wanazoziamini, huwa watawala, na hivyo kusababisha utupu (vacuum) wa dira.

Wanapokuwa na fikra zao wanazoziamini huwa na dira, nao huwa viongozi. Huongoza watu wao kuelekea kule wanakokuamini, hata kama ni kubaya.

Panapotokea utupu (vacuum) wa fikra za wenye dhamana, fikra za nje huziba utupu huo. Katika mazingira haya wanajitokeza wengi kujaza utupu huu kwa kuwa madalali wa watawala. Wanageuza Ikulu kuwa gulio. Hili ndilo linaloisibu nchi yetu. Tangu Baba wa Taifa aondoke madarakani, nchi imekosa fikra na dira. Viongozi wameacha kufikiri au hawana uwezo wa kufikiri?

Utupu huu wa kukosa fikra mbadala za ndani, unawafanya viongozi wetu kila kukicha kutimkia nje ya nchi kusaka mawazo na fikra mpya. Ni dhahiri watu wa nje wakijaza utupu wetu, watajifaidisha kwanza wao! Tahadhari! Katika historia ya dunia, hakuna taifa lililoendelezwa na fikra za taifa jingine. Kila taifa huvutia kwake kwa kuchuma kwa wengine.

Fikra zitakazokomboa taifa hili lazima zitoke huku huku. Watu wapo! Vichwa vipo! Vimebanwa na mfumo.
Nieleweke hapa! Sikatai wawekezaji. Ila sikubali kuwa ufumbuzi wa matatizo yetu ya umaskini utaletwa na wawekezaji na wafadhili wa nje. Sasa narejea kwenye hoja!

Chimbuko la fikra ya hoja ya sera ya majimbo
Naam! Baada ya kutafiti kwa kina, kwa upande mmoja nilibaini kuwa ukubwa wa nchi yetu na utajiri wake wa asili vimelemaza taifa letu. Kwa upande wa pili, nilibaini na hivyo kuamini kuwa mfumo wetu wa utawala umeshindwa kutumia rasilimali watu na maliasili yetu kwa maendeleo ya taifa.

Kwanza, nilishangazwa na idadi ya Watanzania wasiojua ukubwa wa kijiografia wa nchi yao. Ni idadi ndogo sana ya Watanzania wanaojua kuwa nchi yetu yenye ukubwa wa kilometa za mraba laki tisa na arobaini na tano elfu (945,000 km2) ni zaidi ya ukubwa wa nchi za Kenya, Uganda, Burundi, Rwanda, Lesotho na Swaziland zikichanganywa!

Tanzania kwa idadi ya watu (milioni 38) ni nchi ya 38 kati ya nchi 195 za dunia. Katika Afrika, Tanzania ni ya saba ikizidiwa na Nigeria (milioni 132), Misri (milioni 79), Ethiopia (milioni 75), Kongo (milioni 63), Afrika Kusini (milioni 44) na Sudan (milioni 41).
Ni dhahiri basi kuwa Tanzania ni nchi kubwa ya kutisha, huku ikiwa yenye rasilimali za kupindukia.

Ukubwa na utajiri huu kama hautawekewa mkakati, unaweza kuwa kikwazo kikubwa ambacho watawala wetu hawajaweza kukiona.
Aidha, kama hautadhibitiwa mapema, unaweza kuwa chanzo cha migongano ya ndani kwa ndani, kwani kuna utupu wa kutisha. Tanzania haiwezi kuendelea kutegemea kila kitu kutoka Dar es Salaam!

Chini ya utawala wa Mwalimu Nyerere, chini ya mfumo wa utawala wa kijamaa, nchi yetu ilitawaliwa kutoka kati, yaani kutoka makao makuu ya serikali. Serikali ilisimamia na kumiliki njia zote kuu za uchumi (command economy), ambazo ni pamoja na ardhi, maliasili zote, biashara, viwanda, mabenki, majengo n.k.

Hata mfumo wetu wa kiutawala ulipata maagizo kutoka Dar es Salaam na hivyo kufanya makao makuu ya nchi na kiongozi mkuu kuwa na mzigo mkubwa sana wa kusimamia rasilimali za asili za taifa. Ujamaa ulikwama. CCM, tangu enzi za Mzee Ali Hassan Mwinyi, ikautelekeza kisirisiri. Jambo la ajabu! Itikadi kuu ya nchi inatelekezwa kisirisiri bila wananchi kujua. Hii ndiyo fedheha ya watawala wasio viongozi.

Kwa upande wa siasa, nchi nayo ikaingizwa kichwa kichwa kwenye mfumo wa vyama vingi. Balaa likaanzia hapa!

Tangu wakati huo, mserereko wa uchumi wetu umekuwa wa soko (market economy). Ujamaa umebakia kuwa usanii wa kuombea kura kwa wananchi.

Sera za ubinafsishaji sasa zikaanza na baadaye kushamiri chini ya utawala wa Awamu ya Tatu ya Rais Benjamin William Mkapa. Nchi yetu nayo haikusalimika na mabadiliko ya mifumo ya kiuchumi na kisiasa ya dunia. Hii ilitokana na kufa kwa vita baridi kati ya mataifa ya mashariki ya kijamaa na yale ya Magharibi ya kibepari.

Nchi yetu hapa iliingia kwenye mfumo wa uchumi wa soko kwa kushinikizwa bila maandalizi ya kutosha yaliyosababishwa na kukosekana kwa fikra za ndani. Rasilimali za taifa ghafla zikawa kama hazina mwenyewe. Viongozi wetu wakaanza kuzigawa kwa wageni bila kuweka mkakati wa ndani wa kuwezesha wazawa. Kupitia ubinafsishaji na sera za uwekezaji, viongozi wetu nao wakaanza ‘kujikatia' mapande yao. Familia zao, wapambe wao nao hawakucheza mbali. Wawekezaji wa sampuli mbalimbali nao wakaingia ulingoni.

Kama nilivyokwisha kusema, nchi sasa ikageuzwa shamba la babu, ambapo kila mwenye kapu huvuna, na babu hana nguvu ya kuzuia. Uongozi wa nchi sasa ukawa biashara. Ufisadi wa kutisha ukazaliwa rasmi. Kazi ya kugawa rasilimali ya taifa ikaendelea kufanyikia Dar es Salaam. Bunge likageuzwa kituko. Likawa idara ya CCM, na likatumika kupitisha maagizo ya wakubwa, si matakwa ya wananchi.

Mali za nchi zikawa zinagawanywa na kikundi kidogo cha watu chini ya Rais, huku kikidhani kina akili kuliko Watanzania wote.
Watanzania tukaendelea kupewa matumaini ya neema. Kila kukicha zinatolewa takwimu tamu tamu za kuonyesha uchumi unakua. Ni kweli, pato la taifa lilikua! Lakini cha kujiuliza, lilikua kwa faida ya nani ilhali wananchi waliendelea na wanaendelea kuwa maskini?
Sasa, hebu tuchambue bila woga ufisadi uliofanyika chini ya utawala wa Awamu ya Tatu, na ambao Rais Kikwete ameahidi kuuenzi na kuulinda! Mwanzo wa kuelemewa kwake.


Nchi imekwama; tayari Kikwete amelemewa (2)

Na Freeman Aikaeli Mbowe
Mwenyekiti Taifa


WIKI iliyopita, nilianza kujadili hoja mpya iliyobeba kichwa cha habari kisemacho: "Nchi imekwama, tayari Kikwete amelemewa!"
Nilimalizia makala ile kwa kusema: "Sasa, hebu tuchambue bila woga ufisadi uliofanyika chini ya utawala wa Awamu ya Tatu, na ambao Serikali ya Rais Kikwete imeahidi kuuenzi na kuulinda, ikiupachika jina la wema! Mwanzo wa kulemewa kwake!"
Tafakuri yangu kuhusu hoja hii, itajadiliwa kwa makala kadhaa. Hivyo basi, ufisadi wa utawala wa CCM wa awamu zote (na si wa Awamu ya Tatu tu) baada ya kuondoka Baba wa Taifa kwenye uongozi, utajadiliwa katika mtiririko wa makala zangu kama jibu la kwa nini nchi imekwama na ni vipi Kikwete amelemewa litajibiwa.

Ningependa kuweka msimamo! Sifurahii nchi yetu kukwama. Sifurahii rais wetu kuelemewa. Nasikitika sana na ninamwonea huruma sana rais. Amebeba mzigo mkubwa na macho ya Watanzania milioni 38 yanamtazama yeye tu. Pamoja na kuwa ni jukumu alilolitafuta kwa nguvu zote, kulemewa kwake kunaongezwa na kujikuta anakosa majibu mengi yatokanayo na majukumu kibao yanayomkabili. Ni matatizo ya kuwa na mfumo wa kumlimbikizia mtu mmoja ambaye ni rais na Serikali Kuu mamlaka ya kutisha.

Wengine tunaandika kwa sababu tunataka umma uelewe fikra zetu na uzihukumu au kuzitafakari kwa faida ya nchi yetu. Tunaandika ili watawala wetu waelewe watawaliwa wao tunawaza nini kuhusu muktadha wa nchi yetu! Wiki iliyopita, niliandika na hata siku zilizopita nimepata kusema kuwa, mfumo wetu wa utawala umeshindwa kuutumia ukubwa wa nchi sambamba na utajiri wake wa asili na badala yake umekuwa sababu kuu ya kukwama kwa nchi yetu. Serikali Kuu imejilimbikizia madaraka, sasa yanawalemea. Nchi ni kubwa mno, waziri mmoja na wizara yake hawezi kuongoza na kupata tija.

Mikoani na wilayani wanangojea fedha kutoka Serikali Kuu. Tumeua uwezo wa watu kufikiri na kujiendeleza. Lugha ni mfadhili na serikali ifanye hili na lile! Mfumo wetu wa utawala kwa muda mrefu umejenga mlolongo wa viongozi wasio na ridhaa ya wananchi ‘kuwatawala.' Wengi wa viongozi hawa wa kupachikwa, wamekuwa hawayaelewi maeneo yao ya kazi hadi siku wanapoteuliwa!
Wengi hutumia zaidi ya miaka miwili kujifunza utamaduni na mila za wanaowatawala! Wale wasio na uwezo wa kujifunza wanaendelea kuwa mzigo na kikwazo kwa wananchi wanaowatawala.

Hawa ni pamoja na wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya na makatibu tarafa. Wengi wao wanaishia kufanya kazi za uenezi wa chama chao kwani hana taaluma ya kumuongoza kufanya jingine! Utawala wa majimbo ungewataka waende kuomba ridhaa ya wananchi, hakuna dezo!

Hebu funga macho ufikirie na kutafakari: Mtu anateuliwa kuwa mkuu wa wilaya kuwaongoza watu zaidi ya laki nne. Kwa maana hii, anakuwa na mamlaka ya mwisho katika wilaya hiyo. Katika maisha yake yote, hajawahi kuishi au angalau kufika katika wilaya hiyo.
Mtu huyu katika maisha yake, hajawahi kuwa kiongozi katika ngazi yoyote. Pengine shuleni hakubahatika kuwa hata kiongozi wa darasa! Hana taaluma yoyote inayohusiana na utawala au uongozi wa watu. Anapikwa kwa ‘semina elekezi' kwenye Hoteli ya kitalii ya Ngurdoto kwa wiki moja!

Ghafla anasimamia vyombo vya ulinzi na usalama! Anastahili kuwa na majibu ya mikakati ya eneo asilolijua! Ana mamlaka na roho za watu zaidi ya laki nne katika wilaya!

Ana bahati huyu! Anajuana na rais au waziri mkuu! Alipiga vigelegele sana wakati wa kampeni! Kapata zawadi! Nayo ni tuzo ya utawala asioujua, ambao kwa upande wa pili ni kukwama kwa wananchi wa wilaya hiyo kwa muda wote ambao rais ataamua kumbakisha hapo. Huku ni kufanya mzaha na maisha ya watu!

Ukuu wa wilaya sasa ghafla kila mtu anaona anaustahili. Hakuna vigezo wala sifa. Ni mapenzi ya ‘wazee'. Ukielezwa kundi la wapambe waliokuwa kwenye ‘waiting list' baada ya Uchaguzi Mkuu utajua sasa uongozi si dhamana tena, bali ni vituko. Nakataa jambo lisilo na mipaka!

Wananchi wanahoji wabunge wao! Hawana uwezo wa kuwahoji wakuu wa wilaya. Wako pale kusimamia masilahi ya waliowateua na si wanaowatawala! Kwa mtaji huu tunategemea vipi miujiza ya maendeleo? Wananchi nao kwa upande wa pili, hawawajui watawala wao wala historia yao, hadi pengine siku ya mazishi yao kwenye historia ya marehemu! Mungu aepushe mbali! Siwatakii vifo ‘watawala wetu' ila najenga hoja ya namna ilivyo vigumu wananchi kuwajua watawala wao wa kupachikwa!

Nikiri jambo moja. Wako wakuu wa mikoa, wilaya na hata tarafa ambao wamekuwa na uwezo na dhamira ya kweli ya kuwatumikia wananchi katika eneo walilopangiwa. Wachache wamekuwa chachu ya maendeleo. Nawapongeza. Hata hivyo, hii haiondoi ukweli kuwa sasa muda umefika wa wananchi kutopachikiwa viongozi.

Hiki ni kionjo kimojawapo cha kusudio la sera ya majimbo, kwamba viongozi wetu wa kisiasa, wachaguliwe na wananchi na wawe na ridhaa ya kuwaongoza. Wale wa kuteuliwa na rais, wawe kwa mujibu wa taaluma na uadilifu wao. Aidha, pawepo mipaka ya mwingiliano katika utendaji wa chama cha siasa na serikali, kwani tumeridhia siasa ya mfumo wa vyama vingi, hivyo tuna wajibu wa kucheza kwa mujibu wa sheria zake.

Tafakari nyingine muhimu ni kusudio la mkakati wa kutumia kwa faida ukubwa na utajiri wa nchi yetu. Kwa hali ilivyo leo, mamlaka yote ya rasilimali za asili za taifa hili yanamilikiwa na Serikali Kuu ikitokea Dar es Salaam. Mayai yote tumeweka mikonnoni mwa kundi la watu wachache. Wanapokosa mwelekeo, Watanzania wote wanakwama. Tanzania leo ni Dar es Salaam. Ukichunguza takwimu utaona uchungu na kuwasikitikia Watanzania hasa wale waishio mikoani.

Makusanyo ya kodi za serikali, ni kigezo kizuri cha kupima uwezo wa watu wa kununua bidhaa na huduma katika eneo lolote.
Katika kujenga hoja yangu, nitatumia takwimu za msingi kuhusu Mkoa wa Dar es Salaam dhidi ya mikoa mingine hususan Kanda ya Ziwa, yaani Mwanza, Shinyanga, Mara na Kagera. Nitajenga hoja kuwa, rasilimali ziko mikoani, takwimu za makusanyo sanjali na fedha kiasi zilizokusanywa ziko Dar es Salaam ilhali maisha bora na fedha za uhakika zikiwa katika nchi za wawekezaji.
Hebu linganisha mapato ya Mamlaka ya Kodi Tanzania kwa miaka ya fedha 2004/2005 na mwaka 2005/2006 kwa mujibu wa taarifa za TRA.

Mwaka wa fedha 2004/05, TRA walikusanya shilingi trilioni moja, bilioni 679 na milioni nane.
Kati ya hizi, shilingi trilioni moja, bilioni 71, milioni 442 zilikusanywa katika Mkoa wa Dar es Salaam. Hii ni sawa na asilimia 82 ya mapato yote ya serikali yatokanayo na kodi. Mikoa mingine yote iliyobakia ilikusanya shilingi bilioni 299 milioni 802, ambazo ni sawa na asilimia 18 tu ya mapato ya serikali kupitia kodi.

Mkoa wa Mwanza ulikusanya shilingi bilioni 37, milioni 52 tu kwa mwaka, sawa na asilimia 2.2 ya makusanyo ya nchi nzima. Shinyanga ilikusanya bilioni 18, milioni 689, ambazo ni asilimia moja nukta moja (1.1%) ya mapato ya TRA kwa mwaka!Mkoa wa Kagera ulikusanya shilingi bilioni saba, milioni 252, sawa na asilimia sifuri nukta nne tatu (0.43%), na Mkoa wa Mara ulikusanya shilingi bilioni 34, milioni 548, sawa na asilimia 1.82 (1.82%) ya mapato ya TRA.

Kanda nzima ya Ziwa yenye wakazi zaidi ya milioni 10 ilikusanya kodi ya shilingi bilioni 93, milioni 683 sawa na asilimia tano nukta tano saba (5.57%) ya pato la taifa! Mwaka 2005/06, TRA walikusanya shilingi trilioni 2, bilioni 40, milioni 393. Mkoa wa Dar es Salaam pekee, ulikusanya shilingi trilioni moja, bilioni 697, milioni 321. Hii ni sawa na asilimia themanini na tatu (83%) ya mapato yote ya serikali yatokanayo na kodi.

Mikoa mingine yote iliyobakia ilikusanya shilingi bilioni 343, milioni 75, ambazo ni asilimia 17 tu ya mapato yote ya TRA kwa mwaka.
Mkoa wa Mwanza ulikusanya shilingi bilioni 40, milioni 696, sawa na asilimia moja nukta tisa (1.9%). Shinyanga ilikusanya shilingi bilioni nne, milioni 889; sawa na asilimia sifuri nukta mbili tatu (0.23%) ya mapato ya nchi nzima.

Mkoa wa Kagera kwa mwaka huo wa 2005/06 ulikusanya shilingi bilioni sita, milioni 619, sawa na asilimia sifuri nukta tatu mbili (0.32%) ya pato lote la TRA kwa mwaka. Mkoa wa Mara ulikusanya shilingi bilioni 34, milioni 548, ambazo ni sawa na asilimia moja nukta sita tisa (1.69%). Kanda nzima ilikusanya shilingi bilioni 86, milioni 742 kwa mwaka, ambazo ni sawa na asilimia nne nukta 25 (4.25%) ya pato lote kwa mwaka.

Kanda ya Ziwa ina utajiri wa ajabu. Kuanzia idadi ya watu, ardhi safi, mvua za kutosha, ziwa, madini, pamba, mifugo n.k

Mauzo ya nchi kwenda nchi za nje (exports) yanategemea sana kanda hii. Katika mwaka 2006, kwa mujibu wa taarifa za uchunguzi, dhahabu ambayo hutoka kanda hiyo ilichangia asilimia 43.7% ya bidhaa zote zilizouzwa nje. Samaki wa Ziwa Victoria walichangia asilimia 8.2 na pamba asilimia 3.3. Bidhaa hizi tatu za Kanda ya Ziwa pekee zimechangia asilimia 55.2 ya bidhaa zote zilizouzwa nje ya nchi.

Kwa ulinganisho wa makusanyo ya kodi na uuzaji bidhaa nje zilizotokana na kanda hii, ni dhahiri kuna mushkeli wa kutisha katika mikakati yetu ya kumiliki na kufaidisha wananchi na maliasili zao. Aidha, ni ushuhuda tosha kuwa, maliasili nyingine kibao zilizozagaa nchi nzima hazijawekewa mkakati wowote. Wote wanasubiri Serikali Kuu na kituo kimoja cha uwekezaji kitafute wawekezaji! Tunajilundikia majukumu yanayotuelemea.

Je? Kama mauzo nchi za nje kutoka Kanda ya Ziwa ni makubwa kiasi hiki, inakuwaje kodi yake iwe ndogo mno? Huu ni ushuhuda kuwa ‘wajanja' (wezi hawa) wanaivuna kanda hii na kuwaacha wananchi katika umaskini wa kutisha. Najua watajitetea kuwa makampuni makubwa yanalipia kodi Dar es Salaam. Wanaweza hata kudai kodi inayokusanywa si kigezo cha kupima umaskini! Mimi nasema ni kigezo tosha!

Ni dhahiri basi, kanda hii itabaki kuambulia mapanki, mashimo ya migodi, vumbi la migodi na misaada midogo ya zahanati, barabara za vumbi pengine na madarasa.
Kodi inaondoa fedha mifukoni mwa wananchi. Ikikusanywa, ni uthibitisho wa mzunguko halali wa fedha unaoambatana na uwezo wa kununua bidhaa na huduma kwa wananchi. Ni uthibitisho wa uchumi kumilikiwa na wenyeji.

Nina hakika, pangekuwa na serikali ya Kanda ya Ziwa (Jimbo la Ziwa), yenye viongozi wa kuchaguliwa na wananchi wa kanda hii, yenye mamlaka na maliasili, nao wakahusishwa sambamba na Serikali Kuu, mapato ya maliasili hizi yasingefujwa na kuhamishwa kwa kiasi inavyofanyika sasa. Serikali hii ya kanda yenye kuwajibika kwa wananchi wake ingesimamia maliasili ile. Ingekuwa na kituo chake cha uwekezaji kusaidia mikakati ya kanda. Ingelipa fungu kubwa la mgawo kwa Serikali Kuu. Serikali Kuu ingetumia fungu hilo kusaidia kikamilifu maeneo mengine.

Serikali Kuu imejikuta ina mamlaka na mali nyingi kiasi cha kushindwa kuzidhibiti. Kwa kweli ya Mungu, ni laana kwa Kanda ya Ziwa kuwa maskini kiasi hiki. Hii ni kanda inayotoa wabunge wengi, tena wa CCM, na sijui ni kwa nini hawalioni tatizo la kanda yao. Sijui wanangoja nini CCM – labda uwaziri. Nasisitiza, Kikwete amelemewa. Tunahitaji ku – overhaul nchi hii, ndiyo mwanzo wa salama yetu! Tumekwama, tusione haya kukiri! Nimesema na ninarudia: "Tanzania, hata ukimleta malaika, kwa mfumo wetu wa utawala – kazi itamshinda!"
Nchi imekwama; tayari Kikwete amelemewa (3)

Na Freeman Aikaeli Mbowe
Mwenyekiti Taifa

WIKI iliyopita nilimalizia makala yangu kwa kusema, Tanzania hata ukimleta malaika, kwa mfumo wetu wa utawala kazi itamshinda.
Hii ni kauli nzito. Inatia woga na inahitaji ujasiri kuitafakari na kuikabili. Wanasiasa ni watu wa ajabu kidogo. Wanasiasa, watawala wa Tanzania ni watu wa ajabu sana! Hata wanapoona chembe ya ukweli, wengi hukataa kuukiri hadharani. Hapa ndipo dhana ya kukwama inapoota mizizi.

Bila kujali ni chama gani cha siasa kiko madarakani, nchi yetu inahitaji mabadiliko makubwa ya kifikra, kimtazamo na hivyo kimkakati. Ni muda muafaka sasa kuachana na mazoea. Tufanye maamuzi magumu kwa ujasiri, tena bila woga, kama kweli tunakusudia kuiweka nchi yetu katika njia ya maendeleo endelevu. Lazima kama taifa, tukubali kutembea kwenye njia ya mabonde, vilima na miiba ili tufikie azima ya kujenga taifa lenye uhuru wa kweli, amani ya kweli na ya kudumu.

Maamuzi ya kuikwamua nchi iliyokwama kamwe hayawezi kuwa mepesi. Hayawezi kufikiwa kwa kukumbatia yaleyale na pengine walewale waliotukwamisha.
Hayawezi kufikiwa kwa kuchekeana wala kuoneana haya. Hayaji penye misingi ya kuleana na kulindana. Hayawezekani penye mwelekeo wa utawala wa kutaka sifa na mbwembwe (populist and pompous politics). Hayawezi kufikiwa kwa viongozi wetu wakuu hususan rais kucha kutwa akitembeza bakuli la kuomba misaada nje ya nchi kwa wahisani na wafadhili bila kwanza kuweka misingi sahihi ya ndani ya kujikwamua.

Wawekezaji makini hawaendi kwenye nchi iliyojaa rushwa, isiyo na nishati na miundombinu ya uhakika, eti kwa sababu wameombwa na rais. Nchi iliyoshindwa hata kuweka majina ya mitaa mipya maeneo kadhaa mapya yaliyopimwa ilhali meya anashinda uwanja wa ndege kupokea na kusindikiza kila kukicha. Misaada tumepewa na tunapewa sana! Mikopo tumepewa na tunapewa sana! Madeni tumefutiwa na tunafutiwa sana! Bado tumekwama! Bado tunaomba! Tukipata kidogo cha ndani, tunakifuja kisha tunaendelea kukinga bakuli! Hivi hatuoni aibu?

Kwa kipindi cha miaka thelathini iliyopita, Tanzania ni nchi ya kwanza katika Afrika chini ya Jangwa la Sahara isiyokuwa na vita, kwa kupewa misaada ya kimaendeleo. Hili nalo ni ulemavu wa kutisha na chimbuko jingine la kukwama kwetu! Nitalijadili siku yake!
Wenye dhamana ya kuongoza taifa wanahitaji kuchagua kati ya mawili:
Mosi, utawala wa haki (justice) ambapo sheria na taratibu (law and order) zinasimamia fikra pana na mikakati endelevu (long term vision and sustainable strategies) zenye kwanza kulenga masilahi ya taifa na watu wake, Au, pili, kuendeleza utawala wa mazoea (business as usual) na wenye kutaka sifa ambao hutegemea zaidi kauli za viongozi sambamba na matukio ya dharura (management by crisis) bila kujali sheria na taratibu za nchi.

Katika makala zilizopita, nilijaribu kuainisha jinsi mfumo wetu wa utawala ulivyo hodhi. Mfumo unaorundika maamuzi yote nyeti yakiwamo yanayohusu miliki ya rasilimali zote kuu za taifa mikononi mwa kundi dogo linaloitwa Serikali Kuu. Aidha, nilijaribu kuainisha jinsi Serikali Kuu, hususan rais alivyolundikiwa na kutwishwa majukumu makubwa ya kimaamuzi bila kujali ukubwa na upana wa mtandao wa nchi yetu na bila hata mifumo ya kumdhibiti! Nilitoa mifano rahisi ya kufikirisha kuhusiana na hali ya kiuchumi ya Kanda (Jimbo) la Ziwa.

Leo nitaendeleza mjadala zaidi katika uchumi na nitajenga hoja kuhusu tija za kiuchumi zitakazoweza kutokana na mfumo wa utawala wa majimbo. Mfumo unaokusudia kutoweka mayai yote kwenye kapu moja. Hizi ni fikra zangu binafsi zinazojengwa na uelewa pamoja na hisia zangu. Naziamini. Fikra zangu hizi zinatokana na uchambuzi binafsi wa mazingira yetu, uzoefu wa nchi nyingine mbalimbali sambamba na vionjo mbalimbali kutoka kwenye tafiti za wachumi mbalimbali wa zaidi ya karne tano zilizopita.

Si mawazo ya Benki ya Dunia (World Bank) au Shirika la Fedha Duniani (IMF). Si sharti, ni fikra mbadala zilizo wazi kwa mjadala.
Kwa ukubwa wa nchi, rasilimali zetu za asili na idadi ya watu, nchi yetu inaweza kugawanywa katika majimbo nane. Majimbo haya yatajitegemea kiuendeshaji (semi autonomous) isipokuwa kwa yale maeneo yatakayosimamiwa na sera kuu za taifa kwa mujibu wa maridhiano ya kikatiba.

Rasilimali za kila jimbo zikitumiwa ipasavyo kwa mikakati endelevu sambamba na ushindani unaoambatana na uhuru wa ushirikiano wa moja kwa moja kati ya jimbo na jimbo (inter province economic cooperation), kila jimbo katika kipindi cha miaka isiyozidi kumi ijayo, linaweza kuwa na uchumi unaolingana na uchumi wa taifa zima la Tanzania kwa sasa.

Kwa kuanzia, kila jimbo linaweza kuchagua vipaumbele vyake katika masuala ya kiuchumi na kuweka mkakati wa ndani wa kuviendeleza kutokana na mazingira yake. (specialization). Mara nyingi, mitazamo yetu imelenga kuangalia kilichopo leo na kutoona fursa zilizopo. Tunakuwa wepesi wa kufikiria kuvuna bila kujua tuna wajibu mkubwa wa kupanda, kupalilia na kisha ndiyo hatimaye tuvune. Kwa hali ilivyo leo, jimbo la Ziwa (mikoa minne ya Kagera, Mwanza, Shinyanga na Mara) linatoa zaidi ya nusu ya mauzo yetu nchi za nje.

Kanda ya Ziwa ingekuwa na uhuru wa kujiendeleza bila kuomba kila kitu sambamba na maelekezo kutoka Serikali Kuu, leo jimbo hili pekee lina uwezo (economic potential) wa kuwa na uchumi unaolingana na Tanzania nzima katika kipindi cha miaka isiyozidi kumi.
Kwa kuwa na uhuru wa kiuchumi bila kubughudhiwa na Serikali Kuu, sanjali na fursa za ziada (comparative advantage), serikali ya jimbo hili inaweza kujiwekea mipango yake endelevu na kuweza kuzalisha na kulisha bidhaa na vyakula si Tanzania pekee, bali pia nchi nyingine za Maziwa Makuu.

Aidha, inaweza kuweka taratibu zake za kisera za kiuchumi kulingana na msukumo wa soko katika eneo la Maziwa Makuu (market forces) kuliko kukwazwa na kifungo cha sera za biashara zinazotawala Tanzania nzima. Nikiwa bungeni, nakumbuka mvutano mkubwa baina ya baadhi ya wabunge wa Mkoa wa Kagera waliokuwa wanailalamikia Serikali Kuu kuwanyima ruhusa wakulima wa kahawa wa mkoa huo kuuza kahawa yao Uganda.

Kwenye soko la Uganda ambalo halikuwa na urasimu, wakulima hawa waliweza kulipwa mara moja, tena bei zaidi ya mara tatu ya ambayo wangeipata kwa kuuza kahawa yao katika mfumo wa Tanzania.
Kwa mfumo wetu, kahawa yote huuzwa kupitia soko la kimataifa la kahawa la Moshi.

Leo hakuna hata mkoa mmoja umeweza kuweka mkakati wake wa ndani wa kuweza kuuza moja kwa moja bidhaa zake nje ya nchi. Makampuni yapo, lakini si katika mkakati wa kisera wa kimkoa. Kuna Watanzania wengi tu ambao mfumo wetu ungeruhusu, wangeweza kuleta ufanisi wa kutisha katika majimbo mbalimbali. Majimbo yote hayawezi kulingana katika rasilimali na hivyo nguvu za kiuchumi. Hii ni hali halisi ya maisha duniani katika nyanja yoyote. Kamwe, binadamu hawalingani.

Hata mikoa yetu leo ina tofauti kubwa za kirasilimali na kimaendeleo. Cha msingi hapa, ni lazima kuweka mfumo ambao utaweza kuendeleza majimbo yenye upungufu (na si uhaba) wa rasilimali, bila kuathiri au kukwamisha majimbo yenye rasilimali nyingi?
Mfumo wetu wa utawala, bila kujua umeendelea kuipokonya baadhi ya mikoa rasilimali watu wake (systematic internal brain drain) na kuwaamishia kwenye baadhi ya mikoa hususan Dar es Salaam panapoonekana kitovu cha kila kitu. Ukweli Dar es Salaam ni kitovu cha biashara tu.

Hali hii imesababisha baadhi ya mikoa kubaki duni kimaendeleo, na siri hapa ni utawala wa majimbo ambao sasa badala ya watu kukimbilia Dar es Salaam penye Serikali Kuu, watu watarudi kuendeleza kwao, na kikubwa zaidi kushiriki katika uongozi wa jimbo lao.
Ni vyema kukumbushana kuwa suala la uraia chini ya utawala huu ni suala la kitaifa. Hivyo kwenu si tu pale ulipozaliwa au kukulia, bali popote pale utakapoamua kuishi katika mipaka ya Tanzania.

Tujiulize, leo ni wasomi wangapi wakishapata shahada ya chuo kikuu au kufuzu elimu yoyote ya vyuo vya elimu ya juu mbali na wale walioko kwenye Serikali Kuu, Serikali za Mitaa na asasi zisizo za kiserikali hubaki mikoani, achilia mbali wilayani? Haya ni maswali magumu ya kujiuliza!

Juhudi za kujenga uchumi ni lazima sasa zipanuliwe na zisiwe suala la Dar es Salaam pekee. Jimbo la kusini ambalo limependekezwa kushirikisha mikoa ya Lindi, Mtwara, Wilaya ya Tunduru na sehemu za kusini za Mkoa wa Pwani, ambalo leo huonekana mojawapo ya sehemu maskini ya nchi yetu, ni eneo lenye utajiri wa kutisha! Gesi pekee, ingetosha kubadilisha uchumi na maisha ya Watanzania waishio eneo hili, achilia mbali, mabonde yenye rutuba, pwani ndefu na nzuri, korosho na hata madini ya vito! Lakini wapi!

Kila kitu kinabebwa, kama si kwa malori, ni meli na mabomba na kupelekwa Dar es Salaam kufidiwa na wajanja. Wananchi hoi! Wabunge wao kucha ni kulalamika na kuendelea kuiomba serikali iwaonee huruma. Ndugu zangu wa kusini, hapendwi mtu hapa! Siri ya mafanikio yenu iko mikononi mwenu! Tunahitaji usimamizi makini, sahihi na wenye kujali rasilimali zetu (sustainable and starategic utilization of our natural resources).

Tanzania leo hakuna mkoa hata mmoja usio na rasilimali, achilia mbali mikoa kadhaa ikiunganishwa kuwa jimbo. Ni kosa kufikiri kuwa rasilimali zetu ni lazima ziwe madini na vito! Watu na ardhi bila hata kipande kimoja cha madini ni rasilimali tosha ikiwekewa mkakati sahihi. Tanzania hatuna jangwa popote. Lazima leo tukumbuke kuwa kwa mfumo wetu, uzembe wa Serikali Kuu, ni janga kwa nchi nzima.

Tukumbuke mfano hai wa ufisadi, uzembe na tamaa ya wachache katika Serikali Kuu na sekta ya nishati na umeme ulivyoweza kuingiza zaidi ya asilimia 80 ya taifa kwenye adha ya mgawo wa umeme! Serikali Kuu tuliyo nayo leo ni sawa na mtaka yote kwa pupa ambaye hatimaye hukosa yote. Kwa kuwa halmashauri za wilaya hazina chanzo cha uhakika cha mapato, Serikali Kuu hushika mpini, na hali hii imeathiri kwa kiasi kikubwa ari ya utendaji na hata tija ya wataalamu wachache walioko katika ngazi za wilaya.
Hebu tena tuchukue mfano mwingine wa Wizara moja ya Kilimo.

Nimekuwa bungeni kama mbunge na nimekuwa diwani katika Halmashauri ya Wilaya ya Hai, hivyo ninayoyaandika nimeyashuhudia na si mambo ya kubuni. Nimeshuhudia jinsi nchi nzima inavyotegemea Serikali Kuu kama chanzo cha mapato na hata maelekezo.
Tunaye waziri mmoja wa Kilimo anayesimamia kilimo nchi nzima. Kila kitu kinachohusu kilimo katika nchi hii kiko chini yake.
Kuanzia mazao makuu ya biashara kama pamba, kahawa, korosho, katani, chai, tumbaku, maua na pareto hadi mazao ya chakula, zikiwamo nafaka, mboga na hata matunda!

Ni wazi kwa mzigo huu, ufanisi hauwezekani, kwani ni vigumu kwa waziri hata na wataalamu wote wa wizara kuweza kusimamia sekta hii nyeti kwa tija inayostahili. Kwa upana huu wa majukumu, specialization haiwezekani. Najua wengine watahoji kuwa mbona kuna wataalamu wa kilimo mikoani na hususan wilayani? Hawa ni tegemezi. Hawana mamlaka wala maamuzi bila kibali cha Serikali Kuu. Asilimia zaidi ya 95 ya mipango yao inategemea mafungu na kibaya zaidi maelekezo kutoka Serikali Kuu. Kwamba nchi nzima wenye akili ya kuwaza kuhusu kilimo wako Dar es Salaam tu!

Hawa ni kundi kibao la wataalamu wa kilimo ambao wenyewe si wakulima na utaalamu wao wa kilimo umeishia kwenye nadharia, na wachache tafiti miaka kadhaa wakiwa vyuoni. Kwa mazoea na utamaduni huu, tutaendelea kuua kilimo, kumnyonga mkulima na kuukumbatia umaskini. Tutaendelea kubadilisha mawaziri wa kilimo na kila mmoja atatoka na lawama kuwa wizara imemshinda.
Tungekuwa na utawala wa majimbo leo, kila jimbo lingekuwa na wizara yake ya kilimo. Juhudi (kama zipo) zinazofanywa na wizara moja ya kilimo iliyoko Dar es Salaam leo, zingerudufishwa (multiplied) mara nane.

Tusingekuwa tumeweka mayai yetu yote katika kapu moja. Upungufu wa sera au uzembe wa kundi dogo lililoko Dar es Salaam, kamwe lisingekuwa tatizo kwa nchi nzima. Kila Jimbo lingekuwa na sera na mikakati yake ya kilimo inayojitosheleza na inayotokana na mazingira ya jimbo. Hii ni pamoja na hali ya hewa, ikiwamo misimu ya mvua.

Katika hali hii, ni rahisi kila jimbo kuwa na mazao machache yanayoweza kuwekewa mipango madhubuti ya ugani (extention services) itokanayo na matokeo ya tafiti sahihi za eneo. (research and development through appropriate technology). Badala ya kupanua Serikali Kuu, tunastahili kuipunguza na kutoa madaraka ngazi za jimbo ili kurahisisha maamuzi na kuruhusu mikakati ya kila jimbo kusimamia rasilimali zake na kuziendeleza.

Nilieleza siku za nyuma, kuwa Serikali Kuu inastahili kubaki na wizara nyeti hususan za Ulinzi na Usalama, Mambo ya Ndani, ikiwamo Uhamiaji, Fedha na Mambo ya Nje. Kwa utaratibu utakaoafikiwa, kila jimbo litachangia sehemu ya mapato yake kwa Serikali Kuu kwa ajili ya miradi au mipango ya kitaifa. Narudia na nitarudia sana. Hoja ya kuutazama upya muundo wa utawala wa nchi yetu unahitaji mjadala wa kitaifa. Utakuwa ni upungufu mkubwa na ufinyu wa fikra kwa yeyote kuliona suala hili kwa jicho la ushindani wa vyama vya siasa.

Tunaogopa nini kukabiliana na fikra hii sambamba na changamoto zake?
Maendeleo ya Tanzania yataletwa kwa kuweka maridhiano na masilahi ya kitaifa mbele. Vyama vya siasa, taasisi na asasi mbalimbali zenye kujadili mustakabali wa nchi yetu na hata watu binafsi visiwe kikwazo kwa maridhiano ya kitaifa, bali viwe chimbuko la fikra mbadala za kulikwamua taifa letu lilipokwama.

Nchi imekwama; tayari Kikwete amelemewa (4)
Na
Freeman Aikaeli Mbowe
Mwenyekiti Taifa


NIMEKUWA kwa wiki kadhaa, nikijadili fikra ya kubadilisha mfumo wa utawala wa nchi yetu kuwa wa majimbo. Wakati naanza mjadala huu, nilitahadharisha kuwa suala hili ni pana na litachukua muda kulielezea, ‘kufundishana' na hatimaye kuendeleza mjadala wa kitaifa.

Nimekuwa najadili mada tatu kwa pamoja. Ya kwanza, nchi imekwama, ya pili, Kikwete amelemewa; na tatu tufanye nini kujikwamua.
Wananchi kadhaa wamekuwa wakichangia mawazo tofauti katika kila hatua. Nimeshangazwa na kufarijika kujua Watanzania wengi ndani na nje ya nchi wana kiu ya kutafuta ufumbuzi wa kujitoa kwenye kukwama kwetu! Ni hatua, kwani kugundua kuna tatizo ndio msingi wa mabadiliko.

Nayafanyia kazi na tuendeleze mjadala. Bado nahitaji mawazo mengi kwani hili ni suala letu sote, bila kujali tofauti zetu za dini, itikadi, rangi, kabila au jinsia. Sisi ni Watanzania, na jambo hili ni la Tanzania! Kabla sijaendelea na tafakuri yangu ya leo, nimeona ni bora angalau leo nidokeze barua pepe moja niliyoipata kutoka kwa Mtanzania mmoja. Nanukuu:

"… Sijui lengo lako nini katika makala zako. Kama lengo lako ni kufurahisha walalahoi vizuri – well done; na kama unafanya kazi yako – excellent. Lakini kama haupo kati ya hayo, fahamu kuwa nchi haijakwama na Kikwete hajalemewa. Wanakula nchi. Sasa wewe ulitaka wafanyeje? Ulitaka wafanye kazi ya kanisa? Mali iko bwelele.

Huna ubavu nini? Sharti la mali hii ni moja, lazima ukubali kuuawa au kuuliwa. Wewe vyote unaogopa. Uko kwenye kundi la wanaume, wanawake! Unakumbuka mzee mzima alisema hawezi kuwaachia mbwa wachukue nchi? Ulielewa maana yake? Unawajua hao dogs? Wanaoelewa wamekaa kimya, wanaishi kwa amani na utulivu.

Sikusudii kujadili hili. Nimeliwasilisha ili wenye kupenda walitafakari. Akili ni nywele, kila mtu ana zake. Kwa msingi huu basi, leo naomba tafakuri yangu ihamie kwenye jambo jingine linalonikera na kusumbua fikra zangu. Lina uhusiano wa karibu sana na "kukwama kwetu." Hili si jingine bali ni kile kinachoitwa sasa ‘mabilioni ya Kikwete'. Ni zaidi ya miezi minane sasa, vyombo vya habari, viongozi wa serikali na CCM na hata wananchi wa kawaida wanajadili kwa njia moja au nyingine mabilioni au mamilioni ya Kikwete.

Jambo hili sasa limechukua sehemu kubwa ya fikra ya wananchi na viongozi na sasa kuwa ndiyo hoja ya msingi ya mjadala kuhusu mkakati wetu kama nchi wa kupambana na umaskini.
Msamiati huu ulifikiwa baada ya hatua mbili za viongozi wetu wakuu, kukiuka katiba na taratibu za usimamizi wa fedha za serikali. Hatua ya kwanza ilianzishwa na waziri mkuu alipotangaza kuwa serikali itatoa shilingi za Kitanzania milioni 500 kwa kila mkoa kwa ajili ya kukopesha wananchi.

Tamko hili la waziri mkuu alilitoa katika mazingira ya kutatanisha kwani halikuwa sehemu ya bajeti ya serikali. Hii ilikuwa Dodoma.
Wakati bado wadau kadhaa makini wakijadili kulikoni, rais mwenyewe akaongeza dau akiwa kwenye mikutano ya hadhara katika Mkoa wa Mara. Akaahidi kuwa sasa kiwango kitaongezwa maradufu na kufikishwa shilingi bilioni moja. Kauli hii nayo ilitolewa nje ya mipango ya bajeti ya serikali.

Katika mazingira ya kawaida, mtu waweza kuonekana mchawi kwa kuhoji ukiukwaji huu wa taratibu za matumizi ya fedha za serikali. Hii ni kwa sababu kwa walio wengi wanaona ni hatua muhimu na muafaka ya kupambana na umaskini, na kwamba fedha zimelengwa kwenda kwa wananchi, tena inavyosemekana wale walio maskini!

Ninachopenda kukumbusha hapa ni suala la kikatiba ambalo si waziri mkuu wala rais aliye juu yake. Kwa mujibu wa katiba yetu, mapato yote na matumizi ya serikali yanapaswa kujadiliwa na kuidhinishwa na Bunge. Haya yamefafanuliwa na Katiba ya nchi sura ya tatu, sehemu ya kwanza, ibara ya 63(1) hadi 63(3), ibara ndogo ya (a) hadi (e).

Aidha, maelezo ya ziada zaidi yametolewa katika katiba ya nchi, sura ya saba sehemu ya pili, inayozungumzia "mfuko mkuu wa hazina na fedha za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania" ibara ya 135, hadi ibara ya 140. Pamoja na vifungu hivi kutoa mamlaka kwa matumizi ya serikali kuidhinishwa na Bunge, imetoa fursa kwa serikali kuweza kufanya matumizi "kwa jambo lolote la haraka na dharura."

Mpango wa mabilioni ya Kikwete haukuwa wa haraka wala dharura bali ulikuwa wa papara. Usingestahili kupewa fedha nje ya mpango wa bajeti ya serikali. Tabia ya Serikali ya Awamu ya Nne kufanya matumizi nje ya bajeti sasa inageuka utamaduni.
Fedha za ziada zilizoahidiwa wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu nazo ni nje ya bajeti. Hii ni hatari, kwani inafanya maana yote ya Bunge kudhibiti matumizi ya serikali kuwa kupoteza muda.

Aidha, kama ni lazima, basi serikali ifanye matumizi kama hayo nje ya bajeti, bado ina wajibu wa kupeleka bungeni bajeti ndogo yaani ‘supplementary budget' kupata baraka za Bunge. Huu ndiyo utawala bora! Leo kuna taarifa kuwa serikalini kuna nakisi ya bajeti (budget deficit) kubwa – yaani matumizi yaliyozidi maidhinisho ya bajeti. Hii inatokana na matumizi mengi holela ambayo hayakupitishwa na Bunge. Suala la bajeti nitalijadili siku za usoni.

Pamoja na nia njema inayoweza kuhusishwa na mpango huu wa mabilioni ya Kikwete, ukweli ni kuwa mpango huu ni wa kukurupuka, hauna maandalizi, umejazwa siasa na hatima yake itakuwa kupoteza fedha za wananchi (si za Kikwete) na kama kawaida, hakuna atakayewajibishwa.

Kadhalika, ni vyema niweke wazi kuwa uchumi wa nchi au mkakati wa kuwawezesha wananchi haufanywi hivi. Mkakati wa kuwanyanyua wananchi kiuchumi ni mkakati mpana unaohitaji ufuatiliaji na tathmini makini (monitoring and evaluation). Leo katika mpango huu hamna kitu. Ni sanaa tupu.

Katika kupambana na umaskini, dhana sahihi ni kutoa kipato (au chanzo cha mapato) kwa wananchi. Hii inaweza kuwa kwa njia ya kujiajiri au kuajiriwa. Haiwezekani kwenye taifa kila mtu akawa mfanyabiashara. Siku zote watakuwapo waajiri na waajiriwa.
Jambo hili (sijui niliite sera, mkakati, dharura au nini! – manake ni jambo lililozuka tu, bila mpango wa utafiti!) linanikumbusha sera ya ‘kuwajaza watu mapesa' ya Bwana John Cheyo, Mwenyekiti wa Chama cha UDP.

Cheyo alipokuja na sera yake hii, ambayo kwa kweli kwa wale wenye kupenda kufuatilia sera za vyama mbali mbali, watagundua kuwa ilipotoshwa kwa makusudi na chama tawala. Sera hii ilizungumzia kunyanyua uchumi wa taifa ili hatimaye wananchi waongezewe uwezo wao wa matumizi kwa kuwa na kipato cha uhakika mifukoni mwao (purchasing power). Wapotoshaji wakasema Cheyo anakusudia kugawa fedha!

Sasa leo yamejiri upande wa pili! Wanagawa wao, tena bila mkakati. Ni muhimu kukumbuka kuwa nchi yetu na watu wake si ‘guinea pigs', yaani viumbe wa kufanyiwa majaribio ya kisiasa, kiuchumi na kisayansi. Serikali inapokuja na mkakati wowote, unastahili kuwa endelevu na hivyo wenye maandalizi ya kutosha baada ya utafiti wa kina wa ni nini kusudio la mkakati wenyewe.
Mpango wa mabilioni ya Kikwete ulilenga zaidi sifa za kisiasa na mikakati dhaifu ambayo kamwe haiwezi kuwaondoa wananchi kwenye umaskini na hauwezi kuwa endelevu. Naomba hapa Watanzania wajiulize mambo yafuatayo:

Ni vigezo gani vya kisayansi vilivyotumika kupangia kila mkoa idadi sawa ya fedha? Kwa mujibu wa takwimu za sensa za mwaka 2002, Mwanza ina watu milioni 2,942,148, Lindi wakazi 791,306 na Pwani wakazi 889,154. Hivi kweli mgawo wa shilingi bilioni moja kwa mkoa kama Dar es Salaam wenye watu zaidi ya milioni nne utasimamiwaje bila maandalizi? Ni tija gani inakusudiwa na mpango huu? Mpango huu ni wa muda gani?

Unakusudia kuwainua wazawa wangapi na kwa vigezo gani?
Iweje serikali inayokusanya kodi zaidi ya shilingi bilioni 200 kwa mwezi na kuogelea kwenye anasa za kutisha imege "kabilioni kamoja" eti kuwaondolea wananchi umaskini na wananchi kukesha wakijawa matumaini hewa? Hivi ni Watanzania wangapi wanajua kuwa kila mwezi CCM inachota Hazina shilingi bilioni moja ambazo ni sawa na kiasi kinachotolewa kwa wananchi wote wa mkoa kwa miaka mitano?

Siku zote, panapokosekana ‘vision' mambo kama haya ya aibu na kiini macho hujitokeza. Nia njema ya kuwasaidia wananchi haiwezi kuletwa na mipango isiyofanyiwa utafiti na isiyotekelezeka. Mikakati ya kuwawezesha wazawa wa nchi hii haihitaji pupa, bali inahitaji mkakati makini wenye kuthubutu na usio na mwelekeo wa kutaka sifa za kisiasa. Mkakati wowote wa kulikwamua taifa, lazima uachane na sifa. Uangalie vigezo sahihi vya kiuchumi sambamba na hali halisi ya wananchi wetu. Lazima mpango wowote wa sampuli hii uwe na malengo.

Kwa jinsi ulivyobuniwa kwa misingi ya zimamoto, mpango huu ni kiini macho. Ni mpango ambao madhara yake ni kuwa sasa wananchi walio wengi wamekita fikra zao kwenye hicho kinachoitwa mabilioni, wakiamini sasa ufumbuzi wa matatizo yao umepatikana. Huku ni kulemazana na ni hatari. Kama juhudi za makusudi hazikufanyika kurekebisha udhaifu huu, fedha hizi ziko njiani kupotea. Badala ya kuwalaumu wataalamu wa mabenki yetu tuwapongeze kwa angalau kuweka utaratibu wa udhibiti.

Kinachojidhihirisha hapa ni kuwa serikali ilimwaga mapesa kwenye mabenki bila makubaliano na taratibu kamili. Huku ni kukosa uchungu na fedha za walipa kodi. Nani kasema kwamba, mtu kuwa mkuu wa wilaya, mkuu wa mkoa, waziri, waziri mkuu hata rais, basi ana uwezo wa kusimamia biashara na hata kuelekeza watu wafanyeje biashara?

Nchini mwetu tuna TCCIA (Tanzania Chamber of Commerce, Industries and Agriculture). Tuna CTI (Confederation of Tanzania Industries) na juu ya yote, tuna Tanzania National Business Council, yaani Baraza la Biashara la Taifa ambalo nalo limejaa wanasiasa na watendaji wa serikali kuliko wadau.
Hivi hawa wote wameshindwa kupendekeza mfumo sahihi wa mkakati endelevu wa wazawa?
Hawa ni wadau wa biashara. Japo wengi wao ni wafanyabiashara wakubwa, nina hakika wana uwezo mkubwa wa kuishauri serikali njia muafaka ya kutoa mikopo midogo midogo ambayo itakuwa endelevu kwa wafanyabiashara wadogo wadogo.

Kama nao hawa ni sehemu ya maamuzi haya ya siasa na ya aibu, basi kazi ipo! Masuala ya mikopo ni masuala ya biashara. Ni vyema Kikwete na Lowassa wakumbuke kuwa si kila mtu ni mfanyabiashara. Hata Kikwete mwenyewe sijui kama amewahi kuendesha biashara yoyote!

Pengine ingemsaidia kujua ‘principles' rahisi za biashara. Biashara ni fani inayoendeshwa na ufahamu wa sita (ufahamu wa ziada). Kwa Kiingereza, ufahamu huu huitwa ‘instincts'.
Katika biashara, mtaji ni jambo la msingi lakini si hitaji pekee! Aidha, elimu si kigezo tosha cha kufanikiwa katika biashara. Biashara huhitaji nidhamu ya juu kuifanikisha. Mtu hawezi kusukumwa kwenye biashara kwa kutanguliziwa fedha!

Kama hoja ni kuandikiwa mradi unaouzika, mbona miradi itaandikwa sana! Kigezo cha uzoefu (track record) ni muhimu katika dharura hii! Haya ni baadhi ya maamuzi magumu yanayohitaji kufanyika ili kweli twende mbele. Ila kama suala ni siasa na kudanganyana, matokeo yatatuumbua.
Siku zote, wazo hutangulia biashara na fedha inapotangulia biashara, kamwe biashara hiyo haidumu. Hii ni ‘principle' rahisi ambayo viongozi wetu wanastahili kuielewa na kuisimamia katika wazo zima la kuwawezesha Watanzania.

Njia muafaka, kama serikali ilikusudia kuinua ajira na kipato cha wananchi, ingefikiria kwanza kuwawezesha wale ambao tayari wameonyesha mafanikio katika kukabiliana na biashara zao bila mtaji wa serikali. Hawa tayari wanajua mbinu za biashara na ‘guiding principles zake,'. Ni rahisi kupanua biashara zao wakiongezewa mtaji na hivyo kupanua ajira na hata pato la taifa. Fedha za wananchi zitakuwa salama, na ajira zitaongezeka.

Pili, kama taifa, tuna sababu ya kuwa na mpango wa muda wa kati wa kujenga tabaka au kundi la wafanyabiashara wa kati na wenye taaluma katika kila nyanja ya uchumi wa nchi. Hawa waandaliwe kitaaluma na wategemewe kuingiza ‘know how' katika nyanja mbalimbali watakazojiandaa nazo. Hatuna njia ya mkato katika hili.
Lazima sasa tujenge kwa nguvu ‘middle-class'. Hii ni programu maalumu.

Tatu, lazima sasa tuachane na mambo ya kufikirika. Ghafla Tanzania imekumbwa na ‘fashion' ya kitu kinachoitwa SACCOS! Hiki ni kichekesho.
Kulazimisha watu kuungana kwenye SACCOS ni kiini cha kufuja fedha kama ilivyokuwa wakati wa maduka ya ushirika.
Pale watu wanapoamua kuungana wenyewe, sawa! Lakini wasilazimishwe na serikali. Serikali iruhusu watu binafsi wenye sifa ya uwezo wa biashara wakope fedha hizi kwa masharti nafuu, waone kama katika wiki mbili itabaki fedha benki! SACCOS zinaua ‘private sector initiative' ambayo leo tunazungumza kuiendeleza.

Siku zote fedha za pamoja zinakosa nidhamu ya kuzidhibiti. Nchi hii mbona hatujifunzi madhara ya kulazimishana!
Hivi karibuni, akiwa Morogoro, Waziri Mkuu aling'aka na kuhoji inakuwaje mikopo haijatolewa mkoani humo! Akatoa amri, mabenki yatoe mikopo haraka na wapunguze masharti, kwani serikali iko tayari kuweka dhamana ya shilingi bilioni tano fedha ikipotea!
Jamani Waziri Mkuu anazungumzia fedha zake binafsi au kodi za Watanzania wote?

Hivi hizi fedha kuitwa ‘mabilioni ya Kikwete' tayari viongozi wameanza kujenga utukufu kwamba wana uwezo wa kuziazimisha na kuzitoa bila hata kujali zikipotea?
Haya, karudi rais kutoka ughaibuni, naye na lake. Akapingana rasmi na waziri mkuu wake kama vile wanaongoza serikali mbili tofauti. Ndiyo kukosa maandalizi. Rais yeye anasema masharti ni lazima. Nakubaliana naye. Hii ndiyo hali halisi popote duniani, masuala ya fedha na biashara yanapojiri.

Katika kila hatua, mtu yeyote, awe rais, waziri mkuu, mkuu wa mkoa, mkuu wa wilaya, maofisa wa benki na hata sisi wananchi, tuna wajibu wa kwanza kujua, fedha hizi si za rais bali ni fungu kutoka kodi ya wananchi wote na Watanzania watastahili kupata mrejesho wake mbele ya safari. Zikipotea, basi na waliohusika na upotevu wawajibishwe.

Kumekuwa na habari za kuchanganya kuhusu utoaji wa mikopo hii. Ni vyema sasa serikali ikaweka tena hadharani taarifa zote za msingi kuhusiana na mikopo hii. Matamko mbalimbali yanawachanganya Watanzania kujua ni nini hasa kinajiri. Ikubali aibu lakini iokoe fedha zetu.

Maamuzi ya kisiasa ndiyo yaliyoua benki za NBC, THB, TIB (ya wakati huo) na taasisi zetu nyingine. Viongozi waliidhinisha mikopo kwa kutumia ‘memo' kwenda kwa wakurugenzi na mameneja wa mabenki haya. Matokeo yake, leo wote tunayajua.
Biashara yoyote inapoendeshwa kwa kutanguliza siasa na si misingi ya biashara, inashamirisha wizi na lazima ife. Nina hakika Kikwete na Lowassa wanakumbuka sana shirika la biashara la CCM lililoitwa SUKITA.

Shirika hili lilichota mabilioni ya fedha kutoka kwenye benki za umma bila kufuata taratibu za kibenki. Matokeo yake, mabilioni yamepotea, SUKITA imekufa kinyemela, madeni ya mabenki hatuambiwi yameishia wapi. Huu ulikuwa wizi wa CCM na uhujumu wa uchumi. Hakuna aliyeguswa! Ni watu hawa hawa tunategemea leo wana tiba ya uchumi na umaskini wetu!
Ni vyema Watanzania wakumbuke katika kipindi cha Awamu ya Tatu ya uongozi wa rais mstaafu Mkapa, taifa lilipoteza mamilioni ya fedha kimya kimya kupitia mikopo iliyotolewa kisiasa kupitia halmashauri za wilaya, manispaa na jiji, kwa vilivyoitwa vikundi vya kina mama na vijana! Asilimia kubwa ya mikopo hii haikurejeshwa.
Hii ni changamoto.

Kikwete ametamba Denmark kwamba alijiandaa kwa miaka kumi kuwa rais. Nakubaliana naye. Alijiandaa kupata cheo cha urais na sasa tunategemea atuonyeshe kilichomsukuma kuutaka urais! Nikubaliane na wengine. Nchi imekwama, lakini Kikwete hajalemewa! Yeye anaona yote sawa tu!

Ughaibuni kwa sana! Mambo yanaenda na hata Real Madrid wanaweza kuja!
Kazi ipo!


Mabadiliko ya Kweli, Uhuru wa Kweli


 
haya yoote ni mazuri sana, lakini kwa jk na chama chake hapa ni sawa na kumpigia mbuzi gitaa tuwaoni matumbo yao na auaji kwa raia kwanza watz badaye, ngoja vijana wa lumumba waje, au nepi na mwizi wa wake za watu waje na comrade wao mzee wa kudadadaaaadeedekiiiiii............
 
100 kamanda then ninaombi kidogo kama utakubaliana nami.mimi nadhan kuna umuhimu wa kurudisha baadhi kama sio zote sera za kijamaa mana moja ya tatizo kubwa linaloikumba nchi ni kuhusu matabaka baina wenye nacho na wasio nacho sasa unadhani 2fanyaje hapo kamanda.last naamin uliyoongea yana mana kubwa kwa taifa letu
 
100 kamanda then ninaombi kidogo kama utakubaliana nami.mimi nadhan kuna umuhimu wa kurudisha baadhi kama sio zote sera za kijamaa mana moja ya tatizo kubwa linaloikumba nchi ni kuhusu matabaka baina wenye nacho na wasio nacho sasa unadhani 2fanyaje hapo kamanda.last naamin uliyoongea yana mana kubwa kwa taifa letu
Zabushir,
Wewe unadhani ni kwa nini CCM chini ya Mwinyi waliamua kuliua Azimio la Arusha? Kwa sababu waliamini katika sera za matabaka. Na tabaka la juu ni wao watawala. Kinachotokea sasa si bahati mbaya. Kilipangwa.
 
Hapo ndio ninapo muona MH MBOWE NI KICHWA CHA KIUKWELI.nimekuwa mwanachama wa CHADEMA kwasababu moja kubwa nayo ni CHAMA KINA NJIA MBADALA ya kuipeleks Nchi kwenye mafanikio,tatizo letu kama NCHI mh MBOWE amelichambua kinagaubaga,hongera sana.
 
Zabushir,
Wewe unadhani ni kwa nini CCM chini ya Mwinyi waliamua kuliua Azimio la Arusha? Kwa sababu waliamini katika sera za matabaka. Na tabaka la juu ni wao watawala. Kinachotokea sasa si bahati mbaya. Kilipangwa.

kimsingi katika jamii yoyote ile matabaka hayakwepeki. Kutakuwa na watu wenye nacho na wasio nacho. Jukumu la serikali zinazo wekwa na wananchi ni kuasisi sera zinazo wabeba kundi la kati ambalo ndio kiunganishi cha walio juu na waliochini.

Ujamaa ulilenga kujenga jamii ya watu walio sawa wakati hata ukiwapa watu fursa sawa hawawezi kuwa sawa kwani naturally tumezaliwa tukiwa tofauti namna tunavyo waza, kutenda na hata tunavyo himili magonjwa.

Mtu aliye ugua mwaka mzima kamwe hawezi kumkuta mtu aliye zalisha mfululizo mwaka mzima.na ndio maana tofauti za kipato hazikwepeki.
 
kimsingi katika jamii yoyote ile matabaka hayakwepeki.kutakuwa na watu wenye nacho na wasio nacho.jukumu la serikali zinazo wekwa na wananchi ni kuasisi sera zinazo wabeba kundi la kati ambalo ndio kiunganishi cha walio juu na waliochini.ujamaa ulilenga kujenga jamii ya watu walio sawa wakati hata ukiwapa watu fursa sawa hawawezi kuwa sawa kwani naturally tumezaliwa tukiwa tofauti namna tunavyo waza, kutenda na hata tunavyo himili magonjwa.mtu aliye ugua mwaka mzima kamwe hawezi kumkuta mtu aliye zalisha mfululizo mwaka mzima.na ndio maana tofauti za kipato hazikwepeki.
Usisahau kuwa ilikuwa Ujamaa na Kujitegemea. Usiache Self Reliance. Tulikuwa na Socialism & Self Reliance; achilia mbali Ujamaa kama wewe unaona inapotosha, tuchukue Self Reliance = kujitemea; kila mtu atapata kwa jasho lake. Siyo kwa kuiba, siyo kwa kutapeli.

Huwezi kuwa na nchi ikajiita ati ni Nchi wakati haina Middle Class, watu wa kati. Hebu twambie hivi Tanzania kuna middle class?? Kama ipo ni asilimia gani ya population? Nchi isiyo na middle class haiwezi kuendelea. Tanzania is one!
 
Hivi majuzi, kuna memba wapya wamejiunga baada ya mabandiko ya ndugu Zitto, wakisema eti mwenyekiti wa chadema hawezi kuandika articles kama ilivyo kwa Zitto.

Binafsi ninatambuwa na nilikuwepo hapa jukwaani wakati mwenyekiti wa chadema akiwa member humu na alikuwa akibandika makala zake na kuziita "tafakuri", zilikuwa makala za nguvu!

Nadhani walikuwa watoto hao kina mwavuli, sasa wanasema eti hawajui kuwa mwenyekiti wao anaweza kuandika makala. Nikajuwa wamelishwa sumu. Sasa waje hapa kuchangia kama wanataka. Nilichowahakikishia ni kwamba wataifahamu JF taka wasitake!
 
Usisahau kuwa ilikuwa Ujamaa na Kujitegemea. Usiache Self Reliance. Tulikuwa na Socialism & Self Reliance; achilia mbali Ujamaa kama wewe unaona inapotosha, tuchukue Self Reliance = kujitemea; kila mtu atapata kwa jasho lake. Siyo kwa kuiba, siyo kwa kutapeli.

Huwezi kuwa na nchi ikajiita ati ni Nchi wakati haina Middle Class, watu wa kati. Hebu twambie hivi Tanzania kuna middle class?? Kama ipo ni asilimia gani ya population? Nchi isiyo na middle class haiwezi kuendelea. Tanzania is one!
OSA NI kuwa na ownership ya pamoja.yaani mtu mvivu finally na yeye anapata mgao wake.ownership ya aina hii haichochei ushindani katika kubadili mazingira kuwa mali.hakuna anayejali mali kama viwanda watu wanakosa uchungu navyo na hivyo kufa. ubepari unataka kila mtu afanye kazi na asiye fanyakazi asile maana yake ni kwamba afe kwasababu ni mvivu.
 
Kuhusu utawala majimbo binafsi naona ni muhimu sana, ila hasa hapa kamanda unaongelea autonomy ya maeneo husika kujiamlia mambo yanayowahusu na si kuamuliwa na serikali kuu uaani kutokea dar. Hakuma mwenye uchungu na aibu kwa huyu maskini maana hata hawakutani mara kwanmara, huku kijijini tunakufa ila serikali wala haina taarifa iko mbali sana.

Wametuletea viongozi (mkuu wa mkoa, mkuu wa wilaya, mkurugenzi) wote hao hawana mpango bali wako kazini kama wafanyakazi wengine na si kama viongozi bali ni watawala kwa kutumia nguvu waliopewa na aliyewaleta.

Rais na mawaziri waongoza Dar es salaam na kututmia wateule wao kutuongoza, huwezi amin wakati Rais anzindua daraja la kigamboni wazwazi kwenye vyombo vya hbari na wala haogopi tutamfikiliaje maan sis huku barabara za vumbi hata baiskeli zinapita kwa shida!

Hii nci ni kubwa tukubari tu, majimbo yatatusaidia siso wanyonge. Ila kwa hivi dar tutaamia hata ni kuja kwa miguu na kulala kwenye viabaraza maana pakulala hatutapata mpaka kieleweke maana tumechoka na unyonyaji huu nadani ya nchi moja!
 
Back
Top Bottom