Mwenyekiti wa Chama cha demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe
Mwenyekiti wa Chama cha demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, amesema mbunge mmoja wa chama chake ni sawa na wabunge 30 wa Chama Cha Mapinduzi, (CCM).
Alisema hayo wakati wa uzinduzi wa kampeni ya Chadema iliyofanyika juzi Usa River, wilayani Arumeru.
Katika uzinduzi huo, Chadema kilikuwa kina mnadi mgombea wake Joshua Nassari anayewania kuwa mbunge wa Jimbo
la Arumeru Mashariki kujaza nafasi iliyoachwa wazi na Jeremia Sumari aliyefariki dunia hivi karibuni.
Ninaomba wananchi wa Arumeru, mnipatie Nassari kuwa mbunge , nadhani mmeona kazi za wabunge wa Chadema
wakiwa bungeni, akisimama kutoa hoja utawaona wale wa chama cha magamba wanavyopata shida
mbunge mmoja wa Chadema ni sawa na wabunge 30 wa chama cha magamba, alisema huku akishangiliwa.
Alisema wabunge wa Chadema pamoja na uchache wao bungeni, lakini wamekuwa wakiwameza wabunge wa chama tawala wapatao 257.
Alisema endapo Nassari ataingia bungeni, atakuwa ameiongezea nguvu Chadema kwa uwingi wabunge ambapo nguvu yake itakuwa sawa na wabunge magamba wa CCM 30, alisema na kuongeza kuwa endapo mgombea wake
atachaguliwa chama chake kitakuwa na uwakilishi wa wabunge 49 bungeni.
Mbowe alisema wabunge wa chama chake ni machachari na wamekwenda bungeni kufanya kazi moja tu ya kutetea maslahi ya Watanzania.
CHANZO: NIPASHE