Nassari aanza kuchimba visima
Mbowe ashukuru Wana-Arumeru
Shamrashamra za ushindi zatawala
Mbunge mteule wa Jimbo la Arumeru Mashariki (Chadema), Joshua Nassari (kulia) akiwa na Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, Godbles Lema (Kulia) wakiongoza wafuasi wa chama hicho baada ya Nassari kutanganzwa mshindi wa uchaguzi mdogo wa Jimbo hilo jana.
WasomiI kadhaa wametaja sababu zilizofanya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kushinda uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Arumeru Mashariki lililokuwa likishikiliwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM), kuwa ni pamoja na wananchi kutoona CCM ikijivua gamba kwa vitendo.
Wa kwanza kutaja sababu hizo, ni Mkuu wa Idara ya Sayansi ya Siasa na Utawala ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk. Benson Bana, alipozungumza na NIPASHE jana.
Dk. Bana ambaye pia ni Mhadhiri Mwandamizi wa UDSM, alisema moja ya sababu zilizoiponza CCM kufikia kunyanganywa na Chadema jimbo ililokuwa ikilishikilia, ni kutotekeleza kwa vitendo dhana ya kujivua gamba iliyoinadi kwa wananchi.
Sasa wananchi si wajinga, hawaoni gamba limetoka, alisema Dk. Bana.
Alisema sababu nyingine inatokana na CCM kukaa madarakani muda mrefu, jambo ambalo alisema halikubaliani kabisa na hulka ya binadamu, hasa vijana ambao siku zote hupenda mabadiliko.
Na vijana si kwamba wako mijini tu, wako hadi vijijini pia. Wanafuatilia mambo, wanasoma magazeti, wanasikiliza redio, alisema Dk. Bana.
Alitaja sababu nyingine kuwa ni mikakati mizuri ya ushindani wa kisiasa iliyonayo Chadema, ikiwamo kujitambulisha katika makundi maalum katika jamii tofauti na CCM ambayo alisema imebaki na fikra mgando ya kutegemea wakulima na wafanyakazi.
Alisema pia Chadema imefanikiwa kuwa na mikakati mizuri ya kuendesha kampeni za kisiasa, ikiwa ni pamoja na matumizi ya helikopta ambayo imekiwezesha kuwafikia wananchi kirahisi vijijini.
Sababu nyingine alisema ni Chadema kujikita zaidi katika kunadi sera zinazoeleweka kwa wananchi.
Alisema Chadema imekuwa na mwenendo huo tangu katika kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 ambao uliipa mafanikio makubwa katika medani za kisiasa nchini.
DK. LWAITAMA: SIOI HAKUWA MGOMBEA MBADALA
Naye Mhadhiri Mwandamizi wa UDSM, Dk. Azaveli Lwaitama, alisema CCM ilikosea kumteua Sioi Sumari kuwa mgombea wake wa ubunge jimboni humo.
Dk. Lwaitama alisema uteuzi huo haukuungwa mkono na wananchi kwani walidhani kwamba, lengo la CCM lilikuwa ni kutaka kuendeleza siasa za kifamilia.
Alisema pia vyombo vya juu vya maamuzi vya CCM havikuangalia wananchi kuwa wanamuona Sioi kama ni gamba kutokana na kuwa sehemu ya watu wanaotajwa kuwa ni magamba ndani ya CCM.
Dk. Lwaitama alisema sababu nyingine, ni timu ya watu waliopelekwa na CCM Arumeru kumnadi Sioi, kama vile Livingstone Lusinde, Stephen Wasira na Mwigulu Nchemba, kwamba hawakuwa makini katika uendeshaji wao wa kampeni, hali iliyofanya CCM ionekane kuwa ni chama cha wahuni.
Alisema pia baadhi ya maneno yaliyotamkwa na Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa, juu ya mtoto wa ndugu wa Mwalimu Julius Nyerere, Vincent Nyerere, hayakuifurahisha familia yake (Mwalimu Nyerere) kwa kuwa yalitaka kuigawa.
MOLLOIMET: NI SIASA ZA GHILIBA
Mbunge wa zamani wa Monduli (CCM), Luteni Leipilal Ole Molloimet, alisema ushindi wa Chadema ni matokeo ya siasa za ghilba na uongo zinazoendeshwa na watawala.
Akizungumza kwa njia ya simu kutoka kijijini kwake Isinya-Meremeta wilayani Longido jana, Ole Molloimet, alisema wananchi wamechoshwa na siasa hizo zinazoenezwa na CCM na serikali yake, hivyo kuona haja ya kuwa na mbadala wa viongozi.
Ole Molloimet aliyewahi pia kuwa Mkuu wa Wilaya akihudumu katika wilaya saba tofauti, alisema kampeni zilizofanywa na CCM hazikugusa matakwa ya wapigakura.
Alisema walioshiriki kuzifanikisha kampeni hizo, akiwemo Mkapa, walishindwa kuzungumza ukweli unaohusu maisha ya wananchi wa jimbo hilo, badala yake wakajikita kwenye kauli na ahadi za uongo.
Mkapa alienda Arumeru Mashariki bila kujua kwamba CCM wanampoteza, kwa maana matatizo yaliyopo kule yalikuwepo tangu yeye (Mkapa) akiwa madarakani na hakuyatatua kwa miaka 10 ya utawala wake, alisema.
KAULI ZA WABUNGE WA CCM
Mbunge wa Mwibara (CCM), Alphaxard Ligora, alisema: Kwa hakika CCM tumepigwa, lakini ni sehemu ya kujiandaa na kujiimarisha zaidi.
Mbunge wa Lulindi (CCM), Jerome Bwanausi, alisema ushindi wa Chadema dhidi ya CCM ni ishara ya kushamiri demokrasia na uhuru wa kufanya uamuzi kwa wananchi.
NASSARI ATANGAZWA MSHINDI
Mgombea wa Chadema, Joshua Nassari, alitangazwa mshindi wa ubunge Jimbo la Arumeru Mashariki baada ya kupata kura 32,972 kati ya kura 60,699 zilizopigwa.
Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo hilo, Trasias Kagenzi, alitangaza matokeo rasmi ya uchaguzi huo, kuanzia saa 12:14 juzi asubuhi.
Mshindani wake wa karibu, Sioi Sumari kupitia CCM, alipata kura 26,752 wakati Mazengo Adam wa AFP alipata kura 139, Mohamed A Mohamed wa DP (77), Hamis Juma Kiemi wa NRA (35), Kirita Moyo wa SAU (22), Abraham Chipaka wa TLP (18) na Charles Msuya wa UPDP (18).
Kagenzi alisema idadi ya kura halali zilikuwa 60,038 wakati 661 ziliharibika. Watu 127, 455 walijiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapiga kura.
Mbwembwe zilianza kuanzia usiku wa kuamkia jana, baada ya maelfu ya wakazi wa maeneo hayo na kutoka maeneo jirani ya Arusha mjini na mkoani Kilimanjaro kuanza kuonekana kwa wingi kuanzia saa 12:00 baada ya kuanza kupata matokeo ya awali ambayo yalionyesha kuwa kwenye vituo vingi mgombea wao alikuwa akiongoza.
Katika ukumbi wa Mamlaka ya Mji Mdogo wa Usa River, ambako ndio majumuisho ya kura yalikuwa yakifanyika, viongozi na wapambe wa CCM hawakuonekana isipokuwa mawakala wao.
Badala yake eneo hilo lilikuwa na wapenzi wengi na viongozi wa ngazi mbalimbali wa Chadema akiwemo Mwenyekiti wa Taifa, Freeman Mbowe na wabunge.
Majira ya saa 6:00 usiku Sumari aliingia katika viwanja vya ofisi hizo ambavyo vilikuwa vimejaa askari wengi kutoka Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU).
Baada ya kuingia kwenye ukumbi ghafla salamu ya Peoples ilipigwa na kuitikiwa na wanachama wao kwa sauti kubwa ya Power.
Sauti nyingine ilisikika kutoka kwa Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema akisema na kuitikiwa, wao wana fedha, sisi tuna Mungu.
Sumari ambaye alionekana kutokuwa na furaha hakuweza kukaa ndani ya ukumbi huo kwa muda mrefu na alitoka nje mara kadhaa kabla ya kutoka kabisa majira ya saa 10:00 na hakurudi tena hapo.
Msimamizi wa Uchaguzi wa jimbo hilo, Kagenzi, baada ya kumtangaza Nassari kuwa mshindi alimkabidhi hati maalum ya utambulisho kuwa ndiye mbunge.
Katika hati hiyo, Sumari au wakala wake yeyote hakusaini. Wagombea wengine wa vyama vya NRA, TLP na UPDP nao pia hawakusaini hati hiyo.
Akizungumza baada ya kukabidhiwa hati hiyo, Nassari alisema: Tulianza na Mungu na tumemaliza na Mungu
sio tu kwa kura peke yake bali tutafanya hivyo hata kwa masuala ya maendeleo pia.
Alimshukuru Mungu kwa kumwezesha kuwa na maono ya kuwa mbunge, na akakishukuru chama chake kwa kumpa idhini ya kuwa mgombea wa kiti hicho na akawashukuru pia wapigakura kwa kumchagua.
Aliwashukuru pia polisi kwa kufanya kazi kubwa ya kusimamia ulinzi wakati wote wa kampeni za uchaguzi na hata wakati wa upigaji kura.
Hata hivyo, alimwomba Kamanda wa Polisi wa Wilaya ya Arumeru, kuwaachia huru wapenzi wa chama hicho waliokamatwa usiku wa kuamkia jana kwa madai ya kufanya fujo na mikusanyiko.
Alisema angependa kusherehekea ushindi wake akiwa pamoja na waliokamatwa na kuwekwa rumande.
Aliahidi kuwa vipaumbele atakavyozingatia katika kipindi chake ni kutafuta ufumbuzi wa ardhi, maji, elimu na kuanzisha mfuko wa maendeleo wa vijana na wajane.
Aidha, alisema leo ataanza kazi rasmi kwa kuchimba visima viwili vya maji katika kata ya Mororoni.
Aliwahamasisha wafuasi hao kujitokeza kwa wingi kwenda kufanya kazi hiyo, ambapo alisema tayari amekwishapata fedha kwa ajili hiyo kutoka kwa Mbunge wa Moshi Vijijini, Philemon Ndesamburo (Chadema).
Baada ya kumaliza kuzungumza, wafuasi hao walianza kuimba nyimbo nyingi za tambo dhidi ya mafisadi, huku wakisema mwisho wa CCM umefika.
Baadhi walikuwa wakisikika kwamba wamepunguza idadi ya mafisadi na wasingependa kuona wanaoshika nafasi za uongozi kuwa ni watu wa aina moja tu.
Kulikuwa na idadi kubwa ya magari, pikipiki na watu waliokuwa wakitembea kwa miguu kutoka kwenye viwanja vya ofisi hizo hadi ofisi za Chadema zilizopo umbali wa karibu kilomita tano hivi.
Wengi wao wakionekana kuwa ni vijana waliokuwa waakiimba, kucheza na kushangilia ushindi wao, huku wakisema wanataka kumfanyia sherehe kubwa ya kumpongeza.
Ushindi wa Nassari umepokewa vema na wakazi wengi wa Jiji la Arusha, huku baadhi yao wakisema wamefanikiwa kuwa na ukanda wa majimbo ya Chadema kuanzia Karatu, Arusha Mjini, Arumeru Mashariki, Hai, Moshi na Rombo.
CCM YAKUBALI KUSHINDWA, YAIPONGEZA CHADEMA
Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimekubali matokeo ya uchaguzi huo na kumpongeza Nassari kwa ushindi.
Pia kimewapongeza wananchi wa jimbo hilo kwa kumchagua Nassari na kuwatakia kila la heri, na kimemtaka mbunge huyo pamoja chama chake kutimiza ahadi walizozitoa kwa wananchi.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema kuwa CCM kinakubali matokeo hayo na kuwa kinaamini matokeo hayo ni sauti ya wana-Arumeru na ni uungwana kukubali matakwa ya wananchi.
Tunaipongeza Chadema na wana Arumeru na sasa CCM inajipanga upya na kuangalia wapi tulipoteleza ili 2015 tulikomboe jimbo letu, hivyo tuache maneno na mijadala tukawatumikie wananchi, sisi ambao ndiyo wapinzani wao tunasema kuwa tumekubali na yamekwisha, alisema.
Aidha, Nape alisema kuna maoni ya watu wengi hasa kwenye mitandao ya kijamii ambayo CCM imeyapokea na itayafanyia kazi.
Akizungumzia matukio mbalimbali yaliyotokea katika mchakato wa uchaguzi huo, ambapo wabunge wawili wa Chadema walijeruhiwa kwa mapanga huko Mwanza, na vurugu zilizotokea mkoani Mbeya, Nape alisema CCM kinayalaani, na kimesikitishwa na matukio yote hayo ya uvunjifu wa amani, na kinawapa pole wote walioathirika kwa namna moja au nyingine.
Kuna wenzetu wametokea na kutuhusisha na matokeo yale, kwa kudai kuwa yalifanywa na vijana wa CCM, siyo sawa, hivyo tuiachie dola ifanye kazi yake, CCM haina mpango wa kufanya mambo kama hayo, alisema.
WENGI WAOGOPA KUPIGA KURA
Idadi kubwa ya wanananchi wameshindwa kupiga kura kutokana na kuogopa wingi wa polisi waliokuwa wanazunguka katika Jimbo la Arumeru Mashariki pamoja na wananchi wengi kutojua haki zao.
Kauli hiyo ilitolewa na mwangalizi wa uchaguzi, Martina Kabisana, wakati akizungumza na waandishi wa habari, baada ya Nassari kutangazwa mshindi.
Alisema idadi kubwa ya wananchi walishindwa kujitokeza kupiga kura kutokana na kuwaogopa askari ambao walikuwa wengi wakizunguka katika maeneo mbalimbali.
Unajua sio watu wote, wapo sawa watu wengine wameshindwa kuja kupiga kura mara baada ya kuona askari wengi wakiwa wanazunguka huku wakiwa na mabomu na silaha, hivyo waliingia woga na ndio maana wakashidwa kuja kupiga kura, alisema Kabisana.
Alibainisha kuwa woga huo unasababishwa na kutokuwa na elimu ya kutosha ya kupiga kura na elimu ya uraia.
Pia alibainisha kuwa kuna watu wengi pia ambao walipoteza shahada zao za kupigia kura na hiyo ndiyo sababu kubwa iliyofanya waliopiga kura kuwa wachache kuliko wale ambao wamejiandikisha.
Alibainisha kuwa zoezi lilikwenda vizuri, ila alitoa wito kwa Tume ya Taifa ya Uhaguzi (Nec) kujitaidi kuelimisha wananchi kuhusiana na haki yao ya kupiga kura na kuwahamasisha kutunza shahada zao za kupigia kura.
SHAMRASHAMRA ARUMERU
Mji wa Usa River jana ulitawaliwa na shamra shamra za kila aina, umati mkubwa ulijitokeza kumlaki Nassari, huku mvua kubwa iliyonyesha ikishindwa kuzima sherehe hizo.
Aidha, helkopta ya Mbunge wa Moshi Mjini, Ndesamburo, ikionyesha mbwembwe katika eneo la viwanja vya Shule ya Msingi Leganga Usa River, wakati ilipomleta mbunge huyo.
Wakati burudani za kila aina zikiendelea, Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi, alito burudani ya kuwaburudisha wakazi wa jimbo hilo, ikiwa moja ya kusherehekea ushindi.
Akizungumza jana katika mkutano huo, Mbunge wa Musoma Mjini ambaye alikuwa Meneja kampeni, Vincent Nyerere, alisema kuwa licha ya kupata ushindi, amesikitishwa na kujeruhiwa kwa wafuasi wa chama hicho.
Alisema kuwa pamoja na hila za CCM za kuwateka wafuasi wao na kuwajeruhi, hazikufanikiwa, baada ya kuibuka kidedea kwa kupata ushindi mnono.
Nyerere aliahidi kutoondoka katika jimbo hilo mpaka kesi ya Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, itakapotolewa hukumu Aprili 5, mwaka huu.
Kwa upande wake, Lema, aliomba wakazi wa jimbo hilo kutoa ushirikiano kwa Mbunge wao, ili waweze kuleta mabadiliko ya kweli.
Alisema amefurahishwa kupata Mbunge wa chama chake ambaye anaamini atampa nguvu katika kufanya kazi za kuendeleza taifa.
Alisema kwa ushindi waliopata, umetuma salamu kwa Mbunge wa Monduli (CCM), Edward Lowasa, ambaye alikuja jimboni humo kumnadi mkwe wake, Sioi.
Lema alisema sio salamu kwa Lowasa bali hata kwa Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka, ambaye alimshangaa kwa kusimama bungeni kumrushia makombora Lowasa, lakini baada ya hapo aliambatana naye kumnadi mkwe wake, Sioi.
Mbunge wa Mjini Moshi, Phillimon Ndesamburo, alisema kuwa atatoa ushirikiano kwa kumsaidia Nassari, kujenga visima alivyoahidi katika kata mbalimbali.
Katibu Mkuu, Dk. Wilbroad Slaa, alisema kada mashuhuri wa CCM na mfadhili wa Chadema, ambaye ni mfanyabishara, Mustafa Sabodo, amempongeza Nassari kwa ushindi huo, na ameahidi kumsaidia uchimbaji wa visima vinne alivyoahidi katika kata za jimbo hilo.
Dk. Slaa alichukua nafasi ya pekee kumkabidhi Kiongozi wa kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe, kumlea Nassari bungeni na kumtaka ampe ushirikiano wote ili aweze kutimiza ahadi zake za Arumeru Mashariki.
Huyu mtoto mdogo anahitaji maziwa na mumpe ushirikiano wote, mkishirikiana na Mkurugenzi wa wabunge wa Chama chetu, John Mrema, sababu mtoto anahitaji maziwa ili kukua, alisema.
Dk. Slaa alisema ushindi wa Chadema katika jimbo hilo na katika kata tatu ni hukumu dhidi ya uwongo na ufisadi na utawala mbovu.
Mwenyekiti Mbowe, alisema uchaguzi huo wameweza kushindana na fedha chafu, nguvu za dola na nguvu za wachawi, ila kwa sababu ya kauli na nguvu ya Mungu wameibuka na ushindi.
Alisema kuwa wamempokea Nassari kwa mikono miwili na wiki ijayo watakwenda naye bungeni kuapa na kuanza kazi mara moja.
Lakini nachukua nafasi hii kumkabidhi Mheshimiwa Lema Joshua aje naye bungeni, ili sisi tukaandae mapokezi ya kila aina kwa mbunge huyu na wapenzi wa chama watakaomsindikiza, alisema.
Mbowe alisema kuwa ushindi wa Nassari unahitaji kumpa ushirikiano mkubwa kwa kumwombea, ili aweze kuleta ushindi ambao utaingiza wabunge wengine watakaoleta harakati bungeni.
Aidha alitumia muda huo kuwashukuru Watanzania, waliochagua madiwani katika kata tatu nchini, ambapo alisema katika maeneo yote waliyoshinda mabomu yamepigwa na watu wameumizwa na kuibuka washindi.
Hizi ni salamu kwa Jeshi la Polisi na napeleka salamu kwa IGP Mwema, kwamba wafahamu hao wanaowapiga mabomu leo kesho watakauwa viongozi wao, hivyo natoa wito tusigombane leo kwa sababu ya vyama vya siasa, tunapaswa kuweka tofauti zetu pembeni, alisema.
Aidha alimuasa Nassari kutenda haki kwa wakazi wa jimbo lake, bila kubagua wafuasi wa chama chochote na kuwaasa wabunge wengine na viongozi kuacha kubweteka kwa kujipongeza, bali wanapaswa kuanza kazi ya kutafakari kazi ya uandikaji Katiba Mpya kwa ajili ya ukombozi wa taifa.
Baada ya Bunge hili tunaenda kuanza kampeni, katika mikoa yote ili kuwaeleza wananchi dhamira yetu, lakini tunataka kudhihirisha utawala wa Mungu katika nchi hii, katika uandikaji wa katiba mpya, pia tunataka kuamsha mwamko wa utawala ambao leo umejisahau, alisema.
Pia alipongeza Kata ya Mbuguni, Maji ya Chai, Poli, Kingori, lakini kata za Usa River idadi ya wapiga kura ilikuwa chache, hali iliyoonyesha wengi waliuza shahada zao.
Naomba hili lisijirudie tena, tusiuze shahada zetu na kubaki kuwa washangiliaji tu, haitasaidi kitu pasipo piga kura, alisema.
Kwa upande wa Vijana aliwataka wawe na uvumilivu wa kutunza shahada zao, hivyo aliwataka kuwa makini mwakani 2013 kwa kujiandikisha katika daftari la wapiga kura.
Nawaomba mwakani mjitokeze kwa wingi mjitokeze kujiandikisha katika daftari hili, ili kuleta mabadiliko katika taifa letu na muhimu sana kwa hili, kwani njia pekee ni kujiandikisha kwa wingi kuleta mabadiliko kwa Taifa letu 2015, alisema Mbowe.
Mbowe aliwapongeza wafuasi zaidi ya 200 wa Chama hicho, waliotoka katika mikoa mbalimbali nje ya Arumeru kwa ajili ya kuhakikisha ushindi unapatikana kwa kuishi katika vijiji kwenye kata mbalimbali za jimbo hilo.
Nassari alisema mwaka 2010 alipoamua kugombea ubunge akiwa kijana mdogo, alikwenda kwa Godbless Lema kuomba ushauri wa kugombea nafasi hiyo.
Alisema Lema alimshauri akapambane katika chama na akipitishwa kura za maoni, amfuate atampatia Sh. milioni kumi na alipomfuata baada ya kupitishwa Lema alichukua karatasi alimwandikia tumaini, jipe moyo na utashinda, akampa akamwambia hiyo ndiyo milioni kumi.
Alisema kuwa baada ya kutangazwa kuwa Mbunge alishangilia kwa dakika 15 na baada ya hapo alikosa raha na kuanza kuwaza jinsi ya kuyatatua matatizo ya Arumeru, hasa kwa wamama wanaonyanyasika, vijana na wazee, hivyo aliomba ushirikiano ili aweze kutatua changamoto zilizopo.
Naomba mnitie moyo na kuna kata nimeshinda na kuna kata nimeshindwa, lakini kwa kuonyesha upendo nitaanza na kata walizonipa kura chache, lakini nashukuru sana leo mmetuma salama kuwa hata mtoto wa maskini anaweza kuwa kiongozi, alisema.
Imeandikwa na John Ngunge, Salome Kitomari, Restuta James, Cynthia Mwilolezi na Woinde Shizza, Arumeru; Samson Fridolin, Muhibu Said na Mashaka Mgeta, Dar.
SOURCE: NIPASHE