Waziri wa zamani katika Serikali ya Awamu ya Pili na ya Tatu, Mateo Qaresi.PICHA|MAKTABA
Na Joseph Lyimo, Mwananchi
Posted Jumapili,Novemba23 2014 saa 10:38 AM
Kwa ufupi
Kauli hiyo ya Qaresi imekuja wakati makada mbalimbali wa CCM wameshatangaza nia, wengine wakitajwa kutaka kuwania nafasi hiyo ya juu zaidi katika uongozi nchini.
Babati. Waziri wa zamani katika Serikali ya Awamu ya Pili na ya Tatu, Mateo Qaresi amesema kuwa Chama cha Mapinduzi (CCM) kwa sasa hakina mgombea mwenye sifa ya kuwa rais wa awamu ya tano wa Tanzania.
Qaresi ameyasema hayo hivi karibuni mjini Babati katika mahojiano maalumu na gazeti hili, ambapo alidai kwamba CCM kwa sasa imepoteza sifa zote za kutawala kwa sababu hakina tena misingi ya kuwatetea wafanyakazi na wakulima bali sasa ni chama cha matajiri.
Mwanasiasa huyo ambaye pia aliwahi kuwa mbunge wa Babati kwa tiketi ya CCM, alisema kuwa chama hicho hakiwezi kutoa rais bora anayeweza kuwavusha Watanzania walipo sasa na kuwapeleka mahali pazuri zaidi kwa sababu ina viongozi wasiojiamini, hawawezi kutoa uamuzi mgumu katika kuendesha nchi.
Mpaka sasa kwa watu wanaotajwa tajwa kuwa watawania urais kwa CCM, mimi naona hakuna mwenye sifa kwa sababu CCM haiwezi kumpitisha kiongozi mzuri na mwadilifu kwa kuwa watu wanatumia fedha na huwezi kupata kiongozi mzuri kwa kutumia fedha, alisema Qaresi na kuongeza:
Kuna ambaye ameshatangaza kwamba mwakani atagombea urais na ameshatenga fedha za kufanyia kampeni kwani ameanzisha kampuni yake na hana tatizo, fedha anazo za kutosha. Maana yake nini? Kwamba ana uwezo wa kuwahonga watu, sasa mtu wa namna hiyo anafaa kuwa rais?
Kauli hiyo ya Qaresi imekuja wakati makada mbalimbali wa CCM wameshatangaza nia, wengine wakitajwa kutaka kuwania nafasi hiyo ya juu zaidi katika uongozi nchini.
Baadhi ya waliotangaza nia ni January Makamba ambaye ni Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Mbunge wa Nzega, Dk Hamisi Kigwangallah.
Pia, wanaotajwa yumo Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye, Stephen Wasira ambaye ni Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Rais, Dk Asha Rose Migiro, Waziri wa Sheria na Katiba na Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja.
Hata hivyo, Qaresi alisema kazi ya urais ni ngumu na siyo ya mchezo kama wanavyodhani baadhi ya watu ndio maana utaona kuwa mtu hajamaliza hata miaka mitano katika ubunge, anatangaza nia ya kutaka kugombea urais.
Miaka mitano hajaimaliza anataka kugombea urais, wakati hana historia kubwa ya uongozi. Wengine wanajulikana kuwa wana kashfa nyingi, lakini bado wanataka nafasi hiyo, alisema.
Alisema kwamba nchi ikipata rais legelege, haitachukua muda mrefu itachafuka, kwani ataendeleza mambo ya kilegelege yanayoendelea na kuacha watu wenye fursa waifisidi nchi hii kwa kuwa hakuna mtu anayewachukulia hatua.
Hivi sasa tangu juu mpaka chini, hakuna kinachoendelea. Watendaji wengi wamekata tamaa, uwajibikaji umekuwa duni, kwani watu wanakwenda tu kazini, ili mradi wanapokea mshahara. Tukimpata rais legelege, hatuna miaka miwili nchi itachafuka, alisema Qaresi na kuongeza:
Qares: CCM hakuna anayefaa kuwa rais - Kitaifa - mwananchi.co.tz