Bunge linapokuwa mchezo wa kuigiza
na
Freeman Aikaeli Mbowe
Naam, hatimaye Bunge wiki hii linamaliza mkutano wake wa nane ambao pamoja na mambo mengine umepitisha bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2002 - 2003. Mimi pamoja na Waheshimiwa wenzangu tunafungasha kurudi majimboni mwetu.
Kwa takriban miezi miwili mimi na Waheshimiwa wenzangu tumebebeshwa makabrasha mbalimbali yenye taarifa kadhaa za serikali na asasi zake. Lengo (angalao) ni kujua kilichofanyika katika mwaka wa fedha uliopita na kadhalika mipango ya Serikali katika mwaka ujao wa fedha. Kwa mzigo huu wa makabrasha, hata mikono imeshupaa kidogo!
Msema kweli ni mpenzi wa Mungu. Nina hakika asilimia 75 ya makabrasha haya hayafunguliwi achilia mbali kusomwa. Yote haya husababishwa na kupewa pengine kwa makusudi makabrasha haya siku hiyohiyo ya Waziri kuwasilisha hoja yake. Wabunge wachache hupata nafasi ya dakika zisizozidi 15 kuchangia Wizara hiyo kwa siku hiyo hiyo moja.
Gharama ya kuchapisha na "kubind" makabrasha haya ni mzigo mkubwa kwa Serikali na hivyo mlipa kodi! Si unajua tena! "Mnoko" mkabidhi lundo la makabrasha dakika za majeruhi na lazima atalewa.
Mada yangu ya leo inalenga kwenye kujadili kama miezi miwili tuliyolipwa (labda tuliyojilipa) posho kwa kutumia kodi za wananchi tumefanya kazi waliyotutuma au tumekuwa tunaigiza mchezo wa luninga.
Kabla sijaingia kwenye uchambuzi wa kina wa ni kwanini naamini kuwa bunge letu leo ni "Talk Show" nitapenda kuainisha majukumu ya nguzo tatu za utawala wa nchi yetu kama ilivyo kwa nchi nyingine zenye kuamini dhana ya utawala bora na demokrasia. Ikumbukwe kuwa kuamini ni suala moja na kutekeleza ni jingine.
Napenda kunukuu vifungu viwili vya kwanza vya utangulizi wa Katiba yetu vinavyoainisha misingi yake:
"...Kwa kuwa sisi wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tumeamua rasmi na kwa dhati kujenga katika nchi yetu jamii inayozingatia misingi ya uhuru, haki, undugu na amani:
Na kwa kuwa misingi hiyo yaweza tu kutekelezwa katika jamii yenye demokrasia ambayo serikali yake husimamiwa na bunge lenye wajumbe waliochaguliwa na linalowawakilisha wananchi, na pia yenye mahakama huru zinazotekeleza wajibu wa kutoa haki bila woga wala upendeleo wowote..."
Kwa tafsiri hii basi, bunge lina wajibu mkubwa kwa niaba ya Watanzania wa kutunga sheria na hatimaye kisimamia Serikali katika utendaji wake wote. Sura ya tatu , Sehemu ya kwanza Ibara ya 62 mpaka 65 ya katiba yetu inaainisha waziwazi madaraka haya ya Bunge juu ya Serikali. Aidha, Rais kama kiongozi mkuu wa Nchi ni sehemu ya Bunge.
Serikali nayo ina wajibu wa kusimamia na kutekeleza pamoja na mambo mengine maagizo ya Bunge. Aidha ina wajibu wa kusimamia ulinzi na Usalama wa nchi, raia wake na mali zao.
Kwa upande wake, Mahakama ina wajibu wa kusimamia haki kwa mujibu wa sheria zilizotungwa na Bunge chini ya Sheria Mama ambayo ni Katiba ya Nchi.
Naam, kinachoendelea leo ndani ya Bunge letu ni kinyume na msingi wote wa Katiba na dhana nzima ya Bunge kusimamia Serikali.
Shughuli za kila siku za Bunge husimamiwa na kanuni ambazo Bunge linajitungia lenyewe. Kanuni za Bunge letu leo ndiyo chimbuko (naamini la makusudi) la kupoka madaraka ya Bunge na hatimaye kugeuza Bunge kuwa mchezo wa kuigiza.
Kanuni ya 13 (1), (2) na (3) ya kanuni za Bunge inatambua uwepo wa Kamati za wabunge za vyama. Kimsingi, sina tatizo na uwepo wa kamati za vyama. Usongo wangu ni pale vikao hivi vinapotumika vibaya kupoka maslahi ya Umma kwa dhamira ya kudumisha maslahi ya "Status Quo." Ni katika vikao hivi wanasiasa wenzetu hawa wanadhihirisha Siasa Si Hasa. Wakileta "fyoko", huitwa kwenye vikao hivi na wakitoka ndani huwa kama wamemwagiwa maji ya barafu na ukiwasalimia pengine hata majibu wasikupe kwani wakionekana watahusishwa na wapinzani!
Tunachoambiwa ni kuwa Bunge letu limeiga utaratibu huu wa kisekta kutoka Bunge la India. Aidha, kanuni zetu nyingine zinatokana na kanuni za mabunge mengine ya Jumuiya ya Madola (Commonwealth) ikiwemo Bunge la Uingereza. Spika wetu ni Mwenyekiti wa Mabunge ya Jumuia ya Madola. Spika wetu ni mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM vilevile. Utajazia mwenyewe!
Ndiyo, tunaweza kudai kuwa Bunge letu linaongozwa na mfumo unaoitwa "Three Line Whip". Utaratibu huu unawezesha vyama vyenye wabunge kusimamia wabunge wake. Ni vyema ieleweke kuwa kwa wenzetu waliokomaa kidemokrasia huwathibiti Wabunge wao kwenye masuala ya sera tu na sio Uhuru na Haki yao kuhoji mienendo ya uendeshaji wa Serikali. Kwa Bunge letu, utaratibu huu unatumiwa kuwafunga Wabunge midomo. Hivyo, la msingi hapa ni Je? Mfumo huu wa Bunge una maslahi kwa Taifa letu au unang'ang'aniwa kudumisha maslahi na matakwa ya viongozi wakuu?
Pamoja na Bunge kuwa na mamlaka ya kujitungia kanuni zake yenyewe kwa mujibu wa kifungu namba 89(1) na (2) cha katiba ya nchi; kanuni hizi hazistahili kupoka uhuru wa msingi wa Kikatiba wa Bunge kusimamia Serikali. Wakati huo huo Kanuni hazistahili kupoka Uhuru na Haki za msingi za Kikatiba za Wabunge kutoa mawazo yao kwa uhuru bila kuathiriwa na mizengwe ya kamati za wabunge kama vyama vya siasa. Kadhalika hata vyama vyenyewe ambavyo tiketi zake zimewawezesha wabunge kuingia Bungeni havina haki kikatiba kupoka Uhuru wa kutoa mawazo wa wabunge wao.
Bila kujali msimamo wangu au ule wa Waheshimiwa Wabunge wenzangu wa Vyama vyetu vya Mageuzi (ambao kiukweli tunaburuzwa Bungeni kutokana na uchache wetu) wote tunastahili lawama labda kwa kutokazana kuwaambia Watanzania kwa kina jinsi Bunge letu leo lilivyofanywa mchezo wa Luninga.
Aidha, baada ya kutafakari kwa kina mwenendo wa Bunge tangu niingizwe na wale wapenzi wangu wa Hai (Mungu awabariki sana), leo nadiriki kusema kuwa ADUI namba moja wa maslahi ya Watanzania sio Serikali yao bali ni Wabunge wa Chama cha Mapinduzi ambao kwa udhaifu, woga na labda ubinafsi wao wanaruhusu Serikali yao iburuze Bunge wao wakiwamo!
Nasema hivyo kwa sababu wao ndio wengi bungeni na Katiba ya nchi imewapa Wabunge mamlaka yote ya kudhibiti Serikali. Aidha, kanuni hizi za Bunge zinazopoka madaraka yake zinapitishwa na wabunge hawa hawa wa CCM walio wengi Bungeni.
Kwa udhaifu huu wa Wabunge wa CCM, leo kimsingi Bunge haliwezi kubadilisha mipango yeyote ya Serikali. Uhuru kidogo wa mawazo na mapendekezo hutolewa katika kamati za Kisekta. Bunge letu leo lina Kamati Nane za Kisekta. Kila Mbunge anakuwa kwenye kamati mojawapo ya kisekta. Kamati hizi zina wastani wa wabunge 30 kila moja. Kwa mantiki hii basi anapata wasaa wa kunusa angalao kidogo moja ya nane ya shughuli za Serikali! We fikiria, Wataalam "waliobobea" wa Serikali hutayarisha bajeti zao kwa miezi kadhaa na kutayarisha "misaafu" ya maelezo. Kamati ya Kisekta ya Bunge hupitia "misaafu" hii kwa siku moja kwa kila Wizara na kisha utasikia "...Ipiteee!!!" Hapo utawaona wataalam wa wizara wakiangaliana na wakati mwingine kama kuonyeshana ishara kuwa Waheshimiwa hawa hawajui wafanyalo. Hata wakijua, Muda uko wapi?
Kundi hili la wabunge 30 likishapitisha bajeti ya Wizara Fulani kundi lingine lote la Wabunge zaidi ya 250 halina tena mamlaka ya kubadilisha chochote ila hubakia kuigiza mchezo wa luninga ambao hauna tofauti na porojo. Piga kelele hata upasuke koo; unafurahisha genge!
Hali hii imepelekea kuua ari ya wabunge ya kuchambua kwa kina mwenendo mzima wa Bajeti ya Serikali. Aidha hali hii imegeuza Bunge letu chanzo cha ajira na posho kuliko kufanya kwa dhamira yale umma wa Watanzania wangetegemea Bunge lao lifanye.
Kwa upande mwingine, Serikali kwa kujua Bunge lina meno ambayo yamegeuzwa ya plastiki hali heshimu tena Bunge. Inadhubutu kufanya maamuzi na kuletea Bunge kama taarifa. Aidha, hii inapelekea hata baadhi ya Mawaziri kujibu hoja za wabunge kwa dharau na kejeli wakati wa majumuisho ya wizara zao wakijua fika kuwa wabunge wanafanya kazi ya upambe na hawawezi kubadilisha chochote.
Serikali haikuomba Bunge ruhusa ya kununua ndege wala rada. Sio nia yangu kuingia kwenye hoja ya kama kweli ni kipaumbele sahihi kununua vifaa hivi vya bei mbaya kwa kuzingatia umaskini wetu. Ni nia yangu kuonyesha jeuri ya Serikali kudharau Bunge.
Suala la ndege limeletwa Bungeni kama taarifa kuwa Serikali ina mpango wa kununua ndege ya Rais na tayari imeshatenga fedha zake za ndani kiasi cha Tshs 7,000,000,000.00 kama malipo ya awali.
Wapinzani tulikataa katakata mpango huu na hata kutoka nje ya ukumbi wa Bunge. Wenzetu wa CCM walituzomea na hatimaye kuipitisha bajeti nzima ikiwepo mpango huu wa ndege kwa mbwembwe bila hata kuhoji masuala ya msingi kama thamani ya jumla ya ndege, aina ya ndege, itokako na inatakiwa kulipiwa kwa muda gani! Watanzania hili ndilo Bunge lenu mnalodaiwa kulipa ushindi wa kishindo kwa bao la kisigino.
Naomba niweke rekodi sawa. Ninaposema Wabunge wa CCM Watanzania wasifikiri hawa ni watu wasiwasi!
Hili ni kundi kubwa lenye wasomi wengi waliobobea kwenye fani mbalimbali. Vilevile linajumuisha Wazee kadhaa ambao wanaheshimika na jamii ya Watanzania kwani kwa nyakati kadhaa wamekuwa viongozi waandamizi katika Serikali yetu, CCM na Mashirika kadhaa ya Umma bila kusahau taasisi za kimataifa.
Ingekuwa wanakuja Bungeni na vyeti vyao basi ingehitajika masjala kubwa kuliko Bunge lenyewe kizihifadhi. Pamoja na taaluma zao na ukweli kuwa wanatoka miongoni mwa Watanzania ambao ni masikini sana, wenzetu hawa wamekubali kusindikiza hoja za Serikali kwa msemo wao wenyewe; nanukuu "mia kwa mia". Hebu fikiria: Anasimama mtu msomi aliyebobea anapongeza kwa dakika tano, kisha analalamika kwa dakika kumi na mwishowe anaunga mkono hoja asilimia mia kwa mia! Wenzake wanamshangilia! Kasheshe tupu! Hii ndiyo dhana nzima ya Bunge kuwa mchezo wa luninga.
Inaumiza na kusikitisha hali hii inapoendelea kila siku katika Bunge. Hoja za msingi hazionekani. Bunge letu leo linapenda kung'ang'ania vitu "trivial." Hivi kweli sakata la IGP Mahita lilihitaji kuwa hoja ya nguvu kiasi hicho kuliko hata suala la ndege na rada?
Hata wale watani zangu wanaojifanya wao ni wakereketwa sana; mnajua Chama Chenu cha CCM kinapata ruzuku zaidi ya milioni 750 kwa mwezi? Hii ni zaidi ya Shilingi za Kitanzania Bilioni Tisa! Yaani kwa tarakimu ni: Tshs 9,000,000,000.00 kwa mwaka. Je? Mlikwisha ona mapato na matumizi ya Chama chenu? Je? Ruzuku hii inawafikia huko Wilayani na Mikoani?
Nawauliza watani zangu hawa kwani wao ndio wenyewe wa kuomba na hata kulazimisha michango wakati Chama chao kikizoa mamilioni kila mwezi kwenye hazina ya nchi kwa kigezo cha ruzuku ya vyama vya siasa. Hapo ni bila kuongezea "Michango ya Hiari" kutoka kwa wafanyabiashara na asasi mbalimbali zinazobembeleza fadhila kwa gharama za walalahoi!
Kwa sisi Wabunge wa upinzani (bila kuwasahau wachache ndani ya CCM - ambao kamwe hawatajionyesha) kinachoendelea bungeni kinaweza kufananishwa na hali katika eneo la ajali. Katika maeneo ya ajali unaweza kumkuta mtu anakata roho na huna uwezo wa kumsaidia. Aidha, unachanganyikiwa unapomwona kibaka akijaribu kumpora mtu aliyezimia! Mengine utajaza mwenyewe.
Laiti wanamageuzi tena "Viongozi" na "wapenzi wa ruzuku" wangelijua ni mabilioni mangapi yanapotea nchi hii na upinzani ukishuhudia bungeni bila kuwa na uwezo wa kuzuia. Laiti wangejua hiyo chambo ya karoti wanayopewa ya vimilioni wastani wa 20 ni tone la maji baridi ndani ya bahari ya chumvi ili kuhalalisha "Wenzao" kuzoa mabilioni! Ndugu zangu wapinzani njaa isitupe ukomo wa kuona. Tusisahau kuna msemo usemao "Ukimwona adui akililia wembe ameze, mpe ni bwege"
Bunge leo linatumika kuhalalisha jeuri ya Serikali. Kila mara najiuliza : Inawezekanaje wasomi wa nchi hii wakawa "so timid"?
Napenda kuamini kuwa wengi wa wabunge wetu wa CCM wanajaribu kulipa fadhila ya kubebwa na Serikali wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2000. Aidha, sasa naamini adabu hii ya woga (kwa gharama ya Watanzania masikini) inatokana na tumaini la kurushiwa angalao kamkate kadogo kupitia kuteuliwa kushika nyadhifa mbalimbali ikiwemo Uwaziri, wajumbe wa bodi na kadhalika!
Ni ukweli usiofichika kuwa wabunge wenzetu wa CCM wanathibitiwa vilivyo. Mkikutana pembeni hawaishi kulalamika kama vile hawajui upeo wa mamlaka yao waliyopewa na katiba ya nchi. Wanachoamini, Wanachoongea mtaani na wanachofanya Bungeni ni mbingu mbili tofauti.
Siku zote huwa nasema na ninajua msemo huu hauwafurahishi wahusika. "Penye udhia tia Rupia" Kwa vyama vya upinzani ni ruzuku kwa wabunge, ni nyongeza ya mishahara na posho, na kwa wananchi ni Takrima, mashati, fulana na kofia za kijani. Tusidanganyane na kibwagizo cha sera bwana! Kwa mtaji huu lazima watu wapete! Kweli umaskini huzaa umaskini na kujiondoa katika mzunguko huu kunahitaji kazi ya ziada na kujitoa mhanga kwa hali ya juu.
Bunge linafungwa wiki hii na Watanzania walio wengi wanajua kuwa hoja kubwa ya Bunge hili ilikuwa Mahita, Ukarabati wa Ikulu, Rada na Ndege! Sina hakika ni wangapi wanajua kuwa pamoja na majitapo yote ya serikali na jeuri yake ya kulazimisha matumizi ya ajabu ajabu bado kwa kiasi kikubwa inategemea misaada hata kwa kujilipa mishahara!
Sina hakika ni wangapi wanajua kuwa katika mwaka huu wa fedha Serikali yao itatumia zaidi ya shillingi Trillioni 2.2 kujiendesha? Kwa kuweka kwenye tarakimu ni sawa na: Tshs 2,219,212,000,000.00. Katika fedha zote hizi Shilingi bilioni 720 tu ndizo zitatumika kwa matumizi ya maendeleo ambapo kati yake Serikali yetu imechangia Shilingi bilioni 95.662 na wafadhili wamechangia Shilingi bilioni 624.465 kwa njia ya mikopo na misaada.
Hebu wenzetu wa vyombo vya habari sasa wasaidieni Watanzania kwa kuchambua kwa kina undani wa bajeti ya kila idara na Wizara za Serikali badala ya kuendeleza utamaduni uliozoeleka wa kuripoti "Mchezo wa Luninga."
Sasa niwarudie Watanzania na kwa maana hii Watanzania wote bila kujali itikadi zao za kisiasa. Ni lini tutajua kuwa tuna wajibu wa kushiriki "process" nzima ya kukomboa nchi yetu?
Ni lini mtajua kuwa kazi ya kujikomboa kutoka kwenye umaskini sio kazi ya wanamageuzi bali ya Watanzania wote wenye usongo kwa njaa na umaskini unaotukabili?
Ni lini tutajua kuwa Bunge letu ni Mchezo wa Luninga na kamwe kwa uwiano uliopo halitaweza kutetea maslahi ya wanyonge?
Ni lini ndugu zangu wapenzi wa ruzuku mtajua kuwa nguvu ya umma (People's Power) inashinda nguvu ya pesa, jeshi au dola?
Ni lini viongozi wetu watajua kuwa Sauti ya Wengi ni Sauti ya Mungu?
Viongozi wa Serikali na CCM wanastahili kujua kuwa nchi hii imemwagiwa mafuta ya umaskini na majuto. Wananchi walio wengi sasa wanakosa tumaini. Mtu aliyekosa tumaini ni mbaya kuliko Simba aliyejeruhiwa.
Siku masikini hawa wa Tanzania tunaowadhihaki kila siku kwa propaganda ya amani na utulivu (wakati hawana amani ya aina yeyote kwenye kaya zao) watasema basi - mjue hakuna cha mswalie mtume.
Burundi, Rwanda, Siera Leone, Congo na hata Somalia yalianza kidogo kidogo viongozi wakaambiwa na wapambe wao kuwa wasijali, wamevaa suti za hariri na jeshi lina vifaa vya kisasa.
Nimalizie kwa Salaam kwa Mheshimiwa Rais. Ninakupongeza kwa mengi mazuri uliyofanya. Tumia muda wako uliobaki kuweka mazingira ya wewe kuingizwa katika vitabu vya historia ya nchi hii, Africa na Dunia nzima kama "Stateman" na sio "President."
Andaa mazingira mazuri ya kuwezesha uchaguzi ujao kuwa huru na haki kwa kuridhia mabadiliko ya msingi katika katiba yetu ambayo pamoja na mengine yatahusisha Tume huru ya Uchaguzi. Mhe. Rais hakikisha wagombea binafsi wanaruhusiwa ili nchi yetu ipate watu makini wa kushiriki utawala badala ya dhana potofu kuwa wanatakiwa wawe makada na watoke kwenye vyama vya siasa pekee!
Mhe. Rais, achia bunge lako madaraka ya kuthibiti Serikali. Kama Bunge litaachiwa Uhuru wake lifanye kazi bila mizengwe, nakuhakikishia ufanisi wa Serikali yako utaufurahia pamoja na wale wote wenye nia njema na nchi hii. Wasaidizi na wapambe wako wasikuchuuze. Wananchi wako tunataabika sana pamoja na matumaini lukuki yatokanayo na sera zako za kuboresha uchumi.
Maadam wewe ni sehemu ya Bunge, shauri uwepo wa kamati ya Bunge ya kushughulika na Rushwa na hii isimamiwe na wabunge wa vyama vya upinzani kama ilivyo Kamati ya Bunge ya Mahesabu ya Serikali. Tutakusaidia kazi hii ambayo inaonekana nzito sana kwako na wasaidizi wako.
Nawatakia Watanzania wote kila la Heri