Connection ni conspiracy yenye lengo la kuhakikisha masikini anabaki masikini na tajiri azidi kupeta. Kwa kifupi huu ni mpango wa kishetani ambao inabidi upigwe vita kwa nguvu zote. Madhara yake ni.
1. Elimu kuchukuliwa poa.
2. Kutengeneza matabaka masikini na tajiri(Racist)
3. Undugulazition makazini.
4. Kutokuwa na ubunifu makazini sababu kigezo cha kuajiriwa kinakuwa ni undugu
5. Na madhara makubwa kabisa ni VITA za wenyewe kwa wenyewe.
Kiukweli vijana tuliokosa connection tunaumia sana kwa yanayoendelea kwenye ajira na sio kwamba hatuna uwezo hapana Bali uwezo tunao kuanzia darasani(vyeti) mpaka uwezo binafsi ila connection tu ndo inatufanya tuonekane hamnazo.
Tanzania ni yetu sote kama jamii tupinge ubaguzi unaofanyika kwenye ajira.
Habari ya kupata kitu kwa connection inaweza kuwa nzuri au mbaya. Kwenye kazi tunaaswa kutengeneza "professional network", kujuana na watu tutakaoweza kusaidiana nao kitaaluma, kibiashara na kadhalika.
Jambo hili likifanywa kwa nia na njia nzuri, si jambo baya. Maisha hayawezi kuepuka kabisa connection.Kuna watu uliosoma nao, ulioishi nao, uliokua nao, unawajua vizuri.Ukiwa na nafasi ya kufanya kitu unaweza kuwafikiria zaidi kuliko watu ambao huwajui.Hususan nakusudia kuzungumzia watu wenye sifa.
Tatizo linakuja pale connection ndiyo inayokuwa sifa kubwa inayoangaliwa, hata mtu hana sifa anapewa pande kwa sababu ana connection tu.
Hapo tunaharibu kazi.
Katika kitabu chao wasomi wa uchumi Daron Acemoglu (MIT) na James A Robinson (Chicago) "Why Nations Fail: The Origins of Power, Prosperity and Poverty" wamechambua sana sababu nyingi zinazofanya nchi nyingine ziwe masikini na nyingine ziwe tajiri.
Sababu walizozitaja ni nyingi, na chambuzi zao ni ndefu na za kisomi sana kwa mimi kuzifupisha hapa, hivyo kufaidika kabisa kama hujasoma kitabu, kitafute. Ila kitu kimoja kikubwa kabisa walichoandika ni kwamba, nchi zinazokuwa masikini mara nyingi zinakuwa hivyo kwa kuwa na mfumo wa watu kupata fursa kwa connections.
Mfumo huu una tabia hizi.
1. Unapendelea watu kwa connection, si kwa uwezo.
2. Kwa sababu ya 1 hapo juu, unanyima watu wenye uwezo fursa
3. Watu wenye uwezo wakinyimwa fursa, na wasio na uwezo wakipewa fursa kwa upendeleo, mfumo mzima wa uchumi unadorora.
4. Kupendelea watu kwa connections tu, bila kuangalia sana uwezo, kunafanya watu wengi waone kuwa na uwezo hakuna maana na hivyo kutokuwa na nia ya kuwa na uwezo zaidi. Kama watu wanapata kazi kwa kujuana, na wewe hata usome mpaka Ph.D utaachwa tu, watu wengi ambao hawana connection wataona hakuna haja ya kuongeza uwezo.
5. Kupendelea watu kwa connection bila kuangalia uwezo kunaleta matabaka ya walio ndani ya mfumo na walio nje, walio nje wakijiona wametengwa sana, watauhujumu mfumo uanguke ili "malaika waishi kama mashetani..."
6. Mfumo huu unawanyima hata watu ambao wana connections fursa za kujiendeleza zaidi, kwa kuwa wengi wanabweteka kwa kuona hakuna haja ya kujiendeleza kama wanachohitaji ni connections tu. Hata ambao wangeweza kuwa na uwezo zaidi wanabweteka.
7. Mfumo huu unatengeneza matajiri wachache wenye hela nyingi na masikini wengi wanaopigania "hela ya kula". Kiuchumi hii ni hali mbaya, kwa sababu uchumi unategemea sana mzunguko wa fedha unaofanywa na watu wengi. Kama fedha zimefungiwa kwa watu wachache, hazizunguki, uchumi wa nchi utadorora.
8.Mfumo huu ukiendelea sana, under ceteris paribus, unakuja kuzaa maisha mafupi, magonjwa, umasikini, vifungo vya jela zaidi, kukosa elimu, matatizo ya afya ya akili, mimba za utotoni na mapinduzi ya nguvu ya kijamii.
9. Mfumo huu husababisha kutowiana kimilinganyo kwa kiuchumi miongoni mwa jamii (social and economic inequality)
10. Hatima ya mfumo huu ni kwamba hauna manufaa hata kwa wale ambao mwanzoni huwa wananufaika nao. Ndiyo maana matajiri wakubwa wenye akili kina Bill Gates na Warren Buffet wanafanya juhudi za kupunguza inequality.
Binafsi nilikuwa napiga vita sana mfumo huu, ambao nilivyoanza kazi Tanzania ulikuwa umeshika moto.
Kiasi kwamba, nilivyopata kazi yangu ya kwanza, watu wote walianza kuniambia "Mzee (baba yangu) kakuunganishia eeh". Wakati yeye alikuja kuambiwa baada ya mimi kupata kazi.
Nikaona isiwe tabu.
Nikajikata Marekani ambako hanijui mtu na kazi nitakayofanya itatokana na mimi kusimama mwenyewe, wala hakuna mtu wa kuniambia "Mzee kakuunganishia eeh"