rosemarie
JF-Expert Member
- Mar 22, 2011
- 6,887
- 3,412
MBUNGE wa Jimbo la Msalala na Waziri wa zamani wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige, amedai kuwa Chama cha Mapinduzi (CCM) kitakufa kutokana na tabia ya viongozi wake kuendesha chama kwa kuegemea majungu na wivu wa madaraka.Kauli hiyo aliitoa jana katika ofisi za CCM wilaya ya Kahama, mbele ya mwenyekiti wa chama hicho mkoa wa Shinyanga Khamis Mgeja na viongozi wengine wa mkoa na wilaya.Maige alidai kuwa vitendo vya majungu na uongo uliokithiri vimechukua nafasi kubwa kwa baadhi ya viongozi wa ngazi mbalimbali, hali ambayo itasababisha chama hicho kupoteza uwezo wa kuongoza na kuanguka.Alidai kuwa viongozi wachapakazi na wazalendo kwa nchi yao, wamekuwa wakipigwa vita kali na baadhi ya watendaji serikalini, bungeni na ndani ya chama hicho kwa maslahi binafsi.Maige alisema hasikitiki kuondolewa katika nafasi ya uwaziri, bali kinachomuuna ni kutimuliwa bila hata kupewa nafasi ya kujieleza katika ngazi zote husika ndani ya serikali na chama."Sikupewa nafasi yoyote, iwe ni katika kamati za Bunge au ndani ya chama kama zilivyo kanuni zetu. Hakuna aliyetaka kunisikiliza, na wengi waliosikia uzushi wa tuhuma zangu, waliamini na kuchukua maamuzi," alisema.Alidai kwa kipindi chote alichokuwa waziri, alipambana na mambo mengi mazito kwa kuzingatia kuwa wizara hiyo ni nzito na yenye utajiri mkubwa, lakini ameshangaa kuona kuwa mwisho wa uzalendo wake ni kuondolewa kwa aibu."Silalamiki kuondoka kwa vile hiyo ilikuwa ni dhamana, lakini sikufurahishwa kuondolewa kwa tuhuma ambazo kwanza sio za kweli, na pili sikupewa fursa ya kuzijibu kwa ufasaha na kwa uchambuzi makini wa kitaalamu. Hii ni hatari kwa sababu inaua chama kwa kupoteza watendaji wenye uchungu na taifa lao," alisema mbunge huyo.Alilaani kitendo cha baadhi ya wanachama wa CCM kushabikia kuondolewa kwake kwenye uwaziri ambapo walidhihirisha namna ambavyo si wakomavu wa kisiasa kwa kudhani kwamba wanamkomoa pasipo kuzama kwa kina na kubaini kuwa wao ndio watakaoathirika hasa kwa kuwa posho zao na mishahara zinatokana na jimbo hilo kuendelea kuwa mikononi mwa CCM na si vinginevyo.Alidai kuwa fitina na majungu aliyofanyiwa na viongozi wenzake ndani ya chama hicho, yamewakera wana CCM wengi, kiasi kwamba wazee zaidi ya 300 wa jimbo lake wamemfuata wakitaka awaeleze msimamo wake ikiwa atahama ama ataendelea kuwa ndani ya CCM."Wamekuja wazee hawa, wanawake kwa wanaume na vijana wengi, wakisikitika na kile kilichonitokea. Wanataka niwaambie kama nabaki CCM au naondoka, ili nao wanifuate," alisema.Aliongeza kuwa kwa kuwa yeye ni zao la wananchi wa Msalala, ni jukumu la wananchi kumuamlia hatima yake, na yeye atakuwa mtiifu kwao.Maige alidai inasikitisha kuona kuwa kuna nguvu kubwa za upinzani nchini, hususan chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), wakati wao CCM wamekalia majungu na fitina zisizo na maana.Hivyo, ametahadharisha kuwa wana CCM, wasishangae jimbo hilo likichukuliwa na wapinzani katika uchaguzi mkuu ujao, na wala hatakuwa na hasara.Aliongeza kuwa CCM yenye nyenzo zote za usafiri ikiwemo magari na pikipiki, imeshindwa kuhamasisha watu wilayani kote lakini CHADEMA wasiokuwa hata na baiskeli wamepita jimbo zima wakifanya mikutano yao na kugawa bendera zao kama njugu.Maige alimshambulia Mwenyekiti wa Kamati ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, James Lembeli, akidai kuwa alipeleka taarifa ya uongo na iliyojaa unafiki kwa lengo la kumng'oa kwenye uwaziri na kwamba ndio maana baada ya lengo lao kutimia walitimkia Japan kujipongeza.Alimtaka Lembeli ambaye pia ni Mbunge wa Kahama, kwa kuwa ametekeleza lengo lake la kumng'oa kwenye uwaziri sasa waketi meza ya mazungumzo kuwaletea maendeleo wananchi wa Kahama kwa kuwa kabla ya kupata wadhifa huo walikuwa marafiki na walitembea pamoja kwenye majimbo yote ya Kahama na Msalala kwenye mikutano yao.Naye Katibu Msaidizi wa CCM Wilaya ya Kahama, Hamad Masoud, alisema suala la ugomvi kati ya wabunge hao litafikishwa kwenye Kamati ya Maadili ya chama ili liweze kufanyiwa kazi.Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga Khamis Mgeja aliwapa pole wana Kahama kwa kile alichodai kumpoteza mpiganaji, na zawadi kwa wananchi wa eneo hilo, hivyo kuichezea bahati hiyo ni ujinga kwa wale wasiopenda maendeleo."Nafasi hizi hutolewa na Rais na haulizwi; ndivyo hivyo anapoamua kumpumzisha aliyemteua pia haulizwi. Inapotokea eneo kupata waziri ni fursa nzuri ya kupiga hatua katika maendeleo leo Kahama fursa hiyo haipo tena," alisema Mgeja.
Tanzania Daima
Tanzania Daima