• Wasubiri barua zao kujibu mapigo, CCM yawaita Mapacha Watatu
WAKATI Chama cha Mapinduzi (CCM), kikijipanga kuwaandikia barua makada wake watatu wanaotuhumiwa kwa ufisadi, Edward Lowassa (Monduli), Rostam Aziz (Igunga) na Andrew Chenge (Bariadi Mashariki), makada hao wanasubiri kukabidhiwa barua hizo ili watoe kile waliochokiita maamuzi mazito dhidi ya CCM, Tanzania Daima Jumatano limejulishwa.
Makada hao maarufu kwa jina la Mapacha Watatu, wanasubiri kukabidhiwa barua hizo ili wavunje ukimya na kueleza upande wa pili wa shilingi kwa madai kuwa kwenye kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), hakukuwa na azimio lolote lililopitishwa la kuwataka wapewe siku 90 za kujiengua na pia hakukuwa na azimio la kuandikiwa barua.
Mmoja wa makada hao, aliliambia Tanzania Daima Jumatano mjini Dodoma kuwa Rais Jakaya Kikwete na chama chake wamefanya jambo la hatari dhidi yao pengine kwa kujua au kutokujua lakini lazima wajibu mapigo ili jamii ielewe.
"Sitaki kuzungumza sasa hivi na huo ndio msimamo wetu. Waswahili wanasema akutukanaye hakuchagulii tusi, tunaangalia, tunafuatilia kwa karibu mambo yote kuanzia ndani ya vikao hadi sasa kinachoendelea kwenye mikutano ya hadhara hakika ni udhalilishaji wa hali ya juu. Tusubiri barua, tutajua la kufanya," alisema kada huyo, mmoja wa watuhumiwa wa ufisadi.
Aidha, baadhi ya watu wa karibu walidokeza kuwa kitu cha kwanza kinachotarajiwa kufanywa na makada hao mara tu baada ya kukabidhiwa barua zao, ni kurejesha kadi za CCM, hatua itakayofanya wapoteze majimbo yao ya uchaguzi, lakini watahakikisha lazima chama kithibitishe ufisadi wao.
Kada huyo hakutaka kuzungumza kwa undani jinsi walivyopokea maamuzi ya NEC na hatua inayoendelea kwenye mikutano ya hadhara inayohutubiwa na Katibu Mkuu, Willson Mkama, Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, na viongozi wengine wa sekretarieti mpya ambao jana walitua mkoani Iringa.
Katika mikutano ya hadhara inayodaiwa kuwa ni ya kujitambulisha, Nape amekuwa akiwataja Mapacha Watatu: Lowassa, Rostam na Chenge kwamba wametakiwa kujiondoa kwenye ujumbe wa NEC ndani ya siku 90, vinginevyo watang'olewa kwa nguvu.
Nape ambaye hadi sasa bado ni Mkuu wa Wilaya ya Masasi, alienda mbali kwa kusema watuhumiwa hao hivi karibuni wataandikiwa barua na kuorodhesha tuhuma zao; na kusisitiza azimio la NEC la kuwataka wang'oke vinginevyo wataenguliwa na chama.
Hata hivyo, katika hatua nyingine, azimio la kutoa siku 90 kwa watuhumiwa hao wa ufisadi limeibua vita ya kisiasa kati ya mwenyekiti wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete, na makada hao.
Wadadisi wa mambo ya siasa, wanaona kuwa kilichotokea mjini Dodoma ni muendelezo wa minyukano ndani ya CCM kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa 2015 na siku za baadaye pia kwani mkakati wa kujivua gamba, ulipangwa makhsusi kwa ajili ya kuwaengua wao wakati orodha ya mafisadi ndani ya chama hicho ni ndefu.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili na kuthibitishwa na mmoja wa wajumbe wa NEC wanaodaiwa kupanga kusuka mpango huo, umethibitisha pasipo shaka kwamba Rais Kikwete, aliendesha vikao kwa kupanga wajumbe kutoa hoja za kuwang'oa Chenge, Lowassa na Rostam.
Kiongozi mmoja wa siku nyingi wa CCM aliyezungumza na Tanzania Daima Jumatano anasema hoja ya kutaka Kamati Kuu na sekretarieti nzima kujiuzulu, ililenga kuwatema Mapacha Watatu, ndani ya vikao hivyo vyenye nguvu kwa njia ambayo ingemuepusha Rais Kikwete katika lawama za moja kwa moja.
"Chama chenye maadili, falsafa, mwongozo na itikadi, hakiwezi kuwapigia kampeni watu wanaohusishwa na ufisadi kwamba wanafaa huku kikisema hakuna ushahidi, halafu baada ya kupata ubunge na wengine hata kuongoza kamati nyeti za Bunge, chama hichohicho kinawataka watoke kwa madai kuwa hawafai. Ushahidi wa sasa kwamba hawafai, wameupata wapi?" alihoji mjumbe mmoja wa NEC.
Wadadisi wa mambo ya siasa wanaohoji hatua hiyo, wanasema uongozi mpya wa CCM ulipaswa kujikita kueleza matarajio ya chama siku zijazo na mikakati ya kujiimarisha na kueleza maazimio mengine ya NEC.
"Nape na wenzake hapaswi kuendelea kumzungumzia Lowassa na wenzake; haya mambo wameyamaliza kwenye vikao. Wanapaswa kueleza matatizo ya msingi ya chama na taifa kwa ujumla, hasa utekelezaji wa Ilani ya CCM," alisema.
Anasema ingawa wanakubaliana kimsingi na hatua ambazo CCM inatakiwa kuzichukua dhidi ya watuhumiwa wa ufisadi, wanashangazwa na hatua ya Nape kutangaza azimio ambalo si sehemu ya mambo yaliyojadiliwa na kukubalika ama kwa kura au kwa kauli moja na wajumbe wote.
Hatua ya Nape inafananishwa na matukio ya hivi karibuni hususan wakati John Chiligati akiwa Mkuu wa Idara ya Uenezi na Itikadi kwamba amepata kutaja mara kadhaa taarifa isiyo sahihi ya maazimio ya vikao vya Kamati Kuu na Halmashauri Kuu tofauti na kile kilichojadiliwa ndani ya vikao hivyo.
Chiligati alipata kulalamikiwa kwa kutoa taarifa potofu kuhusu maamuzi ya Kamati Kuu kuhusu uamuzi wa ama kuilipa au kutoilipa fidia kampuni ya uzalishaji umeme ya Dowans ambayo inaidai Tanzania karibu shilingi bilioni 100.
Chiligati anatajwa pia kupata kutoa maazimio ya kupotosha wakati aliposoma maazimio ya Halmashauri Kuu ya Taifa kuhusu utata ulioibuka baada ya kukatwa kwa jina la Hussein Bashe katika kinyang'anyiro cha uteuzi wa mgombea ubunge kwa tiketi ya CCM kwa jimbo la Nzega katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana.
WAKATI Chama cha Mapinduzi (CCM), kikijipanga kuwaandikia barua makada wake watatu wanaotuhumiwa kwa ufisadi, Edward Lowassa (Monduli), Rostam Aziz (Igunga) na Andrew Chenge (Bariadi Mashariki), makada hao wanasubiri kukabidhiwa barua hizo ili watoe kile waliochokiita maamuzi mazito dhidi ya CCM, Tanzania Daima Jumatano limejulishwa.
Makada hao maarufu kwa jina la Mapacha Watatu, wanasubiri kukabidhiwa barua hizo ili wavunje ukimya na kueleza upande wa pili wa shilingi kwa madai kuwa kwenye kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), hakukuwa na azimio lolote lililopitishwa la kuwataka wapewe siku 90 za kujiengua na pia hakukuwa na azimio la kuandikiwa barua.
Mmoja wa makada hao, aliliambia Tanzania Daima Jumatano mjini Dodoma kuwa Rais Jakaya Kikwete na chama chake wamefanya jambo la hatari dhidi yao pengine kwa kujua au kutokujua lakini lazima wajibu mapigo ili jamii ielewe.
"Sitaki kuzungumza sasa hivi na huo ndio msimamo wetu. Waswahili wanasema akutukanaye hakuchagulii tusi, tunaangalia, tunafuatilia kwa karibu mambo yote kuanzia ndani ya vikao hadi sasa kinachoendelea kwenye mikutano ya hadhara hakika ni udhalilishaji wa hali ya juu. Tusubiri barua, tutajua la kufanya," alisema kada huyo, mmoja wa watuhumiwa wa ufisadi.
Aidha, baadhi ya watu wa karibu walidokeza kuwa kitu cha kwanza kinachotarajiwa kufanywa na makada hao mara tu baada ya kukabidhiwa barua zao, ni kurejesha kadi za CCM, hatua itakayofanya wapoteze majimbo yao ya uchaguzi, lakini watahakikisha lazima chama kithibitishe ufisadi wao.
Kada huyo hakutaka kuzungumza kwa undani jinsi walivyopokea maamuzi ya NEC na hatua inayoendelea kwenye mikutano ya hadhara inayohutubiwa na Katibu Mkuu, Willson Mkama, Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, na viongozi wengine wa sekretarieti mpya ambao jana walitua mkoani Iringa.
Katika mikutano ya hadhara inayodaiwa kuwa ni ya kujitambulisha, Nape amekuwa akiwataja Mapacha Watatu: Lowassa, Rostam na Chenge kwamba wametakiwa kujiondoa kwenye ujumbe wa NEC ndani ya siku 90, vinginevyo watang'olewa kwa nguvu.
Nape ambaye hadi sasa bado ni Mkuu wa Wilaya ya Masasi, alienda mbali kwa kusema watuhumiwa hao hivi karibuni wataandikiwa barua na kuorodhesha tuhuma zao; na kusisitiza azimio la NEC la kuwataka wang'oke vinginevyo wataenguliwa na chama.
Hata hivyo, katika hatua nyingine, azimio la kutoa siku 90 kwa watuhumiwa hao wa ufisadi limeibua vita ya kisiasa kati ya mwenyekiti wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete, na makada hao.
Wadadisi wa mambo ya siasa, wanaona kuwa kilichotokea mjini Dodoma ni muendelezo wa minyukano ndani ya CCM kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa 2015 na siku za baadaye pia kwani mkakati wa kujivua gamba, ulipangwa makhsusi kwa ajili ya kuwaengua wao wakati orodha ya mafisadi ndani ya chama hicho ni ndefu.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili na kuthibitishwa na mmoja wa wajumbe wa NEC wanaodaiwa kupanga kusuka mpango huo, umethibitisha pasipo shaka kwamba Rais Kikwete, aliendesha vikao kwa kupanga wajumbe kutoa hoja za kuwang'oa Chenge, Lowassa na Rostam.
Kiongozi mmoja wa siku nyingi wa CCM aliyezungumza na Tanzania Daima Jumatano anasema hoja ya kutaka Kamati Kuu na sekretarieti nzima kujiuzulu, ililenga kuwatema Mapacha Watatu, ndani ya vikao hivyo vyenye nguvu kwa njia ambayo ingemuepusha Rais Kikwete katika lawama za moja kwa moja.
"Chama chenye maadili, falsafa, mwongozo na itikadi, hakiwezi kuwapigia kampeni watu wanaohusishwa na ufisadi kwamba wanafaa huku kikisema hakuna ushahidi, halafu baada ya kupata ubunge na wengine hata kuongoza kamati nyeti za Bunge, chama hichohicho kinawataka watoke kwa madai kuwa hawafai. Ushahidi wa sasa kwamba hawafai, wameupata wapi?" alihoji mjumbe mmoja wa NEC.
Wadadisi wa mambo ya siasa wanaohoji hatua hiyo, wanasema uongozi mpya wa CCM ulipaswa kujikita kueleza matarajio ya chama siku zijazo na mikakati ya kujiimarisha na kueleza maazimio mengine ya NEC.
"Nape na wenzake hapaswi kuendelea kumzungumzia Lowassa na wenzake; haya mambo wameyamaliza kwenye vikao. Wanapaswa kueleza matatizo ya msingi ya chama na taifa kwa ujumla, hasa utekelezaji wa Ilani ya CCM," alisema.
Anasema ingawa wanakubaliana kimsingi na hatua ambazo CCM inatakiwa kuzichukua dhidi ya watuhumiwa wa ufisadi, wanashangazwa na hatua ya Nape kutangaza azimio ambalo si sehemu ya mambo yaliyojadiliwa na kukubalika ama kwa kura au kwa kauli moja na wajumbe wote.
Hatua ya Nape inafananishwa na matukio ya hivi karibuni hususan wakati John Chiligati akiwa Mkuu wa Idara ya Uenezi na Itikadi kwamba amepata kutaja mara kadhaa taarifa isiyo sahihi ya maazimio ya vikao vya Kamati Kuu na Halmashauri Kuu tofauti na kile kilichojadiliwa ndani ya vikao hivyo.
Chiligati alipata kulalamikiwa kwa kutoa taarifa potofu kuhusu maamuzi ya Kamati Kuu kuhusu uamuzi wa ama kuilipa au kutoilipa fidia kampuni ya uzalishaji umeme ya Dowans ambayo inaidai Tanzania karibu shilingi bilioni 100.
Chiligati anatajwa pia kupata kutoa maazimio ya kupotosha wakati aliposoma maazimio ya Halmashauri Kuu ya Taifa kuhusu utata ulioibuka baada ya kukatwa kwa jina la Hussein Bashe katika kinyang'anyiro cha uteuzi wa mgombea ubunge kwa tiketi ya CCM kwa jimbo la Nzega katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana.