Love Story: Stolen Love

Tuwaseme

JF-Expert Member
Oct 8, 2014
645
1,188
UTANGULIZI

Mvua ikiwa inaendelea kunyesha, Takribani masaa 12 Toka Angela afikishwe katika Hospitali ya Mkoa wa Iringa, Mlango wa Wagonjwa Mahututi (ICU) Unafunguliwa na Daktari anaonekana akitoka nje. Baadhi ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Tumaini waliokuwepo pale nje, akiwemo Mpenzi wake Martin, Rafiki yake Restuta na Master P, kwa haraka wanasimama na kumfuata kwa lengo la kutaka kujua hali ya Mwenzao.
“Dokta Mgonjwa wetu anaendeleaje” Hilo lilikuwa swali la kwanza kutoka kwa Martin kwenda kwa Daktari.
“Anaendelea vizuri na tunamshukuru Mungu kwamba fahamu zake zimerudi” Alisema Daktari.
“Asante Mungu” Walisikika baadhi ya Wanafunzi wakisema hivyo.
“Vipi tunaruhusiwa kumuona??” Aliuliza Restuta
“Ndio mnaruhusiwa kumuona, isipokuwa Martin na Maria Kama Wapo” Alisema Daktari na Kisha Kuendelea “Hiki ni Chumba cha wagonjwa Mahututi kwa hivyo mtaingia kwa Makundi na hatuhitaji Kelele” Alivyomaliza kusema hayo, Daktari Alirudi ndani ya ICU.
Dada yake na Angela ambaye ni Maria hakuwepo Hospitalini wakati huo na wala hakujali kwa kumsababishia Mdogo wake Maumivu Makali kiasi hicho, alitegemea kupata taarifa zote juu ya maendeleo ya Mgonjwa kutoka kwa Restuta, ambaye Alimtuma kwenda Hospitalini hapo kwa kazi Maalumu.
Lakini kwa Upande wa Martin aliyekuwepo Hospitalini hapo Usiku kucha alishtushwa na Kauli ya Daktari ya kutoruhusiwa kwenda kumuona mpenzi wake Angela.
“Martin Usijali nitaongea nae, kila kitu kitakuwa Sawa” Alisema Restuta kwa sauti ya Taratibu na Kisha Wanafunzi wengine waliokuwepo, walionekana wakianza kuingia ndani ya ICU kwenda kumuona Angela.
Licha ya Kwamba Kulikuwa na Wagonjwa Mahututi Kadhaa ndani ya ICU kwa muda huo, Lakini Walivyofika ndani hawakupata shida kutambua Kitanda alicholala Angela, kwani kilikuwa ni Kitanda cha Mwisho Upande wa Kushoto mwa Chumba hicho, walimkuta Angela akiwa amelala Kitandani ila macho yake yakiangalia Mlangoni kama mtu aliyekuwa akiusubiria Ujio huo.
Mkononi alikuwa amewekwa Dripu ya Maji na Kichwani alionekana kufungwa Bandeji katika ile sehemu iliyopasuka. Kwa kumuangalia tu ilitosha kufahamu ni maumivu kiasi gani alikuwa nayo kwa wakati huo. Alivyowaona wenzie wakiingia na kumzunguka katika Kitanda alicholala, machozi yalianza kumtoka kwa wingi.
“Angela Jikaze Mama Usilie” Alisema Restuta kwa Sauti ya kunong’oneza huku akiwa amemkumbatia pale Kitandani.
“Pole Angela Usijali Utapona” Walisema Baadhi ya Wanafunzi.
“Ahsanteni sana” Angela alisema kwa sauti ya Chini iliyojaa Maumivu huku akijifuta Machozi yaliyokuwa yakiendelea kupenya na kutoka kwenye Kingo za Macho yake.
“Shem Mimi nina Zawadi Yako Kutoka kwa Martin” Alisema Master P huku akimkabidhi Zawadi ya Maua. Martin baada ya kuzuiliwa kuingia ICU kumuona Angela alimuomba Rafiki yake Master P amsaidie kufikisha Maua hayo kwa Angela.
“Kamwambie Siwezi Kuyapokea” Alisema Angela.
“Tafadhali Shemeji Usifanye hivyo” Master P alisisitiza.
Ghalfa, Master P akiwa bado anambembeleza Angela kupokea zawadi hiyo, Martin alifungua Mlango wa ICU na kuingia ndani, moja kwa moja akielekea kwenye Kitanda Alicholala Angela.
“Martin toka Nje Tafadhali” Walisema Madaktari waliokuwemo ndani ya Chumba kile huku wakimfuata Martin kwa Kasi na kumzuia kwa mbele ili asiendelee kwenda kwenye Kitanda alicholala Angela. Kila Mtu aliyekuwemo ICU alishtushwa na Kitendo hicho cha Martin kwani hakuna aliyekitegemea.
“Usitake tutumie nguvu kukutoa nje” Walisema Madaktari wale huku wakimsukuma Martin kuelekea kwenye Mlango wa Chumba hicho.
“Muacheni” Alisema Angela kwa Sauti iliyojaa Maumivu.
Kauli hiyo ya Angela iliwafanya Madaktari wale kumuachia Martin kwenda kumuona. Martin alifika kwenye Kitanda cha Angela akihema na Kumkumbatia Angela huku Machozi yakimtoka kwa Wingi. Kwa Martin kuondoka pale bila kumuona Angela akiwa katika fahamu zake ingekuwa ni Kosa Jingine ambalo hakuwa tayari kulitenda.
Moyo wake ulikubali kosa alilofanya na kumsababishia Mpenzi wake maumivu hayo Makali lakini aliona bado ana nafasi ya kumuomba Msamaha kwa kilichotokea.
“Nisamehe Angela” Alisema Martin kwa sauti iliyochanganyika na Kilio huku akiwa bado amemkumbatia Angela.
“Nilishakusamehe Martin ila Sitaki kukuona, Ninapokuona Unanikumbusha Vitu ambavyo Sitaki Kuvikumbuka” Alisema Angela.
“Unajua kuwa Nakupenda na siwezi kukaa bila Kukuona” Alisema Martin kwa Sauti ya Kunong’oneza.
“Nilikuwa najua Mwanzo ila kwa sasa Sijui, Nadhani Dada yangu Maria anakufaa zaidi kuliko Mimi” Alisema Angela huku Machozi yakimtoka
“Muda wa kuona Wagonjwa umekwisha, Wagonjwa wanataka Kupumzika” Aliingilia kati Maongezi hayo Mmoja kati ya Wale Madaktari Wawili waliokuwa wakimsukuma Martin kutoka Nje. Baada ya Kusikia Kauli hiyo, Wanafunzi wote walimuaga Angela na kuanza kutoka nje ya ICU.


SEHEMU YA KWANZA

Martin Jonathan Chota ni Kijana aliyezaliwa miaka 24 iliyopita katika Kijiji cha Kalenga Mkoani Iringa. Ni Mtoto wa pili na wa Mwisho wa Mzee Jonathan Peter Chota na Bi. Maria Emmanuel Magova. Mtoto wao wa kwanza aliitwa Justine.
Toka akiwa mdogo Martin alikuwa ni kijana mtulivu, msikivu na mnyenyekevu.
Tofauti na watoto wengine wa rika lake, Martin alipenda sana kuimba. Toka akiwa mdogo alidhihirisha uwezo wake wa kuimba. Aliwahi kujiunga na Kwaya ya Kanisani kwao bila kuwashirikisha wazazi wake.
Martin alikuwa ni mwimbaji mdogo kuliko wote katika Kwaya hiyo, lakini watu walivutiwa sana na uimbaji wake. Sauti nzuri, uwezo wake wa kukariri Mashairi na kupiga Gitaa kwa ufasaha vilizidi kumpatia sifa kemkem.
Martin alikuwa tofauti sana na Kaka yake Justine. Justine muda wote alionekana mwenye hasira, mkali, kiburi na mgomvi. Kutokana na vitendo vyake hivyo vya ukatili, watu wengi kijijini hapo walizoea kumuita ‘Nunda’, Jina ambalo lilikuwa maarufu Kijijini Kote.
Justine alifahamika kwa tabia yake ya kupenda kujikweza, ukorofi na ubinafsi. Justine alimchukia mtu yeyote aliyejitokeza kumwonya.
Mara kadhaa alionekana akigombana na wazazi wake juu ya tabia zake hizo lakini hakubadilika. Wazazi wake waliamini tabia zake hizo wenda zilitokana na Justine kuugua sana maradhi ya kichwa, kitaalamu ‘Hemiplegic Migraine Headache’ alipokuwa mdogo kiasi cha wazazi wake kukata tamaa kama mtoto wao angepona.
Martin na Justine walikuwa kama watoto wa wazazi tofauti, walikuwa na tabia zisizoshahabiana. Japo Martin alijitahidi kumheshimu na kumuonesha upendo kaka yake, lakini juhudi zake ziligonga mwamba, Justine hakujali.
Mama yake alijitahidi kumtetea mtoto wake huyu lakini ilifika kipindi alichoshwa na vitendo vyake hasa pale Justine alipokataa kuendelea na masomo ya Kidato cha Tano na Cha Sita licha ya kwamba alifaulu vizuri Mitihani yake ya Kumaliza Kidato cha Nne. Kila siku alikuwa mtu wa matukio na Kila mtu Kijijini Kalenga alimfahamu hivyo.

Pale tabia ya Justine ilipozidi kuwa mbaya zaidi kwa kujihusisha na vitendo viovu kama vile ulevi wa pombe, mihadarati pamoja na kuchanganya wasichana ilipelekea akiwa na umri wa miaka 27 wazazi wake kumfukuza nyumbani.

“Toka nyumbani kwangu nakwambia” Hiyo ilikuwa sauti ya Mzee Jonathan Peter Chota akiongea na Justine siku ambayo Justine alirudi nyumbani akiwa amelewa kupitiliza.
“Haya Maisha tu Mzee” Kwa sauti ya kilevi, akiyumba yumba Justine alimjibu Mzee Jonathan huku akiwa ameshikilia Chupa ya Pombe aina ya ulanzi mkononi.

“Maisha gani kutwa nzima umelewa, mwili mzima unanuka pombe, hukumbuki hata kufanya usafi wa mwili wako, siku ya ngapi leo haujaoga, nakwambia nimechoshwa na tabia zako mbovu, rudi ulikotoka na nisikuone tena nyumbani kwangu” Mzee Jonathan aliendelea kusema huku akimsukuma Justine atoke nje ya uzio wa nyumba yao.

Justine aliyumba yumba mpaka nje pembezoni kidogo mwa ukuta wa nyumba yao akadondoka chini, alijaribu kusimama akashindwa na kuamua kulala hapo. Haikupita muda usingizi Ulimpitia.


*********************

Kwa upande wa Martin katika Maisha yake, alitumia muda wake mwingi kumtumikia mungu. Aliipa Elimu kipaumbele akiamini atafanikiwa, ili siku moja aje kuisaidia familia yake iliyokuwa ikiishi katika lindi la umaskini.
Kitu ambacho kilimfanya Martin kupendwa na watu wa rika zote ni tabia yake njema. Upole, Uzuri wa sura, urefu kiasi na rangi yake ya kahawia ilizidi kuipamba sura yake na kumfanya kuwa kivutio kwa wadada wengi aliokutana nao.
Hata wakati anasoma shahada yake ya Uandishi wa Habari (Bachelor of Arts in Journalism) katika Chuo Kikuu Kishiriki cha Tumaini tawi la Iringa, alisumbuliwa sana na wanafunzi wa kike waliokuwa wakimhitaji kimapenzi.
Barua za kumtaka kimapenzi, Martin alikuwa ameshazizoea hakumbuki hata kama kuna nyingine aliwai hata kuzisoma au kuzijibu, anachokumbuka alitumia muda wake mwingi katika Masomo..
Kati ya Wanafunzi chuoni hapo waliomtaka na kumsumbua Martin Kimapenzi ni Mabinti wawili wa familia moja, Maria & Angela, Mabinti wa Mchungaji Moses Kalinga.
Maria ambaye ni Mkubwa alimpenda sana Martin licha ya kwamba alijua wazi kuwa Martin yupo katika mahusiano ya kimapenzi na Mdogo wake Angela, lakini hakusita kumuonyesha hisia zake za mapenzi Shemeji yake Martin. Wakati wote alitamani kuona Martin akiwa wake japo alitaka kufanya hivyo kwa siri kubwa bila mdogo wake kujua.
Mabinti hawa wa Mchungaji Tajiri na Maarufu Tanzania na Afrika, Mch. Moses Kalinga wa Kanisa la Eagles Revival Outreach Ministry (EROM), Wote wawili wanasoma Kozi moja na Martin.
Baba yao kabla ya kurudi Tanzania, alikuwa akihudumu kama Mchungaji Msaidizi katika Makao Makuu Ya Kanisa Hilo la Eagles Revival Outreach Ministry (EROM) lililopo Johannesburg Nchini Africa Kusini na baadae kurudi Nyumbani Tanzania. Licha ya Kwamba alirudi ili kuwa Mchungaji Mkuu wa Kanisa hilo Tanzania lakini pia aliweza kuanzisha Kampuni ya EMG (Erom Media Group) iliyomiliki Kituo Cha Television Kilichoitwa EROM Tv na EROM FM Radio. Vyombo vyote vya habari vikiwa Jijini Dar es Salaam.
Maria ni binti yake aliyempata baada ya Miaka 10 ya Ndoa yake na Bi. Anna Emmanuel.
Maria alitokea kumpenda sana shemeji yake kiasi cha kushindwa kuzuia hisia zake. Kila walipokutana alitumia muda wake mwingi kumtazama Martin bila kuchoka. Maria aliumia sana alipoona Martin haoneshi kuvutiwa na chochote kutoka kwake.
Maria hakupenda kumwona Martin akiwa karibu na msichana yoyote Chuoni hapo. Alikuwa na wivu kwa shemeji yake pengine kumzidi hata Angela mwenyewe. Maria hakujua kwa nini alimpenda Martin kiasi kile.
Maria alijaribu kutumia kila mbinu ili amnase shemeji yake Kimapenzi, alitumia uwezo wa kifedha waliokuwa nao wazazi wao ili kumpata Martin lakini ilishindikana. Kwa Kifupi, Maria hakuwa tayari kumkosa Martin. Maria aliumia moyo kila alipowaona pamoja Mdogo wake Angela na Martin.

********************

Martin akiwa Chuoni hapo aliendeleza kipaji chake cha kuimba, tofauti na alivyokuwa mdogo, safari hii alikuwa akiimba nyimbo tofauti tofauti, aliimba nyimbo mbalimbali za wasanii maarufu duniani kama wakina Paul McCartney, Boyz II Men, Elvis Presley na wengine wengi. Uwezo wake wa kuimba ulimuongezea umaarufu zaidi.Chuo Kizima walimfahamu Martin kwa Uimbaji wake.
Akiwa Mwaka wa Mwisho wa Masomo yake, Wiki Moja kabla ya kufanya Mitihani yao ya Mwisho Ya kumaliza Chuo (University Examination), Serikali ya wanafunzi chuoni hapo iliandaa Bonanza lililoshirikisha wanafunzi kutoka Kozi mbalimbali. Lengo la Bonanza Lilikuwa ni kujenga Ushirikiano miongoni mwa wanafunzi na Pili, Kuweka miili na akili zao sawa ili kujiandaa na mitihani yao ya Mwisho.
Mashindano hayo yaligawanywa katika Makundi mawili, Kundi la kwanza ni la michezo iliyopangwa kufanyika mchana kama Mpira wa Miguu, Mpira wa Kikapu, Mpira wa Pete, Kukimbiza Kuku, Kukimbia na Gunia na Riadha.
Mashindano ya Kuimba, Kucheza Muziki na Ucheshi (Stand-Up Comedy) yaliwekwa katika Kundi la Pili na kupangwa kufanyika usiku katika Ukumbi Maarufu chuoni hapo wa Multi- Purpose, Ukumbi Maalumu kwa kufanyika matukio mbalimbali yanayotokea chuoni hapo.
Wanafunzi walivyopata habari hiyo kila mmoja alifurahi, Waliokuwa tayari walianza kujiandikisha kushiriki.Kila mmoja alijitamba kufanya vizuri zaidi ya mwenzake.
Wanafunzi Waliisubiria siku ya Mashindano hayo kwa hamu kubwa.

****************

Maria toka mashindano yatangazwe alipita katika kila kona ya Mbao za Matangazo Chuoni hapo kutafuta jina la Martin ili kuona mchezo atakaoshiriki lakini hakubahatika kuliona Jina la Martin mahala popote.
Maria alishindwa kumuuliza Mdogo wake Angela kwa nini hajaona jina la Martin kwenye Mbao za Matangazo, aliamua kwenda kumdadisi rafiki wa karibu na Martin aliyeitwa Peter Matiang’i, alijua kwa jinsi Peter alivyokuwa muongeaji asingeweza kumficha kitu, angeweza kupata majibu ya maswali yake.
Peter ni raia wa Kenya, aliyefika Tanzania kwa ajili ya Masomo, alifahamika Chuo kizima Kwa uongeaji wake. Kutokana na kuwa Mshehereshaji (Mc) katika matukio mbalimbali yaliyokuwa yakifanyika Chuoni hapo, wanafunzi wengi walizoea kumuita “Master P”.
Maria alizunguka maeneo mbalimbali ya Chuoni hapo kumtafuta Master P, alifanikiwa kumkuta katika Kiwanja cha Mpira wa Kikapu akifanya mazoezi kwa ajili ya kujiandaa na Mashindano. Maria alimsubiri mpaka alivyomaliza mazoezi na kumfata.
“Mambo P” Maria alimsalimia
“Poa tu Maria, kumbe na wewe unapenda Basket Ball” Master P aliongea huku akionekana kunywa Maji.
“Kiasi sio sana” Maria alisema
“Basi kwa sababu umeanza kuja uwanjani ntakufanya uupende mchezo huu, basket ni mchezo mzuri sana” Safarii hii waliongea huku wakionekana kuondoka uwanjani, wakipita nyuma ya Maktaba Kubwa ya Chuoni hapo kuelekea upande yalipo Mabweni ya Kiume. Baada ya maongezi ya hapa na pale, Maria akaona atoe la moyoni.
“Mbona rafiki yako simuoni” Maria aliuliza
“Nani?....Martin” Master P aliuliza.
“Ndio”
“Mbona yupo,nilimwacha amelala bwenini”
“Simuoni akifanya mazoezi kama nyinyi”
“Martin amesema hatoshiriki Mashindano ya Mwaka huu, tumemshawishi tumeshindwa tumeona bora tumwache na maamuzi yake”
“Au anaumwa?” Maria alisema.
“Anaumwa wapi, nikikwambia sababu yenyewe utacheka eti kwa sababu hajalipa ada ya muhula huu ndiyo anasema hawezi kushiriki mashindano, sasa sijui ada ina uhusiano gani na haya Mashindano”
“Master P ada ina uhusiano, ili mtu yoyote aweze kushinda katika shindano lolote anahitaji kuwa na utulivu wa fikra, kama Martin bado hajalipa ada hawezi kuwa na utulivu wa fikra na wenda kweli ndiyo sababu inayomfanya kushindwa kushiriki, atakuwa anafikiria vitu viwili kwa wakati moja”. Aliongea Maria.
Mazungumzo kati ya Master P na Maria yaliendelea mpaka walipofika karibu na Bweni analokaa Master P na Martin lijulikanalo kama German-America, waliagana. “Usisahau kumsalimia Martin”. Hayo ndiyo yalikuwa maneno ya Mwisho ya Maria wakati wanaagana na Master P.
Martin alikuwa miongoni mwa wanafunzi walioshindwa kujiandikisha kushiriki katika Mchezo wowote. Hii ilitokana na ukweli kwamba Martin alikuwa na hofu kubwa ya kushindwa kufanya mitihani yake ya kumaliza Chuo, iliyokuwa inakaribia kutokana na kutolipa Ada. Hali hiyo ilimkosesha raha.
Mara kwa mara aliwapigia simu wazazi wake kuwakumbusha kuhusu Ada, wazazi wake walimjibu bado wanatafuta wakipata watamtumia, majibu ambayo yalimkatisha tamaa zaidi.
Katika Kipindi chote cha Maandalizi ya Mashindano hayo, Martin hakujihusisha na chochote, alikuwa Mnyonge sana. Muda mwingi alitumia kufikiria namna atakavyopata ada ili aweze kufanya mitihani.

******************

Justine mara baada ya kufukuzwa na wazazi wake kijijini kalenga alipanga mikakati ya kwenda Jijini Dar es Salaam, kutafuta maisha. Siku nyingi alikuwa na ndoto ya kufika Mji huo, kutokana na sifa kemkem alizowai kuzisikia kuhusu Mji huo alitamani kufika na aliamini atafanikiwa kupata kazi yoyote itakayo mpatia kipato. Kwa kuwa hakuwa na maelewano mazuri na wazazi wake hata safari yake hiyo alipanga kuwa siri hakutaka mtu yoyote hajue.
Akiwa amekaa pembezoni mwa nyumba yao mara baada ya kuamka na kukumbuka kuwa amefukuzwa nyumbani na wazazi wake, Justine alijipapasa kwenye mifuko ya suruali yake na kukuta amebakiwa na sh 200.
Bila hata ya kujikung’uta vumbi, Justine aliinuka na kwenda ndani ya uzio wa nyumba yao ambako alimkuta baba yake akiwa amepumzika kwenye Mkeka akisoma gazeti.
“Nani amechukua hela yangu” Kwa sauti ya juu Justine alimuuliza baba yake
“Nani achukue hela yako, kwa hela gani hasa uliyokuwa nayo” Mzee Jonathan alimjibu.
“Nauliza tena, nani amechukua hela yangu, nilikuwa na elfu 1 mfukoni siioni”
“Usitupigie kelele hapa, kwanza nilishakwambia sitaki kukuona nyumbani kwangu”
Kwa sauti ya jazba “Halafu we mzee usinichanganye, nimekuuliza hela yangu iko wapi unaniletea habari nyengine” Kisha akamgeukia mama yake ambae muda wote alikuwa kimya akiwatazama “Mama mwambie mume wako tabia ya kufatilia maisha ya watu aache, kuna watu wengine tumepinda, tutakuja kufanya tukio hapa tuwepe lawama, halafu kila siku nasema kama Pombe nakunywa mimi, niacheni, tena nakunywa kwa pesa zangu mwenyewe”
“Justine…..!!” Mama yake aliita na kuendelea “Kama kweli mimi ni mama yako nisikilize ninachotaka kukwambia, mwanangu unakoelekea sasa ni kubaya. Siku hizi umekuwa mlevi kupindukia, hukumbuki hata kula. Hata Mafundisho ya dini…….” Kabla hajamalizia anachotaka kusema, Justine akadakia“Kumbe Bi. Mkubwa na wewe wale wale tu umeshirikiana na mume wako kuniibia hela yangu”
Baada ya majibizano ya muda mrefu na wazazi wake, Justine alichukua uamuzi wa kuondoka nyumbani kwao.
Akiwa bado ana randa randa mitaani, aliwaza namna ya kupata nauli itayomfikisha stendi ya Miyomboni, stendi kuu ya daladala iliyopo Iringa Mjini ambapo angeweza kufika na kujipanga na safari yake ya kuelekea Dar es Salaam siku inayofuata.

********************

Hatimaye, Siku iliyokuwa ikisubiriwa kwa hamu kubwa ikawadia, ilikuwa ni Jumamosi iliyosheheni shamra shamra za hapa na pale. Kila mwanafunzi alionekana ni mwenye vyuso ya furaha.
Hali ya hewa ya Baridi ilizidi kuipamba siku hiyo kuwa ya aina yake. Kelele za Mavuvuzela ya hapa na pale yalisikika kutoka kila pembe ya Chuo hicho. Lugha za Kebehi, Vijembe na Kejeli zilitawala. Muda ulipofika, wanafunzi walianza kumiminika viwanjani.
Michezo ilifanyika katika viwanja mbalimbali vilivyopo Chuoni hapo kutegemeana na asili ya mchezo husika. Kundi la kwanza la Michezo liliendelea na kumalizika jioni, wanafunzi walipata nafasi ya kupumzika kwa ajili ya michezo mingine itakayofanyika usiku.
Jioni ya Siku hiyo, ndiyo ilipangwa kufanyika sehemu ya pili ya Mashindano hayo katika Ukumbi wa Multi- Purpose. Muda ulipofika wanafunzi walianza kumiminika kwa wingi katika Ukumbi kwa ajili ya kushuhudia Mashindano yaliyosalia. Vipengele vilivyokuwa vikishindaniwa wakati huu ni Kucheza Muziki, Ucheshi na Kuimba.
Ndani ya Ukumbi, nderemo na vifijo vilisikika. Waliofanya vizuri katika Mashindano ya Mchana walionekana wakishangilia na kuzunguka kila Pembe ya Ukumbi huo, Kelele za Mavuvuzela zilishamiri.
Jukwaa lilipambwa kwa vitambaa vya rangi za kuvutia na maua mbalimbali. Muziki ulipofunguliwa kila mmoja alishangilia na kuingia kati kucheza. Ukweli ilikuwa ni siku ya furaha kwa wanafunzi wengi. Mc wa shughuli hiyo, Master P alipanda Jukwaani na kuanza kuchombeza maneno ya hapa na pale.
“Sema yeaaah”
Kisha Master P aliwatangazia ratiba ya usiku huo kuwa wataanza na kipengele cha Ucheshi, Kucheza Mziki na watamaliza na Waimbaji. Akatumia fursa hiyo kumkaribisha Jukwaani Mlezi wa Wanafunzi (Dean of Students) Chuoni hapo, Rev. Emmanuel Aswile, kwa ajili ya kufungua rasmi Mashindano hayo.
Mashindano yalianza na amsha amsha ya hali ya juu, washiriki wote walionekana kujipanga vizuri.
Ufundi wa kutumia maneno, ucheshi na mbwembwe alizokuwa nazo Mc vilizidi kupendezesha shughuli. Mashindano yaliendelea huku kukiwa hakuna dalili ya Martin kuweza kushiriki.
Maria akiwa ndani ya Ukumbi alizunguka huku na kule kuona labda atamwona Martin lakini hakufanikiwa. Alipepesa macho yake kumtafuta mdogo wake Angela nae pia hakufanikiwa kumuona ndani ya Ukumbi. Kutomuona Martin na Angela katika Ukumbi huo lilikuwa pigo jingine kwake sababu aliamini fika kuwa watakuwa pamoja. Alizungusha Macho kila kona ya ukumbi huo bado hakufanikiwa kuwaona.
Minong’ono ya hapa na pale kuhusu kutoonekana kwa Martin katika Mashindano hayo ilianza kusikika ndani ya Ukumbi. “Leo Martin hayupo?”Watu waliulizana bila Majibu.

******************

Wakati Mashindano yakiendelea ndani ya Ukumbi, Martin alikuwa amekaa na Angela, nje ya Bweni lake wakiongea mambo yao huku akipiga Gitaa na kwa Sauti ya Taratibu akiimba Wimbo aliochaguliwa na Angela Uitwao ‘Do you remember Me’ ulioimbwa na Mwanamuziki wa Kimarekani Mwanadada V. Bozeman. Angela aliupenda sana Wimbo huo.

Kwa kifupi, Martin na Angela pale Nje, walifanya mambo yao mengine kabisa kana kwamba hakuna kilichoendelea Chuoni hapo Usiku huo. Angela aliamua kama Martin hatokwenda ukumbuni basi na yeye hatokwenda pia.
“Huo Wimbo Naupenda sana” Alisema Angela.
“Usijali nitakuimbia Kila utakapohitaji nifanye hivyo” Alisema Martin kisha akasimamisha kupiga Gitaa na kuendelea kusema.
“Hivi unajua Siku za kuendelea kuwepo chuoni zimekwisha, Karibu tunamaliza Chuo” Alisema Martin huku akimwangalia Angela Usoni.
“Siku zinakimbia jamani, ni kama Juzi tu tulipoingia hapa, nakumbuka ulivyokuwa ukiangaika kunipata" Alisema Angela na kuachia tabasamu pana.
Wote wawili walijikuta wakicheka.
“Ni kweli niliangaika sana kukupata mpaka kuna wakati nilitamani kukata tamaa”
“Mwanaume hatakiwi kukataa tamaa, unatakiwa kupambana kumpata mwanamke unayempenda, mwanamke anahitaji kubembelezwa, wakati mwengine mwanamke anakukataa sio kwamba hakupendi bali anataka kupima kiasi cha upendo ulionao kwake”
“Ni kweli lakini Maneno yako yalikuwa makali sana kiasi cha kunikatisha tamaa bado kidogo ningechoka kukubembeleza” Alisema Martin huku akilisimamisha Gitaa lake Pembeni ya Ukuta.
“Nilikuwa nataka kujua uvumilivu wako, unajua kuna wakati katika mahusiano mnapitia mambo mengi ambayo kama wapenzi mtapaswa kuombana msamaha, kusameheana na kuvumiliana, Hata katika maisha ya kawaida kuna wakati mungu anakupitisha katika nyakati ngumu, kama hautakuwa mvumilivu basi unaweza kujikuta unafanya matendo mabaya, uvumilivu ni muhimu katika kufanikisha jambo lolote”
“Ule ulikuwa sio uvumilivu, ilikuwa ni mateso”
“Sio mateso mpenzi wangu, Unajua kuwa wewe ni Mwanaume wangu wa Kwanza, hivyo nilikuwa nataka kujua kama nikikukabidhi moyo wangu utakuwa salama”
“Moyo wako utakuwa salama siku zote za Maisha yetu, halafu nimekumbuka kitu kuna Siku nilikuuliza nini Kirefu cha KJ Kwenye hii Cheni yako” Martin alisema huku akishika Mkufu wa Dhahabu ulioning’inia vizuri kwenye shingo ya Angela.
“Endelea kuwa Mvumilivu kuna Siku nitakwambia Kirefu chake, ila tu fahamu kwamba hizi herufu zina Maana kubwa sana kwangu”
Wakiwa bado wanaendelea kuongea, Ghafla Maria alifika na Kuwakatisha mazungumzo yao.
“Martin Mambo” Maria akiwa ameongozana na Rafiki yao Restuta, alisikika akimsalimia Martin huku akimwangalia usoni mdogo wake Angela.
Maria baada ya juhudi zake za kuwatafuta Ukumbini kushindikana aliona aje kuwaangalia Bwenini.
“Poa Shem, mambo vipi” Martin Alijibu huku akimpa Mkono Maria na rafiki yake.
“Safi tu” Maria aliitikia na kumgeukia Mdogo wake “Angela mbona nakupigia simu haupokei na Martin simu yake haipatikani?”
“Simu yangu nimeiacha kwenye chaja Bwenini na Simu ya Martin imeharibika toka jana ameipeleka kwa fundi ameambiwa kesho asubuhi itakuwa tayari, vipi dada ulikuwa unasemaje?”
“Nilitaka tu kujua uko wapi maana Ukumbini sijakuona na Tulikwenda Mpaka Bwenini kwako haukuwepo”
“Nipo huku dada angu, Martin aliniomba nije kuonana nae”
“Ok…Twendeni Ukumbini basi”
“Natamani kwenda ila sijisikii vizuri shemeji yangu” Martin alidakia na kisha kuendelea “ Wiki nzima hii naumwa ila natumai ukumbini kila kitu kinakwenda sawa” Martin alidanganya bila kujua kwamba Maria anajua sababu iliyomfanya kushindwa kushiriki kwake Mashindano hayo.
“Ok, Pole sana Shem, Umekwenda Hospitali?”
“Alikwenda na kuna dawa alipewa atumie” Angela kwa sauti ya taratibu alimsaidia Martin kudanganya huku akimwangalia Martin usoni na kuachia tabasamu kwa mbali.
“Aya Pole sana basi ngoja sisi tuwaache” Maria aliongea huku akiwapa mikono ya kwa kheri wawili hao na kuondoka mahali pale kuelekea Ukumbini.

*******************

Akiwa ukumbini , Fikra zake zilitawaliwa na Martin, roho yake iliumia sana kuwakuta pale nje pamoja. Alichukia kuona anadanganywa wakati anajua hasa sababu iliyomfanya Martin kushindwa kushiriki Mashindano hayo. Alijitahidi kujizuia chuki yake kwa mdogo wake lakini alishindwa taratibu alianza kumchukia mdogo wake. Aliona Mdogo wake anakuwa kikwazo cha yeye kushindwa kufanikiwa mambo mengi katika maisha yake.
Kiufupi ni mwili wake tu ndiyo uliokuwepo pale Ukumbini lakini fikra zake hazikuwepo kabisa. Fikra zake zilikuwa nje ya Ukumbi, zilimpeleka moja kwa moja mpaka kwenye kule nje, alimwona Martin na Maria pale nje ya Bweni.
Kutokana na Hasira na wivu kuchanganyika, Maria alijikuta anashikwa na kitu Fulani kama Kwikwi kwenye Shingo yake. Alijitahidi kunywa maji lakini ilishindikana, ile hali iliendelea kumtesa. Alijaribu kujizuia asilie lakini kwa mbali machozi yalipenya kwenye Kingo za mboni ya macho yake na kutoka nje. Alichukua Kitambaa na kujifuta Machozi.
Kilichomfanya Maria kulia sio tu upendo wake kwa Martin bali pia aliumia kuona mtu anayekuwa kikwazo cha yeye kutimiza ndoto za kuwa na mwanaume anayempenda ni mdogo wake, Angela.
Alijitahidi kujichanganya na wenzake kwa kuamua kucheza muziki ili hasahau kilichotokea lakini fikra zake hazikumpa ushirikiano bado zilitawaliwa na wivu.
Mashindano yakiwa katika hatua za mwisho, akiwa bado hajasahau kilichotokea dakika 15 zilizopita, Ghalfa Maria alishtushwa na Mlio wa simu yake ya Mkononi, alipoangalia vizuri ulikuwa ni Ujumbe Mfupi wa Maneno.

*******************

“Kaka hapo naomba nauli” Hiyo ilikuwa ni sauti ya Kondakta wa daladala aliyopanda Justine kutoka Kijijini Kalenga kwenda Miyomboni.
“Unapenda kudai nauli mara mbili unafikiri watu tuna pesa za kuokota, nimeshalipa” Justine alisema kwa sauti nzito.
“Haujalipa nauli”
“Jifanye umesahau ukitegemea nitalipa mara mbili, tena nipe chenji yangu kabisa”
“Umetoa Shilingi ngapi”
“Elfu 5”
“Kumbuka vizuri bado haujalipa nauli”
“Nimetoa nauli halafu usinizingue”
“Achana nae anaonekana Mtata huyo” Alidakia Dereva wa Daladala hiyo.
“Dereva acha kuingilia mambo yasio kuhusu” Justine alimjibu Dereva ambae alionekana kuingilia mabishano yao, na kisha akamgeukia Konda “Nipe Chenji yangu, halafu nishushe hapo kwenye tuta”
“Dereva simamisha gari kwanza, nimeibiwa Simu na Pesa zangu” Alisikika Bibi Mmoja ndani ya ile Daladala akilalamika.

******************

Ujumbe Mfupi wa Maneno aliopokea Maria kwenye Simu yake ya Mkononi akiwa Ukumbini, ulionesha kuwa amepokea kiasi cha Pesa kutoka kwa Mama yake, Bi Anna Emmanuel. Kwa mara ya kwanza toka atoke kule Bwenini alitabasamu.
Toka siku aliyofahamu kutoka kwa Master P kuwa Martin hatoshiriki Mashindano hayo kwa kushindwa kulipa Ada ya Muhula huo, Maria alifanya Juhudi za kuwasiliana na Mama Yake ili kuhakikisha anamsaidia Martin kupata Ada. Alifanya Juhudi hizo ili Martin aweze kushiriki Mashindano hayo.
Baada ya Kupokea Pesa hizo, Maria aliona anayo nafasi nyengine ya kuwa karibu na shemeji yake Martin. Alipomshirikisha Restuta kuhusu wazo lake hilo la Kumsaidia Martin ada, Alionekana akimuunga Mkono kwa kuamini kuwa njia hiyo itazidi kumweka karibu na Martin.
Kwa haraka Maria akiwa ameongozana na rafiki Yake walitoka nje ya Ukumbi na kuelekea kwenye moja ya Duka la Wakala kwa ajili ya kutoa Pesa hizo. Walimkuta Mhudumu akijiaanda kufunga Duka.
“Dada samahani nataka kutoa Pesa” Alisema Maria
“Mngechelewa Kidogo tu Mngekuta nimeshafunga” Alisema Mhudumu.
Maria alivyofanikiwa kutoa pesa kwa Wakala, walirudi Ukumbini na Moja kwa moja walikwenda sehemu aliyosimama Master P na kumnong’oneza “Martin yuko wapi”. Maria aliuliza akijifanya kama hajui sehemu alipo Martin. “Nadhani atakuwa Bwenini” alisema Master P. Maria akaendelea “Master P nisaidie kitu, Mzigo huu naomba ukampe Martin, ni Pesa ya Ada, tumia maneno yoyote utakayowezaila usimwambie kama hizi Pesa zimetoka kwangu”. Maria alitaka kufanya siri ili Mdogo wake Angela asijue kinachoendelea.
Baaada ya kusikia maneno hayo kutoka kwa Maria, Master P aliduwaa, Macho ya mshangao yalimtoka. Siku ile wakati wanatoka kwenye Kiwanja cha Mpira wa Kikapu, Master P alijua maongezi yao yaliishia pale. “U cant be serious, Umepata wapi Pesa zote hizi?” Kwa sauti ya Mshangao Master P aliuliza.
“Hayo mengine tutaongea baadae Master P, nenda kwanza kampe hizi Pesa” Maria aliongea huku akimpatia ile Bahasha, kisha akaendelea“Ombi la mwisho, naomba umshawishi Martin aje kuimba, hata wimbo mmoja tu, nitafurahi” Master P aliipokea Bahasha na kwa haraka alitoka nje ya ukumbi kuelekea Bweni la German-America kumfata Martin huku akifikiria Maneno atakayotumia kumshawishi Martin apokee pesa hizo bila kujua kama zimetoka kwa Maria.
“Martin kuna mzigo wako nilitumiwa na Baba yako, amesema ni Pesa za ada halafu alitaka kujua kwa nini haupatikani nikamwambia kuwa simu yako imeharibika” Master P alisema hayo huku akimkabidhi Martin ile Bahasha.
Master P alifikiria kutumia Mbinu hiyo, akijua wazi kuwa kwa kusema hivyo ataweza kupunguza idadi ya Maswali kutoka na urafiki wao wa muda mrefu hadi kufahamiana mpaka nyumbani. Japo Wazazi wa Martin hawakuwai kumtumia ada motto wao kwa utaratibu huo lakini asingeshangaa sana kama wazazi wake wangeweza kufanya hivyo kutoka na Urafiki mzuri uliopo kati yake na Master P.
Taarifa hiyo ya kutumiwa ada na wazazi wake kama alivyoambiwa na Master P, haikumfurahisha tu Martin bali pia iliibua hisia za furaha kwa Angela pia.
Master P hakuchukua muda mwingi Pale, alirudi ukumbini na kumkuta Mshiriki aliyemuacha akiimba akimalizia. Mshiriki huyo alipomaliza kuimba, Master P alipanda Jukwaani na kuchukua Kipaza Sauti na Kusema.
“Mshiriki wetu wa mwisho kutufungia Mashindano yetu ya leo, akiimba wimbo wa “I will make love to you” ulioimbwa na “Boyz II Men” si mwingine bali ni……Martin Jonathan Chota” Ukumbi mzima ulizizima.
Wanafunzi wakiendelea Kushangilia, Martin alionekana akipanda Jukwaani huku akiwa amebebelea Gitaa lake, alianza kuimba na kupiga Gitaa kwa Wakati Mmoja. Kwa Kifupi, Wanafunzi wengi walifurahi kumuona Martin akiimba.

STOLEN LOVE
 
Wanafunzi wakiendelea Kushangilia, Martin alionekana akipanda Jukwaani huku akiwa amebebelea Gitaa lake, alianza kuimba na kupiga Gitaa kwa Wakati Mmoja. Kwa Kifupi, Wanafunzi wengi walifurahi kumuona Martin akiimba.


SEHEMU YA PILI

“Nimekwambia Nipe chenji yangu halafu nishushe hapo kwenye tuta” Justine aliendelea kujibizana na Kondakta wa Daladala
“Hakuna Kituo subiri mpaka Kituoni” Kondakta alimjibu Justine huku akimrudishia chenji yake.
“Nishushe kuna kitu nimesahau”
“Nimekwambia hakuna kituo”
“Konda kumbe na wewe unapenda Makelele, amekwambia Mshushe sasa ubishi wa nini si umshushe tu” Alisikika Bibi mmoja aliyekaa kiti cha nyuma.
“Abiria wengine wasumbufu, haya dereva mwache hapo kwenye tuta” Kondakta aliongea huku akimwangalia Justine kwa hasira.
Justine bila kusema chochote alishuka haraka haraka na kuvuka upande wa pili wa barabara.
“Dereva simamisha gari kwanza, nimeibiwa Simu na Pesa zangu” Alisikika Yule Bibi akilalamika.
“Bibi una uhakika kuwa umeibiwa?” Aliuliza Dereva wa Daladala
“Ndio, Pochi yangu hii hapa imekatwa pembeni na kiwembe, pesa zangu zilikuwa kwa ajili ya kwenda kununulia dawa za mifugo” Bibi alisema huku akiwaonesha abiria wengine sehemu pochi yake ilipokatwa na kiwembe.
“Bibi labda itakuwa umeibiwa huko ulikotoka, kwani ilikuwa na Shilingi ngapi?”
“Imeibiwa humu humu ndani, mpaka napanda daladala ilikuwepo”
“Sasa mpaka unaibiwa bibi ulikuwa wapi”
“Nilikuwa nimesinzia mjukuu wangu”
“Bibi ilikuwa shilingi ngapi” Kondakta alidakia
“Elfu 50”
“Usawa huu elfu 50 ni nyingi sana, tena maskini ya mungu bibi wa watu wenda kajichanga mwaka mzima kuipata hiyo Pesa” Alisema Dereva
“Jamani abiria Kama kuna mtu yeyote amechukua pesa ya Bibi arudishe kabla hatujadhalilishana, kuweni na huruma” Alisema Kondakta, kisha na kuendelea “Dereva simamisha gari tukaguane”
“Hakuna abiria kushuka” Alisema Dereva
Mara baada ya Dereva kusimamisha gari, hatua iliyofuata ilikuwa ni abiria mmoja mmoja kukaguliwa.
“Ilikuwa ni simu ya aina gani Bibi” Aliuliza Kondakta
“Nokia”
“Nokia ya aina gani”
“Hata sijui”
“Ukiiona utaikumbuka”
“Ndio”
“Bibi kama hautapata pesa na simu yako ruksa geuza mtu Simba” Kondakta alisema na kusababisha abiria wote waliopo kwenye daladala kuangua Kicheko. Zoezi la kuwakagua abiria wote 15 walimo kwenye daladala lilichukua takribani dakika 10 hivi na kukamilika bila Mwizi kubainika na kuamua kuendelea na safari yao. Ndani ya daladala mazungumzo yote yalikuwa ni kuhusu wizi huo. Kila abiria alionesha kusikitishwa kwake na tukio hilo.
Baada ya juhudi zake za kutafuta nauli ya kumfikisha Miyomboni na Dar es Salaam kushindikana, Justine aliamua kutumia mbinu hiyo ya wizi ili kupata Nauli.
Kwa Ujumla hayo ndiyo yalikuwa Maisha ya Justine, Kaka yake na Martin. Justine alifanikiwa kufika Miyomboni majira ya saa moja jioni baada ya kuamua kubadili daladala na kupanda daladala nyengine. Kwa kuwa alishafanikiwa kupata nauli itakayoweza kumfikisha Dar es Salaam alipanga safari yake kuwa siku inayofuata.

**********************

Martin akiwa katika Moja ya Ukumbi wa Blonquist, uliopo katikati ya Chuo hicho, akijiandaa kwa ajili ya Mitihani iliyokuwa ikikaribia, mara baada ya kutoka mjini kuchukua simu yake kwa fundi, alipokea ujumbe mfupi wa maneno kwenye Simu yake. Alipoufungua ujumbe ule ulionesha kuwa ametumiwa Pesa na alipoendelea kuusoma zaidi ujumbe ule alitambua kuwa Pesa hizo zimetoka kwa Baba yake Mzee Jonathan. Alinyanyua simu yake na Kumpigia.
Baada ya kama dakika 5 kumaliza maongezi na Baba yake, Martin alielewa kuwa Pesa zile ametumiwa kwa ajili ya Malipo ya ada na kwamba hakuna pesa zozote ambazo baba yake alimtumia rafiki yake Master P. Martin alishangaa.
“Master P zile Pesa alizitoa wapi” Martin alijiuliza. Kwa haraka Martin alitoka nje ya Ukumbi ule na kuelekea Bwenini kumfuata Master P. Alimkuta akiwa ameshikiria ndoo, taulo begani akijiandaa kwenda kuoga. Alipofika hakusema kitu chochote alibaki akimuangalia usoni Master P.
“Vipi kuna tatizo?” Master P alimuuliza
“Ndio” Martin alisema kisha akaendelea “Zile Pesa ulizonipa ulizitoa wapi?”
“Kwani vipi” Master P aliuliza huku akitabasamu
“Nijibu kwanza”
“Si nilikwambia kuwa Wazazi wako wamekutumia”
“Sio kweli, baba ametoka kunitumia ada sasa ivi” Martin aliongea huku akimuonesha Master P ule Ujumbe wa kutumiwa pesa kwenye Simu yake.
“Hahahaha” Master P alicheka na kuendelea “Ngoja nikwambie tu ukweli ndugu yangu, japo aliyenipa zile Pesa aliniomba nisimtaje, zile Pesa alitoa Maria”
“Maria yupi”
“Maria Shemeji yako”
“What? Unasema Shem ndo alitoa zile Pesa?” Martin alishangaa
“Ndio” Alijibu Master P
“Alijuaje kama bado sijalipa Ada”
“Hayo mengine mimi sijui yametoka wapi ila alisema nisikwambie kama Pesa zimetoka kwake”
“Na Bora ambavyo hukusema kama zimetoka kwa Maria maana Angela asingeelewa”
“Mimi nilifanya kama nilivyoagizwa” Master P aliongea huku akiinua ndoo yake kuelekea bafuni huku akimwacha Martin akiwa bado haamini kilichotokea.

**********************

Usiku wa siku hiyo, Martin alipanga kumtafuta Maria ili amshukuru kwa Kitendo cha kumsaidia kupata ada. Aliamini ni wachache sana wenye kuweza kuwa na moyo kama huo.
Licha ya kwamba alijua Mpenzi wake Angela asingefurahishwa na kitendo alichofanya dada yake cha kutoa Pesa kwa siri, lakini aliona bado kuna haja ya kumshukuru Maria kwa alichokifanya. Alipanga kukutana na Maria bila Angela kujua, kwa sababu alijua, kama Angela angejua angeuliza maswali mengi ambayo yeye kama Martin hakuwa na Majibu nayo kwa wakati huo. Kwa hiyo alipanga kukutana na shemeji yake kwa Siri. Na hivyo ndivyo ilivyokuwa.
Alimtumia Maria ujumbe mfupi wa maneno kwenye simu yake ya Mkononi wa kumuomba kuonana nae baadaye.
“Shem mambo vip, Kama utakuwa na nafasi naomba kuonana na wewe”
Maria nae bila kuchelewa kupitia simu yake alijibu
“Safi tu Shem wangu, Kuna nini shem wangu”
“Usijali shem tukionana utaelewa dhumuni la wito wangu”
“Sawa shem nakuja japo unanitisha”
*****************************

Usiku huo wakiwa wamekaa Pembezoni mwa uwanja wa Mpira wa Kikapu, waliweza kuongea mambo mengi. Maria alifurahi kupata nafasi aliyoitafuta kwa kipindi kirefu. Aliona ushindi hupo karibu yake.
“Shem umependeza sana leo” Alisema Martin
“Asante Shem” Maria aliongea kwa sauti ya taratibu akiwa na kiu ya kutaka kujua alichoitiwa na Martin.
“Shem kikubwa kilichonifanya nikutafute ni kukushukuru kwa msaada wako, Master P amenieleza kila kitu”
“Ha Ha Ha Master P nae, Usijali shem wangu”
“Asante sana shem, ulizitoa wapi pesa zote zile”
“Alinitumia Mama, kwani kuna tatizo?”
“Hapana, nimeuliza tu”
“Nilifanya kila namna kuwasiliana na Mama ili nimshawishi anitumie pesa nikusaidie kulipa ada”.
“Angela ndiyo itakuwa aliyekwambia kuwa sijalipa Ada”
“Hapana sio Angela, ni Master P” Alipofika hapo alimtazama martin usoni na kisha akaendelea “Usijali nilimdanganya Mama kuwa Pesa aliyonitumia kwa ajili ya kulipa Ada iliibiwa Bwenini na hivyo nimeshindwa kulipa Ada”
“Ulifanya vyote hivyo kwa ajili yangu?” Martin aliuliza
“Ndiyo Shem, wewe ni shemeji yangu kwa hiyo sipo tayari kuona unapata shida, kama naweza kukusaidia nitafanya hivyo na nilimwambia Mama kuwa siku ile ndiyo ilikuwa siku ya mwisho kulipa Ada na kama sitolipa Ada siku ile sitoruhusiwa kufanya mitihani yangu ya kumaliza muhula na baada ya Mazungumzo, nilifanikiwa kumshawishi akakubali kunitumia Pesa”
“Sijui hata nikushukuru vipi, umefanya jambo kubwa sana kwa ajili yangu”
“Usijali shem vitu vya kawaida tu, leo wewe, kesho mimi naweza kuwa na shida ukanisaidia”
“Nimekuelewa shem ila kama hautojali wazazi wameshanitumia ada tayari, ningependa kukurudishia pesa yako” Martin aliongea huku akimuonesha Maria Bahasha iliyokuwa na Pesa ndani yake.
“Hapana Martin usijali mimi ile pesa sikukukopesha nilikupa kama shemeji yangu”
“Lakini wazazi wameshanipatia Ada tayari”
“Usijali, wewe kaa nayo utafanyia mambo mengine”
Martin alijikuta akikosa maneno ya kusema zaidi na kubaki akimtazama Maria.
“Nikwambie Kitu shem” Maria alivunja Ukimya
“Niambie”
“Na mimi nina shida yangu ya muda mrefu sijui nikikwambia utanisaidia??”
“Usijali shem kama ipo kwenye uwezo wangu nitakusaidia”
“Nina imani ipo kwenye uwezo wako”
Kila muda ulivyozidi kwenda, Maria alijikuta akivutiwa na jinsi Martin alivyokuwa akiongea. Maria alizidi kuchanganyikiwa na kifua kipana cha Martin. Maria alimsogelea zaidi Martin na kumshika mikono yake na kwa sauti ya kubembeleza huku mapigo yake ya moyo yakidunda kwa kasi na machozi yakimlengalenga alisema.
“Shem samahani lakini kama shida yangu itakukwaza”
“Niambie tu shem wala usijali”
“Naomba usinishangae kwa nitakachokwambia maana sio kawaida yangu” Maria alisema na kisha kuvuta pumzi ndefu na kuendelea “Shem kusema ukweli kabisa toka siku ya kwanza nakuona nilitokea kuvutiwa na wewe, najua kuwa unatoka na Mdogo wangu lakini nimeshindwa, imebidi tu niseme ukweli wangu, naomba uwe mpenzi wangu hata kwa siri moyo wangu utaridhika”
“Shem..” Martin aliita akiwa haamini alichokisikia
“Najua unachotaka kusema ni kuhusu mdogo wangu Angela, usijali, kama nilivyosema itakuwa siri kubwa kati yangu na yako”
“Lakini Shem…”
“Usitake kuniambia hauwezi kunitatulia shida yangu, ukiona mpaka nimevaa ujasiri wa kukwambia hivi ujue ni kwa jinsi gani nakupenda, katika maisha yangu sikuwai kuwaza kuja kujidharirisha hivi mbele ya mwanaume kwa ajili ya mapenzi”
Kabla Martin hajasema alichotaka kusema, Ghafla walishtuliwa na Sauti ya Mtu aliyefika pale bila wao kujua.

*******************

Safari ya Justine kwenda Jijini Dar es Salaam akitokea Mkoani Iringa ilichukua takribani Masaa Tisa. Hatimaye alifanikiwa kufika Jijini Dar es Salaam.
Mara baada ya kushuka kwenye Bus katika Stendi Kuu ya Mabasi ya Mikoani ya Ubungo, akiwa amebebelea begani Mfuko wake wa Sandarusi, alipokelewa na Joto Kali, tofauti na alivyozoea hali ya hewa ya Baridi Mkoani Iringa.
Kwa kuwa ilikuwa ni mara yake ya kwanza kufika katika Mji huo, Justine alijikuta akivutiwa na Kelele za hapa na pale kutoka kwa Madereva taxi waliokuwa wakigombania Abiria kwa ajili ya kuwapatia Huduma ya Usafiri. Alisimama kidogo kuwaangalia jinsi walivyovutana, aliachia tabasamu fupi na kisha akaendelea na Safari yake ya kutoka nje ya eneo la Stendi.
Alipofika nje ya Stendi, Justine alishangaa kuona Watu walivyofurika katika kila Pembe na kila mtu aliyemwona alionekana kutingwa na shunguli fulani. Aliona Jinsi Barabara zilivyozidiwa na Misongamano ya magari.

Mradi wa Mabasi yaendayo kasi ndiyo uliomshangaza zaidi. Hakupata kuona Mabasi mazuri, makubwa na ya Kisasa ya aina hiyo yakifanya kazi ya kubeba abiria kama daladala za kawaida. Alizoea kuona Mabasi Makubwa yakibeba abiria waendao Mikoani.Kwa kifupi Kila kitu kilikuwa Kigeni Machoni mwa Justine.

Ukweli Justine hamu yake kubwa ilikuwa ni kufika Jijini Dar es Salaam,Swali la wapi atafikia halikuwa na mashiko yoyote katika akili yake. Aliamini Kufika kwake Jijini Dar es Salaam ni sehemu ya Mafanikio aliyokuwa akiyatafuta siku zote. Mambo mengine alijipa moyo kuwa yatafata baadae.

Alivuka barabara na kuelekea upande wa pili wa barabara ambako aliona vijana kadhaa wakiosha Vioo vya Mbele vya Magari mbalimbali yaliosimama kwenye foleni za Mataa. Alikwenda moja kwa moja mpaka kwa Kijana mmoja aliyekuwa akiosha gari aina ya Totota Rav 4, aliyevalia Kofia yenye rangi ya ugoro naT-Shirt nyekundu iliyochafuka na kubadilika rangi hadi kuwa nyeusi.

“Mambo vipi” Justine alimsalimia Yule Kijana.


“Poa tu, Nikusaidie nini” Yule Kijana alimjibu kwa haraka haraka huku akiendelea kuosha Kioo.

“Natafuta Kazi”

“Unazingua mwanangu, ningekuwa na uwezo wa kuwapatia watu kazi, nisingefanya kazi ya kuosha Magari, Umetokea wapi”

“Iringa” Alijibu Justine.

“Umekuja Dar kufanya nini”

“Nimekuja kutafuta Maisha”

“Aliyekwambia Dar Maisha yanapatikana kirahisi nani, Mjini Vyuma Vimekaza”

“Nimekuja kujaribu bahati yangu”

“Kama unatoka Iringa wanyaru wenzako wale pale wamesimama pembeni ya Barabara” Yule Kijana alisema huku akigeuza shingo yake, na kwa sauti ya Juu alisema “Buda msikilize ndugu yako”

“Unasemaje Sule” Kwa mbali Buda aliuliza

“Ndugu yako huyo hapo ametoka Iringa Msikilize” Alisema Sule kwa sauti ya Juu


“Iringa unatoka sehemu gani Mdogo wangu” Aliuliza Buda mara baada ya Justine kufika pale.

“Kalenga karibu na Msikiti wa Sheikh Zuberi”

“Kweli wa Nyumbani, Mimi kwetu Iringa Mjini, Maeneo ya Kihesa mpaka Semtema yote wananijua, kama unakwenda kwetu unashuka kituo kinaitwa Ngome, utakuta kuna shule ya Msingi, Ukimuuliza hata mtoto mdogo, wapi kwa Mzee Mbilinyi, atakupeleka mpaka Mlangoni”

“Sawa”

“Kwa hiyo Dar umeingia lini na umekuja kufanya nini”

“Ndiyo naingia hivi, Nimekuja kutafuta kazi”

“OK, Aisee Karibu sana, Una Mtu wa kukusaidia kupata Kazi”

“Hapana Sina”

“Sasa utafanyaje, maana kazi za siku hizi kujuana sana, kama hakuna mtu unayemjua inakuwa ngumu sana kupata kazi, umesoma?”

Justine alitingisha Kichwa ishara ya kwamba hajasoma.

“Sasa utafanya Kazi gani mdogo wangu bila Elimu, wenzio sisi hatujasoma ndiyo maana tunabangaiza Mjini hapa”

“Naomba nisaidie kupata Kazi hata ya kuosha Magari”

“Kazi ya kuosha Magari hatafutiwi mtu, ni kuchangamka kwako tu, ukiona Magari yamesimama yakisubiri yaruhusiwe na Mataa, unawai fasta kuosha kioo cha mbele na nyuma ya gari ukimaliza unamfata Dereva akupe Kiasi chochote alichonacho”

“Asante sana”

“Unaitwa nani” Buda aliuliza

“Justine”

“Mimi naitwa Majuto Mbilinyi ila hapa Ubungo wamezoea kuniita Buda, kikubwa mdogo wangu usiwe mnyonge”

Akiwa anaendelea kuongea na Buda aliona Gari ndogo aina ya Toyota Mark X ilifika pale na Buda aliingia ndani.

“Ahsante sana, Maji mnachota wapi? Na Vifaa mnatoa wapi”

“Sule atakupa maelekezo yote” Alisema Buda huku akiingia kwenye Gari iliyomfata.

Justine alifarijika sana kukutana na Buda, Licha ya kwamba alikuwa na Uchovu wa Safari lakini hakutaka kupoteza muda, mara moja aliingia kazini kama alivyoelekezwa.

********************

Martin na Maria wakiwa bado wapo pale kwenye Uwanja wa Mpira wa Kikapu, Ghafla walishtuliwa na Sauti ya Mtu aliyefika pale bila wao kujua. Mtu huyo si mwingine bali ni Angela, akiwa ameambatana na Restuta.
Kwa sauti ya upole iliyochanganyika na Kwikwi ndani yake Angela alisema “Martin nini kinaendelea mbona siwaelewi toka lini mkasogeleana hivyo”.
Martin na Maria walishtuka sio kwa sababu hawakutegemea Watu kwenda maeneo yale la hasha, Ni kawaida kukuta watu wamekaa maeneo ya viwanja hivyo nyakati za Usiku ila walishtuka kwa sababu hawakutegemea Watu hao kuwa ni Angela na Restuta.
“Kwani kuna ubaya gani tukisogeleana” Alisema Maria safari hii sio kwa sauti ya upole bali kwa Ukali kidogo
“Huoni Ubaya, Mnataka tuwafikiriaje” Alidakia Rafiki yao Restuta.
“Tupo kwenye Mazungumzo yetu” Maria aliongea huku akimkata Jicho kali Restuta.
“Mazungumzo gani hayo yasiyoisha kwa zaidi ya saa nzima sasa” Angela alisema na kisha alimtazama Martin ambaye muda wote huo alionesha kushikwa na Sintofahamu, akiwaza nani aliyemwambia Angela kuwa yupo uwanjani muda huo na Maria.
“Martin nimekuuliza nini kinaendelea” Sauti hiyo ya Angela ilimzindua Martin kutoka kwenye dimbwi la mawazo. Martin alivyosikia hivyo alijitoa taratibu kwenye Mikono ya Maria na kwenda hadi pembeni alikosimama Angela.
“Sio kama unavyofikiria Angela, tulikuwa na mazungumzo ya kawaida tu”
“Sio kama ninavyofikiria nini wakati tumekaa pale tukiwaangalia kwa muda mrefu, tumesikia kila kitu mlichokuwa mkiongea” Angela aliongea huku akilia na kisha kumgeukia Maria “Dada Kweli wewe wa kunifanyia hivi, hata siamini”
“Nimefanya nini cha ajabu embu tokeni zenu au mnataka kutujazia watu, mtu kukaa na shemeji yake kuongea ndo iwe Ajabu” Maria alijitetea huku macho yake ya hasira muda wote yakimuangalia Restuta.
“Martin kitu gani mlichokuwa mnaongea mpaka hukutaka na mimi niwepo”
“Si umesema umesikia kila kitu, sasa unataka kujua nini tena” Maria alidakia.
“Nyie wote Rafiki zangu lakini Maria ulichofanya sio Kizuri” Alisema Restuta
“Sio Kizuri nini” Maria aliongea kwa sauti ya Ukali
“Dada angu nakuheshimu sana” Alidakia Angela
“Kama una niheshimu usingekuja hapa kuvuruga mazungumzo yetu”
“Angela usijali nitakueleza kila kitu tukitoka hapa” Martin aliingilia kati kwa sauti ya Upole
“Umekosa wanawake wote mpaka uwe na dada yangu” Maria aliuliza.
“Angela usiseme hivyo, Mimi na Maria hatuna chochote kinachoendelea” Alisema Martin
Martin alimgeukia Maria aliyesimama pembeni na kumwambia“Maria mwambie Angela Ukweli”
“Kweli unataka nimwambie Ukweli?” Aliuliza Maria
“Ndiyo, mwambie Ukweli”
“Ukweli ni huu mdogo wangu, Martin hakutaki unamlazimisha tu” Alisema Maria
.”Maria” Martin Aliita kwa sauti ya Juu kidogo na Mshtuko kwa sababu hakutegemea Maria angesema hivyo.
“Dada nimekukosea nini mpaka unafanya yote haya” Aliuliza Angela
“Kwani hujui ulichonikosea katika Maisha yangu?? Nimekuwa Mpweke kwa miaka yote kwa sababu yako, usitake niseme mambo ambayo usingependa kuyasikia” Alisema Maria kwa sauti ya Juu huku machozi yakimtoka kutokana na kukumbuka Jambo fulani.
“Nimefanya nini mpaka nistahili maumivu yote haya” Alisema Angela
“Mbona siwaelewi” Martin aliingilia Kati
“Kuna siku utaelewa ukweli wote Martin, Utaelewa maumivu ninayoyapitia katika maisha yangu sababu ya Angela” Alisema Maria huku akilia kwa hasira na kisha kumvamia Mdogo wake Angela.
“Nakuchukia Angela” Alisema Maria huku akimshambulia mdogo wake kwa makofi.
Wanafunzi waliosikia mvutano huo walianza kutoka Mabwenini na kukusanyika katika eneo hilo.
“Maria unafanya nini” Martin alisema wakati akijaribu kuwatenganisha Maria na Angela. Restuta nae hakuwa nyuma katika kuwatenganisha ndugu hao wasipigane.
“Niacheni” Maria alisema kwa Sauti ya Juu huku akihema kwa nguvu.
Kuja kutahamaki, Maria alimsukuma Angela hadi akadondoka chini na Kichwa chake kujigonga kwa nguvu kwenye Jiwe lililopo karibu yake na kupoteza fahamu.
“Ameua” Walisema kwa Mshtuko baadhi ya wanafunzi waliokuwepo katika eneo lile, baada ya kuona Angela akitokwa na damu nyingi kichwani.

******************************
 
Back
Top Bottom